Sunday, August 26, 2012

Mrejesho wa ufuatiliaji wa hali duni ya barabara jimboni Ubungo


Nimeziandikia mamlaka husika za Serikali kutoka ofisini na kwenda kukagua wa ubovu wa barabara za Kimara-Mavurunza-Bonyokwa, Ubungo Maziwa-Kisiwani Darajani- Mabibo External, Makuburi-Kibangu-Makoka ili kuweza kufanya maamuzi ya matengenezo ya haraka.

Nimechukua hatua hiyo baada ya kuona hali halisi ya barabara hizo nilipozitembelea kati ya tarehe 24 na 25 Agosti 2012 na pia kutokana na maoni ya wananchi niliokutana nao katika tarehe hizo kwenye kata za Kimara, Mabibo na Makuburi.

Kwa upande wa Barabara ya Kimara-Mavurunza-Bonyokwa ambayo tayari Wizara ya Ujenzi imekubali kuihudumia, leo tarehe 27 Agosti 2012 nitapeleka barua kwa meneja wa TANROADS Mkoa wa Dar es salaam kutaka hatua zake kwa hali mbovu ya barabara hiyo pamoja na kuwa kero wa wananchi inamwaibisha Rais Kikwete mbele ya wakazi husika kwa kuwa alitembelea mwaka 2010 na kuahidi itajengwa kwa kiwango cha lami.

Aidha, mwaka 2011 ilifanyiwa matengenezo ya kawaida lakini kwa sasa imeharibika tena kufuatia mvua zilizonyesha, hali mbovu ya barabara hiyo inaathiri pia hatua za kupunguza msongamano kwenye barabara ya Morogoro wakati huu ujenzi wa mradi wa mabasi yaendayo haraka (DART) unapoendelea kwa kuwa barabara hiyo hutumika kama njia mbadala kutoka Manispaa ya Kinondoni mpaka Manispaa ya Ilala.

Kuhusu barabara Ubungo Maziwa-Kisiwani Darajani-Mabibo External leo nitamkumbusha Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam ambaye pia ni mwenyekiti wa bodi ya barabara kwa mkoa afuatilie kutoka mfuko wa barabara fedha za ujenzi wa daraja kwa dharura kwa kuwa kwa hali ya sasa na uzito wa magari yanayopita daraja linaweza kuvunjika na kusababisha maafa. Aidha, asimamie pia utekelezaji wa upande wa TANROADS kwa kuwa fedha za kuanza ujenzi wa barabara hiyo zilishatengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012 na nyingine katika bajeti ya mwaka wa fedha 2012/2013.

Kwa upande wa barabara ya Makuburi-Kibangu-Makoka mpaka sasa matengenezo yanasubiri malipo yafanyike ya fidia ya nyumba chache zilizobaki kiasi cha shilingi milioni 64, suala ambalo Manispaa ya Kinondoni inapaswa kulitolea kauli kwa kuwa lilipaswa kukamilika katika mwaka wa fedha 2011/2012 uliomalizika tarehe 30 Juni 2012, leo nimemuagiza katibu msaidizi wa mbunge kufuatilia suala hilo katika ofisi za Manispaa. Mpaka kufikia tarehe 3 Mei 2012 jumla ya shilingi milioni 122 zilikuwa zimeshalipwa kama fidia, hivyo Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Manispaa ya Kinondoni kuharakisha malipo ili kuepusha gharama za fidia kuongezeka kwa kuzingitia kuwa iwapo malipo yangefanyika kwa wakati mwaka 2010 gharama za fidia zingekuwa milioni 80 tu lakini sasa zimeongezeka mpaka kufikia zaidi ya milioni 180.

Wakati hatua za haraka za serikali zikisubiriwa kuwezesha matengenezo makubwa nitawaeleza karibuni utaratibu kwa kushirikiana na madiwani kwa ajili ya kuunganisha wananchi wa maeneo husika na wadau wengine ili kufanya matengenezo madogo kupunguza kero.

Izingatiwe kuwa tarehe 24 na 25 Agosti 2012 nimekwenda mitaa mbalimbali ya kata 12 kati ya 14 za Jimbo la Ubungo kuhamasisha wananchi kushiriki kwenye sensa ya watu na makazi na kujiandaa kutoa maoni ya katiba mpya.

Aidha wananchi niliokutana nao wamepata fursa ya kuuliza maswali kuhusu hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo na mrejesho kuhusu mkutano wa nane wa bunge ambapo pamoja na kupata majibu nimepokea pia mapendekezo ya masuala ya kuyapa kipaumbele katika kuwawakilisha na kuwatumikia jimboni katika kipindi cha mwezi Septemba mpaka Oktoba 2012 kabla ya kuanza kwa mkutano wa tisa wa bunge na pia kuhusu maandalizi ya mwaka 2013.

John Mnyika (Mb)
Jimbo la Ubungo
27/08/2012

1 comment:

Emmanuel Lema said...

Mbunge wangu nakushukuru sana kwa mrejesho huu muhimu na wa kueleweka. Tunasubiri tu utekelezaji wa haraka wa hatua hizi. Naamini kabisa kuwa kama madiwani wetu wakifuatilia kwa karibu hatua ambazo umeshazichukua ni wazikuwa wahusika watakuwa punctual.

Barabara yetu ya kuja makoka angalau kwa sasa inapitika bila tabu nyingi baada ya greda kuchimba lakini hatua zaidi hasa kuweka mitaro na kusawazisha pamoja na kuwa na outlet ya kuaminika kuingia Mandela Road ni muhimu ili kuongeza idadi ya daladala ziendazo makoka na kurasimisha njia ya daladala. Hivi vitapunguza adha kwa wananchi na kujenga imani ya wananchi kwa serikali.

Hata hivyo mbunge wangu jambo muhimu ni kwa wananchi kuwa na imani na wewe mbunge ambaye walikuchagua kwa kura nyingi na imani kubwa. Usikubali kurudishwa nyuma na madiwani. Wao ndiyo mikono na miguu yako kwa wananchi, wao ndiyo macho na masikio yako kwa wananchi. Wakilala wao wananchi watapoteza imani na sisi CHADEMA.

Tunwajibika sote kwa maendeleo yetu.

Emmanuel P Lema
box 35041 DSM
0717/0767 151125/0686 878384