Wednesday, June 29, 2011

Niliyochangia katika mjadala wa bajeti 2011/2012

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Lakini kwanza niseme tu kwamba nimesikia michango humu Bungeni inayosema mambo mawili makubwa. Kwanza inasema Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani ameiga kutoka mawazo ya Serikali bila kuishukuru Serikali kwa mawazo yake, lakini pili mawazo kwamba CHADEMA kwenye hotuba ya Kambi ya Upinzani haikutekeleza ilani yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba Serikali imeiga mawazo mengi sana kutoka kwa CHADEMA, ni jambo zuri na kwa sababu mawazo haya yako kwenye Ilani ya CHADEMA ya mwaka 2010 na hayapo kwenye ilani ya CCM.

Serikali kwenye hotuba ya Waziri wa Bajeti imezungumza kuhusu mchakato wa Katiba mpya ambayo haipo kwenye Ilani ya CCM, bali iko kwenye Ilani ya CHADEMA na Serikali imeiga, ni vizuri. Serikali imezungumza kuhusu kupunguza gharama za maisha ambayo haijachambuliwa kwa kina kwenye Ilani ya CCM, lakini humu imechambuliwa na CHADEMA imeeleza ni namna gani ambavyo kuna haja ya kupunguza gharama za maisha kwa wananchi.

Serikali imeiga wazo la wingi wa posho na CHADEMA ilizungumza kwa kina sana na kwa takwimu kuhusu ukubwa wa posho na haja ya kuunganisha posho, kupunguza posho na kadhalika ili kuboresha mishahara ya wafanyakazi na kusukuma mbele maisha na wakati huo huo kuweka uchumi sawa.

Hili wazo nalo Serikali imelichukua, lakini imelichukua ndivyo sivyo. Sasa mimi niseme tu kwamba ni vizuri watu wakawa wanasoma ilani za vyama vingine ili kujua asili ya haya mawazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kumekuwepo na wazo kwamba hotuba ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni haikutekeleza ilani hii. Kuna mambo humu tumeyasema kwenye hotuba ya Kambi na ninaomba tu Serikali iyachukue kwenye bajeti ijayo kama haiingizi sasa ambayo yamo kwenye Ilani na ambayo ni mambo yanayotekelezeka japo awali walisema hayatekelezeki.

Tulisema elimu bure na tulisema bure Kidato cha Kwanza mpaka Kidato cha Sita na tukasema elimu ya juu tunavunja Bodi ya Mikopo, tunatengeneza mamlaka nyingine ya ugharamiaji wa elimu kwa mfumo tofauti.

Kwenye bajeti ya mwaka huu, Msemaji wa Kambi Rasmi ameeleza kwa kina ni namna gani ambavyo tutagharamia elimu kwenye shule za umma za kutwa, ni namna gani watoto wa kike watasoma bure na tumeeleza kwamba yanatekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu jambo lingine la msingi kwamba kuna mambo walikuwa wanasema hayatekelezeki kwamba huwezi kushusha Pay As You Earn kodi ya wafanyakazi mpaka 9%. Sisi tumeteremsha na tunaomba Serikali ikubali hili wazo na tumeonyesha jinsi gani ambavyo linatelekezeka kwa ajili ya kutetea maslahi ya wafanyakazi.

Tumezungumza muda mrefu kwenye Ilani kuhusu haja ya kutoa pension kwa wazee ikasemekana kwamba wazo hili halitekelezeki. Tumeeleza jinsi gani ambavyo suala la kutoa pension kwa wazee wote inawezekana kabisa. (Makofi)

Kwa hiyo, naiomba tu Serikali katika haya mawazo ambayo hayapo katika bajeti ya Serikali na yenyewe katika hitimisho la Waziri ayatolee kauli na kuyaingiza kwenye utekelezaji. Kuna wengine wamesema kwamba bajeti kivuli haijazungumza kuhusu suala la kupunguza gharama za vifaa vya ujenzi na kumwondolea mzigo Mtanzania maskini.

Kuna mchumi mmoja anaitwa Rostow, tatizo ni kwamba bajeti hizi zinaweza zikawa zinasomwa kama vitabu vya A, E, I, O, U, tusome kiuchambuzi wa kiuchumi. Unapozungumza kuinua viwanda ni lazima utengeneze kitu kinachoitwa pre-conditions for take off, kwamba uweke msingi ili uwekezaji kwenye viwanda uende kwa nguvu kubwa zaidi.


Ukiangalia falsafa ya bajeti ya Kambi Rasmi ya Upinzani ambayo mimi naiunga mkono, kwa kweli imejikita katika kuhakikisha gharama za uzalishaji zinapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmezungumza kutaka uwekezaji mkubwa kwenye gesi na hili naomba Waziri katika majumuisho yake alitolee kauli kwa sababu kama Waziri Kivuli wa Nishati na Madini naelewa kwamba ujenzi wa bomba kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam na baadaye Tanga ambao ungepunguza sana gharama za uzalishaji ikiwemo kwenye viwanda hivi vya cement kama cha Wazo Hill pale Dar es Salaam na viwanda vingine, bomba hili Serikali ya China iko tayari kuingiza pesa kwa condition kwamba Serikali ya Tanzania iwekeze bilioni 181 kama 15% ya mtaji. Nimepitia Vitabu vyetu vyote hivi vya Bajeti ya Maendeleo na kadhalika, hiki kitu hakipo. Mimi niwaombe tu kwamba kama tunataka kupunguza gharama za uzalishaji, ikiwemo uzalishaji wa cement lazima tu-invest kwenye gesi na falsafa ya mchango wetu ambao mimi nauunga mkono ni kwamba tulinde viwanda vya ndani, hiyo ndiyo principle. Viwanda vyetu vya saruji, iwe ni Mbeya, Tanga au Dar es Salaam vingeweza kuwekewa mazingira ya kupunguza cost za uzalishaji na kulinda na kumsaidia Mtanzania kwenye ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihamie eneo lingine, mimi siungi mkono bajeti hii iliyo mbele yetu mpaka Serikali itoe maelezo ya kina sana na siungi mkono siyo kwa sababu niko Upinzani, kwa sababu kuna hoja Serikali imeleta nyingi tu hapa katika Mikutano iliyopita nimeziunga mkono, Maazimio yale ya SADC, UNESCO na mambo mengine, lakini hili siungi mkono na siungi mkono kwa sababu wananchi wa Jimbo langu walionileta hapa, wamenituma nisiunge mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Waziri kusoma Hotuba ya Bajeti, mimi niliandika kwenye ukurasa wangu wa mtandao kwamba hotuba hii ya Waziri imejaa matumaini hewa na bajeti ni ya kiini macho na nilisema hivyo kutokana na takwimu za bajeti yenyewe. Ukichukua kwa mfano suala dogo tu la tozo la faini kwa Madereva kwa mfano kwa watu wanaoendesha vyombo vya usafiri, Waziri alisema kwamba faini inapanda mpaka shilingi 50,000, Muswada wa Sheria ya Fedha unasema faini inapanda mpaka shilingi 300,000, Kitabu cha Mapato ya Serikali, Kitabu cha Mapato ukiangalia faini sehemu ya Wizara husika inaonesha Serikali haikusudii kugeuza leseni na faini hizi kama chanzo cha mapato lakini mantiki ya kupandishwa kwa kiwango hiki iko wapi? Madereva wa pikipiki wa Mbezi, Madereva taxi wa Ubungo na watumiaji wengine wa vyombo vya usafiri wa daladala na kadhalika wamenituma katika hili nisiunge mkono bajeti kwa sababu hii unless hiki kitu kiondolewe. Tatizo siyo ukubwa wa faini, faini ya shilingi 20,000 tu sasa hivi iliyopo, ama 40,000 ama ngapi, tatizo ni enforcement ya Sheria, rushwa iliyotapakaa. Kwa hiyo, unapoongeza kiwango cha faini, unaongeza tu kiwango cha rushwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja kwamba, kweli ajali ziko nyingi hata kwenye pikipiki kule Dar es Salaam ajali zinaongezeka sana lakini tufikirie zaidi. Mimi ningeshukuru kama Waziri angekuja na mkakati kwamba sasa tunahakikisha kupitia Chuo cha Usafirishaji pale Dar es Salaam tunatoa mafunzo kwa Madereva pikipiki, Idara yetu ya Traffic inakwenda kutoa mafunzo inafanyaje mambo kama haya, ningetarajia kwamba haya ndiyo yangekuwa kipaumbele. Kwa hiyo, katika hili siungi mkono kwa sababu hiyo niliyozungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii inasema kwamba kipaumbele ni nishati na kadhalika, lakini ni maneno. Nimezungumza suala la bomba la gesi ambalo linahitaji investment ya bilioni 181 na ningeweza kuzungumza mengine lakini kwa sababu nina platform nyingine ya Uwaziri Kivuli nitazungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihamie kwenye eneo lingine la msingi sana ambalo linafanya nisiunge mkono bajeti hii. Bajeti inasema principle kubwa tunakwenda kupunguza gharama za maisha kwa wananchi, tunapunguzaje kwa sababu gharama zetu zinapanda kwa sababu ya nishati ikiwemo mafuta na umeme, basi tunapunguza tozo kwenye mafuta. Kauli hiyo ni kauli ya kiini macho ndiyo maana Waziri alipotoa hoja yake akasema ufafanuzi atautoa tarehe 22 wakati tutakapojadili Muswada wa Sheria ya Fedha, nimeupitia huu Muswada tutakuja kuujadili baadaye, lakini principle ya kukuza tozo haiwezi kusaidia kushusha kwa kiwango kikubwa bei ya mafuta sababu tozo zote za taasisi hizi SUMATRA, TBS changanyanga na EWURA na kila kitu haifiki 3% ni 2.3% tu ya bei ya mafuta. Tozo za makampuni binafsi ya mafuta ni 2% jumla ya tozo zote hazifiki hata 5%. Sababu kubwa ya bei ya mafuta kuwa juu kwenye Taifa letu ni ukubwa wa kodi, asilimia 26 ya bei ya mafuta kwa lita ni kodi, ni takribani shilingi 600. Sasa Muswada huu haujagusa kodi, hotuba haijagusa kodi, vitabu vya mapato havijaigusa kodi kwa sababu hiyo bei ya mafuta itashuka hata Serikali ikijitahidi vipi kati ya shilingi 100 mpaka shilingi 200 ugumu wa maisha utaendelea kuwa pale pale kwa ari, kasi na nguvu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza kuhusu nishati ya gesi ambayo ingetumika majumbani kama LPG, gesi hii kama watu wangeitumia ingepunguza bei ya nishati nyingine. Tunazungumzia kuhusu gesi kutumika kwenye magari ambayo ingeshusha nusu ya nauli Dar es Salaam au nusu ya gharama. Investment kwenye gesi na miundombinu ya gesi siyo bomba tu lile na mitandao ya gesi, vituo vya kujazia mafuta ya gesi na kadhalika ni kama vile imeachiwa TPDC tu peke yake na hiyo retention ya 50% kama tunataka kupunguza gharama za maisha lazima pamoja na kupunguza kodi kwenye mafuta twende kuwekeza kwa nguvu sana kwenye nishati mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inasema tutapunguza gharama za maisha kwa sababu tutapunguza bei ya chakula, tutafungua strategic grain reserve na mambo mengine yamezungumzwa sana humu kwenye hotuba, lakini ni matumaini hewa na kwa fact kama kwenye mwaka huu wa fedha uliomalizika, Serikali imefungua ghala, Serikali ikifungua ghala maana yake mimi na wewe na Mtanzania mwingine tunaingia loss kwa sababu yale mahindi tumeyaweka mle kwenye ghala kwa pesa zetu, ime-inject kwenye soko lakini bei haijashuka. Niwaeleze tu siri moja na Waziri ukitaka nitakuletea taarifa kimaandishi, bei haishuki Manzese pale kwa sababu chakula kinachotolewa hiki cha kutoka katika hii grain reserve watu wanabeba wanakwenda kuuza nje kwa bei kubwa zaidi, kwa hiyo haishushi sembe pale Dar es Salaam, sijui Makurumla sijui wapi sembe haishuki, enforcement iko weak. Kwa hiyo, nitaunga mkono hoja kama haya yatatolewa ufafanuzi wa kina sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti hii kuna mambo humu ya maji, barabara na kadhalika na kwa kwetu sisi Dar es Salaam mtu ukisikia maji, barabara na kwa Ubungo kulivyo na shida ya maji mtu anaweza kusema kwa nini huyu anakataa kuunga mkono bajeti wakati bajeti inazungumza kuhusu maji, barabara, tatizo ni matumaini hewa maana kuna tofauti kati ya maneno na matendo. Ukiingia sasa kwenye Kitabu cha Bajeti cha Maendeleo cha Wizara ya Maji, ile specific section ya Wizara ya Maji, ukiangalie investment ambayo imewekwa pale kwa ujenzi wa bwawa la Kidunda ambayo ingesaidia siyo watu wa Morogoro tu kwa sababu Kidunda iko Morogoro, ingeboresha flow ya maji kwenye Ruvu Juu ambayo inge-service watu wa Ubungo kuanzia Kiluvya, Kwembe na kwingineko, investment ni ndogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija mradi wa Kimbiji na Mpera, Mkuranga na Kigamboni ambao utasaidia vilevile Ubungo na maeneo mengine ya Dar es Salaam, Serikali ilisema hata kwenye Baraza la Mawaziri najua Mheshimiwa Pinda atakubaliana na mimi walisema kwamba sasa tutaingiza pesa za ndani ili tatizo la maji Dar es Salaam liishe, lakini ukiangalia 35 bilioni ni expectation za pesa za nje. Mimi nitaunga mkono hoja tu kama kweli tukidhamiria kwa dhati kutenga rasilimali kwa ajili ya kuboresha hii miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri amesema kwenye hotuba yake kwamba sasa hii bajeti inakwenda kuondoa tatizo la foleni Dar es Salaam, lakini ukipitia bajeti ya Wizara ya Ujenzi kwenye kifungu kinachohusika na decongestion of Dar es Salaam, kupunguza foleni Dar es Salaam, kimetengewa bilioni tano peke yake, sisi wa Dar es Salaam nikiwemo mimi wa Ubungo ambao takribani 80% ya mapato yanatoka kwetu five billion decongestion, 20 billion fly over, siungi mkono hoja mpaka tupate kwanza ufafanuzi wa kina kutoka kwenye Serikali, ahsante. (Makofi)

Chanzo: Hansard-Tarehe 16 Juni 2011 Kikao Cha Sita Mkutano wa Nne

3 comments:

Anonymous said...

Mnyika naunga mkono analysis zako. Its gd u did ur hmwrk kabla ya kuongea. big up.Nyirenda

allen mchaki said...

""ingeboresha flow ya maji kwenye Ruvu Juu ambayo inge-service watu wa Ubungo kuanzia Kiluvya, Kwembe na kwingineko, investment ni ndogo sana.""

Ahsante Mbunge wangu kwa kuigusa Kwembe,maji huku ni shida kuu,HATA MIMI SIUNGI MKONO MATUMAINI HEWA YA CCM;

Simon said...

Asante Mbunge, nami siungi mkono na yote uliyoyaeleza kama waziri ni mwelewa anahitaji akuunge mkono na haraka sana abadilishe mwelekeo wa wizara husika.