Thursday, December 31, 2009

Mwaka 2010: Pamoja Tunaweza


MWISHO wa mwaka ni wakati wa kutafakari tulikotoka, tulipo na tunakotaka kwenda katika mwaka mpya. Ni kipindi muhimu kwa taasisi na hata watu binafsi kufanya tathmini na kujiwekea malengo. Kwa binadamu mmoja mmoja yanaweza kuwa ni malengo ya kiuchumi, kijamii na hata ya kisiasa.

Maamuzi ya masuala ya kiuchumi na kijamii mara nyingi ni masuala binafsi. Hata hivyo, malengo ya kisiasa hususan yale yanayohusu utumishi wa umma ni muhimu kwa maamuzi yake kufanyika kwa kuzingatia mwelekeo wa kiongozi husika lakini pia kwa kurejea utashi wa wananchi iwe ni faraghani au hadharani.

Hii ni kwa sababu uongozi wa umma wa kuchaguliwa hufanyika katika medani ya demokrasia ambayo inahusisha utawala wa watu kwa ajili ya watu.

Katika uchaguzi yapo mambo manne ya muhimu katika kuhakikisha ushindi. Mosi, ni mgombea: haiba, wasifu na uwezo wake kwa ujumla. Pili ni ajenda: ujumbe wenye dira unawagusa wapiga kura na kuamsha kuungwa mkono.

Tatu ni oganaizesheni: huu ni mtandao mzima wa kuratibu vuguvugu la ushindi, unaweza kuwa wa kijamii, kisiasa ama kitaasisi. Nne, rasilimali: hii ni kwa ajili ya kuwezesha kwa hali na mali kampeni husika, iwe ni fedha, zana, mawazo au nguvu kazi.

Baadhi ya watu hudhani kwamba rasilimali ni jambo la kwanza kuwezesha ushindi, uzoefu wa kimataifa unadhihirisha kuwa katika kufanikisha kampeni za uchaguzi kipaumbele cha kwanza ni mgombea, cha pili ujumbe, cha tatu ni oganaizesheni.

Rasilimali huongezeka kwa kadiri ya tija na ufanisi wa vipaumbele vitatu vinavyotangulia kwa nadra mtiririko huu unaweza kubadilika kutokana na upekee wa kimazingira ya kisiasa.

Tumebakiza siku chache kuingia mwaka 2010, kipindi kingine cha kuelekea uchaguzi mkuu wa udiwani, ubunge na urais nchini. Tayari heka heka zimeshaanza na kauli mbalimbali zimeshaanza kutolewa za kheri na za shari.

Kwa kweli fikra kuhusu uchaguzi ujao zilishaanza toka 14 Desemba mwaka 2005 kwa wale wanaoamini kuwa mwisho wa uchaguzi mmoja ni mwanzo wa uchaguzi mwingine.

Binafsi nakumbuka mwaka huo wa 2005 wakati mjadala ukiendelea kuhusu utata wa matokeo ya uchaguzi wa ubunge katika jimbo la Ubungo ambapo mimi nilikuwa mmoja wa wagombea tayari wadadisi wengine wameanza kuulizia masuala ya uchaguzi wa 2010.

Hali hii ilijitokeza hata katika mkutano wangu na wanahabari Desemba 22, 2005 kwa ajili ya kuwashukuru wapiga kura na kuelezea mafanikio yaliyopatikana, mapungufu yaliyojitokeza na hatua ambazo nilipanga kuzichukua.

Hata baada ya kutoa msimamo huo, bado mjadala uliendelea katika kipindi cha Januari mpaka Mei 2006; takribani nusu mwaka baada ya uchaguzi mkuu kumalizika. '

Hivyo, baadhi ya masuala hayo niliwajibika kuyajibu kupitia hotuba yangu ya kuwashukuru wananchi na kuelekeza mwelekeo niliyohutubua jimboni Ubungo Mei 28, 2006.

Ilinibidi niandike pia waraka kwa wananchi wa ubungo na watanzania Juni 4, 2006 wakati huo nikiwa ziarani nchini Marekani waraka ambao ulisambaa kwa umma kupitia vyombo vya habari na njia zingine za mawasiliano ya umma ikiwemo mikutano ya hadhara niliporejea. Waraka huo uliobeba ujumbe ‘kuvunjika kwa koleo sio mwisho wa uhunzi’ uliweza kutuliza kwa muda mjadala.

Katika waraka huo nilielezea masuala mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa azma ya kufungua kesi namba moja ya mwaka 2006 katika Mahakama Kuu ya Tanzania kupinga matokeo ya uchaguzi wa ubunge katika jimbo la Ubungo.

Kesi hiyo ambayo nilisimamiwa na Wakili Tundu Lissu ilipigwa danadana za kiufundi kipindi chote na kuishia hewani mwaka 2007 kwa kile kilichoelezwa na wakili wangu kuwa ni kukosekana kwa dhamira ya dhati ya kuisikiliza kesi hiyo.

Hata hivyo, miaka takriban mitatu iliyopita ya 2006, 2007, 2008 na hata mwaka huu wa nne unaomalizika wa 2009, swali ambalo nimekuwa nikiulizwa ni kugombea ubunge wa jimbo la Ubungo 2010.
Nimekuwa nikiulizwa swali hili katika mikutano ya hadhara ya kisiasa katika ziara ambazo tumekuwa tukizifanya katika kata zote za jimbo la Ubungo. Katika kipindi chote hicho swali hilo hilo limekuwa likiulizwa hata kwenye shughuli na matukio ya kijamii yawe ni ya kirafiki, kidini, misiba, harusi, michezo, miradi ya jumuiya, ufuatiliaji wa kero za wananchi nk.

Wakati wote majibu yangu yamekuwa kati ya haya matatu nitajibu wakati muafaka ama umma utajibu ama Mungu akipenda! Najua katika kipindi chote majibu haya yamekuwa yakiwaweka katika mkanyiko waulizaji kwa sababu mbalimbali.

Wapo wenye mtazamo kwamba majibu kama hayo ni ishara ya kutokuwa na uhakika ama kupima upepo. Wapo wenye imani kwamba kwenye uongozi wa kuchaguliwa sifa mojawapo ya uongozi ni kuutaka uongozi.

Wapo ambao katika kipindi hicho hicho wamekwenda mbele zaidi kuweka msimamo wao bayana kwamba ni lazima nigombee tamko la wazi la hivi karibuni likiwa ni la mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Makoka na wananchi wa eneo hilo la Novemba 29, 2009. Msimamo huo waliutoa kwenye mkutano wa hadhara wa kuwashukuru wananchi ambao walinialika kama mgeni rasmi.

Kilichonisukuma kuandika makala hii ni majadiliano yanayoendelea hivi sasa kwenye mtandao kupitia www.facebook.com/john.mnyika kuhusu ‘Ubunge Ubungo 2010: Nigombee Nisigombee?’

Wachangiaji wote waliotoa maoni yao mpaka sasa wamenitaka nigombee huku wakitoa sababu mbalimbali. Wapo waliotoa hoja ya kutambua uwezo, haja ya kubeba harakati za kizazi kipya kushiriki kwenye uongozi wa taifa letu, kufanya vizuri mwaka 2005 na kuhoji kuhusu mikakati ya kuhakikisha ushindi mwaka 2010.

Mchangiaji mmoja alirejea mfano wa Barack Obama ambaye alikuwa na mashaka kuhusu kugombea kwake lakini mmoja wa washauri wake wa karibu akamweleza kwamba ‘usipogombea umechagua kushindwa; lakini ukigombea una chaguo la kushinda ama kushindwa’. Walatini wana msemo ‘Sauti ya watu ni sauti ya Mungu’. Si lengo la makala haya kujadili hoja mbalimbali ambazo zimetolewa katika mjadala huo.
Naandika makala kuwezesha tafakari ya wengine ambao ni sehemu ya wapiga kura ama wananchi kwa ujumla hawana fursa ya kushiriki majadiliano kwenye tovuti.

Tafakari pana zaidi tunapoelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010; nini kinawasukuma wagombea kujitokeza kugombea: dhamira binafsi ama msukumo wa umma au vyote?

Mwaka 2005 wakati huo nikiwa na miaka 24 nilipojitokeza kugombea kwa mara ya kwanza nilieleza kwamba ilikuwa ni dhamira yangu binafsi baada ya kuona nina kipawa/kipaji cha uongozi.
Kusukumwa na dhamira ya ndani inaweza kuwa jambo la kawaida kwa mgombea ambaye utumishi wake bado haujaonekana kikamilifu mbele ya umma.
Lakini vipi kwa mgombea ambaye anafahamika tayari: nguvu alizonazo, udhaifu alionao, fursa alizonazo na vikwazo vinavyomkabili, naye asukumwe na dhamira binafsi pekee?
Kwa mgombea ambaye tayari anafahamika ni muhimu pamoja na dhamira yake binafsi pawe pia na msukumo wa umma hii ni kwa sababu nafasi za kuchaguliwa kama ubunge ni za kuwakilisha wananchi.
Ni muhimu sehemu ya wananchi iwe ni wanachama wa chama, wapiga kura ama baadhi ya watu katika jumuia waone haja hiyo.
Kuungwa mkono kwa namna hiyo katika dhamira ya kugombea na kuhusisha umma katika kufikia maamuzi nyeti kama hayo yanaweka msingi muhimu wa kuwa mwakilishi wa wananchi husika na hata kuwashirikisha wananchi katika kukabiliana na changamoto za kimaendeleo.
Kwa upande mwingine, kupanua wigo katika kufikia azma ya kugombea ni njia ya kuunganisha nguvu ya umma hata katika kampeni za uchaguzi. Katika siasa za ushindani ni muhimu harakati za uchaguzi zikaendeshwa katika mfumo wa vuguvugu hususan kwa wagombea wanaopitia vyama mbadala ambavyo havitegemei nguvu ya dola.

Hivyo, ni muhimu kwa yoyote anayetaka fulani agombee katika eneo fulani, mosi, amtake kugombea kama sehemu ya msukumo wa umma. Pili, ajiunge na harakati za kufanikisha ushindi wake kwa hali na mali.
Ushindani wa namna hiyo ulijidhihirisha nchini Marekani mwaka 2008 mpaka 2009 kwa wagombea kuungwa mkono na umma; kuanzia wakati wa kura za maoni za ndani ya vyama mpaka kwenye kampeni za uchaguzi mkuu.

Tunaweza kushiriki kuleta mabadiliko kwa kugombea na kuchaguliwa ama kwa kuchagua viongozi kwa kupiga kura. Ndio maana nachukua fursa hii kuwahimiza Watanzania ambao watakuwa na umri wa miaka 18 na kuendelea mwaka 2010 kutimiza wajibu huu wa kiraia.

Hivyo, kwa wapiga kura wapya na wote ambao kwa sababu moja au nyingine hawana kadi za mpiga kura wajitokeze kujiandikisha kupitia uboreshaji wa daftari la kudumu unaoendelea ambao kwa upande wa Dar es salaam utafanyika mapema mwaka 2010.

Izingatiwe kuwa hii ni awamu ya mwisho kabisa ya mchakato huo; kabla ya uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba hivyo kukosa kujiandikisha ni kujikosesha haki ya kikatiba ya kuchagua kiongozi unayemtaka.
Hata hivyo, izingatiwe kuwa kushiriki kuleta mabadiliko ni zaidi ya matukio ya kugombea ama kupiga kura ni pamoja na kushiriki katika mchakato mzima wa kuleta mabadiliko kwa njia mbalimbali. Mwito wa Mahatma Gandhi kuwa wakala wa mabadiliko unayotoka kuyaona’ unabeba dhana hii.

Swali la kujiuliza, je wewe uko tayari kuwa wakala wa mabadiliko unayotaka kuyaona? Kama Ndio; je umeshawasiliana na chama ambacho unaamini ni chombo cha kuwezesha mabadiliko hayo na kuwaunga mkono viongozi hata ikiwa ni kwa kuwapa ushauri? Ama umeshashirikiana kwa hali na mali au walau kuwasiliana na mgombea mtarajiwa ambaye unaamini anaweza kupeperusha bendera ya kuongoza mabadiliko?

Kugombea nafasi za kuchaguliwa zinazohusisha kuwakilisha umma hakupaswi kuwa suala la mtu binafsi. Matokeo ya kuwaachia wagombea binafsi ama vyama vyao pekee ni kuwa na viongozi ambao baada ya kuchaguliwa kwao kwa sababu waliingia kwa dhamira zao na wakafanya kampeni ‘kivyaovyao’; hawawajibiki kwa umma.
Hivyo tunapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ni muhimu kwa wapiga kura na wananchi kwa ujumla kutambua kwamba suala la uongozi wa kuchaguliwa kuwakilisha umma ni wajibu wa pamoja.
Ni wajibu wa yoyote anayetambua kwamba Mwenyezi Mungu ameijalia nchi yetu na watu wake rasilimali; iwe ni vipaji vyetu, kodi zetu ama maliasili: Hivyo tunawajibika kujenga taifa lenye kutoa fursa ya ustawi wa wananchi. Pamoja Tunaweza!

Ni wajibu wa pamoja wa watumishi wa umma iwe ni walimu, polisi, wahudumu wa sekta ya afya n.k, ama wafanyakazi binafsi ambao wanataka mabadiliko kutoka katika mishahara midogo na mazingira magumu ya kazi, maslahi duni na kujenga taifa lenye kuthamini utaalamu. Pamoja Tunaweza!

Ni wajibu wa wazazi, wanafunzi, wazee, wanawake na masikini kwa ujumla wenye kuathirika na kuongezeka kwa gharama za maisha na kuporomoka kwa huduma za kijamii nchini iwe ni elimu, afya, maji, mafao ya wastaafu na waotaka pawepo mifumo thabiti ya usalama na haki katika jamii ili kuepusha migogoro. Pamoja Tunaweza.

Ni wajibu wa Watanzania wote wenye kukerwa na ufisadi unaolitafuna taifa huku hatua zinazostahili kushindwa kuchukuliwa kutokana na ufisadi kutapakaa katika mfumo mzima wa utawala na kuteteresha hata utawala wa sheria. Tufanye mabadiliko turejeshe uwajibikaji na maadili ya taifa. Pamoja Tunaweza!

Ni wajibu wa matajiri na wenye fursa wanaoona hatari inayolinyemelea taifa kutokana na kuongezeka kwa pengo kati ya wenye nacho na wasiokuwa nacho, ukosefu wa ajira hususani kwa vijana nk ambayo ni mabomu ya wakati yenye athari vizazi hata vizazi yanayoweza kuepukwa kwa kuweka pembeni ubinafsi na kujali maendeleo ya sekta zinazogusa mustakabali wa waliopembezoni. Pamoja Tunaweza!

Ni wajibu wa wapenda demokrasia wote wanaotambua kwamba hujuma za kwenye uchaguzi zinaweza kudhibitiwa kwa kuunganisha nguvu ya umma ikiwemo kwa kujenga vuguvugu thabiti la ulinzi wa kura. Pamoja Tunaweza!

Tukumbuke; mabadiliko ya kweli katika taifa letu hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile, chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale. Kwa falsafa ya Chukua Chako Mapema; Tanzania yenye neema haiwezekani. Tuunganishe nguvu kubadili mfumo wa utawala; mabadiliko yanawezekana.

Tunahitaji uongozi wenye dira na uadilifu wa kulikomboa taifa; hivyo ni jukumu letu sote kuhakikisha viongozi tunaowahitaji wanashinda. Kwa maneno ya Mwalimu Nyerere jukumu la namna hii linaweza kutekelezwa kama kila mmoja akitimiza wajibu wake; umoja ni nguvu. Kidole kimoja hakivunji chawa; kuelekea uchaguzi mkuu 2010: pamoja tunaweza!
John Mnyika anapatikana kupitia 0754694553 na mnyika@chadema.or.tz; makala hii imetoka: http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=11672

Wednesday, December 30, 2009

UN na usalama wa raia toeni taarifa

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


UN ITOE TAMKO RASMI KUHUSU KIKAO CHA BARAZA LA USALAMA KILICHOJADILI TAARIFA YA TIMU YA WATAALAM JUU YA USAFIRISHAJI WA SILAHA NA UTOROSHAJI WA DHAHABU HARAMU DRC

Wizara ya Usalama wa Raia watoe kauli kuhusu hatua zilizofikiwa katika kumchunguza Bande Ndagundi na wengine wanaotajwa kwenye mtandao wa biashara ya silaha wanaoishi Tanzania

Kurugenzi ya Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa (CHADEMA) inauomba Umoja wa Mataifa (UN) kutoa tamko rasmi kuhusu matokeo ya kikao cha Baraza la Usalama la UN kilichojadili hivi karibuni taarifa ya Timu ya Wataalamu iliyoundwa na umoja huo kufuatilia utekelezaji wa maazio ya UN kuhusu vita DRC ikiwemo usafirishaji wa silaha na utoroshaji wa dhahabu katika maeneo husika.

Haja ya kutaka tamko rasmi toka UN inatokana na taarifa zinazoendelea kusambaa kwa njia ya mtandao zinazoonyesha kwamba tayari vikao rasmi vya UN vimeshaijadili taarifa hiyo. Baadhi ya taarifa hizo ni pamoja na Ripoti Maalumu(Special Report) ya jarida la kimataifa la Africa Confidential ya hivi karibuni(inayopatikana kupitia
www.africa-confidential.com) taarifa hizo zinaonyesha kwamba Baraza la Usalama limekaa Novemba 20; Novemba 25 na mwezi Disemba kupitia taarifa husika.

Ni muhimu kwa Umoja wa Mataifa kutoa tamko hivi sasa kwa kuwa mwanzoni mwa mwezi Disemba UN kupitia ofisi yake ya Tanzania ulieleza kwamba taarifa ya timu ya wataalamu haikuwa rasmi mpaka baada ya kujadiliwa na vikao hivyo; sasa kama tayari vikao hivyo vimeshakaa kama inavyodokezwa katika vyanzo hivyo vya kimataifa ni wakati wa umoja wa mataifa kutoa tamko rasmi kuhusu maudhui ya ripoti yake rasmi.

Pia kwa kuwa serikali ya Tanzania ilitoa kauli kupitia Balozi wetu wa Kudumu katika Umoja wa Mataifa, Dr Augustine Mahiga kwamba ingewasilisha taarifa ya ufafanuzi wake kuhusu tuhuma zilizomo kwenye ripoti hiyo zinazoitaja taasisi za Tanzania na baadhi ya watanzania; ni wakati muafaka wa ripoti hiyo ya Serikali ya Tanzania kama imeshawasilishwa nayo kuwekwa hadharani na Wizara ya Mambo ya Nje au UN.

UN izingatie kuwa mpaka sasa Wizara ya Mambo ya Nje haijawasiliana rasmi na wawakilishi wa wananchi(wabunge), vyama vya siasa na wadau wengine wa msingi kupata maoni yao kuhusu tuhuma zilizomo kwenye ripoti husika ili kutoa msimamo wa pamoja hivyo ni muhimu kwa milango ya majadiliano kuhusu suala hili kuendelea kufunguliwa.

Tunapenda pia kuukumbusha Umoja wa Mataifa(UN) kuwa hali hii ya Serikali ya CCM kutoshirikisha vyama vingine na wadau wengine katika maamuzi ya msingi yanayohusu taifa inachangiwa hodhi (monopoly) ya chama kimoja bungeni; na hivyo kupunguza uwezo wa kambi ya upinzani kuiwajibisha serikali kikamilifu.

Hivyo, wakati tunatafakari ripoti ya Kikundi cha Wataalamu kilichoundwa UN; ni wasaa pia wa UN Tanzania kupitia UNDP kuongeza kasi ya kuisimamia serikali kutekeleza marekebisho ya kisheria na kitaasisi ya kuwezesha uchaguzi wa 2010 kuwa huru na haki. Hii ni kupitia programu yake ya kusimika demokrasia (deepening democracy program) na kusimamia vizuri mfuko wa uchaguzi wa mwaka 2010 (UN Basket Fund for Elections).

Wakati huo huo: Kurugenzi ya Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa(CHADEMA) inaitaka Wizara ya Usalama wa Raia kauli kuhusu hatua zilizofikiwa katika kumchunguza Bande Ndagundi na wengine wanaotajwa kwenye mtandao wa biashara ya silaha wanaoishi Tanzania.

Itakumbukwa kwamba mwanzoni mwa mwezi Disemba Jeshi la Polisi kupitia kwa Mkuu wa Jeshi hilo(IGP) na Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Jinai (DCI) walitoa kauli kwamba jeshi hilo limeanzisha uchunguzi wa kina kuhusu wote waliotuhumiwa kwenye ripoti hiyo.

Mwezi unaelekea kumalizika bila taarifa kutolewa kuhusu kuendelea kwa uchunguzi huo; pamoja na kuwa masuala ya uchunguzi mengine ni ya siri, lakini hatua za mchakato wa uchunguzi ni jambo la kawaida kuelezwa ili kujenga imani kwa umma na wadau wote kwamba serikali imezipa uzito unaostahili tuhuma hizi kwa lengo la kusafisha taswira ya taifa letu kwa wananchi wake na jamii ya kimataifa kwa ujumla.

Ikumbukwe kwamba Jeshi la Polisi limekuwa likitoa taarifa kuwa linafanya uchunguzi wa kina lakini baada ya hapo uchunguzi unaishia hewani ama matokeo yake hayawekwi hadharani. Mathalani mpaka sasa Jeshi la Polisi halijaeleza hatua zilizochukuliwa katika sakata ya Dr Wilbroad Slaa(Mb) kuwekewa vinasa sauti chumbani kwake; tuhuma za kushambuliwa kiharahamia viongozi wa CHADEMA zinazohusisha viongozi wa CCM katika chaguzi ndogo za Kiteto, Busanda na Biharamulo; nk.


Imetolewa tarehe 30 Disemba 2009 na:




John Mnyika
Mkurugenzi wa Mambo ya Nje
mnyika@chadema.or.tz
0754694553

Tuesday, December 29, 2009

Mwaka 2009 umeanza na kuisha kwa ufisadi na malumbano bila uwajibikaji

Mwisho wa mwaka ni wakati wa kutafakari tulipotoka, tulipo na tunapotaka kwenda katika mwaka mpya. Kwa taifa ni fursa ya kufanya tafakari hiyo katika muktadha wa hali na mwelekeo wa taifa kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Yapo masuala na matukio mengi ambayo tunaweza kushawishika kuyatafakari mathalani: hali ya mwaka huu wa 2009 kugubikwa na migomo mbalimbali vyuoni, makazini nk; kutetereshwa kwa misingi ya utawala wa sheria na haki kwa kurejea hukumu ya kesi ya Zombe na wenzake, kesi ya Dereva wa Mohamed Trans, kesi ya Ajali ya Chenge inayoendelea, kesi za Mramba, Yona, Liumba nk; yaliyojiri ndani ya CHADEMA wakati wa mchakato wa uchaguzi wa ndani ya chama; mabomu ya Mbagala; ripoti ya UN na tuhuma kwa Tanzania na watanzania kuhusu silaha nk; ajali na maafa mbalimbali; kuzinduliwa kwa mkakati wa kilimo kwanza; chaguzi za marudio Busanda na Biharamulo; hali ya kisiasa Zanzibar; orodha ni ndefu sana.

Lakini kwa Tanzania toka CHADEMA na viongozi wake kwa kushirikiana na vyama vingine tutoe orodha ya mafisadi (list of shame) mnamo Septemba 15, 2007; ni vigumu kutathmini na kupanga mikakati ya kidemokrasia na kupanga dira ya maendeleo bila kutafakari kuhusu hoja ya ufisadi na haja ya uwajibikaji katika taifa letu.

Hivyo katika kuyatafakari masuala na matukio yaliyojitokeza mwaka 2009 ni muhimu kujadili jinsi mwaka husika ulivyoanza na kuisha kwa ufisadi na malumbano bila uwajibikaji kamili wenye kukabiliana na changamoto za ujinga, umasikini na maradhi katika nchi yetu ambayo Mwenyezi Mungu ameijadilia utajiri wa rasilimali.

Mwaka ulianza mwezi Januari 2009 kwa malumbano yaliyotokana na malalamiko ya Salum Londa (Mjumbe wa NEC CCM na Meya wa Manispaa ya Kinondoni) na Yusuph Makamba (Katibu Mkuu wa CCM) yaliyotokana na kauli ya Halima Mdee bungeni mwishoni 2008, akimtuhumu Makamba “kumlinda” Meya Londa, ambaye alisema anatuhumiwa kwa ufisadi, matumizi mabaya ya madaraka na uuzaji wa viwanja maeneo ya Kawe, Kinondoni. Kwa hiyo, mwaka ulianza kwa tuhuma za ufisadi zilizohusu Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni; manispaa ambayo sehemu kubwa ya viongozi wakuu wa serikali na vyama vya siasa wanaishi.

Mwaka unaisha mwezi Disemba 2009 jinamizi la ufisadi limeendelea kuinyemelea Manispaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam, baada ya kukubali kuuziwa matrekta 27 ya kuzoa takataka yasiyokuwa na viwango kutoka kwa mfanyabiashara, Yusuf Manji. Dalili za kuwepo vitendo vya ufisadi zimeonekana wazi baada ya Baraza la Madiwani la Manispaa hiyo ambalo ndilo lililopitisha zabuni hiyo kugawanyika katika makundi mawili na kuendeleza malumbano bila uwajibikaji. Lakini tuhuma dhidi ya halmashauri hii haziishii kwenye zabuni pekee bali uuzaji na umilikishaji wa ardhi kinyume cha taratibu mathalani Eneo la Ufukwe wa Coco (coco beach) na umegaji wa kiwanja cha shule ya Msingi Kawe nk. Naandika haya mkononi mwangu nikiwa na taarifa ya siri yenye mihutasari na saini za viongozi wa CCM na Halmashauri ya Kinondoni ambazo zinathibitisha wazi kabisa tuhuma hizo zikitaja kwa majina na viwango vya rushwa ambazo zilitolewa ikiwemo kwa madiwani katika kashfa hizo. Taarifa hizo nitaendelea kuziweka hadharani mwaka 2010 kwa lengo la kuchochea uwajibikaji na mabadiliko ya kweli.

Ikumbukwe kwamba kauli za kupinga ufisadi ziliendelea mwezi Februari, mathalani Dk Wilbroad Slaa akihutubia wananchi sokoni Kariakoo Dar es salaam, katika mkutano wa Operesheni Sangara alirudia mwito wa kutaka Rais Mstaafu Mkapa ashtakiwe kufanya biashara akiwa Ikulu; kuchukua Kiwira kwa bei chee na kushinikiza kulazimisha wabunge waivunje NBC yeye kuchota Milioni 500 kutoka ABSA kama cha juu. Katika mkutano huo uliorejewa na vyombo vya habari Dr Slaa alitetea msimamo wake kuhusu posho za wabunge akieleza dhambi kwa yeye kupokea 180,000 kwa siku wakati walimu wanapokea kiasi hicho kwa mwezi. Mishahara na posho za wabunge ni moja ya masuala yaliyozusha malumbano na mgawanyiko hususani miongoni mwa wabunge katika mwaka huu unaomalizika na kuendeleza mjadala kuhusu kukosekana kwa usawa katika mgawanyo wa keki ya taifa katika nchi yetu.

Mwezi Machi; Wakati sakata la ujenzi wa maghorofa pacha ya Benki Kuu ya Tanzania (BOT) likinguruma mahakamani kwa kushitakiwa maofisa wake wawili waandamizi, tuhuma nyingine za ziada zikajitokeza tena kuhusu ujenzi wa majengo hayo. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh, akathibitisha tuhuma hizo kwa kutamka hadharani kuwa Taasisi ya Kuchunguza na Kudhibiti Rushwa (Takukuru) kuchunguza mashaka yaliyomo kwenye mkataba wa bima wa ujenzi wa maghorofa hayo na kuchukua hatua stahili. Ilibainika kuwa mkataba wa bima wa ujenzi wa makao makuu ya BoT unaacha maswali mengi kutokana na kuwa na mapungufu kadhaa mathalani kukosekana kwa dhamana ya bima, gharama za bima zilizolipwa kuonekana zimezidi kiwango, kuingia mikataba miwili inayofanana na kuwepo kwa taarifa zinazokinzana kwenye mkataba wa bima wa awamu ya pili; ujumla tuhuma hizo zilihusu matumizi ya zaidi ya bilioni 10 za kitanzania. Mwezi huu wa Disemba mwaka unaishia kwa tuhuma zingine hivi sasa zikuhusu matumizi ya anasa ya zaidi ya Bilioni moja(yaani milioni zaidi ya 1000) kutumika kwa ujenzi wa nyumba ya gavana wa BOT ndani ya mkoa wa Dar es salaam ambapo wananchi wakufa kwa magonjwa yanayotibika kwa kukosekana kwa dawa katika hospitali za serikali; huku malumbano yakiendelea bila uwajibikaji.

Mwezi Aprili 2009 zikatolewa taarifa za ziada ufisadi uliojikita zaidi katika Wizara ya Maliasili na Utalii. Ukaanikwa mtandao wa rushwa, ukiukaji sheria na kanuni za matumizi ya fedha za umma, unafanywa na maofisa wa wizara hiyo; kwa kiwango kikubwa ukiibuliwa kutokana serikali ya Norway inayofadhili mradi wa matumizi bora ya maliasili kushindwa kuivumilia hali hiyo iliyokuwa ikiendelea chini kwa chini kwa muda mrefu. Katika taarifa ya tathmini ya matumizi ya fedha za wafadhili wa Norway ambayo ilitolewa kipindi hicho, maofisa wa wizara hiyo si tu walithibitika kuwa mafisadi, walionekana pia kufanya vitendo kadhaa vya jinai, ikiwa ni pamoja na kughushi nyaraka kwa lengo la kufanya ubadhirifu. Hii ni kwa mujibu wa ripoti ya ukaguzi wa matumizi ya fedha kwa miradi mitano, iliyokuwa chini ya Programu ya Udhibiti wa Maliasili (MNRP) ulifanywa na Athur Andreasen na Kailas Bhattbhatt ambayo ilianika kwa maelezo na vielelezo ufisadi na ubadhirifu huo uliohusu mabilioni ya fedha.

Mwishoni mwa Mwezi Aprili 2009, msamiati ambao ulipotolewa kupitia orodha ya mafisadi 15 Septemba 2007 ulikuwa mgeni kwa wananchi walio wengi ambao walizoea kutumia neno rushwa; ukapata mwenza wake.

Hali hii ilitokana na Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, kuwataja watu watano wanaotuhumiwa kuhusika na ufisadi mkubwa nchini ambao aliwaita ‘mafisadi papa’ na kuitaka serikali iwashughulikie haraka iwezekanavyo ili kuinusuru nchi kuyumbishwa nao. Hatua hiyo ilizua malumbano makali zaidi ambayo wengine walifikia hatua ya kuona kwamba yangeligawa taifa na kusababisha uvunjaji wa amani.

Mwanzoni mwa mwezi Mei mmoja wa ‘mafisadi papa’ Rostam Aziz(Mbunge wa Igunga CCM) akajitokeza na badala ya kujibu tuhuma yeye akaishia kuja na msamiati mwingine ‘fisadi nyangumi’; hali hiyo ilisababisha miezi miwili iliyofuatia kugubikwa na malumbano bila uwajibikaji. Hiyo ilikuwa ni awamu ya kwanza ya mwaka wa 2009.

Hali hiyo imejirudia tena katika awamu ya pili ya kufungia mwaka 2009; mafisadi wameendelea kuachwa wakitamba na kuliteteresha taifa. Mtiririko wa matukio unaonyesha kwamba CCM imetekwa na mafisadi, mivutano ndani ya NEC yao na mpasuko wa dhahiri katika kikao cha Wabunge wao na wazee wa chama chao cha hivi karibuni Dodoma na kauli zilizofuatia baada ya hapo za kulumbana hadharani bila uwajibikaji; ni ishara za hali hiyo. Katikati ya malumbano hayo alikuwemo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais(Utawala Bora), Sophia Simba ambaye kwa nafasi yake kama waziri ambaye anasimamia taasisi nyeti kama usalama wa taifa na ile ya kuzuia na kudhibiti rushwa(TAKUKURU) na kudhihirisha rangi halisi za watawala walioko madarakani na haya ya kubadili mfumo mzima wa utawala.

Mwezi Julai 2009 ilitoka kauli ya matumaini kwamba bado wapo watanzania wanaotaka uwajibikaji. Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana nchini, Mhashamu Dk. Valentino Mokiwa, alitaka serikali kuziendesha kesi za ufisadi kwa kasi, vinginevyo zitaonekana kama ni usanii kwa wananchi; akitoa mwito kwamba kesi hizo zimalizike kabla ya mwaka 2010 ili taifa liweze kusonga mbele.

Kauli hiyo ilitolewa wakati ambapo taifa likiwa katika malumbano kuhusu waraka wa wakatoliki. Kwa ujumla, mjadala kuhusu waraka huo ulionekana kuligawa taifa katika makundi mawili makubwa; ndani ya bunge na nje ya bunge. Hata vyama vya siasa navyo viligawanyika katika makundi mawili; vingine vikiutetea waraka huo na vingine vikiupinga. Mwezi mmoja baadaye, mnamo Agosti ukatolewa waraka mwingine- waraka wa waislamu. Hata hivyo, katika hali ilizua malumbano mengine tofauti yenye ishara ya mgawanyiko kuhusu waraka huo; wakati kiongozi wa Kamati Kuu ya Saisa ya Shura ya Maimamu Tanzania, Amiry Mussa Kundecha anatangaza kuzindua waraka huo; Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) likatoa kauli kuwa halikuwa taarifa kuhusu kuzinduliwa kwa waraka huo na wala halihusiki.

Kuna mambo kadhaa ya kutafakari kutokana na masuala na matukio hayo: Mosi, ni ishara ya kupanuka kwa mapambano dhidi ya ufisadi, ambayo mwanzoni yalibezwa kuwa ni chuki ya CHADEMA na wapinzani wengine dhidi ya serikali. Kutolewa kwa nyaraka hizo ni ishara ya viongozi wa dini kuingia katika vita hii wakijikita zaidi katika kuhamasisha haki na kupinga aina zote za dhambi na dhulma kama sehemu ya kusimamia maadili. Pili, ni kuibuka kwa mjadala wa nafasi ya dini katika siasa hususani katika uchaguzi. Ni wazi kwamba mgawanyiko wa kimtazamo na kimaamuzi kuhusu matukio hayo na masuala yaliyojitokeza utakuwa ni moja ya hoja na changamoto za msingi tunapoelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Kutokana na matukio na masuala hayo; mikutano ya Bunge la Bajeti lililoanza mwezi Julai na hata Mkutano wa mwezi Novemba 2009 yalijitokeza mambo ambayo yaacha maswali kuhusu dhamira yetu ya pamoja ya kupambana na ufisadi na kutetea rasimali za taifa.

Pamoja na Spika wa Bunge kuapa kwamba suala la utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu Richmond kumalizika kikao cha Novemba; kikao kimemalizika bila suala hilo kumalizika. Ufisadi wa EPA nawe umefanyiwa usanii wa hali ya juu wa kisiasa, kwa bahati mbaya ukiongozwa na mkuu wa nchi. Hotuba ya Rais Kikwete aliyoitoa bungeni ya kutamka msamaha kwa waliorejesha fedha za wizi; ni sehemu ya hali hiyo. Mhimili wa Bunge, umeshindwa kumwajibisha Rais katika hili kwani hata hotuba hiyo ya Rais pamoja na ahadi za Spika kuwa ingejadiliwa bungeni mpaka leo haijawahi kutolewa. Nachukua fursa hii kutoa mwito kwa ikulu kuiweka wazi Hotuba hiyo ya Rais Kikwete ijadiliwe na umma; kwani muda mrefu sana umepita toka tuelezwe kwamba hotuba hiyo imerudishwa ikulu ‘kukarabatiwa’. Kushindwa huku kuwa na kumbukumbu za Bunge zilizohadharani (Hansard) za suala nyeti kama hili la Hotuba ya Rais Bungeni kuhusu hali ya taifa (state of the nation address) na aibu kwa Spika aliyetangaza kuendesha bunge kwa viwango na kasi.

Funga mwaka ikawa ni masuala yaliyojiri kwenye kongamano la Mwalimu Nyerere mwanzoni mwa Mwezi Disemba na matokeo ya mjadala uliofuatia baada ya tukio hilo wa takribani mwezi mzima ambalo limeanika hadharani uongozi ulioko madarakani hususani namna ambayo wako tayari kutetea ufisadi. Kinara wa siasa hizo za ‘mipasho’ akiwa ni Katibu Mkuu wa chama kinachotawala(CCM), Yusuph Makamba. Ama kwa hakika mwaka huu ulikuwa na kauli ambazo ni aibu kwa taifa na zinafaa kuhifadhiwa kwa ajili ya kumbukumbu za vizazi vijavyo. Lakini watanzania wakumbuke kwamba kutekwa huku na mafisadi, chanzo chake ni viongozi wengi walioko madarakani kuingizwa kwa nguvu ya fedha za ufisadi.

Hali hii inatufanya tukumbuke; mabadiliko ya kweli katika taifa letu hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile, chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale. Kwa falsafa ya chukua chako mapema; Tanzania yenye neema haiwezekani. Tuunganishe nguvu kubadili mfumo wa utawala; mabadiliko yanawezekana. Tunahitaji uongozi wenye dira na uadilifu wa kulikomboa taifa; mwaka 2010 tuache malumbano tusimamie uwajibikaji.

Saturday, December 26, 2009

Miaka 48 ya Uhuru: Tusake mabadiliko ya kweli tupate uhuru wa kweli-3

Katika makala zangu zilizotangulia nilieleza kwamba kumbukumbu ya miaka ni wakati wa kutafakari taifa letu lilipotoka, lilipo na tunapotaka liende. Katika makala hizo niliitathmini hali ya kiuchumi na kijamii miaka 48 baada ya uhuru na kuhimitimisha kwamba; uhuru wa kiuchumi na kijamii katika taifa letu utapatikana kupitia mabadiliko ya kweli, yenye kuhimili misukosuko ya ukoloni mamboleo; na kujenga taifa lenye kutumia vizuri rasilimali katika kutoa fursa kwa raia wake huku likilinda utadamuni za haki za kijamii (social justice). Katika makala hii nigeukie tathmini ya kisiasa nikiamini kwamba takafakari kuhusu uhuru haipaswi kufanyika tarehe 9 Disemba pekee bali ni mchakato unaopaswa kuendelezwa na mtanzania yoyote mwenye kuamini kwamba uhuru wa kweli, si uhuru wa bendera bali ni uhuru dhidi ya umasikini, ujinga, maradhi na ufisadi. Uhuru wa kweli, ni uhuru wenye kuleta maendeleo kisiasa, kijamii na kiuchumi.

Mwaka 1961, tulipata uhuru wa kisiasa wa kujitawala na kufanya maamuzi ya kisiasa kwa kushusha bendera ya mkoloni na kupandisha ya Tanganyika. Hii ilikuwa pia ishara ya kubadili watawala kutoka wakoloni kwenda kwa viongozi wazawa kupitia chama cha TANU. Lakini je, ni kweli tuna uhuru wa kweli wa kisiasa ama tuna uhuru wa bendera?

Baada ya Uhuru, viongozi wa kwanza wakiongozwa na Mwalimu Nyerere walianza mikakati ya kujenga taifa (National Building) kwa kuchukua maamuzi magumu ya kujaribu kuleta uhuru na umoja. Kuanzia katika maamuzi kama ya ‘uhuru na umoja’, ‘uhuru na kazi’ na hata baadaye ‘uhuru na maendeleo’; huku kauli mbiu kama ‘siasa ni kilimo’ zikitumika kusukuma ajenda husika.

Baadhi ya maamuzi magumu ya kisiasa ni pamoja na: Muungano katika ya Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964; kufutwa kwa Mfumo wa Vyama vingi mwaka 1965; kutangazwa kwa Azimio la Arusha mwaka 1967 kulikofuatiwa na utaifishaji (nationalization) wa njia kuu za kiuchumi- kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kufuata siasa ya ujamaa na kujitegemea; kufutwa kwa dhana ya serikali za mitaa mwaka 1972 na kuanzishwa kwa madaraka mikoani nk. Kwa ujumla kati ya kipindi cha mwaka 1961 mpaka 1985 taifa lilioongozwa kufanya maamuzi mengi ya kisiasa yenye taathira kubwa ya kiuchumi na kisiasa ambayo inaonekana hadi leo. Si lengo la makala haya kuchambua kila uamuzi na faida na hasara zake; katika kipindi husika ambacho Urais wa taifa letu uliongozwa na Mwalimu Julius Nyerere.

Kwa ujumla maamuzi mengi yaliyofanyika wakati huo yaliwezesha kujengwa kwa taifa lenye umoja; hata hivyo maamuzi hayo hayo yamedumaza utamaduni wa ushindani katika taifa letu iwe ni kwenye sekta za kiuchumi na hata siasa yenyewe. Mathalani, uamuzi wa kufanya chama kishike hatamu, ulifanya moja kwa moja taasisi ambazo zinapawa kuwa huru kugeuzwa kuwa mihimili ya chama kinachotawala; kuanzia vyama vya wafanyakazi, asasi za kiraia na hata jeshi ambalo baada ya maasi(mutiny) ya mwaka 1964, jeshi mpya la wazalendo(JWTZ) liliundwa na askari kutoka umoja wa vijana wa TANU(TYL). Uhuru wa fikra uliminywa kiitikadi, kisheria na kimatendo kwa kutumia kivuli cha kutaka kujenga umoja wa kitaifa. Wakati huo huo, katika kipindi husika kuliendelezwa kwa kiasi kikubwa sheria na mfumo wa utawala tuliorithi kutoka kwa mkoloni.

Awamu ya Pili ya Utawala Tanzania kati ya mwaka 1985 mpaka mwaka 1995 chini ya Rais wa wakati huo- Ali Hassan Mwinyi; nao ulikuwa na maamuzi yake ambayo ni muhimu kukumbukwa kihistoria. Kwa kiasi kikubwa maamuzi hayo ya kisiasa yakifanyika kwa shinikizo kutoka nje, ambapo maamuzi ya kiuchumi ndiyo kwa kiwango kikubwa yaliyokuwa yakiamua hatma ya mwelekeo wa kisiasa. Kwa masharti ya Benki ya Dunia (WB) na Taasisi ya Fedha ya Kimataifa(IMF), Tanzania ikafanya ‘geuka nyuma’ ya kisiasa, kwa maelezo ya kufuata sera za ubinafsishaji na soko huria. Kumbe mambo yote yalikuwa ni barakoa (mask) ya kutupeleka kwenye utamaduni wa ubinafsi na soko holela. Kati ya matukio ya kukumbukwa wakati huo ni pamoja na: Maamuzi ya Zanzibar ya mwaka 1991 ambayo yalifuta misingi muhimu ya Azimio la Arusha, hususani iliyohusu maadili ya uongozi na nchi kuingia katika mfumo wa vyama vingi mwaka 1992. Hata hivyo, mageuzi yote hayakuendena na kuandikwa kwa katiba mpya, na matokeo yake ni sheria na hata utamaduni wa kisiasa kuendeleza misingi ya chama tawala kuwa chama dola; mithili ya nchi kuendelea kuwa katika mfumo wa chama kimoja. Ripoti za Tume ya Nyalali na Tume ya Kisanga zinaweza kutupa picha ya ziada ya hali ya kisiasa katika kipindi husika na maamuzi ambayo yalipaswa kufanyika.

Awamu ya tatu ya utawala chini ya urais wa Benjamin Mkapa kati ya mwaka 1995 mpaka mwaka 2005 ulitaasisisha misingi ya soko holela na ubinafsi na hivyo kuliondoa taifa katika misingi ya uwajibikaji na kulitumbikiza katika utamaduni wa ufisadi. Ukiweka katika mizani, mafanikio ya Mkapa katika kuweka misingi ya kiuchumi iliyojikita zaidi katika utandawazi, uwekezaji wa kigeni na unyonyaji wa kodi toka kwa wananchi masikini hayawezi kulingana na hasara ya ufisadi na uuzaji wa rasilimali ambao ulifanyika katika awamu yake ya utawala. Ni katika kipindi hicho hicho ambacho maamuzi ya siasa zetu katika uchaguzi, yameanza kuwekwa katika nguvu zilizo nje ya nguvu ya umma wa watanzania. Uhuru wa kisiasa unazidi kuterereka kwa uhuru wa kiuchumi kupotea na taratibu tumeingia katika ukoloni mamboleo huku watawala wa ndani wakiwa ni makuwadi tu wa siasa za nje zinazotuongoza.

Awamu ya nne imeingia mwaka 2005 chini ya Rais Jakaya Kikwete na kuahidi kuendeleza yale yaliyoachwa na awamu ya tatu kwa ari, nguvu na kasi mpya. Kauli tata baada ya safari za mara kwa mara za nje ya nchi na hali tete ya migogoro katika sekta ya ardhi hususani kati ya wawekezaji kutoka nje na wazawa ni mambo ambayo yanahitaji tafakari ya kina tupate mwelekeo mbadala wa kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Miaka 48 baada ya uhuru; tumeweka reheni uhuru wetu wa kisiasa; CCM imeshindwa kutoa uongozi wa kisiasa na kufanya taifa kudumbukia katika siasa chafu na uongozi mbovu. Ombwe hili la uongozi, lenye ishara zote za kushindwa kufanya maamuzi bora katika masuala ya msingi yanayolikabili taifa; limesababisha misingi ya haki na utawala wa sheria inazidi kupuuzwa.

Toka CHADEMA na viongozi wake kwa kushirikiana na vyama vingine tutoe orodha ya mafisadi (list of shame) mnamo Septemba 15, 2007; mafisadi wameendelea kuachwa wakitamba na kuliteteresha taifa. Mtiririko wa matukio unaonyesha kwamba CCM imetekwa na mafisadi, mivutano ndani ya NEC yao na mpasuko wa dhahiri katika kikao cha Wabunge wao na wazee wa chama chao cha hivi karibuni Dodoma; ni ishara za hali hiyo. Lakini watanzania wakumbuke kwamba kutekwa huku na mafisadi, chanzo chake ni viongozi wengi walioko madarakani kuingizwa kwa nguvu ya fedha za ufisadi. Pamoja na Spika wa Bunge kuapa kwamba suala la utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu Richmond kumalizika kikao cha Novemba; kikao kimemalizika bila suala hilo kumalizika. Ufisadi wa EPA nawe umefanyiwa usanii wa hali ya juu wa kisiasa, kwa bahati mbaya ukiongozwa na mkuu wa nchi. Hotuba ya Rais Kikwete aliyoitoa bungeni ya kutamka msamaha kwa waliorejesha fedha za wizi; ni sehemu ya hali hiyo. Mhimili wa Bunge, umeshindwa kumwajibisha Rais katika hili kwani hata hotuba hiyo ya Rais pamoja na ahadi za Spika kuwa ingejadiliwa bungeni mpaka leo haijawahi kutolewa. Nachukua fursa hii kutoa mwito kwa ikulu kuiweka wazi Hotuba hiyo ya Rais Kikwete ijadiliwe na umma; kwani muda mrefu sana umepita toka tuelezwe kwamba hotuba hiyo imerudishwa ikulu ‘kukarabatiwa’. Kushindwa huku kuwa na kumbukumbu za Bunge zilizohadharani (Hansard) za suala nyeti kama hili la Hotuba ya Rais Bungeni kuhusu hali ya taifa (state of the nation address) na aibu kwa Spika aliyetangaza kuendesha bunge kwa viwango na kasi.

CCM hii hii leo inabuka kuwaghilibu watanzania kuwa imeanza kutafuta vyanzo visafi vya fedha za kampeni zake. Wakati wetu ni huu; tusidanganyike. Wachukue hatua kwanza kuhusu kampuni ya Kagoda na mengineyo ambayo fedha zake zilitumika kwa wagombea wa chama hicho kwenye kampeni za mwaka 2005. Watanzania wakumbuke kwamba utapeli kama huu wa kisiasa ulifanyika katika uchaguzi uliopita ambapo viongozi hawa hawa wa CCM walizunguka kupokea michango ya wafanyabiashara; kumbe wafanyabiashara hao ndio wale wale wa EPA. CCM iwaeleze watanzania ina mkakati gani wa kuchota fedha chafu katika uchaguzi wa 2010 ambao utakwenda sambamba na mfumo wa kuzisafisha kupitia kinachoitwa michango toka kwa wapenzi na wanachama wake?

Uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa uliofanyika mwaka huu ulikuwa ni aibu kwa taifa na ishara ya wazi ya CCM kuhubiri demokrasia huku ikipanga kila mbinu za kupora ridhaa ya umma miaka 48 baada ya uhuru. Kutokana na serikali yenyewe ya CCM kujisimamia yenyewe uchaguzi; Waziri Mkuu Mizengo Pinda alikiuka kanuni alizozitunga mwenyewe kwa kutoa tangazo kwenye vyombo vya habari Julai 25, 2009 kuwa uandikishaji wa wapiga kura ungefanyika kwa siku 21 kama kanuni zilivyohitaji katika mwezi Septemba. Lakini cha kushangaza, akatoa tangazo lingine baadaye chini ya siku tisini ambazo kanuni zimeelekeza la kutaka uandikishaji ufanyike mwezi Oktoba; na hivyo kufanya usikamilike chini ya siku 21 kabla ya uchaguzi kama kanuni zilivyohitaji. Akaenda mbele zaidi kutenga kanuni zenye kutoa mwanya kwa watendaji wa kiserikali kusimamia chaguzi hizo na hivyo kutoa mwanya wa uvurugaji wa uchaguzi. Uchaguzi wenye wapiga kura wachache waliolazimishwa kuandika wenyewe majina ya wagombea na vyama vyao. Kwa vyovyote vile, uchaguzi huu hauwezi kuwa kipimo kamili cha mwelekeo wa kisiasa katika uchaguzi wa mwaka 2010 ambao utasimamiwa na chombo tofauti kwa sheria na taratibu tofauti. CCM ikatengeneza mazingira ya kutumia uchaguzi huu kukatisha tama matumaini ya mabadiliko. Waziri Mkuu mwenyewe akawa mstari wa mbele kulipotosha bunge kwa kutangaza matokeo, kabla hata Wizara ya TAMISEMI haijamilisha kupokea matokeo toka maeneo mbalimbali ya nchi. Hivyo, idara ya kumbukumbu za Bunge(hansard) inapaswa itoe hotuba ile hadharani kama ilivyo; taifa liweze kujadili kama kweli matokeo yale ni kamili ama zilikuwa ni propaganda tu za kufanya umma uamini kwamba CCM ilishida kwa kiwango kilichotajwa. Hata hivyo, pamoja na hujuma zote vipo vyama vilivyopanda kisiasa ukilinganisha matokeo ya mwaka 2004 na haya ya 2009; CHADEMA ikiwa kinara katika kundi hilo.

Kama kuna tishio la umoja na amani ya nchi basi ni uchaguzi katika nchi ambayo watawala hawataki kuachia madaraka. CCM inajivuna kwamba inafanya chaguzi za amani huku doa pekee likitajwa kuwa ni chaguzi za Zanzibar. Lakini ukweli ni kuwa hali ya CCM kutumia nguvu za dola, na makada wake kutumia vikundi vya kiharamia kumwaga damu ni utamaduni wao kila wanapozidiwa, kwenye pande zote mbili za Muungano. Viongozi wa CCM ni vinara wa vurugu kwenye chaguzi za marudio kama ilivyothibitika Kiteto, Tarime, Busanda na Biharamulo. CCM ya sasa na viongozi wake ni tishio kwa amani na usalama wa taifa letu hususani katika kipindi cha chaguzi. Kizazi kipya kijikumbushe ujumbe wa Malcom X, ‘ballot or bullet’; tuwabane CCM na mawakala wao kwa nguvu ya umma, tuwaeleze wazi kwamba amani ni tunda la haki. Uzoefu duniani unaonyesha kuwa risasi haziwezi kushindana na umma wenye kutaka kuleta mabadiliko kidemokrasia kupitia sanduku la kura.

Katika kutafuta uhuru wa kweli wa kisiasa tuendelee kudai mabadiliko ya katiba ili tuweze kubadili sheria na mazingira ya kisiasa pamoja na CCM imehodhi mamlaka ya umma na kukataa kuandikwa kwa katiba mpya nchini. Watanzania wasitarajie CCM kwa uwingi wake bungeni ikubali kuandikwa kwa katiba mpya na tume huru ya uchaguzi. CCM wanajua kuwa kuandikwa kwa katiba mpya kutaweka misingi ya uwajibikaji, ikiwemo kushughulikiwa kikamilifu kwa mafisadi. CCM inahofu pia kuwa kuundwa kwa tume huru ya uchaguzi kutakiondoa chama hicho madarakani. Tutumie mbinu mbadala kusukuma mabadiliko yanayokusudiwa kwa kuunganisha Nguvu ya Umma. Kama ilivyowezekana wagombea wa upizani kushinda katika baadhi ya wajimbo ndivyo ambavyo inapaswa kuwa katika chaguzi zinazofuata. Katiba mpya itaandikwa baada ya kufanya mabadiliko ya kuondoa hodhi ya chama kimoja bungeni na kuchagua uongozi mbadala.

Ili kupata uhuru wa kweli kwa kisiasa tunahitaji mabadiliko ya mfumo wa kiutawala. Haiwezekani tukaendelea kuwa na mfumo wa utawala tuliorithi kwa mkoloni wa kuwapa madaraka makubwa viongozi wa kuteuliwa kama wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa; hodhi ya utawala ikiwa kwa serikali kuu badala ya kuongozwa kwa nguvu ya umma kupitia viongozi waliochaguliwa na umma kidemokrasia. Kwa pamoja tunapaswa kufanya maamuzi ya kulitoa taifa letu katika kufilisika kimaadili na kiitikadi na kukubaliana tunu za kitaifa zenye kuwezesha misingi ya uwajibikaji. Uhuru wa kweli wa kisiasa utakuja kwa kubadili uongozi na kuweka madarakani uongozi wenye dira, maadili na msimamo wa kufanya ukombozi wa taifa kisiasa na hatimaye kuleta tija kiuchumi na manufaa ya kijamii. Hivyo, tuuchukulie uchaguzi wa viongozi kama harakati za kutafuta uhuru wa kweli; tukiacha uchaguzi wetu kutawaliwa na nguvu za ziada nje ya ridhaa ya umma iwe ni kwa fedha haramu au shinikizo la ndani na nje tunaitumbukiza nchi yetu katika ukoloni mamboleo. Uhuru wa kweli ni pamoja na uhuru wa kuchagua na kuchaguliwa katika chaguzi huru na haki na uhuru wa kushiriki katika maamuzi ya kisiasa kwa ujumla. Tukiacha viongozi wa kisiasa wakatutawala kwa mwelekeo wao, bila maridhiano ya pamoja; tutakuwa tumepata uhuru tu wakuondoa wakoloni toka nchi za kigeni na kuingiza ‘wakoloni’ wa ndani. Ni muhimu siasa zetu zitatuwezesha kunufaika na rasilimali zetu: iwe ni vipaji vyetu, kodi zetu au maliasili za nchi yetu. Tunahitaji mjadala wa kitaifa kufikia azma hiyo.

Saturday, December 19, 2009

Taarifa kwa Umma: Serikali itoe tamko hatua iliyofikiwa

TAMKO KWA VYOMBO VYA HABARI

TAARIFA YA KURUGENZI YA MAMBO YA NJE YA CHADEMA KWA SERIKALI NA WATANZANIA KUHUSU RIPOTI YA KUNDI LA WATAALAMU WA UMOJA WA MATAIFA YATOLEWA

• CHADEMA tunahimiza watanzania kuipitia ripoti ya UN ambayo imetafsiriwa na kuchambuliwa katika lugha ya kiswahili.
• “Tuchafuke tusafishe tujisafishe: kujadili ni uzalendo wa kutetea maslahi ya taifa”-Mkurugenzi wa Mambo ya Nje (CHADEMA), John Mnyika
• Waziri Mwinyi atoe tamko la kujibu Tuhuma toka ripoti ya Kundi la Wataalamu wa UN zizazohusu Ulinzi na Jeshi


Taarifa inatolewa kwa umma kupitia vyombo vya habari kuhamasisha umma kupitia taarifa ya awali iliyotafsiriwa katika lugha ya Kiswahili kuhusu Ripoti ya UN inayopatikana kupitia www.chadema.or.tz ili kuendeleza mjadala wa umma kuhusu ripoti husika.

Aidha kupitia Kurugenzi ya Mambo ya Nje inatoa mwito kwa Serikali kuweza kutoa tamko kuhusu hatua zilizofikiwa za maandalizi ya taarifa ya Serikali kuhusu ripoti ya UN. Hii ni kwa sababu siku chache zimebakia kwa serikali kuwasilisha ripoti yake kwa Umoja wa Mataifa huku mpaka sasa serikali haijawasiliana na wananchi ama walau wawakilishi wa wananchi kupata maoni yao ili kujenga msimamo wa pamoja kama taifa kuhusu yaliyoibuliwa na ripoti husika.

Tunatoa mwito pia kwa Umoja wa Mataifa (UN) nao ukayatafakari masuala yaliyomo kwenye taarifa yetu ya awali wakati inapojiandaa kuipitia Taarifa ya Serikali ya Tanzania kuhusu Ripoti husika ambayo serikali kupitia kwa Balozi wake wa Kudumu kwenye Umoja wa Mataifa (Dr Mahiga) imetangaza kwamba itawasilisha mwezi huu wa Disemba mwaka 2009. Watanzania na Umoja wa Mataifa(UN) wazingatie kuwa maoni hayo ya Serikali inayoongozwa na CCM si msimamo wa Watanzania wote kwa kuwa si wananchi, wala vyama vyao, wala wawakilishi wao(kwa maana ya wabunge wa kambi zote) wamehusishwa katika kuandaa ripoti husika. Hivyo, Watanzania na hata Umoja wa Mataifa, unapaswa kuzingatia kuwa mjadala kuhusu ripoti hii unapaswa kuendelea ili Taifa la Tanzania lipate msimamo wa pamoja kuhusiana na ripoti husika; ili wawakilishi wetu kwenye UN wakazungumze matakwa ya watanzania badala la maoni yao binafsi ama ya serikali inayoongozwa na chama kimoja ndani ya mfumo wa vyama vingi. Ni muhimu nikarudia pia kutoa rai niliyoitoa awali kwamba ripoti ya Kikundi cha wataalamu kilichoundwa na UN ipaswa pia kujadiliwa muktadha wa Orodha ya Mafisadi (list of shame) iliyotolewa na CHADEMA.

Aidha ikumbukwe kuwa tunakubaliana na hoja kwamba Serikali ya Tanzania imechafuliwa katika Ripoti hiyo ya UN kwa baadhi ya viongozi wake, ama raia wake kutajwa kwa namna moja au nyingine katika ripoti hiyo; aidha serikali yenyewe kama taasisi imechafuliwa kwa kuonyeshwa kwamba haitekelezi kikamilifu maazimio ya Umoja wa Mataifa (UN) ambayo serikali yetu ni mwanachama. Lakini nchi ya Tanzania kama taifa, na watu wake wote kwa ujumla wake; hawajachafuliwa. Kama Nchi ya Tanzania, na wananchi wake wote wakatoa kauli ya pamoja ya kuwatetea watu wachache ndani na nje ya serikali waliotajwa katika kashfa hii; hapo ndipo tutakapochafuka wote kwa ujumla wake. Lakini kama Nchi yetu, na watu wake; tukakubaliana kuchukua hatua ya kusafisha uchafu unaoichafua sisi na taifa letu; ni wazi tutasafishika na heshima ya taifa letu itaendelea kulindwa na kujilinda kote duniani.

Kwa kutumia lugha ya picha; ni kama vile nchi yetu ni mtaro; sasa mtaro unaweza kuwa na uchafu, ukipiga kelele kwamba hakuna uchafu wakati uchafu unaonekana basi utaonekana una utamaduni wa uchafu ndio maana unaona ni jambo la kawaida kuwa kwenye mazingira ya uchafu; wewe ni mchafu. Lakini ukichukua hatua ya kuingia ndani ya mtaro, na zana zako za kusafishia; utachafuka kidogo, utaweza kusafisha mtaro, utatoka na utajisafisha. Mtaro utabaki safi, na wewe utabaki safi; na wewe na mtaro wako wote mtakuwa safi na kuitwa wasafi.

Kadhilika kwa Tanzania, mjadala huu kuhusu uchafu iliotolewa na ripoti ya UN unapaswa kuendelea ili tuujue vizuri uchafu wenyewe wakati wa mjadala huu tutaonekana kuwa tuna uchafu lakini tutaweza kuingia tukachafuka kidogo tukausafisha na nchi yetu itabaki ikiwa safi na sisi wenyewe tutathibitika mbele ya jamii ya kimataifa kuwa ni wasafi na hatupendi uchafu na unapojitokeza tunachukua hatua za kuuondoa.
Hivyo, tunatoa taarifa hii kwa tahadhari kubwa ya kizalendo kwa kuwa najua suala hili linagusa kwa namna au nyingine vyombo vyeti na masuala tete yanayoelekezwa kwa nchi yetu yanayogusa jeshi, polisi, usalama wa taifa, chama tawala, serikali yake, na viongozi wake. Mambo tunayoyaandika yanagusa genge la mafisadi na watumiaji vibaya wa madaraka; wengine wakiwa ni wafanyabiashara, wengine wakiwa ni viongozi, wengine wakiwa ni wahalifu waliokubuhu na waasi wenye kufanya mauaji.

Katika mukatadha huo, ni muhimu kwa wananchi kuendelea kupuuza kauli za wenye kueneza uchochezi kwamba CHADEMA iache siasa zenye kuichafua Tanzania; eti itangulize ‘uzalendo’. Wananchi wajiulize ni nani anaichafua Tanzania; kati ya waliofanya ufisadi na/ama kutumia madaraka vibaya na kuitumbukiza Tanzania katika kashfa kama hizi za usafirishaji wa silaha na utoroshaji wa madini kutoka maeneo yenye vita vya wenyewe kwa wenyewe au mtu anayetaka mjadala kuhusu suala hili ili utoke msimamo wa pamoja wa wazalendo wote wenye kukerwa na mambo hayo ili kulirudisha taifa kwenye mkondo unaostahili wenye kulinda heshima ya Tanzania kitaifa na kimataifa?

Hawa wangetaka kutanguliza maslahi ya pamoja ya Tanzania wasingekurupuka kutoa kauli ya serikali ya CCM bila kushirikisha umma wa watanzania ama wawakilishi wa wananchi. Viongozi wa serikali hawana haki ya kusema kwa niaba ya watanzania katika masuala tata bila kupata maoni yetu au ya kambi yetu bungeni. Wananchi tuwaambie wazi watu kama hao kwamba; kila wanachokisema ni msimamo wao na serikali ya chama chao au taasisi zao; hakiwakilishi msimamo wa watanzania wote.

Waambie wazi kuwa kama wanataka watanzania tusivuane nguo hadharani; walio kwenye mamlaka ; kabla ya kutoa kauli, walau waombe maoni ya wawakilishi wa wananchi au taasisi zinazowakilisha wananchi; diplomasia iliyokomaa inatambua umuhimu wa maridhiano baina ya viongozi kabla ya kutoka hadharani katika masuala tete ya kitaifa. Tuko tayari kwa majadiliano kama watanzania kuhusu suala hili ili tutoke na msimamo wa pamoja kama taifa. Kuhoji uzalendo wa wanaotaka watanzania waliotajwa kwenye ripoti ya Kikundi cha Wataalamu kilichoundwa na UN ni sawa na kuwatetea mafisadi ama waliotumia vibaya madaraka yao waliotuhumiwa kwenye ripoti husika.

Ikumbukwe kuwa tuhuma za Tanzania kujihusisha na vita vya DRC zilianza toka wakati taifa hili linaasisiwa. Tofauti ya watawala wa sasa ni kwamba uongozi wa Nyerere ulikuwa unasema wazi kuwa unasaidia waasi, na UN inajua. Lakini wakati ule walioitwa waasi ni wazalendo waliokuwa wakipambana dhidi ya watawala wa kidikteta ambao walikuwa ni makuwadi wa ubeberu na ukoloni mamboeleo katika Afrika. Sera ya wakati huo ya mambo ya nje ya Tanzania ilikuwa ni kuleta ukombozi Afrika nzima (hata ikiwa ni kwa kuunga mkono vita vya msituni) na kueneza umajumuhi wa kiafrika (Pan Africanism).

Serikali ya sasa ipo tofauti; kwanza haina msimamo endelevu; pili, sera yake ya mambo ya nje haieleweki; tatu, masuala ya sasa ya usafirishaji wa silaha ama utoroshaji wa madini toka maeneo yenye vita ambao yanasemwa kuwa yanafanywa na serikali ama watanzania yanahusu zaidi miradi binafsi ya watu ambayo wanaindesha kwa ama kuzitumia taasisi za kiserikali au kuruhusu mianya kwa kutowajibika kusimamia utawala wa sheria ikiwemo kuheshimu maazimio ya Umoja wa Mataifa (UN) ambayo nchi yetu imetia saini.

Hivyo wapenda demokrasia na maendeleo ndani na nje ya Tanzania wanapaswa kuunga mkono rai tuliyoitoa Disemba Mosi, 2009: Kwamba wazalendo wote, waliokerwa na Tanzania ‘kuchafuliwa’ na ripoti hiyo ya Kikundi cha Wataalamu wa UN, wanapaswa kuwashinikiza watanzania wote wanaoishi Dar es salaam, Kigoma na kote duniani ambao wametajwa kwenye taarifa hiyo kwa majina yao; wajitokeze kutoa kauli za kusafisha majina yao, tukiridhika na hoja zao, katika utetezi wao; basi na sisi tutajiunga katika kundi la kuwatetea na kuwasafisha. Viongozi na taasisi za serikali zilizotajwa kwa namna moja au nyingine katika taarifa hiyo iwe kwa majina au kwa matukio zijitokeze kuelezea kutajwa kwao; tukiridhika na maelezo yao na vielezo vyao, tutajiunga katika kazi ya kizalendo ya kuwatetea na kuwasafisha. Na hii isiwe kwa taarifa ya UN pekee; iwe pia Orodha ya Mafisadi, katika vipengele vinavyohusiana na Kampuni za Meremeta, Tangold, Deep Green nk.

Kosa kubwa la Wizara ya Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa katika sakata hili ni kufikiri kwamba yenyewe tu ndiyo inayowajibika kulitolea ufafanuzi na taarifa kuhusu tuhuma zilizoibuliwa na Kundi la wataalamu lililoundwa na UN. Narudia tena kumuomba Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuwashinikiza Mawaziri wengine ambao sekta zao zimeguswa kutoa kauli za kujibu ama kufafanua hoja zilizoibuliwa ndani ya ripoti hiyo, ambayo tayari Wizara ya Mambo ya Nje ameshafanya kosa la kisiasa la kuitumbukiza serikali kwenye malumbano mapema kwa kuliibua suala hili na kuituhumu UN kabla hata Tanzania kufafanua ama kujieleza kwenye Kamati ya Vikwazo. Kwa kuanzia ni muhimu kwa Wizara ya Mambo ya Usalama wa Raia na ile ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa zikatoa maelezo na vielelezo kuhusu suala hili. Hivyo, mawaziri wanaopaswa kufutia kutoa kauli ni: Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa; Hussein Mwinyi na Waziri wa Usalama wa Raia; Lawrence Masha.


Ikumbukwe kuwa Wizara ya Ulinzi ilishatoa kauli fupi ya kukanusha tu kwa ujumla bila kujibu hoja kwa hoja. Hatahivyo, pamoja na kuwa natambua kwamba ni muhimu kwa Jeshi letu, kutunza siri za mikakati yetu ya kijeshi. Wizara ya Ulinzi na Jeshi La Kujenga Taifa ina wajibu wa kutoa kauli za ufafanuzi; na awasilishe maelezo na vielelezo ili serikali ipeleke UN yenye kujibu maswali yafuatayo: Je, kwa kuwa aliyekuwa Balozi wa Tanzania Burundi ambaye alikuwa ni mmoja wa majenerali wa jeshi, namba yake ya simu imetajwa kutumika kuwasiliana na waasi; JWTZ haina sera ya kuendelea kuwatumia maafisa wake waandamizi wa jeshi wanaoitwa wastaafu, wanaotumwa kwenye nchi zenye vita kama ilivyo DRC kuweza kufanya kwa barokoa ya ubalozi majukumu yanayoyofanana na uambata wa kijeshi? (Millitary attacheship). Kama hivyo ndivyo, wizara inaweza kutuambia ni mawasiliano gani ya kijeshi yalikuwa yakifanyika baina ya namba ya simu ya balozi wetu na makamanda wa vikundi vya waasi DRC hususani FDLR na maswahiba wao ndani FARDC? Kwa kuwa mabalozi wetu kuwasiliana na vikundi vya waasi katika nchi ambazo serikali yetu inatambua serikali zake za kiraia ni jambo lisilokubalika na halina uhusiano wowote na ‘siri kuu za jeshi’ wala ‘maslahi ya taifa’; kwanini nini serikali isituleze mawasiliano yaliyokuwa yakiendelea kama inavyotuhimiwa kwenye ripoti ya kundi la Wataalamu lililoundwa na UN? ( Ni muhimu kwa Waziri Mwinyi kutoa tamko hivi sasa kwa kuwa aliyekuwa Balozi wa Tanzania Burundi ameshaondoka katika Ubalozi husika na hana tena kinga kamili ya Kibalozi. Je uamuzi wa Rais Kikwete kuteua Balozi Mpya wa Tanzania Burundi hivi karibuni unauhusiano wowote na kutajwa kwa jina la balozi wa Zamani katika ripoti ya UN?).

Kwa kuwa silaha za kivita ni kubwa, sio ndogo kama sindano kiasi kwamba zinaweza kupita bila kuonekana; Wizara ya ulinzi inazielezeaje tuhuma ya silaha kupitishwa Tanzania ambazo zimeelezwa na Kundi la Wataalamu wa UN kwa maelezo na vielelezo? Wizara inaweza kulieleza taifa silaha hizo zimekwenda nchi gani na kwa makubaliano gani ya kijeshi? Mwisho, kwa kuwa Kamati ya Vikwazo ya UN kuhusu DRC iliundwa toka mwaka 2004; pamoja na kuwa ripoti ya Kundi la Wataalamu wa UN imegusia zaidi miaka ya 2007 mpaka 2009; Wizara inazizungumziaje taarifa zilizozagaa katika mitandao mbalimbali zinazohusisha Meremeta, Tangold; Deep Green na makampuni mengine yaliyosajiliwa kwa majina ya vigogo wa serikali ya awamu ya tatu ambayo yanatajwa kuhusika na biashara haramu za silaha na utoroshaji wa madini toka maeneo yenye vita; kampuni ambazo mojawapo serikali imesema kwamba inahusika na JWTZ? Izingatiwe kuwa CHADEMA ilishaweka msingi wa taarifa hizo kwenye orodha ya mafisadi iliyotolewa 15 Septemba 2009.


Masuala haya na mengine mengi zaidi nikayoyachambua kadiri siku zinavyokwenda yanapaswa kujadiliwa na wananchi ama wawakilishi wao; ili tuweze kutoka na msimamo wa pamoja. Pia UN na Kundi la Wataalamu wake kuiuliza serikali itoe maelezo ya kina wakati wa mapitio ya taarifa husika. Ni utaratibu wa kawaida kwamba ufuatiliaji kama huu uliofanywa kwa kuwa ulihusu Tanzania; serikali itapewa fursa kuandika ripoti ya nchi (country report) kufafanua mambo ambayo yametajwa kabla ya kamati ya vikwazo kufanya maamuzi yake ama kuikubali ripoti husika na mapendekezo yake ama kutoa maelekezo mbadala ya kutaka uchunguzi zaidi katika maeneo ambayo Kundi la Wataalamu limeeleza katika ripoti yake kuwa uchunguzi wake bado haujamilika. Inashangaza kwamba serikali inatumia nguvu kubwa, kubeza ripoti hii na kutishia wanahabari wasiendelee kuandika wakati ripoti imeweka bayana kwamba uchunguzi bado haujakamilika; serikali itaweka wapi uso wake kama uchunguzi zaidi ukaibua uchafu zaidi? “Tuchafuke tusafishe tujisafishe: kujadili ni uzalendo wa kutetea maslahi ya taifa”


Imetolewa leo tarehe 20 Disemba, 2009 Mkoani Tanga; Tanzania:




John Mnyika
Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa
0754694553



Tuesday, December 15, 2009

Miaka 48 ya Uhuru: Tusake mabadiliko ya kweli tupate uhuru wa kweli-2

Katika makala yangu iliyotangulia nilieleza kwamba kumbukumbu ya miaka ni wakati wa kutafakari taifa letu lilipotoka, lilipo na tunapotaka liende. Takafakari hii haipaswi kufanyika tarehe 9 Disemba pekee bali ni mchakato unaopaswa kuendelezwa na mtanzania yoyote mwenye kuamini kwamba uhuru wa kweli, si uhuru wa bendera bali ni uhuru dhidi ya umasikini, ujinga, maradhi na ufisadi. Uhuru wa kweli, ni uhuru wenye kuleta maendeleo kisiasa, kijamii na kiuchumi. Katika makala hiyo iliyotangulia niliitathmini hali ya kiuchumi miaka 48 baada ya uhuru na kuhimitimisha kwamba; uhuru wa kiuchumi katika taifa letu utapatikana kupitia mabadiliko ya kweli, yenye kuhimili misukosuko ya ukoloni mamboleo; na kujenga taifa lenye kutumia vizuri rasilimali katika kutoa fursa kwa raia wake. Leo tutafakari sekta nyingine.

Nchi hii imewekwa rehani kijamii; ndoto ya waasisi wa taifa hili la kujenga taifa lenye uhuru na umoja inafifia. Viongozi wa CCM wanatembea kifua mbele wakizusha mijadala ya ukabila na udini yenye kuligawa taifa. Umoja kati yao umetoweka na sasa wanaparuana wao kwa wao. Chini ya sera mbovu za CCM matabaka yanazidi kumea katika taifa, pengo kati ya masikini na matajiri linazidi kukua kila kukicha. Umasikini unazidi kuongezeka. Utafiti wa hivi karibuni unaonyesha kwamba kati ya mwaka 2005 Rais Kikwete na CCM walioahidi maisha bora kwa kila mtanzania mpaka sasa; katika kila watanzania kumi; saba wamesema kwamba hali yao ya maisha haijawa bora. Na kati yao; asilimia hamsini hali yao imekuwa mbaya zaidi. Nyufa hizi ni tishio kwa amani ya nchi yetu.

Miaka 48 baada ya uhuru, huduma za kijamii zinazidi kudorora; kwa kiwango cha huduma hizo na hata upatikanaji hususani kwa watanzania masikini. Elimu ni sehemu ya uhuru wa kweli kwa vijana; kwa Tanzania ya leo mfumo mzima wa elimu ujenga matabaka. Ukiwa mkoani Dar es salaam na kutembelea shule mbalimbali kuanzia chekechea mpaka sekondari; baina ya shule binafsi na za umma, utofauti wa mazingira ya kusomea ni wa kiwango cha juu. Pamoja na kuongezeka kwa idadi ya madarasa katika shule za umma, bado kuna tatizo la ubora wa madarasa yenyewe yaliyojengwa kwa ukilinganisha na kiwango cha fedha za michango ya wananchi zilizotumika. Kijana wa mtazanzania wa kawaida anasoma katika shule yenye kiwango duni cha elimu kutokana na uhaba wa walimu na vifaa vya kufundishia. Ishara ya kuporomoka huko kwa elimu, ni wimbi la viongozi wa serikali hiyo hiyo inayosimamia kususa kusomesha watoto wao katika shule za umma. Tunahitaji sera na uongozi mbadala; huu ni wakati wetu, tusidanganyike.

Vijana wa vyuo vikuu ni wajibu wao kuwa mstari mbele kusaka mabadiliko; kwani ni mashuhuda wa namna ambavyo serikali inavyofanya matumizi ya anasa, fedha za umma zikipotea kwa ufisadi. Hatima ya yote mzigo unarudi kwa mwanafunzi na wazazi wake kupitia sera za uchangiaji ambao wengine imewanyima fursa ya kusoma.


Miaka 48 baada ya uhuru vijana wanapoteza maisha yao kwa wingi kwa magonjwa yanayoweza kutibika kama malaria na hata kipindupindu. Pamoja na sera ya uchangiaji kuwa mzigo wa watanzania walio wengi bado vifaa na madawa havipatikani hususani katika hospitali na zahanati za umma. Vijana wa kike wajawazito, ambao kila mara matukio ya vifo vya watoto wao kutokana ubovu wa huduma za afya wanaweza kutoa vizuri zaidi kilio hiki. Chini ya utawala wa sasa huduma za jamii kwa ujumla zimegeuzwa bidhaa badala ya kuwa huduma; ikiwemo huduma kama elimu, afya, maji nk. Ni wakati wetu; tusidanganyike. Tuunganishe nguvu mabadiliko ya kisera na kiuongozi yatayowezesha huduma za kijamii kuwa bora na kuwafikia watanzania walio wengi. CHADEMA ni chama cha mrengo wa kati; tunaamini kwamba hata katika mfumo wa soko ni lazima kwa taifa kuwa na mifumo ya ulinzi wa kijamii (social security) inayogusa makundi mbalimbali katika maeneo mbalimbali ya huduma za kijamii.

Miaka 48 baada ya uhuru, ahadi za serikali ya CCM kwa makundi maalum mathalani wanawake, wazee, vijana na wenye ulemavu zimekuwa ni maneno matupu bila vitendo. Sera zao zinatutazama kama watu tunaohitaji kusaidiwa badala ya kuwa wadau wa msingi wa kimaendeleo. Ni wakati wetu; tusidanganyike. Chini ya uongozi mbadala, badala ya wazee wetu kuonekana kuwa kundi linalopaswa tu kubebwa na kuhudumiwa, sera mbadala zitaboresha kiwango na mifumo ya malipo ya wastaafu na kupanua wigo wa mifuko ya kijamii kujumuisha ajira ambazo haziko kwenye mkondo uliozoeleka.

Uboreshaji wa mifumo ya wastaafu itawezesha wazee wetu kuwa na fursa ya kupata huduma za msingi na kuwa na kipato stahili cha kuwakimu hata baada ya kumaliza utumishi wao kwa taifa. Laana ya wazee wastaafu wanaotangatanga na kulazimika kudai haki zao kwa nchi zenye kuwatezwa zinapaswa kuwa chachu ya kufanya mabadiliko.

Pamoja na CCM chini ya Rais Kikwete kujigamba kuweka mstari wa mbele wanawake, sifa hizo zipo kwenye vyombo vya kitaifa vya uteuzi tu. Ni wakati wetu; tusidanganyike. Tunahitaji uongozi na sera mbadala kubadili mifumo ya kisiasa na mitazamo ya kijamii kuweza kujenga taifa lenye kutoa fursa kwa makundi yote ya kijamii kuweza kushindana na kushinda.

Ni muhimu nikakumbusha kuwa athari kubwa zaidi ya kiuchumi ambayo inataathira pia kwa hali ya kijamii ni utegemezi ambao taifa letu limeingizwa kwa kutegemea misaada kutoka nje huku rasilimali za taifa zikifyozwa kibeberu. Ni ukoloni huu mpya ndio ambao unanifanya nitamke kwamba tunahitaji kudai uhuru wa Tanzania. Tunahitaji uhuru wa kweli. Wakati wetu ni huu, tusidanganyike. Mwanafalsafa Frantz Fanon, aliwahi kusema kwamba kila kizazi lazima, nje ya uvungu uvungu kiutambue utume wake; ama kiutumize au kiusaliti. Kizazi cha wakati huo, kilidai uhuru, na kujenga misingi ya taifa(national building) ingawa misingi hiyo imekuja kuvurugwa na kuturudisha kwenye ukoloni mambo leo(neo colonialism). Ni wajibu wa kizazi chetu; kudai uhuru wa kweli, uhuru dhidi ya umasikini, ujinga, maradhi; hatuwezi kudai uhuru huo bila kumpiga vita adui ufisadi. Wajibu wa kizazi chetu ni kuweza kupambana katika mazingira ya ushindani wa ndani na nje ya nchi yetu; kujenga taifa tukitazama kizazi chetu na kijacho.

Pigo kubwa kwa mwelekeo wa taifa letu, na utumwa wa kiutamaduni unaoendelea kumea. Vijana wanaweza kubebeshwa mzigo wa lawama wa kuiga tamaduni za kigeni kwa kiwango chenye kupoteza utaifa wetu; ukweli ni kuwa chanzo cha yote haya ni uongozi usio na maono. Unapokuwa na uongozi wenye sera ambazo hata vyombo vya habari vya umma vinakuwa ni vioo vya tamaduni za nchi zingine; usitegemee vijana kubeba urithi wa nchi yao. Viongozi wetu wanapaswa kujifunza, nchi zilizofanya mapinduzi ya kiuchumi; muhimili thabiti wa mwelekeo wao ni tamaduni zao. Kinyume chake, nchi zenye viongozi wabinafsi; viongozi wasiojiamini, viongozi wasiowajibika, ni matokeo ya utamaduni wa ufisadi. Ni wakati wetu, tusidanganyike. Tunapoazimisha miaka 48 ya uhuru, tuhamasishe mabadiliko ya kweli; kwa kuweka mkazo katika kujikwamua kifikra; kuanzia katika desturi zetu; fasihi zetu; muziki wetu; michezo yetu; familia zetu: vyote vituelekeze katika kujenga taifa lenye kukumbuka tulipotoka na kutengeneza mweleko mwafaka wa vizazi vijavyo. Maneno ya Wimbo wa Bob Marley (Redemption Song) ya mwito wa kujikwamua kutoka utumwa wa kiakili yanafumbo linaloposwa kufumbuliwa katika kutafuta mabadiliko kupata uhuru wa kweli.

Mwandishi wa makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje(CHADEMA) anayepatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.or.tz na http://mnyika.blogspot.com/

Tuesday, December 8, 2009

Miaka 48 ya Uhuru: Huu ni wakati wetu; tusidanganyike!

Wakati wetu ni huu, tunapoadhimisha miaka 48 ya uhuru. Ni wakati wa kutafakari taifa letu lilipotoka, lilipo na tunapotaka liende. Makala hii inakulenga zaidi wewe uliyezaliwa baada ya uhuru; tunaounda sehemu kubwa ya taifa hili. Ni kwa ajili pia ya watanzania wote wenye kuamini kwamba uhuru wa kweli, si uhuru wa bendera bali ni uhuru dhidi ya umasikini, ujinga, maradhi na ufisadi. Uhuru wa kweli, ni uhuru wenye kuleta maendeleo kisiasa, kijamii na kiuchumi. Uhuru huu utapatikana kupitia mabadiliko ya kweli, yenye kuhimili misukosuko ya ukoloni mamboleo; na kujenga taifa lenye kutumia vizuri rasilimali katika kutoa fursa kwa raia wake.

Wakati wa uhuru taifa hili lilikuwa na watu chini ya milioni 10; sasa Dar es salaam pekee ina wananchi takribani milioni nne, karibu nusu ya Tanzania ya wakati huo ikiwa Tanganyika. Sasa taifa lina watu takribani milioni 40; hivyo taifa letu watu wake takribani robo tatu ni kizazi cha baada ya uhuru. Maanake katika kila watu kumi tunaopishana nao barabarani, saba ni kizazi cha baada ya uhuru. Hiki ni kizazi chetu, hili ni taifa letu. Huu ni wakati wetu, tusidanganyike kwamba wakati wetu bado.

Si nia yangu kuanzisha mgogoro kati ya kizazi kipya na kizazi cha zamani cha taifa hili; na wala si kusudio langu kusema kwamba hatuwahitaji wazee katika harakati za demokrasia na maendeleo. Kwani ni afadhali kuwa na kiongozi mzee mwenye maono na maadili kuliko kuwa na kiongozi kijana fisadi asiyekuwa na dira wala mwelekeo. Taifa hili ni la watanzania wote, wa rika zote, wa hali zote, kila mmoja ana umuhimu na nafasi yake kama kilivyo kila kiungo katika mwili wa binadamu. Dhamira yangu, ni kusema kwamba wakati huu ni wetu; tusidanganyike. Yoyote yule, ambaye anaukubali ukweli huu, awe ni kijana wa sasa ama kijana wa zamani, huyo tukubaliane nae.

CHADEMA inaukubali ukweli huo; tangu wakati wa kuanzishwa kwake. Vijana wa zamani katika CCM, walipoudumaza uzao wao kwa kuwaita vijana kuwa ni taifa la kesho, na Umoja wa Vijana wa chama hicho chini ya nidhamu ya uoga kukubaliana ukandamizaji huo. Utawala huo uliposhindwa kuhimili kuingia kwa mfumo wa vyama vingi kutokana na shinikizo la ndani na nje, vijana wa zamani wenye fikra mbadala na moyo wa ujana walioanzisha CHADEMA kama Wazee Edwin Mtei na Bob Makani wakaja na kauli mbiu mbadala kuwa: Vijana; Taifa la leo mnamo mwaka 1992. Baadaye kauli mbiu hii ilibadilika kuwa: Vijana; Nguvu ya Mabadiliko.

Kwa sasa serikali ya CCM na hata Baraza la Vijana wa CHADEMA (BAVICHA) wote wanamtafiri kijana kuwa ni binadamu mwenye umri usiozidi miaka 35(wakianzia miaka 12, 15, 16 au 18 kutegemea muktadha); ni takribani asilimia 40 ya watanzania. Watoto na vijana kwa ujumla wetu tunakaribia asilimia 70 kwa watu wote nchini. Sisi vijana peke yetu ni zaidi ya asilimia 60 ya nguvu kazi ya Tanzania. Ndio roho na injini za taifa letu. Huu ni wakati wetu, tusidanganyike.


Pamoja na kuwa harakakati za uhuru zilifanyika kona zote za nchi wakazi wa Dar es salaam, wanabeba historia ya harakati za uhuru wa taifa letu; ni wakati muafaka kutafakari masuala haya, mwaka huu ambapo kumbukumbu ya uhuru inafanyikia kitaifa katika mkoa huu. Harakakati za uhuru wakati huo ziliratibiwa kwa busara za wazee wenye imani kwa vijana kuwa vijana ni nguvu ya mabadiliko.

Ni wazee wa Dar es salaam ndio waliomuita Mwalimu Nyerere toka Pugu, kwa mchango wao wa hali na mali, kijana wao, akawa mwenyekiti wa taifa wa chama cha wakati huo cha TANU akiwa na miaka 32, akaongoza harakati za uhuru, mpaka nchi ikapata uhuru. Akiongoza nchi hii vizuri katika miaka ya kwanza ya uhuru, akiweka misingi ya muda mrefu ya taifa yenye kutazama mbele kwa miaka mingi kiuchumi, kisiasa na kijamii; misingi ambayo wazee wa leo wa CCM na vijana wao wameitupilia mbali baada ya kufa kwake.

Kosa moja la Nyerere lilikuwa ni kuweka mkazo sana kwa dola kwa maana ya serikali kumiliki njia za uzalishaji; badala ya uchumi kimilikiwa na umma. Kosa hili lilifanya serikali ishindwe kubeba mzigo mkubwa wa kusimamia sera kisiasa wakati huo huo kufanya utekelezaji kwa kuendesha njia za uzalishaji mali za kiuchumi wakati huo huo ikiwa inatoa huduma za kijamii. Kwa ujumla pamoja na kuimba haja ya kujitegemea, dola ikazalisha raia wategemezi kifikra, ambao chini ya mfumo wa chama kimoja na mwelekeo finyu wa kiuchumi; walipoteza ujasiri wote wa ushindani. Ni kosa hili, ndio lilifanya wakina Mtei kuanzisha CHADEMA yenye inayoamini katika mfumo wa soko la kijamii; lenye kuhakikisha kwamba uchumi unamilikiwa na wananchi. Huu ni mfumo wa kiuongozi wa kisera na kirasilimali ambao unahakikisha kuwa rasilimali za nchi zinatumika kwa manufaa ya maisha ya wananchi wake; kwa kujenga taifa lenye kutoa fursa. Mjadala huu wa dhima ya itikadi katika nadharia ya maendeleo nimewahi kuuandikia makala za kadhaa cha kiuchambuzi zinazopatikana kwenye tovuti: www.chadema.or.tz.

Lakini afadhali kosa la Nyerere linaweza kusameheka, lakini makosa ya warithi wake, baada ya kung’atuka kwake na baadaye kufa kwake yameacha majeraha makubwa yanayohitaji taifa hili likombolewe upya. Wakati wetu ndio huu; tusidanganyike.

CCM hiyo yenye kuongozwa kwa fikra za kifisadi na utupu wa kiitikadi, ikaondoa nchi katika ujamaa, ikaipeleka katika soko holela; sio soko huria. Chini ya sera zake na uongozi wake, njia za uzalishaji mali zikauzwa kwa bei chee; toka kwa dola kwenda kwa wageni, na kwa tabaka la wachache linalojifunika kwa kivuli cha mabepari uchwara wa ndani; wengi wao wakiwa kwenye korido za utawala wa CCM na serikali yake. Marehemu Profesa Chachage, aliwaita watu hawa, makuwadi wa soko huria- hawa kwa kweli, ni makuwadi wa kiuchumi (Economic Hitmens).

Wakahitimisha kwa maamuzi ya Zanzibar, ya kufuta misingi muhimu ya maadili ya uongozi mnamo mwaka 1991; kwa hiyo wakati CHADEMA inaanzishwa, waasisi wake walizitafakari hali hizi.

Halafu bado miaka 48 baada ya Uhuru; CCM wanaendelea kuwadanganya watanzania, na hata kushinikiza katiba ya nchi hii kuwa nchi hii inafuata siasa ya ujamaa na kujitegemea. Chama kinachotawala kinapoongoza huku kina ombwe na kiitikadi, kimefilisika kimaadili; lazima taifa litakuwa na uongozi dhaifu.

Na kwa kweli si maneno yangu kwamba CCM inawadanganya watanzania, ni maneno ya Mwasisi wa chama hicho, na mwandishi wa Azimio la Arusha ambaye kabla ya kufa kwake aliandika moja ya kitabu chenye sehemu ya wosia wake wa mwisho kwa taifa; Kitabu cha uongozi wetu na hatma ya Tanzania; Nyerere ameandika wazi, CCM inawadanganya wa Tanzania, namnukuu: “Halmashauri Kuu ya Taifa iliketi Unguja ikabadili Azimio la Arusha bila kwanza kutafuta maoni ya wananchi. Na walikuwa na haki ya kufanya hivyo, maana sera ni yao, ubaya wao ni kwamba jambo lenyewe walilifanya kwa hila na janja janja, na hadi sasa wanaendelea kuwadanganya wananchi kwamba sera ya CCM bado ni Ujamaa na Kujitegemea”

Kwa hiyo nchi hii iko rehani; kiuchumi, kijamii na hata kisiasa kama ambavyo nitaelezea katika mfululizo wa makala hizi za kumbukumbu ya miaka 48 ya Uhuru wa nchi yetu. Kiuchumi, tukashuhudia viwanda vikiuzwa kwa bei ya kutupa na vingine kugeuzwa magofu baada ya kuuzwa kwake. Hapa Dar es salaam, ambapo maadhimisho yanafanyika mwaka huu, ukienda Jimbo la Kawe, utaona yale mahame ya Tanganyika Packers, kile kilikuwa ni kiwanda cha kusindika nyama, kilichokuwa kikitoa ajira kwa vijana kwa watanzania. Kile kilikuwa kinawezesha bidhaa za wafugaji kusindikwa. Sasa, mpaka vijana wa kimasai nao wanakimbilia kwa wingi Dar es salaam kuwa wasusi na walinzi. Kiwanda hiki ni mfano wa viwanda vingi vilivyoingia hali hii inayochangia katika ukoloni wa kiuchumi; wa kutegemea kuwa bidhaa za nje na kutegemea kusafirisha bidhaa ghafi kwenda nje ya nchi. Pale Jimbo la Ubungo, Kiwanda cha Nguo cha Urafiki kinazidi kudidimia; nyumba za wafanyakazi ziliuzwa kinyemela kwa kivuli cha ubinafsishaji, mpaka mitambo mingine imeuzwa kama chuma chakavu; pamoja na wafanyakazi kulipwa mishahara duni hata maghorofa ya wafanyakazi yanaendeshwa kibiashara badala ya kuwa huduma ya msingi kwa wafanyakazi. Hii ni mifano tu, hali hii ni maeneo mengi ya taifa letu.

Miundombinu nayo imeachwa hohehahe, hali ya usafiri wa reli inazidi kuwa mbaya usafirishaji wa abiria na mizigo kwa njia hii unazidi kupungua mwaka hadi mwaka; mathalani kutoka tani 1,169,000 mwaka 2005 mpaka tani 429,000 mwaka 2008. Serikali inazidi kuingiza fedha za walipa kodi katika uwekezaji wa kibadhirifu na kudhoofisha miundombinu iliyojengwa kwa jasho la umma. Hali ya viwanja vyetu vya ndege na shirika la umma la ndege (ATCL) ni ya kuliaibisha. Utawala wa CCM unaolinda, kila wakati unatuingiza katika kugharamia shirika hili kwa maamuzi mabovu katika vipindi tofauti tofauti. Serikali inayoongozwa na CCM imeshindwa kufanya upanuzi wa Bandari kubwa; badala yake wameingia mikataba mibovu ya upakuzi wa mizigo inayopelekea kupunguza hata kiasi cha shehena kinachohudumiwa katika bandari zetu. Wakati washindani wetu nchi za jirani, ambao wametoa fursa kwa vijana wenye kufiria na kuona mbali na kuunga mkono vyama vyenye sera mbadala; wanapanua bandari zao na kuwekeza katika miundombinu, sisi ambao tuko katika nafasi bora zaidi ya bandari zetu kupata soko kubwa la nchi za maziwa makuu tunabaki tumetahayari kutokana na sera legelege na uongozi mbovu chini ya CCM. Wakati wetu ni huu, tusidanganyike. Wakati wa kudai uhuru, ni vijana makuli wa pale bandarini ndio waliokuwa mstari wa mbele kwenye kudai uhuru; hawakuigopa serikali dhalimu ya kikoloni kwa kuwa hawakuwa na cha kupoteza kama wenye kazi za kola nyeupe(white collar) waliokuwa kwenye serikali ya mkoloni. Ndio maana huwa nafarijika kila ninapoona vijana wasio na ajira na watanzania wa kawaida kwa ujumla wakitaka mabadiliko ya kweli ili kupata uhuru wa kweli. Tabaka hili, halina cha kupoteza isipokuwa umasikini wao na malipo watakayopata ni kuishi kwenye taifa lenye kutoa fursa.

Serikali ya CCM inapita ikijivuna kuboresha miundombinu kwa kutumia takwimu za kuongezeka kwa idadi ya wanaotumia simu za mkononi; lakini hebu tuiangalie kwa undani hii sekta. Ukuaji wake umekuwa kwa nguvu ya sekta yenyewe kwa sababu za nje ya sera za serikali, hii imefanya mchango wake katika ukuaji wa uchumi wa taifa na hata kubadili kipato cha watanzania mmoja mmoja mwenye simu kuwa ni finyu. Tathmini ya serikali ya CCM yenyewe ya hivi karibuni katika maeneo mbalimbali ya nchi inaonyesha kwamba katika kila watanzania kumi (10) wenye simu, ni watanzania wawili(2) ndio wanatumia simu zao kwa matumizi binafsi na biashara; hivyo asilimia kubwa ya watanzania watumia simu kwa matumizi binafsi pekee na si biashara ama shughuli za uzalishaji. Kwa hiyo, tuitumie teknolojia hii hii kuleta ukombozi, ndio maana namuomba kila mwenye simu hapa ya mtandao wa Zain au Vodacom atume neno CHADEMA kwenda namba 15710 kama mchango wake katika kupambana na ufisadi na kutetea rasilimali za taifa. Kwa wenye mitandao mingine huduma hii itafuata katika siku za usoni; huu ndio ubunifu wa kisiasa ndani ya chama kinachoongozwa na kizazi kipya.

Tumehadithiwa na wazee wetu, kwamba wakoloni walitutawala ili kupata nguvu kazi ya bei chee; kupata malighafi kwa ajili ya viwanda vyao na kupata masoko kwa ajili ya bidhaa zao. Tulipotafuta uhuru, ilikuwa ni dhamira yetu kuondoa udhalili huu. Miaka 48 baada ya uhuru, tujiulize; je hali hii imebadilika? Ukweli uko tofauti na kuondoa tabasamu lote la kusherehekea uhuru wetu. Mfumo mpya wa kikoloni ndani ya taifa lenye uhuru wa bendera; ndio unaofanya wafanyakazi kutoa nguvu kazi yao kwa bei chee kwa kulipwa mishahara midogo na kupata maslahi duni. Sasa utumwa huo unabisha hodi kwa wakulima, kupitia mikakati ya kilimo mipya inayoendelezwa hivi sasa yenye kupokonya ardhi kwa watanzania wa kawaida kwa kisingizio cha kupanua mashamba kumbe mwishowe watanzania watakuja kuwa manamba. Mgogoro wa ardhi huko Zimbabwe unapaswa kutufundisha somu kuwa kumiliki ardhi ndio ishara kuu zaidi ya uhuru wa mwananchi. Miaka 48 baada ya uhuru viwanda vyetu vinaendelea kufa huku tukilazimishwa kisera kujibidiisha kuwa watafutaji wa malighafi na kuzisafirisha kwenda viwanda vya nje zikiwa ghafi na hivyo kushindwa kuwa na uwiano wa kimalipo(Balance of Payment). Wakati tukiua viwanda vya ndani na kupunguza uzalishaji; tunafungua mipaka yetu kwa kiwango cha ajabu na kuingiza bidhaa za nje zikiwemo zisizokuwa na kiwango. Taratibu tunajenga uchumi wa kuwa wachuuzi wa bidhaa kutoka nje. Uhuru wetu uko wapi?

Lakini athari kubwa zaidi ya kiuchumi ni utegemezi ambao taifa letu limeingizwa kwa kutegemea misaada kutoka nje huku rasilimali za taifa zikifyozwa kibeberu. Ni ukoloni huu mpya ndio ambao unanifanya nitamke kwamba tunahitaji kudai uhuru wa Tanzania. Tunahitaji uhuru wa kweli. Wakati wetu ni huu, tusidanganyike. Mwanafalsafa Frantz Fanon, aliwahi kusema kwamba kila kizazi lazima, nje ya uvungu uvungu kiutambue utume wake; ama kiutumize au kiusaliti. Kizazi cha wakati huo, kilidai uhuru, na kujenga misingi ya taifa(national building) ingawa misingi hiyo imekuja kuvurugwa na kuturudisha kwenye ukoloni mambo leo(neo colonialism). Ni wajibu wa kizazi chetu; kudai uhuru wa kweli, uhuru dhidi ya umasikini, ujinga, maradhi; hatuwezi kudai uhuru huo bila kumpiga vita adui ufisadi. Wajibu wa kizazi chetu ni kuweza kupambana katika mazingira ya ushindani wa ndani na nje ya nchi yetu; kujenga taifa tukitazama kizazi chetu na kijacho.

Kwa hiyo, mkazi wa kule Loliondo na majirani zake wanaoswagwa wao na mifugo yao, huku Waziri wa Serikali yake ya CCM akiwalinda raia wa nje, na hata kutochukua hatua pale ambapo hata mawasiliano ya simu katika eneo hilo yanasomeka kama vile eneo hilo na ni miliki ya nchi nyingine; anahitaji uhuru wa kweli. Huyo ni mfano tu, watanzania waliowengi; wanatoka maeneo mbalimbali ya nchi yenye rasilimali ambayo yameporwa; iwe ni maeneo ya migodi, maeneo ya uwindaji, maeneo ya uwekezaji katika kilimo cha mashamba makubwa. Sasa hii laana ya rasilimali (resource curse) kwangu mimi ni moja ya visababishi vya kuvunjika kwa amani nchini. Tunaelekea kwenda kuchimba mafuta na uranium; nchi hii iko mashakani kama hatutabidili sera. Wakati huu ni wetu, tusidanganyike. Mwenyezi Mungu ametujalia rasilimali, lakini tukiendelea kuacha uongozi mbovu madarakani; rasilimali hizi ni tishio kwa usalama wetu wenyewe. Hivyo, tusake mabadiliko ya kweli; tupate uhuru wa kweli.

Mwandishi wa makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje(CHADEMA) anayepatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.or.tz na http://mnyika.blogspot.com

Monday, December 7, 2009

Ripoti ya Kundi la UN: Tuchafuke tusafishe tujisafishe-kujadili ni uzalendo wa kutetea maslahi ya taifa

TAMKO KWA VYOMBO VYA HABARI

TAARIFA AWALI YA KURUGENZI YA MAMBO YA NJE YA CHADEMA KWA SERIKALI NA WATANZANIA KUHUSU RIPOTI YA KUNDI LA WATAALAMU WA UMOJA WA MATAIFA YATOLEWA

CHADEMA yatimiza ahadi ya kuitafsiri ripoti na kuichambua katika lugha ya Kiswahili.
“Tuchafuke tusafishe tujisafishe: kujadili ni uzalendo wa kutetea maslahi ya taifa”-Mkurugenzi wa Mambo ya Nje (CHADEMA), John Mnyika
Tunamtaka Waziri Masha ajibu tuhuma toka ripoti ya Kundi la Wataalamu wa UN zizazohusu Usalama wa Raia kama sehemu ya utetezi ambao Tanzania itawasilisha UN kuanzia leo

Leo tarehe 7 Disemba 2009 tunatoa rasmi kwa umma kupitia mtandao wa www.chadema.or.tz taarifa ya awali ya kurugenzi ya Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa ya CHADEMA kwa serikali na watanzania kuhusu ripoti ya kundi la wataalamu wa Umoja wa Mataifa (UN). Tunatoa taarifa hii ikiwa ni sehemu ya kutekeleza ahadi yetu tuliyoitoa Disemba Mosi, 2009 wakati wa Mkutano na Waandishi wa Habari ya kuitafsiri taarifa ya UN kwa lugha ya Kiswahili na kuitoa hatua kwa hatua sambamba na maoni yetu ili watanzania waweze kuijadili kikamilifu na hatimaye tuweze kutoka na msimamo mmoja kama taifa kuhusu ripiti hiyo.

Napenda kuwasilisha kwa umma tafsiri ya kwanza na uchambuzi wa awali wa maudhui ya ripoti hiyo ya Kundi la Wataalamu wa UN kwa ajili ya kusambazwa, kusomwa na kutafakariwa na serikali na watanzania kwa ujumla. Aidha ni muhimu Umoja wa Mataifa (UN) nao ukayatafakari masuala haya wakati inayapitia Moani ya Serikali ya Tanzania kuhusu Ripoti husika ambayo serikali kupitia kwa Balozi wake wa Kudumu kwenye Umoja wa Mataifa (Dr Mahiga) imetangaza kuwa itayawasilisha leo tarehe 7 Disemba 2009. Watanzania na Umoja wa Mataifa(UN) wazingatie kuwa maoni hayo ya Serikali inayoongozwa na CCM si msimamo wa Watanzania wote kwa kuwa si wananchi, wala vyama vyao, wala wawakilishi wao(kwa maana ya wabunge wa kambi zote) wamehusishwa katika kuandaa ripoti husika. Hivyo, Watanzania na hata Umoja wa Mataifa, unapaswa kuzingatia kuwa mjadala kuhusu ripoti hii unapaswa kuendelea ili Taifa la Tanzania lipate msimamo wa pamoja kuhusiana na ripoti husika; ili wawakilishi wetu kwenye UN wakazungumze matakwa ya watanzania badala la maoni yao binafsi ama ya serikali inayoongozwa na chama kimoja ndani ya mfumo wa vyama vingi. Ni muhimu nikarudia pia kutoa rai niliyoitoa awali kwamba ripoti ya Kikundi cha wataalamu kilichoundwa na UN ipaswa pia kujadiliwa muktadha wa Orodha ya Mafisadi (list of shame) iliyotolewa na CHADEMA.

Nakubaliana na hoja kwamba Serikali ya Tanzania imechafuliwa katika Ripoti hiyo ya UN kwa baadhi ya viongozi wake, ama raia wake kutajwa kwa namna moja au nyingine katika ripoti hiyo; aidha serikali yenyewe kama taasisi imechafuliwa kwa kuonyeshwa kwamba haitekelezi kikamilifu maazimio ya Umoja wa Mataifa (UN) ambayo serikali yetu ni mwanachama. Lakini nchi ya Tanzania kama taifa, na watu wake wote kwa ujumla wake; hawajachafuliwa. Kama Nchi ya Tanzania, na wananchi wake wote wakatoa kauli ya pamoja ya kuwatetea watu wachache ndani na nje ya serikali waliotajwa katika kashfa hii; hapo ndipo tutakapochafuka wote kwa ujumla wake. Lakini kama Nchi yetu, na watu wake; tukakubaliana kuchukua hatua ya kusafisha uchafu unaoichafua sisi na taifa letu; ni wazi tutasafishika na heshima ya taifa letu itaendelea kulindwa na kujilinda kote duniani.

Kwa kutumia lugha ya picha; ni kama vile nchi yetu ni mtaro; sasa mtaro unaweza kuwa na uchafu, ukipiga kelele kwamba hakuna uchafu wakati uchafu unaonekana basi utaonekana una utamaduni wa uchafu ndio maana unaona ni jambo la kawaida kuwa kwenye mazingira ya uchafu; wewe ni mchafu. Lakini ukichukua hatua ya kuingia ndani ya mtaro, na zana zako za kusafishia; utachafuka kidogo, utaweza kusafisha mtaro, utatoka na utajisafisha. Mtaro utabaki safi, na wewe utabaki safi; na wewe na mtaro wako wote mtakuwa safi na kuitwa wasafi.

Kadhilika kwa Tanzania, mjadala huu kuhusu uchafu iliotolewa na ripoti ya UN unapaswa kuendelea ili tuujue vizuri uchafu wenyewe wakati wa mjadala huu tutaonekana kuwa tuna uchafu lakini tutaweza kuingia tukachafuka kidogo tukausafisha na nchi yetu itabaki ikiwa safi na sisi wenyewe tutathibitika mbele ya jamii ya kimataifa kuwa ni wasafi na hatupendi uchafu na unapojitokeza tunachukua hatua za kuuondoa.
Hivyo, naandika waraka huu kwa tahadhari kubwa ya kizalendo kwa kuwa najua suala hili linagusa kwa namna au nyingine vyombo vyeti na masuala tete yanayoelekezwa kwa nchi yetu yanayogusa jeshi, polisi, usalama wa taifa, chama tawala, serikali yake, na viongozi wake. Mambo ninayoandika pia yanagusa genge la mafisadi na watumiaji vibaya wa madaraka; wengine wakiwa ni wafanyabiashara, wengine wakiwa ni viongozi, wengine wakiwa ni wahalifu waliokubuhu na waasi wenye kufanya mauaji.

Katika mukatadha huo, ni muhimu kwa wananchi kupuuza kauli za wenye kueneza uchochezi kwamba CHADEMA iache siasa zenye kuichafua Tanzania; eti itangulize ‘uzalendo’. Wananchi wajiulize ni nani anaichafua Tanzania; kati ya waliofanya ufisadi na/ama kutumia madaraka vibaya na kuitumbukiza Tanzania katika kashfa kama hizi za usafirishaji wa silaha na utoroshaji wa madini kutoka maeneo yenye vita vya wenyewe kwa wenyewe au mtu anayetaka mjadala kuhusu suala hili ili utoke msimamo wa pamoja wa wazalendo wote wenye kukerwa na mambo hayo ili kulirudisha taifa kwenye mkondo unaostahili wenye kulinda heshima ya Tanzania kitaifa na kimataifa?

Hawa wangetaka kutanguliza maslahi ya pamoja ya Tanzania wasingekurupuka kutoa kauli ya serikali ya CCM bila kushirikisha umma wa watanzania ama wawakilishi wa wananchi. Viongozi wa serikali hawana haki ya kusema kwa niaba ya watanzania katika masuala tata bila kupata maoni yetu au ya kambi yetu bungeni. Wananchi tuwaambie wazi watu kama hao kwamba; kila wanachokisema ni msimamo wao na serikali ya chama chao au taasisi zao; hakiwakilishi msimamo wa watanzania wote.

Waambie wazi kuwa kama wanataka watanzania tusivuane nguo hadharani; walio kwenye mamlaka ; kabla ya kutoa kauli, walau waombe maoni ya wawakilishi wa wananchi au taasisi zinazowakilisha wananchi; diplomasia iliyokomaa inatambua umuhimu wa maridhiano baina ya viongozi kabla ya kutoka hadharani katika masuala tete ya kitaifa. Tuko tayari kwa majadiliano kama watanzania kuhusu suala hili ili tutoke na msimamo wa pamoja kama taifa. Kuhoji uzalendo wa wanaotaka watanzania waliotajwa kwenye ripoti ya Kikundi cha Wataalamu kilichoundwa na UN ni sawa na kuwatetea mafisadi ama waliotumia vibaya madaraka yao waliotuhumiwa kwenye ripoti husika.

Ikumbukwe kuwa tuhuma za Tanzania kujihusisha na vita vya DRC zilianza toka wakati taifa hili linaasisiwa. Tofauti ya watawala wa sasa ni kwamba uongozi wa Nyerere ulikuwa unasema wazi kuwa unasaidia waasi, na UN inajua. Lakini wakati ule walioitwa waasi ni wazalendo waliokuwa wakipambana dhidi ya watawala wa kidikteta ambao walikuwa ni makuwadi wa ubeberu na ukoloni mamboeleo katika Afrika. Sera ya wakati huo ya mambo ya nje ya Tanzania ilikuwa ni kuleta ukombozi Afrika nzima (hata ikiwa ni kwa kuunga mkono vita vya msituni) na kueneza umajumuhi wa kiafrika (Pan Africanism).

Serikali ya sasa ipo tofauti; kwanza haina msimamo endelevu; pili, sera yake ya mambo ya nje haieleweki; tatu, masuala ya sasa ya usafirishaji wa silaha ama utoroshaji wa madini toka maeneo yenye vita ambao yanasemwa kuwa yanafanywa na serikali ama watanzania yanahusu zaidi miradi binafsi ya watu ambayo wanaindesha kwa ama kuzitumia taasisi za kiserikali au kuruhusu mianya kwa kutowajibika kusimamia utawala wa sheria ikiwemo kuheshimu maazimio ya Umoja wa Mataifa (UN) ambayo nchi yetu imetia saini.

Hivyo wapenda demokrasia na maendeleo ndani na nje ya Tanzania wanapaswa kuunga mkono rai tuliyoitoa Disemba Mosi, 2009: Kwamba wazalendo wote, waliokerwa na Tanzania ‘kuchafuliwa’ na ripoti hiyo ya Kikundi cha Wataalamu wa UN, wanapaswa kuwashinikiza watanzania wote wanaoishi Dar es salaam, Kigoma na kote duniani ambao wametajwa kwenye taarifa hiyo kwa majina yao; wajitokeze kutoa kauli za kusafisha majina yao, tukiridhika na hoja zao, katika utetezi wao; basi na sisi tutajiunga katika kundi la kuwatetea na kuwasafisha. Viongozi na taasisi za serikali zilizotajwa kwa namna moja au nyingine katika taarifa hiyo iwe kwa majina au kwa matukio zijitokeze kuelezea kutajwa kwao; tukiridhika na maelezo yao na vielezo vyao, tutajiunga katika kazi ya kizalendo ya kuwatetea na kuwasafisha. Na hii isiwe kwa taarifa ya UN pekee; iwe pia Orodha ya Mafisadi, katika vipengele vinavyohusiana na Kampuni za Meremeta, Tangold, Deep Green nk.

Kosa kubwa la Wizara ya Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa katika sakata hili ni kufikiri kwamba yenyewe tu ndiyo inayowajibika kulitolea ufafanuzi na taarifa kuhusu tuhuma zilizoibuliwa na Kundi la wataalamu lililoundwa na UN. Wakati umefika sasa wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuwashinikiza Mawaziri wengine ambao sekta zao zimeguswa kutoa kauli za kujibu ama kufafanua hoja zilizoibuliwa ndani ya ripoti hiyo, ambayo tayari Wizara ya Mambo ya Nje ameshafanya kosa la kisiasa la kuitumbukiza serikali kwenye malumbano mapema kwa kuliibua suala hili na kuituhumu UN kabla hata Tanzania kufafanua ama kujieleza kwenye Kamati ya Vikwazo. Kwa kuanzia ni muhimu kwa Wizara ya Mambo ya Usalama wa Raia na ile ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa zikatoa maelezo na vielelezo kuhusu suala hili. Hivyo, mawaziri wanaopaswa kufutia kutoa kauli ni: Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa; Hussein Mwinyi na Waziri wa Usalama wa Raia; Lawrence Masha.
Ikumbukwe kuwa Tarehe 2 Disemba 2009 Jeshi la Polisi nchini limesema kuwa Tanzania haihusiki kwa namna yoyote ile katika kashfa ya kuwapatia silaha waasi wa serikali za mataifa mengine kama ilivyotangazwa na baadhi ya vyombo vya habari. Mratibu wa Udhibiti wa Silaha hapa nchini Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACP) Dominick Hayuma, amesema kuwa taarifa za Kundi la Wataalamu lililoteuliwa na UN hazina ukweli wowote. Amesema kuwa Tanzania ina uhusiano mkubwa na serikali za nchi jirani na ndiyo maana majeshi ya polisi katika ukanda wa nchi za Maziwa Makuu na Pembe ya Afrika na zile za kusini mwa Afrika (SADC) zinashirikiana katika masuala ya operesheni kwa lengo la kudhibiti kwa pamoja vitendo vya kihalifu. Amesema kuwa kuna baadhi ya mashirika ya ndani na nje ya nchi wanakusanya taarifa za uongo kwa lengo la kujipatia fedha ama kuleta uchochezi baina ya nchi moja na nyingine.
Nichukue fursa hii kuwatahadharisha wataalamu wetu wa polisi kutokuingizwa kutoa kauli za kisiasa katika mambo yanayostahili maelezo na vielelezo. Ni vizuri zikatolewa kauli za kisera kuhusu masuala hayo; ushahidi wa kuingia ama kutoka kwa silaha za kijeshi katika nchi yetu uko wazi hata kwa wananchi waoishi katika mikoa ya mpakani na nchi za eneo la maziwa makuu. Wananchi ni muhimu wawatake polisi ambao tunawalipa kwa kodi zetu, wakae mbali na mijadala ya kisera na ya kisiasa ili kutenganisha kati ya jeshi na propaganda za wanasiasa. Tabia hii ya kutumwa na viongozi wa CCM ndio ambayo inafanya Polisi wetu kushiriki katika kuiba kura na kuhujumu wapinzani wakati wa uchaguzi. Polisi wetu wajue kwamba mishahara midogo wanayolipwa na maslahi duni wanayoyapata ni matokeo ya uongozi mbovu wa serikali hiyo hiyo ya CCM inayofanya waweke pembeni maadili ya taaluma zao; na kuitetea na hata kuipigania nyakati za uchaguzi. Hivyo, polisi ikae mbali na mapambano ya kisiasa baina ya vyama, ikiwemo mapambano ya hoja kwa ajili ya kupata msimamo wa pamoja wa watanzania. Polisi ibaki na jukumu la kusimamia sheria na kuhakikisha kwamba utawala wa sheria unazingatiwa badala ya kukanusha tu bila maelezo na vielelezo ripoti ya Kundi la wataalamu wa UN ambayo imewataja kwa majina watanzania wanatuhumiwa kuvunja sheria lakini polisi haijawakamata mpaka sasa.

Ni muhimu kwa Wizara ya Usalama wa Raia hususani kupitia kwa Waziri Lawrence Masha ikitoa tamko ikiwemo kutoa maelekezo kwa Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) kuwachunguza watu wote na taasisi zote za Tanzania zilizotuhumiwa kwenye ripoti hiyo likiwemo jeshi la polisi lenyewe. Wizara ya Usalama wa Raia ijibu maswali na kufafanunua masuala yafuatayo, ikiwemo kwa kutoa maelezo na vielelezo kwa Umoja wa Mataifa kwamba: Je, taarifa ya kwamba polisi waliizunguka meli inayotuhumiwa katika ripoti hiyo ya Kundi la Wataalamu wa UN anaizungumziaje? Je, polisi hao walikuwa wa nchi gani? Kama ni watanzania walikwenda kufanya nini kwa maelekezo ya nani? Aidha ripoti ya Kundi la Wataalamu, inataja kwamba yapo maduka ya masonara yaliyokuwa yananunua madini yaliyotoroshwa kutoka DRC? Na kwamba kwa maelezo ya mmojawapo wa wamiliki wa maduka yaliyotajwa kwenye taarifa hiyo alidai kwamba kuna wakati ambapo idara ya uhamiaji iliwahi kuendesha msako dhidi ya wafanyabiashara hao? Je, serikali inayazungumziaje madai hayo? Je, serikali yake iko tayari kuwachunguza raia wote wa kigeni wanaotajwa kwenye ripoti hiyo wanaoishi mpaka sasa Dar es salam, Kigoma na kwingineko katika nchi yetu? Je, Wizara yake inamzungumziaje raia wa DRC aliyetajwa katika ripoti ya Kundi la Wataalamu wa UN kwa jina la Bande Ndagundi, ambaye anatuhumiwa kuishi nchini kwa zaidi ya miaka 27 anayejishughulisha na biashara zinazohusiana na masuala ya kijeshi? Je, Waziri Masha au wawakilishi toka Wizara yake wamewahi kuwasiliana na mtu huyo anayedaiwa kuendelea kuishi Dar es salaam? Ni muhimu kwa Wizara hususani Waziri husika kutoa kauli kuhusu mtu huyu kwa kuwa imeelezwa kwa uwazi ikiwemo kwa yeye mwenyewe kusema kwenye barua zake ikiwemo ile ya tarehe 17 July 2009 kuwa ana mawasiliano ya karibu na viongozi wa juu wa serikali, polisi, jeshi na chama tawala.

Masuala haya na mengine mengi zaidi nikayoyachambua kadiri siku zinavyokwenda yanapaswa kujadiliwa na wananchi ama wawakilishi wao; ili tuweze kutoka na msimamo wa pamoja. Pia UN na Kundi la Wataalamu wake kuiuliza serikali itoe maelezo ya kina wakati wa mapitio ya taarifa husika. Ni utaratibu wa kawaida kwamba ufuatiliaji kama huu uliofanywa kwa kuwa ulihusu Tanzania; serikali itapewa fursa kuandika ripoti ya nchi (country report) kufafanua mambo ambayo yametajwa kabla ya kamati ya vikwazo kufanya maamuzi yake ama kuikubali ripoti husika na mapendekezo yake ama kutoa maelekezo mbadala ya kutaka uchunguzi zaidi katika maeneo ambayo Kundi la Wataalamu limeeleza katika ripoti yake kuwa uchunguzi wake bado haujamilika. Inashangaza kwamba serikali inatumia nguvu kubwa, kubeza ripoti hii na kutishia wanahabari wasiendelee kuandika wakati ripoti imeweka bayana kwamba uchunguzi bado haujakamilika; serikali itaweka wapi uso wake kama uchunguzi zaidi ukaibua uchafu zaidi? “Tuchafuke tusafishe tujisafishe: kujadili ni uzalendo wa kutetea maslahi ya taifa”


Imetolewa na:


John Mnyika
Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa
0754694553


Sunday, December 6, 2009

Kauli zangu ziarani Ubungo

Jana Jumamosi tarehe 5 Disemba nimeanza ziara ya siku mbili katika Jimbo la Ubungo; kwa nafasi yangu kama Mwenyekiti wa Mkoa wa Kinondoni Kanda ya Dar es salaam. Nimefanya mikutano miwili ya hadhara. Mkutano wa kwanza nimeufanya katika Kata ya Ubungo kuanzia saa 10:30; jirani kabisa na kituo cha mabasi ya mikoani(Ubungo Bus Terminal).

Nikihutubia mkutano huu, niliwashukuru wananchi wa Dar es salaam waliotuunga mkono kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa na kuwapongeza kwa ushindi uliopatikana. Niliwaeleza kuwa mwaka 2004, CHADEMA ilishinda viti 2 tu katika uchaguzi wa serikali za mitaa. Lakini mwaka huu wa 2009, pamoja na hujuma zote na uchaguzi kuwa ovyo ovyo; tumeweza kushinda viti 11 ambalo ni ongezeko la asilimia nyingi wakati vyama vingine idadi yao ya viti imeshuka.

Nikawaeleza hali hii inatia matumaini tunapoelekea uchaguzi wa mwaka 2010; na nikawaambia kwamba lazima Dar es salaam iwe kitovu cha mabadiliko nchini. Nikitumia nafasi yangu nyingine ya Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa nikawaeleza kwamba katika nchi nyingi za Afrika zilizofanya mageuzi chachu ya mabadiliko hayo huwa ni miji mikubwa kama Dar es salaam lakini inashangaza kwamba kwa upande nchi yetu hali ni tofauti.

Wakazi wa Dar es salaam wanafurahia hoja za wabunge wa upinzani kama wakina Dr Slaa ambao wamepatikana kwa kuchaguliwa majimbo ya vijijini, wakati ambapo majimbo yote saba ya Dar es salaam ni CCM. Hata kwenye udiwani; hakuna diwani hata mmoja mkoa mzima wa Dar es salaam kutoka upinzani. Hii ni aibu kwa taifa na ni matusi kwa wananchi ambao wanapata fursa ya kuwa karibu na vyombo vya habari na kwa sehemu kubwa ni watu waliopata fursa ya kwenda shule.

Hivyo ni muhimu wawezeshe harakati hizi za mabadiliko, na nikawatangazia kwamba siku hiyo tuanaanza kusambaza rasmi vipeperushi vya kuunga mkono CHADEMA kwa njia mbadala katika jimbo la Ubungo.

Nitawatangazia rasmi kwamba sasa wanaweza kujiunga ama kuchangia CHADEMA kwa kutuma neno CHADEMA kwenda namba 15710 kwa wateja wa Zain na Vodacom. Hii inafanya kwamba hata kama wametingwa na majukumu mengine bado wanaweza kabisa kufanya harakati za kisiasa kwa kutumia simu zao. Nikawatangazia pia kuwa kama wanataka kuwasiliana na CHADEMA jimbo la Ubungo watume ujumbe au wapige simu kwenda namba 0784222222.

Nikawaambia kwamba wakumbuke maneno tuliyowaambia mwaka 2005 kwamba mabadiliko ya kweli katika taifa letu; hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile; chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale kwa ari, nguvu na kasi mpya; na kwamba kwa falsafa ya chukua chako mapema(ccm) ya chama cha mafisadi(ccm) Tanzania yenye neema haiwezekani.

Nikawakumbusha kwamba mwaka 2005, wakati nagombea ubunge katika jimbo hilo, nilisimama katika eneo hilo hilo na kutangaza kwamba kuna ufisadi na upotevu wa mapato Mradi wa Kituo cha Mabasi Ubungo(UBT) ambao unafanywa na kampuni ya familia ya Kingunge na vigogo katika Halmashauri ya Kinondoni. Wakati huo, CCM wakiwemo baadhi ya vigogo hao walikanusha. Lakini sasa miaka michache baadaye Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amekwenda na kutaka ukaguzi maalum(Special Audit) ambayo imebaini mambo ambayo niliyashayasema mwaka 2005. Hata hivyo, kama kawaida ya CCM ya kulindana; Pinda mpaka sasa amekalia ripoti hiyo ya CAG. Amesubiri mkataba wa Kampuni ya familia ya Kingunge (Smart Holdings) umalizike badala ya kuvunja mkataba na kuwachukulia hatua za kisheria. Na kutokana na hayo, kampuni hiyo imehamishwa katika ulaji mwingine kwa kupewa katika mazingira tata tenda ya kukusanya mapato katika jesho la wamachinga(Machinga Complex). Hivyo, nikatoa mwito kwa Waziri Mkuu Pinda kuiweka hadharani mapema iwezekanavyo ripoti ya CAG kuhusu mradi wa UBT ili iweze kujadiliwa na umma tukiwemo wananchi wa ubungo ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa kampuni hiyo na wanafamilia hao ambao walikuwa wakidanganya kwamba mapato kwa siku ni milioni moja na ushee; wakati serikali imeanza tu kukusanya mapato imeweza kupata takribani milioni nne kwa siku. Pia, nikatoa mwito kwa wamachinga kupaza sauti kudai jingo lao kwani hata wao wanavikundi na vyama vyao ambavyo vinapaswa kuhusishwa kwenye ukasanyaji wa mapato.

Mkutano wa pili nimeufanya kata ya Kimara eneo la Kimara matangini ambapo pia nilianza kwa kuwashukuru wananchi wa kutuunga mkono katika uchaguzi wa mitaa ya kata hiyo. Niliwaeleza kwamba pamoja na hujuma walizofanyiwa ikiwemo makaratasi ya kupigia kura katika kata hiyo kuisha asubuhi, na mengine kuletwa jioni tena yakiwa yametolewa nakala(photocopy) kwenye maduka ya jirani hapo hapo Kimara kwa idadi isiyojulikana; bado upinzani uliokuwepo umeipa somo CCM na wenyeviti wake waliotangazwa kuwa wameshinda.

Niliwaleza kwamba mwaka 2004; wenyeviti hao walipita bila kupingwa lakini sasa wameshinda kwa ushindani mkali uliohusisha CCM kutoa wapiga kura maeneo mengine na kuwahamishia kupiga kura hapo Kimara kwa kutumia karatasi hizo zilizoongezwa. Nikawaeleza kwamba kutokana na hali hiyo, yapo maeneo ambayo tumefungua kesi kama Msewe, Baruti nk.

Nikawatangazia rasmi wenyeviti wa serikali za mitaa kwa tiketi ya CCM na viongozi wa chama chao kwamba wanapaswa kutekeleza wajibu wao ipasavyo wa kuwatumikia wananchi kwa kuwa tofauti na udiwani na ubunge ambapo kiongozi akichaguliwa amechaguliwa hakuna namna ya kumuondoa mpaka uchaguzi mwingine kwenye serikali za mitaa hali ni tofauti. Nikaweleza wananchi kwamba sheria inawaruhusu kupiga kura ya kutokuwa na imani na kuwaondoa kama watashinda kutekeleza wajibu ipasavyo ikiwemo kuitisha mikutano ya wananchi na kuwasomea taarifa za mapato na matumizi. Pia kama watashindwa kufuatilia kero za msingi za wananchi, mathalani katika Mtaa wa Golani kuna tatizo na daraja na kero kubwa ya maji. Kama viongozi hao watashindwa kushirikiana na wananchi kuondokana na kero hizo; CHADEMA tutashirikiana na wananchi kuchukua hatua zinazostahili kabla hata ya uchaguzi ujao wa serikali za mitaa.

Nikawaeleza kwamba taifa letu kwa sasa linapita katika wakati mgumu kutokana na kukua kwa matabaka katika jamii. Nikawaeleza kwamba pamoja na kukua kwa tabaka kati ya masikini na matajiri tabaka baya zaidi ni lile la kukosekana kwa usawa katika utawala wa sheria na mifumo ya utolewaji wa haki. Mathalani watuhumiwa wa ufisadi tuliowataja kwenye orodha ya mafisadi, bado wengi wao wanatamba barabarani mpaka hivi sasa na kwa sehemu kubwa wakilindwa na vyombo vya usalama vinavyoendeshwa na kodi za watanzania; lakini kwa mwananchi mlipa kodi anayeishi Kimara hali yake ya usalama ni tete kutokana na majambazi kuruhusiwa kutamba mara kwa mara. Hivyo suluhisho ni kufanya mabadiliko ya kiuongozi na kisera ili kuunganisha nguvu ya umma kushughulikia masuala hayo. Nikawaeleza kwamba sera kuu ya CHADEMA ambayo tunaiita falsafa yetu ni Nguvu ya Umma ama people’s power. Chini ya Sera hii tunaamini kwamba rasilimali za watanzania iwe ni maliasili; kodi zetu ama vipaji vyetu vinapaswa kutumika kwa manufaa ya wananchi hivyo tunataka kujenga taifa lenye kutoa fursa.

Nikawaeleza changamoto iliyopo ni upotoshaji unaondelea wa kila kitu; hata ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka kuitwa kuwa unafanyika kwa maslahi ya Taifa. Nikatolea mfano kuwa baada ya ripoti ya UN kutolewa Waziri wa Mambo ya Nje, Benard Membe alijitokeza na kuikana yote kwa ujumla wake kwa maelezo kwamba analinda maslahi ya Taifa. Waziri Membe katika hali hiyo, kama kweli angetaka kulinda kikamilifu maslahi ya taifa angetangaza kufanya uchunguzi juu ya watu waliotajwa ili kutetea taswira ya Tanzania kama nchi. Badala yake, kuikana ripoti nzima ni kufisha watu waliofanya vitendo haramu kwa kutumia kivuli cha maslahi ya taifa. Badala yake ni muhimu kwa serikali kuchukua hatua ikiwemo kuchunguza na kuchukua hatua; badala ya kubeza na kufunika hali ambayo inaweza kuiathiri zaidi nchi katika medani ya kimataifa. Ni kama ukiwa na mtaro wa uchafu, wakati mwingine unawajibika kuingia ukachafuka, ukausafisha na baadaye ukajisafisha. Tanzania itasafishwa kwa serikali kuingia katika mtaro kusafisha uchafu iliofanywa na watanzania wachache kwa maslahi yao binafsi; sio ya taifa ili nchi na watanzania wote kwa ujumla tuweze kusafishwa mbele ya jamii ya kiamataifa.

Leo nitakuwa na mikutano mingine Goba, Mbezi na Sinza ikiwa ni mwisho wa ziara ya awamu ya sasa.