Tuesday, May 24, 2011

Kauli kuhusu mauaji na kukamatwa na wabunge Tarime

KAULI YA KATIBU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI KUHUSU VITENDO VYA JESHI LA POLISI KWA RAIA NA KUKAMATWA KWA WABUNGE WA CHADEMA

Katibu wa Wabunge wa Kambi Rasmi ya Upinzani inayoongozwa na CHADEMA nalaani vitendo vinavyofanywa na Jeshi la Polisi kwa kusababisha mauji ya raia na kukwepa kufanya uchunguzi kamili na huru kuhusu wahusika wa vifo hivyo na kuingilia haki za msingi za jamaa za marehemu na wananchi wa eneo husika kushiriki katika maziko ya wakazi wenzao na hatimaye kupatiwa haki nyingine zinazostahili kutokana na madhila yaliyotokea.

Aidha nakemea hatua ya jeshi la polisi ya kuwakamata wabunge wa CHADEMA, Tundu Lissu na Esther Matiko wakiwa katika kazi ya kuwatumikia wananchi na natoa mwito waachiwe mara moja; wao pamoja na wote waliokamatwa nao.

Tundu Lissu (Mb) ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Sheria na Katiba aliitwa na wahanga wa tukio husika pamoja na chama kwenda kusimamia haki za msingi za familia za marehemu baada ya polisi kukataa kufanya uchunguzi na pia kuminya mazingira ya haki kupatikana.

Akiwa katika kutekeleza wajibu huo, jana (23 Mei 2011) alitaarifiwa na familia za marehemu na wananchi wengine kwamba polisi ina mpango wa kuchukua miili ya marehemu usiku na kuipeleka kusikojulikana na kuombwa kuungana nao katika kuwapa huduma za kisheria katika hatua zote. Aliambatana na familia za marehemu, wananchi na viongozi wa chama kufuatilia suala hilo ndipo alipokamatwa yeye na wengine na kuwekwa rumande kuanzia jana mpaka hivi sasa.

Esther Matiku ambaye ni mbunge wa viti maalum kupitia mkoa wa Mara anayetokea Tarime akiwa katika eneo lake la kazi leo (24/05/2011) alijulishwa na wananchi wa Nyamongo kwamba maiti ambazo walizichukua polisi kwa nguvu zingine wamezitelekeza njiani na kuitwa kwa ajili ya kushuhudia na kuchukua hatua zinazostahili kwa niaba ya wananchi. Akiwa katika kushughulikia suala hilo naye alikamatwa na jeshi la polisi na kuwekwa rumande mpaka hivi sasa.

Ifahamike kwamba matukio ya Nyamongo na Tarime kwa ujumla ni matokeo ya uongozi wa serikali kushindwa kusimamia vizuri sekta ya madini ikiwemo kuacha kuchukua hatua zinazostahili kwa wakati wa miaka kadhaa sasa kutokana na vitendo vya ukiukwaji wa sheria na mikataba vinavyofanywa na kampuni Barick Africa Gold na vile vinavyofanywa na polisi na vya kifisadi vinavyofanywa na viongozi wengine wa kiserikali wanaonufaika na hali hiyo yenye athari kwa wananchi katika maisha yao kutokana na mauji, uchafuzi wa mazingira, upotevu wa mapato ya umma na watanzania wa eneo husika kutokunufaika kwa rasilimali.

Naungana mkono na wananchi na wadau wote waliotoa mwito kufanyika kwa uchunguzi huru wa vifo (inquest) ili hatua stahili ziweze kuchukuliwa na kwa nafasi yangu nyingine kama Waziri Kivuli wa Nishati na Madini nitatoa tamko karibuni lenye kueleza kwa kina udhaifu wa serikali ulivyosababisha mauji hayo na kutaka wahusika akiwemo waziri kuwajibika.

Aidha, kwa mara nyingine narudia tena kutoa pole kwa familia za marehemu ambao wanapitia kipindi kigumu wakati huu kutokana na matukio yanayoendelea; Mwenyezi Mungu awape uvumilivu wa kusimamia haki na ukweli kwa mustakabali wa taifa.

Imetolewa tarehe 24 Mei 2011 na:

John Mnyika (Mb)
Katibu wa Kambi Rasmi ya Upinzani
Na Wabunge wa CHADEMA

Mbunge afanya ziara ya Mtaa kwa Mtaa

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ambaye pia ni Mwenyekiti wa CHADEMA katika Mkoa wa kichama wa Kinondoni amefanya ziara ya kichama katika kata za Mabibo na Manzese jana (22/05/2011) kwa lengo kujenga oganizesheni ya chama ngazi ya chini.

Katika ziara hiyo Mnyika ameingiza wanachama wapya na kufungua misingi/matawi ya chama katika mitaa mbalimbali ya kata hizo sambamba na kuzindua ofisi za chama katika maeneo hayo.

Katika ziara hiyo Mnyika akiambatana na viongozi wa chama na wanachama wa chama hicho walitembea kwa miguu katika nyumba mbalimbali kuwashukuru wananchi kwa kumchagua na kufuatilia masuala ya kimaendeleo.

“ Pamoja na kuwa baada ya uchaguzi nilifanya mikutano ya hadhara ya kiserikali kwa ajili ya kuwashukuru; nimekuja kwenu leo kwa kuwa niliahidi kwamba mkinichagua nitarudi kwa njia ile ile niliyopitia kuomba kura ili kuwashukuru na kushirikiana nanyi kutimiza wajibu”, alisema Mnyika.

Akihutubia wananchi wakati wa uzinduzi wa ofisi ya CHADEMA katika kata ya Mabibo Mtaa wa Jitegemee, Mnyika alieleza manufaa ya kuchagua vyama mbalimbali katika kuleta uwajibikaji kwa kuwa kwa mara ya kwanza halmashauri ya Kinondoni imeweza kutenga bilioni tano katika bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012 kwa ajili ya matengenezo ya barabara.

Mnyika alisema kwamba jumla ya shilingi milioni 595 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo maalum ya Barabara ya kutoka Mburahati mpaka Mabibo eneo la Chuo Cha Usafirishaji (NIT) na kuahidi kuendelea kushirikiana na madiwani kuondoa kasoro nyingine zilizobainika katika bajeti iliyopitishwa.

Akizindua ofisi ya chama kata ya Manzese Mnyika alieleza umuhimu wa kuwa chama thabiti kwa ajili ya kusimamia vizuri utendaji wa serikali na viongozi wa kuchaguliwa na wananchi.

“ Hayati Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kwamba chama legelege, huzaa serikali legelege. Ombwe la kiungozi lililopo kwenye serikali hivi sasa katika ngazi mbalimbali ni ishara ya udhaifu wa chama kinachotawala; CHADEMA lazima ionyeshe tofauti katika kuwawajibisha viongozi wake waweze kuutumikia umma ipasavyo”, alisema Mnyika.

Mnyika alisema CCM inazungumza kujivua gamba lakini bado mafisadi wanakumbatiwa ndani ya serikali na pia serikali inashindwa kushughulikia kikamilifu kero za wananchi kama maji na kupanda kwa gharama za maisha wakati kodi za wananchi hazitumiwi vizuri.

Mnyika alisema kwamba ofisi hiyo ya chama isifanye tu kazi za kuhudumia wanachama bali izibe pengo pale wananchi wanapokwenda kuwasilisha malalamiko yao kwa ofisi za kiserikali lakini hatua stahili hazichukuliwi kwa wakati.

“ Wajibu wenu uwe ni kuunganisha nguvu ya umma, nimetembelea mitaa mbalimbali ya Manzese na kukutana vioski vingi vya Kampuni ya Maji Dar es Salaam (DAWASCO) havitoi maji na sehemu kubwa ya miundombinu ya maji iliharibiwa wakati wa utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa barabara na haikurejeshwa. Viongozi wa ngazi ya chini wa kiserikali hawajafuatilia kero hii kwa muda mrefu; hivyo ni wajibu wenu kuwasukuma na mkikwama mtaarifu ngazi za juu kwa hatua zaidi”, alieleza Mnyika.

Akihutubia Mkutano wa hadhara katika Mtaa wa Chakula Bora kata ya Manzese ikiwa ni sehemu ya kuhitimisha ziara hiyo Mnyika aliwaeleza wananchi hatua ambayo amefikia katika kutekeleza ahadi ya kuwawakilisha wananchi kwa kuweka kipaumbele katika masuala ya elimu, ajira, maji, maji, miundombinu, uwajibikaji, usalama, ardhi na afya katika kipindi cha miezi mitano toka achaguliwe na kuahidi kuendelea kuwashikirisha wananchi katika kila hatua atakayofikia.

“ Kuanzia wiki hii tunaanza vikao vya kamati za bunge mpaka mwezi Juni mwanzoni ambapo mkutano wa bunge utaanza rasmi, na hili ni bunge muhimu la bajeti hivyo kuna mambo mengi zaidi itakwenda kuwawakilisha katika mkutano huo na nawashukuru kwa hoja mbalimbali ambazo mmenitaka niziwekee mkazo”, alisema Mnyika.

Imetolewa tarehe 23 Mei 2011 na:

Aziz Himbuka
Katibu Msaidizi
Ofisi ya Mbunge Ubungo

Tamko kuhusu Umeme

TAMKO LA WAZIRI KIVULI (MSEMAJI WA KAMBI RASMI YA UPINZANI) WIZARA YA NISHATI NA MADINI JUU YA MASUALA, MATUKIO NA MWELEKEO WA SERIKALI KUHUSU UMEME KATIKA KIPINDI CHA MWEZI MEI

Utangulizi

Katika kipindi cha Mwezi Mei yameibuliwa masuala na wadau mbalimbali na zimetolewa kauli kadhaa na serikali kuhusu umeme.

Baadhi ya masuala na matukio hayo ni pamoja na kuanza kwa mgawo mkubwa wa umeme, kutokutekelezwa ipasavyo kwa hatua za dharura za kuongeza uzalishaji wa umeme, tuhuma za ufisadi katika sekta husika na masuala mengine kuhusu umeme yenye kuathiri uchumi wa taifa na maisha ya wananchi hususani wa kipato cha chini.

Kambi ya Upinzani inayoongozwa na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kupitia kwa Waziri Kivuli wa Nishati na Madini imekuwa ikifuatilia kwa karibu matukio na kauli hizo na kubaini kwamba serikali kupitia Wizara husika ya Nishati na Madini haijawajibika ipasavyo kuchukua hatua stahili au kutoa mwelekeo wenye matumaini kwa watanzania hususani katika masuala yafuatayo:

Kuhusu mgawo wa umeme unaotokana na upungufu wa gesi:

Nchi iko katika mgawo mkubwa hivi mpaka tarehe 26 Mei 2011 kwa kile kilichoelezwa ni kutokana na kampuni ya uzalishaji wa gesi asilia ya Songo Songo ya Pan African Energy Tanzania Limited ambayo imetangaza kutosambaza gesi katika kipindi hiki kwa ajili ya ukaguzi na ukarabati mkubwa wa mitambo ya gesi. Hali hii imetokana na mamlaka husika kutokuwajibika ipasavyo kwa kuwa matengenezo haya yalifahamika kwa serikali kuanzia mwishoni mwa mwaka 2010 na mwezi Februari 2011 suala hili lilijadiliwa ndani ya serikali lakini hatua stahili hazikuchukuliwa kwa wakati kufanya ufuatiliaji na udhibiti uliohitajika.

Kumekuwepo tuhuma za muda mrefu kwamba kampuni ya Pan African imekuwa haifanyi matengenezo ya ukamilifu na kwa wakati hata hivyo Wizara inayohusika haikueleza hatua ambazo zimechukuliwa hali ambayo imeongeza hitaji la matengenezo makubwa kwa wakati mmoja yaliyosababisha gesi kutokusambazwa na kuleta upungufu wa umeme wa kati ya MW 200 mpaka 359 katika kipindi husika. Kwa kuwa serikali ilifahamu mahitaji ya matengenezo hayo miezi mingi kabla ingeweza kuweka mfumo wa uhifadhi wa gesi kwa ajili ya kuepusha hasara ambayo inalikumba taifa hivi sasa. Aidha serikali imekuwa pia ikifahamu kuhusu tatizo lingine la kutopanuliwa ipasavyo kwa miundombinu ya kusafirisha gesi (re rating) kunakopaswa kufanywa na kampuni ya Pan African.

Hali hii ya utegemezi wa serikali kwenye sekta ya gesi kwa makampuni yenye mwelekeo wa udalali imesababisha hasara kwa serikali lakini ina mwelekeo pia wa kuhatarisha usalama wa nchi katika siku za usoni kama hatua stahili hazitachukuliwa; hivyo Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA) inapaswa kuchunguza hali hiyo na kuchukua hatua stahili. Aidha Serikali inapaswa kupitia upya mikataba na makampuni ya Songas, Pan African na Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) ili kuondoa migongano na kupunguza mzigo kwa taifa wakati gesi asilia ni mali asili ya watanzania sanjari na kupanua wigo wa usafirishaji wa gesi katika mwaka wa fedha 2011/2012.

Kuhusu kusuasua kwa hatua za dharura za kupunguza upungufu wa umeme:

Kwa upande mwingine, natahadharisha kwamba mgawo mkubwa na wa muda mrefu utalikumba taifa kuanzia mwezi Julai 2011 kutokana na hatua za dharura kutochukuliwa kwa wakati. Pamoja na Serikali kushikilia msimamo wa kukodi mitambo ya umeme wa MW 260 ambayo itatumika kwa kipindi cha miezi sita pekee kwa gharama za zaidi ya bilioni 400 badala ya kuweka mkazo katika kununua mitambo kama ambavyo imeshauriwa na wadau mbalimbali; Wizara ya Nishati na Madini haijawajibika kwa kiasi cha kutosha kuhakikisha nchi haikumbwi na mgawo katika kipindi husika.

Mchakato wa kutekeleza mpango wa dharura umecheleweshwa na hivyo kuna hatari ya mitambo hiyo kuwa tayari kutoa huduma mwezi Januari katika kipindi ambacho haihitajiki na kusababisha hasara kwa taifa kama ilivyokuwa kwa mitambo ya Richmond/Dowans.

Hivyo, serikali inapaswa kutangaza kusitisha mara moja mpango huo na kuelekeza fedha hizo za umma katika hatua za dharura za kununua mitambo ya kudumu; kinyume na hapo itathibitika kwamba kuna mazingira ya ufisadi katika mpango huo wenye kutaka kuongeza mzigo wa madeni kwa TANESCO na gharama za umeme kwa wananchi wa kawaida.
Izingatiwe kwamba madhara na hasara yote ambayo wananchi, sekta binafsi na serikali imekuwa ikipata kuanzia mwezi Februari mwaka 2011 mpaka Disemba 2012 kwa kipindi cha takribani mwaka mzima inatokana na kutokuwajibika kikamilifu kwa mamlaka husika kwa kuwa dharura ilifahamika toka mwaka 2008 na serikali ikapanga kwamba utekelezaji wa miradi ya MW 60 wa kutumia mafuta mazito Mwanza na Mradi wa MW 100 wa kutumia gesi asilia Ubungo, na wa MW 200 Kiwira ilipaswa kukamilika Februari 2011; hata hivyo kutokana na uzembe na ufisadi sasa miradi hiyo itakamilika 2012/2013.

Hivyo, serikali kupitia TANESCO na kwa kushirikiana na sekta binafsi iweke mazingira wezeshi ya kisheria, kikanuni na kibajeti msingi wa utekelezaji wa miradi ya Kiwira (MW 200), Somangafungu (MW 230), Mnazi Bay (MW 300), Kinyerezi (MW 240), maporomoko ya Ruhudji (MW 358) ili ianze kwa haraka zaidi kwa mwaka wa fedha 2011/2012 tofauti na kusubiria mpaka mwaka 2013/2014 kama serikali inavyopanga hivi sasa.

Kuhusu tuhuma za ufisadi katika manunuzi kwa ajili ya miradi ya umeme:

Mpaka sasa serikali haijawajibika ipasavyo kushughulikia tuhuma za ufisadi katika ununuzi wa mafuta mazito ambayo Waziri wa Nishati na Madini alieleza bungeni tarehe 6 Aprili 2011 kwamba zimetumika bilioni 46 kwa ajili ya kuendesha mitambo ya kufua umeme ya IPTL. Hata hivyo, mwezi Mei Wizara ya Nishati na Madini kupitia taarifa nyingine imesema kwamba fedha zilizotumika kwenye ununuzi wa mafuta katika kipindi husika ni bilioni 28; bila kueleza sababu za kutofautiana kwa maelezo ya waziri bungeni na haya yaliyotolewa sasa na Waziri. Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA) ulishatoa tamko kwamba pamoja na RITA kusimamia IPTL hawana mamlaka, fedha hazipitii kwao na kwamba hata taratibu zote za manunuzi na maamuzi mazito hufanywa na serikali kuu. Wizara ya Nishati na Madini ilipaswa kutoa maelezo kuhusu tuhuma hizo na iwapo Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeanza kuzichunguza. Kutokana na hali hiyo, Kamati ya Nishati na Madini inapaswa ifanye uchunguzi maalum kama ilivyoombwa na Zitto Kabwe (Mb) ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati za Hesabu za Mashirika ya Umma.

Pia pamekuwepo malalamiko mbalimbali kuhusu mazingira ya kupitishwa kwa zabuni za ununuzi wa nguzo, transforma na nyaya za umeme kwa kiwango kikubwa toka nje ya nchi huku viwanda vya ndani mathalani TANALEC ABB, East African Cables (hususani kampuni tanzu ya Tanzania Cables) na vingine vikididimia. Hali hii imesababisha pia kukwama kwa utekelezwaji wa miradi mbalimbali ya kusambaza umeme kutokana kwa kile kinachoelezwa kuwa ni vifaa kutokupatikana kwa wakati toka nje ya nchi.

Hitimisho:

Hivyo kutokana na hali hiyo; kama sehemu ya kutekeleza wajibu wa kibunge wa kuisimamia serikali tamko hili linatolewa kutaka Wizara ya Nishati na Madini hususani Waziri wake William Ngeleja (Mb) kuwajibika kutokana na athari za kutochukua hatua kwa wakati na Rais Jakaya Kikwete akiwa ndiye Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri kueleza kwa umma hatua ambazo serikali yake inakusudia kuchukua kurekebisha hali hiyo ikiwemo kuwachukulia hatua kwa wanaohusika. Rais Kikwete alishatembelea Wizara na kutoa maagizo na akarudia tena maagizo yale yale kwa kutumia mamilioni ya walipa kodi kupitia semina elekezi; kinachotakiwa hivi sasa sio maagizo tena bali ni mkuu wa nchi kuchukua hatua. Aidha iwapo tamko hili halitazingatiwa maelezo na vielelezo zaidi vitawasilishwa kwenye vikao vya kambi rasmi ya upinzani na hatimaye masuala husika na mengine zaidi yataibuliwa bungeni kwa ajili ya wahusika kuwajibishwa na pia vipaumbele kuzingatiwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012.

Imetolewa tarehe 22 Mei 2011 na:

John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli (Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani)
Wizara ya Nishati na Madini

Saturday, May 21, 2011

Mbunge atoa rambirambi msiba wa msanii

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika amesema kuwa amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Mkurugenzi wa kikundi cha maigizo na filamu cha Jakaya Theatre Arts.

Mnyika aliyasema hayo jana (15/05) alipotembelea nyumbani kwa familia ya marehemu katika kata ya Ubungo Jijini Dar es salaam kwa ajili ya kuwasilisha rambirambi.

Akizungumza na mbunge, Chediel Senzighe ambaye ni kaka wa marehemu na mmoja wa wasanii wa kundi hilo anayefamika kwa jina la kisanii kama “Kakoba Chapombe” alisema kwamba marehemu alifikwa na mauti katika ajali iliyotokea juzi eneo la Kimara Resort baada ya kontena la lori la mizigo kuanguka kwenye kituo cha basi.
Chediel ameeleza kuwa maziko ya Thomas Senzighe yanatarajiwa kufanyika kesho na kwamba mwili wa marehemu utaagwa Ubungo eneo la Gide.

Kwa upande mwingine Mnyika amesema kwamba marehemu Thomas Senzighe ameacha pengo katika medani ya sanaa kwa kuwa alikuwa mhimili nyuma ya mafanikio ya kikundi hicho ambacho kimeonyesha maigizo mbalimbali kupitia kituo cha luninga cha ITV mathalani ‘Taharuki’, ‘Kivuli’, ‘Mwiba’ na ‘Kovu la Siri’

Mnyika alisema kwamba mara ya mwisho kuwasiliana na marehemu alimjulisha kwamba wanaandaa filamu na kwamba pamoja na filamu marehemu amekuwa akijishughulisha na kazi za lugha ya Kiswahili kupitia tovuti www.swahilicenter.com.

Imetolewa tarehe 16 Mei 2011

Mbunge ahimiza Wananchi Kwembe kushiriki Mkutano wa Maji

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika anahimiza wakazi wa Mtaa wa Kwembe kuitikia mwito wa Kamati ya Maji ya Mtaa huo kujitokeza kwa wingi katika mkutano wa watumiaji wa maji wenye kulenga kuunganisha nguvu katika kukamilisha utekelezaji wa miradi ya kuwezesha maji kupatikana katika maeneo yao.

“Nimepokea taarifa ya katibu wa Kamati Joyce Manyerere kuwa Mkutano utafanyika siku ya Jumamosi tarehe 21 Mei 2011 saa nane mchana katika ofisi ya Mtaa wa Kwembe; nahimiza wananchi husika kuitikia mwito huo”.

Manyerere ameeleza kwamba ufungwaji wa mashine mpya ya kusukuma maji yenye uwezo wa kusukuma Lita 90,000 za maji kwa saa moja katika mradi wa maji safi ya bomba katika Mtaa wa Kwembe, Kata ya Kwembe Manispaa ya Kinondoni umekamilika na majaribio ya kusukuma maji kutoka bomba kuu la Ruvu kuanza rasmi.

Kukamilika kwa kazi hiyo kumefanya Mtaa huo kupata ufadhili mwingine wa kujengewa tanki la kuhifadhi na kusambaza maji kupitia vituo vitano chini ya ufadhili wa mradi wa “Maji Yetu” unaofadhiliwa na Jumuia ya Ulaya (EU) na Belgian Technical Cooperation (BTC). Ujenzi wake unatarajiwa kuanza hivi karibuni.

Aidha Shule 3 ikiwemo moja ya Msingi, mbili za Sekondari pamoja na zahanati ya Mtaa wa Kwembe vinatarajiwa kupata ufadhili wa kujengewa miundombinu ya kuhifadhi maji kutoka Shirika la SAWA mara tu baada ya maji safi ya bomba kuanza kutiririka Mtaa wa Kwembe.

Ili kukamilisha miradi yote hii watumiaji wote wa maji safi ya bomba ambao ni pamoja na wakazi wote wa Mtaa huo, wenye viwanja na mashamba katika Mtaa wa Kwembe watakuwa mkutano wa watumiaji maji utakaofanyika Jumamosi Tar 21 Mei 2011, saa nane mchana katika Ofisi ya Serikali ya Mtaa Kwembe.

Ajenda za mkutano huo ni pamoja na:- Kutambua na kuwaorodhesha wahitaji wa huduma ya maji safi ya bomba katika Mtaa wa Kwembe; Kupanga utaratibu wa usambazaji wa vituo vya maji na mabomba binafsi; Kujadili na kupitisha mchakato wa kuanzisha Umoja/Kampuni ya Watumiaji Maji Mtaa wa Kwembe.

Mkutano huu unafuatia wa awali ambao ulifanyika tarehe 30 Januari 2011 ambapo Mbunge Mnyika alihudhuria na kushirikiana kwa hali na mali katika jitihada za kutatua kero ya maji.

Katika mkutano huo wa kwanza ilibainika kwamba mradi wa maji Kwembe ulichangiwa na washirika wa kimaendeleo mwaka 2000 lakini maji hayatoki kutokana na kutokamilika kwa mradi katika kipindi cha takribani miaka kumi toka fedha za mradi huo zitolewe kwa pamoja na mambo mengine kukosekana nguvu ya wananchi.

Baadhi ya sababu nyingine ni pamoja na kampuni iliyotekeleza mradi huo kutaka marekebisho kadhaa yafanyike katika mfumo wa mabomba yanayounganisha tanki na kupokea na kupokea maji kutoka bomba kuu na pampu kabla ya kuwashwa.

Kamati ya maji ilianisha vifaa vinavyohitajika kuwa ni kuondoa kona kali la kupokea maji toka bomba kuu, kufunga vifaa vya kulinda mashine isiharibike pamoja na vifaa vingine na hatimaye mbunge na wananchi wengine walichangia sehemu ya gharama za vifaa hivyo.

Chanzo: Aziz Himbuka (20/05/2011)

Sunday, May 15, 2011

Matengenezo barabara ya Mbezi Makabe kuanza

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika amesema kwamba matengenezo maalum ya barabara ya Mbezi mpaka Makabe kupitia Lubokwe na mji mpya yataanza mwezi huu mara baada ya kupungua kwa mvua zinazoendelea hivi sasa.

Mnyika aliyasema hayo juzi (8/5/2011) akizungumza katika mkutano wa wananchi wa Mtaa wa Mbezi Luis uliofanyika katika eneo la Kona ya Miembesaba.

Mnyika amesema matengenezo hayo ambayo yanatarajia kugharimu takribani milioni 170 yametokana na malalamiko ya muda mrefu ya wananchi wa Mbezi Makabe kuhusu ubovu wa barabara hiyo.

Kwa upande mwingine, Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi wa Barabara Mtaa wa Mbezi Luis, Samwel Kirama alimshukuru mbunge kwa kushiriki katika mkutano huo na kumweleza kwamba fedha kutoka mradi wa TASAF awamu ya pili cha shilingi milioni 28 zimeingizwa katika akaunti ya mradi kwa ajili ya ujenzi wa barabara nyingine katika eneo hilo.
Kirama alisema kwamba fedha hizo zitatumika kufanya ukarabati wa barabara ya Mazulu mpaka Kwa Kidevu kupitia Miembesaba kwa kiwango cha changarawe pamoja na kuweka mifereji ili barabara iweze kupitika katika vipindi vyote.

Mkutano huo uliazimia kwamba ramani ya ujenzi wa barabara hiyo ijulikane kwa wakazi wote ili kutoa ushirikiano katika maeneo ambayo yanagusa miti na kuta kutokana na ujenzi holela.

Aidha mkutano huo wa wananchi ulikubaliana kwamba tathmini ya maeneo ya barabara ya mbele ya mradi huo iendelee ili kuweza kujua mahitaji kwa ajili ya kutafuta vyanzo mbadala kwa kadiri iwezekanavyo.

Diwani wa Kata hiyo, James Kajale aliahidi kufuatilia Manispaa ya Kinondoni kuhusu uwiano kati ya matumizi nguvu kazi na suala la ufanisi wa utekelezaji wa mradi ili hatua za ujenzi zianze mapema.

Chanzo: Aziz Himbuka

Saturday, May 14, 2011

Hoja Binafsi kuhusu Kituo Ubungo (UBT)

Utangulizi
Kituo Kikuu cha Mabasi Ubungo (UBT) kilifunguliwa rasmi tarehe 6 Desemba 1999 pamoja na mambo mengine uanzishwaji wa kituo hiki ulikuwa na dhumuni la kutoa huduma kwa wasafiri pamoja na watumiaji wengine na pia kuongeza mapato ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam.

Katika kipindi cha kati ya mwaka 2004 mpaka 2008 tumeibua tuhuma mbalimbali za ufisadi na upotevu wa mapato katika Kituo hicho zikiwemo zinazohusu Kampuni ya Smart Holdings ya Familia ya Kingunge Ngombare Mwiru; hata hivyo katika kipindi chote zimekuwa zikikanushwa na serikali na chama kinachotawala.

Hatimaye Tarehe 15 Machi 2009 Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliagiza ufanywe uchunguzi maalum (Special Audit) na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu makusanyo ya Kituo Kikuu cha Mabasi cha Ubungo (UBT) ili kuboresha mapato ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam.

Tarehe 28 Julai 2009 Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Bw. Ludovick Utoh, alikabidhi ripoti hiyo kwa Waziri Mkuu ambayo pamoja na mambo mengine ilieleza kasoro za ukusanyaji wa ovyo na tuhuma za ubadhirifu wa mapato ya Kituo Kikuu cha Mabasi cha Ubungo.

Kutokana na matatizo ya kiuendeshaji na kiutawala yaliyoripotiwa katika tarifa za Mkaguzi na mdhibiti wa fedha za serikali pamoja na taarifa zingine kuhusu kituo kutofanyiwa kazi kwa ukamilifu Nawasilisha hoja binafsi kwa mujibu wa Kanuni ya 19 (1) na (5) ya Kanuni za kudumu za Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ( ambayo katika hoja hii itajulikana kwa upande mwingine kama Halmashauri) ambayo mimi ni mjumbe ili hatua stahili ziweze kuchukuliwa.

Maelezo ya Hoja
Kutokana na ukaguzi maalumu uliofanywa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa hesabu za serikali mambo yafuatayo yalibainika;

• Kuwa Halmashauri iliingia mkataba na kampuni ya M/s Smart Holding kama wakala wa kukusanya mapato katika kituo cha mabasi Ubungo. Kutokana na mkataba huo kampuni tajwa ilitakiwa kuilipa Halmashauri kiasi cha shilingi 1,500,000 kwa siku kwa mapato ya magari yanayoingia kwenye kituo pamoja na tozo ya ulinzi wa magari yaliyokuwa yakiegeshwa na ada ya kuingia. Hata hivyo baada ya ukaguzi uliofanywa uligundua kuwa kiasi cha shilingi 4,618,629 ilikuwa ni mapato ya kila siku ukilinganisha na kiasi kilichopo kwenye mkataba huo ambacho Halmashauri ilikuwa ikipokea.

• Kuwa ilibainika kuna upangishaji holela wa majengo ya biashara bila idhini ya mmiliki. Kwa mfano mpangaji alilipa kiasi cha shilingi 130,000 kwa mwezi kama kodi kwa mmiliki wakati mpangaji alikuwa anapata mapato ya kiasi cha shilingi 600,000 kwa kupangisha watu wengine (subletting).

• Kuwa kiasi cha shilingi 146,692,226 zilikusanywa na wakusanyaji wa mapato lakini mapato hayo hayakupelekwa benki.

• Kuwa Halmashauri iliingia mkataba na wafanyabiashara ndogondogo 100 kuendesha shughuli za biashara ndani ya kituo bila kuainisha maeneo au majengo ambayo watayatumia kwa shughuli zao.

• Kuwa Halmashauri iliingia mkataba wa miaka 14 na M/s Riki Hill Hotel na mkataba utaisha Julai 20 mwaka 2023; hata hivyo mapitio ya makubaliano hayo yanaonyesha mapungufu yafuatayo;

i. Mkataba ulisainiwa miaka miwili baada ya shughuli kuanza.

ii. Mkataba ulisainiwa na Mkurugenzi wa Halmashauri na sio Mstahiki Meya kama ambavyo taratibu zinataka.

iii. Uongozi wa Halmashauri ulishindwa kutoa nyaraka za kwa namna gani mkodishwaji huyo alivyopatikana na pia mkodishwaji alikuwa anatumia eneo kubwa kuliko ilivyokuwa ikionekana katika mkataba.

• Kuwa Halmashauri iliingia mkataba na kampuni ya M/s Abood Bus Service kupanga katika eneo la 2070 sqm kujenga na kutumia na badae kulitoa jengo kwa mmiliki na kutakiwa kulipa 500,000 kwa mwezi; hata hivyo mapungufu yafuatayo yalionekana:

i. Hakuna ushahidi wa kimaandishi uliotolewa kwa wakaguzi kuthibitisha kiasi cha shilingi 44,220,660 kama gharama za ujenzi.

ii. Hakuna nyaraka iliyoonyesha jinsi mkataba wa ukodishwaji ulivyopatikana.

iii. Mkataba haukuonesha eneo ambalo lilipaswa kuendelezwa.

iv. Hakuna vigezo vilivyotolewa kuhalalisha malipo ya shilingi 500,000 kwa mwezi kwa eneo hilo.

• Kuwa uongozi wa kituo cha Ubungo kwa makusudi kabisa ulibadilisha kiwango cha upangaji cha shilingi 6,000 kwa futi za mraba 784.08 hadi shilingi 5,000 ambazo zilitakiwa kulipwa na kampuni ya M/s Clear Channel, kiwango ambacho kilitakiwa kutozwa kwa kampuni ya Bill Board advertisement kinyume na kiwango kilichowekwa na Kanuni za Halmashauri ya Jiji ya 1997 na hivyo kusababisha hasara ya kiasi cha shilingi 3,920,420 kwa Halmashauri kwa miaka mingi mfululizo.

• Uongozi wa Halmashauri kwa makosa yao wenyewe ya kivipimo ulisababisha kushuka kwa kiwango cha mapato kiasi cha shilingi 74,529,840 kwa miaka miwili kuanzia Julai 2007 hadi Juni 2009.

• Kuwa katika mkataba kati ya Halmashauri na kampuni ya M/s Globe Accountancy Services (wakala) ili kukusanya mapato kwa niaba ya Halmashauri kwa miaka mitatu kutoka tarehe 5/10/2001 hadi 4/10/2004 bila ushahidi wowote wa kimaandishi kuonyesha kuwa taratibu zote za kitenda zilifuatwa na pia taratibu za manunuzi hazikufuatwa.

• Kuwa hakuna utaratibu uliozingatiwa katika kuwapa mikataba M/s Scandnavia Express Service ltd, Riki Hill Hotel, Kiwembo Motors na Smart Holding kama wakala wa kukusanya mapato, na pia nyaraka kwa ajili ya ukaguzi hazikuweza kutolewa.

• Pamoja na mambo mengine kampuni ya Smart Holding kama wakala wa kukusanya mapato ilitumia vitabu vya risiti ambavyo ni vigumu kwa Halmashauri kudhibiti na hivyo kuwa vigumu kugundua kiasi cha mapato walichokuwa wanakusanya.

• Kuwa kampuni ya Scandnavia ilikuwa haina mkataba rasmi na Halmashauri katika eneo walilokuwa wanalitumia na pia kampuni haikulipa kiasi cha shilingi 236,486,400 kuanzia Septemba 2005 hadi Mei 2009 kama ilivyotakiwa.
Pamoja na mapungufu hayo yaliyoelezwa na taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali; yamejitokeza pia masuala mengine katika kipindi cha kati ya mwaka 2009 mpaka 2011 yanayohitaji kushughulikiwa:

• Hata hivyo mnamo tarehe 30 Oktoba 2010 Halmashauri ilisaini mkataba na kampuni ya Konsad Investments Limited kwa ajili ya kukusanya mapato kwa niaba ya Halmshauri. Hata hivyo, kampuni hiyo imekuwa wakati mwingine haiwasilishi makusanyo ya 5,650,000 kwa siku kwa Halmashauri kama ilivyokubaliwa.

• Kampuni ya Konsad imeanza kutekeleza Sheria Ndogo mpya (By Law) ya kupandisha viingilio vya kituoni bila ridhaa ya Jiji. Pamoja na Uongozi wa Kituo kukanusha wakati wa ziara ya Mstahiki Meya ya tarehe 4 Februari 2011 ushahidi wa risiti unaonyesha kwamba tayari walishaanza kutoza hususani wananchi wanaoingia kwenye kituo. Suala la kupandisha viwango vya viingilio vinavyowagusa wananchi wengi wakati vyanzo vingine vyenye kuleta fedha nyingi zaidi vinaachwa huku huduma zikiwa hazijaboreshwa linahitaji kufanyiwa maamuzi mbadala na kutolewa tamko kwa umma.

• Katika ziara yangu ya Kituoni ya tarehe 28 Januari 2011 ya kusikiliza malalamiko ya mawakala nilibaini kuwepo kwa haki zao ambazo zinaminywa na mazingira magumu ya kufanyia kazi ikiwemo uchache wa ofisi za kukatia tiketi. Pia, kuna matitizo ya ulinzi kituoni hususani nyakati za usiku kwa ajili ya abiria wanaoshuka usiku. Kadhalika, kumekuwa na matatizo ya umeme yanayohusisha ubovu wa baadhi ya taa, umeme kuwa mdogo ukilinganisha na mahitaji na pia jenereta la Kituoni haliwashwi kwa wakati umeme unapokatika.

• Mpango wa Biashara (Business Plan) wa kuwezesha Jiji kukiendeleza kituo husika kuwa cha kisasa kwa lengo la kukuza biashara na kupanua huduma utakaohusisha ujenzi wa majengo ya kisasa yanayoendana na mahitaji ya kitaifa na kimataifa haujaanza kutekelezwa. Pamoja na changamoto za kiutendaji, sababu mojawapo inayoelezwa ni kusudio la ujenzi wa miundombinu (Depot and Transfer Station) unatarajiwa kufanywa na Wakala wa Mabasi yaendayo haraka (DART).

HOJA:Kutokana na maelezo hayo naomba kutoa hoja kwamba Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam lipitishe maazimio yafuatayo:

(1) Taarifa Kamili ya Ukaguzi Maalum (Special Audit) uliofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu Kituo Kikuu cha Mabasi cha Ubungo (UBT) itolewe hadharani na ijadiliwe katika Baraza la Madiwani wa Jiji.

(2) Mikataba yote iliyoingiwa kinyume na taratibu ivujwe au ipitiwe upya ili kuwa na mfumo ambao utawezesha Halmashauri kuweza kupata mapato ya kutosha kwa mujibu wa thamani ya mali na kanuni zinazohusika.

(3) Uchunguzi ufanyike wa tuhuma za mazingira ya ufisadi na ukiukwaji wa kanuni katika kuingiwa kwa mikataba tajwa ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa wahusika.

(4) Malimbikizo yote ya madeni yafuatiliwe na kulipwa ili Halmashauri iweze kupata mapato kwa ajili ya kutoa huduma za msingi za wananchi.

(5) Kwa kuwa Kituo cha Mabasi Ubungo kinachangia takribani nusu (50%) ya mapato ya jiji basi mkazo uwekwe katika kuboresha mazingira ya kituo kwa kufanya ukarabati na uendelezaji. Aidha mapungufu ya dharura ambayo yanaathiri zaidi watumiaji wa kituo yafanyiwe kazi katika mwaka wa fedha 2011/12.

(6) Kwa kuwa hakuna mgawo wowote ambao ngazi za Manispaa, kata na mtaa zinapata kutokana na mapato yanayotokana na Kituo cha Mabasi Ubungo; wakati majadiliano yakiendelea kuhusu suala hili, Jiji litenge bajeti ya Kituo Cha Mabasi Ubungo (UBT) kuchangia shughuli za kijamii (Corporate Social Responsibility) katika maeneo ya Jimbo la Ubungo.

(7) Taarifa ya Kina kuhusu Mradi wa Mabasi yaendayo kwa Haraka (DART) iweze kuwasilishwa eneo linalohusika na mradi huo liweze kufahamika ili Jiji lianze kutekeleza Mpango wa Biashara wa kuendeleza Kituo husika katika maeneo ambayo yataendelea kuwa kwenye usimamizi wa Jiji.

(8) Pendekezo lililotolewa katika kikao cha Kamati ya Fedha na Uongozi cha tarehe 11 Mei 2011 liidhinishwe na kutekelezwa ili kusitisha kutekeleza Sheria ndogo ya kuongeza kiwango cha kiingilio kwa wananchi toka sh 200 mpaka 300 na kufanya mapitio ya sheria ndogo husika ili nguvu za ukusanyaji mapato zielekezwe katika vyanzo visivyoongeza mzigo kwa wananchi wa kawaida wanaotumia Kituo Kikuu Cha Mabasi cha Ubungo.

Naomba kuwasilisha,

John Mnyika(Mb)-Jimbo la Ubungo
Mjumbe wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam
13/05/2011

Sunday, May 8, 2011

Matengenezo ya Barabara Golani-Saranga yaanza; daraja Burura latengewa fedha

Taarifa inatolewa kwa umma kwamba jana tarehe 6 Mei 2011 Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ametembelea kata za Saranga na Kimara kufuatilia utekelezaji wa mipango ya maendeleo.
Akizungumza na wananchi waliomzunguka katika eneo la Golani ambapo matengenezo ya barabara yameanza, Mnyika aliwaeleza wananchi hao kwamba matengenezo hayo yatahusisha ukarabati wa barabara kuanzia Kimara Suca, Golani, Saranga mpaka Temboni.

Aidha Mnyika aliwatangazia wananchi hao kwamba jumla ya shilingi milioni zaidi ya mia tano (501,973,470) zimetengwa kwenye bajeti ya Halmashauri ya Kinondoni kwa mwaka wa Fedha 2011/2012 kwa ajili ya kujenga Daraja Kubwa la Burura/Golani katika Mto Ubungo.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Saranga Ephraim Kinyafu alimshukuru mbunge kwa jitihada za kufuatilia kero za wananchi.

“Kwa zaidi ya miaka kumi wananchi wa eneo hili wamekuwa na kero ambapo nyakati za mvua mawasiliano hukatika lakini katika kipindi kisichofikia hata mwaka mmoja umefanikiwa kushawishi fedha kutengwa kwa ajili ya mradi huu muhimu”, alisema Kinyafu.

Kwa upande mwingine, akizungumza na wakazi wa Mavurunza katika mkutano uliofanyikia katika ukumbi wa G5 Mnyika aliwataarifu wananchi kwamba matengenezo ya Barabara ya Kimara, Mavurunza mpaka Bonyokwa nayo yanatarajiwa kuanza mwezi huu baada ya kupungua kwa mvua.

Akijibu swali la Mwenyekiti wa umoja wa wakazi hao ujulikanao kama Wanaume Upendo, Cleophas Malima kuhusu hatua mahususi ambazo zimechukuliwa na mbunge kuhusu barabara husika ambayo imekuwa kero kwa wananchi; Mnyika alisema kwamba hatua hizo zinahusisha ngazi mbili.

“ Mtakumbuka kwamba ujenzi wa barabara ya Kimara Bonyokwa ni kati ya ahadi ambazo alizitoa Rais Jakaya Kikwete mwezi Mei mwaka 2010. Mara baada ya uchaguzi katika vipindi mbalimbali nimefuatilia kwa karibu utekelezaji wa ahadi hii.

Zoezi la kuipandisha hadhi barabara hii kuwa ya mkoa limeshafanywa na wakala wa barabara (TANROADS) na upembuzi yakinifu umefanyika hivyo kupitia kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Dar es salaam ambacho mimi ni mjumbe cha tarehe 02 Februari 2011 nilitoa mwito kwamba tathmini ya fidia iweze kufanyika mapema zaidi ya ilivyopangwa awali ili hatua za ujenzi zichukuliwe kwa wakati.

Tarehe 21 Aprili 2011 nimewaandikia barua TANROADS yenye kumbukumbu na OMU/MB/006/2011 kuwakumbusha kuzingatia suala hili katika vipaumbele vya bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012 kama sehemu ya mkakati wa kupunguza foleni katika jiji la Dar es salaam kwa kuwa barabara hiyo inaungana na Tabata Segerea”, Alisema Mnyika.

Mnyika aliendelea kufafanua kuwa wakati hatua hiyo ikisubiriwa kunahitajika hatua ya dharura katika kipindi hiki cha mpito kutokana na ubovu mkubwa wa barabara hivyo tarehe 19 Aprili 2011 kupitia kikao cha Kamati ya Fedha na Uongozi cha Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni alitoa mwito kwa mkurugenzi kuhakikisha mhandisi anatembelea eneo hilo na hatua za haraka kuchukuliwa.

Mnyika aliwaeleza wakazi hao kuwa ameshafuatilia katika manispaa na kwamba matengenezo ya barabara hiyo yataanza mwezi huu ili kupunguza adha kwa wananchi na kwamba ukarabati huo usipoanza kwa wakati atawaeleza hatua zitazochukuliwa.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kimara Pascal Manota alimueleza mbunge maeneo korofi katika barabara hiyo hususani maeneo ya vyumba vinane, kwa kyauke mpaka darajani na kusisitiza kuwa iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa daraja mojawapo litasombwa na maji kutokana na barabara kubomoka na hivyo kusababisha hasara zaidi kwa umma.

Imetolewa tarehe 07/05/2011 na:

Aziz Himbuka
Katibu Msaidizi
Ofisi ya Mbunge