Tuesday, June 21, 2011

Mbunge awataka DAWASCO kutoa maelezo kuhusu kero ya maji

MBUNGE AWATAKA DAWASCO KUTOA MAELEZO KUHUSU HATUA AMBAZO WAMEZICHUKUA KATIKA KUSHUGHULIKIA MATATIZO YA UPATIKANAJI WA MAJI KATIKA MAENEO MBALIMBALI YA JIMBO LA UBUNGO

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ameandikia barua Kampuni ya Maji Safi na Maji taka Dar es salaam (DAWASCO) kuwataka kutoa maelezo kuhusu hatua ambazo wamezichukua katika kushughulikia matatizo ya upatikanaji wa maji katika maeneo mbalimbali ya jimbo la Ubungo.

Mnyika amesema kwamba iwapo DAWASCO haitatoa maelezo mapema ataeleza hatua za kibunge ambazo atazichukua ili kuhakikisha kampuni hiyo inatimiza wajibu wa kushughulikia kero ya maji katika kata mbalimbali za jimbo hilo.

Ifuatayo ni nukuu ya baadhi ya maelezo yaliyo katika barua ya Mbunge kwa DAWASCO:
“Tarehe 19 Januari 2011 niliiandikia barua ofisi yako yenye kumbu. Na. OMU/ MJ/004/2011 kuwaalika DAWASCO kuja kushiriki na kutoa mada katika Kongamano la Maji Jimbo la Ubungo; hata hivyo hakuna mtendaji yoyote toka ofisi yako aliyefika kutimiza wajibu husika wala barua tajwa kujibiwa.

Tarehe 15 Machi 2011 niliandika tena barua kwa ofisi yako kuwasilisha Ripoti ya Kongamano husika na kutoa mwito kwa hatua kuchukuliwa; hata hivyo ofisi yako mpaka sasa haijaeleza hatua ambazo imechukua au walau kutambua kupokea ripoti husika.
Tarehe 27 Februari 2011 na tarehe 6 Machi 2011 nilifanya mikutano na wananchi katika kata ya Goba kuhusu maji; pamoja na kuwa mradi katika eneo hilo uko chini ya wananchi vielelezo vilitolewa vya malalamiko ya muda mrefu kutaka hatua kuchukuliwa na DAWASCO kuhusu uharibifu wa mita na pia mapendekezo ya kutaka huduma katika eneo husika kutolewa na DAWASCO moja kwa moja.

Tarehe 26 Machi 2011 nilifanya ziara kata Kata ya Makuburi katika Mitaa ya Makoka, Muongozo na Kibangu na kubaini kwamba wananchi wa maeneo husika wamekuwa na ukosefu wa maji kwa miezi kadhaa hata katika maeneo ambayo hapo awali yalikuwa yakipata maji na hivyo kutoa mwito kwa DAWASCO kuchukua hatua za haraka.

Tarehe 7 Mei 2011 nilifanya ziara kata ya Kimara na kubaini kwamba ujenzi wa visima katika mitaa iliyoanishwa na DAWASCO kwa mujibu wa ahadi ya Rais Kikwete ya tarehe 24 Mei 2010 haujakamilika kwa maeneo mengi.

Tarehe 8 Mei 2011 nilifanya ziara katika kata za Mbezi na kubaini upungufu mkubwa wa maji wakati kukiwa na upotevu wa maji katika maeneo ya Msigani.

Tarehe 22 Mei 2011 nilifanya ziara katika kata za Mabibo na Manzese na kubaini ukosefu wa maji katika maeneo ambayo yalikuwa yakipata maji awali ikiwemo upungufu wa maji katika magati ya DAWASCO.

Tarehe 29 Mei 2011 nilifanya ziara kata ya Saranga na kubaini malalamiko ya muda mrefu ya wananchi kuhusu kero ya maji ikiwemo kutokujulikana ama kutokufuatwa kwa ratiba ya mgawo wa maji.

Aidha katika kipindi husika nimepokea barua toka wateja na wananchi kuhusu maombi mbalimbali ambayo wameyawasilisha kwenu bila hatua stahiki kuchukuliwa au walau kupatiwa majibu kwa ukamilifu.

Mathalani maombi ya kuunganishiwa maji ya wananchi wa eneo la Burula (katika barabara ya Kimara Suca kuelekea Golani- barua yao ya tarehe 9 Agosti 2010), Mbezi Msakuzi (Hatua za utekelezaji baada ya barua ya DAWASCO/WSP/187/Vol III/42 ya 25/03/2009; Wananchi wa Msigani kwa ajili ya Wakazi wa kwa Mjanja ( Barua ya S/M/MSG/KN/001/2011 ya tarehe 10/01/2011 ambayo ilieleza mapendekezo yao mahususi kuhusu hatua zinazopaswa kuchukuliwa na kuomba mkutano kati yao na DAWASCO ili kujadili maombi yao), Wananchi wa Malambamawili (kwa barua yao SM/MSG/MWL/KN/DWSC/02/2011 ya tarehe 3/2/2011).

Naelewa kwamba utatuzi wa kero ya maji katika Mkoa wa Dar es Salaam ikiwemo jimbo la Ubungo unahitaji hatua za muda mrefu, muda wa kati na muda mfupi. Hata hivyo, zipo hatua ambazo zingeweza kuchukuliwa kwa haraka kuhusu mapendekezo yaliyotolewa na wananchi katika Kongamano na pia maombi ambayo yamewasilishwa DAWASCO bila kupatiwa majibu yoyote.

Nataka kupatiwa maelezo kuhusu shughuli ambazo zimetekelezwa na DAWASCO katika kipindi cha kuanzia mwezi Januari 2011 mpaka Mei 2011 katika kuboresha upatikanaji wa maji kwenye maeneo mbalimbali ya jimbo la Ubungo ikiwemo kuelezwa hatua mahususi ambazo zimechukuliwa kufuatia ripoti ya Kongamano na barua za wananchi.”

Pamoja na kuwa zipo hatua ambazo zimefanyika katika kupunguza kero ya maji katika maeneo kadhaa ya Jimbo la Ubungo kufuatia Kongamano la Maji lililoitishwa na Mbunge tarehe 31 Januari, 2011; bado hali kwa ujumla wake hairidhishi suala ambalo limemfanya Mbunge kutaka maelezo ya kina kutoka DAWASCO kama sehemu ya kutimiza wajibu wake wa kusimamia serikali.

Imetolewa tarehe 14 Juni 2011:

Aziz Himbuka
Katibu Msaidizi
Ofisi ya Mbunge Ubungo

3 comments:

Anonymous said...

dawa yapo ni kuwashitaki hivi hivi kwenye public court...mpaka kieleweke

Anonymous said...

Ni kweli mkuu,
Haiwezekani haki yetu kisha tuibembeleze, Lazima watupe hayo maji, kama hawataki waseme

Anonymous said...

Mi ni mwananchi wa Goba, wananchi wengi wanauliza, kile kikao chako cha mwisho Diwani wetu aliahidi, Kujenga Daraja linaunganisha Makongo na Goba na alisema mkandarasi alishapatikana na kazi itaanza mapema, lakini mpaka sasa kimya.

Alizungumzia kuwa Kituo cha polisi mpaka leo hamna kinachoendelea na wanchi wanauliza kama mtefunya wajinga au ?

Ishu ya tatu alisema tank la maji limesha jengwa na sasa tutapata maji kupitia tegeta B, lakini mpaka sasa kimya, wananchi nao wanauliza pia.

Mwisho wanaulizia swala barabara, mwaka huu tupo kwenye mpango wa rami,

OMBI LETU, KUNA TIMU YA GOBA-HAM UNITED HATUNA JEZI TULIKUWA TUNAOMBA MSAADA KUTOKA KWAKO. PIA TUNAOMBA UANZISHE MNYIKA CUP

MHESHIMIWA TUNAOMBA MAJIBU KWA HAYO MAOMBI NA MASWALI YETU