Wednesday, February 25, 2015

CHADEMA: YANAYOJIRI NJOMBE - BVR



1. Ikiwa zoezi la uandikishaji limeanza leo tarehe 23 Feb na likitarajiwa kuzinduliwa rasmi kesho tarehe 24 Feb na Waziri Mkuu Pinda, Naibu Katibu wa CHADEMA upande wa Tanganyika ameanza Operesheni R2R BVR ambapo asubuhi mpaka mchana alikuwa katika Mji wa Makambako akipitia mitaani pamoja na msafara wa viongozi wa chama hicho ngazi mbalimbali kuhamasisha wananchi kujiandikisha.

Aidha, Operesheni hiyo imehusisha kukagua utaratibu wa uboreshaji kwa kutumia BVR kwenye vituo mbalimbali ambapo imebainika kwamba udhaifu uliokuwepo wakati wa majaribio na mwingine mpya umebainika katika sehemu kubwa ya vituo vilivyotembelewa.

Baada ya kubaini udhaifu huo Mnyika na timu ya maafisa wa CHADEMA iliyoweka kambi katika mkoa wa Njombe ikihusisha wataalamu wa TEHAMA (ICT) wamekutana na Mkurugenzi wa NEC Mallaba na kueleza kuhusu udhaifu huo.

Mfano katika kituo cha Malombwe mpaka saa 6 mchana mashine zilikuwa hazifanyi kazi. Hali kama hiyo imejitokeza katika kituo kituo cha Liamkena ambapo uandikishaji ni taratibu kwa kiwango mpaka saa 4 waliandikishwa watu watano tu.

2. Aidha, pamekuwepo na tatizo la watu wenye mikono yenye vidole sugu kutokana na kufanya kazi ngumu mashine kugoma kuwatambua na hivyo kukataliwa kujiandikisha.

Hali kama hiyo imejitokeza mfano katika kituo cha Sigfrid, Malombwe na vituo mbalimbali. Kufuatia hali hiyo ambapo Operesheni R2R BVR iliamua kutembelea vituo zaidi na kubaini kwamba vipo ambapo mashine hazikuwa zikifanya kazi kabisa mathalani Lumumba.

Kwa ujumla katika vituo vingi ukiondoa matatizo ya mashine upo pia udhaifu wa waandikishaji na waendeshaji wa vifaa vya BVR (Kit Operators) ambao wanashindwa kutumia mashine hizo na walipohojiwa baadhi walikiri kwamba wamepewa mafunzo siku moja kabla ya kuanza uandikishaji huku wakiwa hawajawahi kutumia kompyuta wala kuwa na ujuzi wa ICT.

Wapo waandikishaji ambao walionyesha kutokuwa na ufahamu wa upigaji picha na hivyo kufanya zoezi kwenda taratibu na pia kupiga picha zinazoonekana vibaya.

Kasi ndogo ya uandikishaji huku siku zikiwa saba na kwa kituo inaashiria bayana kwamba wapo wananchi ambapo mwishowe watakosa fursa ya kujiandikisha.

Operesheni R2R BVR imebaini mpaka sasa kuwa pamoja na kutumia alama za vidole mfumo umeacha mianya mpiga kura kujiandikisha zaidi ya mara moja katika vituo tofauti tofauti kwa kuwa hakuna mawasiliano ya kimfumo kati ya kituo kimoja na kingine.

Mfumo unategemea kwamba taarifa zikitumwa kanzidata kuu (central databank) ya tume ndiyo itakayochambua wakati ambapo hakutakuwa na mawakala katika hatua hiyo kuthibitisha uondoaji wa wapiga kura waliojiandikisha zaidi ya mara moja kwa kuzingatia kwamba katika kipindi cha uhakiki wa daftari la awali napo hakuna mwingiliano baina ya daftari la eneo kwa eneo wakati wa ukaguzi.

Aidha, CHADEMA imeweka mawakala katika vituo vyote lakini wanapata vikwazo vya namna vya kudhibiti uchakachuaji katika hatua ya usafirishaji wa takwimu ambapo mifumo miwili inatumika kwa wakati mmoja; wa kutumia simu na ule wa kuhamisha kwa kutumia kifaa cha kuhifadhi taarifa (flash drive) bila uhakiki wa mawakala.

Operesheni R2R BVR katika mazingira hayo haitaishia tu kuwa na mawakala kwenye vituo bali kukagua mfumo mzima.

4. Naibu Katibu Mkuu Mnyika ametaka Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika uzinduzi wa BVR Makambako tarehe 24 Feb aeleze namna Serikali ilivyoiwezesha tume kushughulikia udhaifu huo kwa kuzingatia kwamba mabilioni yametumika kwenye zabuni ambayo imeleta vifaa vibofu hali inahitaji uchunguzi kufanyika kubaini iwapo hali hiyo imetokana na ufisadi au imefanywa makusudi kuachia mianya ya uchakachuaji katika uchaguzi.

Mara baada ufuatiliaji huo jioni ya leo patafanyika Mkutano wa uzinduzi wa Operesheni R2R BVR jukwaani katika Jimbo la Njombe Kusini na kesho kutwa tarehe 25 Operesheni R2R inahamia wilaya ya Wang'ing'ombe kwenda kuhamasisha wananchi kujiandaa kujiandikisha.
Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano -CHADEMA

Monday, February 23, 2015

Rai Maalumu kwa Zoezi la Uandikishaji ktk Daftari la Kudumu kwa mfumo wa BVR

Nimeingia katika Mkoa wa Njombe kwa ajili ya uzinduzi wa R2R BVR (Region by Region Biometricn Voter Registration) kwa Mkoa huu (Njombe) leo Jumatatu 23 Februari, 2015 utakaofanyika Njombe Mjini.

Baada ya uamuzi wa NEC kwamba uandikishaji unaanza Halmashauri ya Mji Mdogo wa Makambako pekee, nimeanzia katika mji huo na kubaini kwamba bado kuna udhaifu katika maandalizi ya BVR hata katika eneo hilo dogo tofauti na kauli ya uongo ya Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Rehema Nchini kwamba maandalizi yote yako kamili ikiwemo ushiriki wa wadau. 

Itakumbukwa wakati Mwenyekiti wa NEC, Jaji Lubuva alipotangaza kusogeza mbele uandikishaji toka 16 Februari, 2015 mpaka 23 Februari, 2015 alisema lengo ni kuvipa vyama nafasi ya kujiandaa na kuweka mawakala. Lakini mpaka sasa vyama havijapewa orodha ya vituo kwa ajili ya kuweka mawakala na kuna utata kuhusu idadi halisi ya vituo hata kwa upande wa eneo dogo la Makambako. 

Halmashauri imeitisha kikao kwa niaba ya NEC ikasema vituo ni 44 bila kutoa orodha wala kuelekeza viko wapi, baadae ghafla wamebadili na kusema ni 87 lakini hata hivyo hawajatoa orodha mpaka sasa

Friday, February 20, 2015

Mnyika: Kauli ya Chenge ni kiburi cha kifisadi.

Mhe. Andrew Chenge (MB)

Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, amemkosoa Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), kwa kujiita ‘nyoka wa makengeza’ kwa madai kwamba, anastahili kuitwa ‘nyoka wa ufisadi’.

Mnyika katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, alisema wananchi wanapaswa kumuita Chenge ‘nyoka wa ufisadi’ badala ya kujisifia kuwa ni ‘nyoka mwenye makengeza’ kwa kuwa amehusika katika kutafuna mali ya umma.

“Kauli ya Chenge kama ilivyokuwa kwa ile ya ‘vijisenti’, ni kiburi cha kifisadi,” alisema Mnyika.