Monday, October 29, 2012

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Awali ya yote niwatikie nyinyi wanahabari kheri ya sikukuu na kupitia kwenu nifikishe salamu kwa ndugu zetu waislam na watanzania wote katika kuadhimisha Iddi Ell-Hajj.

Tarehe 15 Oktoba 2012 nilitoa taarifa kwa umma kuwa niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge kusudio la kuwasilisha Muswada Binafsi wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (The Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka 2012 kwa hati ya dharura kwa mujibu wa Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007) iwapo Serikali haitatoa kauli kwa umma ya ratiba ya kupata mapendekezo toka kwa wadau wa hifadhi ya jamii pamoja na kamati husika ya kudumu ya Bunge na kuwasilisha muswada husika bungeni kama ilivyoazimiwa bungeni tarehe 6 Julai 2012.

Kufuatia hatua yangu na hatua za wadau wengine Serikali kinyume na msimamo wa awali ambalo ulielezwa na Naibu Waziri wa Kazi na Ajira Makongoro Mahanga tarehe 14 October 2012 ambaye alieleza kuwa marekebisho ya kurejesha fao la kujitoa hayatafanyika mpaka mkutano wa kumi wa Bunge mwezi Februari mwaka 2013; Serikali imechapa katika gazeti la Serikali Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali na. 40 Juzuu namba 93 ambao katika sehemu ya 6 vifungu vya 13, 14 na 15 imependekeza kurejesha fao la kujitoa kwa upande wa mfuko mmoja wa mashirika ya umma (PPF) hata hivyo muswada huo haujawasilishwa kwa hati ya dharura kama ilivyoazimiwa na kuahidiwa.

Kwa upande mwingine, sehemu hiyo ya sita ya muswada huo wa marekebisho ya sheria mbalimbali haijakidhi mahitaji na matakwa ya azimio la bunge la tarehe 6 Agosti 2012 lililoungwa mkono na wabunge katika kikao cha 41 cha Mkutano wa Nane wa Bunge na itasababisha mgogoro mwingine katika ya serikali na wafanyakazi kwa upande mmoja, wafanyakazi na waajiri kwa upande mwingine na kuathiri uchumi wa nchi na maisha ya wafanyakazi katika maeneo mbalimbali nchini kwa kutoresha fao la kujitoa katika mifuko mingine ikiwemo NSSF, PSPF na LAPF.

Kwa kuzingatia kuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara imeeleza kuwa Rais ndiye mkuu wa Nchi na Kiongozi wa Serikali na Ibara ya 34 imeeleza kwamba mamlaka yote yapo mikononi mwake na kwamba madaraka hayo yanaweza kutekelezwa na watu wengine kwa niaba yake na kwamba Ibara ya 35 imeeleza bayana kwamba shughuli zote za serikali zitatekelezwa na watumishi wa serikali kwa niaba yake; wakati umefika sasa wa wafanyakazi na wadau wengine kuchukua hatua za kuwezesha  Rais kuingilia kati kabla ya mkutano wa Bunge kuanza tarehe 30 Oktoba 2012 kutumia madaraka na mamlaka yake kuondoa udhaifu uliojitokeza wa Waziri wa Kazi na Ajira Gaudencia Kabaka, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Fredrick Werema na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) Irene Isaka kutokutekeleza kwa wakati na kwa ukamilifu mapendekezo na maamuzi ya Bunge pamoja na ahadi za Serikali kwa wabunge.

Mosi; Rais azingatie masharti ya Kanuni za Kudumu za Bunge na kutia saini hati ya  dharura ya kuwezesha muswada wa marekebisho ya sheria mbalimbali wenye vifungu vya nyongeza vinavyowezesha fao la kujitoa kurejeshwa kwa mifuko yote ikiwemo NSSF, PSPF na LAPF kuwasilishwa bungeni. Kanuni ya 80 Fasili ya 4 inaelekeza kwamba “Muswada wowote wa sheria wa Serikali wa dharura hautaingizwa kwenye shughuli za Bunge bila ya kuwa na hati iliyowekwa saini na Rais inayoelekeza kuwa muswada uliotajwa kwenye hati hiyo ni wa dharura”.

Iwapo Rais hataweka saini hati ya dharura au Serikali haitawasilisha bungeni hoja kwa mujibu wa Kanuni ya 93 fasili ya 4 bunge litabanwa na fasili ya 1 ambayo inakataza bunge kushughulikia hatua zaidi ya moja katika mkutano mmoja wa bunge; tafsiri yake ni kwamba sheria hii itasubiri kupitishwa katika mkutano wa kumi wa Bunge mwezi Februari 2012 na hivyo wafanyakazi kuendelea kunyimwa mafao ya kujitoa kinyume na azimio la Bunge.

Pili, Rais atengue tangazo na agizo la Mamlaka ya Udhibiti wa Hifadhi ya Jamii (SSRA)  kueleza kuwa “kufuatia kuanza kutumika kwa Sheria hiyo (ya 13 Aprili 2012) maombi mapya ya kujitoa yamesitishwa kwa kipindi cha miezi sita hadi pale miongozo itakapotolewa ili kuwezesha Mamlaka na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kutoa elimu kwa Wadau” ambalo limesababisha mifuko yote kuacha kutoa mafao ya kujitoa hata kwa wafanyakazi .

Hii ni kwa sababu marekebisho ya sheria ya mifuko ya hifadhi ya jamii kwa upande wa kusitisha fao la kujitoa yaliyofanyika tarehe 13 Aprili 2012 yalihusu zaidi Mfuko wa Mashirika ya Umma (PPF); hivyo hayakupaswa kabisa kutumika kama sababu ya kusitisha mafao kwa mifuko yote ikiwemo NSSF, PSPF na LAPF na kwa upande mwingine wafanyakazi wanaodai mafao hayo kabla ya kujiunga na mifuko hiyo walijiunga wakiwa wameelezwa kama kati ya haki na stahili zao ni pamoja na kupata fao la kujitoa mazingira yakilazimisha hivyo kabla ya pensheni ya uzeeni. Hivyo, kusubiriwa kwa marekebisho ya sheria hakupaswi kuwa kisingizio cha kuendelea kusitisha mafao yao ya kujitoa, ama sivyo Rais aeleze sababu za ziada za kuzuia mafao ya kujitoa kwa kuzingatia Taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali juu ya uendelevu wa mifuko katika siku  chache zijazo kufuatia kushindwa kwa makampuni na Serikali yenyewe iliyokopeshwa na mifuko ya hifadhi ya jamii kuheshimu matakwa ya malipo ya mikopo kutoka mifuko husika ambayo fedha zake zinatokana na makato ya pensheni toka kwa wafanyakazi na waajiri.

Rais arejee kumbukumbu rasmi ya Bunge (Hansard) ya tarehe 7 Agosti 2012 za kikao cha 42 cha Mkutano wa Nane wa Bunge ambao nilishika mshahara wa Waziri Bunge lilipokaa kama kamati na  “nilitaka ufafanuzi wa kisera wa Serikali pamoja na uamuzi wa kuahidi kwamba kwenye mkutano wa Bunge ujao italeta Muswada wa dharura kuhusiana na Fao la Kujitoa, nilitaka kauli ya Serikali juu ya agizo lilitolewa na SSRA la kusitisha utoaji wa mafao ya kujitoa katika kipindi hiki cha miezi sita (6) na kuhusiana na wafanyakazi waliosimamishwa katika hatua ya kudai hayo mafao.

Sasa iwapo Wizara inatoa kauli ya kutengua sitisho hilo na vilevile inatoa kauli ya kutaka kurejeshwa kwa wafanyakazi waliosimamishwa katika hatua ya madai ya fao hili la kujitoa”. Waziri wa Kazi na Ajira alijibu kuwa “tutalifanyia kazi agizo hilo”, hata hivyo mpaka sasa agizo hilo la SSRA halijatenguliwa na wafanyakazi waliosimamishwa wengine hawajarudishwa mpaka hivi sasa na baadhi wamefukuzwa kazi kabisa kutokana na mgogoro uliosababishwa na Serikali kusitisha fao la kujitoa bila kuzingatia haki za binadamu, mazingira ya ujira nchini na ushirikishwaji wa wafanyakazi na wadau wengine muhimu wa hifadhi ya jamii.

Wenu katika utumishi wa umma,


John John Mnyika (Mb)
26/10/2012

Monday, October 22, 2012

KAULI TATA KUHUSU HALI TETE YA UMEME, UKWELI KWA UKAMILIFU UELEZWE

Katika kipindi cha zaidi ya mwezi mmoja kuanzia mwanzoni mwa mwezi Septemba 2012 mpaka leo tarehe 21 Oktoba 2012 viongozi na watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme nchini (TANESCO) wamenukuliwa na vyombo vya habari na wakitoa matumaini potofu kwa wananchi kuhusu hali ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini sanjari na uboreshaji wa utendaji wa Shirika la Umeme (TANESCO).

Viongozi na watendaji hao waliozungumza kwa nyakati tofauti na kutoa kauli mbalimbali ni pamoja Waziri Prof. Sospeter Muhongo, Naibu Waziri wa Nishati George Simbachawene, Katibu Mkuu wa Wizara Eliackim Maswi na Kaimu Mkurugenzi wa TANESCO Felchesmi Mramba.

Kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini natoa mwito kwa wanahabari na umma kuzipokea kwa tahadhari kauli hizo kwa kuwa hazielezi ukweli kamili kuhusu hali tete ya umeme kutokana na kususua katika utekelezaji wa Mpango wa Dharura wa Umeme kama nilivyohoji bungeni tarehe 27 Julai 2012.

Wednesday, October 17, 2012

MUSWADA KWA HATI YA DHARURA NA WAZIRI KUTAKIWA KUTOA MAELEZO KUHUSU FAO LA KUJITOA


Mwanzoni mwa wiki tarehe 15 Oktoba 2012 niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge kusudio la kuwasilisha Muswada Binafsi wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Sheria za Hifadhi ya Jamii (The Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka 2012 kwa hati ya dharura kwa mujibu wa Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007) iwapo Serikali haitatoa kauli kwa umma ya ratiba ya kupata mapendekezo toka kwa wadau wa hifadhi ya jamii pamoja na kamati husika ya kudumu ya Bunge kwa kuzingatia kuwa vikao vya kamati za kudumu za bunge vimeanza tarehe 15 Oktoba 2012 bila suala hilo kuzingatiwa.

Nimefikia uamuzi huo kwa kuwa mpaka sasa ikiwa zimebaki siku chache Mkutano wa Tisa wa Bunge kuanza tarehe 30 Oktoba 2012 ambao Serikali iliahidi kuwa italeta marekebisho ya Sheria ya Hifadhi ya Jamii, mpaka sasa Serikali haijaitisha mkutano na wafanyakazi pamoja na wadau wa jamii kupokea mapendekezo hali ambayo inaashiria upo uwezekano muswada huo usiwasilishwe kwa wakati.

Lengo la Muswada huo ni kufanya marekebisho yenye kuboresha mfumo wa utoaji wa mafao nchini ikiwemo kuwezesha kutolewa kwa fao la kujitoa (withdrawal benefits) na mafao mengine muhimu ambayo hayatolewi katika utaratibu wa sasa wa mifuko mbalimbali ya hifadhi ya jamii.

Kwa upande mwingine kufutwa kwa mafao ya kujitoa msingi wake haupo kwenye marekebisho ya sheria yaliyofanyika tarehe 13 Aprili 2012 pekee bali ni udhaifu katika mfumo mzima wa kisera na kisheria wa hifadhi ya jamii nchini hali ambayo inahitaji wadau kutaka mabadiliko makubwa.

Hivyo, Waziri wa Kazi na Ajira kutoa kauli kwa umma kuhusu maelekezo aliyoyatoa Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) baada ya mkutano wa nane wa Bunge kufuatia mapendekezo niliyotoa bungeni ya kuitaka Wizara husika kutoa muongozo wa kisera wa kutengua taarifa kwa umma iliyotolewa ya kueleza kuwa “kufuatia kuanza kutumika kwa Sheria hiyo (ya 13 Aprili 2012) maombi mapya ya kujitoa yamesitishwa kwa kipindi cha miezi sita hadi pale miongozo itakapotolewa ili kuwezesha Mamlaka na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kutoa elimu kwa Wadau”.

Wenu katika uwakilishi wa wananchi:

John Mnyika (Mb)
15/10/2012

Monday, October 15, 2012

TAARIFA KWA UMMA: Madini, Mafuta na Gesi

Spika wa Bunge Anna Makinda ndani ya wiki moja atumie madaraka na mamlaka yake kutangaza kwa umma kamati nyingine ya kudumu ya Bunge itayoshughulikia masuala ya gesi asili kabla na wakati wa mkutano wa tisa wa Bunge uliopangwa kuanza tarehe 30 Oktoba 2012 kufuatia hali tete na tata kuhusu sekta ndogo ya gesi asilia nchini na kwa kuzingatia umuhimu na unyeti wa sekta hiyo katika uchumi wa nchi na maisha ya wananchi.

Pamoja na mambo mengine aelekeze kamati hiyo kupokea na kujadili Taarifa ya Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge ya mwaka 2011 kuhusu Sekta Ndogo ya Gesi Asili ikiwemo juu ya hatua iliyofikiwa katika kushughulikia tuhuma za ufisadi, madai ya mapunjo ya fedha za mauzo ya Gesi asili na hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya sera, mpango mkakati na sheria ya gesi asili.

Hatua hii ni muhimu kufuatia ukimya wa Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo kuhusu kauli yangu ya tarehe 4 Oktoba 2012 ya kutaka Taarifa ya ufafanuzi kuhusu utafutaji wa mafuta na gesi asili nchini iliyotolewa na Wizara ya Nishati na Madini tarehe 21 Septemba 2012 ifutwe kwa kuwa italinda ufisadi na kukwaza utetezi wa rasilimali za taifa.

Mnyika: Spika aunde Kamati ya Gesi

WAZIRI Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika, amemtaka Spika wa Bunge, Anna Makinda, kutumia madaraka na mamlaka yake kutangaza kwa umma kamati nyingine ya kudumu ya Bunge itakayoshughulikia masuala ya gesi asili kabla na wakati wa mkutano wa Bunge ujao mwishoni mwa mwezi huu.

Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo kupitia CHADEMA, alisema hatua hiyo ni kutokana na hali tete na tata kuhusu sekta ndogo ya gesi asilia nchini na kwa kuzingatia umuhimu na unyeti wa sekta hiyo katika uchumi wa nchi na maisha ya wananchi.

Thursday, October 11, 2012

NIMECHUKUA HATUA YA KUWASILISHA KWA TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA SUALA LA MATATIZO YA MAJI KATIKA KATA YA GOBA ILI HATUA ZA HARAKA NA ZA KUDUMU ZICHUKULIWE

Kazi ya mbunge ni kuwakilisha wananchi, kushiriki katika kutunga sheria na kuisimamia serikali ili kuwezesha maendeleo kwa pamoja na mambo mengine kuhakikisha huduma za kijamii ikiwemo upatikanaji wa maji zinaboreshwa.

Tarehe 10 Oktoba 2012 ikiwa ni sehemu ya kufanya kazi hiyo nimekwenda kwa niaba ya wananchi Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na kuwasilisha malalamiko ya uvunjwaji wa haki za binadamu za kupata huduma ya maji na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora katika uendeshaji wa miradi ya maji kwenye kata ya Goba katika Manispaa ya Kinondoni.

Wednesday, October 10, 2012

KIJANA AU MDAU WA MASUALA YA VIJANA WIKI YA VIJANA IMEANZA LEO; UMEPANGA KUFANYA KAZI GANI MOJA KWA MUSTAKABALI WA VIJANA NA TAIFA?


Kuanzia leo Oktoba 8 mpaka 14 vijana bila kujali itikadi tunapaswa kuungana kote nchini kuadhimisha wiki ya taifa ya vijana. Hata hivyo, toka wiki hii ilipoanzishwa na Serikali mwaka 2003 imekuwa ikiadhimishwa bila mwitikio wa kiasi cha kutosha katika ngazi mbalimbali isipokuwa katika maeneo ambayo wiki hii imekuwa ikiadhimishwa kitaifa kwa kufanya maonyesho ya namna mbalimbali. Hivyo, nia ya taarifa hii ni kuhimiza vijana, serikali na wadau mbalimbali ili maadhimisho ya mwaka huu yawe na hamasa na maana zaidi kwa maisha ya vijana wa Tanzania na Taifa kwa ujumla.

Aidha, maadhimisho ya kila mwaka ya wiki ya vijana yamekuwa yakichanganywa pamoja na kilele cha mbio za Mwenge na Maadhimisho ya siku ya Mwalimu Nyerere kitaifa. Matokeo yake wiki ya vijana imekuwa ikifunikwa na shamrashamra za mbio za Mwenge na hatimaye kupoteza malengo ya msingi ya kushughulikia masuala yanayowagusa vijana moja kwa moja.

Pia zaidi ya maadhimisho yanafanyika kitaifa Shinyanga ni vyema mkazo ukawekwa katika kufanya maadhimisho katika ngazi mbalimbali hususani wilayani. Hivyo maafisa maendeleo wa vijana wa wilaya walau mwaka huu wajitokeze kutembelea vikundi vya vijana, kuratibu matukio ya asasi za vijana na kuhamasisha mijadala ya vijana kuhusu mustakabali wao na taifa kwa ujumla.

Natoa mwito kwa vijana nchini kushiriki kikamilifu katika maadhimisho ya wiki ya taifa ya vijana ya mwaka huu iliyoanza  Oktoba 8 ambayo kilele chake kitafikia Oktoba 14. Kila kijana wa Tanzania afanye walau kitu kimoja katika wiki hii kama sehemu ya maadhimisho ya wiki ya jamii-kama ni kusaidia wasiojiweza, kufanya usafi wa mazingira, kufanya majadiliano kuhusu mustakabali wa vijana na taifa, kuonana na viongozi kuzungumza nao kuhusu maendeleo katika maeneo yao kuhusu masuala ya elimu, ajira, afya, ukuzaji wa vipaji vya vijana, michezo, ushiriki wa vijana katika uongozi na mengineyo.

Wiki hii ni muhimu kwa sababu kwa upande mmoja, vijana ndio kundi linaloathirika zaidi na mabadiliko ya kisiasa, kiuchumi na kijamii yanayojiri nchini kwetu na duniani kwa ujumla. Kwa upande mwingine vijana ndio chachu ya mabadiliko katika taifa lolote duniani kutokana na nguvu, ubunifu, na uwingi wetu.

NB: Maelezo haya kwa sehemu kubwa yalikuwa sehemu ya Taarifa kwa Umma niliyoitoa tarehe 5 Oktoba, nayasambaza leo kuwakumbusha kwa ajili ya hatua kila mmoja kwa nafsi na nafasi yake.

Maslahi ya umma kwanza.

Sunday, October 7, 2012

KUELEKEA WIKI YA VIJANA: WAZIRI AELEZE HATUA ILIYOFIKIWA KATIKA KUANZISHA BARAZA LA VIJANA, BENKI YA VIJANA NA KUPANUA WIGO WA AJIRA KWA VIJANA

Nikiwa mmoja wa vijana wa Tanzania na mbunge kijana sikubaliani na utaratibu mzima ulivyopangwa wa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dkt Fennela Mukangara kutoa ratiba ya maonyesho na maadhimisho mengine bila kueleza hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa ahadi zilizotolewa kwa vijana katika maadhimisho kama hayo mwaka 2011 na pia kuweka mkazo katika maonyesho katika Mkoa mmoja badala ya masuala na matukio muhimu yenye kugusa maisha ya vijana wa katika maeneo mbalimbali nchini mijini na vijijini.

Ikumbukwe kwamba Tarehe 4 Oktoba 2012 Waziri alizungumza na vyombo vya habari kueleza kuhusu maadhimisho ya Wiki ya Taifa ya Vijana. Waziri alieleza kuwa maadhimisho hayo yatahusisha maonyesho yatakayoanza tarehe 8 na kufikia kilele chake tarehe 14 Oktoba 2012 kwenye kilele cha mbio za Mwenge na kumbukumbu ya kifo cha Mwalimu Nyerere mkoani Shinyanga. Waziri ameeleza kuwa mgeni rasmi katika kilele cha maonyesho na maadhimisho hayo anatarajiwa kuwa Rais Jakaya Kikwete.

Saturday, October 6, 2012

Taarifa ya ufafanuzi kuhusu utafutaji wa mafuta na gesi asili nchini iliyotolewa na Wizara ya Nishati na Madini tarehe 21 Septemba 2012 ifutwe kwa kuwa italinda ufisadi na kukwaza utetezi wa rasilimali za taifa:


Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo afute taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo kuwa lengo la agizo lake la kupitiwa kwa mikataba yote 26 ya utafutaji mafuta na gesi asili ni “kuhakikisha kwamba endapo kuna mapungufu katika mikataba hiyo, mapungufu hayo yasijirudie tena katika mikataba mipya ya baadaye” kwa kuwa ikiachwa ilivyo italinda ufisadi na kukwaza utetezi wa rasilimali za taifa.

Ufafanuzi uliotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini unatoa mwanya kwa mikataba mibovu kulindwa wakati ambapo kuna madai tuliyotoa toka mwaka 2011 kwamba baadhi ya mikataba hiyo imeingiwa kifisadi na mwaka huu wa 2012 zimeibuka tuhuma za vigogo wa serikali kuingiziwa fedha kifisadi katika akaunti zao za nchini Uswisi na makampuni ya nje ya utafutaji mafuta na gesi asili.

Tafsiri ya ufafanuzi huo uliotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini ni kwamba hata kama mikataba iliyopo ina mapungufu yasiyozingatia maslahi ya taifa, matokeo ya mapitio hayo hayatarekebisha mikataba iliyopo bali mikataba ya baadaye.

Taarifa hiyo ya Katibu Mkuu wa Wizara ni ya kurudi nyuma tofauti na kauli za awali za Waziri Muhongo zilizokubaliana na madai yetu ya toka mwaka 2011 ndani na nje ya bunge ikiwemo kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini ya kutaka mikataba yote ipitiwe upya, isiyozingatia maslahi ya taifa ivunjwe au ifanyiwe marekebisho makubwa na mikataba mipya isiingiwe mpaka kwanza kuwepo sera na sheria bora zenye kulinda uchumi na usalama wa nchi.

Itakumbukwa kwamba tarehe 15 Septemba 2012 wakati wa uzinduzi wa Bodi Mpya ya Wakurugenzi ya Shirika la Maendeleo la Petroli Tanzania (TPDC) Waziri wa Nishati na Madini aliagiza bodi hiyo kuipitia mikataba yote 26 ya utafutaji mafuta na gesi asili ili kujiridhisha endapo maslahi ya taifa yalizingatiwa.

Agizo hilo la Waziri limeendana na mapendekezo niliyotoa mwaka 2011 ya kutaka mapitio ya mikataba yote ya mafuta na gesi asili ambapo pamoja na mambo mengine niliitaka Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini na taasisi zake kuacha kuingia mikataba ya muda mrefu  ya utafutaji wa mafuta na gesi asili katika maeneo mbalimbali nchini yenye mianya ya kuhujumu uchumi wa nchi na haki za wananchi masuala ambayo yalipingwa na Waziri wa zamani.

Kutokana na kutozingatiwa kwa mapendekezo hayo tarehe 21 Februari 2012 nilitoa kauli ya kutaka Waziri wa Nishati na Madini wa wakati huo William Ngeleja kuwajibishwa kwa kuendelea kuruhusu kusainiwa kwa mikataba bila maagizo ya msingi kuzingatiwa na kueleza kwa umma sababu za serikali kuendeleza usiri na kuacha kufanya mapitio ya mikataba mibovu iliyopo.

Nilitoa kauli hiyo baada ya tarehe 20 Februari 2012 Serikali kusaini mkataba wa kutafuta mafuta na gesi asili na kampuni ya Swala katika maeneo ya Kilosa Mkoani Morogoro na Pangani Mkoani Tanga na Januari 2012 Serikali kuweka saini mikataba na kampuni za kimataifa za Petrobras Tanzania Ltd, Heritage Rukwa Tanzania Ltd na Motherland Industies Ltd na Oktoba 2011 Serikali kusaini mikataba mingine na kampuni za Ndovu Resource na Heritage Oil za Uingereza kwa ajili ya utafutaji wa nishati ya mafuta na gesi katika kisiwa cha Songosongo na Ziwa Rukwa huku nchi ikiwa haina mwelekeo sahihi wa sera, sheria, mipango na usimamizi wa sekta hizo nyeti kwa usalama na uchumi wa nchi na maisha ya wananchi kwa ujumla.

Waziri Muhongo na Katibu Mkuu Maswi wanapaswa kuendelea kuonyesha kwa maneno na matendo tofauti yao na viongozi waliowatangulia katika Wizara ya Nishati na Madini Waziri Ngeleja na Katibu Mkuu Jairo kwa kutoa ufafanuzi wa ziada na kuchukua hatua zaidi vinginevyo taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa tarehe 21 Septemba 2012 itakuwa ni mwendelezo wa kulinda udhaifu wa kimfumo uliojikita katika Wizara hiyo na serikali kwa ujumla.

Ni vizuri Waziri na Katibu Mkuu wakaendelea kuzingatia ushauri niliwapa bungeni kwamba sehemu kubwa matatizo katika sekta za nishati na madini yamechangiwa na sababu za kibinadamu za kutowajibika ipasavyo kisera, kimaamuzi, kiusimamizi na kiutendaji kwa viongozi wa kiserikali wenye dhamana na watendaji wengine na hivyo kusababisha ugumu wa maisha kwa wananchi na kuathiri uchumi wa nchi; hivyo nguvu zielekezwe katika kurekebisha hali hiyo.

Imetolewa tarehe 4 Oktoba 2012 na:

John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini

Thursday, October 4, 2012

THE PEACE PRAYER


Lord, make me an instrument of your peace.
Where there is hatred, let me sow love.
Where there is injury, pardon.
Where there is doubt, faith.
Where there is despair, hope.
Where there is darkness, light.
Where there is sadness, joy.
O Divine Master,
grant that I may not so much seek to be consoled, as to console;
to be understood, as to understand;
to be loved, as to love.
For it is in giving that we receive.
It is in pardoning that we are pardoned,
and it is in dying that we are born to Eternal Life.
Amen.

NB: October 4th, though in between meetings my thoughts flashed back the memories of the time we spent at San Damiano and the life we lived with OFM friars. During all those years, this prayer was like stigmata in my vision and values. Humanity and humanness requires us (regardless of what we have or who we are) to have humility for humankind. In leadership it should be translated into action through servitude. It reflects The Golden rule, which is not only inherent in all major religions whether Western or Eastern but also entrenched in the African Traditions under UBUNTU. If any of FRASEMA Alumnae reads this memoir please let us get in touch via johnmnyika@gmail.com.  

Wednesday, October 3, 2012

Mnyika ‘akomalia’ ujenzi wa shule na barabara Mburahati

Na Mwandishi Wetu

Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika amesema kuwa mgogoro kuhusu eneo la ujenzi wa Shule ya Sekondari Mburahati umeelekea kupatiwa ufumbuzi ambapo sasa mapendekezo ni kujenga shule hiyo katika mwaka wa fedha 2012/2013 katika eneo la wazi jirani na kituo cha polisi katika kata hiyo hivyo wakazi wanapaswa kutoa maoni yao iwapo pendekezo hilo ni muafaka.