Thursday, September 12, 2013

Mnyika ahoji ziliko fedha za DECI

na Shehe Semtawa

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amemtaka Gavana wa Benki Kuu, Benno Ndulu, kuwaeleza waliokuwa wanachama wa Kampuni ya Development Entrepreneurship for Community Initiative (DECI) fedha zao zilizotaifishwa na serikali kutoka kwenye taasisi hiyo ziko kwenye akaunti gani.

Mnyika alisema kuwa wakati sakata la DECI linaanza mwaka 2009, serikali ilitaifisha jumla ya sh bilioni 19, sawa na asilimia 40 ya fedha zote ambazo wanachama wa taasisi hiyo iliyokuwa ikiendesha na kusimamia mchezo wa upatu walikuwa wakidai.

Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara juzi Mtaa wa Mavurunza, Kata ya Kimara baada ya kuulizwa swali na mmoja wa wananchi aliyetaka kujua hatima ya fedha zao, Mnyika alitoa tahadhari kuwa danadana inayotaka kufanywa na serikali inaweza kutia shaka kuwa fedha hizo hazipo.

”Sasa naomba nimjibu yule mwananchi aliyetaka kujua hatima ya fedha za DECI. Mtakumbuka hili suala nimekuwa nikitaka majibu yake bungeni, lakini kila mara wanatumia kisingizio kuwa suala hili liko mahakamani.

Tuesday, September 10, 2013

Mnyika: Serikali imalize tatizo la maji

na Abdallah Khamis

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika, ameitaka serikali kuhamisha nguvu na kasi zilizotumika katika ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara kuelekea jijini Dar es Salaam na kumaliza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi hususan katika Jimbo la Ubungo.

Mnyika alitoa kauli hiyo juzi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kata ya Kimara, Mtaa wa Mavurunza na kusisitiza hakuna suala muhimu kama maji kwa wananchi na kwamba kunahitajika ufumbuzi wa muda mfupi na mrefu, ikibidi kwa hali ya dharura.

Alisema kama serikali inaweza kutumia muda mfupi kujenga na kutandaza bomba hilo kwa nini ishindwe kufanya hivyo kwa mabomba ya maji, ambayo ni uhai wa wananchi.

“Tunaendelea kupambana kuhakikisha tatizo la maji tunalipunguza na kuliondoa kabisa, ninachowaomba ni sauti zenu na mshikamano wenu, suala hili ni uhai wa watu, kama maji ni tatizo maana yake uhai wa binadamu uko shakani,” alisema Mnyika.