ADVERT

Sunday, March 18, 2012

WIKI YA MADAI YA MAJI

Mwito wa kushiriki wiki ya madai ya maji kupitia mitandao ya kijamii:

Nimerejea toka Afrika Kusini nilipokuwa kikazi na kukuta Wizara ya Maji imezindua maadhimisho ya Wiki ya Maji kuanzia tarehe 16 Machi na kilele kitakuwa Siku ya Kimataifa ya Maji tarehe 22 Machi 2012.

Ujumbe wa mwaka huu ni “Maji na Usalama wa Chakula”, hata hivyo tunahimizwa kuadhimisha ujumbe mpya bila kuelezwa matokeo ya ujumbe wa mwaka mmoja uliopita wa “Maji kwa ajili ya Miji: Kukabiliana na changamoto mbalimbali mijini”.

Kazi ya wabunge na bunge kwa mujibu wa katiba ibara ya 63 ni kuwawakilisha wananchi na kuisimamia serikali na mamlaka zake katika kuwezesha maendeleo kwa kutumia rasilimali za umma na za wadau wengine.

Kwa nafasi hiyo natoa mwito kwa wananchi wa Jimbo la Ubungo na wa Jiji la Dar es salaam kwa ujumla kwamba badala ya kuadhimisha sherehe za maji bila ya maji kila mmoja ashiriki kwa namna mbalimbali katika Wiki ya Madai ya Maji.

Kila mmoja anaweza kushiriki kwenye wiki hii ya madai ya maji kwa njia mbalimbali, njia mojawapo ambayo natoa mwito kwa wananchi wa Jimbo la Ubungo kuitumia ni kushiriki madai ya maji kupitia mitandao ya kijamii kwa kuandika barua pepe kwa bodi ya Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) kuitaka ifanye kazi ipasavyo ya kuharakisha upatikanaji wa maji kwa mujibu wa sheria, kanuni, mipango na mikataba.

Waandikie wajumbe wa bodi ya DAWASA madai ambayo unataka wayafanyie kazi katika eneo lako na nakala ya barua pepe hiyo kuituma kwa mbungeubungo@gmail.com kwa ajili za hatua zaidi za kibunge za uwakilishi na usimamizi.

Bodi ya DAWASA ni kama ifuatavyo: Mwenyekiti Dr. Hawa E. Sinare(e.sinare@rexattorneys.co.tz), Makamu Mwenyekiti-Alhaj Said H. El-Maamry-elmaamry@cats-net.com, wajumbe: Bw. Laston Msongole (lmsongole@mof.go.tz), Bi. Mary Mbowe (mrymboowe@yahoo.co.uk) , Bi. Christine Kilindu(christinekilindu@cti.co.tz), Bw. Daniel Machemba (dmachemba@tccia.com, dmachemba@gmail.com), Alhaj Bakari Kingobi (brmkingobi@yahoo.com), . Mary G. Musira(drtc@cats-net.com), B. Florence S. Yamat (yamatf@dawasa.co.tz), Mh. Amina N. Mkilagi (Mb), Mhandisi. Archard Mutalemwa-Afisa Mtendaji Mkuu (dawasaceo@dawasa.co.tz).

Tuungane pamoja kutaka serikali kuu na serikali za mitaa zitumie wiki hiyo kutoa maelezo kwa umma kuhusu hatua iliyofikiwa katika kutekeleza miradi ya maji na pia kuharakisha uzinduzi wa miradi ilicheleweshwa.

Njia hii ya kuunganisha nguvu ya umma kwa kutumia TEHAMA (SMS, facebook, twitter, email na njia nyingine) tuliitumia tarehe 1 Disemba 2011 wakati wa kuhamasisha umma kushiriki mkutano wa wadau uliotishwa na EWURA kuhusu ombi la TANESCO kupandisha bei ya umeme kwa wastani wa 155% (zaidi ya mara tatu ya bei iliyokuwepo).

Hatimaye umeme ulipandishwa lakini si kwa kiwango hicho cha awali bali kwa wastani wa 40% kwa kuzingatia pia viwango vya utumiaji. (Suala la Umeme nimeanza kuchukua hatua zingine kama Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kutokana na matatizo yanayoendelea kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Dharura wa umeme na nitatoa kauli kuhusu mgawo wa umeme unaoendelea kinyemela).

Izingatiwe kuwa nilipanga kwenye wiki hii ya madai ya maji kuunganisha nguvu ya umma kwa kuwaongoza wananchi kukutana na serikali na mamlaka nyingine zinazohusika hata hivyo itabidi kutumia njia mbadala za kuwasilisha madai.

Hii ni kwa sababu kuanzia kesho tarehe 19 Machi 2012 nitakuwa mfululizo mahakamani kwenye kesi ya uchaguzi wa Jimbo la Ubungo wa mwaka 2010. Hivyo, wakati kesi hiyo ikiendelea nitaendelea kutumia njia nyingine za kibunge kuchukua hatua kuhusu masuala ya maji lakini natoa mwito kwa wananchi nanyi kwa upande wenu kila mmoja kuchukua hatua zinazowezekana katika wiki hii ya madai ya ya maji. Umoja ni Nguvu.

Maadhimisho ya Wiki ya Maji bila ya Maji

Upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es salaam miaka michache baada mwaka 1961 ulikuwa zaidi ya asilimia 68; hivi sasa miaka 50 baada ya uhuru tumerudi nyuma na upatikanaji kuwa wastani asilimia 55 tu tena kwa mgawo.

Uchakavu na wa miundombinu kutokana na mabomba kutokarabatiwa ipasavyo pamoja na uharibifu katika mitandao ya maji wa kujiunganishia kinyemela na kiholela umesababisha ongezeko kubwa la upotevu wa maji mpaka kufikia kati ya asilimia 40 hadi 45.

Hali ni mbaya zaidi kuhusu uondoaji wa maji taka ambapo ni asilimia 18 tu ya makazi ndiyo yaliyounganishwa katika mtandao wa maji taka na hivyo kuleta uchafuzi wa mazingira hususani katika maeneo yasiyopimwa. Hata katika maeneo yaliyopimwa kama Sinza mitandao ya maji taka haijakarabatiwa na kupanuliwa kwa wakati kwa kuzingatia ongezeko la watu suala ambalo lisipochuliwa kwa uzito unaostahili madhara yatatokea katika siku za usoni.

Katika muktadha huo hakuna sababu ya kusherekea wiki ya maji bila maji katika maeneo mbalimbali ya jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es salaam kwa ujumla hivyo Wizara ya Maji na mamlaka nyingine husika zitumie wiki hii kutoa majibu ya msingi kwa wananchi kuhusu namna ambavyo wataongeza kasi ya kushughulikia kero ya maji.

Itakumbukwa kwamba akihutubia Bunge mwezi Juni mwaka 2010 wakati wa kuwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara ya Maji ya mwaka wa fedha 2010/11 Waziri Mark Mwandosya aliahidi kwamba usanifu wa bwawa la Kidunda linatarajiwa kutoa mchango mkubwa wa utatuzi wa kero ya maji kwa wananchi wa Ubungo lingekamilika mwezi Septemba mwaka huo wa 2010; lakini mwezi Machi 2011 Waziri Mwandosya kauli tofauti kuwa upembuzi yakinifu wa ujenzi wa bwawa hilo utakamilika mwezi Juni mwaka 2011 na ujenzi mwaka 2013.

Kwa sababu hiyo, ni muhimu kuendelea kuwasilisha madai ili taratibu zote za msingi zikakamilishwa mwaka huu wa 2012 kwa haraka; hivyo pamoja na kutenga bilioni sita kwenye bajeti ya mwaka 2011/2012 kwa ajili ya ulipaji fidia iongeze fedha kwa ajili ya ujenzi kuanza. Maamuzi haya yafanyike pia kuhusu kuharakisha upanuzi wa Bomba la Ruvu Chini na ujenzi wa bomba jipya toka Ruvu Juu kama Serikali ilivyoahidi bungeni wakati wa kujibu swali langu la msingi tarehe 13 Aprili 2011.

Aidha, DAWASA ambayo ndiyo mamlaka yenye dhamana ya mtandao wa maji katika jiji la Dar es salaam ieleze ni lini maeneo ya pembezoni yenye mtandao wa mabomba maarufu kama mabomba ya wachina hususani ya Kimara Bonyokwa, King’ong’o, Mbezi kwa Msuguri, Malambamawili yataanza kutoa maji.

Kama hatua za dharura, DAWASA iharakishe kukamilisha uchimbaji wa visima virefu nane vyenye kuweza kuhudumia kwa ujumla wakazi zaidi ya elfu thelathini wa Kimara Mavurunza, Bonyokwa, Kilungule na King’ong’o kama ilivyoahidiwa na Rais Jakaya Kikwete mwezi Mei mwaka 2010.

Visima hivi ni suluhisho la dharura wakati tukiendelea kufuatilia suluhisho la kudumu linalopaswa kuhusisha pamoja na mambo mengine kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mikataba, kudhibiti ufisadi unaofanywa katika mtandao ikiwemo kukabiliana na upotevu wa maji unaondelea na kupanua miundombinu.

DAWASA ieleze pia mpango ilionao wa kumalizia maeneo ambayo hayakufikiwa na mtandao wa mabomba ya maji hususani ya pembezoni ya Saranga, Makoka, Msakuzi, Kibamba, Kwembe, Msakuzi, Goba, Mpiji Magohe, Makabe, Msumi, Kilungule nk.

Kwanini madai ya sasa ya maji yaelekezwe DAWASA kwa niaba ya Serikali?

Ni muhimu ikazingatiwa kuwa kwa mujibu wa katiba ibara ya 8 mamlaka na madaraka yote ni ya umma, serikali na vyombo vyake vinafanya kazi kwa niaba; hivyo wiki hii ya madai ya maji iwezeshe kuongeza msukumo katika kazi za kuboresha upatikanaji wa maji kwa njia mbalimbali.

Njia mojawapo ni pamoja na kuwasilisha madai ya mamlaka husika na kutaka majibu kuhusu kazi ambazo zinafanyika na katika wiki hii ya madai ya maji, pamoja na kuwa wahusika wa masuala ya maji ni wengi kwenye sekta ya umma na sekta binafsi; ni muhimu nguvu zielekezwe kwa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA).

Hii ni kwa sababu kwa mujibu wa Sheria ya DAWASA (Dar es salaam Water and Sewerage Authority Act no.20 of 2001) kifungu cha 22 DAWASA ndio chombo kikuu cha utekelezaji wa mipango na sera za serikali kuhusiana na maji, ugavi wa maji, huduma za maji taka na uhifadhi wa maji katika Jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es salaam kwa ujumla.

Tarehe 1 Julai 2005 DAWASA ilitoa mkataba wa ukodishaji (lease agreement) kwa DAWASCO ambao unaitaka DAWASCO kuendesha miundombinu ya maji na kuhakikisha matengenezo ya mtandao wa maji katika jiji la Dar es salaam.

Hata hivyo, uhusiano wa DAWASA na DAWASCO ni kama wa mwenye duka na muuza duka; ambao kunaweza kuwa na matatizo ya muuza duka lakini lakini panaweza kuwa na matatizo ya uhaba wa bidhaa na duka lenyewe ambayo kimsingi yanamhusu mwenye duka.

Hivyo, katika wiki hii ya madai ya maji nguvu zielekezwe kwenye kuisimamia DAWASA ambayo kwa mujibu wa kifungu cha 33 cha sheria tajwa inatumia kodi za wananchi wote ikiwemo ambao hawapati huduma ya maji toka kwao na pia tozo za wateja wanaopata maji kwa mgawo, hivyo DAWASA inawajibika kuhakikisha huduma zinapatikana kwa kuzingatia sheria, kanuni, mikataba na mipango.

Bodi ya DAWASA inapaswa kwa kuzingatia mamlaka yake kwa mujibu wa kifungu cha 10 cha Sheria tajwa na majukumu mengine ya DAWASA kwa kurejea vifungu vya 6, 7 na 8 vya sheria husika kuhakikisha huduma ya maji safi na maji taka inapatikana kwa wananchi.

Mtakumbuka kwamba Machi Mosi 2012 niliungana na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) katika kata saba Jimboni Ubungo kwenye kazi za kuboresha upatikanaji wa maji.

Tarehe 2 Machi 2012 nilifanya mkutano na wanahabari na kutaka hatua za ziada kuchukuliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) na Wizara ya Maji.

Nashukuru kwa hatua ambazo zimeanza kuchukuliwa na DAWASCO na EWURA katika masuala kadhaa; hata hivyo sijaridhika na namna ambavyo DAWASA na Wizara ya Maji wanavyoshughulikia masuala ya maji katika maeneo mengi; hivyo wiki ya madai ya maji kupitia mitandao ya kijamii itumike kuongeza msukumo wa umma kabla ya kuchukua hatua zaidi za kibunge katika Mkutano wa Saba wa Bunge unaotarajiwa kuanza tarehe 10 Aprili 2012.

John Mnyika (Mb)

Jimbo la Ubungo

18/03/2012

Friday, March 9, 2012

Mamlaka ya Urais yawezeshe uwajibikaji kumaliza mgogoro wa Serikali na Madaktari

Jana tarehe 8 Machi 2012 asubuhi nilitoa tamko kwa niaba ya CHADEMA la kutaka kauli ya haraka ya Rais Jakaya Kikwete ya kutengua uteuzi wa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Hadji Mponda na Naibu Waziri wa wizara husika Dk. Lucy Nkya kutokana na udhaifu wao mkubwa wa kiongozi waliouonyesha katika kushughulikia mgogoro wa madaktari ambao umedumu kwa muda wa takribani miezi miwili.

Nilieleza kusitikitishwa na ukweli kwamba Rais Kikwete toka mgogoro utokee hajatumia ipasavyo mamlaka yake ya kikatiba kwa mujibu wa ibara ya 34 na 35 na tarehe 5 Februari 2012 aliahidi kwamba atazungumzia kwa kina suala la mgomo wa madaktari lakini badala yake akalizungumza kwa ufupi tarehe 29 Februari 2012 katika hotuba yake kwa taifa bila kuchukua hatua za msingi hali inayoashiria ombwe la uongozi.

Nilieleza kuwa iwapo Rais Kikwete haitatoa kauli viongozi wakuu wa CHADEMA wataeleza hatua za ziada ambazo chama kitachukua kuiwajibisha serikali. Jioni Serikali ilieleza kuwa leo Rais angezungumza na wazee wa Dar es salaam, na leo imetolewa taarifa kuwa atazungumza nao kesho.

Jana usiku na leo asubuhi masuala kadhaa yameendelea kuhusu mgogoro huu, mosi; hukumu ya mahakama ya kazi, pili; uamuzi wa serikali na wadau wake kufanya propaganda dhidi ya madaktari tatu; uamuzi wa serikali kufanya mawasiliano na uongozi wa madaktari.

Friday, March 2, 2012

DAWASCO kufuata ratiba ya mgawo, ndani ya wiki moja DAWASA, EWURA na TANESCO nao wachukue hatua

Kazi ya mbunge ni kuwakilisha wananchi na kuisimamia serikali na vyombo vyake kuwezesha maendeleo. Naomba niwape mrejesho kwa muktasari; Machi Mosi tulikuwa pamoja na DAWASCO kwenye kata za Sinza, Makurumla, Mburahati, Msigani, Mabibo, Saranga, Kwembe na Makuburi tukifanya kazi za kuboresha upatikanaji wa maji katika Jimbo la Ubungo.

Itakumbukwa kwamba Septemba 2011 baada ya kwenda DAWASCO na wananchi maji yalianza kupatikana kwa kuzingatia ratiba ya mgawo kwenye maeneo zaidi ambayo hapo awali yalikuwa hayapati mgawo; hata hivyo mara baada ya mafuriko ya Disemba kisingizio cha kuharibika kwa miundombinu kikafanya ratiba husika kutokuzingatiwa kwa mwezi mzima wa Januari na mwezi Februari; hali ambayo ilirejesha kwa kiwango kikubwa pia biashara ya kinyemela ya maji.

Baada ya kuchukua hatua ikiwemo kuiandikia DAWASCO tarehe 14 na hatimaye kuwapa muda siku tatu kutoa majibu kwa umma DAWASCO ilieleza kuwa pamoja na mafuriko ratiba ya mgawo kwenye maeneo kadhaa ya Dar es salaam ilishindwa kuzingatiwa kutopata umeme wa uhakika kwenye mitambo yao ya Ruvu na pia kuharibika kwa pampu moja Ruvu Juu.

Tuliendelea kufuatilia kwa karibu suala hilo na hatimaye DAWASCO ilikamilisha matengenezo ya pampu husika hata hivyo bado kuna maeneo ambayo yalishindwa kupata mgawo kutokana hujuma katika miundombinu zikiwemo za mitandao haramu ya maji katika maeneo mbalimbali.

Wednesday, February 29, 2012

Ratiba ya mbunge na DAWASCO kwenye kata leo, hatua zaidi zitafuata

Leo Machi Mosi nitakuwa pamoja na DAWASCO katika kata mbalimbali za jimbo la Ubungo kuchukua hatua za kuboresha upatikanaji wa maji kupitia ziara ya kikazi: Sinza (Saa 3-4 As), Mabibo/Makurumla (4-5), Makuburi (5-6), Saranga (6-7 mch), Msigani (7-8), Kwembe (8-9 jn).

Izingatiwe matatizo ya maji katika maeneo mengi ya jiji la Dar es salaam ikiwemo katika Jimbo la Ubungo yamedumu kwa muda mrefu, tumepewa kazi ya kuwawakilisha kuisimamia serikali na mamlaka zake kupunguza kero husika katika kipindi cha muda mfupi; tunao wajibu wa pamoja wa kuziba pengo la miaka 50 katika kipindi cha chini ya miaka 5. Katika kipindi cha mwaka mmoja toka tupewe dhamana na dhima yapo maeneo ambayo tumewezesha yameanza kupewa mgawo wa maji, tuendelee kuunganisha nguvu ya umma zaidi katika mwaka huu wa pili wa 2012 yaongeze maeneo mengi zaidi.

Baada ya ziara hii tutawapa mrejesho kuhusu ratiba ya mgawo wa maji na hatua ambazo DAWASCO itapaswa kuendelea kuchukua. Nitawaeleza pia hatua za ziada ambazo tunapaswa kuchukua za kupanda ngazi kwenye mamlaka zingine hususan DAWASA, EWURA, Wizara ya Maji, Ofisi ya Rais na wadau wengine.

Tuendelee kushirikiana kila mmoja akichukua hatua kwa njia yake, maoni na ushauri pia unakaribishwa, wenye kutaka kuunganisha nguvu ya umma kupitia maandamano ya kuja kwa mbunge nao nawakaribisha; izingatiwe kuwa, maandamano yatayoratibiwa na ofisi ya mbunge kuwalenga wahusika wa juu zaidi yenyewe bado siku yake, tutafikia hatua hiyo iwapo serikali haitashughulikia kwa haraka masuala ambayo yanaweza kufanyika mwezi huu na kuonyesha kwa vitendo dhamira ya kutenga rasilimali za kutosha kwa mipango mingine inayoendelea kutekelezwa. Ni wakati wa mabadiliko ya kweli; tuwajibike. Maslahi ya Umma Kwanza, Twende Kazi.

Hatua nilizochukua kuhusu barabara ya Kibangu-Makoka na fidia ya Riverside

Nilichukua hatua kuhusu barabara Kibangu-Makoka na Januari nilikwenda Makuburi kuchangia matengenezo ya barabara husika , leo nimemweleza diwani kazi iharakishwe na kuhusu fidia ya wananchi wa Riverside Manispaa imenihakikishia kuwa italipwa mwezi Machi 2012; kesho nitakuwepo tena Makuburi kwa ajili ya kufuatilia masuala ya maji.

Kazi ya mbunge ni kuwakilisha wananchi na kuisimamia serikali. Kama sehemu ya wajibu huo nilitumiwa SMS na baadhi ya wananchi wa Kibangu na Makoka katika kata ya Makuburi kuhusu ubovu wa barabara ulioongezeka mara baada ya mafuriko ya mkoa wa Dar es salaam. Pamoja na kuwa barabara hii ni ya ngazi ya mitaa kwa maana ya halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, nilichukua hatua ya kuunganisha nguvu pamoja na diwani na wananchi kwa ujumla.

Izingatiwe kwamba kuhusu barabara hii nilitimiza wajibu wa uwakilishi baada ya kukutana na wananchi wa eneo husika mwaka 2010 na kunitaka niipe kipaumbele katika bajeti, kwa kushirikiana na diwani tulifanya hivyo na hatimaye barabara hii imetengewa fedha takribani milioni 100 kwa ajili ya kufanyiwa matengenezo na Manispaa ya Kinondoni katika mwaka huu wa fedha 2011/2012.

Hata hivyo, baada ya kupokea malalamiko ya siku za karibuni nilifika tena tarehe 7 Januari 2012 na kufanya mkutano na wananchi katika shule ya msingi Mabibo/Makuburi kwa ajili ya kuanza harambee ya kuunganisha nguvu ya wananchi kufanya ukarabati wa dharura wakati ambapo matengenezo makubwa ya Manispaa yakisubiriwa.