Tuesday, March 1, 2011

Taarifa ya Mkutano wa Mbunge na Wananchi Goba

TAARIFA YA MKUTANO WA MBUNGE WA JIMBO LA UBUNGO NA WANANCHI W A KATA YA GOBA TAREHE 27/02/2011.

Utangulizi
Mnamo tarehe 07/02/2011 Mbunge wa Jimbo la uchaguzi Ubungo aliziandikia mamlaka za kiserikali barua yenye kumb: OMU/UW/002/2011 kutoa taarifa kuwa atakuwa na mkutano wa hadhara wa kiserikali katika kata ya Goba eneo la Mwembemadole tarehe 27/02/2011 kuanzia saa tisa alasiri hadi saa kumi na mbili jioni.

Lengo la mkutano tajwa lilikuwa kuzungumza na wananchi kuhusu mambo mabalimbali ya kimaendeleo hususani sekta za Maji, Ardhi, Umeme, Barabara pamoja na ulinzi na usalama.

Mkutano huo ulifanyika kama ulivyokuwa umepangwa na kuhudhuriwa na Afisa Mtendaji wa Kata ya Goba, Diwani wa Kata ya Goba, Diwani wa viti maalumu wa Kata ya Goba pamoja na mwenyekiti wa mtaa wa Goba.

Ufunguzi
Afisa Mtendaji wa Kata ya Goba alifungua mkutano saa 9:25 alasiri na kumkaribisha Diwani wa Kata hiyo Mh. Kisoki ili aweze kutoa nasaha na maelezo kwa ufupi kabla ya kumkaribisha Mbunge. Diwani alitoa maelezo ya awali kama ifuatavyo;
Diwani alimshukuru Mbunge wa kuitisha Mkutano na wananchi ambao ndio mkutano wa kwanza kufanyika kwenye kata ya Goba toka uchaguzi wa mwaka 2010 na kutumia fursa hiyo kumshukuru wananchi kwa kumchagua yeye pamoja na mbunge.
Usafiri; alisema lipo daraja la kuunganisha Goba na Makongo ambapo tayari mkandarasi DEL MONTE amekwisha kuteuliwa ili ujenzi uanze.
Ulinzi na Usalama; wamewasiliana na polisi ili kuwe na uwezekano wa kujenga kituo cha polisi na wakapewa kazi ya kutafuta eneo ili kituo kijengwe. Eneo limepatikana ingawaje nusu ya shamba hilo lina kesi na wanafanya utaratibu wa kuanza kutumia sehemu ambayo haina kesi ili kuanza ujenzi. Alisema pia wanafanya mchakato wa kujenga vituo vidogovidogo ili kuweza kuboresha ulinzi kulingana na jiografia ya eneo la Goba ambayo ni kubwa mno.

Ardhi; alimuomba Mbunge kubeba swala la fidia kwa wananchi kwa wale ambao maeneo yao yanapitiwa na miradi hasa ya barabara kwa sababu swala hilo lineleta migogoro baina ya wananchi na mamlaka za kiserikali. Na pia alimuomba Mbunge kusemea barabara ya Mbezi Luis Tangi Bovu kupitia Goba ijengwe kwa kiwango cha lami. Pia Kata ya Goba ina mapori mengi sana na pindi wananchi wanapotaka kuyatumia wanaambiwa kuwa yanamilikiwa. Hivyo Diwani alimuomba Mbunge kufuatilia hilo ili pale inapowezekana wananchi wajue ni maeneo gani ambayo wanaweza kuyatumia.

Maji; Diwani alitoa taarifa kuwa Kata ya Goba miradi ya maji mitatu na tayari mradi wa Goba-Kisauke umekamilika kwa kuwa tank limeshajengwa na maji yataanza kuingia usiku wa siku hiyo na tatizo lililopo sasa ni miundombinu kwa ajili ya usambazaji. Mradi wa maji Goba alisema wenyewe unaendelea kuhudumia wananchi. Lakini kamati iliyokuwepo ilishamaliza muda wake na ilishindikana kuivunja kutokana na uchaguzi na pia zipo kazi ambazo zilikua hazijakamilika. Alisema kuwa tayari walishawatangazia wananchi kuwa wateue wawakilishi wawili kila mtaa ili waweze kuingia kwenye kamati ya maji kwenye kikao cha tarehe 06/03/2011.

Baada ya maelezo/ taarifa hiyo Diwani alimkaribisha Mbunge, lakini baada ya kuwasalimia wananchi aliomba kwanza isomwe risala ya wananchi ndipo ataweza kuhutubia wananchi katika mkutano huo.

Risala ya wananchi

Risala ya wananchi ilisomwa na Bw. Dickson mbele ya Mbunge, viongozi wengine pamoja na wananchi . Pamoja na mambo mengine risala hiyo ilijikita kwenye kero sugu ya maji ambayo lawama kubwa ilipelekwa kwa kamati ya muda ya mwaka 2007.

Malalamiko ya wananchi kupitia risala yao ni kama ifuatavyo;

Kwamba kuna unyanyasaji katika upatikanaji wa maji kwa kuwa kuna ubaguzi katika mgawanyo wa huduma hii pale inapopatikana na kwa ujumla kuna upendeleo kwa kuwa kuna wafanyabiashara wa matofali wanapata maji ya kumwagilia matofali huku wananchi wakiendelea kutaabika.

Kuhoji utendaji wa kamati ni kikwazo kwa wananchi, hii inatokea pale baadhi ya wananchi kusingiziwa tuhuma za kuweka sumu kwenye maji ya mradi pale wanapojaribu kuhoji utendaji wa kamati ya maji au wanapoikosoa.
Pia wananchi walisema kuwa kamati ya maji iliyopo sio halali kwa kuwa ilikuwa ni kamati ya muda ilipoundwa mwaka 2007 na kuamriwa kutoa ripoti yake kwa wananchi lakini kamati hiyo haikufanya hivyo toka kipindi hicho mpaka leo.

Pia kuna njama kati ya Dawasco na watendaji wa kamati iliyopo katika kudanganya kiwango cha maji ya kinachotumika swala ambalo linafanya kiwango cha maji kinachotumika kwa mujibu wa mita za Dawasco kuwa tofauti na hali halisi ya maji yanayowafikia wananchi na maji wanayotumia.

Pia kamati hii haina akaunti maalumu ya mradi huu kitu ambacho kinafanya Mwenyekiti na Katibu wa mradi huu kuwa na akaunti ya pamoja ambayo siyo ya mradi. Na wananchi wana mashaka na utendaji wa watu hawa.
Mambo mengine yaliyozungumzwa na wananchi katika risala yao ni pamoja na haja ya kuwa na barabara ya kiwango cha lami pamoja na barabara za mitaa na pia walidokeza kuwa swala la salama linahitaji kupewa uzito wa uwajibikaji kwa kuwa katika kayo kuna changamoto nyingi sana za kiusalama.

Pendekezo : Msomaji wa risala alimalizia kwa kusema kuwa umma uliopo katika mkutano huo ndo uamua kuhusu mapendekezo.

Baadhi ya wananchi walitoa maoni yao baada ya risala hiyo kama ifuatavyo;

i. Wananchi wa Goba wawe kitu kimoja katika kutetea maswala mbalimbali ya kimaendeleo na kuzingatia kwa umakini yale yaliyoainishwa kwenye risala hiyo ya wananchi.

ii. Walimuomba Mbunge kushirikiana na wananchi awaongoze ili kuivunja kamati ya maji ya mradi wa maji Goba na kupata kamati nyingine.


iii. Kusiwe na itikadi za kisiasa katika maendeleo ya watu.

iv. Wajumbe wa kamati ya maji wasichaguliwe kwa mfumo diwani amependekeza kwa kuwa tayari wananchi hawana imani, jambo hilo limetamkwa baada ya mbunge kuitisha mkutano na wananchi kabla ya hapo hakukuwa na dhamira hiyo.


v. Mradi wa maji usiwe ni mali ya watu wachache kwa kuwa ulikuwa ni msaada kutoka shirika la Japan la JICA kwa hiyo inabidi watu wote bila kujali itikadi wanufaike nao.

vi. Kamati ya uchunguzi iundwe ili kubaini ukweli wa tuhuma za kamati ya maji iliyopo ili hatua za kisheria zichukue mkondo wake. Aidha chombo chochote kitakachoundwa kutekeleza mradi kiwe na chombo kingine juu yake kama bodi kwa ajili ya usimamizi.


Hotuba ya Mbunge
Mbunge aliwashukuru wananchi kwa umoja wao kwa kumchagua kuwa mwakilishi wao katika Bunge na pia aliwashukuru kwa kuitikia mwito na kuhudhuria katika mkutano huo muhimu.

Pili alimshukuru Diwani pamoja na viongozi wa kiserikali kushiriki katika mkutano huo na akawaahidi ushirikiano wake wa karibu kwao katika mambo mbalimbali ya kiutumishi.
Alianza kwa kugusia mambo mbalimbali kama ifuatavyo;

Barabara; alisema kuwa amejenga hoja katika kikao cha bodi ya barabara ili barabara ya Mbezi Luis kupitia Goba itajengwa kwa kiwango cha lami ili kuendana na mradi wa mabasi yaendayo kasi ili kuinusuru barabara ya Morogoro na foleni. Alisema kwamba upembuzi yakinifu wa barabara hiyo umekwishanyika isipokuwa tathmini ya fidia bado haijafanywa. Aliomba uongozi wa kiserikali kutoa ushirikiano kwa maafisa watakaofika maeneo yao kutathmini mali za wananchi zitakaoathiriwa na ujenzi wa barabara hiyo. Kuhusu barabara zinazounganisha mitaa Mbunge alimshauri Diwani kuliongelea hilo kwenye vikao vya WDC ili baadae iende Manispaa na akaahidi kuchangia pale atakaombwa kufanya hivyo.

Kituo cha Polisi; alisema kuwa RPC wa Mkoa wa kipolisi Kinondoni alikubali kuhusu ujenzi wa kituo cha polisi akaagiza litafutwe eneo. Na kwa kuwa Diwani amesema eneo limepatikana aliahidi kuwa baada ya kupata specifications atajitahidi kulifuatilia ili kazi ujenzi ianze haraka.

Umeme; kuhusu mtaa wa Matosa ambao bado hakuna umeme alisema kuwa amewasiliana na Waziri wa Nishati na madini na alimuahidi kuwa kwenye mwaka wa wa fedha ujao fedha zitatengwa kwa ajili ya kusambaza umeme katika mtaa huo.

Maji; alijikita sana kwenye swala la maji kwa kuwa alipokea malalamiko mengi sana kutoka kwa wananchi na mengi yaligusa mradi wa maji Goba yaani GOBA WATER USERS ASSOCIATION. Na kwa maana hiyo alishauri kuwa mjadala unahitajika ili kufikia maazimio kuhusu mapungufu ya mradi huo kama ulivyoibuliwa na katika risala ya wananchi pamoja na wananchi wengine waliotoa maoni katika mkutano huo. Kwa miradi mingine alishauri wananchi kuishughulikia kwa karibu ili kuelewa mienendo yake kwa manufaa ya watu wote.

Kuhusu kuvunja kamati ya maji; alisema yafuatayo;
Kuwa kimamlaka yeye hana uwezo wa kuvunja kamati, uwezo huo upo kwa wananchi wenyewe wakiamua kufanya hivyo.

Alitoa angalizo kuwa binafsi hapendi kufanya mambo kwa haraka na akashauri kuwa swala hilo lisiwe kwa haraka ili kuwe na ufanisi wa kupata kamati mpya.

Pia alishauri kuwa mapendekezo ya ripoti ya ukaguzi ya mradi wa maji ya 2007 (ambayo aliigawa siku hiyo kwa wananchi) yazingatiwe.

Uamuzi wa kuvunja kamati iliyokuwepo tarehe 06/03/2011 ulipingwa na wananchi katika mkutano huo, na mbunge alifafanua kuwa kimsingi uhalali wa kamati ya mwanzo ulishapotea toka awali (ab initio) kwa kuwa ilipewa muda maalumu ambao ulishapita toka mwaka 2007

Pia aliasa kuwa swala la maji katika Kata hiyo lisipotafutiwa ufumbuzi linaweza kuhatarisha amani na utulivu katika maeneo hayo. Hivyo inatakiwa ufumbuzi wa haraka kuhusu utatuzi wa swala hilo na la kudumu.

Alishauri pia iundwe kamati ndogo ya wajumbe wanne na kila mtaa utoe mjumbe mmoja. Na baada ya hapo kamati hiyo ndogo itashirikiana na Afisa Mtendaji ili kuandaa mkutano wa tarehe sita ili kupata wajumbe wengine wane na pia kujadili ripoti ya kamati iliyokuwepo. Mbunge ameahidi kuhudhuria katika mkutano huo.



Maazimio
Baada ya hotuba ya mbunge mkutano huo kwa pamoja ulifikia maazimio kama ifuatavyo;

i. Kuwa kamati ya maji iliyopo ivunjwe na wananchi wenyewe.

ii. Wajumbe wanne wachaguliwe ili kuandaa mkutano wa tarehe 06/03/2011 kushirikiana na Afisa Mtendaji wa Kata ya Goba ili kupata kamati kamili.


iii. Kuwa iundwe timu ya uchunguzi ili kuchunguza tuhuma za kamati iliyokuwepo ili kubaini ukweli wa mambo na hatimaye hatua za kisheria zichukuliwe.

iv. Kamati iliyomaliza muda wake ilete ripoti yake iletwe kwenye mkutano wa tarehe 06/03/2011 na ijadiliwe siku hiyo na wananchi.


v. Wajumbe waliochaguliwa ni wafuatao;

a. Monica Modestus Kimario- Mtaa wa Goba

b. Leonard Haule- Mtaa wa Matosa


c. Dickson Luyela- Mtaa wa Kinzudi

d. Nickson Mbando-Mtaa wa Kulangwa

Hadibu za rejea

Kamati ndogo iliyoundwa ilitakiwa kufanya yafuatayo;

i. Kamati ishirikiane na Afisa mtendaji wa Kata ili kuandaa mkutano wa tarehe 06/03/2011.

ii. Kamati hii iandae ripoti yake na itajadiliwa katika mkutano ujao.

iii. Mkutano huo wa tarehe 06/03/2011 uwe na ajenda ya kupokea taarifa kutoka kamati iliyomaliza muda wake.




Mwisho
Mbunge wa Jimbo la Ubungo aliwakaribisha Afisa Mtendaji, Diwani, na Diwani wa viti maalumu kuongea maneno machache kwa ajili ya kufunga mkutano.
Mwisho kabisa Mbunge aliwashukuru wananchi kwa kuhudhuria katika mkutano huo na aliwaomba tena kujitokeza kwa wingi katika mkutano wa tarehe 06/02/2011 ili kupata kamati kamili ya maji.

2 comments:

Unknown said...

Nothing good like a patispatory leadership...that is the way to make assesment from a Micro point...Conglatulations Kaka.

sam2net said...

Well done brother.