Friday, October 23, 2009

Uchaguzi Mitaa: Kampeni mwisho Oktoba 24; Kupiga kura tarehe 25-Mambo Mawili!

Leo tarehe 24 Oktoba ni Siku ya Umoja wa Mataifa lakini pia kwa hapa nchini ni siku ya mwisho ya kampeni za uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa. Upigaji kura ni tarehe 25 Oktoba, 2009.

Kama nilivyobashiri kwenye mfululizo wa makala zangu kuhusu uchaguzi huu kuanzia mwanzoni mwa mwaka huu(Makala hizo zinapatikana kwenye blogu http://mnyika.blogspot.com); pamekuwa na ukiukwaji mkubwa wa kanuni na taratibu za uchaguzi. Uchaguzi si upigaji kura tu na utangazaji wa matokeo; uchaguzi ni mchakato wenye hatua mbalimbali.

Kati ya hatua muhimu za uchaguzi ni pamoja uandikishaji wa wapiga kura; uteuzi wa wagombea; kampeni; elimu ya uraia; upigaji kura na utangazaji wa matokeo- lakini roho ya uchaguzi ni hatua ya ‘usimamizi wa uchaguzi’. Hatua hii huanza mwanzo mpaka mwisho wa uchaguzi. Usimamizi wa uchaguzi ndio kimsingi huamua kama uchaguzi utakuwa huru na haki ama ni uchafuzi tu wa demokrasia na maendeleo.

Nimesikiliza kauli za hivi karibuni za viongozi waandamizi wa CCM na serikali yake; kauli ambazo ni bezo kwa utawala bora.

Alianza Rais Kikwete kwa kusemwa kwamba anatoa mwito kwa wote watakaoshindwa kukubali matokeo badala ya kwenda mahakamani kwa kuwa uchaguzi unaigharimu serikali. Kikwete anayesema hayo akijua kabisa jinsi Wizara ya TAMISEMI(Chini ya Waziri Mkuu Pinda, na Waziri wa Nchi Kombani) imeacha mwanya wa hujuma kwa wagombea kwa kuwatumia watendaji wa kiserikali kama nilivyowahi kubashiri. Kabla kauli ya Kikwete haijakauka, ndani ya Kata yake mwenyewe ya Lugoba; ufa uliotokana na kura za maoni za chama chake, ulisababisha wanavitongoji na vijiji kuhakama CCM kwa wingi na wananchi kuamua kuunga mkono CHADEMA. Kuona hivyo, watendaji wakaamua kuwaengua wagombea waliopitia CHADEMA kwa sababu zisizo na msingi. Wapo walioenguliwa kwa maelezo kuwa hawana kipato kinachowawezesha kuishi; wakulima wa kawaida wanaojulikana kijijini; wengine wakiwa ni wafanyabiashara pale Lugoba miaka nenda miaka rudi. Mmoja baada ya kuleta leseni na risiti za michango ambayo amekuwa akitoa kutokana na biashara yake, bado akaenguliwa kwa kigezo kwamba hana TIN namba! Mgombea wa Uenyekiti wa Kijiji cha Lugoba yeye akaenguliwa kwa maelezo kwamba amedhaminiwa na ngazi ya kata ya chama; jambo ambalo kwa miaka nenda rudi halikuwa na utata miaka nenda miaka rudi kwani kanuni zinaeleza tu kuwa kinachotakiwa ni mgombea kudhaminiwa na chama; kuhusu ngazi gani ni uamuzi wa chama chenyewe. Ya Lugoba ni mfano tu wa jinsi wagombea walivyoenguliwa kwa maelfu katika maeneo mbalimbali ya nchi hususani vijijini. Lakini hata hapa DSM katika uso wa Kikwete mambo hayo hayo yamefanyika; mfano Mgombea wa Uenyekiti hapa Sinza D ameendolewa kwa maelezo kwamba amedhaminiwa na Kata; wakati wagombea wengine wote wameachwa na kimsingi jimbo zima la Ubungo wagombea wamedhaminiwa na kata katika mitaa mbalimbali. Huyu ameondolewa kwa sababu tu Diwani wa Sinza-Mwaking’inda akishirikiana na Meya Londa; swahiba wake mkubwa katika tuhuma zote za Halmashauri ya Kinondoni; wameweza kufanya shinikizo. Ikumbukwe Kamati ya Rufaa ina wajumbe wawili tu wenye kura; mwenyekiti akiwa na Afisa Tawala, katibu wake akiwa ni Afisa ndani ya ofisi yake. Maamuzi hayo, mgombea wetu amepatiwa jana mchana; huku tayari alishaanza kampeni toka tarehe 18 Oktoba. Kamati ya Rufaa ilipaswa kufanya kazi yake mpaka tarehe 18 Oktoba na kutoa taarifa kwa wahusika; lakini kwa kuwa Ofisi ya Afisa Tawala; chini ya Bwana M. Mkapa; inafanya kazi kwa shinikizo, ndio maana haya yanatokea!.

Baadaye Waziri Mkuu Pinda akajitokeza akisikitika kwamba watu wengi hawajajitokeza kujiandikisha na akaja na hoja kuwa sasa serikali inafikiria kuunganisha uchaguzi huu na wa madiwani ili kuongeza mvuto. Watu wakaona Pinda amekuja na wazo jipya, kumbe ukweli ni kuwa hii imekuwa ni hoja ambayo wadau wamekuwa wakiitaja na kutaka serikali ibadili sheria toka mwaka 2004. Lakini Pinda alisahau kuwa kitendo cha ofisi yake kuhodhi mamlaka ya kutoa elimu ya Uraia na mpiga kura kwenye uchaguzi huu kimepunguza nguvu ya wadau wengine kufanya hivyo. Mathalani hapa Kinondoni, ziara zangu za mikutano ya hadhara zilizuiwa na Kamanda wa Polisi kwa maelekezo kwamba vyama vya siasa haviruhusiwi kufanya mikutano ya aina hiyo. Pinda anajua ni ofisi yake ndiyo iliyokiuka kanuni kuhusu uandikishaji; tarehe 25 Julai ilichapa magazeti ratiba sahihi kuwa uandikishaji ungefanyika tarehe 4 mpaka 24 Septemba; hii ingekuwa kwa siku 21, na mchakato ungekamilika siku 21 kabla ya uchaguzi. Lakini baadaye pamoja na kuwa kanuni zinataka ratiba itolewa siku 90 kabla ya uchaguzi; Ofisi yake ikatoa ratiba nyingine mwezi Septemba kuwa uandikishaji ufanyike tarehe 4 mpaka 10 Oktoba; kwa siku 7 tu; na hivyo umekamilika chini ya siku 21 kama kanuni inavyotaka. Lakini anajua kuwa kwa kufanya hivyo, ofisi yake imechanganganya ratiba hiyo na uboreshaji wa Daftari la Kudumu(DKWK) ambao unaendelea. Kwa mfano katika Jimbo lake yeye mwenyewe la Mpanda Kati; kabla ya kuanza kuandikishwa daftari la mitaa; lilianza la Kudumu; hivyo wananchi wengi walijua kwamba wameshajiandisha tayari hawawajibiki kujiandikisha tena.


Kama Kikwete alijua, kauli yake ikafuatiwa na ile ya Makamba ya kutangaza kwamba CCM imepita bila kupingwa. Siku Makamba anatoa kauli hii alikuwa anajua kabisa kule nyumbani kwake Tanga; watendaji walichelewesha fomu na kujifisha ili wagombea wa upinzani wasipate; na pia mamia ya wagombea waliofanikiwa kuchukua fomu baada ya nguvu kubwa wakaenguliwa na watendaji kwa sababu zisizo na uzito wowote; jamii ya hizo hapo juu.

Hata hivyo, ndondondo si chururu; pamoja na hujuma zote hizo, bado idadi ya wagombea wa upinzani imeongezeka hali inayoashiria kupanuka kwa upinzani na vuguvugu la mabadiliko. Makamba anasema CCM imepita bila kupingwa vijiji takribani elfu 3; hii ni dalili njema kwani kwa tafsiri yake ni kwamba zaidi ya vijiji elfu 10 kuna wagombea wa upinzani; kwa upande wa vitongiji anasema elfu 20 wamepita bila kupinga; hii tafsiri yake ni kwamba zaidi ya vitongoji elfu 80; CCM imepata wapinzani. Hili ni ongezeko ukilinganisha na mwaka 2004; ambapo CCM ilipita bila kupingwa vitongoji vingi zaidi na hatimaye ikashinda kwa ujumla kwa asilimia 96 huku vyama vya upinzani vikigawana asilimia 4; hali ya mambo inaonyesha kuwa pamoja na hujuma zote matokeo ya 2009 yatakuwa tofauti sana na yaliyopita. Yapo maeneo ambayo CHADEMA kwa mfano haikuwa na mtandao mpana wa kichama mwaka 2004 lakini sasa imepanuka kuanzia ngazi ya chini; mathalani Jimbo la Ubungo mwaka 2004, CHADEMA ilikuwa na Mgombea 1 tu wa uenyekiti wa Mtaa; Sasa inawagombea kwenye Mitaa 54; wataalamu wa hesabu wanaweza kukukotoa ni ongezeko la Asilimia ngapi, hii ni ishara njema tunapoelekea uchaguzi wa mwaka 2010.

Hata hivyo, tunapoelekea uchaguzi wa kesho Oktoba 25; kuna mambo mawili lazima yatolewe ufafanuzi kwa umma haraka; mambo haya niliwaeleza TAMISEMI ana kwa ana tarehe 8 Oktoba, wakaahidi kuyafanyia ngazi; ukimya wao unaacha maswali mengi. Hata yanahusu mchakato wa upigaji kura hiyo kesho.

Mosi, TAMISEMI haikuwa imepanga utaratibu wa kuwa na wino usiofutika kama ilivyo kawaida; matokeo yake ni kwamba mianya ya watu kupiga kura zaidi ya mara moja imeachwa wazi. Walijieleza kwamba muda hautoshi kwa mujibu wa sheria ya ununuzi kuagiza wino toka nje ya nchi; niliwaeleza njia mbadala ni kutumia wino hata wa ndani. Kama wameweza kuwa na masanduku ya kura ya kawaida na karatasi za kura za kawaida; kwa nini kila halmashauri isipewe maelekezo ya kutafuta wino wake kama zilivyopewa mamlaka ya kutengeneza makaratasi ya kura?

Pili; uchaguzi wa mwaka huu karatasi za kura hazitakuwa na picha za wagombea, wala majina yao wala ya vyama vyao; Mpiga kura atapewa kura iliyowazi ataandika mwenyewe majina ya anaowachagua. Kwa miezi wadau mbalimbali tumekuwa tukihimiza umuhimu wa kuwa na majina na nembo katika karatasi lakini msimamo wa serikali umekuwa ni kukataa kwa sababu mbalimbali. Lakini hivi karibuni, niliwapa pendekezo mbadala ya kwamba majina ya wagombea yasibandikwe nje pekee kama kanuni zinavyoelekeza bali Ofisi ya Waziri Mkuu itoe maelekezo kwa wasimamizi wote majina yabandikwe pia ndani karibu na eneo ambalo mpiga kura atasimama kuandika majina yake.

Haiingii akilini kwa uchaguzi ambao; kwa upande wa mijini ambapo nafasi zinazogombewa ni saba; Mwenyekiti wa Mtaa na Serikali yake yenye wajumbe Sita; eti mpiga kura aingie ndani akiwa amekumbuka majina kamili ya wagombea wote akayaandike mwenyewe kwa ukamilifu wake; na kwamba makosa yanafanya kura inakuwa imeharibika.

Kichekecho zaidi ni vijiji ambapo pamoja na Mwenyekiti, Halmashauri za Vijiji huwa na wajumbe kati ya 15 mpaka hata 25; Je, unaweza kukariri majina kamili ya watu wote hao halafu akapewa karatasi tu ndani ukayaandike? Mfumo huu wa kura; unafanyika katika nchi ambayo asilimia kubwa ya wananchi hawajui kusoma na kuandika!

Hivyo ndiyo vituko vya uchaguzi huu; na kwa kweli matokeo ya uchaguzi hayawezi kuwa kiashiria kamili cha matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 ambayo mfumo na utaratibu wake ni tofauti kabisa. Tufuatilie tuone!

No comments: