Tuesday, December 31, 2013

Kheri na fanaka kwa mwaka mpya 2014. Nimerudi!

Nimerejea toka kwenye mafungo na tafakari, kumradhi kwa wote mlionikosa simuni na mtandaoni. Nawatakia mwaka mpya wenye upendo na uadilifu

Sunday, December 1, 2013

Ujenzi wa Kituo cha Polisi Kata ya Sinza-Mchango wa Mfuko wa Jimbo



Ukaguzi nilioufanya katika Kata ya Sinza; ujenzi wa kituo cha polisi kwa fedha kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo.

Mfuko wa Jimbo umetenga milioni 10; tayari umeshatoa milioni 3.5 zilizofikisha jengo mpaka hatua hiyo. Taratibu za utoaji fedha zilikwamisha mradi toka mwezi Mei mwaka 2013.

Wednesday, November 27, 2013

Taarifa kwa umma kuhusu serikali kupandisha bei ya umeme

Gazeti la Tanzania Daima Toleo na. 3280 la tarehe 26 Novemba 23 limenukuu kauli iliyotolewa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini George Simbachawene wakati akizungumza na kipindi cha Kumepampazuka kilichorushwa na Redio One juu ya Serikali kupandisha bei ya umeme kama Shirika la Umeme (TANESCO) lilivyoomba.

Katika habari hiyo Simbachawene amenukuliwa akisema kwamba endapo kuna mwananchi yeyote atakayeona gharama za umeme ni kubwa ni vema akaamua kuwasha kibatari au akae giza. 

Rais Jakaya Kikwete anapaswa kumwagiza Waziri wa Nishati na Madini Prof Sospter Muhongo kuwaomba radhi wananchi kwa kauli hiyo iliyotolewa na Naibu Waziri Simbachawene kwa niaba ya wizara anayoiongoza.

Aidha, ni vyema Rais Kikwete kwenye hotuba yake kwa taifa ya mwisho wa mwezi huu akawaeleza wananchi iwapo uamuzi huo wa kupandisha kwa mara nyingine bei ya umeme ndio utekelezaji wa ahadi ya maisha bora aliyoitoa kwa watanzania kuanzia kwenye uchaguzi wa mwaka 2005.

Hii ni kwa sababu kupandisha bei ya umeme kuna athari ya kuchangia katika ongezeko la gharama na ugumu wa maisha kwa kuwa shughuli za uzalishaji na maisha ya kila siku zinategemea kwa kiwango kikubwa nishati.

Thursday, November 21, 2013

Mgao wa umeme na uongo nyuma yake!

Mgawo huu wa umeme ni wa ufisadi wa kimikataba Songosongo/PAT na udhaifu wa Mpango wa Dharura wa Umeme; Bungeni Muhongo alinijibu uongo.

Mgawo wa Umeme ufisadi wa PAT na udhaifu wa ukarabati wa visima ulijulikana toka Julai na Novemba 2011; Prof Muhongo alisema uongo kuficha.

Trilioni 1 ilitumika kuficha uongo wa Prof Muhongo Mgawo wa Umeme kwenye manunuzi ya mafuta mazito; Ufisadi, PAT, visima, gesi umemshinda.

MgawowaUmeme Prof Muhongo alisema uongo mara 2 bungeni; 1. 28 Julai 2012 baada ya kumhoji kwenye hotuba 27 Jul http://mnyika.blogspot.com/2012/07/hotuba-ya-kambi-rasmi-ya-upinzani.html

Uongo wa mara ya 2 wa Prof Muhongo bungeni kuhusu MgawowaUmeme ni wa Mei 23 nilipohoji baada ya hotuba ya 22 Mei: http://mnyika.blogspot.com/2013/05/hotuba-ya-msemaji-wa-kambi-rasmi-ya.html

Halafu kwa maagizo ya IMF/WB wanataka kupandisha bei ya umeme kufidia ufisadi kukodi mitambo ya dharura/ununuzi mafuta na mikataba mibovu.

Thursday, October 24, 2013

Wednesday, October 16, 2013

Ujenzi wa Kisima cha Maji Safi-Msigani!


Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika alipotembelea ujenzi wa kisima cha maji kilichojengwa katika mtaa wa Msigani, Kata ya Msigani, ujenzi wa kisima hicho umechangiwa na fedha za mfuko wa jimbokiasi cha Tsh 3.5 milioni katika kumalizia ujenzi huo.

Thursday, September 12, 2013

Mnyika ahoji ziliko fedha za DECI

na Shehe Semtawa

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amemtaka Gavana wa Benki Kuu, Benno Ndulu, kuwaeleza waliokuwa wanachama wa Kampuni ya Development Entrepreneurship for Community Initiative (DECI) fedha zao zilizotaifishwa na serikali kutoka kwenye taasisi hiyo ziko kwenye akaunti gani.

Mnyika alisema kuwa wakati sakata la DECI linaanza mwaka 2009, serikali ilitaifisha jumla ya sh bilioni 19, sawa na asilimia 40 ya fedha zote ambazo wanachama wa taasisi hiyo iliyokuwa ikiendesha na kusimamia mchezo wa upatu walikuwa wakidai.

Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara juzi Mtaa wa Mavurunza, Kata ya Kimara baada ya kuulizwa swali na mmoja wa wananchi aliyetaka kujua hatima ya fedha zao, Mnyika alitoa tahadhari kuwa danadana inayotaka kufanywa na serikali inaweza kutia shaka kuwa fedha hizo hazipo.

”Sasa naomba nimjibu yule mwananchi aliyetaka kujua hatima ya fedha za DECI. Mtakumbuka hili suala nimekuwa nikitaka majibu yake bungeni, lakini kila mara wanatumia kisingizio kuwa suala hili liko mahakamani.

Tuesday, September 10, 2013

Mnyika: Serikali imalize tatizo la maji

na Abdallah Khamis

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika, ameitaka serikali kuhamisha nguvu na kasi zilizotumika katika ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara kuelekea jijini Dar es Salaam na kumaliza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi hususan katika Jimbo la Ubungo.

Mnyika alitoa kauli hiyo juzi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kata ya Kimara, Mtaa wa Mavurunza na kusisitiza hakuna suala muhimu kama maji kwa wananchi na kwamba kunahitajika ufumbuzi wa muda mfupi na mrefu, ikibidi kwa hali ya dharura.

Alisema kama serikali inaweza kutumia muda mfupi kujenga na kutandaza bomba hilo kwa nini ishindwe kufanya hivyo kwa mabomba ya maji, ambayo ni uhai wa wananchi.

“Tunaendelea kupambana kuhakikisha tatizo la maji tunalipunguza na kuliondoa kabisa, ninachowaomba ni sauti zenu na mshikamano wenu, suala hili ni uhai wa watu, kama maji ni tatizo maana yake uhai wa binadamu uko shakani,” alisema Mnyika.

Wednesday, August 28, 2013

Uzinduzi wa Kampeni ya Kuchangia Maabara na Madawati chini ya Shirika la UDI



Mhe. John Mnyika akishirikiana na Mratibu John Mallya kuonyesha bango lenye ujumbe wa harambee ya kuchangia maabara na maktaba iliyozinduliwa Agosti 21, 2013

Thursday, August 15, 2013

Leo Agosti 15, 2013: Sengerema na Mwanza Mabaraza ya wazi ya Katiba Mpya

Sengerema: Endeleeni kutoa maoni kwa maneno na maandishi kwenye baraza letu la katiba linaloendelea uwanja wa Wenje kata ya Nyamburukano

Mwanza: Baraza la wazi la Jiji likijumuisha pamoja Wilaya za Ilemela na Nyamagana litaanza saa 9 alasiri Uwanja wa Magomeni kata ya Kirumba.

Mwenyekiti Mbowe na mimi tutashiriki katika michakato hiyo.

Maslahi ya Umma Kwanza!!

Monday, August 12, 2013

Leo Agosti 13, 2013 Busega, Maswa, Meatu, na Bariadi; tukutane tushiriki mabaraza ya wazi ya katiba.

Leo Agosti 13, 2013 Busega, Maswa, Meatu, na Bariadi; ni kushiriki kikamilifu baraza la wazi la katiba. Mwenyekiti Mbowe na mimi tutajumuika nanyi kupitia rasimu ya katiba mpya.

Busega: Baraza la wazi la katiba leo litaanza saa 3 asubuhi.

Maswa: Wanachana na wapenzi hudhurieni baraza la wazi la katiba kuanzia saa 5 kamili

Meatu: mtaanza baraza la wazi la katiba saa 7 mchana. Wanachama na waalikwa mkifika anzeni kutoa maoni yenu juu ya rasimu; tuko pamoja!

Bariadi: ni haki na wajibu kushiriki baraza la wazi la katiba leo tarehe 13 Agosti kuanzia saa 9 alasiri.

Shime tushiriki kikamilifu na kuitumia fursa hii kwa maslahi ya taifa letu.

Thursday, August 8, 2013

Salamu za Eid-Al-Fitr na kutembelea kata ya Malamba Mawili!

Saa 5 mpaka 8 mchana nitakuwa pamoja na viongozi wenzangu Malamba Mawili (Eneo la Stendi Mwisho). Tutagawa zawadi kwa watoto pamoja na kutoa salamu za Eid-Al-Fitr. Tutasambaza nakala za rasimu ya katiba mpya vijiweni na kwa wawakilishi wa makundi ya kijamii yenye malengo yanayofanana.

Tunaanza muda huo ili kuheshimu wajib wa salaat ya Eid na sunnah ya khutbah asubuhi. Imekuwa ni kawaida kwa siku ya Eid kuwa pia ni wasaa kwa kusikiliza hotuba juu ya wajibu kwa Allah lakini pia kwa binadamu wengine. Ni wakati wa ummah kukumbushwa masuala muhimu katika jamii. Tunamaliza mapema kutoa fursa ya mikusanyiko mingine.

Nitazungumza na umma kuhusu mchakato wa katiba na kutoa pia mrejesho juu ya masuala ya maendeleo ikiwemo juu ya ujenzi/matengenezo ya Barabara ya Kinyerezi-Malamba Mawili Mbezi, kuhusu maji na juu ya masuala mengine muhimu ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Kwa wakazi wa maeneo jirani yanayozunguka Malamba Mawili ya Kifuru, King’azi, Msingwa, Msigani na mengineyo mnaweza kuja kujumuika nasi. 

Kwa maelezo zaidi na maelekezo naomba muwasiliane na Ali Makwilo 0715/0784691449.

Eid Mubarak!

Kwa mkazi wa Kisopwa, Sinza, Manzese, Mbezi Makabe, Malambamawili, Mshikamano au Msigani; naomba usome hapa na kunipa mrejesho juu ya ardhi na mipango miji

Tarehe 12 Julai 2012 katika mchango wangu bungeni ikiwa ni sehemu ya wajibu wa kuwawakilisha wananchi na kuisimamia Serikali niliitaka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na mambo mengine:

Itatue mgogoro kati ya Manispaa ya Kinondoni na Halmashauri ya Kisarawe kuhusu wananchi wa Kisopwa na Mloganzila kuitwa kwamba wako Kisarawe badala ya Kinondoni.

Ichukue hatua juu ya maeneo ya wazi/umma yaliyovamiwa katika kata ya Sinza ambapo mabango yamewekwa, muda wa notisi umeisha lakini majengo bado yapo.

Imtaje wazi mwendelezaji mwenza wa Mji wa kiungani (satellite town) wa Luguruni, masharti ya mkataba na lini uendelezaji unaanza.

Itoe nakala ya mipango ya uendelezaji upya kata ya Manzese.

Iharakishe mipango ya uhakiki na urasimamishaji katika maeneo ya Mbezi Makabe, Malamba Mawili, Mshikamano na Msigani.

Mwaka mmoja umepita, kuna mambo nimepewa na majibu na kazi imefanyika na kuna masuala bado.

Mkazi wa Mabibo na maeneo jirani nakutaarifu kuwa nitahutubia mkutano wa hadhara kwenye eneo la Sahara leo siku ya 8/8 kuanzia saa 9 alasiri mpaka 11 jioni ulioandaliwa na chama. Njoo na waalike na wengine.

Mkutano huo una malengo matatu: Mosi; kuwasilisha mrejesho wa kazi jimboni za utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyogharamiwa na Mfuko wa Jimbo katika maeneo yenu.

Pili; nitafanya kazi ya kuuchambua mchakato wa mabadiliko ya katiba unaoendelea ikiwemo kuhusu rasimu ya katiba mpya.

Tatu; kupokea maoni/mapendekezo ya masuala muhimu ya kuyazingatia katika kazi ya kuwawakilisha wananchi kwenye vikao vya kamati za Bunge vinavyoanza wiki ijayo na Mkutano wa Bunge unaoanza mwishoni mwa mwezi huu.

Itakumbukwa kwamba tarehe 21 Julai 2013 nilitaka kutimiza azma hiyo kwenye eneo tajwa lakini Jeshi la Polisi lilizuia mkutano kwa maelezo yasiyokuwa ya kweli kwamba kulikuwa na ziara ya Makamu wa Rais katika Jimbo la Ubungo.

(Msaidizi katika Ofisi yangu ameeleza hapa kwa kirefu: http://www.youtube.com/watch?v=VyHF5O-P-Vk&feature=c4-overview&list=UUs0TcFkgqs2OYd6x5E68nhg ).

Nitashiriki kwenye Iftar nyumbani kwa Marehemu Mbwana Masoud Makurumla leo 8/8 jioni; wasiliana na Aziz (OMU) 0784/0715-379542 kutuunga mkono kwa hali na mali. Ramadan Kareem.

Kwa ndugu zangu na wenzetu waislamu, ni siku ya 30 ya mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadan. Siku ya 30 ni kati ya siku kumi za mwisho za mfungo ambazo wapo wanaomini kwamba usiku ni siku ya “usiku wa nguvu”. Siku na usiku ambao Mtume Muhammad (SAS) alipokea ufunuo wa kwanza wa Q’uran yaani Laylat al-Qadr.

Katika siku hii ya 30 nitaungana pamoja na familia ya Marehemu Mbwana Masoud, majirani zake wakazi wa Kata ya Makurumla na wengine mtakaojumuika nami katika Iftar nyumbani kwa familia ya marehemu . Jioni tutaanza na tende na futari itafuata baada ya swala ya maghrib.

Marehemu Mbwana Masoud alikuwa ni mmoja wa wanachama wa CHADEMA walijitolea kusafiri kwenda Igunga kwa ajili ya kuwa wakala kwenye uchaguzi uliofanyika tarehe 2 Oktoba 2011.

Monday, July 29, 2013

Hali tete na tata ya kituo cha mabasi cha Ubungo (UBT)- Hatua ambazo nimeanza kuzichukua

Katika siku za karibuni nimepokea malalamiko kuhusu hali tete na tata katika Kituo cha Mabasi cha Ubungo (UBT) kinachosimamiwa na kuendeshwa na Halmashauri ya Jiji la Dar Es Salaam. 

Kufuatia malalamiko hayo, nimechukua hatua zifuatazo mpaka sasa: Mosi, tarehe 15 Julai 2013 nilifanya ziara ya ghafla kujionea hali halisi, sehemu ya ziara hiyo inaweza kutazamwa kupitia: 
http://www.youtube.com/watch?v=JuPGoz-JI-I , ambapo nilibaini kwamba hatua za haraka zinahitajika. 

Nimeshuhudia hali ya uchafu ikiwemo utiririkaji wa maji machafu ndani ya Kituo cha Mabasi ambayo yanatuama na hadi kubadilika rangi na kuwa ya kijani ambapo ni hatarishi kwa abiria na watu wanaofanya shughuli zao ndani ya kituo. Pia, kuna vyoo vichache ukilinganisha na idadi ya abiria na watumiaji wengine wa Kituo. Hali hiyo inaweza kusababisha magonjwa ya mlipuko.

Nimejulishwa hali ya usalama ndani ya kituo ni tete; usalama ndani ya kituo ni mdogo sana kwa abiria na nimepewa taarifa za matukio ya uhalifu ambayo yamesababisha pia madhara kwa abiria.

Nimetembelea kituo na kukuta kuna usumbufu mkubwa sana kwa abiria na watumiaji wengine wa Kituo baada ya maeneo ya awali ya kupumzikia kwa abiria na wasindikizaji kubomolewa. 

Thursday, July 25, 2013

Chenge (Mb) amesema kodi ya kadi za simu (SimCardTax) ni sahihi kwa utafiti wao; aulizwe kupitia 0754782577 atoe maelezo zaidi na vielelezo vya ziada

Leo tarehe 25 Julai 2013 chombo kimoja cha habari kimemnukuu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Andrew Chenge (Mb) akisema kwamba uamuzi kuhusu kodi/tozo ya kadi/laini za simu haukuwa wa kubahatisha. Chenge amesema kwamba kamati yake ilifanya utafiti wa kina na kisha kufikia uamuzi wa kuona tozo hiyo ni sahihi.

Ni muhimu akatakiwa kupitia namba yake 0754782577 atoe maelezo zaidi kuhusu usahihi wa tozo hiyo na aeleze ni wapi wananchi na wadau mbalimbali wanaweza kupata vielelezo vya utafiti walioufanya.

Aidha, wenye maswali kuhusu nini hasa kilijiri kwenye kamati ya bajeti mpaka kamati hiyo ikakataa jedwali la marekebisho nililowasilisha tarehe 27 Juni 2013 kabla ya muswada wa sheria ya fedha kupitishwa bungeni tareheb 28 Juni 2013 kwa kuwa yeye ambaye ndiye msemaji wa kamati ameanza kutoa majibu. 

Pia, aeleze iwapo yupo tayari kumshauri Spika aruhusu kamati ya bajeti ikutane kwa dharura wiki ijayo kufanya kazi ya kupitia matumizi ya Serikali kwa lengo la kuanisha maeneo ambayo Serikali inaweza kubana matumizi kwa haraka kufidia pengo la bilioni 178 zinazotafutwa kwenye tozo hiyo ya simu. Hatua hii itawezesha kodi hiyo kuacha kutozwa bila ya kulazimika hata kuongeza vyanzo vingine vya fedha iwapo Serikali inasuasua kupanua wigo wa mapato.

Friday, July 19, 2013

Kufuatia kauli za Serikali magazetini kuhusu mimi na kodi ya umiliki wa kadi za simu; nijibu tu kwa ujumla kwamba SITAACHA. Badala yake naomba kuwapatia namba zao: Makamba 0767783996 na Mgimwa 0754/0684765644, tunachohitaji ni kauli ya Serikali kuwa kodi imesitishwa na itaondolewa na sio siasa chafu.

Kwa mliotaka msimamo wangu juu ya kauli ilinukuliwa jana tarehe 18 Julai 2013 na Gazeti la Majira kwamba Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia Januari Makamba kwamba; “Mnyika anaangalia upepo unakoelekea, akiona watu wanalalamika ndipo anaongea namsihi aache kufanya siasa katika jambo hili”, naomba kutumia mtandao huu kutoa majibu ya ujumla kwa maswali na masuala yote kama ifuatavyo:

Nieleze kwamba sitaacha kufanya siasa kwenye jambo hili mpaka kodi hiyo itakapofutwa kuwawezesha wananchi wa kipato cha chini kubaki na fedha walau kidogo kwa maendeleo.

Sitaacha kufanya siasa kwa sababu ndio kazi yangu ambayo wananchi walinichagua kuifanya ya kuwawakilisha na kuisimamia Serikali ambayo yeye Makamba ni sehemu yake. Sitaacha kufanya siasa kwa sababu Mwalimu Nyerere alisema ili nchi yetu iendelee inahitaji watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora.

Ambacho sitafanya ni siasa chafu kama hizo ambazo Makamba amefanya za kusema uongo, kwa kuwa naamini anafahamu kabisa kwamba sijaanza kuongea kuhusu suala hili baada ya malalamiko ya wananchi bali jambo hili nilianza kulishughulikia bungeni mara baada ya Waziri wa Fedha kuwasilisha jedwali la marekebisho la kuanzisha kodi lukuki za simu ikiwemo hii. Katika mchango wangu bungeni, nieleza kwamba muswada huo wa sheria ya fedha kwa kupandisha kodi kwenye mafuta na simu ni ‘muswada wa majanga ya kuwaongezea mzigo wa gharama za maisha kwa wananchi.

Wednesday, July 17, 2013

Kodi ya kadi ya simu (SimcardTax): Maoni ya awali ya wananchi juu ya hatua za kuchukuliwa

Nawashukuru kwa maoni ambayo mmenitumia kuhusu hatua zinazopaswa kuchukuliwa kufuatia kuanzishwa kwa ushuru wa bidhaa kwa kadi za simu (sim card) kwa wamiliki wa simu za kiganjani/mkononi.

Bado naendelea kuchambua maelfu ya maoni yaliyotolewa katika mijadala na niliyotumiwa kwa barua pepe. Nitoe mrejesho wa awali kwamba kwa muktasari mapendekezo niliyoyachambua mpaka sasa yanapendekeza hatua zifuatazo kuchukuliwa:

Monday, July 15, 2013

Mnyika aponda sera za michezo za CCM

Na Mwandishi Wetu

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika amesema ukosefu wa maandalizi ya mapema katika micheo kunatokana na sera za Chama Cha Mapinduzi (CCM), ndiko kunakoibua matokeo mabovu katika sekta hiyo hususan kwa timu ya soka ya taifa, Taifa Stars.

Mnyika ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, aliyasema hayo jana wakati akizindua michuano ya Mama Kevin Cup kwenye viwanja vya Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Chang’ombe (DUCE), jijini Dar es Salaam.

Mnyika alisema katika ilani ya uchaguzi ya Chadema 2010, waliahidi masualaya michezo hususan Tanzania kucheza fainali za Mataifa ya Afrika na Kombe la Dunia Brazil mwakani endapo wangekabidhiwa cnchi, lakini kutokana na baadhi ya maeneo kutowataka waingie serikali mpya, hayo yameshindikana chini ya sera mbovu za CCM.

Saturday, July 13, 2013

Mkutano wa hadhara leo Julai 13, 2013 Dar es Salaam!

Msimamo wetu kuhusu rasimu ya katiba mpya na mustakabali wa taifa utatolewa leo Jumamosi ya Julai 13, 2013 kwenye mkutano wa hadhara katika viwanja vya Shule ya Ukombozi-Manzese kuanzia saa 8 mchana.

Hotuba zitatolewa na viongozi mbalimbali wakiwemo Dr.W.Slaa, T.Lissu, M.Marando nk nathibitisha nami nitakuwapo kuwakaribisha Jimboni Ubungo.

Wananchi wote mnakaribishwa. Njoo wewe, njoo na yule!

Mabadiliko ya Kweli, Uhuru wa Kweli!

Muhimu: Shule ipo jirani na Manzese TipTop. Maelekezo wasiliana na: M/Kt wa Kata ya Manzese Ali Makwilo 0784-691449 au 0715-691449 au 0769-658593

Thursday, July 11, 2013

KAULI YA WAZIRI WA FEDHA KUHUSU KODI YA LINE ZA SIMU NI KIELELEZO CHA UDHAIFU WA SERIKALI NA UZEMBE WA BUNGE; NIANDIKIE SASA KUHUSU HATUA ZA KUCHUKUA JUU YA SUALA HILI KUPUNGUZA MZIGO WA GHARAMA ZA MAISHA KWA WANANCHI

Katika kipindi cha Hot Mix cha EATV muda mfupi uliopita Waziri wa Fedha amesema kwamba mawazo ya kutoza elfu moja kwa mwezi kwenye kila laini ya simu ni ya wabunge. 

Kauli inayokaribiana na hiyo imewahi kuandikwa pia na Naibu Waziri wa Wizara yenye dhamana na sekta mawasiliano kwenye mitandao ya kijamii katika siku za karibuni. Baadaye alifuata Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha na sasa waziri mwenyewe. Mwaka 2012 nilitahadharisha kuhusu udhaifu wa Rais (na Serikali) na uzembe wa Bunge katika masuala yanayohusu maandalizi ya bajeti, hususan kutozingatiwa kwa mpango wa taifa wa maendeleo na ongezeko la mara kwa mara la gharama za maisha kwa wananchi. Kwa kauli hizi za Serikali udhaifu na uzembe huo unaendelea kujihidhirisha.

Kauli hizi za Serikali ni za kujivua mzigo wa lawama baada ya malalamiko ya wananchi kuhusu kodi hii na nyinginezo kwa kuhamisha mzigo huo kwa wabunge.

Ni muhimu badala ya kutoa kauli za ujumla za kulaumu wabunge, Serikali ijitokeze itaje kwa majina na wabunge gani hasa walitoa mawazo hayo. Mimi sijawahi kutoa wazo hilo wala kuliridhia. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwenye Hotuba yake juu ya Muswada wa Sheria ya Fedha ilipinga pendekezo hilo lililokuwepo katika jedwali la marekebisho lililowasilishwa na Wizara ya Fedha. Katika kuhakikisha kwamba kifungu hicho hakipitishwi, niliwasilisha jedwali la marekebisho ya sheria kutaka kifungu hicho kiondolewe katika muswada wa sheria ya fedha na marekebisho yake yaliyowasilishwa na Serikali.

Wednesday, May 22, 2013

Maoni na Mapendekezo ya CHADEMA juu ya Rasimu Muongozo uliotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuhusu Mabaraza ya Katiba ya Asasi, Taasisi na Makundi yenye mlengo yanayofanana


1.0. UTANGULIZI 

Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Sura ya 83 (kifungu cha 18 (3)) imetoa wajibu kwa tume wa kuunda Mabaraza ya Katiba kwa ajili ya kupitia na kutoa maoni juu ya Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume.

Kifungu cha 17 (8) kinaeleza kuwa, isipokuwa kama mazingira yatahitaji vinginevyo, Tume itabuni utaratibu unaofanana ambao utatumika kila upande wa Muungano. 

Kifungu cha 18 (6) kinaeleza aina nyingine ya Mabaraza ya Katiba kwa kueleza kuwa Tume inaweza kuruhusu Asasi, Taasisi au Makundi ya Watu kuwasilisha maoni yao kuhusu Rasimu ya Katiba. 

Ikumbukwe kwamba Kamati Maalum ya CHADEMA ilikutana na Tume ya Mabadiliko ya Katiba tarehe 7 Januari 2013 kuwasilisha maoni ya CHADEMA kuhusu katiba mpya kama ilivyoalikwa lakini pia kutumia fursa hiyo kuwasilisha mapendekezo ya CHADEMA kuhusu marekebisho na maboresho yanayohitajika kuhusu mchakato wa mabadiliko ya katiba ili kupata katiba bora. 

Tarehe 31 Januari 2013 Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilitoa taarifa kwamba imeamua kuwa Mabaraza ya Katiba yatakuwa katika makundi mawili yafuatayo: Mabaraza ambayo Tume itayasimamia na kukusanya Maoni (Mabaraza ya Katiba ya Wilaya – Ngazi ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa) na Mabaraza ambayo Tume haitayasimamia. Mabaraza hayo yatajisimamia yenyewe na kukusanya maoni yatakayowasilishwa kwenye Tume kwa mujibu wa maelekezo. (Mabaraza ya Katiba ya Asasi, Taasisi na Makundi ya Watu). 

CHADEMA baada ya kupitia muongozo huo na kwa kuzingatia kuwa tayari tume ilishafanya uamuzi kuwa mabaraza ya katiba yatakuwa ya wilaya, tarehe 14 Februari 2013 kiliwasilisha maoni na mapendekezo yake kuhusu uteuzi wa wajumbe ambayo kwa sehemu kubwa hayakuzingatiwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na hivyo kusababisha matatizo makubwa katika mchakato mzima wa uteuzi wa mabaraza ya katiba ya wilaya. 

Kufuatia hali hiyo katika Maoni ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusu hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tulitangaza kwamba CHADEMA itajitoa ushiriki wake katika mchakato wa Katiba Mpya endapo mambo yafuatayo hayatapatiwa ufumbuzi hadi kufikia tarehe 30 Aprili, 2013: 

HOTUBA YA MSEMAJI WA KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI WIZARA YA NISHATI NA MADINI JOHN JOHN MNYIKA (MB) KUHUSU MAONI YA KAMBI RASMI YA UPINZANI JUU YA MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA MWAKA 2012/2013 NA MAKADIRIO YA MATUMIZI YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014

(Inatolewa chini ya kanuni ya 99(9) toleo la mwaka 2013)


A: UTANGULIZI

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Waziri wa Nishati na Madini ilianzishwa kwa mujibu wa kipengele cha 21 cha Nyongeza ya Waraka wa Rais uliochapishwa kama Tangazo la Serikali Na. 494 la tarehe 17 Desemba 2010. Majukumu ya Ofisi hii yameainishwa katika Tangazo la Ukasimishaji wa Majukumu ya Kiuwaziri la mwaka 2010 (The Ministers [Assignment of Ministerial Functions] Notice, 2010) lililochapishwa katika Gazeti la Serikali kama Tangazo la Serikali Na. 494A la tarehe 17 Desemba 2010.

Mheshimiwa Spika, Katika kujadili Mapitio ya Utekelezaji kwa mwaka wa fedha 2012/2013 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2013/2014 naomba tuyatafakari maandiko ya katika muktadha wa uongozi wetu wa leo na hatma ya sekta hizi mbili muhimu za nishati na madini.

Mheshimiwa Spika, Mwalimu Nyerere katika kitabu chake cha TUJISAHIHISHE katika ukurasa wa pili tutafakari kwamba, naomba kumnukuu ‘ukweli una tabia moja nzuri sana. Haujali mkubwa wala mdogo; haujali adui wala rafiki. Kwake wote ni sawa. Pia ukweli unayo tabia ya kujilipiza kisasi kama ukipuuzwa.Ukiniona nataka kulipiga teke jiwe kwa kuwa nafikiri kuwa ni dongo au mpira, natumaini utanionya. Lakini nikilipuuza onyo lako kwa sababu eti wewe ni mdogo au kwa sababu sikupendi, nitalipiga teke, basi litanivunja dole japo ningekuwa nani. Ukweli haupendi kupuuzwapuuzwa.


Mheshimiwa Spika, Tuendelee kutafakari maandiko ya Nyerere kwamba ‘Wakati mwingine, mtu tunayempinga huwa anamakosa kweli, lakini hoja tunazozitoa ni za kinafsi na hazihusiani kabisa na hoja zake.Nikisema mbili na tatu ni sita, nakosa. Lakini ni bora kunionyesha kwamba pengine nilifikiri tunazidisha kumbe tunajumlisha.Ni kweli mbili mara tatu ni sita;lakini mbili na tatu ni tano, siyo sita. Lakini ukijaribu kuwashawishi wenzetu wakatae mawazo yangu na kukubali yako kwa kusema kuwa meno yangu ni machafu ,au natoa kamasi daima, utakuwa unatumia hoja ambazo hazina maana, Huu ni mfano wa upuuzi; lakini mara nyingi hoja tunazozitumia kuwashawishi watu wakatae mawazo ya wale tusiowapenda,au kukubali mawazo yetu, huwa hazihusiani kabisa na mambo tunayojadili’.

Sunday, May 19, 2013

Waraka kuhusu muswada wa Baraza la Vijana la Taifa wa Mwaka 2013

Vijana wenzangu na wote wenye dhamira ya kuwezesha maendeleo ya vijana nchini, salaam! 

Mtakumbuka kwamba mwezi Januari 2013 nilitoa taarifa kwa umma ya kueleza kuwa niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge Muswada Binafsi wa Sheria ya Baraza la Vijana la Taifa na kuomba hatua za ziada toka ofisi ya Bunge kwa kuzingatia Kanuni ya 21 na Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za Bunge. 

Toka wakati huo muswada huo mpaka sasa Mei 2013 haujachapwa katika gazeti la Serikali na nimepokea barua toka kwa ofisi ya Bunge kwamba wamepokea ushauri toka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwa muswada huo hauwezi kuchapishwa katika gazeti la Serikali kwa kuwa umekiuka masharti ya ibara ya 99 ya Katiba ya Nchi. 

Sababu ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutoa ushauri huo ni kuwa muswada unalenga pamoja na mambo mengine kupitia kifungu cha 31 kipengele cha kwanza kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwa madhumuni ya kugharamia shughuli za baraza la vijana la taifa, mipango ya baraza na kutekeleza miradi ya vijana kwa ajili ya maendeleo ya vijana. 

Kwa maoni yangu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ametoa ushauri huo bila kuzingatia kwamba kifungu cha 31 kipengele cha pili kinataja vyanzo mbalimbali vya fedha za mfuko ikiwemo kutaja kuwa fedha za mfuko zitatokana na fedha zilizotengwa na Serikali na Bunge kwa ajili ya Baraza kwa mujibu wa Ibara ya 135 kifungu cha pili cha katiba ya Nchi.

Monday, March 25, 2013

Mnyika na harakati za kuhakikisha Maji ndani ya Jimbo la Ubungo

21 Machi, 2013 Mnyika aitwa Ikulu, JK awakumbuka Mabwepande
na Asha Bani

HOJA ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA) kuhusiana na suala la tatizo la upatikanaji wa maji katika Mkoa wa Dar es Salaam, inaelekea kupata ufumbuzi kutokana na Rais Jakaya Kikwete kumuita Ikulu mbunge huyo Jumatatu wiki ijayo.

Wengine walioitwa kukutana na rais ni Mkuu wa Mkoa, Mecky Sadick, wakuu wote wa wilaya pamoja na wabunge na wataalamu kutoka Wizara ya Maji.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika uzinduzi wa daraja la Mtaa wa Golani, Kata ya Saranga, Rais Kikwete alisema kuwa kutokana na wananchi wa kata hiyo kupiga kelele kuhusiana na suala la maji ameamua kukutana na viongozi hao ili kupatiwa ufumbuzi.

Mwaliko wa kushiriki ufuatiliaji wa mradi wa maji na mkutano wa mbunge na wananchi katika kilele cha wiki ya maji kitaifa na siku ya maji kimataifa leo tarehe 22 Machi Mtaa wa Makoka kata ya Makuburi.

Leo tarehe 22 Machi ni kilele cha wiki ya maji kitaifa na siku ya kimataifa ya maji. Katika kazi zake ikiwa ni sehemu ya siku hiyo Mbunge wa Ubungo John Mnyika saa 9 alasiri atakuwepo eneo la Uluguruni Mtaa wa Makoka Kata ya Makuburi kufanya ufuatiliaji wa mradi wa maji.

Mradi umetekelezwa kwa ushirikiano na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) baada ya kuchochewa kwa kuchangiwa milioni kumi na Mfuko wa Maendeleo (CDCF) Jimbo la Ubungo ambao Mnyika ni mwenyekiti wake pamoja na kuunganisha nguvu za wananchi katika maeneo husika.

Aidha, baada ya kukagua mradi huo kuanzia saa 10 Jioni mbunge atafanya mkutano na wananchi kwa ajili ya kutoa ujumbe kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jiji la Dar Es Salaam zinazopaswa kuchukuliwa hata baada ya wiki ya maji.

Pia kufuatia mwaliko wa Rais Jakaya Kikwete wakukutana tarehe 25 Machi 2013 na Mkuu wa Mkoa, DAWASA, DAWASCO, Mnyika na wabunge wengine wa Mkoa wa Dar es Salaam kujadili hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji, mbunge atatumia mkutano wake na wananchi kusikiliza maoni na mapendekezo kuhusu hatua za ziada zinazopaswa kuchukuliwa.

Imetolewa tarehe 22 Machi 2013 na: 

Gaston Shundo 

Afisa katika Ofisi ya Mbunge Ubungo

Picha za Uzinduzi wa Daraja la Suka-Golani!

















Tujikumbushe harakati na jitihada mbalimbali ambazo zilifanywa mpaka kufikia hatua ya sasa kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora ya miundombinu ya barabara ya Suka-Golani hapa:

1 May, 2012  Daraja Golani-Suca na Barabara Mburahati-Mabibo

Mkandarasi aliyepewa zabuni ya ujenzi wa daraja la Golani-Suka anapaswa kuanza mapema ujenzi wa daraja hilo muhimu linalounganisha kata za Kimara na Saranga ili kupunguza kero kwa wananchi hasa wakati wa mvua.

Mwezi huu wa Aprili nimefuatilia kuhusu hatma ya daraja hilo na hatimaye mkataba wa ujenzi wa daraja husika umesainiwa kati ya Manispaa ya Kinondoni na Mkandarasi Kika Co. Ltd kwa gharama za shilingi milioni 447.

Hata hivyo, ujenzi wa daraja husika haujaanza suala ambalo linahitaji Manispaa ya Kinondoni kumsimamia kwa karibu mkandarasi husika ili ujenzi uanze kwa haraka kwa kuwa mchakato wa zabuni ulianza kuanzia mwanzoni mwa mwaka 2012.

Izingatiwe kwamba kutokuwepo kwa daraja katika eneo hilo mwaka miaka mingi kumefanya mawasiliano katikati maeneo hayo kuwa magumu nyakati za mvua na kusababisha madhara ya kibinadamu na mali wananchi wanapovuka mto katika eneo hilo wakati wa mafuriko.

Baada ya kuwawakilisha wananchi kutaka ujenzi wa daraja hilo lilingizwa kwenye bajeti ya Manispaa ya Kinondoni kwa mwaka wa fedha 2011/2012 hata hivyo miezi ikiwa imebaki takribani miwili kabla ya mwisho wa bajeti husika ujenzi wa daraja hilo ulikuwa haujaanza bado.

Hatua kama hiyo inahitajika pia kwa barabara ya Mburahati mpaka Mabibo NIT ambayo inapaswa kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami ikiwa imetengewa kiasi cha shilingi milioni 504 kwa ajili ya kuchangia katika kupunguza msongamano wa magari katika barabara ya Morogoro . 

Tathmini ya utekelezaji wa bajeti inaonyesha kwamba kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ni ndogo pengo ambalo linapaswa kuzibwa kwa kusimamia kwa karibu miradi inayopaswa kuanza katika muhula uliobaki wa mwaka wa fedha 2011/2012.

Rejea: http://mnyika.blogspot.com/2012/05/daraja-golani-suca-na-barabara.html 


January 27, 2012 Kuhusu Msongamano wa Magari DSM na Ziara Kwembe: http://mnyika.blogspot.com/2012/01/kuhusu-msongamano-wa-magari-dsm-na.html

Thursday, March 21, 2013

MNYIKA ATAKA KAULI YA RAIS KIKWETE KUHUSU UJENZI WA MACHINGA COMPLEX NA JUMBA LA VIWANDA VIDOGO JIMBONI UBUNGO

Mbunge wa Jimbo la Ubungo John Mnyika ametoa mwito kwa Rais Jakaya Kikwete kueleza sababu za kutokutekelezwa mpaka sasa kwa ahadi zake alizotoa mwaka 2010 za ujenzi wa Machinga Complex na jumba la viwanda vidogo katika jimbo hilo kuchangia katika kupanua wigo wa ajira kwa vijana. 

Mnyika aliyasema hayo akijibu swali la mwakilishi wa vijana katika mkutano wake na wananchi alioufanya katika ofisi za Serikali ya Mtaa wa Muungano katika kata ya Manzese uliofanyika mwishoni mwa wiki (16/03/2013). 

Mwakilishi huyo wa vijana alitaka kufahamu hatua ambazo mbunge amechukua kufuatilia kuhusu maeneo ya kufanyia biashara kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo katika jimbo la Ubungo. 

“Kazi ya mbunge ni kuwawakilisha wananchi na kuisimamia serikali ili kuwezesha utatuzi wa kero, matatizo ya maeneo ya wafanyabiashara ndogo ndogo yamedumu kwa muda mrefu kutokana na udhaifu katika mipango miji na hivyo maeneo ya wafanyabiashara na masoko kuuzwa, kuvamiwa au kuwa machache. Nimefuatilia suala hili, kuna ambao wamepata maeneo na wengine wengi bado”, alijibu Mnyika.

Wednesday, March 20, 2013

RUFAA DHIDI AGIZO LA ACP CHARLES KENYELA KAMANDA WA POLISI WA MKOA WA KIPOLISI WA KINONDONI KUZUIA MKUTANO WA HADHARA WA MBUNGE NA WANANCHI TAREHE 16 MACHI 2013



Kumb. Na. OMU/US/003/2013                                                                                               18/03/2013 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,
S.L.P 9223, 
Dar es Salaam. 

Mheshimiwa: 


RUFAA DHIDI AGIZO LA ACP CHARLES KENYELA KAMANDA WA POLISI WA MKOA WA KIPOLISI WA KINONDONI KUZUIA MKUTANO WA HADHARA WA MBUNGE NA WANANCHI TAREHE 16 MACHI 2013 


Kwa barua hii nawasilisha rasmi rufaa kwa kutumia kifungu cha 43 (6) cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma za Polisi wasaidizi sura ya 322 (The Police Force and Auxilliary Service Act Cap 322 RE 2002) dhidi ya agizo la ACP Charles Kenyela Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni kuzuia mkutano wa hadhara wa mbunge na wananchi tarehe 16 Machi 2013. 

Katika kushughulikia rufaa hii zingatia kuwa tarehe 4 Machi 2013 niliwasilisha taarifa kwake kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha Sheria ya Kinga, Madaraka na Haki za Bunge na. 3 ya mwaka 1988 (The Parliamentary Immunities, Powers and Privileges Act) kuwa tarehe 16 Machi 2013 nilipanga kufanya mkutano na wananchi Jimboni. 

Katika taarifa hiyo kupitia barua yangu yenye Kumbu. Na. OMU/US/001/2013 ambayo nilitoa pia nakala kwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Afisa Tawala wa Wilaya ya Kinondoni, Afisa Mtendaji wa Kata ya Manzese na Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Muungano, nilieleza kwamba mkutano huo nilipanga kuufanya katika Kata ya Manzese Eneo la Bakheresa kuanzia saa 3 asubuhi mpaka saa 5 Asubuhi. 

Katika taarifa hiyo nilieleza kwamba lengo la mkutano huo ni kuwapa mrejesho wananchi kuhusu masuala niliyoyawasilisha katika Mkutano wa Kumi wa Bunge uliomalizika tarehe 08 Februari 2013 na kupokea mambo ya kuyazingatia kuelekea Mkutano wa Kumi Na Moja wa Bunge unaotarajiwa kuanza tarehe 9 Aprili 2013. 

Hata hivyo, kupitia mkutano wake na vyombo vya habari tarehe 14 Machi 2013 na barua yake iliyoletwa ofisini kwangu tarehe 15 Machi 2013, ACP Charles Kenyela Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni alitoa agizo la kuzuia mkutano wa hadhara wa mbunge na wananchi niliopanga kuufanya tarehe 16 Machi 2013. 

Katika agizo hilo alilolitoa chini ya kifungu cha 43 (2) na 43 (3) Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma za Polisi sababu iliyohusu mkutano kwa mujibu wa barua yake yenye Kumb. Na. DSM/KINONDONI/SO.7/2/CHADEMA/284 ni: 

“Eneo la Manzese Bakhresa ambalo unakusudia kufanyia mkutano siyo eneo halali kwa ajili ya mikutano. Eneo hilo kwa mujibu wa maelekezo ya Manispaa ya Kinondoni kupitia mipango miji ni eneo linalotumika kwa ajili ya kuegesha magari makubwa (malori) na ndio maana liko katika eneo kuu la barabara ya Morogoro ambayo iko katika matengenezo. Kuruhusu mkutano wako kufanyikia hapo ni kukiuka sheria ya mipango miji ya Manispaa ya Kinondoni pamoja na kuingilia shughuli za ujenzi wa barabara unaoendelea hivi sasa na kuwabugudhi watumiaji wengine wa eneo hilo”.

Tuesday, March 19, 2013

LEO NDIO MWISHO; OMBA UWAKILISHI KWENYE MABARAZA YA KATIBA SASA

Leo tarehe 20 Machi 2013 ni siku ya mwisho ya wananchi kuwasilisha maombi ya kuwa wajumbe wa mabaraza ya katiba ya ngazi ya wilaya ambayo yana wajibu muhimu wa kupitia rasimu ya katiba na kutoa maoni iwapo imezingatia maoni ya wananchi yaliyokunywa katika hatua ya wananchi binafsi na makundi mbalimbali katika jamii. 

Nawakumbusha ambao bado hamjawasilisha maombi na mna dhamira ya kutimiza wajibu huu wa kiraia na kikatiba kwa kuwasilisha barua ya maombi kwa watendaji wa mitaa/vijiji. 

Kuna nafasi nane kwa kila mtaa kwa Dar es salaam, nne kwa maeneo mengine ya Tanzania Bara katika makundi yafuatayo; mwanamke, kijana, mtu mzima na mtu mwingine yoyote: kwa Zanzibar tatu kwa kila shehiya. 

Sifa ni raia, miaka 18 au zaidi mwenye kujua kusoma, kuandika, hekima, busara, uadilifu, uwezo wa kujieleza na kupambanua mambo ambao najua wengi mnazo. Sifa nyingine ni kuwa mkazi wa kudumu kwenye mtaa au kijiji ambayo haimaanishi kwamba ni lazima uwe mwenye nyumba, hata wapangaji mnaruhusiwa kuomba. Sio lazima uwe mwanachama wa chama chochote cha siasa na uteuzi wa awali utafanywa na mkutano mkuu wa mtaa wenu au kijiji chenu ambao wajumbe ni wakazi wote wa mtaa/kijiji husika. 

Tuesday, March 5, 2013

TUTAFANYA MAANDAMANO KWENDA WIZARA YA MAJI TAREHE 16 MACHI 2013; NIMESHAWASILISHA NOTISI, TUENDELEE NA MAANDALIZI

Tarehe 16 Machi 2013 nitaongoza maandamano ya amani ya wananchi kwenda kwa Waziri wa Maji kusimamia uwajibikaji kuwezesha hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es salaam.

Wote mlioshiriki mkutano wa tarehe 10 Februari 2013 (Kwa wale ambao hamkushiriki mnaweza kutazama video hii: http://www.youtube.com/watch?feature=player_embedded&v=O0txSoHqfGY ) , mtakumbuka tulimpa wiki mbili Waziri kujitokeza kwa wananchi kujibu hoja alizokwepa kujibu bungeni.

Tutakusanyika kata ya Manzese eneo la Bakhresa (jirani na daraja) saa 5 asubuhi na tutapita barabara ya Morogoro kuelekea kata ya Ubungo zilipo ofisi za Wizara ya Maji kufuatilia majibu ya ukweli na ukamilifu kuhusu hatua tisa za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka nilizopendekeza kwa niaba ya wananchi bungeni kupitia hoja binafsi na masuala mengine ambayo wananchi watataka yatolewe majibu siku hiyo.

Kila mmoja anaweza kuendelea na maandalizi ya kushiriki kwa kuwa tayari tarehe 4 Machi 2013 nimewasilisha notisi kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni na Maafisa wa Polisi Wasimamizi wa Maeneo kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 43 cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma Saidizi Sura ya 322 (The Police Force and Auxiliary Service Act, Chapter 322).

Sunday, March 3, 2013

WAZIRI MKUU PINDA AINGILIE KATI; WIZARA NA TANESCO HAWAJAJIBU UKWELI KUHUSU MGAWO WA DHARURA WA UMEME

Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kwa nyakati mbalimbali kati ya tarehe 28 Februari na 2 Machi 2013 kupitia baadhi ya vyombo vya habari wametoa majibu yasiyokuwa ya kweli juu ya mgawo wa dharura wa umeme uliotokea mwezi wa Februari. 

Katibu Mkuu wa Wizara Eliackim Maswi na Afisa Habari wa TANESCO Badra Masoud wote wameeleza kwamba hakukuwa na mgawo wa umeme bali kilichotokea ni matatizo madogo madogo ya mitambo na kwamba matengenezo yanaendelea. 

Kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini ninazo taarifa kwamba ukweli ni kuwa umetokea mgawo wa umeme wa dharura kutokana na upungufu zaidi wa kina cha maji katika mabwawa ya kufua umeme, upungufu wa fedha za kununua mafuta mazito ya kuendesha mitambo ya kufua umeme wa dharura na upungufu wa gesi asili ya kuendeshea mitambo ya kufua ya umeme. 

Hivyo, Waziri Mkuu Mizengo Pinda anapaswa kuingilia kati kuwaeleza ukweli wananchi ikiwemo hatua zilizochukuliwa kuhakikisha kwamba hali hiyo haiendelei mwezi Machi kinyume na ahadi iliyotolewa bungeni tarehe 28 Julai 2012 kwamba mgawo wa umeme ungekuwa historia. 

John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini 

02 Machi 2013

Saturday, March 2, 2013

WANANCHI OMBENI UJUMBE WA MABARAZA YA KATIBA LAKINI PINGENI ‘MIANYA YA UCHAKACHUAJI’ WA UTEUZI KWENYE KATA ILIYOWEKWA NA MUONGOZO ULIOTOLEWA NA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA BILA KUZINGATIA MAONI YA WADAU

Mwongozo kuhusu Muundo, Utaratibu wa kuwapata wajumbe wa mabaraza ya Katiba ya Wilaya (Mamlaka za Serikali za Mitaa) na uendeshaji wake uliotangazwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba haujazingatia maoni ya msingi yaliyotolewa na wadau mbalimbali ikiwemo Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). 

CHADEMA inawatahadharisha wananchi kuhusu ‘mianya ya uchakachuaji’ iliyotolewa na muongozo huo kwa kuzingatia kuwa ‘uchakachuaji’ wa uteuzi wa wajumbe wa mabaraza ya katiba, ni ‘uchakachuaji’ wa utoaji maoni kwenye mabaraza ya katiba, ambayo ni hatua ya awali ya ‘uchakachuaji’ wa rasimu ya katiba. 

Kwa mujibu wa Muongozo huo, ‘mianya ya uchakachuaji’ imeachwa kwenye ngazi ya kamati ya maendeleo ya kata ambayo wajumbe wake ni madiwani na wenyeviti wa mitaa/vijiji ambao kwa mujibu wa matokeo ya chaguzi za mwaka 2009 na 2010 kuna hodhi kwenye vikao hivyo ya chama kimoja (CCM).

Friday, March 1, 2013

RUFAA DHIDI YA UENDESHAJI WA BUNGE USIOKUWA WA HAKI NA UKIUKAJI WA KANUNI WA NAIBU SPIKA JOB NDUGAI KATIKA KUONDOA HOJA BINAFSI YA MAJI

Tarehe 28 Februari 2013 nimewasilisha rasmi rufaa kwa mujibu wa Kanuni ya 5 (4) dhidi ya uendeshaji wa Bunge usiokuwa wa haki wa Naibu Spika Job Ndugai kwa kukiuka kanuni ya 58 (5) kwa kulihoji bunge kinyume na kanuni kufanya uamuzi badili wa kuondoa hoja binafsi kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jiji la Dar es salaam.

Nimefanya hivyo baada ya kupata kumbukumbu rasmi ya Bunge (Hansard) za kikao cha tano cha tarehe 4 Februari 2013 cha mkutano wa kumi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katika Mkutano huo Naibu Spika Job Ndugai alisema na kufanya maamuzi kwamba: “Sasa ninahoji wanaoafiki kwamba hoja hii iondolewe waseme ndiyo…..hoja imeondolewa. Walioafiki Wameshinda”; wakati mtoa hoja sikuwa nimeomba idhini yoyote ya hoja yangu kuondolewa.

Maamuzi hayo ni kinyume na Kanuni ya 58 Fasili 5 ambayo inaelekeza kwamba “Endapo hoja imefikishwa Bungeni, mtoa hoja anaweza tu kuiondoa hoja yake kwa kusimama mahali pake na kusema ‘Ninaomba ruhusa kuondoa hoja’ na papo hapo Spika ataliuliza Bunge kama linaafiki hoja hiyo kuondolewa na inapotokea Wabunge walio wengi watakubali, Spika atasema ‘hoja hiyo inaondolewa kwa idhini ya Bunge’ na hoja hiyo itakuwa imeondolewa na Bunge litaendelea na shughuli inayofuata”.

Ushahidi wa Kumbukumbu Rasmi za Bunge (Hansard) za kikao tajwa unathibitisha ukiukwaji huo wa kanuni kama ifuatavyo:

Wednesday, February 27, 2013

NCHI IMEINGIA TENA KWENYE MGAWO WA UMEME, SERIKALI IELEZE WANANCHI UKWELI NA HATUA KUHUSU UDHAIFU KWENYE UTEKELEZAJI WA MPANGO WA DHARURA

Nchi imeingia tena katika mgawo wa umeme kinyume na ahadi iliyotolewa na Waziri wa Nishati na Madini Prof Sospeter Muhongo bungeni tarehe 28 Julai 2012. 

Hali hiyo ni matokeo ya Serikali kutozingatia tahadhari niliyoitoa bungeni tarehe 27 Julai 2012 kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani na kwa nyakati mbalimbali kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini juu ya hali tete iliyotarajiwa kuwepo na hatua zinazopaswa kuchukuliwa katika utekelezaji wa mpango wa dharura wa umeme. 

Ikiwa ni sehemu ya wajibu wa kibunge wa kuisimamia Serikali nawataka viongozi na watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kuacha kuficha hali ya mambo na kuwaeleza ukweli wananchi kuhusu mgawo wa umeme uliojitokeza na hatua za haraka zinazochukuliwa kurekebisha hali hiyo. 

Iwapo Wizara na TANESCO hawatatoa matangazo ya ukweli kwa wananchi, kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini nitaeleza vyanzo vya mgawo wa umeme uliojitokeza ili hatua ziweze kuchukuliwa wakati huu ambapo wajumbe wa kamati ya nishati na madini wenye wajibu wa kuisimamia Serikali kwa niaba ya Bunge katika sekta hizo nyeti hawajateuliwa.

Monday, February 25, 2013

Mnyika amuweka Maghembe kitanzini

NA RICHARD MAKORE

Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, amemuweka katika wakati mgumu Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, baada ya kutoa hadharani namba ya simu ya waziri huyo ili wananchi wamuulize ni lini atatekeleza ahadi ya kuwapatia huduma ya maji wananchi wa jimbo hilo.

Mnyika alitoa namba ya simu ya Profesa Maghembe na Naibu wake, Dk. Binillith Mahenge, wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika viwanja vya Goba mwisho na kuwataka wananchi kuwauliza viongozi hao wakuu wa Wizara ya Maji ni lini watapatiwa huduma ya maji ambayo imekosekana kwa zaidi ya miaka miwili sasa.

Mnyika alisema Profesa Maghembe akihututubia wananchi hao aliwapa namba ya simu ‘feki’ na kwamba alifanya hivyo kutokana na kuwadharau.

Februari 17 mwaka huu, Profesa Maghembe akihutubia mkutano wa hadhara eneo la Goba mwisho alikaririwa akisema kwamba huduma ya maji ingeanza kupatikana Februari 20, mwaka huu, lakini hadi kufikia juzi ahadi hiyo haijatekelezwa.

Profesa Maghembe alikaririwa akisema serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndiyo ina funguo za kufungua maji ama kuyafunga na kuwataka wananchi wa Kata ya Goba kumuamini kwamba Februari 20, mwaka huu wangepata maji.

Mnyika alisema ni aibu kwa Waziri akiwa na viongozi wa kitaifa wa CCM kutoa ahadi hewa na kwamba ataongoza maandamano makubwa ya wananchi wa jimbo lake kuvamia ofisi za Profesa Maghembe kwenda kudai maji.

Sunday, February 24, 2013

UFUMBUZI WA MADAI YA FIDIA MILIONI 278 KWENYE UJENZI WA BARABARA NA DARAJA GOLANI SUCA

Tarehe 19 Februari 2013 Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alifanya ziara ya kikazi katika kata za Kimara na Saranga kufuatilia kuhusu matengenezo ya barabara na daraja la Golani. 

Mnyika alifanya hivyo siku mbili tangu afanye mkutano wa kikazi na viongozi wa Serikali ya Mtaa wa Kanuni na wananchi katika kata ya Mabibo tarehe 16 Februari 2013 kulitolewa malalamiko kuhusu Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) kutoshughulikia maombi ya wananchi yaliyowasilishwa kwa kampuni hiyo kwa nyakati mbalimbali kati ya mwaka 2010 mpaka 2012. 

Ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji huo kuhusu barabara, Mnyika alikutana na wananchi ambapo walipaswa kulipwa fidia inayokadiriwa kufikia shilingi milioni 278 ili kuruhusu njia mbadala kupatikana kufuatia ujenzi wa daraja katika eneo hilo. 

Aidha, Mbunge amekagua matumizi ya daraja hilo yaliyoanza kupitia njia ya zamani na athari zake katika mfumo mzima wa usafiri katika eneo husika; na kubaini kwamba daraja husika haliwezi kuzinduliwa pamoja na kuwa limeanza kukamilika mpaka ujenzi wa kingo za mito ukamilike pamoja na kupatikana kwa barabara mbadala baada ya wananchi kulipwa fidia. 

Mara baada ya ziara hiyo Mbunge alikutana na uongozi wa Manispaa ya Kinondoni na kuwasilisha madai hayo ya wananchi ambao miezi zaidi ya sita imepita toka nyumba zao ziwekewe X bila hata ya kufanyiwa tathmini. Baada ya Mnyika kuwawakilisha wananchi hao uongozi wa Manispaa umeamua kutuma timu ya uthamini na mara baada ya uthamini huo, kutuma uongozi kukamilisha majadiliano na wananchi husika kabla ya tarehe 25 Februari 2013

Saturday, February 23, 2013

Ziara Kimara: Ukaguzi ulipaji fidia, upanuzi wa barabara na kuhakiki ujenzi wa daraja!


Mbunge wa Ubungo, John Mnyika akizungumza na mkazi wa Kimara Korogwe, Richard Paul wakati mbunge huyo alipokutana na wakazi hao kutaka kujua fidia wanazotaka kulipwa kutokana na upanuzi wa barabara, pia alitembelea ujenzi wa daraja katika eneo hilo. 



Tuesday, February 19, 2013

BAADA YA HOJA BINAFSI NA KUSUDIO LA MAANDAMANO; WAZIRI WA MAJI NA MKUU WA WILAYA WAENDA GOBA NA MAENEO MENGINE KUFUATILIA MIRADI YA MAJI

Nitafuatilia ahadi alizotoa Waziri wa Maji Prof. Jumanne Maghembe tarehe 17 Februari 2013 kuwa maji yataanza kutoka kata ya Goba tarehe 20 Februari 2013 na ziara ya Mkuu wa Wilaya Jordan Rugimbana kwenye kata hiyo. 

Hata hivyo, ni vizuri umma ukatambua kuwa pamoja na mabadiliko ya hoja kwa kuongeza maneno ya kupendekeza hoja kuondolewa yaliyofanywa na Waziri wa Maji Prof. Jumanne Maghembe kinyume na kanuni za Bunge tarehe 4 Februari 2013, maelezo na hoja binafsi niliyowasilisha bungeni yameongeza uwajibikaji wa Waziri wa Maji, Mkuu wa wilaya ya Kinondoni na Halmashauri kuhusu masuala ya maji. 

Siku chache baada ya kutangaza tarehe 10 Februari 2013 kwenye mkutano wa hadhara kuipa Serikali wiki mbili, Mkuu wa Wilaya na Meya wa Halmashauri ya Kinondoni waliitisha mkutano na viongozi wa mitaa pamoja na kamati za miradi ya maji ya jumuiya na leo tarehe 18 Februari 2013 Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Jordan Rugimbana ameanza ziara ya ufuatiliaji wa miradi ya maji katika Jimbo la Ubungo. 

Sunday, February 17, 2013

HALI TETE YA UPATIKANAJI WA MAJI JIJINI DSM; DAWASA NA DAWASCO WAWAJIBISHWE

Kwa nyakati mbalimbali kuanzia mwezi Januari mpaka Februari 2013 pametokea matatizo ya kuharibika kwa baadhi ya mitambo na kupungua kwa uzalishaji wa maji katika vyanzo vya mto Ruvu na hivyo kusababisha matatizo ya maji kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam na maeneo yanayohudumiwa na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) katika Mkoa wa Pwani. 

DAWASA imeingia mkataba wa uendeshaji na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO) wa kutekeleza majukumu mbalimbali ikiwemo kuendesha mitambo, kusimamia usambazaji wa maji na kufanya matengenezo na kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu huduma zinazotolewa. Aidha, DAWASCO wanapaswa kuzingatia mikataba ya huduma kwa wateja ambayo inaitaka kutoa taarifa kwa umma pale kunapotokea matatizo ya maji. 

Kwa kuzingatia mikataba hiyo, DAWASA na DAWASCO wanapaswa kutoa matangazo kwa umma kuhusu matatizo mapya yaliyojitokeza mwezi Januari na Februari 2013 ili kuepusha matatizo hayo kuhusishwa na hatua ya kuwasilishwa na kuondolewa bungeni kwa hoja binafsi niliyoiwasilisha tarehe 4 Februari 2013 juu ya hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam. 

Kwa wakazi wa Kibamba, Kwembe, Msigani, Mbezi, Saranga na Kimara ni muhimu wakatambua kwamba nimefuatilia na kujulishwa kwamba palikuwa na tatizo la kupungua kwa uzalishaji wa maji katika chanzo cha Ruvu Juu ambalo limerekebishwa tarehe 12 Februari 2013 hivyo maji yataendelea kupatikana kwa mujibu wa ratiba ya mgawo kama ilivyokuwa awali katika maeneo ambayo yalikuwa yakipata maji tangu mwaka 2012. 

Kwa wateja ambao bado watakuwa na matatizo katika maeneo yao wawasiliane na DAWASCO kupitia namba ya huduma kwa wateja 022 55 00 240 au 0779090904 au info@dawasco.com ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa. 

Monday, February 11, 2013

Sunday, February 10, 2013

Waraka wa Kwanza kwa mwaka 2013 wa Mbunge kwa Wananchi


“Maji; kwa Nguvu ya Umma”:

Waheshimiwa Wananchi wenzangu, Katiba ya Nchi pamoja na ubovu wake inatamka katika Ibara ya 63 (2) kwamba “Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa katiba”.

Hata hivyo kutokana na uzembe wa uongozi wa Bunge wa kushindwa kuzingatia na upuuzi wa wabunge wengi wa CCM kuridhia hoja ya kuondolewa hoja yangu binafsi; Bunge limeshindwa kutimiza wajibu wake wa kuisimamia Serikali kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es Salaam.

Katiba ya Nchi ibara ya 8 (1) inatamka kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii kwa hiyo wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, na serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa katiba.

Ibara hiyo inaendelea kueleza kwamba lengo kuu la serikali ni ustawi wa wananchi, Serikali itawajibika kwa wananchi na wananchi watashiriki katika shughuli za Serikali yao kwa mujibu wa masharti ya katiba hii.

Kwa kuwa wananchi mmekoseshwa fursa ya kushiriki kupitia mwakilishi wenu niliyewasilisha hoja binafsi kwa kuzingatia wajibu wa kibunge na mamlaka ya madaraka ya Bunge kwa mujibu wa ibara ya 63 na 100 ya Katiba ya Nchi; kwa waraka huu naiwasilisha hoja binafsi yangu kwenu wananchi muijadili na kufanya maamuzi mtayoona yanafaa.

Monday, February 4, 2013

MAELEZO NA HOJA BINAFSI YA KUPENDEKEZA BUNGE LIJADILI NA KUPITISHA MAAZIMIO YA HATUA ZA HARAKA ZA KUBORESHA UPATIKANAJI WA MAJI SAFI NA USHUGHULIKIAJI WA MAJI TAKA KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM KWA MUJIBU WA KANUNI YA 54 FASILI YA (1) YA KANUNI ZA KUDUMU ZA BUNGE TOLEO LA MWAKA 2007

Mheshimiwa Spika; 
Awali ya yote niungane na wote wenye mapenzi mapema katika kuomba ulinzi wa Mwenyezi Mungu wakati tukitimiza wajibu wa kibunge kwa mujibu wa ibara ya 63 ya Katiba ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania wa kuwawakilisha wananchi, kuisimamia serikali, kuidhinisha mipango na kutunga sheria.

Mheshimiwa Spika;
Aidha, kwa namna ya pekee ni kushukuru wewe binafsi na uongozi mzima wa Bunge kwa kunipa fursa hii adimu na adhimu ya kuwasilisha hoja binafsi kwa mujibu wa kanuni ya 54 fasili ya (1) ya kupendekeza bunge lijadili na kupitisha maazimio ya hatua za haraka zaidi za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam.

Mheshimiwa Spika;
Maji ni uhai, hivyo matatizo ya upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam na nchini kwa ujumla kama hatua za haraka zisipochukuliwa yatageuka kuwa janga la taifa. Katika kila watanzania katika Jiji la Dar es Salaam na nchini; kwa wastani mmoja hapati huduma ya maji safi na salama na hali ni mbaya zaidi kuhusu ushughulikiaji wa maji taka.

Wakati baadhi ya nchi duniani zikielezwa kwenye kitabu cha hivi karibuni cha Mnukuzi Maalum wa Umoja wa Mataifa (UN Special Rapporteur) kuwa katika mwelekeo unaostahili kuhusu kuhakikisha haki ya maji na usafi wa mazingira (On the right track; Good practices in realizing the rights to water and sanitation: 2012), hali ni kinyume kwa taifa letu.

Ripoti ya Taasisi ya Kimataifa inayoshughulikia masuala ya maji (WaterAid: 2011) imeiweka Tanzania katika kundi la nchi ambazo haziko katika mwelekeo unaostahili wa kuboresha upatikanaji wa maji safi, ushughulikiaji wa maji taka na usafi wa mazingira (Policy Report: Off Track, Off Target; why investments in water, sanitation and hygiene is not reaching those who need the most).

Mheshimiwa Spika;
Hoja hii inalengo la kuibua mjadala wa hatua za haraka. Kimsingi hatua hizi za haraka hazitanufaisha Mkoa mmoja pekee kwa kuzingatia kuwa Mpango Maalum wa kutatua tatizo la maji katika Jiji la Dar es salaam ni kwa ajili pia ya maeneo mengine ya miradi iliyo sehemu ya mpango huo ya Morogoro mpaka Pwani. Aidha, kujadiliwa na kupitishwa kwa mapendekezo ya hoja hii kutaongeza pia msukumo wa miradi katika maeneo mengine ya mijini na vijijini katika mikoa mbalimbali nchini.

Shukrani zangu za dhati ziwafikie wabunge wenzangu wa vyama vya upinzani na wa chama tawala kwa maoni na mapendekezo yenu yaliyoniwezesha kuirekebisha hoja hii pamoja na ushauri wa Katibu wa Bunge Dr Thomas Kashillilah na maafisa na watendaji katika ofisi ya bunge, kambi rasmi ya upinzani na ofisi ya mbunge wa Jimbo la Ubungo mlioboresha hoja hii kwa manufaa ya Jiji la Dar es Salaam na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika;
Nitumie pia nafasi hii kuwashukuru Watanzania wenzangu wa kada, hadhi na ngazi mbalimbali katika taasisi na maeneo mengi ndani na nje ya nchi mnaoendelea kuniunga mkono kwa hali na mali katika kutimiza majukumu yangu ya kibunge na nafasi nyingine ninazozitumikia.

Nawashukuru sala zenu wakati wa kesi ya msingi na rufaa ya kupingwa kwa matokeo ya ushindi wetu Jimbo la Uchaguzi la Ubungo; kwa pamoja tumeshinda, tuendelee na kazi.

Aidha, pamoja na mjadala huu wa bungeni natarajia kupokea maoni na mapendekezo yenu kuhusu hoja hii kwa njia mbalimbali za mawasiliano ikiwemo kupitia mtandao wa http://mnyika.blogspot.com kwa hatua zaidi. Kaulimbiu yetu ni ile ile: AMUA; Maslahi ya Umma Kwanza.


MAELEZO YA HOJA: 

Mheshimiwa Spika;
Maji ni mojawapo ya mahitaji ya msingi ya binadamu, maji ni uhai. Upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama ni sehemu ya muhimu ya maendeleo ya nchi na maisha ya wananchi. Maji ni lazima kwa matumizi ya majumbani, maji ni muhimu ni moja ya malighafi muhimu katika kazi za uzalishaji iwe ni za viwanda, kilimo, mifugo na shughuli zingine za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika;
Tanzania ni nchi ambayo imejaliwa vyanzo vingi vya maji, vinavyohusisha mito, mvua, maziwa na bahari; kuwepo kwa vyanzo hivi vya maji ni wazi kuwa nchi yetu inaweza kuepukana na shida ya maji inayoikumba jamii ya Tanzania iwapo tutaondoa udhaifu uliopo. Aidha, udhaifu huo unahusisha pia kuziweka vyanzo vyenyewe pia mashakani kwa matendo ya binadamu yenye kuathiri endelevu wa matumizi hali itayozua migogoro katika siku za usoni iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa.

Friday, January 25, 2013

Salamu za Maulid na Barua ya wazi kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba

Nawatakia heri katika Maulid an-Nabi, ni siku ya kukumbuka kuzaliwa na maisha ya Mtume Muhammad (S.A.W)! Ifuatayo ni barua ya wazi kwa tume ya mabadiliko ya Katiba;


BARUA YA WAZI KWA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA 

Mwenyekiti, 

Tume ya Mabadiliko ya Katiba, 

Dar es Salaam 

Mheshimiwa, 

YAH: KUPANUA WIGO WA KUKUSANYA MAONI YA WANANCHI BINAFSI KWA SIMU ZA MKONONI NA MAKUNDI YA WANANCHI KATIKA MABARAZA YA KATIBA 

Nakuandikia nikirejea maelezo yako kwenye mkutano wako na waandishi wa habari tarehe 5 Januari 2013 kuhusu mchakato wa ukusanyaji maoni ya mabadiliko ya katiba. 

Maelezo uliyotoa yanadhihirisha upungufu katika mchakato wa ukusanyaji wa maoni ya wananchi binafsi unaoelezwa kukamilika kwa kuwa na idadi ndogo ya watu waliotoa maoni mpaka sasa ambapo mpaka awamu nne zinakamilika jumla ya watu 318,223 tu ndio waliotoa maoni; kwa tafsiri yangu hii ni sawa na asilimia 0.7 ya wananchi wote zaidi ya milioni 44.9. 

Upungufu huo uko zaidi katika utoaji maoni kwa simu za mkononi ambapo kwa mujibu wa maelezo yako wananchi waliotoa maoni kwa njia hiyo ni 16,261 tu; kwangu mimi hii ni sawa na asilimia 0.08 ya idadi ya wateja wa makampuni ya simu za mkononi ambao watajwa kuwa zaidi ya milioni 20 (mobile phone subscribers).

Thursday, January 24, 2013

Nimemwandikia Spika Bunge liwezeshe ufumbuzi wa mgogoro wa gesi asilia

BUNGE LIINGILIE KATI KUWEZESHA UFUMBUZI WA MGOGORO WA GESI MTWARA. SPIKA ATUMIE MAMLAKA YAKE KUELEKEZA KAMATI ITAYOKUTANISHA SERIKALI NA WANANCHI. RAIS NA SERIKALI WAJISAHIHISHE NA KUONDOA UDHAIFU BADALA YA KUENDELEA KULAUMU NA KUPOTOSHA 

Nimemwandikia barua Spika atumie mamlaka na madaraka yake kutoa nafasi Bunge liingilie kati kuwezesha ufumbuzi wa mgogoro unaoendelea kati ya Serikali na wananchi kuhusu utafutaji, uvunaji, usafirishaji na utumiaji wa gesi asilia kutoka Mtwara.

Katika hatua ya sasa Serikali ni kupitia Wizara ya Nishati na Madini na taasisi zake ni sehemu ya watuhumiwa na washutumiwa hivyo ni muhimu majadiliano kati ya Serikali na wananchi kuwezesha ufumbuzi wa mgogoro huo yakasimamiwa na muhimili mwingine kwa dola.

Rais naye tayari ameshachukua upande bila kusikiliza kwa kina na kuyaelewa madai ya wananchi hivyo katika hali ya sasa ni muhimu kurejea katika madaraka na mamlaka ya wabunge kwa mujibu wa katiba ya nchi kuwezesha ufumbuzi wa mgogoro huu kuepusha hali tete inayoweza kuzuka na kuathiri uchumi na usalama katika maeneo husika.

Katiba ya Nchi Ibara ya 63 (2) inaelekeza kwamba sehemu ya pili ya Bunge (inayoundwa na wabunge) itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa katiba.

Monday, January 21, 2013

SPIKA ASILINDE UFISADI KIWANDA CHA URAFIKI NA WAZIRI KIGODA ASIKWEPE KUTOA MAJIBU

Tarehe 21 Januari 2012 gazeti la Tanzania Daima limemnukuu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Viwanda na Biashara akieleza kuwa wameunda Kamati Ndogo ya Uchunguzi kuhusu ufisadi wa miaka mingi wa Kiwanda cha Nguo cha Urafiki lakini wanasubiri idhini ya Spika kamati hiyo ianze kazi. Habari hiyo imeeleza kuwa Spika ndiye anayekataa uchunguzi huo kufanyika.

Nikiwa mbunge wa Jimbo la Ubungo, mahala kilipo Kiwanda cha Urafiki nasisitiza umuhimu wa Spika kutoa kauli kwa umma kuhusu hatua alizochukua ikizingatiwa kwamba hata kabla ya kamati ndogo ya uchunguzi kuundwa nilishawasilisha kwa Spika wa Bunge maelezo binafsi kuhusu ufisadi huo na mpaka sasa hajatoa idhini yashughulikiwe.

Aidha, majibu ya Waziri wa Viwanda na Biashara Dk Abdalah Kigoda kuwa anafuatilia suala hilo Wizarani hayajitoshelezi kwa kuzingatia kuwa zaidi ya nusu mwaka umepita toka atoe ahadi ya kufuatilia Wizarani; wafanyakazi wa Urafiki na wananchi kwa ujumla wanachohitaji kuelezwa ni hatua zilizochukuliwa mpaka sasa.

Sunday, January 20, 2013

HOTUBA YA JOHN MNYIKA (MB) ALIYOITOA TAREHE 20 JAN, 2013 KATIKA UFUNGUZI WA MKUTANO WA BARAZA LA WANAWAKE WA CHADEMA (BAWACHA) JIMBO LA UBUNGO ULIOFANYIKA KATIKA UKUMBI WA MATUNGUCHA KATA YA SARANGA

Viongozi wa BAWACHA Taifa,

Waheshimiwa Wabunge wa viti maalum,

Viongozi wa CHADEMA Jimbo la Ubungo,

Viongozi wa BAWACHA Jimbo la Ubungo,

Waheshimiwa Madiwani wa kata na viti maalum,

Viongozi wa BAWACHA toka kata zote za Jimbo la Ubungo.

Niungane nanyi katika kumshukuru Mungu kwa kutupa uzima na kuendelea na kazi katika mwaka mpya wa 2013. Kwa wale ambao hatujakutana mwezi huu wa Januari, nitumie fursa hii kuwatakia mwaka mpya mwema wenye upendo na uwajibikaji.

Nawashukuru kwa kunialika kuzungumza machache kwenye Mkutano huu wa Baraza la Wanawake wa CHADEMA (BAWACHA) Jimbo la Ubungo na niwapongeze waandaaji kwa kuweza kuwakutanisha pamoja viongozi kutoka kata zote na wawakilishi wa wanachama kutoka katika matawi na misingi na BAWACHA katika mitaa mbalimbali ya Jimbo la Ubungo.

Mwezi Disemba 2012, CHADEMA taifa kiliutangaza 2013 kuwa ni mwaka wa ‘nguvu ya umma’. Kufuatia tamko hilo la Kamati Kuu, viongozi mbalimbali wa CCM walianza propaganda chafu kupitia vyombo vya habari kuwa CHADEMA imetangaza mwaka wa ‘vurugu’.

Propaganda hizo zinalenga kutisha umma, hususan wanawake wasiunge mkono vuguvugu la mabadiliko (M4C), kujiunga kwenu kwa wingi katika Jimbo la Ubungo kunadhihirisha kuwa wanawake hamko tayari kudanganywa kwa siasa chafu na mnaendelea kuiunga mkono CHADEMA; asanteni sana.

Saturday, January 19, 2013

Ziara Jimboni: KATA YA MANZESE 08 Desemba, 2012

Ziara ndani ya Jimbo: muendelezo wa kutembelea maeneo mbalimbali ya jimboni. Jana, Desemba 08, 2012 ziara kubwa ilifanyika katika kata ya MANZESE.

Ziara ilimudu kutembelea ofisi ya kata (Kilimani), kufungua misingi katika mitaa ifuatayo; Kilimani, Chakula bora, Mvuleni, Midizini, Mwembeni, na Mnazi Mmoja.

Kisha mkutano wa hadhara na wananchi wa mtaa wa Mnazi Mmoja.


Shirika la Umeme (TANESCO) linakabiliwa na ufisadi na uzembe unaoongeza gharama za uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme kwa upande mmoja na uendeshaji wa shirika kwa upande mwingine. Ufisadi na uzembe huo unapunguza uwezo wa TANESCO kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika na unaongeza gharama na bei ya upatikanaji wa umeme hali inayoathiri uchumi wa nchi na maisha ya wananchi kwa kuchangia katika mfumuko wa bei na ongezeko la gharama za maisha. Mzigo wa ufisadi na uzembe katika TANESCO unajitokeza zaidi katika mikataba mibovu pamoja na ukiukwaji wa sheria za ununuzi wa umma, ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.

Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 63 sehemu ya pili ya bunge (inayoundwa na wabunge) ndio chombo kikuu chenye madaraka na mamlaka kwa niaba ya wananchi ya kuisimamia serikali. Hata hivyo, katika kipindi cha kati mwaka 2008 mpaka 2012 maazimio ya Bunge kuhusu sekta ya nishati ikiwemo kuhusu umeme yamekuwa hayatekelezwi kwa wakati na kwa ukamilifu hali inayofanya tuhuma za ufisadi na uzembe kuendelea kujirudiarudia. Katika muktadha huo, ni muhimu kwa kuwa kwa mujibu wa Katiba ya nchi ibara ya 8 madaraka na mamlaka ni ya umma (serikali inafanya kazi kwa niaba tu) ipo haja ya kuanza kuunganisha ‘nguvu ya umma’ katika kushinikiza hatua kuchukuliwa kwa wahusika wa ufisadi na uzembe ili kuweka misingi bora ya uwajibikaji katika sekta ya nishati.

Friday, January 18, 2013

Rais na Mawaziri wanadharau wabunge kuhusu mabadiliko ya mzunguko wa Bajeti

Yaliyojiri na yanayoendelea kujiri ndani ya Baraza la Mawaziri na Wizara ya Fedha kuhusu mabadiliko ya mzunguko na mchakato wa bajeti yanaashiria kwamba Rais na Serikali wanadharau mamlaka na madaraka ya Bunge na wabunge.

Aidha, kutokana na umuhimu wa mzunguko na mchakato wa bajeti katika kuwezesha uwajibikaji kwenye mapato na matumizi ya rasilimali za umma; Waziri wa Fedha anatakiwa aweke wazi kwa umma mabadiliko hayo yaliyofanyika ili wananchi na wadau waweze kutoa maoni na Bunge liweze kuyazingatia wakati wa marekebisho ya kanuni za Bunge yanayotarajiwa kufanywa katika mkutano wa kumi wa Bunge.

Wakati Katibu wa Bunge amenukuliwa tarehe 17 Januari 2013 akisema kwamba pendekezo la mabadiliko ya mzunguko na mchakato wa bajeti bado linajadiliwa na kwamba iwapo litaafikiwa, uamuzi utatangazwa mapema mwezi ujao (Februari 2013) wakati wa mkutano wa Bunge; upande wa Rais na Wizara ya Fedha wameshapitisha na kuanza kutekeleza mzunguko na mchakato mpya wa bajeti kuanzia mwezi Disemba 2012.

Tuesday, January 15, 2013

Sera ya majimbo ni siri ya maendeleo ya nchi na wananchi

Na John J.Mnyika

Mwaka 2007 miaka miwili baada ya uchaguzi wa mwaka 2005 palijitokeza mjadala kuhusu sera ya majimbo. Mwaka 2012 ikiwa ni miaka miwili tena toka uchaguzi wa mwaka 2010 pameibuka kwa mara nyingine mjadala kuhusu sera ya majimbo kufuatia maandamano ya wananchi wa Mtwara juu ya madai ya gesi. Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospter Muhongo amenukuliwa na gazeti moja tarehe 29 Disemba 2012 akiponda sera ya majimbo ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa ni mbovu na haitumiki kokote duniani; kauli ambayo haina ukweli kama nitavyoeleza katika makala hii. Amedai madai ya rasilimali za wananchi wa eneo hayana msingi na kuwaita wote wenye kujenga hoja hiyo kuwa wanataka kuigawa nchi vipande vipande, majibu ambayo ni mwendelezo wa propaganda chafu.

Prof. Muhongo badala ya kujibu hoja za waandamanaji na wananchi wa Mtwara ameamua kuibua ‘vioja’ vya kuishambulia CHADEMA na sera yake ya majimbo. Wakati hata kwa sera za CCM na serikali ya sasa, maandamano ya wananchi wa Mtwara kutaka majibu toka kuhusu manufaa ya miradi ya gesi asili inayotoka katika maeneo yao ni matokeo ya madai ya ufisadi wa baadhi ya viongozi na udhaifu wa Serikali katika kuushirikisha umma katika michakato ya maamuzi ya kisera na kitaasisi kuhusu rasilimali na miradi muhimu ya maendeleo. Aidha, ni matokeo pia Bunge kutokuisimamia kikamilifu Serikali kwa niaba ya wananchi kwa mujibu wa ibara ya 63 ya katiba wakati serikali inapoacha kufafanua masuala yanayohojiwa na wabunge na inapokwepa kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu sekta ya nishati ikiwemo sekta ndogo ya gesi asili.

Saturday, January 5, 2013

Nimewasilisha Muswada Binafsi wa Sheria ya kuunda Baraza la Taifa la Vijana


Jana tarehe 4 Januari 2012 niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge taarifa ya muswada binafsi wa Sheria ya kuunda Baraza la Taifa la Vijana (The National Youth Council Bill, 2013) kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (1) na Taarifa ya Muswada huo kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (2) ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007).

Nimechukua hatua hiyo kwa kuwa kwa miaka zaidi ya kumi Serikali imekuwa ikiahidi karibu kila mwaka bungeni kuwa itawasilisha muswada wa kuunda baraza la vijana la taifa lakini haijawahi kutekeleza ahadi hiyo; nimeamua kuitekeleza ahadi hiyo kwa kupeleka bungeni muswada binafsi wa kuunda baraza la vijana la taifa.

Katika taarifa hiyo ya muswada nimewasilisha madhumuni, sababu pamoja na nakala ya muswada wenyewe wa sheria ya kuanzisha Baraza la Vijana la Taifa kwa madhumuni ya kuanzisha chombo cha kuwaratibu vijana wa Tanzania katika kutekeleza shughuli zao kijamii, kuuchumi, kiutamaduni na kimichezo, na kuchagiza hali ya utambulisho wa Kitaifa wa pamoja na uzalendo.

Friday, January 4, 2013

Washindi wa Shindano la Ujasiriamali Jimbo la Ubungo wapatikana

Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Ubungo kwa ushirikiano na shirika la Maendeleo Ubungo; Ubungo Development Initiative (UDI) waliendesha shindano la kuwainua wajasiriamali wadogo wadogo na hususan vijana wasio na ajira (na walio katika mazingira magumu) kwa kuwataka kuandaa mchanganuo namna gani watatumia Tsh 200,000/- katika kuanzisha au kuiendeleza biashara zao. Washindi waliopatikana ni;
Mshindi wa Kwanza: Joseph R. Shindo (22) kutoka Kata ya Kimara Tsh 200,000/-

Thursday, January 3, 2013

Hatua kuhusu matumizi ya dola milioni 164.6 za “mabomba ya mchina” na mikataba ya miradi ya sasa ya maji jijini Dar es salaam

Tarehe 3 Januari 2013 kwa kutumia kifungu cha 10 cha sheria ya haki, kinga na madaraka ya Bunge nimetaka Wizara ya Maji inipatie nakala ya ripoti ya utekelezaji wa mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam na maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and Sanitation Project-DWSSP) uliotekelezwa kati ya mwaka 2003 mpaka 2010 jijini Dar es salaam.

Nimetaka ripoti hiyo ili kubaini matumizi ya dola milioni 164.6 zinazoelezwa kutumika katika mradi huo maarufu kama wa ‘mabomba ya mchina’ kwa kuwa mpaka sasa mwaka 2013 sehemu kubwa ya mabomba yaliyowekwa wakati wa mradi huo katika Jiji la Dar es salaam hayatoi maji huku kukiwa na upungufu katika uzalishaji, upotevu wakati wa usafirishaji, udhaifu katika usambazaji na tuhuma za ufisadi katika matumizi.

Pamoja na kutaka ripoti ya utekelezaji wa mradi huo, nimetaka pia nakala ya ripoti ya ukaguzi wa kiufundi (technical Audit) uliofanywa na kampuni ya Howard Humphreys kuhusu mradi huo.

Nimetaka pia kupatiwa ripoti za ukaguzi uliofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Kampuni ya Maji Dar es salaam- DAWASCO (Dar es salaam Water Supply and Sewerage Company) na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka-DAWASA (Dar es Salaam Water Supply and Sewerage Authority) kwa mwaka miaka mitatu ya 2009/10, 2010/2011, 2011/2012 ili kuweza kufuatilia hatua zinazostahili kuchukuliwa.

Ufafanuzi wa Waziri Muhongo:ukweli umefichwa, upotoshaji unaendelea!


Nimesoma taarifa ya serikali iliyotolewa na Waziri Prof. Muhongo kufafanua kuhusu miradi ya utafutaji na uvunaji wa gesi asili nchini. Hatimaye serikali imeanza kutoa ufafanuzi suala ambalo ilikwepa kulifanya bungeni hata baada ya kuhoji 2011 na 2012. Hata hivyo ufafanuzi huo haujitoshelezi kwa kuwa kuna ukweli umeendelea kufichwa na upotoshaji umejirudia kama ambavyo nitafafanua katika kauli yangu nitakayotoa siku chache zijazo kwa kuwa leo niko katikati ya kushughulikia usiri na udhaifu katika mikataba na miradi ya Maji jijini Dar es Salaam.

Maslahi ya Umma Kwanza

John Mnyika (MB)
Waziri Kivuli, Nishati na Madini
03 Januari 2013

Wednesday, January 2, 2013

Toka analojia hadi digiti: Nini maoni yetu?


Naomba majibu yenu kwa kuzingatia kuwa kazi ya wabunge ni kuishauri na kuisimamia Serikali: baada ya kutekelezwa kwa uamuzi wa kuhama kutoka analojia kwenda digiti kwa mkoa wa Dar es salaam; kwa watumiaji, nini faida na athari mlioanza kuzipata kwa wenye ving’amuzi?

Na nini kikwazo kwa wengine ambao hamjahamia mpaka sasa? Na nini mnataka watoa huduma na mamlaka zingine kuzingatia? Katika hatua ya sasa, ni muhimu Tanzania Consumer Advocacy Society (TCAS) ifanye tathmini ya kina kwa niaba ya watumiaji kwa ajili ya hatua zake.