Wednesday, January 26, 2011

Kongamano la Kutatua Kero Ya Maji Jimbo la Ubungo 31/01/2010

KONGAMANO LA MAJI JIMBO LA UBUNGO


31/01/2010 CHUO CHA MAJI, UBUNGO

Ndugu Mwananchi,

Napenda kukukaribisha katika kongamano la kujadili utatuzi wa kero ya maji katika jimbo la Ubungo siku ya 31/01/2011 katika Ukumbi wa Chuo cha Maji kuanzia saa tatu asu hadi saa saba mchana.

Kwa juhudi za Mbunge, kukutanisha wananchi, wizara husika, halmashauri, asasi za kiraia, Dawasco, Sekta Binafsi na wadau wengine wowote wa maji kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa kero ya maji katika jimbo la Ubungo.

Tafadhali fika bila kukosa. Pata barua ya mwaliko ama taarifa za ziada kupitia Jonathan (0783-552010).

Karibuni nyote! Maslahi ya Umma Kwanza.

Monday, January 17, 2011

Maoni yangu kwenye Kongamano la Katiba Chuo Kikuu



John Mnyika, Mbunge wa Ubungo akizungumza kwenye Kongamano la Mchakato na Maudhui ya Katiba Mpya lililoandaliwa na UDASA katika Ukumbi wa Nkurumah Chuo Kikuu cha Dar es salaam tarehe 15 Januari 2011

Chanzo: Jamvini kupitia Youtube

Friday, January 14, 2011

Mnyika ahimiza wigo wa bima na hifadhi ya jamii upanuliwe

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amehimiza kupanuliwa kwa wigo wa bima na hifadhi ya jamii kwa kuwawezesha wananchi kukabiliana na athari za umaskini wa kipato na kuongeza ustawi.

Mnyika aliyasema hayo juzi alipowahutubia wanachama wa kikundi cha Kusaidiana Kilungule Darajani (KICHAKIDA), kilichopo Kata ya Kimara, Ubungo, ambapo alikizindua rasmi kikundi hicho na ofisi yao.

Alisema mifumo ya bima na hifadhi ya jamii (social security) inahudumia zaidi watu walio kwenye sekta rasmi na kuacha sehemu kubwa ya wananchi waliopo katika sekta isiyo rasmi, hivyo kuna haja ya kufanyika kwa mabadiliko na mifumo hiyo kurekebishwa.

“Bima na hifadhi ya jamii inahudumia zaidi watu walio kwenye sekta rasmi na kuacha sehemu kubwa ya wananchi walio kwenye sekta isiyo rasmi,” alisema Mnyika.

Aidha, aliwapongeza wananchi wa eneo hilo kwa kuanzisha kikundi hicho, kwani kinatoa baadhi ya huduma za msingi zinazopaswa kutolewa na mifumo rasmi ya bima au hifadhi ya jamii.

Kadhalika, mbunge huyo aliwataka wananchi wa Ubungo kuendelea kuunga mkono hoja ya kuandikwa kwa Katiba mpya na marekebisho ya kisheria ili pamoja na mambo mengine kuwepo kwa mifumo thabiti zaidi ya bima na hifadhi za kijamii kama suluhisho la kudumu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa KICHAKIDA, alimueleza mbunge huyo kwamba kikundi hicho kina wanachama 100 ambapo kinawahudumia wategemezi zaidi ya 500 wanaotoka kwenye kaya za wanachama hao katika matatizo ya kijamii kama maradhi, misiba na mikopo ya elimu.


Chanzo: Tanzania Daima (13/01/2011)

Mnyika ataka Maji yafunguliwe Mbezi

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika amefanya ziara ya ghafla tarehe 3 Januari 2010 ya kutembelea visima na maghati ya maji katika jimbo la Ubungo na kubaini mapungufu katika maghati hayo hususani kuuza maji bei juu tofauti na ile iliyopangwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA).

Mbunge Mnyika ameeleza kuwa kwa mujibu wa agizo la EWURA na: 10-017 la tarehe 10 Juni 2010 bei ya maji katika mabomba ya jumuiya au maghati ya maji inapaswa kuwa shilingi 20 kwa kila lita 20, sawa na shilingi moja kwa lita lakini maghati mengi yanatoza kati ya mia moja mpaka mia tatu hali inayoongeza gharama za maisha na kusababisha ugumu wa maisha kwa watanzania wa kipato cha chini.

Mbunge Mnyika ametoa mwito kwa EWURA kukagua visima na maghati yote ili kuhakikisha agizo hilo linatekelezwa ikiwemo la bei husika kubandikwa kwenye kila eneo ili wananchi watambue haki yao wasitozwe kinyume na viwango vinavyostahili.

Hata hivyo Mbunge Mnyika amesema kwamba katika kufanya hivyo lazima EWURA iwahusishe kwanza wananchi na viongozi wa kuchaguliwa ili hatua zozote zinazochuliwa ziweze kulinda maslahi ya umma.

Mbunge Mnyika alisema kwamba amepokea taarifa toka kwa wananchi kwamba yapo maghati yamefungwa kwa maagizo ya EWURA kutokana na mivutano baina ya DAWASCO, DAWASA na wafanyabiashara binafsi wanaoendesha maghati hayo kuhusu bei ya maji hali ambayo imesababisha baadhi ya wananchi kukosa maji kwa takribani wiki moja.

Mbunge Mnyika ameitaka serikali iingilie kati na kuagiza vioski husika vya maji vifunguliwe ili wananchi waweze kupata huduma hii muhimu ya msingi.

Mbunge Mnyika amesema wananchi hawapaswi kuhukumiwa kwa kunyimwa maji kwa makosa yasiyokuwa ya kwao hivyo serikali kupitia DAWASA na DAWASCO inapaswa kutuma wafanyakazi wake kusimamia vioski husika ili huduma za msingi za maji zikiendelea kutolewa kwa wananchi wakati suala la ongezeko la bei ya maji kinyemela likiendelea kushughulikiwa.

Mbunge Mnyika ameeleza kuwa kwa mujibu wa takwimu za Bajeti ya Kaya asilimia 38 ya wananchi wa Jimbo la Ubungo sawa na wastani wa watu wanne katika kila wakazi kumi wanategemea maji ya vioski na maghati hayo hivyo usimamizi mzuri zaidi unahitajika ili wananchi wasikose huduma za msingi na wasipate kwa gharama nafuu kama ilivyopangwa.

Chanzo: Global Publishers (04/01/ 2011

Monday, January 10, 2011

Moja ya bidhaa za wajasiriamali wanawake


Mbunge wa Ubungo, John Mnyika akipokea zawadi kuku toka kwa Halima Mwagama mweka hazina wa Kikundi cha Wanawake Gide ikiwa ni moja ya bidhaa zinazozalishwa na wanawake wajasiriamali

Mnyika ahimiza wananchi kununua bidhaa za Tanzania

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika, amewahimiza wananchi wa jimbo hilo na Watanzania kwa ujumla kununua bidhaa zinazozalishwa nchini ili kulinda uchumi wa nchi na kuongeza ajira kwa Watanzania hasa wanawake na vijana.

Mnyika alitoa rai hiyo mwishoni mwa wiki wakati akizungumza na wanawake wajasiriamali kwenye hafla ya kusherehekea mwaka 2011, Ubungo jijini Dar es Salaam sambamba na kutembelea miradi ya uzalishaji mali inayoendeshwa na kikundi cha Gide Women Group-GWG.

Alisema ongezeko la mfumuko wa bei hapa pamoja na kusababishwa kwa kupanda holela kwa gharama na mzigo mkubwa wa ufisadi unaochangiwa pia na kupungua kwa uzalishaji wa ndani katika taifa na utegemezi wa bidhaa kutoka nje.

“Wazalishaji wetu wa ndani wapo lakini wanapata changamoto ya kukosa masoko kwa kuwa hapa nchini, kumejengeka utamaduni wa watu kukimbilia bidhaa za nje na pia wajasiriamali wengi kuacha uzalishaji na kujikita kwenye uchuuzi wa bidhaa hizo za kutoka ughaibuni,” alisema.

Mnyika aliongeza kuwa amefurahishwa na jitihada zinazoonyeshwa na wanawake kujiajiri kwa kuanzisha miradi ya ufugaji kuku wa kienyeji, ushonaji wa vitambaa pamoja na utengenezaji wa sabuni za matumizi ya majumbani hali inayowaongezea kipato cha kujikimu na familia zao.

Naye Mwenyekiti wa kikundi hicho, Rita Paul, alimpongeza Mnyika kwa kushinda katika uchaguzi mkuu uliopita na kwamba ana changamoto kubwa ya kushirikiana na vikundi mbalimbali vya maendeleo katika jimbo hilo.

Aidha, alisema kikundi hicho toka kuanzishwa kwake mwaka 2007, kimeweza kupokea hisa toka kwa wanachama wake ambazo thamani yake imefikia Sh. milioni 30 japo bado kinakabiliwa na changamoto mbalimbali.

Mnyika alitumia fursa hiyo kuwahimiza wanawake kushiriki katika mjadala wa katiba mpya kwani unagusa haki za msingi za makundi yote katika jamii na mustakabali wa vizazi mbalimbali.

“Ukifuatilia mjadala wa katiba utakuta umetawaliwa na sauti za wanaume, wanawake wachache sana wametoa misimamo yao, wengi wao ikiwa ni kutokana na nafasi zao kwenye utumishi mathalani, Waziri Celina Kombani, Spika Anne Makinda na wanaharakati kama Ananilea Nkya. Hivyo, nawahamasisha wanawake wa Ubungo kuwa mstari wa mbele kwenye mjadala huu,” alisema Mnyika.

Mnyika alisema katiba ndiyo inayotoa haki za msingi kama za umiliki wa ardhi, huduma za msingi za kijamii na hata uwakilishi kwenye vyombo vya maamuzi hivyo, wanawake wanapaswa kushiriki kujadili kutokana na changamoto za kiuchumi, kijamii na kisiasa zinazolikabili taifa kuwagusa kwa kiwango kikubwa.

Chanzo: Nipashe (10/01/2011)

Hoja ya Katiba Mpya bado ipo

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amesema taarifa ya hoja ya mabadiliko ya Katiba aliyoiwasilisha kwa katibu wa Bunge iko pale pale na mchakato wa kupata maoni ya wananchi na wataalamu wa sheria utaendelea kama ilivyokusudiwa awali.

Mnyika alieleza hayo jana katika taarifa yake kwa vyombo vya habari na kusisitiza muhimu wa hoja hiyo kurejeshwa kwa wananchi kupitia chombo cha uwakilishi cha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema hatua hiyo inatokana na kupokea ushauri na kutakiwa kuendelea na hoja ya mabadiliko ya Katiba mpya baada ya hotuba ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu Katiba mpya kuacha kutoa ufafanuzi kuhusu mchakato wake.

Mbunge huyo alisema Rais Kikwete alionyesha bayana hana mpango wa kuhusisha umma kuanzia hatua za awali, hivyo kupitia kuwasilisha hoja au muswada bungeni ili kuwekwa mfumo wa kisheria wa kuratibu na kuongoza mchakato mzima wa kuandikwa kwa Katiba mpya ya Tanzania.

“Kuna ushahidi kuwa serikali ya Rais Kikwete haina dhamira ya kuandika Katiba mpya inayohusisha umma na badala yake kuendeleza hodhi ya serikali ambayo inaweza kusababisha mapitio yenye kasoro za miaka yote,“ alisema mbunge huyo.

Alisema hatua hiyo ya Rais Kikwete, inadhihirisha anaitaja Katiba mpya kwa maneno bila kuonyesha vitendo kuwezesha mchakato huo kwa kuushirikisha umma kwa ukamilifu.

“Kutokana na maoni niliyopokea na utata wa kauli za serikali kuhusu mchakato wa Katiba mpya naendelea kukamilisha taratibu za kuwasilisha hoja binafsi kwenye Bunge la Februari kuhusu mchakato wa Katiba mpya,” alisema Mnyika.

Alisema kutokana na mjadala unaoendelea inaonekana ipo haja ya suala hilo la mchakato wa Katiba mpya kupata uhalali wa umma kwa kurejea Ibara ya 8 ambayo inatamka madaraka na mamlaka ni ya umma serikali inafanya kazi kwa niaba na Bunge ndicho chombo kikuu cha kusimamia.

Akifafanua zaidi Mnyika alisema wajibu huo unatokana na mamlaka ya Kikatiba yaliyopo kwenye ibara ya 63 (2) na (3) na Ibara ya 98 inayohusika na mabadiliko ya Katiba ya nchi.

Desemba 27, mwaka jana mbunge huyo aliwasilisha hoja binafsi kuhusu madai ya Katiba mpya kwa katibu wa Bunge ili ijadiliwe katika kikao cha Bunge Februari mwaka huu.

Mara baada ya kuwasilisha hoja hiyo, Mnyika alisema Katiba iliyopo sasa imefanyiwa marekebisho mara 14 na kutoa mapungufu 90 ya Katiba ya sasa.

Chanzo: Tanzania Daima (10/01/2011)

Mnyika aendelea na mchakato wa hoja

MBUNGE wa Ubungo, Bw. John Mnyika ameamua kuendelea kuwasilisha hoja binafsi bungeni kuhusu katiba kama alivyokusudia kutokana na serikali kuacha kutoa ufafanuzi wiki moja baada ya mwito wa kutakiwa kufanya
hivyo.

Kwa mujibu wa taarifa aliyoitoa jana kwa vyombo vya habari, Bw. Mnyika alisema kutokana na Rais Jakaya Kikwete na serikali yake kuacha kutoa ufafanuzi kuhusu hoja binafsi wiki moja baada ya mwito wa kutakiwa kufanya hivyo inaonyesha bayana kwamba hakuna mpango wa kuhusisha umma.

"Inaonyesha bayana kwamba hakuna mpango wa kuhusisha umma kuanzia hatua za awali katika mchakato kupitia kuwasilisha hoja au muswada bungeni ili kuwekwa mfumo wa kisheria wa kuratibu na kuongoza mchakato mzima wa kuandikwa kwa katiba mpya," alisema.

Alisema ushahidi kuhusu serikali yake kutokuwa na dhamira ya kuandika katiba mpya inayohusisha umma na badala yake kuendeleza kuhodhi ya serikali ambayo inaweza kusababisha mapitio yenye kasoro zile zile za miaka yote, ni kauli ya Rais Kikwete aliyoitoa mwaka mpya mbele ya mabalozi.

Bw. Mnyika alisema kwenye hafla hiyo Rais Kikwete amerudia tena kauli ya kuunda moja kwa moja tume ya kuratibu na kuongoza mchakato mzima wa maoni bila kuhusisha bunge katika hatua za msingi.

"Baada ya kauli niliyotoa ya kutaka ufafanuzi na matamko yaliyotolewa na wadau mbalimbali ya kueleza kasoro za hatua ya Rais Kikwete ya kutaka kuunda tume nilitarajia kwamba katika kauli yake ya kwanza kabisa ya mwaka huu angetumia fursa hiyo kufafanua suala husika, ikiwemo kueleza kusudio la kupeleka mapendekezo ya mchakato bungeni," alisema.

Bw. Mnyika alisema kuwa hiyo inadhihirisha kwamba Rais Kikwete anataka katiba mpya kwa maneno tu, lakini haonyeshi kwa vitendo kuwezesha mchakato husika kwa kuushirikisha umma kwa ukamilifu.

Alisema kutokana na maoni aliyopokea na utata wa kauli za serikali kuhusu mchakato wa katiba mpya, anaendelea kukamilisha taratibu za kuwasilisha hoja binafsi kwenye bunge la Februari kuhusu mchakato wa katiba mpya, na tayari alikwishawasilisha taarifa ya hoja Desemba 27 mwaka jana.

Mbunge huyo alisema kutokana na mjadala unaoendelea inaonekana bayana kwamba bado iko haja ya suala hilo la mchakato wa katiba mpya kupata uhalali wa umma kwa kurejea Ibara ya 8 ambayo inatamka kwamba madaraka na mamlaka ni ya umma.

Pia kuwa serikali inafanya kazi kwa niaba na bunge ambalo ndicho chombo kikuu cha kusimamia wajibu huo kutokana na mamlaka ya kikatiba yaliyopo kwenye ibara ya 63 (2) na (3) na ibara ya 98 inayohusika na mabadiliko ya katiba.

Chanzo: Majira (10/01/2010)

Mnyika holds stance on constitution

Dar es Salaam. The Ubungo MP, Mr John Mnyika (Chadema), has resolved to continue with his intention of tabling a private motion during the next parliamentary session, to demand that the law-making organ set a system that would be used during the review of the Constitution.

There were conflicting views on the validity of Mr Mnyika’s private motion after President Jakaya Kikwete announced in his end-of-the-year speech that the government had agreed to a major review of the Constitution.

In a press statement he circulated yesterday, Mr Mnyika said he has decided to go ahead with the private motion after consulting stakeholders on President Kikwete’s stand on the Constitution .

In accordance with parliamentary regulations, Mr Mnyika has already notified the clerk of the National Assembly on his intention to table a private motion during the February session.

He said that in reaching the decision to go ahead with his private motion he had consulted constitutional experts, leaders of civil society organisations, religious leaders, his party’s senior officials and Ubungo residents.

“Moreover, one week after President Kikwete was asked, but failed, to give an explanation on how the government was going to deal with the issue, it is clear that there is no plan to involve the public in the Constitutional review process,” said Mr Mnyika.

“My private motion seeks to ensure that people are involved in the process and therefore I will go ahead with the motion,” he said.

Mr Mnyika said President Kikwete’s speech, during the sherry party he organised at the State House last week, was another indication that he has no plans to involve wananchi in the process.

According to Mr Mnyika, in President Kikwete’s speech he insisted that his intention was to form a committee to review the Constitution.

The opposition party official also revealed that in his private motion he would push for Parliament to approve the 15th amendment of the Constitution with the aim of changing Article 98, by introducing a third Sub-Article which would comprise a process that requires the public to be involved in the constitutional review process.

Source: The Citizen (10/01/2011)

Mnyika alia na usimamizi wa maji

MBUNGE wa Jimbo la Ubungo John Mnyika (CHADEMA) amesema usimamizi mbovu wa nishati ya maji unachangia huduma hiyo kutopatika kwa watu wengi zaidi.

Mnyika alitoa kauli hiyo juzi mara baada ya kufanya ziara ya kutembelea visima na maghati ya maji ambapo alibaini uuzaji wa maji kwa bei kubwa tofauti na ile iliyopangwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma ya Nishati na Maji (EWURA).

Alisema asilimia 38 ya wananchi wa jimbo hilo sawa na wastani wa watu wanne wanategemea maji ya vioski na maghati hivyo ni vema kuanzia sasa kukawepo na usimamizi mzuri ili wananchi wengi waweze kuipata huduma hiyo kwa bei nafuu.

Alibainisha kuwa kwa mujibu wa agizo la EWURA, namba 10-017 la Juni 10, 2010 bei ya maji katika mabomba ya jumuiya au maghati ya maji inapaswa kuwa shilingi 20 kwa kila lita 20.

Alisema amepata taarifa kuwa wananchi wanatozwa lita moja kwa shilingi mia moja hadi mia tatu hali inayochangia ugumu wa maisha hasa kutokana kuwa na kipato kidogo.

Aliishauri EWURA kukagua visima na maghati yote ili kuhakikisha agizo hilo linatekelezwa ikiwemo bei husika kubandikwa kwenye kila eneo ili wananchi watambue haki yao wasitozwe kinyume na viwango vinavyostahili.

Mnyika alisema katika kufanya hivyo lazima EWURA iwahusishe kwanza wananchi na viongozi wa kuchaguliwa ili hatua zozote zinazochukuliwa ziweze kulinda maslahi ya umma.


Chanzo- Tanzania Daima (04/01/2011)

Sunday, January 2, 2011

Kauli yangu juu ya tamko la Rais Kikwete kuhusu Katiba Mpya

Mara baada ya hotuba ya Rais Jakaya Kikwete ya tarehe 31 Disemba 2010 nikiwa safarini nimepokea simu na ujumbe wa simu pamoja na barua pepe toka kwa vyombo mbalimbali, baadhi ya viongozi wa kada anuai na wananchi kadhaa wakitaka kujua msimamo wangu kuhusu kauli ya Rais Kikwete kukubali hoja ya kuandikwa kwa katiba mpya na kutangaza kuunda Tume ya mchakato husika.

Aidha baadhi ya simu na barua hizo zimetaka kujua hatma ya hoja binafsi ambayo nilipanga kuiwasilisha kwenye Mkutano wa Bunge wa Mwezi Februari kuhusu mchakato husika; hoja ambayo nimeshawasilisha taarifa yake ya hoja kwa Katibu wa Bunge.
Katika simu hizo na barua pepe wako baadhi ya watu ambao wamekwenda mbele zaidi kwa kutoa maoni wengine wakitaka bado hoja binafsi iwasilishwe bungeni na wengine wakishauri kwamba sasa nguvu zielekezwe katika Tume iliyotangazwa kuundwa na Rais kuhusu mchakato husika.

Katika muktadha huo nimeona ni vyema nitoe kauli rasmi kuhusu suala husika ili msimamo na maoni yangu kuhusu suala husika ufahamike wa wananchi wa Ubungo na Watanzania wenzangu kwa ujumla kuhusu suala hili nyeti linalogusa mustakabali wa taifa letu.

Natambua tofauti aliyoionyesha Rais Kikwete kwenye jambo hili kwa kutambua haja ya katiba mpya kinyume na kauli za watendaji wake ndani ya serikali za hivi karibuni ( Waziri Kombani, Waziri Mkuu Pinda na baadaye Mwanasheria Mkuu Werema) ambao wote walitaka marekebisho ya katiba kwa kuwekwa viraka mbalimbali.

Aidha natambua kuwa kauli ya Rais Kikwete kukubali kuandikwa kwa katiba mpya inaashiria mabadiliko ya kimtazamo kwa upande wake pia ukilinganisha na kauli zake mbalimbali katika kipindi cha kuanzia mwaka 2005 mpaka mwaka 2010 kuhusu suala la mabadiliko ya mfumo wa utawala katika taifa hali inayoashiria kwamba ametambua kuwa hitaji la katiba mpya ni la watanzania waliowengi ambalo limetolewa kauli na wadau mbalimbali.

Pamoja na kukubali kuandikwa kwa katiba mpya bado watanzania wanahitaji kujadili kwa kina na kwa haraka kuhusu mchakato uliopendekezwa ili taifa liende katika mkondo sahihi wa kuanza kutoa maoni.

Ni muhimu kwa wadau wote kutaka kufahamu muundo wa Tume pamoja na hadidu rejea kwa kina ili kuepuka taifa kuanza mchakato kwa njia isiyo kamili; kinyume na hapo watanzania tunaweza ‘kuuziwa mbuzi kwenye gunia’.

Suala hili ni la msingi kwa kuwa Historia ya Taifa letu inaonyesha kwamba Tume zilizoundwa na Marais na kushughulika na masuala yanayogusa Katiba hazikuweza kukidhi matakwa ya wananchi kwa sababu mbalimbali.

Mathalani, taifa linajadili sasa kuhusu mabadiliko ya katiba kutokana na kasoro katika hatua za awali za kuandikwa kwa Katiba ya Kudumu ya Tanzania ya mwaka 1977 ambayo ndiyo tunayoitumia hivi sasa pamoja na marekebisho yake.
Mchakato uliotumiwa na Rais wa wakati huo, Hayati Julius Nyerere ndio ambao unajitokeza sasa kwenye Hotuba ya Rais Kikwete kwa kueleza kwamba Rais anaunda tume na baadaye mapendekezo ya tume yanakwenda moja kwa moja kwenye vyombo vya kikatiba bila kwanza kuwa na .

Matokeo ya utaratibu huu ni wananchi kutoshirikishwa kwa ukamilifu wake katika maamuzi yanayohusu katiba. Tume ya Rais ya wakati huo iliyokuwa chini ya Thabiti Kombo ilifanya kazi ya kukusanya kwa muda mfupi, matokeo yake yakaenda kujadiliwa kwenye Halmashauri Kuu ya chama tawala wa siku moja, na hatimaye yakapelekwa bungeni na kupitishwa baada ya majadiliano ya muda mfupi sana (kumbukumbu za kihistoria zinaonyesha kwa saa tatu tu).

Matokeo ya mfumo huo ni kuandikwa kwa katiba isiyokubalika na umma kwa uwingi wake na kusababisha mpaka sasa marekebisho (viraka) mara kumi na nne na bado kuna mapungufu mengi kwa kiwango cha sasa kukubaliana kuandika katiba mpya.
Natambua kwamba Rais Kikwete amesema kwamba Tume itakwenda kukusanya maoni kwa umma, lakini jambo la muhimu sio kupatikana kwa maoni tu, suala la msingi na maamuzi kuhusu ni maoni ambayo ndiyo yanatumika kama msingi wa katiba mpya na makubaliano ya pamoja kuhusu misingi muhimu ya katiba mpya.

Katika mazingira hayo, ndipo panapojitokeza umuhimu wa kuwa na Mkutano Mkuu wa Taifa Katiba kabla ya mapendekezo ya katiba kupelekwa kwenye mamlaka za kikatiba ambazo kwa mujibu wa katiba ya sasa ibara ya 98 ni Bunge pekee. Kauli ya Rais Kikwete inaashiria kwamba wananchi hawatahusishwa moja kwa moja kwenye kuamua katiba badala yake tume itachukua maoni yake na baadaye maamuzi yatafanywa na bunge kwa niaba yao kama ilivyo kwenye marekebisho ya kawaida ya katiba kwa mujibu wa ibara ya 98 ya katiba.

Izingatiwe kuwa kwa sasa Tanzania haifanyi marekebisho ya Katiba bali tunakwenda kufanya mapitio (review) na hatimaye kuwa na katiba mpya; hivyo suala la ushirikishwaji wa umma sio katika kutoa maoni tu bali kuamua misingi muhimu ya katiba ni suala lenye umuhimu wa pekee ili tuwe na katiba inayokubalika na umma mpana isije yakajirudia tena yaliyojitokeza kwenye kuandikwa kwa katiba ya mwaka 1977.
Kutokana na mapungufu yaliyopo kwenye Katiba hii tunayotumia sasa kwenye ibara ya 98 ambapo haijaweka bayana mchakato wa kuandikwa kwa katiba mpya bali mabadiliko ya katiba, ni muhimu kutumia mamlaka ya ibara hiyo ya katiba kifungu cha pili kuwezesha Bunge kutunga sheria itayosimamia na kuwezesha mchakato wa mapitio (review) ya katiba ili kupata katiba mpya.

Sheria hiyo itawezesha kuwekwa utaratibu wa Kongamano/Mkutano wa Taifa, Tume ya Katiba, Bunge Maalum la Katiba na hata kutafakari uwezekano wa kufanya kura ya maoni (referendum) katika masuala nyeti kama Muungano.

Kutokana na kujitokeza bayana kwa mahitaji ya kisheria kuhusu mchakato inaonekana bayana kwamba bado iko haja ya suala hili la mchakato wa katiba mpya kupata uhalali wa umma kwa kurejea ibara 8 ambayo inatamka kwamba madaraka na mamlaka ni umma serikali inafanya kazi kwa niaba na Bunge ndicho chombo kikuu cha kusimamia wajibu huo kwa kutokana na mamlaka ya kikatiba yaliyopo kwenye ibara ya 63(2) na (3) na ibara ya 98 inayohusika na mabadiliko ya katiba.

Katika mazingira hayo nasubiri kwanza ufafanuzi wa serikali kuhusu mchakato husika ikiwemo kujua kwa kina muundo wa tume, hadidu rejea na kama serikali itapeleka bungeni mapendekezo kuhusu mchakato kabla ya kutoa kauli kuhusu hatma ya hoja binafsi ambayo nilitoa taarifa kuwa nitaiwasilisha bungeni katika mkutano wa mwezi Februari.

Na katika kipindi ambacho nasubiria ufafanuzi wa serikali ambao inapaswa kuuweka hadharani nitaendelea na hatua ambazo nilizitangaza nilipokwenda kuwasilisha taarifa ya hoja tarehe 27 Disemba 2010.

Hata hivyo, kutokana na kauli ya Rais Kikwete na hatua za ziada ambazo natarajia kutoka kwa serikali nitatumia wiki ya kwanza ya mwezi Januari kukutana ana kwa ana na baadhi ya viongozi wa asasi za kiraia, taasisi za dini na vyama vya siasa ikiwemo CHADEMA kuweza kushauriana hatua za ziada za kuchukua.

Kimsingi, kama nilivyoeleza awali, hoja hiyo pamoja na kuwa inaitwa hoja binafsi kwa kanuni za bunge ni mimi ni mwakilishi lakini hoja ya umma kutokana na kuwa katiba mpya ni hitaji la wananchi hivyo maamuzi kuhusu hatma ya hoja husika yatafanywa kwa kushauriana na wananchi na wadau wengine baada ya kupata ufafanuzi wa serikali.
Aidha kabla ya wananchi kuanza kutoa maoni kuhusu maudhui (nini kiwemo ndani ya katiba mpya) natoa mwito kwa wadau wote kujadili kwa kina mchakato (taratibu gani zifuatwe) wa katiba mpya; kwa kuwa mchakato usipokuwa sahihi hata maoni mazuri yakitolewa yanaweza yasifikie hatua ya kufanyiwa kazi kwa ukamilifu na hatimaye tukakosa tija ambayo tunaikusudia kwa kuandikwa kwa katiba mpya miaka 50 baada ya uhuru.

Tukumbuke kwamba mwaka 1991 Rais wakati huo Ali Hassan Mwinyi aliunda tume ya kuhusu mfumo wa vyama Tanzania (maarufu kama Tume ya Nyalali) na kwamba tume hiyo ilikuja na mapendekezo mengi ikiwemo la kutaka kuandikwa kwa katiba mpya, lakini serikali ilichukua machache ikiwemo la kuanza kwa mfumo wa vyama vingi. Mchakato tunaotaka kuuanza sasa ungeshakamilika miaka mingi kama mapendekezo ya wakati ule yangetekelezwa kwa ukamilifu wake.

Kadhalika tukumbuke kwamba mwaka 1998 Rais wa wakati huo Benjamin Mkapa aliunda Tume ya marekebisho ya Katiba (Maarufu kama Tume ya Kisanga aliyoratibu maoni kwa kutumia White Paper), hata hivyo sehemu kubwa ya mapendekezo ya Tume hayakutekelezwa. Na Rais wa wakati huo aliikataa hadharani sehemu kubwa ya taarifa yao na kutangaza kuwa tume imefanya kazi kinyume na hadidu rejea. Wakati huo tume ilielezwa kuwa ilikwenda kinyume na maoni ya wananchi lakini kimsingi ni kwamba mapendekezo ya tume yalikwenda tofauti na misimamo ya serikali ambayo ilianishwa bayana kwenye White Paper. Suala hili lilijitokeza kwa kuwa kuwa kwa mujibu wa Katiba ibara ya 37 Rais katika kufanya kazi zake halazimiki kufuata ushauri wa mtu yoyote; hivyo suala la kuwa na mfumo ambao mapendekezo yake yatakubalika na kuheshimika ni la muhimu sana kabla ya kuanza kutoa maoni ya kuingizwa kwenye katiba mpya.

Ndio, maana ni muhimu kwa mchakato wa sasa kufanyika kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na kuwekewa utaratibu bayana ikiwemo kuitaka tume yoyote itayoundwa kutumia mfumo wa Green Paper ili wananchi wenyewe kuanza kutoa maoni yao kuhusu masuala wanayoyaona kipaumbele badala ya kuathiriwa kimsimamo na serikali au tume yenyewe.

Natambua kwamba Rais Kikwete amedokeza kuwa Tume anayotaka kuiunda itahusisha wadau hata hivyo ni muhimu tume ikaundwa katika mfumo ambao ni shirikishi, sio tu wajumbe kuteuliwa kutoka sekta au kada Fulani bali pia kuwe na mashauriano (consultation) kati ya kada au sekta husika kabla ya uteuzi ili kuwe na uwakilishi badala ya wahusika kujiwakilisha wenyewe au kumwakilisha aliyewateua. Ndio maana katika mazingira hayo, tume inayoundwa kwa sheria ya bunge ingekuwa na uzito zaidi na kazi yake kupata kuungwa mkono. Jambo hili ni muhimu kwa kurejea yaliyojiri katika mchakato wa kuundwa kwa Kamati ya Rais ya kupitia upya mikataba ya madini (maarufu kama Kamati ya Bomani); hali hiyo haipaswi kujitokeza sasa katika mchakato wa kuunda Tume ambayo inashughulika na suala tata na tete la katiba mpya ambalo kukubalika kwa mchakato na chombo kinachoratibu ni hatua ya msingi sana katika kuwa na katiba inayokubalika na umma.

Pamoja na njia ya kibunge ambayo niliidokeza wakati naeleza kusudio la hoja binafsi, Rais Kikwete na serikali yake kwa dhamira ya kuhusisha umma katika kuandika katiba mpya kuanzia katika hatua za awali ingeweza kuitisha Kongamano la Kitaifa (National Congress) kujadili tunu za taifa kitaifa, misingi ya kikatiba, muundo/majukumu ya tume ya katiba, kutoa mwongozo wa bunge la katiba na namna ya kufanya kura ya maoni (referendum). Hivyo, kama serikali haitatoa maelezo yanayokidhi haja na hoja bado Bunge litawajibika kutimiza wajibu wake wa kikatiba kwa niaba ya wananchi kwa kurejea ibara ya 63(2) na (3) ili kuweka mchakato muafaka zaidi wa katiba mpya kama sehemu ya kuisimamia na kuishauri serikali inayoongozwa na Rais Kikwete katika hatua hii muhimu ya kuandika katiba mpya- ambayo ni sheria mama na mkataba kati ya wananchi na serikali.