Tuesday, January 31, 2012

Hatimaye mkataba wa vijana wa Afrika waletwa bungeni kuridhiwa

Kwa Vijana wenzangu kwa nafasi na wote wenye nafsi za ujana, leo ule mkataba wetu wa Afrika (African Youth Charter) hatimaye unaingia bungeni kuridhiwa. Ni matokeo ya harakati zetu za miaka mingi kabla na hata baada ya Rais Kikwete kuusaini Gambia mwaka 2006 lakini ukaishia makabatini. Baada ya kunituma bungeni kuwatumikia mkataba huu ni kati ya mambo niliyohoji mara kwa mara kutaka uletwe bungeni kuridhiwa ili utekelezaji wake uweze kuanza.

Nawashukuru wote tuliounganisha nguvu kwenye harakati za vijana kwa nyakati mbalimbali kuanzia NYF, TYVA, YUNA, TSNP, UDSM, BAVICHA, asasi zingine na mwisho lakini kwa umuhimu mkubwa vijana wote tuliokesha pamoja kulinda kura Loyola.

Kwa kurejea nyuma katika historia, nawaletea moja ya ujumbe nilioandika kwenu na kwa vijana wa Afrika mwaka 2008: http://mnyika.blogspot.com/2008/10/vijana-tufikiri-na-kuungana-kukomboa.html Kila kizazi lazima kiitambue dira na dhima yake; ama kisaliti au kitimize. Tuendelee kuwajibika; kwa pamoja tunaweza.

John Mnyika
Bungeni, Dodoma-01/02/2012

Saturday, January 28, 2012

Taarifa ya Hoja kuhusu utekelezaji wa maazimio juu ya Richmond

Tarehe 25 Januari 2012 nimewasilisha kwa Katibu wa Bunge taarifa ya hoja kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la 2007 Kanuni 54 (4) na 55 (1) kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge juu ya mkataba baina ya TANESCO na Kampuni ya Richmond Development Company LLC.

Hoja hiyo ikipewa nafasi ya kuwasilishwa na kujadiliwa itaongeza msukumo wa utekelezaji wa maazimio ya bunge na hivyo kuchangia katika mapitio ya mikataba yenye kuongeza bei ya umeme; kuweka mfumo wa kulihusisha bunge katika maandalizi ya mikataba yenye maslahi ya taifa ikiwemo katika mafuta, gesi asilia na ujenzi na kuwezesha uwajibikaji na hatua kamili kuchukuliwa kwa waliohusika na ufisadi na uzembe uliolisababishia hasara taifa.

Taaarifa hii ya hoja niliiwasilisha awali tarehe 13 Aprili 2011 na kupatiwa majibu; hata hivyo niliijibu ofisi ya bunge kupatiwa taarifa ya utekelezaji uliofanywa na serikali baada ya Februari 2010 bila kupatiwa majibu hivyo nimeiwasilisha tena ili hoja husika ijadiliwe.

Lengo la Hoja Binafsi nitakayoiwasilisha kufuatia taarifa hiyo ni kutaka uamuzi wa Bunge uliofanyika katika Bunge la Tisa Mkutano wa 18 mwezi Februari 2010 kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge juu ya mkataba baina ya TANESCO na kampuni ya Richmond Development Company LLC; UBADILISHWE.

Friday, January 27, 2012

Kuhusu Msongamano wa Magari DSM na Ziara Kwembe

Nashukuru kwamba jana Serikali ilituma ujumbe wa kuonana ana kwa ana madaktari; hata hivyo ni muhimu ikayafanyia kazi yaliyowasilishwa jana ili leo kuwa na ujumbe mzito zaidi majadiliano yakamilike kwa haraka ili madaktari warejee kazini. Leo naendelea na kazi za kijimbo:

Mosi, nitashiriki mkutano wa wadau kuhusu tatizo la msongamano wa magari katika mkoa wa Dar es salaam. Serikali imeleta kwa dharura mwaliko wa mkutano huo jana hivyo sijapata wasaa wa kuomba maoni yenu kuhusu utekelezaji, mnaweza kuendelea kuyatoa hapa na tutayaunganisha pamoja na kuyawasilisha kwa mamlaka husika. Nimekosa pia fursa ya kuandika uchambuzi wangu kwa ajili ya kuchochea mjadala hivyo hoja zangu nitakwenda kuzitoa moja kwa moja kwenye mkutano papo kwa papo. Kwa ujumla, huu si wakati wa maneno bali matendo; mikutano kuhusu foleni katika jiji la Dar es salaam imeshafanyika kadhaa kati ya mwaka 2005-2010, maoni yametolewa na mipango imeandaliwa. Kinachotakiwa hivi sasa ni kuunganisha nguvu ya wadau katika kuhamasisha na kuharakisha utekelezaji. Na katika kufanya hivyo, kunahitajika nyongeza ya bajeti kwa kuwa kiwango kilichotengwa kwa ajili ya kupunguza msongamano katika jiji la Dar es salaam kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ni kidogo ukilinganisha na ukubwa wa tatizo, kiasi cha mahitaji na hasara ambayo wananchi na nchi inapata kila siku kutokana na msongamano katika Jiji la Dar es salaam.

Kuitishwa kwa mkutano wa leo kumefanya nikumbuke ujumbe wangu ambao niliuandika kwenye mtandao wa Wanabidii tarehe 14 Disemba mwaka 2011 nikichangia mjadala na kujibu baadhi ya maswali yaliyoulizwa. Takribani mwezi mmoja na nusu umepita toka niandike ujumbe huo, ambapo yapo ambayo tayari nimeshayafuatilia mwezi huu wa Januari kupitia vikao vya bodi ya barabara, RCC, Jiji na Manispaa na hatua zimeanza kuchukuliwa kama sehemu ya kuchangia katika kupunguza foleni katika jiji la Dar es salaam hususani Jimboni Ubungo. Hata hivyo, nanukuu mchango wangu huo kwa kuwa kuna mambo bado ambayo niliyasema wakati huo lakini yanaweza kuendelea kujadiliwa na wadau katika mkutano wa leo:

“ Nitachangia tu kwa ujumla bila kutenganisha hatua kati ya za dharura, muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu.

KUHUSU MGOMO WA MADAKTARI

Mgomo wa madaktari unaoendelea hivi sasa umedhihirisha kwamba tuna serikali dhaifu yenye ombwe la uongozi. Haiwezekani wananchi wakawa wanakufa kwa kukosa matibabu stahiki na wengine wakipata madhara kutokana na kuchelewa kupata matibabu sababu ya mgomo wa madaktari halafu viongozi wenye dhamana hawachukui hatua sahihi.

Rais Jakaya Kikwete ambaye ndiye mwenye dhamana kwa mujibu wa katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 33 ndiye kiongozi wa shughuli za serikali na ibara ya 35 shughuli zote za utendaji wa serikali zinatekelezwa na watumishi wa serikali kwa niaba ya Rais; ameondoka kwenda nje ya nchi mgomo ulipoanza na hakuna kauli yoyote mpaka sasa toka kwa Makamu wa Rais wala kwa Ikulu.

Waziri Mkuu Mizengo Pinda badala ya kwenda kwenye eneo la mgomo na kuzungumza na madaktari naye ameishia kuzungumza na vyombo vya habari. Waziri wa Afya Dk. Haji Mponda na Naibu Waziri Dk. Lucy Nkya nao jana wamezungumza na waandishi wa habari badala ya kwenda kukutana na madaktari na kuzungumza nao kuhusu madai yao ya msingi.

Kwa upande wetu CHADEMA tulitoa kauli tarehe 25 Januari 2012 ya kutaka serikali ichukue hatua na tuliona tuipe serikali nafasi ifanye kazi yake hata hivyo serikali haionyeshi kuupa uzito unaostahili mgogoro huu wenye kuathiri hali za wagonjwa na maisha ya wananchi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Saturday, January 14, 2012

TANZIA

Mh. Regia Mtema; Mbunge wa Viti Maalum na 
Waziri Kivuli wa Kazi na Ajira  
Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimepatwa na majonzi makubwa na kinasikitika sana kwa kifo cha Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Taifa, Mheshimiwa Regia Mtema ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum na Waziri Kivuli wa Kazi na Ajira. Mheshimiwa Regia Mtema amefariki leo tarehe 14 Januari 2011 kwa ajali ya gari katika eneo la Ruvu darajani. 

Katika uhai wake marehemu Regia Mtema amefanya kazi mbalimbali za kisiasa na kijamii katika taifa. Marehemu Regia Mtema amezaliwa tarehe 21 mwezi Aprili mwaka 1980 na kusoma shule za sekondari kidato cha kwanza mpaka cha sita katika shule ya sekondari ya Forodhani na Shule ya Wasichana ya Sekondari ya Machame. Marehemu Regia Mtema alipata shahada yake ya kwanza (Bsc Home Economics and Human Nutrition) katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine. 

Mara baada ya kuhitimu masomo yake marehemu Regia Mtema alifanya kazi katika taasisi mbalimbali kabla ya kujiunga na CHADEMA na kuteuliwa kuwa Afisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Vijana ya CHADEMA na baadaye kuteuliwa kuwa Afisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Mafunzo ya CHADEMA nafasi ambayo aliishikilia hadi mwaka 2010 alipoteuliwa kuwa mbunge wa viti maalum. 

Monday, January 9, 2012

Magufuli hajasema kweli; Anaficha Udhaifu wa Serikali na Wizara yake

TAARIFA KWA UMMA

UTANGULIZI

Tarehe 4 na 5 Januari 2011 Waziri wa Ujenzi Mheshimiwa John Magufuli alinukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari akitoa madai mbalimbali juu yangu wakati akijibu kauli za Wabunge wa Dar es salaam juu ya ongezeko la nauli katika vivuko vya Kigamboni na maeneo mengine nchini.Toka Waziri Magufuli atoe kauli zisizokuwa za kweli dhidi yangu badala ya kujibu hoja za msingi nilizotaka maelezo toka wizara yake na serikali kwa ujumla sikutoa tamko kwa kuwa nilikuwa katikati ya kazi mbalimbali jimboni Ubungo na majukumu mengine ya kitaifa.

Hata hivyo, kuna msemo kwamba ‘uongo ukiachwa ukarudiwa rudiwa unaweza kuaminika kuwa ndio ukweli’; hivyo naomba kutoa taarifa kwa umma kujibu madai hayo kwa lengo la kuweka rekodi sahihi.Namheshimu Waziri Magufuli, hata hivyo kauli alizozitoa dhidi yangu zinadhirisha kuwa ameanza kulewa sifa kwa kiwango cha kuwa mpotoshaji na mzushi. Ni vyema umma ukachukua tahadhari kwamba imani ya wananchi juu yake ameanza kuitumia vibaya kulinda uzembe, ubabe na ufisadi.Aidha, ni muhimu akawa anajielekeza kujibu madai ya msingi ya wananchi badala ya kuibua masuala mengine kwa lengo la kuhamisha mjadala; hivyo nitarudia tena masuala ambayo nilitaka ayatolee maelezo na vielezo kwa maslahi ya umma.

Thursday, January 5, 2012

Kuhusu kauli za Waziri Magufuli

Kwa wote mliotaka maoni yangu juu kuhusu kauli za Waziri Magufuli vyombo vya habari kuhusu mbunge wa Ubungo na Jimbo letu. Katika siku hizi tatu sina muda wa malumbano, niko katikati ya kazi ya kuwatumikia wananchi jimboni na kutekeleza wajibu mwingine wa kitaifa. Wananchi na wadau wengine mnaweza kumwambia ukweli mnaoufahamu kuhusu aliyoyasema mkipenda, kwa kuwa matendo yanazungumza zaidi ya maneno. Mjadala huu na mingine ni muhimu pia kubadilisha mifumo na kurejesha utamaduni wa uwajibikaji katika taifa letu. 

Mambo ambayo amesema kwamba siyashughulikii ukweli ni kwamba nilishachukua hatua kwa nyakati mbalimbali kwenye mwaka 2011 ndani ya bunge, kwenye halmashauri na pia nje ya bunge, na matokeo yameanza kuonekana. Baadhi ya hatua hizo nilimhoji yeye mwenyewe au mamlaka za Wizara yake kama sehemu ya kutimiza wajibu wa kibunge wa kuwakilisha wananchi, kutunga sheria na kuisimamia serikali. 

Kwa bahati mbaya amekuwa msahaulifu hata wa kauli zake mwenyewe kuhusu masuala niliyoyaibua, amelewa sifa kwa kiwango cha kusema maneno yasiyokuwa ya kweli, imani juu yake imempa upofu wa kupindisha mambo mbalimbali na kugeuzia watu wengine mambo ambayo yeye mwenyewe au wenzake katika serikali wamefanya uzembe wa kutochukua hatua kwa wakati. Kwa bahati nzuri, ukweli una sifa moja, huwa unadumu milele; nitamjibu hoja kwa hoja nikipata wasaa kwa sasa naendelea na utumishi, maslahi ya UMMA kwanza.

Wednesday, January 4, 2012

Kazi za leo jimboni Ubungo

Leo nimeendelea na kazi za kibunge jimboni katika kata ya Kwembe nimefanya ziara na kukutana na wananchi, wameniuliza maswali kuhusu maji, barabara ya kwenda Mpiji Magohe, Luguruni Satellite town, mgogoro wa ardhi katika eneo la Msakuzi na uharibifu wa daraja katika mto Mdidimua/Kibwegere (Mji Mpya). Nimewajibu hatua ambazo nimechukua kwa kila jambo.

Pia nimekabidhi Jengo la Kituo cha Afya na Mama na Mtoto Kata ya Kwembe Jimboni Ubungo, tulichojenga kwa fedha za Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo (CDCF). Habari zaidi zitafuata; Maslahi ya Umma KWANZA.