Wednesday, August 31, 2011

Salaam za Eid al-Fitr

Nawatakia heri waislamu wote wa jimbo la Ubungo na watanzania kwa ujumla katika kusherehekea sikukuu ya Eid al Fitri.

Aidha nawapongeza waislamu wote ambao waliweka mstari wa mbele usafi wa kweli katika mawazo na matendo katika kipindi chote cha mwezi mtukufu wa Ramadan.

Nawashukuru viongozi wote wa kislamu tulioshirikiana katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadan kwa namna mbalimbali katika kuhamasisha maendeleo ya kiimani na ya jamii kwa ujumla hususani kwa michango katika kufanikisha mashindano ya kuhifadhi Qur’an kwa wanawake kata ya Manzese, ununuzi wa jenereta na ujenzi wa msikiti katika kata ya Saranga.

Nawaomba tuendelee kushirikiana katika kipindi chote cha mwaka kwa kuwa taasisi za dini zina mchango mkubwa katika kudumisha maadili miongoni mwa wananchi na kuchangia katika maendeleo ya nchi kwa ujumla.

Wakati wote kumbukeni Aya 185 Sura 2 (Al Baqara) na maneno mengine matukufu ili kuweka mbele swala, sadaka, uvumilivu na unyenyekevu katika matendo na maisha yetu ya kila siku.

Mwenyezi Mungu abariki umoja na mshikamano wa wananchi kwa ustawi na amani ya taifa letu.

Wenu katika utumishi wa umma,

John Mnyika (Mb)




No comments: