Friday, January 25, 2013

Salamu za Maulid na Barua ya wazi kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba

Nawatakia heri katika Maulid an-Nabi, ni siku ya kukumbuka kuzaliwa na maisha ya Mtume Muhammad (S.A.W)! Ifuatayo ni barua ya wazi kwa tume ya mabadiliko ya Katiba;


BARUA YA WAZI KWA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA 

Mwenyekiti, 

Tume ya Mabadiliko ya Katiba, 

Dar es Salaam 

Mheshimiwa, 

YAH: KUPANUA WIGO WA KUKUSANYA MAONI YA WANANCHI BINAFSI KWA SIMU ZA MKONONI NA MAKUNDI YA WANANCHI KATIKA MABARAZA YA KATIBA 

Nakuandikia nikirejea maelezo yako kwenye mkutano wako na waandishi wa habari tarehe 5 Januari 2013 kuhusu mchakato wa ukusanyaji maoni ya mabadiliko ya katiba. 

Maelezo uliyotoa yanadhihirisha upungufu katika mchakato wa ukusanyaji wa maoni ya wananchi binafsi unaoelezwa kukamilika kwa kuwa na idadi ndogo ya watu waliotoa maoni mpaka sasa ambapo mpaka awamu nne zinakamilika jumla ya watu 318,223 tu ndio waliotoa maoni; kwa tafsiri yangu hii ni sawa na asilimia 0.7 ya wananchi wote zaidi ya milioni 44.9. 

Upungufu huo uko zaidi katika utoaji maoni kwa simu za mkononi ambapo kwa mujibu wa maelezo yako wananchi waliotoa maoni kwa njia hiyo ni 16,261 tu; kwangu mimi hii ni sawa na asilimia 0.08 ya idadi ya wateja wa makampuni ya simu za mkononi ambao watajwa kuwa zaidi ya milioni 20 (mobile phone subscribers).

Thursday, January 24, 2013

Nimemwandikia Spika Bunge liwezeshe ufumbuzi wa mgogoro wa gesi asilia

BUNGE LIINGILIE KATI KUWEZESHA UFUMBUZI WA MGOGORO WA GESI MTWARA. SPIKA ATUMIE MAMLAKA YAKE KUELEKEZA KAMATI ITAYOKUTANISHA SERIKALI NA WANANCHI. RAIS NA SERIKALI WAJISAHIHISHE NA KUONDOA UDHAIFU BADALA YA KUENDELEA KULAUMU NA KUPOTOSHA 

Nimemwandikia barua Spika atumie mamlaka na madaraka yake kutoa nafasi Bunge liingilie kati kuwezesha ufumbuzi wa mgogoro unaoendelea kati ya Serikali na wananchi kuhusu utafutaji, uvunaji, usafirishaji na utumiaji wa gesi asilia kutoka Mtwara.

Katika hatua ya sasa Serikali ni kupitia Wizara ya Nishati na Madini na taasisi zake ni sehemu ya watuhumiwa na washutumiwa hivyo ni muhimu majadiliano kati ya Serikali na wananchi kuwezesha ufumbuzi wa mgogoro huo yakasimamiwa na muhimili mwingine kwa dola.

Rais naye tayari ameshachukua upande bila kusikiliza kwa kina na kuyaelewa madai ya wananchi hivyo katika hali ya sasa ni muhimu kurejea katika madaraka na mamlaka ya wabunge kwa mujibu wa katiba ya nchi kuwezesha ufumbuzi wa mgogoro huu kuepusha hali tete inayoweza kuzuka na kuathiri uchumi na usalama katika maeneo husika.

Katiba ya Nchi Ibara ya 63 (2) inaelekeza kwamba sehemu ya pili ya Bunge (inayoundwa na wabunge) itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa katiba.

Monday, January 21, 2013

SPIKA ASILINDE UFISADI KIWANDA CHA URAFIKI NA WAZIRI KIGODA ASIKWEPE KUTOA MAJIBU

Tarehe 21 Januari 2012 gazeti la Tanzania Daima limemnukuu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Viwanda na Biashara akieleza kuwa wameunda Kamati Ndogo ya Uchunguzi kuhusu ufisadi wa miaka mingi wa Kiwanda cha Nguo cha Urafiki lakini wanasubiri idhini ya Spika kamati hiyo ianze kazi. Habari hiyo imeeleza kuwa Spika ndiye anayekataa uchunguzi huo kufanyika.

Nikiwa mbunge wa Jimbo la Ubungo, mahala kilipo Kiwanda cha Urafiki nasisitiza umuhimu wa Spika kutoa kauli kwa umma kuhusu hatua alizochukua ikizingatiwa kwamba hata kabla ya kamati ndogo ya uchunguzi kuundwa nilishawasilisha kwa Spika wa Bunge maelezo binafsi kuhusu ufisadi huo na mpaka sasa hajatoa idhini yashughulikiwe.

Aidha, majibu ya Waziri wa Viwanda na Biashara Dk Abdalah Kigoda kuwa anafuatilia suala hilo Wizarani hayajitoshelezi kwa kuzingatia kuwa zaidi ya nusu mwaka umepita toka atoe ahadi ya kufuatilia Wizarani; wafanyakazi wa Urafiki na wananchi kwa ujumla wanachohitaji kuelezwa ni hatua zilizochukuliwa mpaka sasa.

Sunday, January 20, 2013

HOTUBA YA JOHN MNYIKA (MB) ALIYOITOA TAREHE 20 JAN, 2013 KATIKA UFUNGUZI WA MKUTANO WA BARAZA LA WANAWAKE WA CHADEMA (BAWACHA) JIMBO LA UBUNGO ULIOFANYIKA KATIKA UKUMBI WA MATUNGUCHA KATA YA SARANGA

Viongozi wa BAWACHA Taifa,

Waheshimiwa Wabunge wa viti maalum,

Viongozi wa CHADEMA Jimbo la Ubungo,

Viongozi wa BAWACHA Jimbo la Ubungo,

Waheshimiwa Madiwani wa kata na viti maalum,

Viongozi wa BAWACHA toka kata zote za Jimbo la Ubungo.

Niungane nanyi katika kumshukuru Mungu kwa kutupa uzima na kuendelea na kazi katika mwaka mpya wa 2013. Kwa wale ambao hatujakutana mwezi huu wa Januari, nitumie fursa hii kuwatakia mwaka mpya mwema wenye upendo na uwajibikaji.

Nawashukuru kwa kunialika kuzungumza machache kwenye Mkutano huu wa Baraza la Wanawake wa CHADEMA (BAWACHA) Jimbo la Ubungo na niwapongeze waandaaji kwa kuweza kuwakutanisha pamoja viongozi kutoka kata zote na wawakilishi wa wanachama kutoka katika matawi na misingi na BAWACHA katika mitaa mbalimbali ya Jimbo la Ubungo.

Mwezi Disemba 2012, CHADEMA taifa kiliutangaza 2013 kuwa ni mwaka wa ‘nguvu ya umma’. Kufuatia tamko hilo la Kamati Kuu, viongozi mbalimbali wa CCM walianza propaganda chafu kupitia vyombo vya habari kuwa CHADEMA imetangaza mwaka wa ‘vurugu’.

Propaganda hizo zinalenga kutisha umma, hususan wanawake wasiunge mkono vuguvugu la mabadiliko (M4C), kujiunga kwenu kwa wingi katika Jimbo la Ubungo kunadhihirisha kuwa wanawake hamko tayari kudanganywa kwa siasa chafu na mnaendelea kuiunga mkono CHADEMA; asanteni sana.

Saturday, January 19, 2013

Ziara Jimboni: KATA YA MANZESE 08 Desemba, 2012

Ziara ndani ya Jimbo: muendelezo wa kutembelea maeneo mbalimbali ya jimboni. Jana, Desemba 08, 2012 ziara kubwa ilifanyika katika kata ya MANZESE.

Ziara ilimudu kutembelea ofisi ya kata (Kilimani), kufungua misingi katika mitaa ifuatayo; Kilimani, Chakula bora, Mvuleni, Midizini, Mwembeni, na Mnazi Mmoja.

Kisha mkutano wa hadhara na wananchi wa mtaa wa Mnazi Mmoja.


Shirika la Umeme (TANESCO) linakabiliwa na ufisadi na uzembe unaoongeza gharama za uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme kwa upande mmoja na uendeshaji wa shirika kwa upande mwingine. Ufisadi na uzembe huo unapunguza uwezo wa TANESCO kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika na unaongeza gharama na bei ya upatikanaji wa umeme hali inayoathiri uchumi wa nchi na maisha ya wananchi kwa kuchangia katika mfumuko wa bei na ongezeko la gharama za maisha. Mzigo wa ufisadi na uzembe katika TANESCO unajitokeza zaidi katika mikataba mibovu pamoja na ukiukwaji wa sheria za ununuzi wa umma, ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.

Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 63 sehemu ya pili ya bunge (inayoundwa na wabunge) ndio chombo kikuu chenye madaraka na mamlaka kwa niaba ya wananchi ya kuisimamia serikali. Hata hivyo, katika kipindi cha kati mwaka 2008 mpaka 2012 maazimio ya Bunge kuhusu sekta ya nishati ikiwemo kuhusu umeme yamekuwa hayatekelezwi kwa wakati na kwa ukamilifu hali inayofanya tuhuma za ufisadi na uzembe kuendelea kujirudiarudia. Katika muktadha huo, ni muhimu kwa kuwa kwa mujibu wa Katiba ya nchi ibara ya 8 madaraka na mamlaka ni ya umma (serikali inafanya kazi kwa niaba tu) ipo haja ya kuanza kuunganisha ‘nguvu ya umma’ katika kushinikiza hatua kuchukuliwa kwa wahusika wa ufisadi na uzembe ili kuweka misingi bora ya uwajibikaji katika sekta ya nishati.

Friday, January 18, 2013

Rais na Mawaziri wanadharau wabunge kuhusu mabadiliko ya mzunguko wa Bajeti

Yaliyojiri na yanayoendelea kujiri ndani ya Baraza la Mawaziri na Wizara ya Fedha kuhusu mabadiliko ya mzunguko na mchakato wa bajeti yanaashiria kwamba Rais na Serikali wanadharau mamlaka na madaraka ya Bunge na wabunge.

Aidha, kutokana na umuhimu wa mzunguko na mchakato wa bajeti katika kuwezesha uwajibikaji kwenye mapato na matumizi ya rasilimali za umma; Waziri wa Fedha anatakiwa aweke wazi kwa umma mabadiliko hayo yaliyofanyika ili wananchi na wadau waweze kutoa maoni na Bunge liweze kuyazingatia wakati wa marekebisho ya kanuni za Bunge yanayotarajiwa kufanywa katika mkutano wa kumi wa Bunge.

Wakati Katibu wa Bunge amenukuliwa tarehe 17 Januari 2013 akisema kwamba pendekezo la mabadiliko ya mzunguko na mchakato wa bajeti bado linajadiliwa na kwamba iwapo litaafikiwa, uamuzi utatangazwa mapema mwezi ujao (Februari 2013) wakati wa mkutano wa Bunge; upande wa Rais na Wizara ya Fedha wameshapitisha na kuanza kutekeleza mzunguko na mchakato mpya wa bajeti kuanzia mwezi Disemba 2012.

Tuesday, January 15, 2013

Sera ya majimbo ni siri ya maendeleo ya nchi na wananchi

Na John J.Mnyika

Mwaka 2007 miaka miwili baada ya uchaguzi wa mwaka 2005 palijitokeza mjadala kuhusu sera ya majimbo. Mwaka 2012 ikiwa ni miaka miwili tena toka uchaguzi wa mwaka 2010 pameibuka kwa mara nyingine mjadala kuhusu sera ya majimbo kufuatia maandamano ya wananchi wa Mtwara juu ya madai ya gesi. Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospter Muhongo amenukuliwa na gazeti moja tarehe 29 Disemba 2012 akiponda sera ya majimbo ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa ni mbovu na haitumiki kokote duniani; kauli ambayo haina ukweli kama nitavyoeleza katika makala hii. Amedai madai ya rasilimali za wananchi wa eneo hayana msingi na kuwaita wote wenye kujenga hoja hiyo kuwa wanataka kuigawa nchi vipande vipande, majibu ambayo ni mwendelezo wa propaganda chafu.

Prof. Muhongo badala ya kujibu hoja za waandamanaji na wananchi wa Mtwara ameamua kuibua ‘vioja’ vya kuishambulia CHADEMA na sera yake ya majimbo. Wakati hata kwa sera za CCM na serikali ya sasa, maandamano ya wananchi wa Mtwara kutaka majibu toka kuhusu manufaa ya miradi ya gesi asili inayotoka katika maeneo yao ni matokeo ya madai ya ufisadi wa baadhi ya viongozi na udhaifu wa Serikali katika kuushirikisha umma katika michakato ya maamuzi ya kisera na kitaasisi kuhusu rasilimali na miradi muhimu ya maendeleo. Aidha, ni matokeo pia Bunge kutokuisimamia kikamilifu Serikali kwa niaba ya wananchi kwa mujibu wa ibara ya 63 ya katiba wakati serikali inapoacha kufafanua masuala yanayohojiwa na wabunge na inapokwepa kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu sekta ya nishati ikiwemo sekta ndogo ya gesi asili.

Saturday, January 5, 2013

Nimewasilisha Muswada Binafsi wa Sheria ya kuunda Baraza la Taifa la Vijana


Jana tarehe 4 Januari 2012 niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge taarifa ya muswada binafsi wa Sheria ya kuunda Baraza la Taifa la Vijana (The National Youth Council Bill, 2013) kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (1) na Taarifa ya Muswada huo kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (2) ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007).

Nimechukua hatua hiyo kwa kuwa kwa miaka zaidi ya kumi Serikali imekuwa ikiahidi karibu kila mwaka bungeni kuwa itawasilisha muswada wa kuunda baraza la vijana la taifa lakini haijawahi kutekeleza ahadi hiyo; nimeamua kuitekeleza ahadi hiyo kwa kupeleka bungeni muswada binafsi wa kuunda baraza la vijana la taifa.

Katika taarifa hiyo ya muswada nimewasilisha madhumuni, sababu pamoja na nakala ya muswada wenyewe wa sheria ya kuanzisha Baraza la Vijana la Taifa kwa madhumuni ya kuanzisha chombo cha kuwaratibu vijana wa Tanzania katika kutekeleza shughuli zao kijamii, kuuchumi, kiutamaduni na kimichezo, na kuchagiza hali ya utambulisho wa Kitaifa wa pamoja na uzalendo.

Friday, January 4, 2013

Washindi wa Shindano la Ujasiriamali Jimbo la Ubungo wapatikana

Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Ubungo kwa ushirikiano na shirika la Maendeleo Ubungo; Ubungo Development Initiative (UDI) waliendesha shindano la kuwainua wajasiriamali wadogo wadogo na hususan vijana wasio na ajira (na walio katika mazingira magumu) kwa kuwataka kuandaa mchanganuo namna gani watatumia Tsh 200,000/- katika kuanzisha au kuiendeleza biashara zao. Washindi waliopatikana ni;
Mshindi wa Kwanza: Joseph R. Shindo (22) kutoka Kata ya Kimara Tsh 200,000/-

Thursday, January 3, 2013

Hatua kuhusu matumizi ya dola milioni 164.6 za “mabomba ya mchina” na mikataba ya miradi ya sasa ya maji jijini Dar es salaam

Tarehe 3 Januari 2013 kwa kutumia kifungu cha 10 cha sheria ya haki, kinga na madaraka ya Bunge nimetaka Wizara ya Maji inipatie nakala ya ripoti ya utekelezaji wa mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam na maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and Sanitation Project-DWSSP) uliotekelezwa kati ya mwaka 2003 mpaka 2010 jijini Dar es salaam.

Nimetaka ripoti hiyo ili kubaini matumizi ya dola milioni 164.6 zinazoelezwa kutumika katika mradi huo maarufu kama wa ‘mabomba ya mchina’ kwa kuwa mpaka sasa mwaka 2013 sehemu kubwa ya mabomba yaliyowekwa wakati wa mradi huo katika Jiji la Dar es salaam hayatoi maji huku kukiwa na upungufu katika uzalishaji, upotevu wakati wa usafirishaji, udhaifu katika usambazaji na tuhuma za ufisadi katika matumizi.

Pamoja na kutaka ripoti ya utekelezaji wa mradi huo, nimetaka pia nakala ya ripoti ya ukaguzi wa kiufundi (technical Audit) uliofanywa na kampuni ya Howard Humphreys kuhusu mradi huo.

Nimetaka pia kupatiwa ripoti za ukaguzi uliofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Kampuni ya Maji Dar es salaam- DAWASCO (Dar es salaam Water Supply and Sewerage Company) na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka-DAWASA (Dar es Salaam Water Supply and Sewerage Authority) kwa mwaka miaka mitatu ya 2009/10, 2010/2011, 2011/2012 ili kuweza kufuatilia hatua zinazostahili kuchukuliwa.

Ufafanuzi wa Waziri Muhongo:ukweli umefichwa, upotoshaji unaendelea!


Nimesoma taarifa ya serikali iliyotolewa na Waziri Prof. Muhongo kufafanua kuhusu miradi ya utafutaji na uvunaji wa gesi asili nchini. Hatimaye serikali imeanza kutoa ufafanuzi suala ambalo ilikwepa kulifanya bungeni hata baada ya kuhoji 2011 na 2012. Hata hivyo ufafanuzi huo haujitoshelezi kwa kuwa kuna ukweli umeendelea kufichwa na upotoshaji umejirudia kama ambavyo nitafafanua katika kauli yangu nitakayotoa siku chache zijazo kwa kuwa leo niko katikati ya kushughulikia usiri na udhaifu katika mikataba na miradi ya Maji jijini Dar es Salaam.

Maslahi ya Umma Kwanza

John Mnyika (MB)
Waziri Kivuli, Nishati na Madini
03 Januari 2013

Wednesday, January 2, 2013

Toka analojia hadi digiti: Nini maoni yetu?


Naomba majibu yenu kwa kuzingatia kuwa kazi ya wabunge ni kuishauri na kuisimamia Serikali: baada ya kutekelezwa kwa uamuzi wa kuhama kutoka analojia kwenda digiti kwa mkoa wa Dar es salaam; kwa watumiaji, nini faida na athari mlioanza kuzipata kwa wenye ving’amuzi?

Na nini kikwazo kwa wengine ambao hamjahamia mpaka sasa? Na nini mnataka watoa huduma na mamlaka zingine kuzingatia? Katika hatua ya sasa, ni muhimu Tanzania Consumer Advocacy Society (TCAS) ifanye tathmini ya kina kwa niaba ya watumiaji kwa ajili ya hatua zake.