Monday, July 16, 2012

Tutibu kiini cha tatizo Sekta ya Nishati ya Umeme!

Kwa nafasi ya Uwaziri Kivuli wa Nishati na Madini,nafahamu kuna ufisadi na ubadhilifu ndani ya TANESCO ambao uchunguzi ni muhimu kwa ajili ya uwajibikaji.Kusimamishwa kwa Mkurugenzi wa TANESCO na maafisa wengine wa shirika hilo kupisha uchunguzi ni muhimu,lakini si muarubaini wa uozo wa kimfumo katika sekta ya nishati nchini nitatoa vielelezo vya kina wakati nitakapo wasilisha maoni ya Kambi ya Upinzani Bungeni katika wizara ya Nishati na Madini.

Hata hivyo ni vyema nikatahadharisha mapema kuwa tukio hili linapaswa kutafakariwa kwa upana kwa kuwa linahusisha masuala mengi ambayo mengine Bodi ya Wakurugenzi imeyaacha nyuma ya pazia.Ukweli wote utakapotoka hadharani wengine zaidi watapaswa kuwajibika au kuwajibishwa kwa maslahi ya Taifa!

Kwa nyakati mbalimbali toka mpango wa dharura wa umeme uwasilishwe bungeni,nimekuwa nikiitahadhalisha na kuihoji serikali(kama sehemu ya jukumu langu la kibunge) kwa uzembe,ufisadi na udhaifu wa kiutendaji katika serikali ambao hasara yake utairejesha nchi katika mgao wa umeme hali ambayo imedhihirika hivi sasa!


Kusimamishwa kwa Mkurugenzi wa Tanesco na watendaji wake ni kafara ya kuficha uzembe na udhaifu wa serikali kwa ujumla wake kwa kuwa taarifa za utendaji wa Tanesco kuhusu mpango wa dharura wa umeme zimekuwa zikijadiliwa kwenye vikao vya wizara ya nishati na madini na hata vikao vya baraza la mawaziri bila hatua muafaka kuchukuliwa.Ninazo nyaraka za ndani za serikali na taasisi zake.Iwapo serikali haitatoa kauli bungeni ni kwanini Waziri wa Nishati na Naibu wake anayehusika na Nishati kutoa taarifa potofu bungeni kuwa hakuna mgao wa umeme,aidha waeleze mkakati dhaifu waliokuwa wakiufanya kupunguza mgao katika kipindi cha bunge ili kuficha udhaifu na uzembe uliokithiri serikalini na katika wizara mahsusi!

John John Mnyika,
Mbunge wa Ubungo (Chadema),
16 Julai,2012

No comments: