Thursday, October 11, 2012

NIMECHUKUA HATUA YA KUWASILISHA KWA TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA SUALA LA MATATIZO YA MAJI KATIKA KATA YA GOBA ILI HATUA ZA HARAKA NA ZA KUDUMU ZICHUKULIWE

Kazi ya mbunge ni kuwakilisha wananchi, kushiriki katika kutunga sheria na kuisimamia serikali ili kuwezesha maendeleo kwa pamoja na mambo mengine kuhakikisha huduma za kijamii ikiwemo upatikanaji wa maji zinaboreshwa.

Tarehe 10 Oktoba 2012 ikiwa ni sehemu ya kufanya kazi hiyo nimekwenda kwa niaba ya wananchi Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na kuwasilisha malalamiko ya uvunjwaji wa haki za binadamu za kupata huduma ya maji na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora katika uendeshaji wa miradi ya maji kwenye kata ya Goba katika Manispaa ya Kinondoni.

Tatizo la maji katika kata ya Goba limedumu sasa kwa kipindi cha miaka mingi kabla ya mimi kuchaguliwa kuwa mbunge, pamoja na kwamba serikali inaowajibu wa kuhakikisha inalinda haki ya kupata maji lakini Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imeshindwa kulinda haki hii kwa wakazi wa Goba.

Ifahamike kuwa miongoni mwa haki za kijamii kwa mujibu wa Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kiutamaduni (“The International Covenant on Economic, Social and Cultural Rights”, ICESCR ) wa 1966 ni pamoja na haki ya kupata maji safi na salama.

Hata hivyo katika nchi yetu inaonekana haki ya kupata maji safi na salama haitiliwi mkazo pamoja na Tanzania kutambua na kuridhia mkataba huo hivyo malalamiko haya ya lengo la kuwezesha tume kusimamia haki za msingi za binadamu na utawala bora katika sekta ya maji.

Ikumbukwe kuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, toleo la mwaka 2005 Ibara ya 130 (b) na (c) inaeleza majukumu ya Tume ya Haki za binadamu na utawala bora kuwa ni pamoja na kupokea malalamiko ya uvunjaji wa haki za binadamu na kufanya uchunguzi juu ya mambo yanayohusu uvunjaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa utawala bora;

Izingatiwe kuwa Sheria ya Haki za binadamu na Utawala Bora namba 7 ya mwaka 2001 kifungu cha 22(1) kinaruhusu malalamiko kwa njia ya maandishi ;

Na Irejewe kuwa kuwa kifungu cha 15(1) (b) (iii) cha Sheria ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, sheria namba 7 ya mwaka 2001, kinaipa nguvu Tume kuchunguza uvunjaji wa Haki za Binadamu ikiwa itapokea malalamiko kutoka kwa mtu anayefanya hivyo kwa niaba ya kundi la watu.

Kwa kutumia mamlaka na matakwa ya Ibara ya 130 ya Katiba ya Nchi na vifungu vya 15 na 22 vya Sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na utawala bora na kwa kuzingatia mikataba ya haki za binadamu ambayo nchi yetu imeridhia nimetaka tume ichukue hatua zifuatazo:

Mosi; Ichunguze na kuchukua hatua dhidi ya waliohusika katika ukiukwaji wa haki za binadamu za wananchi kupata huduma ya maji na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora kwa kushindwa kushughulikia matatizo ya kimfumo kuhusu uendeshaji wa miradi ya maji, kutokutekelezwa kwa wakati kwa vipaumbele vya maji kwa mujibu wa bajeti iliyopitishwa na tuhuma za ufisadi, uzembe na udhaifu wa kiutendaji katika kamati za maji, ngazi ya kata na kwenye idara ya maji ya Manispaa ya Kinondoni.

Pili; Pamoja na kuchukua hatua kwa wahusika waliosababisha uvunjaji wa haki ya msingi ya wananchi kupata huduma ya maji na ukiukwaji wa haki za binadamu; Tume ya Haki za Binadamu ipendekeze hatua za haraka zinazopaswa kuchukuliwa na Manispaa ya Kinondoni kuwezesha huduma ya maji kurejea kwa wananchi, kupanua kwa dharura wigo wa upatikanaji wa maji kwa wananchi wa Kata ya Goba pamoja na kuboresha mfumo mzima wa upangaji, utekelezaji na usimamizi wa miradi ya maji katika Manispaa ya Kinondoni.

Tatu; Aidha, zaidi ya hatua za dharura Tume ya Haki za Binadamu ipendekeze hatua za ziada ya kuchuliwa na Manispaa ya Kinondoni kuwezesha kata ya Goba itoke katika kupatiwa huduma ya maji chini ya Manispaa ya Kinondoni na badala yake ihudumiwe na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) pamoja na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO) ili kuwezesha uboreshaji mpana wa miundombinu kwa ajili ya ufumbuzi wa kudumu.

Nne, Tume ichunguze na kupendekeza masuala mengine ya kushughulikiwa na mamlaka zingine zinazohusika ikiwemo Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Wizara ya Maji na Vyombo vya Ulinzi na Usalama kuhusu masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu na uvunjwaji wa misingi ya utawala bora katika miradi ya maji kwenye kata ya Goba pamoja mfumo wa upatikanaji wa maji kwa ujumla.

Wenu katika kuwakilisha wananchi,

John Mnyika (Mb)
12/10/2012


7 comments:

Unknown said...

mheshimiwa mbunge nakusalimu sana. nafurahi kwa hatua ulizochukua lakini naomba kukujaza na kukujuza taarifa nyingine muhimu kuhusu maeneo yao ya goba, ukianzia goba mpakani kurudi mpaka njia panda kwenda msumi.kuzunguka kurudi makabe, mpiji, urudi mpaka msakuzi uendelee upande mwingine urudi mpaka kibwegere uje utokee kibamba ccm shuka tena upande wa pili mpaka kwembe hadi malamba mawili uje mbezi pandisha mpaka ufike kimara kote huku maji ni historia wenzetu wa temboni mapak stop over hadi kimara bucha walikutana na maji ya mchina zilipitishwa bomba za maji nyumba baada ya nyumba na mita zikafungwa hii ilikuwa project ilisimamiwa na wachina lakini jiulize hayo mabomba yanatoa maji? na watu wengine hupelekewa bili za maji kila mwisho wa mwezi sijui dawasco kimara wanafanya nini.
la pili pia maeneo hayo mengi hayana umeme, barabara nazo ni kituko, watu wa goba wanapanda canter na pickup walau bajaj, mvua zikinyesha mpiji magari hayaendi au yakienda yanaishia njiani, sasa kituko ni hiki tunao watu wakubwawa serikali wanakaa huku, mimi jirani yangu ni ofisa mkubwa wizara ya elimu na kila siku anafatwa na gari la wizara, mwingine na ofisa manispaa ya kinondoni ni kama vile hawaoni hili. si hao tu wapo watoto wa vigogo wa nchi hii wanakaa huku,zipo shule kubwa huku lakini hatukumbukwi wala kusikilizwa wenyewe kama kawaida ya wananchi wa tanzania "TUMESHAJIRIDHIKIA"
maana kama kelele tumepiga mpaka tumechoka maji siku yakija ukanda huu sijui......wapo watu waliweza kuvuta maji kwa gharama zao wanasaidia wananchi wengine kwa kuwauzia cha ajabu ngoja waje hao wahusika wa maji ni kele kwa kwenda mbele eti kwa ni ni mnauza maji mheshimiwa nakushauri siku usitembee kwa msafara halafu pita hayo maeneo moja baada ya lingine uone live mambo yalivyo nitafurahi siku yakiutatuliwa matatizo haya maana itakuwa ni siku ya mapinduzi ya ukanda wa kimara,mbezi na kibamba yote.

TUSHIRIKISHANE WANANCHI KUTENGENEZA MAENDELEO YETU TUSISUBIRI VIONGOZI NA KUKALIA KUPOINT MATATIZO TUSHIRIKI BIA KUTOA NA MAPENDEKEZO YA NINI KIFANYIKE MUNGU IBARIKI TANZANIA NA WOTE WENYE UZALENDO

Anonymous said...

habari ya mchana mh. mbunge..
kati ya mambo ambayo kiongozi mwajibikaji anafanya ni kufuatilia jambo kwa ukaribu na kutoa taarifa kwa wananchi wake ni hatua gani aliyofikia na pengine kama kunavikwazo mabalimbali vilivyojitokeza katika ufuatiliaji huo inakua rahisi kwa wananchi kufahamu kupitia kiongozi huyo..
binafsi naheshimu na kuthamini utendaji kazi wako, na natambua wewe ni kijana ambaye umejitoa kwa ajili yetu sisi tunaokuja nyuma yenu...
nipende kukupa moyo na kusisitiza kuwa usikate tamaa katika utendaji kazi wako..
vikwazo ni vingi sana lakini usikate tamaa..niko pamoja nawe sana na niko pamoja na CHADEMA kwa miaka kadhaa sasa na mapambano bado yanaendelea.

''A GOOD LEADER ALWAYS AIM TO MAKE GOOD HISTORY, HIS FOLLOWERS WILL SING PRAISING VERSES FOR HIM AS A SYMBOL OF HONOR AND RESPECT''
KEEP GOING BRO....JAH BLESS YOU...

says GODLISTEN MALISA...DSM..

godlisten malisa said...

habari ya mchana mh. mbunge..
kati ya mambo ambayo kiongozi mwajibikaji anafanya ni kufuatilia jambo kwa ukaribu na kutoa taarifa kwa wananchi wake ni hatua gani aliyofikia na pengine kama kunavikwazo mabalimbali vilivyojitokeza katika ufuatiliaji huo inakua rahisi kwa wananchi kufahamu kupitia kiongozi huyo..
binafsi naheshimu na kuthamini utendaji kazi wako, na natambua wewe ni kijana ambaye umejitoa kwa ajili yetu sisi tunaokuja nyuma yenu...
nipende kukupa moyo na kusisitiza kuwa usikate tamaa katika utendaji kazi wako..
vikwazo ni vingi sana lakini usikate tamaa..niko pamoja nawe sana na niko pamoja na CHADEMA kwa miaka kadhaa sasa na mapambano bado yanaendelea.

''A GOOD LEADER ALWAYS AIM TO MAKE GOOD HISTORY, HIS FOLLOWERS WILL SING PRAISING VERSES FOR HIM AS A SYMBOL OF HONOR AND RESPECT''
KEEP GOING BRO....JAH BLESS YOU...

Stephen P Mndalila said...

Mheshimiwa Mnyika mimi nitatofautiana na wewe katika swala hili la kutatua matatizo ya maji kwa wananchi wa jimbo la ubongo. Suala hili inalipeleka kisiasa mno kuliko kitaalamu. Siasa na mahakama inachelewesha maendeleo ya wananchi sana hasa katika kutatua matatizo ya lazima kwa wananchi ikiwa kama ni haki yao ya kikatiba! Hapa inavyoonekana ni kwamba unataka kutatua tatizo hili lakini at the same time unataka ku score political points nafikiri kwa mtindo huu miaka mitano itapita na wala suala hili halitatatuliwa na wananchi wataendelea kupata shida ya maji na ninaamini utatumia vipengele hivi wakati wa kampeni ili uchaguliwe tena kwa awamu nyingine. Ushauri wangu ni kama ufuatavyo, wewe umechaguliwa na wananchi wakiwa na imani kwamba utawawakilisha kutatua kero zao kwa kitaalam kama ulivyoahidi kwenye kampeini zako! Unachoakiwa kufanya sasa hivi andaa timu ya mainjinia katika maswala ya maji, wafanye survey ya ya jimbo lako lote wajue idadi ya kaya katika jimbo lote, kisha waangalie mahitaji ya maji kwa siku kwa kila kaya, waangalie ni matanki mangapi makubwa yanatakiwa kujengwa ili kusambaza maji kulingana na mahitaji ya kila siku kwa kaya zote, watafute nini vyanzo vya maji ndani ya jimbo kwanza kabla ya kufikiria vyanzo vya nje ya jimbo lako. Kisha ziangaliwe ni fedha kiasi gani kinachotakiwa kujenga matanki ya maji na pump za kusukuma maji kujaza hayo matanki kila siku. Waangalie kuwe na nishati mbadala ya kuhakikisha kwamba pump hizo zinafanya kazi 24/7 ili kuhakikisha kwamba maji yanakuwa pumped kwenye matanki wakati wote. ziangaliwe gharama za kutandaza bomba katika kaya mbalimbali. Wakusanye gharama zote za kukamilisha mradi huu wa maji. Kisha ukishajua gharama zake kitaalamu wakusanye wananchi wako kisha mkae chini mjadili kwamba pesa ipatikane wapi kutatua tatizo hili. Angalieni wananchi wanaweza kugharamia kiasi gani hata kuchimba mitaro na kunua mabomba ya kujivutia maji majumbani kwao. Na hii itakuwa rahisi kama kuna miundo mbinu mizuri kwamba ili kupunguza mzigo kwa serikali wananchi wawezeshwe kuvuta mabomba kwa gharama zao kwa wale wenye uwezo kwenda kwenye nyumba zao! kinachotakiwa kufanyika ni pawepo na matanki madogo mtaani yatakayowawezesha wananchi kuvuta maji kutoka hapo. Gharama zingine zilipwe na serikali au tafuta wahisani sehemu mbalimbali au fanya harambee mbalimbali za kukusanya pesa. Ninaamini kwenye jimbo lako wapo watu wenye uwezo mkubwa sana wa kuchangia mradi huu, watumieni wananchi kumaliza matatizo yao wenyewe sio kuitegemea serikali kwa asilimia mia moja kutatua kila tatizo kwa mwananchi wake. Mambo ya kesi ni kupoteza wakati na mpaka hukumu itolewe na inaweza hata isitatue tatizo lolote na wananchi wataendelea kupata shida zisizo za lazima! Haya ni mawazo yangu ya bure kwako kwa leo sintakutumia bill yoyote! Nashukuru kwa kunielewa ndimi Stephen Mndalila.

Anonymous said...

Safi Mh. Mnyika kwa japo kuanzisha huu mjadala, maana na mimi pia ni mmoja kati ya watanzania wengi tunaoathirika na kero za kukosekana kwa maji.
Na mie pia sikuungi mkono kwa njia unayotaka kuitumia katika kulitatua hili swala, njia hii haina nia ya dhati katika ufumbuzi wa suala hili, mie naiona imekaa kisiasa sana.
Na kwa njia hii unayotaka kuitumia kutatua matatizo yetu ya maji nadhani wewe hauna shida ya maji, sie hatutaki kesi tunataka maji.
Asilimia kubwa ya wananchi wenye uwezo kidogo wanaoishi katika jimbo lako na majimbo mengine wametumia rasilimali zao kidogo walizonazo wakajichimbia visima vya maji na kuwauzia wenzao, hii inaonyesha kuwa wananchi tupo tayari hata kutumia kidogo tulichokuwa nacho katika kutatua kero zetu ndogondogo, shida kubwa ni nyinyi wanasiasa mnataka kutumia kero zetu kujipatia umaarufu.
Shawishi wadau mbalimbali na wananchi tupo tayari kuisaidia Serikali katika kutatua kero ndogondogo tulizokuwa nazo. Refer mapendekezo ya Stephen P Mndalila yana tija kubwa zaidi ya hizo kesi zako.
Victor Jerome amemaliza vizuri sana, "TUSHIRIKISHANE WANANCHI KUTENGENEZA MAENDELEO YETU TUSISUBIRI VIONGOZI NA KUKALIA KUPOINT MATATIZO TUSHIRIKI BILA KUTOA MAPENDEKEZO YA NINI KIFANYIKE"
Mnatumia mabilioni kurusha mahelkopta kwenye chaguzi, kwa nini sasa msitumie hata robo tu ya hayo mabilioni kutuchimbia visima?
I HATE POLITICS.

Anonymous said...

Stephen P Mndalila,

Mzee, wazo la wananchi kujitatulia matatizo yao wenyewe ni zuri ingawa binafsi siafikiani nalo hasa ukizingatia jinsi yetu ilivyo kwa sasa, mafisadi kibao! Kwa njia hiyo ya kutatua matatizo, mafisadi tena ambayo ni sehemu ya serikali watachekelea sana. Tusifuge ubovu huu maana utazidi kukuza pengo kati ya aliye nacho na tusio nacho, jambo ambalo ni la hatari mno.

Kumbuka anachofanya Mh. Mnyika ni kutimiza moja ya majukumu yake ya ubunge ya kuiisimamia serikali. Acha aiamshe serikali hii ilalayo na kodi zetu.

Asante

Anonymous said...

mi umeme tu goba tukipata utasaidia sana tafadhali chadema kama mnatak
a kura leteni umeme goba na wananchi wameshachanga