Tuesday, April 5, 2011

SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA MSIBA WA MWANAHABARI ADAM LUSEKELELO NA MHADHIRI DR JUSTINE KATUNZI

Nikiwa safarini kwenda Dodoma naomba kueleza masikitiko yangu kwa vifo vya wakazi wawili wa Jimbo la Ubungo ambao wamekuwa na mchango mkubwa kwa taifa letu kwa namna mbalimbali.

Mosi, ni kifo cha mwanahabari mwandamizi Adam Lusekelo ambaye amekuwa mstari wa mbele kupitia kalamu yake kuhamasisha uwajibikaji katika taifa letu. Marehemu Lusekelo amekuwa akiandika kwa kutumia mfumo wa sitiari (satire) kupitia safu maarufu za “In A Light Touch”, “Eye Spy” nk kadhaa vya habari. Natoa mwito kwa wadau wa sekta husika kumuenzi marehemu Lusekelo kwa kukusanya makala zake na kuziweka pamoja katika kitabu kwa jina lake ili maudhui yake ya ukombozi yaendelee kukumbukwa na vizazi vijavyo.

Pili, ni kifo cha mhadhiri katika Chuo Cha Biashara cha Chuo Kikuu Cha Dar es salaam (UDBS) Dr Justine Katunzi ambaye ametoa mchango katika fani ya utawala na usimamizi wa rasilimali kwa kutoa mafunzo na machapisho mbalimbali.

Natuma salamu za rambirambi kwa familia za marehemu na kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu wawe na moyo wa uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.
Wasalaam,

John Mnyika (Mb)
04/04/2011

No comments: