Saturday, April 25, 2009

Siri Zifichuliwe Tubadili Katiba Tulinde Muungano


Siri Zifichuliwe Tubadili Katiba Tulinde Muungano

Na John Mnyika

Wakati serikali ikiwa imeandaa maadhimisho ya miaka 45 ya Muungano katika uwanja wa Taifa, vijana kwa upande wao kupitia Chama cha Wanafunzi wa Siasa(DUPSA), kwa kushikirikiana na Asasi ya Dira ya Vijana(TYVA) na Mtandao wa Wanafunzi Tanzania(TSNP), wao waliandaa mjadala wa umma kuadhimisha siku hiyo katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam.

Binafsi nilipata mwaliko wa kuwa mmoja wa wageni wazungumzaji katika mjadala huo, lakini kutokana na msiba wa karibu; sikuweza kujumuika katika maadhimisho hayo. Makala hii inajumuisha ujumbe wangu wa mshikamano hususani kwa vijana na watanzania kwa ujumla katika kuadhimisha siku hii ya kihistoria kwa taifa letu.

Ni suala lililozuri kuadhimisha Muungano wetu kwa gwaride lenye maonyesho ya silaha lakini ni suala lililozuri zaidi kwa kuudhamisha kwa mjadala wa kuibua siri na sera zenye kutuwezesha kutafakari tulipotoka, tulipo na tunapopaswa kwenda.

Katika kipindi hiki cha miaka 45, yapo baadhi ya mafanikio ambayo kama watanzania tunaweza kujivunia kutokana na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kuunda Taifa la Tanzania uliotangazwa tarehe 26 Aprili 1964. Muungano umeendelea kuwa nyenzo na kitambulisho cha umoja wetu kimataifa, hivyo tumeendelea kuwa na kitu cha kuendelea kujivuna nacho kama watanzania wazalendo.

Muungano umefungua uwanda zaidi wa mwingiliano baina ya Wazanzibar na Watanzania bara umeendeleza mahusiano yaliyoanza kuwepo hata kabla ya ukoloni. Sasa ni jambo la kawaida wananchi wa pande hizi mbili kuhamia katika maeneo mbalimbali ya Muungano. Baadhi ya watanzania ni alama halisi ya Muungano huu wa kifamilia ambao kwa kuwa pengine umeungana kwa damu(kwa watu kuolewa na kuoleana) ni ngumu kutenganishika. Ni wazi kwa vitisho vya miaka hiyo ya sitini, na heka heka za vita baridi iliyokuwa ikiendelea; Muungano uliweka misingi muhimu ya amani-kiulinzi na kiusalama katika eneo la Bahari Hindi kwa upande wa Tanzania.

Hata hivyo, yapo mapungufu katika muungano ambayo mengine yamekwamisha baadhi ya jitihada za kimaendeleo na baadhi yametishia umoja, mshikamano na hata uhai wa muungano wenyewe. Masuala haya yote, yanazua utete wa kisiasa, kiuchumi, kijamii na hata wa kiusalama.

Wakati Muungano wenyewe unaanzishwa hapakuwa na ushirikishwaji mpana wa wananchi kuamua ni aina gani ya Muungano ambayo walitaka kuwa nayo. Hii ni kinyume na sheria za kimataifa na haki za binadamu kwani vyote vinataka wananchi washirikishwe kabla ya kufikia makubaliano ya Muungano. Palikuwa na pupa isiyo ya lazima, mkataba wa Muungano uliridhiwa na bunge 25 Aprili,1964 na Mwl. Nyerere akautia saini siku hiyo hiyo kuwa sheria.

Mijadala ya muungano ilifanyika kwa siri kwani kwa mujibu wa nyaraka mbalimbali ikiwemo simulizi za waliokuwa kwenye korido za mamlaka kwa wakati huo, si wananchi wala waofisa wa serikali walikokuwa wanajua kinachoendelea. Ukiondoa Nyerere na Karume watu wengine wanaolezwa kuwa walikuwa wakifahamu kinachoendelea kwa wakati huo ni pamoja na Rashidi Kawawa, Oscar Kambona, Job Lusinde, Abdallah Kassim Hanga, Abdul-Aziz Ali Twala na Salim Rashidi. Wakati majadiliano yakiwa katika hatua ya mbele, Nyerere inaelezwa kuwa alimuita mwanasheria wake mkuu wa wakati huo, Mwingereza Roland Brown na kumwelekeza aandike rasimu ya hati ya makubaliano ya Muungano bila yoyote kujua. Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar wa wakati huo, Wolf Dourado anaelezwa kuwa alipewa likizo ya wiki moja; badala yake akaja Mwanasheria wa Kiganda, Dan Nabudere kumshauri Karume kuhusu rasimu iliyowasilishwa na Tanganyika.

Jambo kuu la kulitafakari ni dhamira ya kuundwa kwa muungano wenyewe na kuhusisha na dhamira za sasa za kuendeleza muungano wetu. Hili ni suala la msingi katika kuamua mwelekeo wa Muungano wetu ikiwemo utatuzi wa kero zilizopo. Hata hivyo, kumekuwa na utata kuhusu sababu hasa zilizosukuma kuanzishwa kwa muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar. Upo mjadala mkubwa, kama Muungano huu ulianzishwa kwa dhamira za ndani ama msukumo kutoka nje. Wakati wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kuangalia mtiririko wa matukio, ni dhahiri kwamba palikuwa na nia ya ndani ikibeba hisia za Mwalimu Nyerere na wenzake kuhusu haja ya umajununi wa kiafrika(pan Africanism) lakini pia ikisumwa na nguvu za nje wakati huo Zanzibar ikiwa kitovu cha Vita baridi kati ya mataifa ya magharibi na yale ya mashariki. Mjadala huu ni muhimu pia kwa sasa wakati kizazi kipya cha Watanzania kinafikiria kutaka mabadiliko katika mfumo na muundo wa Muungano, kwa kuwa ni vyema kutafakari kama matakwa haya ya sasa nayo ni dhimira ya ndani au ni msukumo tena kutoka nje.

Pamoja na kuanguka kwa dola ya Urusi, hali ambayo wadadisi wa mambo wameiona kwamba ni ashirio la kuisha kwa vita baridi; siasa za kimataifa bado zimebaki na sura ile ile ya heka heka za kibeberu. Ukoloni mamboleo wenye kujifunika katika kivuli cha utandawazi na diplomasia ya kiuchumi unaendelea kupanua mirija yake kupitia njia mbalimbali. Kuibuka kwa mihimili mingine yenye nguvu sambamba na Marekani kama China na heka heka za mataifa ya mashariki kama Irani na nchi nyingine za Uarabuni kwa pamoja yameamsha tena pilika pilika katika eneo la Bahari ya Hindi. Mikikimikiki hiyo ikijidhirisha katika kutafuta rasilimali hususani mafuta, uvuvi, utalii nk kwa kivuli cha barokoa ya uwekezaji kutoka nje. Ikienda sambamba na pilikapilika za kiulinzi na kiusalama zinazofichwa kwa shela ya vita dhidi ya ugaidi na kuhakikisha amani duniani. Huku pakiwa na hekaheka za mivutano ya kiutadamuni baina ya ustaarabu wa magharibi na ule wa mashariki. Hapo ndipo kisiwa cha Zanzibar, kinapokuwa na umuhimu wa pekee kwa Muungano wa Tanzania huku kikikodolewa macho na jamii ya kimataifa.


Kwa upande mwingine dalili za matatizo ya Muungano ziko bayana mathalani malalamiko katika pande zote mbili na dhoruba za vipindi za kisiasa kwa mfano kulazimishwa kwa Alhaj Aboud Jumbe Mwinyi kujiuzulu(Mjadala wa 83/84),sakata la wabunge 55 wa Muungano(90/92) na katika kipindi cha karibuni kujitokeza tena kwa mijadala ya Zanzibar kujiunga na OIC; mjadala wa Zanzibar ni nchi ama si si nchi; mjadala wa mafuta nk. Yote haya ni sehemu ya ishara ya nyufa zilizoko. Kwa vyovyote vile hali hii si nzuri kwa mustakabali wa Taifa.

Ibara ya 6(a) ya hati/mkataba wa Muungano inataja serekali ya Tanganyika. Hata kifungu cha 8 cha sheria ya Muungano namba 22 ya mwaka 1964. Lakini ukiangalia katika hali halisi ya kiutendaji, serikali ya Tanganyika haionekani popote kama ilivyo kwa serikali ya Zanzibar. Hapa ndipo panapoibua hoja nyingi zinazozua mgogoro kuhusu Muungano kama imbavyo ilitokea kwa Jumbe mwaka 1984 na hatimaye kushinikizwa na NEC ya chama kujiuzulu.

Kwa ujumla, masuala ya Muungano yamegubikwa na usiri. Mathalani nakala halisi ya Muungano ambayo ndio inapaswa kuwa mwongozo/msingi imekuwa kitendawili. Huko nyuma iliwahi kusemwa bungeni kuwa nakala hiyo ipo. Lakini miaka ya karibuni serekali imesema nakala hiyo haijulikani ilipo.

Kwa upande mwingine, katiba na sheria zetu zinakataza wananchi kuvunja Muungano, hii ikitafakariwa kwa kina inamaanisha hata kubadili mfumo wa muungano ulioko nk. Mathalani katiba inawataka viongozi wa kitaifa kula kiapo cha kuulinda Muungano kabla ya kuanza kazi yao aidha sheria ya vyama vya siasa inakiondolea sifa ya kusajiliwa chama chochote cha siasa ambacho katiba yake au sera zake ni za kutaka kuvunja Muungano.

Katika hali hii, ili kulinda muungano ni lazima hatua za haraka zikuchuliwe na umma kuhakikisha siri za muungano zinafichuliwa na katiba inabadilishwa ili kulinda Muungano. Ukichambua kwa kina utaona mapungufu mengi ya muungano yanatokana na matatizo ya kimaumbile ya toka wakati wa kuundwa kwa muungano. Hivyo suluhisho la kudumu ni kuusuka upya muungano kupitia katiba mpya. Hii iende sanjari na kuweka misingi madhubuti, wa wazi na wenye kutoa majibu. Katika hili ni ukweli ulio wazi kuwa hoja inayopigiwa upatu zaidi ni ya serekali kuwa na serikali ya shirikisho(ufiderali). Suala hili ni moja ya hoja muhimu za Sera ya CHADEMA ya Mfumo Mpya wa Utawala maarufu zaidi kama sera ya majimbo. Ripoti ya Tume ya Nyalali, imechambua vizuri hoja hii. Hata hivyo, upinzani huu ya hoja hii umejikita katika hofu juu ya kuvunjika kwa Muungano wakati wa mchakato wa katiba mpya ama kura(referundum) hivyo wanajenga hoja kwamba Muungano unaweza kudumishwa katika muundo huu huu kwa kuchota uzoefu wa nchi za Skandnavia kama Finland na Denmark ambapo visiwa vyake kama Faroe, Aaaland na Greenland vinayo mamlaka yake katika maeneo mbalimbali ndani ys serikalia ambazo si za shirikisho(kifiderali). Ama mfano wa Uingereza na Ireland ya Kaskazini. Lakini uzoefu wa kimataifa unaonyesha kwamba kuunda serikali ya shirikisho si kuvunja Muungano, ni kutengeneza muungano wenye kuweza kuridhiwa na kudumu zaidi.

Kwa upande mwingine, liko ombwe kiuongozi na kitaasisi/kimifumo Zanzibar ambalo kwa ujumla wake linaelezwa kuzaa kile kinachoitwa mpasuko wa kisiasa. Sababu ya haraka inayotolewa ni kutokuwa na chaguzi huru na za haki ambazo huzaa migogoro na mivutano mara baada ya chaguzi. Suluhisho la muda mrefu linaloelezwa ni kuweka mazingira ya haki katika chaguzi na ushindani wa kisiasa, na daraja kuelekea hali hiyo inaelezwa kwamba ni kuunda serikali ya mseto chini ya kile kinachoelezwa kuwa ni ‘muafaka’. Hii inaelezwa kuwa ni muhimu katika kutibu majeraha ya kihistoria. Hata hivyo, ukifanya uchambuzi wa ndani hali inaonyesha kwamba marekebisho hayo pekee hayawezi kuweka misingi ya kuziba ombwe la kiuongozi/kimfumo katika sehemu ya Muungano yenye katiba na sheria ya Zanzibar. Ni katika hali hiyo, ndipo unaposikia vilio vya ubaguzi katika Zanzibar yenyewe; ambazo kwa kiasi zimeibua hata hoja ya Pemba kutaka iachiwe ijitawale ndani ya Muungano. Wakati huo huo, mfumo wa sasa wa Muungano hauruhusu kwa uwazi pande mbili za Muungano kutawaliwa na vyama tofauti. Kwa kuwa nchi ipo katika mfumo wa vyama vingi upo uwezekano wa vyama tofauti kushinda katika pande mbili. Hili likitokea patakuwa na matatizo ya kiutawala.

Changamoto hizi haziwezi kukabiliwa na uchaguzi huru pekee, wala kuundwa kwa serikali ya mseto au ya umoja wa kitaifa. Haya ni mambo yanayohitaji mabadiliko katika mfumo wa utawala kama nilivyodokeza hapo juu. Ambayo pia yatahusisha mageuzi katika utamaduni wa kisiasa na mahusiano ya kijamii. Lakini yanapaswa kuhusisha pia marekebisho katika mfumo wetu wa uchaguzi na uwakilishi. Kwa sasa, Tanzania kwa ujumla inatumia mfumo wa uchaguzi wa ‘wengi wape’ ama ‘mshindi anachukua vyote’. Matokeo ya mfumo huu ni kuwa pamoja na vyama vya CUF na CCM kuwa na ushindani katika pande mbili za visiwa hivyo, kila kimoja kinauwakilishi wa upande wake pekee kutokana na ushindi. CUF inaongoza kisiwa cha Pemba, na ina jimbo moja tu la Mji Mkongwe kwa upande wa Unguja. Na CCM inaongoza unguja na haina jimbo hata moja huko Pemba.

Hii ni kwa sababu, chini ya mfumo wa sasa, hata kama wagombea wote wa chama X Unguja wakipata wastani wa kura wa asilimia 45, wa chama Y wakapata asilimia 7 na chama Z asilimia 48; basi wabunge wote na wawakilishi wa upande wa Unguja watatoka chama Z pekee. Chama X na Y havitaambulia chochote pamoja na kuwa na wananchi takribani asilimia 52 wanaounga mkono vyama hivyo. Mfumo huu wa uchaguzi unaendeleza ufa na matabaka katika visiwa hivyo. Ndio maana Mwalimu Nyerere alifikia hatua ya kubashiri kwamba nje ya Muungano, hakuna Zanzibar alipofananisha dhambi ya ubaguzi na kula nyama ya mtu.

Hata hivyo, kama kukiwa na mfumo wa uchaguzi wa mchanganyiko au mchanyato wenye uwakilishi wa uwiano; maana yake ni kwamba kura ambazo CUF itapata Unguja hata zinaweza kutafsiriwa kuwa viti vya ubunge na uwakilishi na kufanya chama hicho kiwe na wawakilishi na wabunge wa wengi toka Unguja. Kadhalika, kura ambazo CCM kwa kawaida huwa inaokoteza kwa upande wa Zanzibar, zinaweza kabisa kujumlishwa na kupata wabunge na wawakilishi wa upande Pemba na hivyo kupunguza mpasuko wa kisiasa. Kwa hiyo suala si kuwa na uchaguzi huru na haki pekee bali kuwa pia na mfumo wa uchaguzi ambapo kila kura itakuwa na thamani na kuwakilisha kikamilifu nguvu ya umma katika utawala na uongozi baada ya uchaguzi.

Kadhalika kama sehemu ya kushughulikia mtanziko wa kisiasa kwa upande wa Zanzibar nakubaliana na tafakuri ya Hayati Profesa Abrahaman Babu kuhusu haja ya vyama mbadala vya kisiasa Zanzibar na pengine kuwa chama mbadala cha tatu(third party alternative) katika siasa za Zanzibar. Hii ni kwa sababu siasa za Zanzibar zinachochea na mgawanyiko unaotokana na vyama viwili vya CUF na CCM. Hii inaelezwa pia na ripoti za waangalizi mbalimbali wa uchaguzi mathalani NORDEM. Inatajwa bayana kuwa ingawa Mwafaka umechangia kuleta mapatano ya muda mfupi, mwafaka huohuo kwa kujikita kwa vyama viwili pekee umeendelea kujenga ufa baina ya pande mbili. Kwa vyovyote vile nguvu ya tatu inahitajika katika siasa za visiwani. Hii ni kwa sababu siasa za Zanzibar na Muungano ni kama kuku na yai.

Pamoja na udhaifu wa katiba za sasa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile Zanzibar bado kuna mambo yangeweza kabisa kushughulikiwa. Mathalani, Utaratibu wa kuingiza mambo katika orodha ya Muungano uwe wazi na msingi wake uwe ni pande zote mbili kuridhia wakati wote. Pamoja na kuwa suala hili limewekewa misingi katika hati ya muungano na katiba, bado utekelezaji wake unaacha maswali. Hii itandoa mgogoro mathalani unafukuta hivi sasa ambapo Zanzibar inahoji ni vipi mafuta yaliingizwa katika orodha ya Muungano na dhahabu almasi kuachwa kuwa si masuala ya Muungano.

Binafsi, nimeiona hati inayosemwa kuwa ni hati ya muungano. Serikali haijawahi kuyakana maudhui ya hati hiyo, ingawa inasema si hati halisi ya Muungano. Wakati umefika wa kuunganisha nguvu ya umma ili kuitaka Serikali iweke wazi nakala halisi ya mkataba wa Muungano. Siri ya Muungano inapaswa kuwa ya watanzania wote sio kikundi cha watawala wachache. Serikali itekeleze kikamilifu hati ya Muungano ikiwemo kuanzisha mahakama ya Muungano ya Katiba.

Pazia kubwa zaidi la usiri katika masuala ya Muungano lifunuliwe. Maamuzi ya kuhusu Muungano yalifanywa na wazee wetu, kwa kuzingatia mazingira ya wakati wao. Mataifa ya nje wanao utaratibu kati nchi zao wa kuweka wazi kwa umma, baada ya miaka fulani nyaraka ambazo zilikuwa zinahesabika kama ni siri kuu ya serikali(Top classified secret). Mathalani, tayari Marekani imeshaweka hadharani nyaraka za siri za taifa lao ikiwemo kuhusiana na ushiriki wao katika suala la Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar. Nyaraka hizo za wazi zinajumuisha ripoti, faksi na mazungumzo mengine ambayo yalifanyika wakati huo ikiwemo mambo ambayo yamefanywa na Shirika la Ujasusi la Marekani(CIA). Nimepitia na kutafakari kwa kina baadhi ya nyaraka hizo ambazo wamezitoa. Si lengo la makala haya kueleza kwa undani ambayo yametolewa hadharani, ila inatosha tu kusema kwamba Serikali ya Marekani imekiri wazi wazi kumshinikiza Mwalimu Nyerere na serikali yake ya wakati huo kutaka Tanganyika ijiunge na Zanzibar.

Kati ya mawasiliano yalitolewa hadharani kuonyesha hali hiyo ni pamoja na ya Frank Carlucci, balozi wa Marekani nchini Zanzibar katika kipindi cha Muungano. Huyu baadaye alikuja kufukuzwa Zanzibar kutokana na shughuli za CIA katika visiwa hivyo, na baadaye alipanda cheo na kuwa mkurugenzi wa shirika hilo la kijasusi na hatimaye baadaye kwa Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo. Kwa kiasi kikubwa, Marekani ilihofia wakati huo wa vita vya baridi kukua kwa ukomonisti katika eneo la Afrika ya Mashariki kutokana na msimamo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya wakati huo. Kwa ujumla, Zanzibar ilionekana kama Cuba ya Afrika Mashariki, wakati Cuba ikilisumbua taifa hilo upande wa Amerika ya Kusini.

Wakati umefika sasa na Tanzania kuweka wazi nyaraka zote za siri kwa upande wake, miaka 45 ya Muungano. Hususani nyaraka za takribani miaka 25 iliyopita za kati ya mwaka 1960 mpaka mwaka 1980 wakati wengine tulipozaliwa. Kuwekwa wazi(declassification) kwa baadhi ya siri hizi, ikiwemo zile zilizomo katika himaya ya Idara ya Usalama wa Taifa ni muhimu kwa mabadiliko katika nchi yetu. Ni lazima kizazi cha sasa cha watanzania kiwezeshwe kuyaelewa mazingira ya wakati huo na ya sasa; na kufanya maamuzi sahihi kuhusu mwelekeo wa Taifa.

Nihitimishe salamu zangu za mshikamano kwa kutoa masuala na maswali ya kuchokoza mjadala. Mjadala kuhusu Muungano si suala la kufanywa katika Siku ya Maadhimisho pekee, ni hitaji endelevu mpaka pale tutakapokuwa na mfumo wa kiutawala unaokidhi kwa kiwango cha kutosha matakwa ya umma. Tujiulieze: Washiriki wa Muungano ni kina nani? Wako wapi? Wanawakilishwa vipi? Wanamamlaka gani? Tuhoji: Mambo ya muungano ni yapi? Kwa nini? mipaka ya upatikanaji wake ni ipi?yanaheshimiwa? Tudadisi: Mzanzibar ni nani?Mtanzania bara ni nani? Nini athari za sifa zao kwa mahusiano na madaraka? Tutafakari: Tanzania ni nchi ya chumi ngapi? Hili linaathari gani kwa Muungano? Mwalimu Nyerere, katika Kitabu chake cha Uongozi wetu na Hatma ya Tanzania, pamoja na kutetea muundo wa sasa wa Muungano anakiri kwamba umma wa watanzania unayo kabisa ridhaa ya kuufanyia mabadiliko muungano. Tofauti yake na wabunge wa CCM wa wakati huo ilikuwa ni katika mchakato tu wa kutimiza azma hiyo. Wakati huo, alieleza wazi kwamba kile walichokuwa wakikisimamia hakikuwemo katika ilani ya wakati huo waliochaguliwa nayo. Akawataka kama wanataka mabadiliko katika Muungano basi wajiuzulu, na nchi iende katika uchaguzi. Wananchi wakichagua mabadiliko hayo, basi hiyo ndio itakuwa msingi wa kuusuka upya muundo wa Muungano. Hivyo, mabadiliko katika muungano wetu yanawezekana, na sehemu muhimu ya kuanzia ni kupitia uchaguzi. Kwa mantiki hiyo basi, siri zifichuliwe, tuchague viongozi bora, tubadili katiba ili tulinde Muungano wetu. Umoja ni Nguvu, utengano ni udhaifu.

John Mnyika ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje(CHADEMA) anapatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.net na http://mnyika.blogspot.com




Thursday, April 16, 2009

Sakata la DECI:Serikali iwajibike kuheshimu utawala wa sheria na kulinda haki za binadamu

Sakata la DECI:

Serikali iwajibike kuheshimu utawala sheria na kulinda haki za binadamu

Nimekuwa nikifuatilia kwa karibu suala la DECI, nikiwa mmoja wa watu waliokuwa na matarajio kwamba pande zote zinazohusika zitachukua hatua stahili kwa mujibu wa sheria na kwa kuzingatia pia haki za binadamu. Hata hivyo, mtiririko wa suala lenyewe unatia mashaka kadiri siku zinavyokwenda. Sakata la DECI linazidi kuchukua sura mpya, hali inayotoa ishara mbaya kiuchumi, kisiasa na kijamii kwa washiriki na washirika wa sakata hilo na watanzania kwa ujumla.

Izingatiwe kuwa baada ya wananchi kulipa kodi, wajibu mmojawapo mkubwa wa kikatiba na kisheria wa serikali ni kuhakikisha kodi hizo pamoja na mambo mengine zinatumika kwa ajili ya ulinzi na usalama wa maisha na mali za raia. Katika kutimiza wajibu huo, wananchi wanatarajia kuwa serikali itaweza kuongoza kwa kuona mbali, na kwa kutimia vyombo vyake kuwalinda raia ikiwemo kuwaelimisha mapema juu ya masuala ambayo yanaweza kuwaathiri wao na mali zao na kukabiliana uvunjifu wa sheria.

Nimefadhaishwa na kauli ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye pamoja na kueleza wazi wazi kuwa DECI imekuwa ikifanya biashara haramu ya upatu wa mfumo wa piramidi(pyramid scheme) bila hata ya kuwa na leseni kwa kazi hiyo ambayo ni kinyume cha sheria. Bado Waziri Mkuu, ameendelea kuruhusu biashara hiyo kuendelea wakati serikali inafanya uchunguzi, huku wakati huo huo akiwataka wananchi kuacha kuendelea ‘kupanda’ fedha zao katika kampuni hiyo. Huu ni undumilakuwili na ugeugeu katika uongozi na usimamizi wa utawala wa sheria na haki za binadamu.

Kigugumizi hiki cha serikali katika kuchukua hatua, kinatokana na uzembe ambao serikali ya CCM imeufanya tangu awali ambao umesababisha kampuni hiyo kufanya kazi kwa miaka zaidi ya miwili huku ikilindwa na vyombo vya dola na ikitoa kodi kwa serikali. Idara ya Usalama wa Taifa, inapaswa kulieleza taifa ilikuwa wapi wakati wote biashara hii ilipoanza na kumea. Kitengo cha Ushushushu(Intelejensia) wa Kifedha na Kiuchumi, kinapaswa pia kuwajibika kutokana na kadhia hii.

Nachukua fursa hii kuitahadharisha serikali kwamba uzoefu wa kimataifa katika nchi mbalimbali ambazo biashara hii ya upatu imefanyika, umeonyesha kwamba mara zote miradi ya namna hiyo imeshindwa kuwa endelevu baada ya muda na kufikia kiwango cha juu cha mtaji na wateja huvunjika na kuacha washiriki wengi wakiwa na hasara. Hasara hizo huchukua sura ya kiuchumi, kisiasa na hata kijamii. Nchini Albania , biashara ya upatu wa piramidi ilipovunjika ilisababisha machafuko katika nchi ambayo yalichangia kwa namna moja au nyingine katika kuondolewa kwa serikali iliyokuwa madarakani katika nchi hiyo. Nchini Kenya, vurugu zilizotokea baada ya kuvunjika kwa biashara kama hiyo zilisababisha vurugu ikiwemo baadhi ya washirika kutupwa kutoka ghorafani. Nchini Ireland (2006) biashara kama hiyo imeelezwa kuleta madhara. Nchini Colombia (2008) machafuko yalitokea katika manispaa za Pasto, Tumaco, Popayan na Santander de Quilichao. Serikali ya nchi hiyo ilibidi kutangaza hali ya hatari ya kiuchumi na kukukamata mali za washirika kwa ajili ya kuwakoa washiriki.

Pamoja na uchunguzi unaoendelea, kwa kuwa serikali imeshakiri kwamba kuna ukiukwaji wa sheria mpaka sasa; serikali inapaswa kuchukua hatua za haraka kulinda mali za wananchi. Kwa kuwa tayari serikali imeshatoa matangazo ya kuwaonya wananchi kuendelea ‘kupanda fedha’ chini ya mfumo huo wa piramidi, kupungua kwa wananchi ‘wanaopanda fedha’ kwa sasa, kutafanya DECI ishindwe kuwalipa ambao walipanda awali, katika mazingira hayo DECI inaweza kufunga yenyewe ofisi zake kabla ya kufungiwa. Uamuzi wa kufunga ofisi kabla ya serikali kuingilia kati utaibua tafrani miongoni mwa washiriki waliojisajili na kupanda fedha zao mpaka sasa; hali ambayo inaweza kuibua matatizo ya kiuchumi yenye athari pia za kisiasa na kijamii. Katika mazingira hayo, serikali inawajibu wa kusimamia sheria wakati huo huo kusimamia haki za binadamu, raia wa Tanzania ambao ni washiriki katika piramidi hilo. Kwa kuwa serikali imezembea na kuachia wananchi(iwe kwa uzembe ama kwa kutokujua) kujiingiza katika hatari hiyo, serikali ina wajibu wa haraka wa kuwaokoa wananchi hao kutoka athari hizo za kiuchumi na kulinda maisha yao.

Aidha wakati suala hili likiendelea kushughulikiwa tunatoa mwito kwa viongozi wa dini kukaa na baadhi ya viongozi wenzao wa dini ambao wanatetea biashara hii ya upatu wa piramidi kuweza kuwaasa kurejea katika misingi ya utawala wa sheria na kuheshimu haki za binadamu za waumini wao na watanzania wengine wa dini na imani mbalimbali. Viongozi wote wa dini waweze kuweka mkazo kuhakikisha fedha 'zilizopandwa' zinarejeshwa kwa wahusika na serikali inatimiza wajibu wake wa kulinda raia na kusimamia utawala wa sheria. Pia, washiriki wa DECI na washirika wao wanapaswa kuwa na utulivu katika kipindi kuepusha madhara yoyote ambayo yanaweza kutokea kama suala hili lisiposhughulikiwa kwa umakini mkubwa.

Serikali isipochukua hatua za haraka kunusuru mwelekeo wa mambo kuhusu kadhia hii wafuatao watawajibika kwa yote yatayotokea: Waziri Mkuu Mizengo Pinda(kwa kushindwa kusimamia utawala wa sheria); Waziri wa Fedha na Gavana wa Benki Kuu(kwa kushindwa kusimamia sekta ya fedha ikiwemo kutoa ushauri kwa vyombo vya dola kuchukua hatua za haraka); Waziri wa Mambo ya Ndani(Kwa kushindwa kulinda mali za raia, na kwa polisi kulinda biashara haramu kwa muda mrefu bila kuchukua hatua za mapema); Usalama wa Taifa(kwa kushindwa kutoa tahadhari ya mapema ya kishushushu ya kuzuia biashara ya upatu wa piramidi kupanuka na kuwa na wateja wengi); Mamlaka ya Mapato(kwa kukusanya kodi bila kuchunguza uhalali kamili wa biashara inayohusika na hivyo kujenga hisia kwamba upatu huo wa mfumo wa piramidi ulikuwa biashara inayotambuliwa na serikali).

Baada ya kuibuliwa kwa ufisadi katika Benki Kuu(BOT) uliohusu akaunti za madeni ya nje(EPA) na masuala mengine kama Meremeta, Tangold na Deep Green ilitarajiwa kwamba vyombo vya serikali vingekuwa vimeamka na kubaini aina zote za hujuma kabla ya kuleta athari kwa wananchi na taifa kwa ujumla, lakini suala hili la DECI limedhihirishwa kwamba bado kuna matatizo makubwa katika mfumo wetu wa utawala. Namna ya kudumu ya kukabiliana na hali hii na kujenga taifa lenye kuheshimu utawala wa sheria na kulinda haki za binadamu ni kuunganisha nguvu ya umma katika kufanya mabadiliko ya kweli katika taifa letu. Mabadiliko hayo yatawezesha kuwa na uongozi wenye kusimamia ipasavyo taasisi za umma na vyombo vya dola katika kupamba na aina zote za ufisadi, kutetea rasilimali za nchi na kuhimiza utamaduni wa uwajibikaji kupitia dira/sera mbadala zenye kujenga taifa lenye kutoa fursa kwa kila raia kuendelea kwa kadiri ya fursa na vipaji ambavyo Mwenyezi Mungu amejalia taifa letu na wananchi wake.

Na John Mnyika
Mkurugenzi ya Mambo ya Nje
0754694553
http://mnyika.blogspot.com/
mnyika@chadema.net

Sunday, April 5, 2009

Tubadili mfumo wa uchaguzi tupate uongozi bora wenye uwiano wa kijinsia-2

Tubadili mfumo wa uchaguzi tupate uongozi bora wenye uwiano wa kijinsia-2

Na John Mnyika
Katika makala yangu iliyotangulia nilianza kutoa mwito kuhusu haja ya kubadili mfumo wa uchaguzi kwa lengo la kupata uongozi bora wenye uwiano wa kijinsia. Katika makala hiyo nieleza uhusiano baina ya demokrasia na mfumo wa uchaguzi wenye uwiano wa kijinsia. Niliuchambua mfumo wa uchaguzi ambao tunautumia hivi sasa hapa nchini wa wengi wape na pia mfumo wa uwiano ambao kwa sasa unatumika Tanzania kwa wanawake pekee ukifahamika zaidi kama viti maalumu. Nilitoa mifano ya ujumla kuhusu uteuzi wa viti maalum ulivyofanyika mwaka 2005 ndani ya CCM na ndani ya CHADEMA. Pia, nilidokeza mabadiliko ambayo CHADEMA imefanya katika katika katiba yake mwaka 2006 ambayo sasa yametoa mamlaka kwa Baraza la Wanawake wa CHADEMA(BAWACHA) kufanya utuezi wa nafasi za viti maalum za wanawake katika chama. Katika makala hii nachambua mfumo mpya wa uteuzi wa wabunge wa viti maalum ambao CCM imeupitisha na kutoa mapendekezo ya mfumo mbadala ambao kama taifa ni vyema tukauzingatia wakati wa kubadili mfumo wa uchaguzi katika nchi yetu.

Tarehe 7 mwezi Machi mwaka 2009, halmashauri Kuu ya Taifa(NEC) ya CCM chini ya Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete ilijadili ajenda ya kuwapata Wabunge/Wawakilishi Wanawake ili kufikia lengo la asilimia 50. Lengo hilo liliwekwa katika Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho ili kutimiza malengo yaliyowekwa katika matamko na makubaliano mbalimbali ya kimataifa kuhusu uwiano wa kijinsia.Katika kikao hicho Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM iliazimia kupendekeza kwa Serikali inayoongozwa na chama hicho kuwa idadi ya Wabunge katika Bunge la Muungano iwe na ukomo wa viti 360. Uamuzi huu wa CCM unalenga kuongeza zaidi idadi ya wabunge nchini, katikati ya mjadala ambao unaendelea hivi sasa kuhusu gharama kubwa ya fedha za walipa kodi inayotumika kuwalipa wabunge ukilinganisha na watumishi wengine wa umma mathalani polisi, walimu, wauguzi nk na pia ukiwianisha na hali ya uchumi wa taifa. CCM inaamua kuongeza tena idadi ya wabunge takribani 40 wapya bila kulieleza kwanza taifa tija ambayo imepatikana kwa ongezeko ambalo lilifanyika hapo awali.

Katika kikao hicho, CCM imeamua pia kwamba nchi iendelee na utaratibu uliopo sasa wa kuwapata Wabunge/Wawakilishi wa Viti Maalum Wanawake. Mfumo ambao katika makala yangu iliyopita nimechambua udhaifu wake. Isipokuwa CCM sasa inataka kwamba idadi yao katika kila chombo ipatikane kutokana na asilimia 50 ya Wabunge/Wawakilishi wote wa majimbo yaliyopo (232). Hapa maana yake ni kwamba CCM imeamua kuacha kutekeleza ahadi ambayo iliitoa kwenye ilani ya kutaka kutekeleza makubaliano ya kimataifa ambayo serikali ya CCM ilisaini yanayotaka uwiano wa asilimia 50 kati ya wanawake na wanaume. Kizio cha kupima uwiano kilipaswa kiwe idadi ya wabunge wa bunge zima na si idadi ya wabunge wa majimbo pekee. CCM pia wamekubaliana kuwa kwa kuzingatia kwamba Bunge litakuwa na ukomo wa viti 360 na kwamba idadi ya majimbo ya uchaguzi yaliyopo sasa ni 232, idadi ya Wabunge Wanawake itakayopatikana ni 116 sawa na asilimia 50 ya Wabunge wote wa Majimbo. CCM imeamua kuwa pawe na Wabunge Wanawake 7 watakaopatikana kwa mujibu wa Katiba ya nchi; hivyo kwa utaratibu huu, Wanawake 109 ndio watakaopatikana kupitia Viti Maalum. Kwa upande mwingine CCM inataka Rais apewe mamlaka makubwa zaidi ya kuteua wabunge kutoka 10 mpaka 14. Suala la Rais kuteua wabunge limekuwa likipingwa kutokana na kuongeza mwingiliano kati ya mihimili ya dola lakini pia uteuzi wenyewe kutokuwa na vigezo na mfumo wa uthibitisho (vetting). Idadi ya Wabunge 116 ukilinganisha na bunge zima linalopendekezwa la wabunge 360 maana yake ni kwamba idadi ya wabunge wanawake ambao itahakikishwa kwa mujibu wa katiba na sheria ni asilimia 33 tu. Hii si asilimia 50 inayotakiwa chini ya mfumo wa uwiano wa kijinsia unaoelezwa kuwa wa 50 kwa 50. Hivyo, wadau wa masuala ya jinsia wanapaswa kuelewa kwamba kauli zinazosemwa na wanasiasa wa CCM kwenye majukwaa kuwa tayari chama hicho kimekubaliana na mfumo wa 50 kwa 50 ni tofauti na maamuzi yao ambayo wameshayafanya katika vikao vyao kuhusu uwiano wa kijinsia utakaokuwepo katika uchaguzi wa mwaka 2010. Ukweli ni kuwa CCM imeshakwepa kutekeleza ahadi ambayo iliitoa katika ilani yake ya uchaguzi mwaka 2005 badala ya 50 kwa 50 badala yake imekuja na mfumo wa uwakilishi wa 33 kwa 67. Maelekezo ya kwamba asilimia 17 iliyobaki itapatikana kwenye majimbo ni ya kisiasa ambayo hayajawahi kutekelezwa katika chaguzi zote tangu Uhuru wa Tanzania.CCM pia katika kikao hicho imepitisha azimio la kuielekeza Serikali ya Muungano irekebishe Katiba ya nchi na sheria ya Uchaguzi ili kuweka ukomo wa idadi ya Wabunge katika Bunge la Muungano kuwa 360, na pia kuhalalisha kisheria utaratibu huu mpya wa kuwapata Wabunge Wanawake kupitia Viti Maalum. Hapa CCM imeguza suala la Katiba ya nchi kuwa hodhi ya chama hicho badala ya mabadiliko yake msingi wake kuwa ni ridhaa ya watanzania wote. Ni dhahiri kwamba bila wananchi kupaza sauti maamuzi haya ya chama kimoja yatageuzwa kuwa ya taifa kwa kutumia vibaya uwingi wao bungeni, tumeona hivyo katika mabadiliko ya sheria ya vyama vya siasa. Lakini pia huu ni ushahidi wa wazi kuwa CCM imeshafanya maamuzi ya kutotimiza ahadi ya kuweka mfumo wa 50 kwa 50 katika uchaguzi wa mwaka 2010. Hata hivyo, katika kikao hicho, CCM haikupitisha azimio lolote kuhusu uwiano wa kijinsia katika uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji wa mwaka 2009 ambao kimsingi ulipaswa uwe ndio msingi wa mwanzo kabisa wa kuhakikisha uwiano wa makundi mbalimbali ya kijamii kiuwakilishi.
Ni wazi suala hili sasa linahitaji mjadala mkubwa wa umma kwa sababu mabadiliko ya katiba na sheria za nchi si hodhi ya chama chochote cha siasa au kikundi cha watu wachache; ni suala la maslahi na matakwa ya umma.

Kwa ujumla, sikubaliani na marekebisho ya mfumo wa uchaguzi yaliyopitishwa na CCM na dhamira ya makala haya ni kutoa mwito kwa wadau wote kulijadili suala hili na kutoa mwelekeo unaostahili. Kwa maoni yangu mfumo wa Uchaguzi urekebishwe na kuruhusu mfumo mchanyato wa uwiano wa kura na mfumo wa “first-past-the-post” badala ya mifumo hiyo iliyotangulia. Mfumo wetu wa uchaguzi unataka Wabunge na Madiwani kupatikana kutoka katika majimbo na kata tu. Marekebisho yaliyopitishwa na CCM yanaturudisha nyuma zaidi. Kwa mfumo wa sasa wabunge wanawake hupatikana kwa uwiano wa kura za Wabunge nchi nzima na Madiwani wa wanawake kutokana na uwiano wa viti vya udiwani ambao kila chama kimepata. Lakini Wabunge Wanawake hawana mamlaka ya kisheria kwa eneo maalumu. Kwa sasa ni rahisi kusema kuwa wanatoka mikoani, lakini hii ni kwa sababu tuna chama kimoja kikubwa na hivyo kupata kura za kuenea mikoa yote. Huko mbele, tena na hawa wagombea binafsi, itatokea mikoa ambayo haitapata wabunge wanawake kwa sababu kura hazitotosha kwa chama kimoja kugawa wabunge kila mkoa. Umefikia wakati sasa kufanya mabadiliko makubwa ya mfumo wa uchaguzi ili kuingiza uwakilishi wa uwiano. Kama nchi tutafakari mambo yafuatayo yanayohusu mabadiliko ya mfumo wa kisiasa wa nchi yetu: Mosi; Wabunge wa kuchaguliwa moja kwa moja na wananchi watokane na Halmashauri za Wilaya za sasa. Mfano, badala ya Wilaya ya Manispaa ya Kinondoni kuwa na Wabunge watatu wa Ubungo, Kinondoni na Kawe, iwe na Mbunge mmoja tu atayewakilisha wilaya nzima. Halmashauri ya Wilaya/Mji/Manispaa/Jiji ndio iwe Jimbo la Uchaguzi. Katika ngazi hii wagombea wasio na vyama waruhusiwe pamoja na wale wenye vyama. Kwa hali ya sasa tutapata Wabunge takribani 130 kutoka kundi hili. Idadi yao itaongezeka kutokana na kuongezeka kwa Halmashauri zitakazoundwa pindi mahitaji yanapotokea. Ikumbukwe kwamba katika ngazi ya chini kitovu cha mamlaka ni halmashauri, ambao ni msingi pia hata katika upangaji wa bajeti taifa.
Haitakuwa tena kazi ya Tume za Uchaguzi kuunda Majimbo ya uchaguzi bali vile vigezo vya kuunda Halmashauri (Baraza la Madiwani) vilivyopo kisheria (Local Government Authorities Acts) ndio vitatumika. Pili; Wabunge kati ya 150 na 200 watokane na kura za uwiano (idadi tofauti inaweza kupendekezwa). Vyama vya siasa vitapata viti kutokana na uwiano wa kura ambao kila chama kimepata katika Mkoa/majimbo.
Chama cha siasa ni lazima kiwe kimepata kwanza asilimia tano ya kura zote zilizopigwa katika Mkoa husika ili kigawiwe viti. Kwa hiyo kila chama kitatengeneza orodha ya wagombea wake kwa kila Mkoa na kuipeleka Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Orodha hii iwe katika hali ambayo kama jina la kwanza ni Mwanaume la pili awe Mwanamke, hali kadhalika kama jina la kwanza ni Mwanamke katika orodha la pili liwe la mwanaume. Mikoa itapata idadi ya Wabunge kutokana na vigezo maalumu, mfano idadi ya watu n.k. Kwa mapendekezo haya tuna uhakika wa kuwa na Wabunge wanawake zaidi ya theluthi moja katika Bunge. Lakini pia tutakuwa na uhakika kwamba kila Mkoa utakuwa na Mbunge au Wabunge wanawake. Ama kama tutakubaliana kwa pamoja kama taifa katika lengo la kuongeza idadi kubwa ya wanawake kuelekea uwiano wa hamsini kwa hamsini(50-50), robo tatu ya wabunge wa uwiano inaweza kuwa ni orodha ya wanawake na robo ikabaki kwa ajili ya wanaume. Lengo la kuwa na orodha ni kuwezesha pia vyama kutumia orodha hiyo kuhakikisha uwakilishi wa makundi ya kijamii mathalani walemavu, vijana na viongozi muhimu wa kijamii ambao ni muhimu kuwepo bungeni.
Mabadiliko haya ya mfumo wetu wa Uchaguzi yana faida nyingi sana. Moja ya faida ni kuvigeuza vyama vyetu vya siasa kutoka katika kushindanisha watu tu, bali pia kushindanisha sera. Kwa sababu wananchi watakuwa wanapiga kura mbili. Kura moja ya chama na kura nyingine ya ama diwani au Mbunge na Rais. Kura ya chama ndio itatufanya kupata wabunge wa uwiano. Wala hatutatumia mfumo mmoja kuzalisha mfumo mwingine. Bali kila mfumo utazalisha Wabunge kuunda Bunge letu. Sisi hatutokuwa wa kwanza kufuata mfumo huu wa uwiano-Msumbiji, Afrika ya Kusini, Ujerumani, Uswidi na hata India.
Vyama vikianza kushindanisha sera tutakuwa tumepiga hatua kubwa sana kama nchi katika kuimarisha mfumo wa demokrasia na kwa kweli hatutokuwa na wasiwasi wa vyama kudhoofika kutokana na wagombea Binafsi kuruhusiwa. Demokrasia ndani ya vyama itaimarika kwani Tume ya Taifa ya Uchaguzi itahakikisha vyama vinapata wawakilishi wake katika Orodha ya Mikoa kidemokrasia. Sehemu ya kuanza kutumia mfumo huu wa uchaguzi wa ni kupitia uchaguzi wa mitaa, vijiji na vitongoji mwaka 2009 ambapo tunaweza kupima mafanikio na kuboresha mfumo mzima wa kitaifa kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa 2010. Ili kutimiza azma hiyo, ni muhimu kufanya marekebisho katika sheria zinazohusu uchaguzi huo lakini pia inabidi kupanua makubaliano ya wadau yaliyofikiwa baina ya vyama na serikali mwezi Februari mkoani Morogoro ili kanuni zitakazotungwa zihusishe uwiano wa kijinsia katika uchaguzi huo.

Hata hivyo, suala kipaumbele halipaswi kuwa kuhakikisha uwiano wa kijinsia tu; suala halipaswi kuwa idadi ya wanawake katika vyombo vya maamuzi, bali ubora wa wawakilishi katika vyombo vya maamuzi na tija yao kwa taifa. Wapo watu wanaopinga wanawake kupewa nafasi katika vyombo vya maamuzi kwa kigezo tu kuwa nafasi za uwakilishi zisitolewe kwa jinsia bali uwezo. Lakini ukiangalia kwa upande mwingine, katika vyombo vyetu vya maamuzi hivi sasa kuna wanaume wengi wenye uwezo mdogo. Kwa mantiki hilo, suala la kuhakikisha kwamba kama taifa tunakuwa na viongozi bora kwenye vyombo vya maamuzi linapaswa kutizamwa kwa upana wake bila kujali jinsia. Pia ieleweke kwamba kipaumbele sio uwepo tu wanawake katika vyombo vya maamuzi, bali uwepo wao unapaswa kuambana na ubora wa kushughulikia masuala yanayohusu umma ikiwemo kuweka mkazo katika masuala yanayowagusa wanawake. Mathalani, wabunge wengi wa viti maalum wameshindwa kushughulikia masuala yanayogusa umma wa watanzania lakini pia wameshindwa hata kuweka mkazo katika masuala yanayogusa wanawake wenzao mathalani vifo vya watoto wadogo na wakina mama wajawazito kutokana na mazingira mabovu katika sekta ya afya nchini.

Ni vyema pia wadau wa masuala ya jinsia wakatazama masuala haya kwa upana wake, kwamba kuwekwa pembezoni kwa kundi moja kijamii mathalani wanawake ni matokeo ya mifumo ya kisiasa kuweka pembezoni makundi ya kijamii kwa ujumla wake. Kwamba kama wadau wakiungana kuhakikisha kuna uwanja sawa wa kisiasa wenye uchaguzi huru na haki ni wazi kuwa makundi yote ya kijamii iwe ni wanawake au walemavu wanaweza kushiriki. Hivyo, haja ya kufanya mabadiliko ya katiba na kisheria yenye kujenga misingi ya haki katika taifa ieleweke kwamba ni ajenda ya pamoja katika taifa. Kurekebisha mfumo wa uchaguzi ili kupata uongozi wenye uwiano wa kijinsia ni sehemu mojawapo ya msingi katika harakati pana zaidi za kupambana na ufisadi, kutetea rasilimali na kujenga taifa lenye kutoa fursa kwa wote.

Mwandishi wa makala hii anapatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.net na http://mnyika.blogspot.com

Tubadili mfumo wa uchaguzi tupate uongozi bora wenye uwiano wa kijinsia-1

Tubadili mfumo wa uchaguzi tupate uongozi bora wenye uwiano wa kijinsia-1

Na John Mnyika

Tubadili mfumo wa uchaguzi tupate uongozi bora wenye uwiano wa kijinsia; huu ni mwito wangu wa leo ambao unajikita katika eneo moja tu: “Mfumo wa Uchaguzi Tanzania”. Mfumo ni roho ya uchaguzi na chaguzi ndio msingi wa Siasa. Kama siasa(nikimaanisha siasa safi) ni hitaji muhimu la maendeleo kama alivyowahi kusema hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere; basi uendeshwaji wa uchaguzi(kwa maana ya uchaguzi huru na haki); ndio njia ya kulipata hitaji hili. Uendeshwaji wa uchaguzi huru na haki hutupatia pia hitaji lingine la msingi kwa maendeleo- yaani “Uongozi Bora”. Suala kuu ni kuwa na mifumo ya kikatiba na kisheria na kiuwanja wa kisiasa ambayo inahakikisha uchaguzi huru na haki. Hili nitalijadili katika makala zangu zitakazofuata siku za usoni tukiwa tunaelekea katika uchaguzi wa mitaa, vijiji na vitongoji mwaka 2009 na uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Hata hivyo, mfumo wa uchaguzi ni moja ya masuala muhimu katika mchakato wa uendeshaji wa uchaguzi wa kidemokrasia. Kwa kuwa demokrasia ni utawala wa watu kwa ajili ya watu, uwakilishi wa makundi mbalimbali ya kijamii katika uongozi ni suala linalopaswa kuhimizwa. Uhusiano wa karibu baina ya hoja ya mfumo wa uchaguzi na haja ya uwiano wa kijinsia unajitokeza katika mazingira hayo.
Wakati suala la mfumo wa uchaguzi limeshawekewa sheria zinazosimamia kwa karibu katika nchi zilizoendelea ambapo demokrasia ya mfumo wa vyama vingi imekuwepo kwa miaka mingi; katika nchi zenye demokrasia changa bado tunaendelea kujiuliza maswali na kuibua masuala kwa lengo kupata mifumo ambayo itakidhi mahitaji yetu.
Shabaha ya makala hii ni kuchochea mjadala ambao utawezesha mapitio ya katiba na sheria zinazotawala siasa Tanzania katika muktadha wa mfumo wa uchaguzi na kuhamasisha marejeo ama mabadiliko yanayostahili. Ni lazima tuhakikishe tunaendelea kuwa na “uchaguzi” badala ya “uchafuzi”.

Masuala ambayo yameibuliwa katika mijadala mbalimbali kuhusu suala hili pamoja na mambo mengine ni tuhuma za uwepo wa ubaguzi, ukabila na upendeleo katika mgawanyo wa viti hivyo. Lakini masuala mazito zaidi, ni mjadala kuhusu dhana na dhima ya viti maalum hususani vya wanawake katika taifa letu katika muktadha wa mfumo wa uwakilishi wa kidemokrasia nchini wenye kuhakikisha uwiano wa kijinsia.

Mfumo unatotumika Tanzania ni Mfumo wa Wengi Wape; hata hivyo kuna Viti Maalumu vya Wanawake katika ngazi ya Ubunge na Udiwani ambavyo vinagawanywa kwa misingi ya uwiano. Mfumo wa Wengi Wape (Plurality-Majority) ni mfumo ambao hutumia wilaya/jimbo za/la uchaguzi na mgombea anachaguliwa kuwakilisha wilaya/jimbo husika. Tawi la mfumo huu linaloitwa kwa Kiingereza First-Past-the-Post (FPTP) ndilo lililo maarufu sana na hutumika katika nchi nyingi zilizo katika Jumuiya ya madola. Katika mfumo huu vyama huteua wagombea na kuwadhamini katika majimbo. Mgombea anaeshinda kwa kura nyingi kuliko wenzake hata kama hazifikii nusu ndio huwa amechaguliwa na kunyakua kiti kinachogombewa. Mfumo huu unatumika katika nchi kadhaa mathalani Uingereza, India, Kenya na Tanzania. Mfumo huu pia husababisha mara nyingi kuwa na chama kimoja chenye uwezo wa kuunda serikali peke yake bila ya kuhitaji vyama vingine na kuwa na mseto. Mfumo huu husaidia wananchi kuchagua watu na sio vyama vya siasa na hivo mpiga kura anaweza kutathmini utendaji wa mbunge au mwakilishi badala ya utendaji wa chama fulani. Mfumo huu ni rahisi kuutumia na unaeleweka miongoni mwa wananchi, wagombea huwa wachache na hata uhesabuji wa kura unakuwa ni rahisi.

Kwa upande mwingine ‘mshindi anachukua vyote’ huathiri ukuaji wa vyama na hivyo nchi kukosa vyama vingi vyenye nguvu. Hii ni kwa sababu, badala ya vyama kufanya kampeni kwa kutumia sera zao, hutumia majina ya watu ambao ni wagombea wao. Hivyo basi mfumo huu hupelekea vyama kuwekwa pembezoni na kushindwa kushindana na kutotoa mbadala. Vyama katika mfumo wa wengi wape huwa vigumu sana kuwajibika kwa wananchi kwani badala ya kurekebisha sera zao vyama hubadili wagombea tu na kuwarubuni wananchi na kushinda tena. Maoni ya wananchi yanakuwa hayaheshimiki kikamilifu na nchi inakosa maendeleo kwa sababu ya demokrasia duni inayosababishwa na mfumo wa wengi wape.

Mfumo wa wengi wape hupelekea kuminya nafasi za wanawake kuchaguliwa kuingia bungeni. Kwa tamaduni za nchi za kiafrika bado kuna imani kwamba mwanamke hawezi kushindana na mwanaume na pia gharama kubwa za uchaguzi katika majimbo, wanawake wanaochaguliwa kuingia bungeni wanakuwa ni wachache sana.

Hali hii inajihidhirisha katika bunge la sasa ambapo katika bunge la lenye wabunge 232 wa kuchaguliwa majimboni, kati yao wanawake waliochaguliwa majimboni hawafiki 20. Hii inaamaanisha kwamba katika bunge letu la sasa, ukiondoa wabunge wa viti maalum vya wanawake; bunge lina zaidi ya asilimia 90 wanaume na wanawake ni chini ya asilimia 10. Ili kufikia lengo la Umoja wa Mataifa(UN) na Umoja wa Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) lililowekwa na baadaye na Umoja wa Afrika(AU), Tanzania ilitenga viti maalum vya wanawake na kufanya uwakilishi wa wanawake hivi sasa katika bunge letu kuwa takribani asilimia 30 katika bunge zima lenye wabunge takribani 320.

Katika mchakato wa uteuzi wa mwaka 2005 ulianzia kwenye ngazi ya wilaya zao na baadaye kupitia kwenye Kamati Kuu ya chama. Mchakato huu uliongozwa na vipengele vya Katiba ya CHADEMA toleo la mwaka 2004 ambayo ilikuwa ikitumika wakati huo. Vigezo hivyo vilijikita katika kuangalia sifa za uongozi na mchango wa kila mwombaji katika kutimiza wajibu kwa CHADEMA na taifa. Hata hivyo kutokana na matarajio ya uchache wa viti, uamuzi wa kupanga orodha ya mwisho baada ya kupata mapendekezo kutoka ngazi za chini za chama ilibidi ufanyike katika ngazi ya taifa. Hata hivyo, uteuzi wa viti hivyo sita ulifuatiwa na shutuma zilizoelekezwa kwa chama kuhusu upendeleo katika uteuzi huo hoja kuu ikiwa ni tuhuma za ukabila katika uteuzi huo. Niliwahi kuandika huko nyuma uchambuzi wangu kuhusu uteuzi wa viti hivyo ikiwemo ufafanuzi kuhusu tuhuma hizo katika mfululizo wa makala unapatikana kwenye http://mnyika.blogspot.com ambapo nimeeleza vigezo vigezo vilivyotumika, mafanikio na udhaifu uliojitokeza. Kwa kuwa na viti hivyo 6 kati ya wabunge wake 11, CHADEMA ina uwakilishi wa zaidi ya asilimia 50 wanawake katika timu yake bungeni.CCM kwa upande wake kwa kuwa ilikuwa na viti zaidi ya 50 iliweza kuvigawa viti hivyo kimikoa na kuwashindanisha wanawake katika maeneo yao. Pamoja na hayo bado pamekuwepo na tuhuma za upendeleo na rushwa katika kampeni za uteuzi ndani ya CCM na jumuia zake.

Jambo moja ambalo watanzania ni vyema wakalifahamu; CHADEMA kama chama kinachokua na kubadilika. Mwaka 2006 kilifanya tathamini ya chama, na kuandaa Mpango Mkakati wa chama 2006 mpaka 2010. Na kati ya mambo ambayo chama kiliyatazama ni mfumo wa uteuzi wa wanawake wa viti maalum. Pamoja na mafanikio yaliyopatikana, na mchango mzuri wa wabunge wetu bungeni ikiwemo wa viti maalum, palionekana changamoto- namna kati ya kuwianisha mfumo wa uteuzi kwa vigezo na mfumo wa uteuzi kwa kugombea pekee. Chama kiliona kuna haja ya kuboresha zaidi mfumo wake wa uteuzi wa wabunge hawa, na hivyo, CHADEMA ikabadili katiba yake. Sasa katiba imetoa fursa ya kuanzishwa kwa Baraza la Wanawake wa CHADEMA (BAWACHA), na pamoja na mambo mengine- BAWACHA ndio ambalo sasa linasimamia uteuzi wa wabunge wa viti maalum mwaka 2010, kupitia ushindani wa wanawake wenyewe. Taratibu za BAWACHA sura ya kumi zinaeleza bayana namna ya wabunge na madiwani wa viti maalum watavyopatikana ndani ya CHADEMA kwa kuteuliwa na wanawake wenyewe.

Hata hivyo kuwa na mfumo wa uchaguzi wenye uwiano katika viti vya wanawake pekee umesababisha viti hivyo kwa kuitwa ‘viti maalum vya wanawake’. Matokeo ya kuwa na mfumo usiotazama suala la jinsia kwa upana wake ni nafasi hizi kubebeshwa taswira ya upendeleo katika katiba na sheria kabla hata ya uteuzi wenyewe. Hivyo, hata mchakato wa uteuzi wake klwa mantiki hiyo, viti hivyo, vitaendelea kuonekana kama ni ‘maalumu’, vya ‘upendeleo’ na kwa ujumla vinagawiwa ‘kibaguzi’ kwa wanawake dhidi ya makundi vingine. Vinapatikana kwa ushindani ‘uliofungwa’ miongoni mwa wanawake wengine. Ni watu wenye mtizamo huu mpana ndio ambao wanamsimamo kuwa viti hivyo ‘vifutwe’. Watetezi wa viti hivi wamekuwa wakijenga hoja wakati wote kuwa viti hivyo ni muhimu, kwa kuwa wanawake wamekuwa wakishindwa kushindana na kushinda majimbo na hivyo kufanya uwakilishi wao kuwa duni. Na wanatoa sababu za kihistoria na sababu za vikwazo vya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni kama vikwazo vya wanawake kupata nafasi za ubunge. Katika hali hiyo, watatezi hao wanaamini kama uwepo wa viti maalum, ni tiba na daraja la kuwawezesha wanawake kupata nafasi katika siasa.(Affirmative action). Lakini Mtandao wa Jinsia Tanzania(TGNP) na Wanaharakati wa Haki za Wanawake(FEMACT) wao wamefanya tathmini ya miaka kumi toka viti maalum viazishwe, wakati wa mapitio ya miaka kumi toka tamko la Beijing na kubaini kwamba viti hivi; havijasadia masuala ya wanawake kupewa kipaumbele katika vyombo vya maamuzi, wala havijasaidia kuwezesha wanawake wengi zaidi kuingia katika siasa na kushinda majimboni. Kwa ujumla, viti hivi vinaonekana kuzua ‘upendeleo’, ‘ubaguzi’ nk miongoni mwa wanawake wenyewe na kunufaisha tabaka la wachache. Wapo wenye mtizamo mkali zaidi, kuwa kwa kutengewa ‘viti maalum’, wanawake wanazidi kusukumwa pembezoni mwa mkondo na mfumo wa uwakilishi. Hivyo, mjadala huu unapaswa kuwa mpana zaidi ili kuhakikisha mfumo wa uwakilishi wa uchaguzi na kisiasa mwaka 2009, 2010 na kuendelea unatoa tija inayostahiki kwa makundi yote ya kijamii. Ndio maana kuna haja ya kubadili mfumo wa uchaguzi kupata uongozi bora wenye uwiano wa kijinsia. Katika makala yangu inayofuata nitachambua mfumo uliopitishwa na CCM na kupendekeza mfumo mbadala.

Mwandishi wa makala hii anapatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.net na http://mnyika.blogspot.com