Sunday, July 31, 2011

Ufisadi Kituo cha Ubungo(UBT) na Usafiri DSM (UDA)-Majibu Bungeni

Ripoti ya Uchunguzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi ya Ubungo (Swali la Nyongeza kuhusu Ufisadi kwenye Shirika la Usafiri Dar es salaam –UDA)

MKUTANO WA NNE: Kikao cha Ishirini na Sita – Tarehe 15 Julai, 2011

MHE. JOHN J. MNYIKA aliuliza:-

Tarehe 15 Machi, 2009 Serikali kupitia Waziri Mkuu iliagiza ufanywe uchunguzi
maalum kuhusu makusanyo ya kituo cha Mabasi cha Ubungo ili kuboresha mapato ya Jiji
la Dar es Salaam. Tarehe 28 Julai, 2009, Serikali ilikabidhi ripoti ya uchunguzi huo kwa

CAG ambayo pamoja na mambo mengine ilieleza kasoro za ukusanyaji na tuhuma za
ubadhirifu wa mapato ya kituo.

Mosi; Je, ni lini Serikali itaweka wazi taarifa hiyo?

Pili; Je, Serikali imechukua hatua gani juu ya kasoro zilizobainishwa kuhusu
mikataba ya kampuni ya Smart Holdings, Rick Hill Hotel, Abood Bus Services, Clear
Channel, Globe Accounting Services na Scandinavian Express Services, ambayo
imesababisha hasara na upotevu wa mapato?

Tatu; Je, Serikali iko tayari kufuatilia na kuchukua hatua za haraka juu ya
malalamiko yanayotolewa na ukusanyaji wa mapato unaofanywa sasa ili kunufaisha
umma kikamilifu?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NAQ
SERIKALI ZA MITAA (TAMISEMI) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la
Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Ubungo, lenye (a) (b) na (c) kama
ifuatavyo:-

Mosi; Mheshimiwa Naibu Spika, Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali
(CAG) alifanya uchunguzi maalum katika kituo Kikuu cha Mabasi cha Ubungo na
kubaini kasoro mbalimbali. Aidha, hoja zilizojitokeza katika taarifa ya Uchunguzi ya
CAG katika kituo hicho zimejitokeza pia katika taarifa ya mwaka ya ukaguzi ya CAG ya
mwaka 2009/2010 ambayo iliwasilishwa hapa Bungeni na hoja hizo zimeaza kufanyiwa
kazi na Halmashauri ya Jiji.

Pili; Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuondoa kasoro zilizojitokeza katika Kituo
hicho, Serikali inapitia upya mikataba ya makampuni na kuhuisha viwango
vinavyotakiwa kukusanywa kulingana na sheria ndogo ya Halmashauri ya Jiji la Dar es
Salaam inayosimamia ushuru huo.

Marekebisho ya viwango hivyo yatasaidia kuongeza mapato yanayokusanywa
katika kituo hicho na kuondoa kasoro zilizokuwepo za ukusanyaji wa mapato.

Ukusanyaji wa ushuru katika kituo hicho kwa sasa unafanywa na Halmashauri ya Jiji la
Dar es Salaam kupitia kwa Wakala aitwae KONSAD INVESTMENT LIMITED ambaye
anakusanya ushuru huo kwa wastani wa shilingi milioni 4 hadi milioni 5.7 kwa mwezi.

Tatu; Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingaia malalamiko yaliyopo, Serikali
tayari imebadilisha Menejimenti ya kituo na itaendelea kuboresha miundombinu yake.
Aidha, katika Bajeti ya mwaka 2011/2012, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam
imetenga kiasi cha shilingi milioni 85 kwa ajili ya kufanya matengenezo katika eneo a
maegesho ya magari. Mpango wa muda mrefu wa Serikali ni kukijenga upya kituo cha
Mabasi kama ilivyoainishwa katika mpango wa biashara wa mwaka 2007.


MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na majibu
yaliyotolewa, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika majibu Naibu Waziri ameeleza kwamba
mkandarasi KONSAD Investment anakusanya milioni Nne hadi milioni Tano kwa
mwezi, lakini kwa mujibu wa taarifa zilizopo ni kwamba toka Mkandarasi aingie
mkataba mwezi Oktoba mwaka 2010, kwa mujibu wa Mkataba alipaswa kukusanya
shilingi milioni 5.6 lakini alifanya hivyo kwa siku mbili tu (mara mbili tu) baada ya hapo
toka wakati huo Oktoba 2010 mpaka leo amekuwa hatekelezi mkataba na ameandika
barua Ofisi ya Waziri Mkuu na inaelekea anakingiwa kifua kuutekeleza huu mkataba.

Mosi; Ningependa kupata kauli kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu na ninajua inafahamu
hili jambo kwa undani, Je, iko tayari sasa kuiruhusu Jiji la Dar es Salaam liweze kuvunja
huu mkataba ambao haunufaishi wananchi wa Dar Es Salaam?

Pili; Suala la udhaifu wa kimikataba wa kituo cha mabasi ya Ubungo ambayo
yanahusisha vile vile sehemu ya eneo litakalohusiana na mradi wa mabasi yaendayo kasi
ambayo linahusiana na Kampuni ya UDA yamefikia kiwango cha juu sana, ninaelewa
kwamba ofisi ya Waziri Mkuu iliandika barua ya kusitisha taratibu za uuzwaji wa hisa za
kampuni ya UDA ambazo zimeuzwa na upotevu wa mali nyingi; ninaomba kauli ya Ofisi
ya Waziri Mkuu kuhusiana na ufisadi uliopo kwenye kampuni ya UDA unaoendelea hivi
sasa, na iko tayari kutoa maelekezo kwa Jiji la Dar es Salaam kuweza kusitisha taratibu
zinazoendelea?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA
NAQ SERIKALI ZA MITAA (TAMISEMI): Mheshimiwa Naibu Spika, nataka
niseme hapa kwamba, Waziri Mkuu alikwenda akamwelekeza CAG aende katika kituo
hiki cha mabasi, akamtaka afanye uchunguzi pale. Walipokwenda pale kwa mara ya
kwanza walikuwa wanakusanya milioni 1.5 kwa siku.

CAG alipofanya marekebisho yale wakafanya na mahesabu na wakamaliza
wakaweka na Menejimenti nyingine pale, ikapanda mpaka milioni 5.7
ninazozizungumza, siyo kwa mwezi ni kwa siku, na kama alivyosema Mbunge kwamba
kampuni ilikusanya kwa siku ya kwanza na siku ya pili na baadaye kukawa na matatizo
hawakukusanya kiasi hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mnyika analifahamu jambo hilo kuliko
sisi sote hapa, tunachojua ni kwamba kuna kampuni nyingine mpya ambayo imekwenda
pale inafanya kazi na hivi tunavyozungumza hapa wanao huu mgogoro anaozungumza na
wameanza kupelekana mpaka mahakamani, kuna mambo ambayo wakati anakwenda kuoperate
ameona kwamba yanakwenda kinyume na jinsi walivyokuwa wamekubaliana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza hapa sasa hivi, tumemwita
Mkurugenzi Mtendaji Kingopi hapa Dodoma tukamuuliza hili analolizungumza hapa,
wameniambia kwamba hili wameliona na wanalifanyia kazi.

Kwa hiyo Mheshimiwa Mnyika ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri hii
tunayoizungumza yaani (DCC) avute subira katika jambo hili. Hili jambo jingine jipya
sasa linaanza kwa sababu huyu ni mpya ambaye tumesema kwa taratibu hizi mpya akaye
pale, kama ikiwezekana tukubaliane leo tukitoka hapa nimwuite Kingobi na wenzake
tukae na tuseme ni nini kilichotokea kwamba kiasi hiki sasa hakiendelei kukusanywa
kama ilivyokuwa siku ya kwanza na siku ya pili kama anavyosema Mbunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la DART analolizungumza hapa, huu ni
mpango mwingine unaokuja, DART tunasimamia sisi Ofisi ya Waziri Mkuu na ujenzi ule
utafanywa chini ya Wizara ya Ujenzi, na hili suala la UDA analolizungumza hapa kwa
pamoja mimi ningemuomba tukutane kwa sababu linahitaji details zaidi ili tuliangalie
pamoja na lile ambalo tumelizungumzia.

No comments: