Friday, June 17, 2011

Mchango wangu Bungeni kuhusu Mpango

MCHANGO WANGU BUNGENI TAREHE 14 JUNI WAKATI WA KUJADILI RASIMU YA MPANGO WA TAIFA WA MIAKA MITANO

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii ya kuwasilisha mapendekezo ya mabadiliko ya kwenye Mpango kwa mujibu wa Kanuni ya 57 na Kanuni ya 58 ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Katiba yetu, Ibara ya 63, Bunge ndiyo chombo kikuu kwa niaba ya wananchi chenye wajibu wa kuishauri na kuisimamia Serikali na katika kutekeleza wajibu huu, Ibara ndogo ya (3) inatamka kwamba, kazi mojawapo ni kujadili na kupitisha mipango ya muda mfupi na muda mrefu na huu ndiyo wajibu tulionao mbele hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza kwenye maeneo mahususi ambayo nimewasilisha mabadiliko ambayo nitaomba yazingatiwe kwa mujibu wa Kanuni ya 57 na 58 kwenye hoja iliyo mbele yetu. Kwanza ni eneo ambalo liko ukurasa wa 117 wa nyaraka hii wa mpango wa miaka mitano. Hili ni eneo linalohusu miradi ya maji, sababu ya kuwasilisha mabadiliko haya ni kwamba huko nyuma kumekuwepo na miradi ya maji ikiwemo miradi mbalimbali katika Jimbo ambalo wamenituma kuwawakilisha la Ubungo. Miradi ambayo ilihusisha ulazaji wa mabomba ambayo yanajulikana zaidi kama mabomba ya Wachina, lakini pamoja na mabomba kuwekwa kwa muda mrefu, wananchi wa maeneo mengi sana ukienda King’ong’o, Mbezi, Mavurunza, Makoka na kwingineko. Serikali imetumia pesa nyingi sana ikiwa kiasi kikubwa ni mkopo kutoka Benki ya Dunia, lakini maji hayatoki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa kuna mpango ambao unalenga kuchangia katika kurekebisha kasoro zilizotokea kipindi cha nyuma, lakini mpango wenyewe kama ukiachwa kama ulivyo utarudia kasoro za kipindi cha nyuma na kasoro kubwa iliyoko kwenye mpango huu ni kwamba ukitazama kwenye hilo jedwali la miradi hii ya maji ya Ruvu juu, Ruvu chini pamoja na ujenzi wa mabwawa Kidunda na visima Kimbiji na Mpera ambayo yangeongeza vilevile uzalishaji wa maji Dar es Salaam, yamegawanywa rasilimali zake katika kipindi cha miaka mitano. Kwa hiyo, ukianza utekelezaji mpaka utakapokamilika, kitakachotokea ni kama kinachoendelea sasa Ubungo, mradi wa mabomba wa Benki ya Dunia umewekwa, maji hayafiki, mabomba yameanza kuharibika, miundombinu imeanza kuharibiwa kwelikweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nafahamu, ndani ya Baraza la Mawaziri, ndani ya Serikali, baada ya mijadala ya umma na sisi kule Ubungo tulifanya kongamano la wananchi la maji, Serikali ikaamua kwamba miradi hii ya Ruvu juu, Ruvu chini, ujenzi wa bwawa Kidunda na visima Kimbiji, Mpera ikamilike kwa ukamilifu wake ifikapo mwaka 2013 na Serikali kwa maana ya Rais akatoa kauli, Waziri wa Maji akatoa kauli hadharani, sasa kilichopo kwenye mpango, kinapingana na Kauli ya Waziri na Rais ya kumaliza miradi hii ifikapo mwaka 2013.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu ya mabadiliko kwenye kifungu hiki ili kurekebisha hii hali, rasilimali zilizotengwa hapa kwa mwaka wa fedha 2014/2015 na mwaka wa fedha 2015/2016 zipunguzwe bila kuathiri jumla, zirudishwe nyuma kwenye miaka mitatu ya kwanza na nimewaeleza kwenye mapendekezo ambayo Wabunge mnayo nakala yake, kiwango cha pesa kinachopaswa kuhamishwa ili miradi ikamilike kwa wakati kuepusha hasara kama iliyoko hivi sasa kutokana na mradi wa mabomba ya Wachina na ili kutimiza kauli ya Rais na Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinyume cha mapendekezo haya ni kutengeneza bomu lingine la wakati la kutumia rasilimali nyingi sana, lakini mradi ukachukua miaka mingi kukamilika, miundombinu ikaanza kuharibiwa kabla hata maji kuanza kupatikana. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge hii ni kauli ya Mheshimiwa Rais, Waziri na Wabunge. Humu kuna Wabunge wa Majimbo mbalimbali ili si kwa ajili ya Jimbo la Ubungo tu, kuna Wabunge wa Mkuranga, Kigamboni, Wabunge wote wa Dar es Salaam na Wabunge wa maeneo mbalimbali ambao wanaamini katika usimamiaji wa kauli hizi kwa ukamilifu wake. Kwenye eneo hili nitaomba niishie hapa nihamie eneo lingine la mabadiliko ninayoyapendekeza. Hili lilikuwa linahusu ukurasa wa 147 kifungu cha A.1.4 ambacho kinahusiana na Kifungu cha 3.4.4 cha Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili liko ukurasa wa 127 ambao ni kifungu cha A1.2.2 ambacho kinatokana na Kifungu cha 3.4.1.1 cha kuhusiana na kupunguza foleni Dar es Salaam. Kwa mujibu wa Mpango huu, yale mapendekezo ambayo wadau wamekuwa wakiyatoa na tumekuwa tukiyatoa kwa muda mrefu kwamba ili kupunguza foleni Dar es Salaam, lazima kuwekeza sana kwenye barabara za pembezoni. Humu kuna barabara zimeingizwa, mapendekezo yale yamekubalika, barabara ya kutoka Goba mpaka Mbezi, Mbezi Malambo Mawili mpaka Kinyerezi, Changanyikeni kwenda Chuo Kikuu kupitia Msewe na nyinginezo. Kabla sijasema pendekezo mahususi ambalo liko hapa kuhusiana na hii barabara nyingine, niombe tu katika kutekeleza Mpango huu ili jambo liharakishwe kwa haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo kubwa litalikumba jiji la Dar es Salaam wakati wa utekelezaji wa mradi wa mabasi yaendayo kasi utakapoanza. Barabara ya Morogoro itakapoanza kutengenezewa njia maalum ya mradi wa mabasi yaendayo kasi, foleni ambayo itakuwepo kwenye barabara ya Morogoro, itakuwa ni foleni ya kihistoria kwa sababu barabara ni nyembamba lakini kutaanza construction pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, maamuzi ya kujenga barabara za kuchuja magari, barabara ya kutoka External kupitia Kilungule mpaka Kimara na nyinginezo inabidi yaharakishwe, naelewa kwamba hizi barabara zote zimeshafanyiwa upembuzi yakinifu, nipendekeze katika utekelezaji tathmini ya fidia ufanyike haraka ili zoezi lifanyike haraka kabla ya kuanza kwa ujenzi wa mabasi yaendayo kasi. Lakini kuna hoja mahususi iko hapa mbele ya barabara hii ambayo naomba iingizwe kwenye schedule, barabara ya kutoka Kimara kwenda Mavurunza mpaka Bonyokwa mpaka Segerea. Hii barabara ni muhimu iingizwe kwenye schedule hii niliyoisema ya barabara, katika ukurasa wa 127, kuna orodha ya barabara na hii barabara haipo, iingizwe kwa sababu ni ahadi ya Rais ya tarehe 24 Mei 2010 alivyokwenda kutembelea Mavurunza na alisema kwamba barabara hii ndani ya miaka mitano itajengwa kwa kiwango cha lami ili kupunguza foleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa isipokuwepo kwenye mpango wa miaka mitano maana yake ni kwamba hii ahadi itakuwa ni ahadi hewa. Sasa ninachosema tu hapa ni kwamba, wengine wanachambua, wanasema ahadi zote za ujumla za Rais zinafikia takriban trilioni 95, sasa hizi za hapa jumla ni trilioni kama 42 plus. Sasa ili kupunguza ule mzigo wa lawama kwamba kuna ahadi nyingi ambazo haziko kwenye Mpango, naomba kutoa pendekezo hapa kwa mabadiliko kwamba barabara hii ya kutoka Kimara kupitia Bonyokwa mpaka Segerea ambayo itaunganisha Majimbo haya mawili na kupunguza foleni iingizwe kwenye hii orodha kama ambavyo nimewasilisha kwenye jedwali la mabadiliko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni suala la nishati, Kifungu cha 3.4.1, kuna mambo mengi ambayo tungeweza kuzungumza kuhusu nishati, lakini hapa kuna pendekezo mahususi sana kwenye ukurasa wa 135, kwenye ile miradi ya umeme. Kuna mradi mmoja ambao Mheshimiwa Rais aliuzungumza Bungeni na baadaye aliuzungumza alipotembelea Wizara na baadaye kukatangazwa kuundwa Kamati ya kushughulikia mradi huo, mradi wa Stigler’s Gorge, lakini mradi huu pamoja na kutangazwa kwamba ndani ya miaka hii mitano utekelezaji wake unaanza, mradi huu kwenye miradi ya umeme inayozungumzwa haupo kwenye orodha ya miradi. Kwa hiyo, mabadiliko ninayoyapendekeza hapa ni kwamba, kwa ajili ya uzalishaji mwingi wa umeme wa Taifa letu na huu ni mradi mkubwa sana utekelezaji wa mradi huu, maandalizi yake ya kirasilimali na kifedha uingizwe ndani ya mpango huu wa miaka mitano ili tuweze kuhakikisha kwamba mradi huu unatekelezwa kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni ukurasa wa 112, mabadiliko mahususi yanahusiana na uzalishaji, manufacturing ya Kifungu 3.4.3, lakini hapa narejea kifungu 1.12, kwanza nashukuru kwamba concept ya Special Economic Zone imeingizwa kwenye Mpango. Nitaomba tu katika utekelezaji wake huko nyuma tumewahi kuwa na mipango ya kuanzisha viwanda, tukiondoa hivi viwanda ambavyo vina motisha maalum na Ubungo ni moja kati ya maeneo ambayo yalikuwa industrial area yaani ukizungumza kuhusu viwanda vya Dar es Salaam unazungumza UFI, uzalishaji wa Zana za Kilimo, unazungumza Ubungo Maziwa, uzalishaji wa maziwa, Ubungo Garment, Urafiki na kadhalika lakini viwanda vile vingi vimefungwa, vingine vinafanya biashara tofauti, hatimaye watu wanakosa ajira. Sasa wakati tunafufua vile viwanda tumeanzisha mkakati mwingine wa maeneo maalum ya viwanda likiwemo hili la Benjamin Mkapa Special Economic Zone lililopo pale Mabibo na kule kuna viwanda vinakusudiwa kuanzishwa. Sasa naomba, vitakapoanzishwa vichangie kwenye ajira lakini tufufue viwanda vile vile vilivyokufa ndani ya Jimbo la Ubungo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa kuna hoja mahususi sana ambayo naomba izingatiwe ni sehemu ya 1.1.2 ambapo ndani ya Mpango huu inakusudiwa kama sehemu ya Benjamin William Mkapa Special Economic Zone kujenga bomba maalum la mtaro kutoka eneo la viwanda kupeleka kwenye mabwawa ya kumwaga uchafu yaliyoko pale Mabibo yanaitwa Mabibo oxidization ponds. Sasa naomba hili pendekezo lizingatiwe, hii hoja ni hoja hatari sana. Kwa sababu kwa mtu anayefahamu jiografia ya Dar es Salaam, mabwawa yale ya Mabibo yameshazusha zogo sana kutokana na uchafuzi wa mazingira usio wa kawaida. Sasa hii ni waste ya kawaida tu imezusha zogo, fikiria uwe na eneo la viwanda lenye viwanda zaidi ya kumi, halafu industrial sewage ijengewe bomba lipeleke kwenye mabwawa ambayo yako katikati ya community ya watu ni janga litakalokuja kutokea baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sasa hoja yangu ninayopendekeza hapa ni kwamba, mabadiliko yafanyike kwenye hiki kifungu na nimeandika text ya Kiingereza sitasoma kwa Kiingereza iingie kwenye rekodi rasmi kwa sababu ni nyaraka rasmi, lakini hoja yangu ni kwamba huu mtaro wa maji machafu uelekezwe, uungane na sewage system inayo-service viwanda badala ya kupelekwa Mabibo oxidization ponds na kwa kiwango cha pesa kilichotengwa technicalities, tutazungumza baadaye, ni jambo ambalo linawezekana ili kuepusha hiyo hatari ya baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kwenyewe kuna uchafuzi mkubwa wa mazingira kwenye mto unaoitwa Mto Ubungo pale eneo la Kisiwani kutokana na uchafu wa majitaka kutoka Hosteli za Mabibo kuishia njiani na kumwagwa mtoni badala ya kumwagwa kwenye mabwawa kwa sababu ya huo udhaifu wa mtandao wa sewage system. Kwa sasa kama hali iko hivyo, je, itakuwaje kama industrial waste ikienda kuelekezwa kwenye eneo kama hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nimalizie rekebisho lililoko kwenye ukurasa wa 146, linahusu kifungu cha…

(Hapa kengele ya pili ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iingie kwenye kumbukumbu rasmi kwa sababu nimeshawasilisha kuhusu Chuo cha Butiama ambacho kipo kwenye hotuba ya Waziri kwamba kitajengwa Chuo cha Butiama, lakini kwenye Mpango wa miaka mitano hakipo. Kwa hiyo, naomba kutoa hoja kwamba hicho Chuo nacho kiingizwe kwenye Mpango pamoja na maelezo mengine ambayo nimeyatoa lakini kutokana na Kanuni…

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.

Nakala ya Mabadiliko yaliyosambazwa kwa wajumbe bungeni ikiwa ni sehemu ya mchango wangu inapatikana kupitia: http://mnyika.blogspot.com/2011/06/mabadiliko-ya-mbunge-kuhusu-mpango-wa.html

2 comments:

Anonymous said...

Mkuu naamini pale Loyola hatukukesha bure kulinda kura zako

Anonymous said...

Frm Kagame:

Mh Mbunge, you are just one of ur kind, and nobody of ur kind, u have impressive move. we cant pay u much rather than support n make sure ur strugle NEVER perish like a candle on the wind.