Sunday, April 1, 2012

CCM inategemea matusi, mafisadi na wamwagaji damu; 'kudumisha amani na utulivu' ni maneno ya kuficha matendo yao maovu


Wabunge: Highness Kiwia na Salvatory Machemli

CCM ni chama chenye kukumbatia matusi, mafisadi, uongo na umwagaji damu; maneno yao juu ya amani na utulivu ni ya kuficha matendo maovu ya viongozi wake.

Poleni wananchi wa Mwanza na wapenda demokrasia na maendeleo kote nchini. Nami nimesikitishwa na naalani tukio la wabunge Highness Kiwia na Salvatory Machemli kushambuliwa kwa mapanga na mawe usiku wa kuamkia leo mara baada ya kampeni za uchaguzi wa udiwani unaofanyika leo. Hakika tukio hili halitaishia kusikitika na kulaani, tutachukua hatua za ziada. Naendelea na mawasiliano na mashauriano na viongozi wakuu walioko Arumeru Mashariki na maeneo mengine na tutaeleza hatua zitazofuata.

Ushahidi wa kimazingira unaonyesha kwamba tukio hilo la Mwanza limefanywa na WanaCCM, ushahidi wa tuhuma za kihistoria unathibitisha kwamba CCM na serikali yake imekuwa na kawaida ya kumwaga damu nyakati za chaguzi kwa njia mbalimbali ikiwemo kwa kukata viongozi wa CHADEMA mapanga, sasa wamefikia hatua ya kushambulia viongozi wa wananchi; wabunge.

Niliwahi kutahadharisha miaka michache nyuma kwamba kadiri CCM inavyoelekea kuondoka madarakani rangi yake halisi kinyume na maneno yao ya kinafiki ya ‘kudumumisha amani na utulivu’, matendo yao halisi yatajihidhirisha ya kuwa chama na serikali inayokumbatia vitisho, vurugu na umwagaji damu kama njia ya kujaribu kujiokoa na kukataliwa na umma. Wanafanya hivyo kwa kutumia vyombo vya dola na vikosi vya chama chao vya vitisho, vurugu na umwagaji damu.

Orodha ya chaguzi ndogo za ubunge zenye matukio kama hayo ni ndefu: Kiteto (2007) wanatuhumiwa mashambulizi ya aina hiyo tena ndani ya kituo cha polisi kwa ushirikiano baina ya askari polisi na vikosi vya CCM; Tarime (2008) wanatuhumiwa kukata mapanga wanachama wa CHADEMA; Busanda na Biharamulo (2009), wanatuhumiwa kukata mapanga viongozi wa CHADEMA; Igunga (2010), walituhumiwa kummwagia tindikali mwanachama wao na kuisingiza CHADEMA na hatimaye CCM ikahusishwa na kifo cha aliyekuwa wakala wa CHADEMA Mbwana Masudi. Nyakati zote hizo Polisi walifungua majalada ya uchunguzi, watuhumiwa baadhi walitajwa kwa majina, lakini mpaka sasa hakuna aliyetiwa hatiani kwa udhalimu huo dhidi ya binadamu.

Vyombo vya dola vinaposhindwa kusimamia utawala wa sheria na chama tawala kinapofanya siasa chafu za uongo, ufisadi na matusi ni wazi huvuka mipaka na kufikia hatua ya kufanya siasa za vitisho, vurugu na umwagaji damu nchi iko mashakani, amani na utulivu unaohubiriwa na CCM ni barakoa tu ya kufisha matendo yao maovu yenye baraka za viongozi wa chama hicho.

Viongozi hao hao watawahi kujitokeza kinafiki mbele ya vyombo vya habari kukanusha kuhusika, kulaani na kutoa pole za uongo; ujumbe wangu kwao na kwa vyombo vya dola, CCM haiwezi kulinda utawala wake kwa njia hizi za kihuni na kiharamia; kwa ukweli, haki na nguvu ya umma hatimaye tutashinda.

Nayaandika haya nikiwa Vijibweni kwenye uchaguzi wa marudio wa udiwani, mbinu hizi haramu za CCM za kutumia uongo, ufisadi na vitisho ndizo hizo hizo zimekuwa zikitumika hapa usiku wa kuamkia jana; matukio ya Arumeru Mashariki, Mwanza na kwingineko yanatupa moyo zaidi kwa kusonga mbele na kuchukua hatua; mpaka kieleweke.


John Mnyika (Mb)

Mkurugenzi wa Habari na Uenezi

01/04/2012

1 comment:

Anonymous said...

Haya ndiyo matokeo ya kushindwa kwa hoja,hope they are on the way to collapse.