Friday, June 22, 2012

Lengo la Kuomba Mwongozo - Sakata la Madaktari

Kwanini niliomba muongozo-Sakata la Mgomo wa Madaktari

Leo nilitaka kuomba muongozo wa Spika kwa mujibu wa Kanuni 49 (2) baada ya Waziri wa Afya kutoa kauli juu ya utekelezaji wa madai ya madaktari. Kanuni hiyo inataka kauli isiwe ya kuzua mjadala lakini aliyoyaeleza waziri juu ya uboreshaji wa maslahi ya madaktari yanazua mjadala kwa kuwa yanatofautiana na majibu ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyoyatoa bungeni jana, (Juni 21, 2012) na pia hayana uhalisi. Mathalani, wakati serikali ikidai imeongeza posho ya kuitwa kazini (on call allowance) toka Februari, 2012 na kutumia bilioni 7.9 kwa miezi michache, imetenga kwa watumishi wa Afya bilioni 18.9 tu kwa mwaka mzima wa 2012/2013 kiwango ambacho hakitoshi.

Hivyo nilitaka kuomba muongozo Spika awezeshe kauli hiyo ijadiliwe kama ilivyokuwa kwa kauli juu ya fedha za rada. Nakusudia kumuandikia barua Spika kushauri aelekeze kamati ya bunge ya huduma za jamii kauli hiyo ya waziri.

Pia bunge halipaswi kunyimwa fursa ya kutumia mamlaka yake kwa mujibu wa ibara ya 63 ya kuishauri na kuisimamia serikali kusuluhisha mgogoro na madaktari ili kuepusha mgomo wenye athari kwa nchi na wananchi kwa kisingizio cha kusudio la serikali kupeleka mgogoro mahakama kuu kwa kuwa mpaka leo taarifa iliyotolewa bungeni bado hakuna shauri katika kitengo cha kazi. Hivyo, Spika anapaswa kutoa jukumu kwa kamati husika ya bunge kuendelea na usuluhishi kabla ya serikali kukimbilia mahakamani.

Wabunge tupewe nakala ya taarifa ya majadiliano ya pande mbili yaliyochukua zaidi ya siku 90 badala ya kupewa hotuba ya nusu saa ya upande mmoja wa serikali pekee.

Hata serikali ikizuia mgomo wa wazi kwa zuio la kimahakama ieleweke kuwa mgomo wa chinichini kwa watumishi wa afya ambao una athari ya muda mrefu kwa maisha ya wananchi nchini.

Mwisho, serikali ipunguze matumizi yasiyo ya lazima na ipanue wigo wa mapato.

John John Mnyika.
Mbunge Jimbo la Ubungo (CHADEMA)
22 Juni, 2012

No comments: