Thursday, July 12, 2012

OFISI YA WAZIRI MKUU HAIKUJIBU UKWELI BUNGENI SWALI LANGU KUHUSU MGOGORO KATI YA SERIKALI NA WALIMU


Ofisi ya Waziri Mkuu imejibu uongo  bungeni kuhusu uwepo wa mgogoro kati ya Serikali na walimu hivyo nakusudia kumwandikia Spika aagize swali hilo lijibiwe kwa ukweli na ukamilifu.
Tarehe 11 Julai 2012 wakati nikiuliza swali la nyongeza kwa ofisi ya Waziri Mkuu kwa niaba ya walimu watumishi wa umma katika Jimbo la Ubungo na nchi kwa ujumla kuwa ni lini serikali itakamilisha kushughulikia madai ya walimu kwa kuwa matatizo walimu yamedumu kwa miaka mingi kwa kiwango cha kufikia hatua ya walimu kutangaza mgogoro na serikali.
Akijibu swali langu kwa niaba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Naibu Waziri Majaliwa Kassim Majaliwa hakueleza kwa ukamilifu ni lini serikali itakamilisha kushughulikia madai ya walimu badala yake akatoa majibu ya uongo kuwa walimu hawajatangaza mgogoro  na serikali.
Hata hivyo, ukweli ni kuwa walimu wametangaza mgogoro na serikali na ushahidi ni tamko la Serikali  yenyewe kuhusu migomo sehemu za kazi lililotolewa na Wizara ya Kazi na Ajira tarehe  9 Julai 2012 ambalo limeeleza kuwa tayari Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) kwa niaba ya walimu nchini kimeishawasilisha mgogoro katika Tume ya Usuluhishi na Uamuzi- Dar es salaam wenye usajili CMA/DSM.ILA/369/12.
Hivyo, naendelea kusisitiza serikali ichukue hatua ya kushughulikia vyanzo vya migogoro na watumishi wa umma badala ya kusubiri mpaka matokeo ya migogoro kama migomo na madhara mengine kwa nchi na wananchi ndio ianze kutumia nguvu kuidhibiti.
Migogoro kati ya serikali na watumishi wa umma ina athari kubwa; wakati migogoro ya madaktari huchangia katika kuathiri hali na uhai wa wagonjwa, migogoro kati ya serikali na walimu inachangia katika kudidimiza ubora wa elimu na kuathiri maisha ya wanafunzi.
Na wabunge  tupewe nafasi ya kuishauri na kuisimamia serikali kwa mujibu wa mamlaka ya bunge ya ibara ya 63 (2) na (3) kwa kuletewa taarifa sahihi na pia kujibiwa maswali kwa ukweli na ukamilifu kabla ya serikali kwenda mahakamani baada ya majadiliano yake na watumishi wa umma kukwama kama ilivyotokea kwa madaktari.
Aidha, Spika aliwezeshe bunge kupokea taarifa maalum ya kamati ya bunge ya huduma za jamii kuhusu madai ya watumishi wa umma ambayo mengi chanzo chake ni ufinyu wa bajeti ili katika mkutano huu wa bunge la bajeti unaoendelea bunge liweze kujadili na kuisimamia serikali kushughulikia vyanzo vya migogoro badala ya matokeo.

John Mnyika (Mb)
Bungeni-Dodoma
13/07/2012

No comments: