Tuesday, June 29, 2010

Mnyika ataka Londa, Kandoro na Makamba wahojiwe ufisadi wa ardhi

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuf Makamba na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Abbas Kandoro, wanastahili kuhojiwa katika kashfa ya uuzwaji viwanja vya wazi katika manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Viongozi hao katika chama tawala na serikali, wanadaiwa kuhusika katika kashfa hiyo walipokuwa Wakuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa nyakati tofauti.

Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Mnyika, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa, Makamba anatajwa kama Katibu Mkuu wa CCM na pia anatajwa kwa nafasi yake alipokuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.

Chadema inataka viongozi hao wahojiwe kwa vile wanatajwa kwenye taarifa ya kamati ya siasa ya halmashauri kuu ya CCM wilayani Kinondoni.

Alisema taarifa hiyo ya siri ya Machi 15, mwaka juzi, ilihusu mgogoro wa madiwani wa manispaa ya Kinondoni dhidi ya Meya wake, Salum Londa, mpasuko miongoni mwa madiwani, ubadhirifu wa fedha, mali ya manispaa na uongozi mbovu katika manispaa hiyo.

Mnyika alisema Kandoro, ambaye ndiye aliyemrithi Makamba kwa nafasi hiyo mkoani humo, anatakiwa ahojiwe kwa vile naye anatajwa katika taarifa hiyo.

Mbali na Makamba na Kandoro, Chadema pia inataka Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi, awaeleze Watanzania alikuwa anafahamu nini kuhusu kashfa hiyo, ambayo inawataja kwa majina Londa na madiwani wengine wa manispaa ya Kinondoni kwenye tuhuma za rushwa na uuzaji wa viwanja.

Katika taarifa hiyo, Londa anatuhumiwa kupokea rushwa ya Sh. milioni 20, na kwa sababu hiyo Chadema, inataka asiishie kuhojiwa tu, bali akamatwe na kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma hizo.

Kwa mujibu wa Mnyika, Chadema inataka viongozi hao wahojiwe na Polisi pamoja na kamati iliyoundwa na Lukuvi hivi karibuni.

Kamati hiyo iliundwa kwa lengo la kupitia maeneo yote ya wazi ya jiji la Dar es Salaam, kuyabaini na kuainisha kama yalivyo katika ramani kuu (master plan).

Hatua hiyo ingefanikisha kufahamu orodha kamili ya maeneo hayo, yalipo, yamepangiwa shughuli gani na wamiliki ni akina nani na utaratibu gani ulitumika kuyagawa.

Mnyika ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Chadema, alisema wanataka viongozi hao wahojiwe na wengine kukamatwa ili kujiridhisha kwamba, dhamira ya kuundwa kwa kamati hiyo si mchakato wa kisiasa wa kuelekea Uchaguzi Mkuu.

Alisema siasa hizo zinaweza kutumiwa kupitia kero zinazowakabili wananchi kwa muda mrefu na mbazo serikali ya awamu ya nne haijazishughulikia tangu iingie madarakani.

“Sasa kama kweli wana dhamira ya dhati ya kuchukua hatua, tunataka polisi na kamati husika wamhoji Makamba kwa sababu anatajwa humu (kwenye taarifa ya CCM) siku zote, anatajwa kama Katibu Mkuu wa CCM, anatajwa kama kwa nafasi yake alipokuwa Mkuu wa Mkoa,” Mnyika alisema.

Aliongeza: “Wamhoji Kandoro, kwa sababu anatajwa humu. Na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wa sasa hivi, Lukuvi, ambaye ndiye ameunda kamati, na yeye awaeleze Watanzania alikuwa anafahamu nini kuhusu hii taarifa ya mwaka 2008.”

Taarifa hiyo ya CCM ni ile inayowataja kwa majina Londa na madiwani wengine kwenye tuhuma za rushwa za uuzaji wa viwanja.

Wakati Chadema ikishinikiza hivyo, sakata hilo linaonekana `kumchanganya akili’ Meya Londa, ambaye hivi sasa anahaha kumsaka mchawi.

Meya Londa aliitisha kikao cha dharura cha Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Kinondoni jana, katika kile kilichoelezwa kuwa ni kuwatafuta madiwani wanaohusika katika uvujishwaji wa taarifa zinazohusu kadhia hiyo.

Kwa mujibu wa habari za kuaminika kutoka ndani ya kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa baraza hilo, Meya Londa anadaiwa kukanusha tuhuma zinazomkabili.

Londa na madiwani wengine watano wa manispaa hiyo, walikwisha kuhojiwa na polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam juu ya tuhuma za uuzaji wa viwanja.

Mmoja wa madiwani waliohudhuria kikao cha jana, alieleza kuwa ajenda iliyotawala kikao hicho ilihusu masuala ya uuzaji wa viwanja vya wazi.

Hata hivyo, madiwani wengine walipoulizwa kikao hicho kilikuwa kinahusu nini, walisema kilikuwa kililenga masuala ya kisiasa yanayokihusu CCM.

Kwa upande mwingine jana maofisa mbalimbali wa serikali walikutana katika manispaa hiyo kwa ajili ya kikao maalumu cha kuendelea kufanya uchunguzi wa kashfa ya uuza viwanja kinyume cha sheria na taratibu.

Kikao hicho kilifanyika ukumbi wa jirani na walipokuwa wamekaa madiwani hao, ambapo pande zote hazikuruhusu waandishi wa habari kuhudhuria.

Alipoulizwa na waandishi wa habari, Londa alithibitisha kufanyika kikao hicho cha madiwani, lakini akasema ajenda kuu ilikuwa ni kuzungumzia masuala ya Chama cha Kuweka na Kukopa (Saccos) ilichoanzishwa na madiwani hao.

“Unajua sisi tuna Saccos yetu hapa kama madiwani na kwa kuwa tunamalizia muda wetu, lazima tuchukue fedha kwa ajili ya kwenda kufanyia kampeni,” alisema.

Meya huyo alionekana kutotaka kujibu maswali zaidi kutoka kwa waandishi wa habari waliofika ofisini kwake, ili kupata ufafanuzi kuhusu kikao alichoitisha.

Awali, Mnyika alisema wanatilia shaka utendaji wa kamati hiyo inayoanza kazi yake leo kwa sababu mbalimbali, ikiwamo muundo wake na uadilifu wa mwenyekiti anayeiongoza, Albina Burra.

Alisema Burra, ambaye ni Mkurugenzi katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kurugenzi anayoiongoza wizarani hapo mwaka 2007, 2008 na 2009, imekuwa ikituhumiwa kwa ufisadi katika mgogoro wa ardhi eneo la Luguruni-Kibamba, katika manispaa hiyo. Burra ni Mkurugenzi wa Mipango Miji na Vijiji katika Wizara hiyo.

Kutokana na hali hiyo, alisema ili shaka iondoke, wanataka kamati hiyo ifanye kazi kwa uwazi, ikiwa ni pamoja na kuviruhusu vyombo vya habari na wadau wengine kufuatilia majadiliano ya kamati, Lukuvi aeleze mamlaka na mipaka ya kazi ya kamati, itakamilisha lini kazi yake na ripoti yake iwekwe hadharani.

Aliwataka wananchi popote walipo kujitokeza kutoa ushahidi kwa kamati na kusema watakaohofia usalama wao, wawasiliane na Chadema kwa namba ya simu 0784222222 na barua pepe: kinondoni@chadema.or.tz This e-mail address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it ili wakawawakilishe.

Pia, alimtaka Lukuvi kuielekeza kamati ili katika kufanya kazi yake leo, izingatie kauli ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa hadharani mwaka huu, alipotembelea Manispaa Kinondoni kwamba anawajua kwa majina madiwani waliouza viwanja vya umma na kuwataka waache jambo hilo, la sivyo atawataja.

Alipoulizwa na Nipashe jana, Makamba alisema hapaswi kuhojiwa, bali anastahili kuulizwa ili aeleze ukweli wa mambo kuhusu mambo yote ya Jiji la Dar es Salaam.

Alisema ameongoza Dar es Salaam kwa takriban miaka 10, hivyo anajua mambo mengi yanayohusu sekta mbalimbali, ikiwamo ardhi.

“Anayehojiwa ni mhalifu, mimi sihojiwi. Londa ndiye anayepaswa kuhojiwa kwa sababu ndiye mwenye matatizo. Mimi niulizwe, nieleze ukweli wa mambo.

Mwingine anayestahili kuulizwa ni Kapteni (John) Chiligati (Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi) yeye anahusika na ardhi,” alisema Makamba.

Kwa upande wake, Kandoro alisema uamuzi wa kuhojiwa au la, uko mikononi mwa Kamati ya Lukuvi, hivyo ushauri uliotolewa na Chadema juu yake, haoni kuwa ni tatizo.

“Kwani tatizo liko wapi? Chadema wametoa maoni yao. Sasa wenye kamati wataamua wanihoji ama vipi,” alisema Kandoro.

Jumatano wiki iliyopita, Lukuvi alimfukuza kazi Ofisa Ardhi wa Manispaa hiyo, Magesa Magesa kwa tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi, akidaiwa kuidhinisha ujenzi katika kitalu namba 1274 na 1275 eneo la Msasani, Peninsula kwa Kampuni ya Tanzania Building Works. Tayari Magesa amefikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili.

Mbali na kashfa hiyo, Manispaa ya Konondoni imejiweka pabaya kutokana na vitendo vya ukiukaji wa sheria, taratibu na kanuni za ardhi, na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kinondoni katika ripoti yake ya uchunguzi wa kadhia ya uvunjwaji wa ofisi ya Kata ya Msasani, imetaka uchunguzi ufanywe dhidi ya watendaji wa Manispaa hiyo.

Kamati hiyo ya Ulinzi ilifikia hitimisho hilo baada ya kubaini vitendo vingi vya ukiukaji wa sheria, kanuni na taratibu vilivyofanywa na watendaji wa Manispaa hiyo, kiasi kinachoamsha kuwepo kwa msukumo wa kufumbia macho kanuni za utumishi wa umma.

CHANZO: NIPASHE-26/06/2010

Friday, June 18, 2010

Nilirudisha fomu ya Ubunge Ubungo 6/6

AHADI ZA JK HAZIJATEKELEZWA-MNYIKA

MKURUGENZI wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. John Mnyika jana alirudisha fomu za kuomba kuwania ubunge katika Jimbo la Ubungo na kumshutumua Rais Jakaya Kikwete kuwa ameshindwa kutekeleza ahadi alizotoa kwa Watanzania, likiwamo la kuleta maji Dar es Salaam.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara kabla ya kurejesha fomu hizo, Bw. Mnyika alisema pamoja na ahadi hiyo ya maji kutotekelezwa na Rais Kikwete kuwatupia mzifo Dawasa na Dawasco, pia ameendelea kutoa 'ahadi hewa' zinazoongeza ugumu wa maisha kinyume na alivyoahidi maisha bora kwa kila Mtanzania wakati anaomba kuchaguliwa.



Akihutubia mkutano huo uliojaa mashabiki wake na wasikilizaji wengine katika eneo la Manzese, Bw. Mnyika alisema baada ya kuingia madarakani serikali ya awamu ya nne kumekuwa na kero nyingi kutokana na viongozi wengi kuwa wabinafsi na hivyo kutumia fedha za umma kujilimbikizia mali.

"Tulitegemea serikali kufufua viwanda vilivyokufa ili kuwapatia ajira wamachinga na mamalishe wanaohangaika katika viwanda hivyo, lakini mambo yamekuwa kinyume na matarajio," alisema Bw. Mnyika.

Alisema mabadiliko ya kweli yatapatikana kwa wananchi kupiga kura kuwachagua viongozi wanaopenda maendeleo.

Bw. Mnyika alikosoa kauli aliyoitoa Rais Kikwete wakati wa ziara yake jijini Dar es Salaam hivi karibuni kuwa anawafahamu kwa majina madiwani wanaouza viwanja na kuwaonya, kuwa ina nia ya kuwalinda wezi.

"Kama Kikwete hatachukua hatua dhidi ya madiwani na meya, suala la kuuza viwanja vya wazi na vya umma, litafikishwa kwa wananchi kuamua," alisema Bw. Mnyika

Alisema mfumo wa sasa umekuwa wa wananchi kutumikishwa na viongozi kwa maslahi yao badala ya viongozi kuwatumikia wananchi kama inavyotakiwa.

Mkutano huo ulisindikizwa na maandamano yalioanzia Manzese hadi Ofisi za CHADEMA Jimbo la Ubungo kurudisha fomu.

Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Jamii (CCJ), Bw. Dickson Ng'hily aliyesema demokrasia haiwezi kuwepo kama nchi itaongozwa na chama kimoja kwa muda mrefu.

"Tumeungana na CHADEMA ili kuwatia moyo Watanzania kuwa hatutakiwi kulala mpaka kieleweke, tunatakiwa kupigana imara hadi tupate maisha bora kwa kuchagua viongozi bora," alisema Bw. Ng'hily.

Chanzo: http://majira.co.tz/index.php?option=com_content&view=article&id=426:ahadi-za-jk-hazijatekelezwa-mnyika&catid=1:latest-news&Itemid=18

Picha mbalimbali wakati nikirudisha fomu zinapatikana hapa:

NIPE NIKUPE: http://nipenikupe.blogspot.com/2010/06/john-mnyika-arudisha-fomu-kwa-kishindo.html

NA

WAVUTI: http://www.wavuti.com/4/post/2010/06/john-mnyika-achukua-fomu-za-ubunge-ubungo.html

Thursday, June 3, 2010

Mnyika achukua fomu ya kugombea Ubunge Ubungo

MKURUGENZI wa Mambo ya Nje wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Bw. John Mnyika amechukua rasmi fomu ya kugombea Ubunge katika Jimbo la Ubungo.

Akichukua fomu hiyo Dar es Salaam jana, Bw. Mnyika aliwataka wananchi kuwapuuza wanasiasa walioshindwa kuongoza nchi na kuitumbukiza kwenye mfumuko wa bei na kuzorotesha maendeleo ya jamii na kuwaachia mafisadi kufuja fedha za umma.

Bw. Mnyika alisema ameamua kuchukua fomu ya CHADEMA kwa kuwa ni chama mbadala na tumaini jipya la Watanzania chini ya falsafa yake ya Nguvu ya Umma.

"Leo nimekuja kuchukua fomu sitatoa hotuba, nitazungumza kwa kirefu siku nitakaporudisha fomu, leo natoa tu rai kwa wananchi wa ubungo na Tanzania kwa ujumla kuwapuuza wanasiasa walioshindwa kuongoza nchi na kuitumbukiza katika mfumuko wa bei na kuzorotesha huduma za jamii huku mafisadi wakiendelea kufuja fedha ya umma," alisema Bw. Mnyika.

Aidha aliwataka wananachi kupuuza kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu takrima akidai kuwa ni za kubariki rushwa kwa kisingizio cha takrima.

Bw. Mnyika alisema kauli ya Rais Kikwete ya kuwa wagombea wanaweza kutoa pombe kwa wananchi, kauli ambayo imetafsiriwa kuwa ni kuchochea rushwa kwenye uchaguzi na suala ambalo rais asipolikanusha, itathibitisha kuwa hakuwa na dhamira ya kweli ya kudhibiti matumizi makubwa ya fedha kwenye uchaguzi.

Aidha alisema kauli hiyo isipokanushwa itakuwa ni ishara ya kutoheshimu utawala wa sheria.

Aliongeza kuwa nia yake nyingine ya kuchukua fomu ya kuwania ubunge katika jimbo hilo ili kupata fursa ya kushiriki kikamilifu katika kuliletea mabadiliko ya kweli jimbo hilo pamoja na Tanzania kwa ujumla kupitia siasa safi na uongozi wenye utawala bora.

Mwanasiasa huyo amewataka Watanzania wengine kujitokeza kugombea kwenye jimbo hilo katika nafasi za udiwani ili Manispaa ya Kinondoni iendeshwe na vyama mbalimbali tofauti ilivyo sasa ambapo Dar es Salaam inaongozwa na CCM.

Bw. Mnyika alichukua fomu hiyo katika Ofisi za CHADEMA Jimbo la Ubungo kutoka kwa Katibu wa Jimbo hilo, Bw. Nasor Balozi.

Chanzo: Majira 17 Mei 2010-http://majira.co.tz/index.php?option=com_content&view=article&id=199:mnyika-achukua-fomu-kugombea-ubungo&catid=1:latest-news&Itemid=18