Sunday, February 27, 2011

Risala ya Wananchi wa Goba kwa Mbunge

RISALA YA WANANCHI WA GOBA KWA MH. JJ MNYIKA, MBUNGE WA JIMBO LA UBUNGO (27 February, 2011)

1.0 Utangulizi:
Awali ya yote tunamshukuru Mungu aliyekusaidia kupita katika ushindaji mgumu wa kuwawakilisha wananchi katika jimbo la Ubungo. Tunawashukuru pia wananchi walioshiriki katika harakati za uchaguzi ambao matokea yake leo ndio nguvu yako inayokuwezesha kusimama kutuwakilisha Bungeni, Serikani na zaidi kuwa kiongozi miongoni mwetu katika kujadili fursa na kupambana na changamoto mbalimbali katika jamii yetu.

Tunatambua kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoainisha mgawanyo wa madaraka wewe sio kiongozi wa serikali wala wa chama bali ni kiongozi-mwakilishi wa wananchi. Hii ni pamoja na waliokuchagua na amabao hawakukuchagua na wa vyama vyote. Ndivyo tunavyoamini pia kwa diwani Mh. Kissoky kwa ngazi ya kata. Tunakukaribisha Kata ya Goba yenye changamoto nyingi. Tunamkaribisha pia Mh. Kissoky na kumpongeza kwa kuchaguliwa kwake tena.

Kwa kutambua hivyo, risala hii imeandikwa na wananchi wenye itikadi tofauti za vyama vya CCM, CHADEMA, CUF na vinginevyo wakifungamanishwa na dhamira moja tu ya kuleta maendeleo na kupambana na ufisadi, uonevu na matumizi mabaya ya dhamana za uongozi na madaraka. Kwetu sisi hakuna bei yeyote ya kununua utu wetu zaidi ya ukweli, uwezo wa utendaji kazi na uadilifu. MASLAHI YA JAMII DAIMA YATATANGULIA MASLAHI BINAFSI. MASLAHI YA NCHI NA YA WANANCHI YATATANGULIA MASLAHI YA CHAMA NA ITIKADI.

2. Matarajio ya Wananchi Kwa Ujio Wako
Tunashukuru katika barua yako ya kutuarifu juu ya ujio wako uliweka vipaumbele vya ziara yako katika Kata ya Goba. Tunakufahamu wewe ni mtu msikivu, makini na mwenye uwezo wa kubaini mambo mengi yanayotokea katika jamii. Hatuhitaji kukuambia kila kitu kwa sababu mengine unayafahamu na katika kampeni zako uliahidi kuyatafutia ufumbuzi. Tunategemea kusikia kutoka kwako mipango na mikakati juu ya utengenezaji wa miundo mbinu na hasa barabara kuu na zile ndogo ndogo zinazoingia na kutoka katika maeneo na mitaa yetu tunayoishi. Tunamashukuru Mungu kwa Kuchanguliwa kuwa Waziri-Kivuli wa Nishati na Madini. Hii itakupa nafasi nzuri ya kuwasaidia wananchi ambao bado wanahitaji kuunganishwa na umeme. Swala la Usalama, Elimu ya watoto na vijana wetu na usalama wa raia na mali zao vinahitaji tu upeo wa kioungozi na maono ya kuunganisha nguvu za wananchi. Tunaamini hilo utalipa uharaka wa kutosha.

Mh. Mbunge, pamoja na hayo yote swala la maji hatuwezi kuliacha kuwa la kawaida kwa sababu maji ni uhai na linagusa maisha na uhai wa kila kiumbe cha Mwenyenzi Mungu. Ni Bora ukakosa maji kwamba hayapo lakini ikifikia mtu akakunyima maji yakiwa yanapita mbele yako tena kwa ukatili tu ni uuaji. Inapofikia mtu ananyeshea matofali kwa ajili ya biashara zake huku majirani zake wakiwemo wazee, wajane na yatima wakiwa wanahangaika kutafuta walau ya kunywa au kupikia chai, hatutakuwa na lugha nyepesi zaidi ya kusema ni ukatili tunaotakiwa kupambana nao kwa nguvu zote hadi pumzi yetu ya mwisho. Tunaamini watu wanaochukia maovu katika jamii hupata upinzaji mkubwa na hata kuzushiwa kesi kwa kutumia mfumo wa sheria au/na utawala. Hiyo imeshatokea kwa wenzetu wachache amabo wamezushiwa tuhuma za kutaka kuweka sumu kwenye maji. Zaidi ya mwaka mmoja sasa waliotuhumu hawajaweza kuthibitisha.

Kama ambavyo umesoma katika taarifa ya ukaguzi wa mradi wa maji ya octoba 2007 tatizo hili limekuwa kubwa kila kukicha. Tunaamini ungekuwa unayafahamu yaliyoendelea kutokea kati ya octoba 2007 mpaka leo ungehuzunika sana . Tunaamini pia sehemu kubwa ya wananchi hawana hizi taarifa kwani zinahuzunisha sana. Tunasema hivi kwa sababu sehemu ya watendaji wa mradi wa maji walikuwa msitari wa mbele kuandamana mwaka 2007 kwenda kwa Mkuu wa Wilaya (Colnel Massawe) na Mkuu wa Mkoa (Kandoro) wakiwatuhumu wanakamati waliokuwa chini ya Ndugu Lupenza. Leo hii watu hawa ni wakatili na waonevu wa kutisha wasiosikiliza la mtu yeyote isipokuwa kiongozi wao mkuu ambaye ameendelea kutumia dhamana za uongozi wake wa kata na Manispaa kuhakikisha wananchi wanendelea kusulibiwa bila huruma. Sisi hatuwezi kupigana lakini uongozi ni dhamana yenye mwisho. Hata walioko kwenye mradi watafikia mwisho na hata viongozi nao wana ukomo wao. Shida ni kwa vipi wataendelea kuishi ndani ya jamii waliyoistesa utakapofika ukomo wa uongozi wao nao wakigeuka kuwa wahitaji sawa na wengine.

Mh. Mbunge tunapojifariji ni sehemu ya kibinadamu inayolenga kupunguza maumivu ya nafsi ambayo yumkini yangeweza kuamsha mitafaruku na jazba zinazoweza kuleta shida katika jamii. Lakini tunafahamu ziko sheria na taratibu zinazomlamzimisha mwananchi au kiongozi wa ngazi yeyote kuishi na kutenda kwa mujibu wa taratibu hata kama hazipendi. Hilo ndilo tunalotaka kusikia kutoka kwako na kwa wananchi waliokusanyika hapa leo. Tunaamini pia kwenye nguvu ya umma pale ambapo suluhisho halitafikia mwisho mwema katika kipindi cha kawaida cha uvumilivu wa mwanadamu. Tunaamini kuwa wanakamati ya maji wamejizatiti kuthibitishia umma kuwa ni watu wasafi na wale wanaowasema ni kwa sababu ya chuki binafsi au uelekeo na maslahi ya kiitikadi/kichama. Kwa sababu hiyo tuhuma zetu tumezifanyia utafiti ambao hatuna mashaka nao.

Madai yetu kwa Kamati ya Maji

I. Kamati hii sio halali-
Kamati hii ilichanguliwa na mkutano wa wananchi (Mkutano wa Mh Keenja (Mb) na Kisoky -Diwani)) tarehe 21 Octoba 2007 na ikaongezewa wajumbe tarehe 27 Octoba 2007. Ilipaswa kufanya ukaguzi wa shughuli za kamati ya kwanza na kuweka mfumo mzuri na kurudi kwa wananchi kutoa taarifa. Kwa kipindi cha miaka 3 na miezi mitano haijarudi kwa wananchi. Hata kwa kutumia kanuni za uendeshaji wa miradi midogo ya maji vijijini haifuati sheria ya uendeshaji na utoaji wa taarifa. Ngvu za kamati, jeuri na ukatili unaashiria kuwepo kwa nguvu kubwa nyuma yao. Tunasema hivyo kwa sababu katika kipindi hiki chote juhudi kubwa imefanyika ili kilio cha wananchi kitatuliwe na mamlaka halali za kiuongozi lakini hatukuzikilizwa. Hii ni pamoja na kutumia ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, TAKUKURU. Hii inaonyesha kupotea kwa maadili katika ngazi mbalimbali ndani ya jamii. yetu

II. Uhujumu wa Mradi
Katika ukaguzi wa mradi wa Maji Octoba 2007, tulionyesha wasiwasi wetu juu ya uwezekano mkubwa wa kuwepo ushirikiano wa kihujuma kati ya watendaji wa mradi na watendaji wa DAWASCO. Hii ilitokana na ukweli kuwa wakati kumbukumbu za DAWASCO zilikuwa zinaonyesha maji yaliyouziwa mradi kuwa mita za ujazo 67,640 (31/10/2007) matumizi ya maji kwa kutumia mita za wateja wachache zilionyesha kiasi cha maji kilichoingia kwenye mradi kuwa zaidi ya lita za ujazo laki mbili (200,000). Hatuna uhakika kama kuna hatua zozote za kiutawala au kisheria zilizochukuliwa kufuatilia na/au kukomesha uharibifu huu.

Yumkini ndio sababu tatizo hili sasa limeongezeka kwa kiwango cha kutisha. Kuna kila dalili ya ushiriakiano wa kifisadi kati ya watendaji wa mradi na watendaji wachache wa Dawasco. Utafiti wetu umejengwa juu ya nguzo zifuatazo;

a. Kuwa, ni ukweli usiopingika kuwa idadi ya watu waliounganishwa maji na matumizi ya maji ni kubwa zaidi mwaka 2010 kuliko ilivyokuwa mwaka 2006/2007;
b. Kiwango cha maji tunachouziwa na DAWASCO kimeshuka toka mita za ujazo 4,335 kwa mwezi March 2008 na kufikia mita za ujazo 1,100 (Oct 2008)
c. Tunamshukuru Mungu pia hata kwa kuwapa upofu wa fikra wanaohusika kwani kuanzia August 2008 matumizi ya maji ya units 1,100 yanalingana kwa kila mwezi. Kwa mienzi 26 inayoishia Dec, 2010 wastani wa mauzo ya maji toka Dawasco kwenda kwenye mradi ni mita za ujazo 884. Akili ya kawaida inakataa kukubali uovu huu unaojengwa kwenye mbinu dhaifu.

d. Katika kipindi cha miaka 6 ya mradi mita tatu tofauti zimetumika na DAWASCO. Yumkini ziliharibika au ni kupoteza ushahidi.

e. Ili kujiridhisha na kutowapa nafasi ya kudanganya tulilazimika kupata bill ya umeme (kutoka TANESCO) unaotumika kusukuma maji pale tangi-bovu. Tulitaka tujiridhishe kama watu wameacha kutumia maji kwa asilimia 75% kama inavyosomeka kwenye invoice ya DAWASCO . Tulitaka kujua-Je nao umeme unaosukuma maji umepungua kwa kiwango hicho hicho. Tungekuta ni hivyo tungejiridhiridha kwa sehemu lakini ilikuwa kinyume kabisa. Kama inavyoonyeshwa kwenye jedwali hapa chini ni kuwa units za umeme ziliongezeka toka wastani wa 2,500 (Oct 2007-May 2008) mpaka units 4,000 (June 2008-Octoba 2008). Kwa uwiano huu inaonyesha matumizi ya majini yalizidi karibu mara mbili hivi. Huu ni uthibitisho tosha kuwa matumizi ya maji yamekuwa yakiongezeka ila bahati mbaya tu hawakuweza kuzishawishi machine za kidigitali za TANESCO zibadilishe kiwango cha units za umeme

Jedwali 1: Matumizi ya Maji na Umeme
Mwezi Mita za Ujazo-Maji Units za Umeme
1 Novemba 2007 –Jan. 2008 8,756 6,520.40
February 2008 7,308 3,121.20
March 2008 5,610 3,697.90
April 2008 2,039 1,455.70
May 2008 1,038 2,672.80
June 2008 709 2,512.70
July 2008 800 4,178.50
August 2008 1,100 4,434.60
September 2008 1,110 4,658.90
October 2008 1,100 3,826.30

f. Sababu nyingine inayotufanya tuamini kuwa kuna ushrikiano wa kifisadi kati ya watendaji wa mradi na DAWASCO ni huu ufuatao. Eti kwa kipindi cha miaka miwili na miezi miwili (miezi 26) inayoishia Decemba 2010 DAWASCO wamefungulia maji mita za ujazo 22,973 sawa na units 884 kwa mwezi. Kiwango hiki ni kidogo kuliko mita za ujazo 24,751 zilizouzwa na DAWASCO kwa miezi saba tu ya kati ya Nov 2007-May 2008. Hili jambo ni kubwa na yumkini laweza kuhitaji nguvu na mamlaka makubwa zaidi ya kiutawala na kisheria
g. Uhujumu wa Mradi Miongoni mwa Wafanyakazi wa Mradi – Mh. Mbunge kuna viashiria vingi vinavyoonyesha jitihada za mfanyakazi binafsi dhidi ya wenzao au kikundi cha wawili au watatu dhidi ya waliobaki. Si nia ya sisi wananchi kuingilia maisha binafsi lakini yanapoingilia haki za wananchi sisi hatutanyamaza. Hatuna haki ya msingi au ya kisheria kuuliza kwa nini Ndugu G. W. Rwegasira (Mwenyekiti wa Mradi) na Bi Lilian B. Mavika (Katibu wa Mradi) wamefungua na kumiliki akaunti ya pamoja benki. Pia hatujui ilifunguliwa lini na kwa makusudi gani. Lakini tunayo haki ya kuuliza ni kwa nini pesa za mauzo ya maji zilipwe kwenye accounti hiyo binafsi?. Kama inavyoonekana kwenye Payment Voucher ya tarehe 28 sept. 2008 –wawili hao walilipwa kiasi cha shillingi laki tano (TZS 500,000) kwa cheki namba 000630 ya sekondari ya St Joseph Millenium. Huyu ni mteja mkubwa ambaye mpaka tunaandika risala hii alishatumia zaidi ya mita za ujazo 5,000 ambazo ni sawa na TZS (5,000 x 2,500) – TZS 12,500,000. Hatujui hizo nyingine zimelipwaje. Tunaomba jambo hili lifuatiliwe kwa makini.
h. Uhujumu kwa Ushirikiano na Wananchi wachache miongoni mwetu wasiokuwa waaminifu – Mh Mbunge katika kufuatilia matatitizo ya maji pamoja na madhaifu yaliyokuwepo kwenye kamati iliyotangulia tuligundua kuwa wapo wananchi miongoni mwetu ambao waliunganishiwa maji bila mita au kuchepua (divert) ili yasisomeke kwenye mita. Pia tuligundua watu waliokuwa wakitumia maji huku mita zao zikiwa zimeharibika. Zipo fununu pia kuwa watu hawa wana ushiriakiano na mafundi bomba. Jamii inawafahamu ila kuna woga wa kutajana kwani baadhi ya watu hawa wana nguvu za kifedha. Pamoja na woga lakini wanaobebeshwa mzigo wa maji ni watu maskini wakiwepo wajane na yatima wasiokuwa na kipato kwa kulipia ndoo ya shs 50/- badalaTZS 17/- zinazoruhusiwa na EWURA au wastani wa shs 25/- au 30/- amabayo ingetosha kabisa kulipa gharama nyinginezo kama kungekuwepo na uadilifu.
Mradi wa Maji Sasa ni Kisu cha Kuikata na Kuipasua Jamii: Mh Mbunge tunakueleza kwa masikitiko na uchungu mkubwa kuwa mradi huu wa maji ni fimbo ya kisiasa au itikadi. Ni chombo cha uhasama na kulipizana visasi. Katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita mtu au au kikundi kilichoonekana kutokumunga mkono Mh. Diwani Kisoky katika kutetea nafasi ya uongozi basi wameadhibiwa kwa kuzuiliwa kupata maji, kuharibu connections zinazokwenda majumbani mwao n.k. Adhabu zina maumivu tofauti. Moja Wana CCM ambao walionekana kutokuunga mkono Bwana Kisoky na wale wanaoonekana kuwa wa itikadi tofauti. Bahati nzuri mafundi bomba ni jeuri na katili wakiwa na uwezo wa kusema chochote mahali popote na kwa yeyote kwani wanao ulinzi.
Hatuna wasiwasi na tunachokisema kwani wenzetu waliweza kuzuliwa kesi ya kuweka sumu kenye maji na kukamatwa na polisi usiku wa saa 9. mpaka leo hawajafikishwa mahakamani. Jambo hili ni la hatari kwani linaweza kusababisha chuki miongoni mwa jamii. Tunafahamu kuwa viongozi wa Kata wangekuwa wameitisha mkutano wa wananchi hii kamati iliyokusudiwa kuwa ya muda ingeshabadilishwa na jamii isingekuwa inaendelea kupata mateso na manyanyaso ya kiwango hiki. Udhaifu wa kamati hii umeendelea kulindwa kwa pazia la kiitikadi. Lakini wanaoumia ni Wana CCM na wengine. Hatujawahi kusikia kuwa wana CCM wana bei tofauti ya maji au miongoni mwetu tunao wana CCM hatujawaji kurudishiwa kiasi fulani kwa siri. Wote tumeendelea kuadhibiwa

3.0 Mapendekezo:
Sisi tumewasilisha kilio chetu kwa niaba ya wananchi. Mh. Umma uliopo mbele yako watoe mapendekezo
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Taarifa ya Ukaguzi ya Wananchi ya mwaka 2007 unaweza kuisoma kupitia: http://mnyika.blogspot.com/2011/02/taarifa-fupi-ya-ukaguzi-wa-uendeshaji_27.html

5 comments:

Anonymous said...

Good job endelea kuwa karibu na wananchi
Kasesela

Eng Joseph Mwaikambo said...

Kazi Mzuri sana mbunge jana ilifanyanyika. Watu wengine walipenda jinsi ulivyoendesha Kikao.

Ingawa kuna baadhi ya vitu hatukupata muda wa kuviongelea.

1. Tulikuwa tunaomba kamati pia ya maji iwawasusishe wasomi ili tuweze kupata fikra za wasomi ili tuweze kwenda mbele.
2. Pump inayosukuma maji tangi bovu iko moja tu na ilitolewa na JICA na kama ikifika leo wananchi wagoba watapata tabu. Kamati inayoundwa iangalie uwezekano wa kununua pump mpya.

3. Maji yanatolewa kwa siku mbili, lakini ni muda mfupi sana, tunaomba hizo siku mbili ziwe kwa masaa 24 au yote 48 kwahizo siku mbili.

4. Goba hamna viwanja vya michezo, tulikuwa tunaomba kiwanja cha shule ya sekondari kichongwe, ili wananchi wapate sehemu ya kichezea na maeneo mangine yaongezwe kwa ajiri ya michezo.

5. Kuliwa kuwa na kombe la diwani cup, lakini kutoka na diwani wetu kuto kutujali, halipo tena. Tulikuwa tunaomba tuanzishe MNYIKA CUP ili tuweze kuwashirikisha vijana katika michezo

Anonymous said...

SDIWANI TUNAOMBA UANZISHE MYIKA CUP

Anonymous said...

Mheshiwa Mbunge, tumependa kazi ya jana, endeleza msimamo.

Vijana Tunaomba MNYIKA Cup kama bwana hapo juu alivyo changia

Anonymous said...

Kaka big up,wafundishe wazee wanaojiita wakongwe bungeni nini maana ya uwakilishi,what ua doing ni uwakilishi sio ubosi kama hawa wazee wanavyotufanya huko mikoani.