Friday, April 22, 2011

Barabara Bonyokwa na Daraja Ubungo Msewe

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ametaka hatua za haraka kuchukuliwa kufanya matengenezo ya Barabara ya Kimara Bonyokwa na daraja la Ubungo Msewe kutokana na uharibifu uliochangiwa na mvua zinazoendelea.

Mnyika aliyasema hayo katika kikao cha Kamati ya Fedha na Uongozi cha Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kilichofanyika mapema wiki hii (19/04/2011) katika ukumbi wa Manispaa hiyo.

“ Nimetembelea barabara ya Bonyokwa ambayo ukarabati wake ulipaswa kufanyika mwaka huu wa fedha; hali ni mbaya, magari yanashindwa kupishana na mawasiliano yanaelekea kukatika. Daraja la Msewe linalounganisha kata ya Ubungo na Chuo Kikuu cha Dar es salaam nalo limezolewa kutokana na mvua zinazoendelea. Hivyo, hatua za dharura zinahitajika kuchukuliwa na Halmashauri. Na kutoa mwito kwa mkurugenzi hususani kupitia idara ya ujenzi kwenda katika maeneo husika na kuchukua hatua za haraka”, Alisema Mnyika.

Kutokana na mwito huo, Mkuu wa Idara ya Ujenzi ya Manispaa ya Kinondoni, Mhandisi Uriyo Athanas aliahidi kufuatilia kwa ajili ya hatua stahiki kuchukuliwa.

Mnyika alisema kwamba ujenzi wa Barabara ya Bonyokwa ni kati ya ahadi za Rais Jakaya Kikwete alizozitoa mwezi Mei mwaka 2010 wakati alipotembelea kata ya Kimara na kuitaka Manispaa kufuatilia kwa wakala wa Barabara (TANROADS) ili barabara hiyo iweze kujengwa kwa wakati.

“Katika kipindi hiki ambacho tunasubiria ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami, matengenezo ya dharura kwa kuweka kifusi yanapaswa kufanywa na Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwa kuwa ndiyo yenye wajibu huo”, Alisisitiza Mnyika.

Kwa upande mwingine, Mnyika alisema kwamba ukarabati wa daraja la Msewe ambalo limezolewa na maji ni suala la dharura katika kupunguza foleni katika barabara ya Morogoro kwa kuwa njia hiyo imekuwa ikiwezesha sehemu ya magari kupitia njia ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
Hatahivyo, Mhandisi Uriyo alieleza kuwa hatua hizo za haraka zinapaswa pia kusubiri kupungua kwa mvua ili kuepusha matengenezo yatayofanyika kuathiriwa na mvua za masika zinazoendelea.

Chanzo: Ofisi ya Mbunge Ubungo

Ps: TANROADS wamekubali kufanya matengenezo kwenye daraja husika kwa haraka

No comments: