Wednesday, February 27, 2013

NCHI IMEINGIA TENA KWENYE MGAWO WA UMEME, SERIKALI IELEZE WANANCHI UKWELI NA HATUA KUHUSU UDHAIFU KWENYE UTEKELEZAJI WA MPANGO WA DHARURA

Nchi imeingia tena katika mgawo wa umeme kinyume na ahadi iliyotolewa na Waziri wa Nishati na Madini Prof Sospeter Muhongo bungeni tarehe 28 Julai 2012. 

Hali hiyo ni matokeo ya Serikali kutozingatia tahadhari niliyoitoa bungeni tarehe 27 Julai 2012 kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani na kwa nyakati mbalimbali kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini juu ya hali tete iliyotarajiwa kuwepo na hatua zinazopaswa kuchukuliwa katika utekelezaji wa mpango wa dharura wa umeme. 

Ikiwa ni sehemu ya wajibu wa kibunge wa kuisimamia Serikali nawataka viongozi na watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kuacha kuficha hali ya mambo na kuwaeleza ukweli wananchi kuhusu mgawo wa umeme uliojitokeza na hatua za haraka zinazochukuliwa kurekebisha hali hiyo. 

Iwapo Wizara na TANESCO hawatatoa matangazo ya ukweli kwa wananchi, kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini nitaeleza vyanzo vya mgawo wa umeme uliojitokeza ili hatua ziweze kuchukuliwa wakati huu ambapo wajumbe wa kamati ya nishati na madini wenye wajibu wa kuisimamia Serikali kwa niaba ya Bunge katika sekta hizo nyeti hawajateuliwa.

Monday, February 25, 2013

Mnyika amuweka Maghembe kitanzini

NA RICHARD MAKORE

Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, amemuweka katika wakati mgumu Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, baada ya kutoa hadharani namba ya simu ya waziri huyo ili wananchi wamuulize ni lini atatekeleza ahadi ya kuwapatia huduma ya maji wananchi wa jimbo hilo.

Mnyika alitoa namba ya simu ya Profesa Maghembe na Naibu wake, Dk. Binillith Mahenge, wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika viwanja vya Goba mwisho na kuwataka wananchi kuwauliza viongozi hao wakuu wa Wizara ya Maji ni lini watapatiwa huduma ya maji ambayo imekosekana kwa zaidi ya miaka miwili sasa.

Mnyika alisema Profesa Maghembe akihututubia wananchi hao aliwapa namba ya simu ‘feki’ na kwamba alifanya hivyo kutokana na kuwadharau.

Februari 17 mwaka huu, Profesa Maghembe akihutubia mkutano wa hadhara eneo la Goba mwisho alikaririwa akisema kwamba huduma ya maji ingeanza kupatikana Februari 20, mwaka huu, lakini hadi kufikia juzi ahadi hiyo haijatekelezwa.

Profesa Maghembe alikaririwa akisema serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndiyo ina funguo za kufungua maji ama kuyafunga na kuwataka wananchi wa Kata ya Goba kumuamini kwamba Februari 20, mwaka huu wangepata maji.

Mnyika alisema ni aibu kwa Waziri akiwa na viongozi wa kitaifa wa CCM kutoa ahadi hewa na kwamba ataongoza maandamano makubwa ya wananchi wa jimbo lake kuvamia ofisi za Profesa Maghembe kwenda kudai maji.

Sunday, February 24, 2013

UFUMBUZI WA MADAI YA FIDIA MILIONI 278 KWENYE UJENZI WA BARABARA NA DARAJA GOLANI SUCA

Tarehe 19 Februari 2013 Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alifanya ziara ya kikazi katika kata za Kimara na Saranga kufuatilia kuhusu matengenezo ya barabara na daraja la Golani. 

Mnyika alifanya hivyo siku mbili tangu afanye mkutano wa kikazi na viongozi wa Serikali ya Mtaa wa Kanuni na wananchi katika kata ya Mabibo tarehe 16 Februari 2013 kulitolewa malalamiko kuhusu Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) kutoshughulikia maombi ya wananchi yaliyowasilishwa kwa kampuni hiyo kwa nyakati mbalimbali kati ya mwaka 2010 mpaka 2012. 

Ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji huo kuhusu barabara, Mnyika alikutana na wananchi ambapo walipaswa kulipwa fidia inayokadiriwa kufikia shilingi milioni 278 ili kuruhusu njia mbadala kupatikana kufuatia ujenzi wa daraja katika eneo hilo. 

Aidha, Mbunge amekagua matumizi ya daraja hilo yaliyoanza kupitia njia ya zamani na athari zake katika mfumo mzima wa usafiri katika eneo husika; na kubaini kwamba daraja husika haliwezi kuzinduliwa pamoja na kuwa limeanza kukamilika mpaka ujenzi wa kingo za mito ukamilike pamoja na kupatikana kwa barabara mbadala baada ya wananchi kulipwa fidia. 

Mara baada ya ziara hiyo Mbunge alikutana na uongozi wa Manispaa ya Kinondoni na kuwasilisha madai hayo ya wananchi ambao miezi zaidi ya sita imepita toka nyumba zao ziwekewe X bila hata ya kufanyiwa tathmini. Baada ya Mnyika kuwawakilisha wananchi hao uongozi wa Manispaa umeamua kutuma timu ya uthamini na mara baada ya uthamini huo, kutuma uongozi kukamilisha majadiliano na wananchi husika kabla ya tarehe 25 Februari 2013

Saturday, February 23, 2013

Ziara Kimara: Ukaguzi ulipaji fidia, upanuzi wa barabara na kuhakiki ujenzi wa daraja!


Mbunge wa Ubungo, John Mnyika akizungumza na mkazi wa Kimara Korogwe, Richard Paul wakati mbunge huyo alipokutana na wakazi hao kutaka kujua fidia wanazotaka kulipwa kutokana na upanuzi wa barabara, pia alitembelea ujenzi wa daraja katika eneo hilo. 



Tuesday, February 19, 2013

BAADA YA HOJA BINAFSI NA KUSUDIO LA MAANDAMANO; WAZIRI WA MAJI NA MKUU WA WILAYA WAENDA GOBA NA MAENEO MENGINE KUFUATILIA MIRADI YA MAJI

Nitafuatilia ahadi alizotoa Waziri wa Maji Prof. Jumanne Maghembe tarehe 17 Februari 2013 kuwa maji yataanza kutoka kata ya Goba tarehe 20 Februari 2013 na ziara ya Mkuu wa Wilaya Jordan Rugimbana kwenye kata hiyo. 

Hata hivyo, ni vizuri umma ukatambua kuwa pamoja na mabadiliko ya hoja kwa kuongeza maneno ya kupendekeza hoja kuondolewa yaliyofanywa na Waziri wa Maji Prof. Jumanne Maghembe kinyume na kanuni za Bunge tarehe 4 Februari 2013, maelezo na hoja binafsi niliyowasilisha bungeni yameongeza uwajibikaji wa Waziri wa Maji, Mkuu wa wilaya ya Kinondoni na Halmashauri kuhusu masuala ya maji. 

Siku chache baada ya kutangaza tarehe 10 Februari 2013 kwenye mkutano wa hadhara kuipa Serikali wiki mbili, Mkuu wa Wilaya na Meya wa Halmashauri ya Kinondoni waliitisha mkutano na viongozi wa mitaa pamoja na kamati za miradi ya maji ya jumuiya na leo tarehe 18 Februari 2013 Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Jordan Rugimbana ameanza ziara ya ufuatiliaji wa miradi ya maji katika Jimbo la Ubungo. 

Sunday, February 17, 2013

HALI TETE YA UPATIKANAJI WA MAJI JIJINI DSM; DAWASA NA DAWASCO WAWAJIBISHWE

Kwa nyakati mbalimbali kuanzia mwezi Januari mpaka Februari 2013 pametokea matatizo ya kuharibika kwa baadhi ya mitambo na kupungua kwa uzalishaji wa maji katika vyanzo vya mto Ruvu na hivyo kusababisha matatizo ya maji kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam na maeneo yanayohudumiwa na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) katika Mkoa wa Pwani. 

DAWASA imeingia mkataba wa uendeshaji na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO) wa kutekeleza majukumu mbalimbali ikiwemo kuendesha mitambo, kusimamia usambazaji wa maji na kufanya matengenezo na kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu huduma zinazotolewa. Aidha, DAWASCO wanapaswa kuzingatia mikataba ya huduma kwa wateja ambayo inaitaka kutoa taarifa kwa umma pale kunapotokea matatizo ya maji. 

Kwa kuzingatia mikataba hiyo, DAWASA na DAWASCO wanapaswa kutoa matangazo kwa umma kuhusu matatizo mapya yaliyojitokeza mwezi Januari na Februari 2013 ili kuepusha matatizo hayo kuhusishwa na hatua ya kuwasilishwa na kuondolewa bungeni kwa hoja binafsi niliyoiwasilisha tarehe 4 Februari 2013 juu ya hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam. 

Kwa wakazi wa Kibamba, Kwembe, Msigani, Mbezi, Saranga na Kimara ni muhimu wakatambua kwamba nimefuatilia na kujulishwa kwamba palikuwa na tatizo la kupungua kwa uzalishaji wa maji katika chanzo cha Ruvu Juu ambalo limerekebishwa tarehe 12 Februari 2013 hivyo maji yataendelea kupatikana kwa mujibu wa ratiba ya mgawo kama ilivyokuwa awali katika maeneo ambayo yalikuwa yakipata maji tangu mwaka 2012. 

Kwa wateja ambao bado watakuwa na matatizo katika maeneo yao wawasiliane na DAWASCO kupitia namba ya huduma kwa wateja 022 55 00 240 au 0779090904 au info@dawasco.com ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa. 

Monday, February 11, 2013

Sunday, February 10, 2013

Waraka wa Kwanza kwa mwaka 2013 wa Mbunge kwa Wananchi


“Maji; kwa Nguvu ya Umma”:

Waheshimiwa Wananchi wenzangu, Katiba ya Nchi pamoja na ubovu wake inatamka katika Ibara ya 63 (2) kwamba “Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa katiba”.

Hata hivyo kutokana na uzembe wa uongozi wa Bunge wa kushindwa kuzingatia na upuuzi wa wabunge wengi wa CCM kuridhia hoja ya kuondolewa hoja yangu binafsi; Bunge limeshindwa kutimiza wajibu wake wa kuisimamia Serikali kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es Salaam.

Katiba ya Nchi ibara ya 8 (1) inatamka kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii kwa hiyo wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, na serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa katiba.

Ibara hiyo inaendelea kueleza kwamba lengo kuu la serikali ni ustawi wa wananchi, Serikali itawajibika kwa wananchi na wananchi watashiriki katika shughuli za Serikali yao kwa mujibu wa masharti ya katiba hii.

Kwa kuwa wananchi mmekoseshwa fursa ya kushiriki kupitia mwakilishi wenu niliyewasilisha hoja binafsi kwa kuzingatia wajibu wa kibunge na mamlaka ya madaraka ya Bunge kwa mujibu wa ibara ya 63 na 100 ya Katiba ya Nchi; kwa waraka huu naiwasilisha hoja binafsi yangu kwenu wananchi muijadili na kufanya maamuzi mtayoona yanafaa.

Monday, February 4, 2013

MAELEZO NA HOJA BINAFSI YA KUPENDEKEZA BUNGE LIJADILI NA KUPITISHA MAAZIMIO YA HATUA ZA HARAKA ZA KUBORESHA UPATIKANAJI WA MAJI SAFI NA USHUGHULIKIAJI WA MAJI TAKA KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM KWA MUJIBU WA KANUNI YA 54 FASILI YA (1) YA KANUNI ZA KUDUMU ZA BUNGE TOLEO LA MWAKA 2007

Mheshimiwa Spika; 
Awali ya yote niungane na wote wenye mapenzi mapema katika kuomba ulinzi wa Mwenyezi Mungu wakati tukitimiza wajibu wa kibunge kwa mujibu wa ibara ya 63 ya Katiba ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania wa kuwawakilisha wananchi, kuisimamia serikali, kuidhinisha mipango na kutunga sheria.

Mheshimiwa Spika;
Aidha, kwa namna ya pekee ni kushukuru wewe binafsi na uongozi mzima wa Bunge kwa kunipa fursa hii adimu na adhimu ya kuwasilisha hoja binafsi kwa mujibu wa kanuni ya 54 fasili ya (1) ya kupendekeza bunge lijadili na kupitisha maazimio ya hatua za haraka zaidi za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam.

Mheshimiwa Spika;
Maji ni uhai, hivyo matatizo ya upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam na nchini kwa ujumla kama hatua za haraka zisipochukuliwa yatageuka kuwa janga la taifa. Katika kila watanzania katika Jiji la Dar es Salaam na nchini; kwa wastani mmoja hapati huduma ya maji safi na salama na hali ni mbaya zaidi kuhusu ushughulikiaji wa maji taka.

Wakati baadhi ya nchi duniani zikielezwa kwenye kitabu cha hivi karibuni cha Mnukuzi Maalum wa Umoja wa Mataifa (UN Special Rapporteur) kuwa katika mwelekeo unaostahili kuhusu kuhakikisha haki ya maji na usafi wa mazingira (On the right track; Good practices in realizing the rights to water and sanitation: 2012), hali ni kinyume kwa taifa letu.

Ripoti ya Taasisi ya Kimataifa inayoshughulikia masuala ya maji (WaterAid: 2011) imeiweka Tanzania katika kundi la nchi ambazo haziko katika mwelekeo unaostahili wa kuboresha upatikanaji wa maji safi, ushughulikiaji wa maji taka na usafi wa mazingira (Policy Report: Off Track, Off Target; why investments in water, sanitation and hygiene is not reaching those who need the most).

Mheshimiwa Spika;
Hoja hii inalengo la kuibua mjadala wa hatua za haraka. Kimsingi hatua hizi za haraka hazitanufaisha Mkoa mmoja pekee kwa kuzingatia kuwa Mpango Maalum wa kutatua tatizo la maji katika Jiji la Dar es salaam ni kwa ajili pia ya maeneo mengine ya miradi iliyo sehemu ya mpango huo ya Morogoro mpaka Pwani. Aidha, kujadiliwa na kupitishwa kwa mapendekezo ya hoja hii kutaongeza pia msukumo wa miradi katika maeneo mengine ya mijini na vijijini katika mikoa mbalimbali nchini.

Shukrani zangu za dhati ziwafikie wabunge wenzangu wa vyama vya upinzani na wa chama tawala kwa maoni na mapendekezo yenu yaliyoniwezesha kuirekebisha hoja hii pamoja na ushauri wa Katibu wa Bunge Dr Thomas Kashillilah na maafisa na watendaji katika ofisi ya bunge, kambi rasmi ya upinzani na ofisi ya mbunge wa Jimbo la Ubungo mlioboresha hoja hii kwa manufaa ya Jiji la Dar es Salaam na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika;
Nitumie pia nafasi hii kuwashukuru Watanzania wenzangu wa kada, hadhi na ngazi mbalimbali katika taasisi na maeneo mengi ndani na nje ya nchi mnaoendelea kuniunga mkono kwa hali na mali katika kutimiza majukumu yangu ya kibunge na nafasi nyingine ninazozitumikia.

Nawashukuru sala zenu wakati wa kesi ya msingi na rufaa ya kupingwa kwa matokeo ya ushindi wetu Jimbo la Uchaguzi la Ubungo; kwa pamoja tumeshinda, tuendelee na kazi.

Aidha, pamoja na mjadala huu wa bungeni natarajia kupokea maoni na mapendekezo yenu kuhusu hoja hii kwa njia mbalimbali za mawasiliano ikiwemo kupitia mtandao wa http://mnyika.blogspot.com kwa hatua zaidi. Kaulimbiu yetu ni ile ile: AMUA; Maslahi ya Umma Kwanza.


MAELEZO YA HOJA: 

Mheshimiwa Spika;
Maji ni mojawapo ya mahitaji ya msingi ya binadamu, maji ni uhai. Upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama ni sehemu ya muhimu ya maendeleo ya nchi na maisha ya wananchi. Maji ni lazima kwa matumizi ya majumbani, maji ni muhimu ni moja ya malighafi muhimu katika kazi za uzalishaji iwe ni za viwanda, kilimo, mifugo na shughuli zingine za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika;
Tanzania ni nchi ambayo imejaliwa vyanzo vingi vya maji, vinavyohusisha mito, mvua, maziwa na bahari; kuwepo kwa vyanzo hivi vya maji ni wazi kuwa nchi yetu inaweza kuepukana na shida ya maji inayoikumba jamii ya Tanzania iwapo tutaondoa udhaifu uliopo. Aidha, udhaifu huo unahusisha pia kuziweka vyanzo vyenyewe pia mashakani kwa matendo ya binadamu yenye kuathiri endelevu wa matumizi hali itayozua migogoro katika siku za usoni iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa.