Monday, March 28, 2011

Mbunge Awasilisha Hoja Binafsi Kuhusu Uvamizi wa viwanja vya Wazi

Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika amewasilisha hoja binafsi kuhusu uuzwaji/uvamizi wa viwanja vya umma maarufu kama viwanja vya wazi kwenye baadhi ya kata za jimbo hilo katika manispaa ya Kinondoni.

Mnyika amewasilisha hoja hiyo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Rafael Ndunguru tarehe 21 Machi 2011 kwa ajili ya kujadiliwa katika mkutano ujao wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni.

Kwa mujibu wa sheria na kanuni wabunge ni wajumbe wa mabaraza ya madiwani ya halmashauri wanazotoka, hivyo Mnyika kwa nafasi yake ya mbunge wa jimbo la Ubungo ni mjumbe wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni.

Mnyika amewasilisha hoja binafsi hiyo kwa mujibu wa kanuni ya 19 ya Kanuni za kudumu za Halmashauri na kanuni nyingine husika.

Katika kipindi cha kati ya mwaka 2005 mpaka 2010 pamekuwepo malalamiko mbalimbali ya wananchi kuhusu uvamizi ama uuzwaji wa viwanja vya umma maarufu kama viwanja vya wazi katika maeneo ya kata mbalimbali za jimbo la Ubungo.

Kutokana na malalamiko hayo Mnyika na viongozi wengine wamekuwa wakitoa shinikizo kwa serikali kuweza kuchukua hatua za haraka ikiwemo kwa kuweka hadharani baadhi ya taarifa za uuzwaji ama uvamizi wa viwanja vya umma.

Kutokana na msukumo huo wa umma tarehe 24 May 2010 Rais Jakaya Kikwete wakati akifanya majumuisho ya ziara ya kukagua hali ya maji katika mkoa wa Dar es Salaam alikiri kuwa yapo maeneo mengi ya wazi yaliyovamiwa na kuwa madiwani wanahusika na sakata hilo.

Kufuatia kauli hiyo ya Rais na malalamiko ya umma aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati huo William Lukuvi alitembelea Manispaa ya Kinondoni tarehe 15 Juni 2010 na kubaini mapungufu kadhaa ya kiutendaji kuhusiana na masuala ya ugawaji wa ardhi yakiwemo maeneo ya umma yaliyozoeleka kuitwa viwanja vya wazi.

Baada ya ziara hiyo Mkuu wa Mkoa aliunda kamati maalumu tarehe 18 Juni 2010 ya kuchunguza maeneo yote ya wazi yaliyovamiwa katika mkoa wa Dar es Salaam.

Taarifa ya tume hiyo ilibaini kuwa Manispaa ya Kinondoni inaongoza kwa kuwa na maeneo mengi ya wazi yaliyovamiwa. Maeneo hayo yanahusisha pia viwanja vya wazi katika kata mbalimbali za jimbo la Ubungo ambalo lakini ripoti kamili haijawahi kuwekwa hadharani isipokuwa Mkuu wa Mkoa alitoa tu muktasari wa baadhi ya mambo katika ripoti hiyo; ripoti nzima kwa ujumla wake imefanywa kuwa siri mpaka hivi sasa.

Katika hoja yake Mbunge Mnyika ameelezea kwa kina aina ya uvamizi au uuzwaji wa viwanja vya wazi na kutaka hatua mahususi za kuchukuliwa ambazo ataziweka hadharani wakati wa kuwasilishwa kwa hoja hiyo.

Baadhi ya Viwanja ya wazi/umma ambavyo vimevamiwa au kuuzwa kinyemela katika kata za jimbo la Ubungo ni pamoja Kiwanja Na. 1022 Kitalu E Sinza; Eneo karibu na kiwanja Na. 636 Kitalu E Sinza; Kiwanja Na. 814, 818 Sinza Block D; Eneo jirani na viwanja Na. 75 na 77 Sinza Block D; Eneo lililopo mkabala na kiwanja Na. 475 Sinza B Eneo karibu na kiwanja Na. 23 Sinza C; Eneo karibu na kiwanja Na. 24 Sinza C; Eneo karibu Na. 765, 789, 790, na 797 Sinza C; Eneo la wazi lililozungukwa na viwanja Na. 21, 23, 25, 27, 29 Sinza B; Eneo la wazi lililozungukwa na viwanja Na.72-74.; Eneo la wazi linalozungukwa na viwanja Na. 1, 2, 89, 90, 141 na 142 Sinza E; Eneo la kiwanja cha michezo na Shule ya Msingi Sinza E; Eneo la wazi jirani na viwanja Na. 77, 79, 81, 151-154; Viwanja Na. 9 na 10 Sinza A; Kiwanja Na. 846 Sinza A. ; Jirani na viwanja Na. 18 na 19 Mtaa wa Malala Makurumla; Jirani na viwanja Na. 73, 78, 80, 82, 84 na 86 Mtaa wa Mengo Makurumla; Eneo la wazi lililopo Mtaa wa Kagera Makurumla ; Eneo la wazi nyuma ya Ubungo terminal (“buffer zone” ya reli); Eneo lipo jirani na kiwanja Na. 148; Nyuma ya jengo la RUBADA na viwanja vingine vya kata zingine za jimbo la Ubungo kwa kadiri ya ripoti ya Kamati/Tume iliyoundwa na Mkoa wa Dar es salaam na taarifa za nyingine.

Itakumbukwa kwamba Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika alishiriki ziara ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof Anna Tibaijuka na viongozi na watendaji wa mkoa wa Dar es salaam iliyofanyika tarehe 14 Disemba 2010.

Mnyika alishiriki ziara hiyo kama sehemu ya kuunga mkono jitihada za kuhakikisha maeneo ya matumizi ya umma (ambayo yamezoeleka kuitwa viwanja vya wazi )yanalindwa na kuendelezwa.
Katika ziara hiyo Mnyika alimpongeza Waziri kwa kuamua kuanza kulifuatilia suala la viwanja vya umma vilivyovamiwa ama kuuzwa kinyemela kwa kuwa ni ajenda ambayo hata yeye kama mbunge wananchi wa jimbo lake la Ubungo walimtuma kuisimamia.

Mnyika alitoa mwito kwa Wizara husika na mamlaka za Mkoa wa Dar es salaam kuiweka wazi ripoti ya tume iliyoundwa mwaka huu kuchunguza kuhusu maeneo ya wazi (maarufu kama Tume ya Lukuvi) ambayo mpaka sasa imegongwa muhuri wa siri.

“Ripoti hiyo ikiwekwa wazi, hatua stahili zinaweza kuchukuliwa kwa haraka zaidi kurejesha maeneo husika kwa matumizi ya umma na kuchukua hatua kwa wote waliotoa vibali vya ujenzi kinyemela ama hati za viwanja kinyemela na kuuza viwanja husika katika mazingira yenye tuhuma za ufisadi”.

Aidha Mnyika alimuomba Waziri wa Ardhi kutembelea pia viwanja vya umma vilivyovamiwa katika jimbo la Ubungo kwenye kata ya Sinza, Makurumla pamoja na maeneo yenye migogoro ya ardhi ili hatua za haraka zaidi ziweze kuchukuliwa. Waziri alikubali ombi hilo na kuahidi kutembelea maeneo husika katika ziara zake za baadaye.

Siku hiyo hiyo ya tarehe 21 Machi 2011 wakati Mnyika akiwasilisha hoja binafsi kwa mkurugenzi kuhusu viwanja vya umma kwa upande mwingine Waziri wa Ardhi, Profesa Anna Tibaijuka amemuomba Rais Jakaya Kikwete wakati alipotembelea Wizara yake kumkingia kifua katika kurejesha viwanja vilivyoporwa.

2 comments:

Anonymous said...

Looh asante Mh. John kwa jitihada hizi ulizozianzisha manake huku Sinza ni kero hasa. Naomba kuripoti juu ya eneo la wazi karibu na kiwanja namba 215 Sinza C ambacho nacho kimevamiwa na kujengwa kagorofa na tajiri mmoja. Thanks

Anonymous said...

ndugu mheshimiwa mbunge wa ubungo samahani sana mimi ni donard bundu kennedy naomba sana mh, kuna mbuge mmoja wa kwimba ana taka kurubuni watu hasa sisi vijana kuwa anataka kutokopesha sasda mimi kama mwenyekiti wa kikundi sijaridhika na hiyo ajenda yahuyu mbunge wa kwimba mimi niko mwanza maeneo ya mwanza hotel nakutakia kazi njema mh,naomba namba yako mheshimiwa ili tuwe tuna chati.