Sunday, January 31, 2010

Hotuba yangu Jimboni Ubungo nikifungua Mafunzo ya Viongozi


HOTUBA YA MGENI RASMI-JOHN MNYIKA (MWENYEKITI WA MKOA WA KINONDONI KANDA MAALUM YA DAR ES SALAAM) KATIKA UFUNGUZI WA MAFUNZO YA VIONGOZI WA CHADEMA JIMBO LA UBUNGO YALIYOFANYIKA KATIKA HOTELI YA DELUXE DAR ES SALAAM TAREHE 31 JANUARI 2010.


Ndugu viongozi na wajumbe wa Kamati ya Utendaji;


Wawakilishi wa Kata mbalimbali;


Wageni Waalikwa, mabibi na mabwana;


Itifaki zote zimezingatiwa:


Nawashukuru kwa kunialika kuja kufungua haya mafunzo kuhusu uendeshaji wa chama na maandalizi ya uchaguzi ambayo yanafanyika Wilaya/Jimbo la Ubungo ndani Mkoa wetu wa Kinondoni Kanda Maalum ya Dar es salaam.


Katika mafunzo yenu mzingatie mambo ambayo ni kipaumbele katika kushamiri kwa chama cha siasa na kushinda kwa wagombea wake. Kwa tafsiri rahisi; chama cha siasa ni jumuia ya watu wenye dhamira inayofanana wakilenga kuchukua dola kwa njia za kidemokrasia ili kuweza kutekeleza azma yao kwa ustawi wa jamii. Na kabla ya kuchukua dola, chama kinakuwa na wajibu wa kuiwajibisha serikali iliyoko madarakani na chama kinachotawala.


Kwa hiyo fursa hii ya mafunzo iwawezeshe kutafakari mambo ya msingi yanayounda chama cha siasa na dhima yake kwa taifa. Msingi wa kwanza ni watu ambao kwenye chama cha siasa ni pamoja na wanachama na wapenzi wa chama, hivyo lazima kujifunza ni kwa vipi CHADEMA katika ngazi zenu na maeneo yetu kinaweza kupata wanachama na wapenzi zaidi na kuwashirikisha katika michakato ya demokrasia lakini pia michakato ya kimaendeleo katika jamii zinazowazunguka.


Msingi wa pili ni dhamira inayofanana, hii ni pamoja na falsafa, itikadi, sera za CHADEMA lakini pia inajumisha malengo na maamuzi ya pamoja. Mafunzo haya yawawezesha kuilewa zaidi dhamira hiyo, kuitafsiri katika muktadha wa mazingira yenu ili kuweza kutekeleza malengo mliyojiwekea kwa kufanya kazi kama timu.
Msingi wa tatu ni kulenga kuchukua dola kwa njia za kidemokrasia; hivyo mafunzo haya yawawezeshe kujipanga zaidi kutimiza wajibu huu. Kwa bahati njema mafunzo haya yanafanyika mapema zaidi kuelekea uchaguzi mkuu wa udiwani, ubunge na urais mwaka 2010. Katika muktadha huo mafunzo yawawezeshe kuhamasisha watanzania waadilifu kutoka ngazi zenu kujitokeza kugombea nafasi hizo na kujipanga vizuri zaidi kwa ajili ya kupata kura na kulinda ushindi.


Nachukua fursa hii kutoa mwito kwenu kuwatangazia wananchi kwamba uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa upande wa Dar es salaam utafanyika kuanzia tarehe 22 mpaka 27 Machi mwaka 2010. Nawaomba watanzania wote ambao watakuwa wamefikia umri wa miaka 18 na kuendelea wakiwemo vijana na wanawake wajitokeze kwa wingi kwenda kujiandikisha. Mafunzo yawawezeshe kutambua njia za kidemokrasia za kutumia kuweza kushinda uchaguzi na kupata dhamana ya kuongoza serikali- njia kuu ikiwa kugombea, kupiga kampeni na kupiga kura. Katika kufanya kuiwajibisha serikali iliyo madarakani na hata kufanya kampeni za uchaguzi natarajia mtatumia njia za kawaida mathalani mikutano ya hadhara, kampeni za mtu kwa mtu, vyombo vya habari nk.


Hata hivyo, katika mazingira ya leo ambapo chama kilichopo madarakani kinaendesha siasa za rushwa na vurugu kikitumia pia vyombo vya dola na watumishi wa umma ni muhimu mkajipanga kuunganisha nguvu ya umma kukabiliana na hujuma ikiwemo kuzuia uwizi wa kura.


Katika mazingira hayo ya kutokuwa na uwanja sawa wa kisiasa ni muhimu mafunzo yakawawezesha pia kufahamu mbinu mbadala za kidemokrasia zinazoweza kutumiwa kushinikiza mabadiliko ya kweli ikiwemo mbinu ya kukataa utii wa kiraia hata pale haki za msingi zinapovunjwa (civil disobedience) mathalani kupitia maandamano nk. Natoa tamko rasmi kama Mwenyekiti wa Mkoa na muwafikishie salamu hizi CCM na vibaraka wao kwamba CHADEMA Mkoa wa Kinondoni hatutakubali kuibiwa kura katika uchaguzi wa mwaka 2010 ndani ya wilaya, jimbo na kata zetu na tunatoa changamoto kwa maeneo mengine ya nchi nayo kujipanga vilivyo kuwadhibiti mafisadi wa kisiasa na wote wanaotumika kuhujumu demokrasia wakati wa uchaguzi.


Watanzania wanahitaji mabadiliko ya kweli, viongozi wa CCM wamekuwa wakitoa ahadi kedekede kwenye uchaguzi lakini utekelezaji ni legelege kutoka na ombwe na uongozi na mfumo mzima wa utawala kuelemewa na ufisadi. Wakati nyinyi mmejumuika hapa kwa ajili ya mafunzo siku ya leo, viongozi wa CCM wamejumuika katika maeneo mbalimbali kuzindua sherehe za wiki nzima ya kile wanachokiita maadhimisho ya miaka 33 ya CCM.


Kwa kweli CCM imefikia kiwango cha juu sana cha kuwapuuza watanzania ambao iliwaahidi kuwaletea maisha bora badala yake imeweka mazingira ya gharama za maisha kupanda kwa Ari, Nguvu na Kasi mpya kupitia kupandisha kodi na bei za bidhaa zinatumiwa na wananchi walio wengi. Nyinyi hapa Ubungo ni mashuhuda wa namna gharama za maisha zimepanda zikiwemo bei za vyakula wakati kipato cha mtanzania wa kawaida wakiwemo watumishi wa umma kipo pale pale na kwa wengine kimeshuka.


CCM ina nini cha kusherehekea kwa wiki nzima? Ni vizuri badala ya kusherehekea CCM ikatumia fursa hiyo kutoa majibu ya kina kwa umma namna viongozi na chama hicho kwa umoja wao wanavyotuhumiwa kwa ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka katika msururu mrefu wa kashfa kuanzia fedha za Akaunti ya Madeni Benki Kuu (EPA) hususani kuhusu kampuni ya Kagoda, Tangold, Deep Green, Meremeta nk. Ni vizuri watanzania wakaendelea kufunguka macho na kutambua unafiki huu wa CCM na viongozi wake ambao wameamua kutumia maadhimisho hayo kufanya propaganda za kurejesha imani kwa wananchi kwa kuwa mwaka huu ni kipindi ambacho tunaelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Kuliko kufanya propaganda zinazohusisha matumizi ya anasa ikiwemo ya fedha za umma zaidi ya bilioni mbili (milioni zaidi ya 2000) ambazo chama hicho kinachukua kila mwezi kutoka serikali zizotokana na kodi yako na yangu badala ya kuendelea kufanya ubadhirifu wapeleke fedha hizo kuwahudumia watanzania wenzetu walioathirika na maafuriko huko Kilosa.


CCM haina cha kujivunia sasa zaidi ya kufilisika kifalsafa, kiitikadi, kimaadili, kisera na hata kiuongozi. Ushahidi wa hali hiyo ni maandiko ya mwasisi wa chama hicho hayati Mwalimu Nyerere ambaye katika moja ya kitabu chake cha mwisho mwisho aliandika wazi kwamba CCM ina kansa ya uongozi kutoka na rushwa. Katika sherehe hizi za CCM zinazoendelea mtawasikia CCM wakijivunia kuwa chama hicho kinafuata siasa ya ujamaa na kujitegemea lakini ukweli ni kwamba chama hicho kimeifanya nchi kuwa tegemezi lakini kubwa zaidi ni kwamba katika kitabu hicho Nyerere alieleza wazi kwamba CCM inawadanganya watanzania kwa kuwa misingi mikuu ya Azimio la Arusha ikiwemo miiko ya uongozi ilifutwa katika maamuzi ya Zanzibar ya mwaka 1991. Hivyo, kama sehemu ya kufuata wosia wa Nyerere natoa mwito kwa watanzania kupuuza kauli za kipropaganda za viongozi wa CCM katika maazimisho yao.


Ufisadi na uongozi mbovu ndani ya mfumo wa utawala chini ya CCM hauko kwenye ngazi ya taifa tu bali umejikita katika ngazi zote za chama hicho na serikali yake. Wakati viongozi wa kitaifa wa CHADEMA wakiongozwa na Mwenyekiti Freeman Mbowe na Katibu Mkuu Dr Wilbroad Slaa wakipambana na mafisadi na kutetea rasilimali za nchi yetu kwenye ngazi ya taifa nyinyi mnapaswa kutimiza wajibu huo kwenye ngazi yenu.


Manispaa ya Kinondoni ambayo jimbo letu la Ubungo na kata zake tupo ni halmashauri ambayo sehemu kubwa ya viongozi wakuu wa serikali na vyama vya siasa wanaishi; lakini pia ndio halmashauri kinara kwa tuhuma za ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka. Tuhuma hizo zikimhusu pia Meya wa Halmashauri hii Bwana Salum Londa ambaye alitajwa mpaka Bungeni kuwa analindwa na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuph Makamba katika kashfa zake.


Kati tuhuma zinazomgusa ni pamoja manispaa kuuziwa matrekta 27 ya kuzoa takataka yasiyokuwa na viwango katika kashfa inayohusisha matumizi ya zaidi zaidi ya milioni 150 wakati ambapo uchafu umekithiri katika mitaa mbalimbali ya halmashauri. Dalili za kuwepo vitendo vya ufisadi zimeonekana wazi baada ya Baraza la Madiwani la Manispaa hiyo ambalo ndilo lililopitisha zabuni hiyo kugawanyika katika makundi mawili na kuendeleza malumbano bila kuchukua hatua zozote za misingi. Lakini tuhuma dhidi ya halmashauri hii haziishii kwenye zabuni pekee bali uuzaji na umilikishaji wa ardhi kinyume cha taratibu mathalani Eneo la Ufukwe wa Coco (coco beach) na umegaji wa kiwanja cha shule ya Msingi Kawe nk.


CHADEMA Mkoa wa Kinondoni tunayo taarifa ya siri yenye mihutasari na saini za viongozi wa CCM na Halmashauri ya Kinondoni ambazo zinathibitisha wazi kabisa tuhuma hizo zikitaja kwa majina na viwango vya rushwa ambazo zilitolewa ikiwemo kwa madiwani katika kashfa hizo ili kupeleka mashtaka kwa umma katika maeneo yenu.


Ndani ya halmashauri hii ambapo ubora wa elimu katika shule za umma unazidi kuporomoka; huduma za afya zinazidi kuterereka hususani katika Hospitali ya Manispaa ya Mwanyamala; maji yanazidi kuwa adimu katika maeneo mengi ya kata za Goba, Kimara nk huku wanayoyapata wanapandishiwa bei kinyemela ama wanavutiwa maji kwa gharama kutokana na tuhuma za ufisadi; itakuwa ni aibu kwa CCM Kinondoni kuitisha sherehe za wiki nzima badala ya kuboresha huduma za kijamii ambazo chini ya sera mbovu na uongozi bomu zinaguezwa kuwa bidhaa ya bei mbaya katika soko holela.


Nimalize kwa suala moja ambalo linaendelea kujadiliwa sasa kutokana na mkutano ulioitishwa na SUMATRA kupata maoni ya wadau kuhusu utoaji wa huduma ya usafiri mijini kwa kutumia makampuni na mashirika ambao kwa kiasi kikubwa ulijadili mradi wa mabasi yaendeyo kasi mkoani Dar es salaam (DART).
Nyinyi kama viongozi na sehemu ya wananchi mzingatie kuwa mradi huu unawahusu sana kwa kuwa unatarajiwa pia kupita katika barabara za Jimbo la Ubungo hususani barabara ya Morogoro. Suala hili pia linahusu mustakabali wa magari ya usafirishaji wa abiria mkoani humu ambayo yanakadiriwa kufikia elfu sita (6,000), nyuma ya magari hayo huzungumzii tu abiria wanaotumia usafiri huo bali pia suala hilo linahusu mustakabali wa ajira za madereva na makondakta wa mabasi hayo pamoja na mazingira magumu ya kazi zao.


Jambo kubwa ambalo limejitokeza katika mchakato mzima ni dhamira ya serikali kufungua milango ya uwekezaji ikiwemo kuruhusu wawekezaji kutoka nje katika sekta ya usafirishaji na kuweka viwango na vigezo ambavyo kimsingi vitaweka pembeni wenye mitaji midogo. Kama kawaida ya Serikali ya CCM na mamlaka zake sababu zinazotolewa ni za kuvutia kisera mathalani kuondoa kero za usafiri kwa kupunguza msongamano ndani ya mabasi na kupunguza foleni za magari barabarani. Hatahivyo, nyuma ya kauli hizi za kisiasa upo ukweli mchungu ambao ni muhimu watanzania wakautambua na kuujadili.


Katika mazingira hayo natoa changamoto kwa SUMATRA na DART kuweka wazi ripoti zao za tathmini (feasibility study) pamoja na mikataba yote inayohusika na mradi huu ili umma wa watanzania hususani wakazi wa Dar es salaam uweze kujadili kwa kina kwa kuwa suala hili halihusu wamiliki pekee bali pia watumiaji wa daladala ambao ni wananchi wa kawaida.


Kauli ya SUMATRA kwamba tayari kuna makampuni toka nje ambayo yameonyesha nia ya kuwekeza katika mradi husika ukichunguzwa kwa kuzingatia kasi ya sasa ya DART kutaka mfumo tofauti wa uwekezaji katika mradi huo inazua maswali mengi. Ni kisingizio hiki kiki cha kutaka mitaji toka nje ndicho kilichosababisha hasara kwa taifa kwa miundo mbinu yetu ya usafirishaji kubinafsishwa kwa bei chee katika mazingira tata bila Tanzania kunufaika na hicho kinachoitwa mitaji mikubwa kutoka nje mathalani katika sekta ya reli (RTL), ndege (ATCL), bandari (TICTS) nk. SUMARTA wanatuhakikishia vipi kuwa DART haitakuwa TRL nyingine tena ndani ya mkoa wa Dar es salaam ikihusisha usafiri ambao unatumiwa na wananchi walio wengi?


Serikali ieleze wazi namna uchumi wa wawekezaji wazawa wenye daladala, na ajira za watumishi wa daladala hususani madereva na makondakta zitavyolindwa katika mchakato mzima. Serikali inapaswa kueleza wazi pia namna ambavyo haki za abiria wa daladala zitavyolindwa ikiwemo kupatiwa huduma bora lakini zenye bei ambayo mtanzania wa kipato cha chini anayeishi Dar es salaam anaweza kumudu.


Nakubaliana na ukweli kwamba foleni katika mkoa wa Dar es salaam ni tatizo lenye athari za kiuchumi ambapo taifa hupoteza takribani bilioni nne kila saa; lakini serikali izingatie kwamba mikakati mipana inapaswa kutekelezwa kukabiliana na hali hii badala ya kufikiri kwamba uwekaji wa makampuni makubwa ya kuendesha mabasi yaendayo kasi ndio suluhisho kuu. Fikra za namna hii za kuongoza kwa dharura ndio ambazo zilitumika kutekeleza mpango wa njia tatu katika baadhi ya maeneo mfumo ambao athari zake zinaendelea kuonekana mpaka sasa. Inashangaza jiji pana lenye takribani milioni nne lenye magari binafsi laki moja tu kuwa na foleni kwa kiwango cha Dar es salaam. Hii ni dalili kwamba tatizo letu la msingi ni udhaifu katika mipango miji. Sasa badala ya kushughulikia matokeo ni muhimu kutekeleza sera zenye kukabiliana na vyanzo vya matatizo.


Hivyo mkazo uwekwe katika kutekeleza sera zenye kupanua jiji kuelekea pembezoni (satellite towns) lakini pia kuheshimu ramani za muda mrefu badala ya kuendelea na mtindo wa ujenzi holela ambao unachochea pia migogoro ya ardhi na kuliingiza taifa katika kubeba mzigo mkubwa wa fidia za mara kwa mara. Pia serikali iwekeze katika barabara za kuchuja magari (filter roads) ili kupunguza msongamano kwenye barabara kuu. Mathalani, hapa jimboni Ubungo haiingii akilini kwamba mtu ambaye yuko Mbezi Loius akitaka kwenda Mbezi Beach upande wa Jimbo la Kawe analazimika kwenda na gari mpaka Ubungo mataa halafu Mwenge ndio anarudi Mbezi. Wakati kama barabara ya kutoka Mbezi Louis kwenda Mbezi Beach moja kwa moja kupitia Goba ingejengwa kwa haraka kiwango cha lami ingepunguza msongamano wa magari. Hivyo hivyo, mwendesha gari kutoka Kibamba kwenda Tegeta analazimika kupita njia hiyo hiyo na kuongeza msongamano wakati angeweza kukatishia Mpiji Magoe au maeneo mengine kama njia hizo zingelindwa dhidi ya uuzaji holela wa viwanja na pia barabara zake zingewekwa lami.


Wakati serikali ya CCM inazungumza kujenga barabara za hewani (flying overs) na mabasi na treni ziendazo kasi (rapid transport), serikali hiyo hiyo inashindwa kuweka mazingira ya huduma za msingi za kijamii kwa wananchi. Hii ni serikali inayojiita masikini inayoendeshwa kwa kuomba omba lakini inataka kuvunja rekodi za kimataifa katika ujenzi na manunuzi kuanzia bungeni, ndege ya rais, rada, majengo pacha ya Benki Kuu, nyumba ya gavana na sasa usafiri katika mkoa wa Dar es salaam.


Hali hii ya kushindwa kutambua vipaumbele kama taifa ndio inafanya kodi za wananchi wa vijijini kutokurejeshwa kuhakikisha maendeleo ya uwiano na hivyo kujenga matabaka yanayosababisha watanzania wengi zaidi kukimbilia Dar es salaam na kusababisha msongamano kuzidi kuongezeka. Kwa hiyo kuleta wawekezaji toka nje, na kuleta mabasi yaendayo kasi havitaweza kuondoa msongamano kama vyanzo vya msingi vya msongamano havitashughulikiwa kisera, kimfumo na kiuongozi.


Mwelekeo mzima wa mradi huu unadhihirisha udhaifu katika mfumo wetu wa utawala ambao serikali kuu na mamlaka zake inahodhi michakato yote ya msingi hata ile ambayo halmashauri zilipaswa kushirikishwa na kuchukua nafasi ya kuwa mstari wa mbele katika kutoa mwelekeo kama suala hili la usafiri katika mkoa wa Dar es salaam na manispaa zake. Lakini ni ishara pia ya uongozi wa muda mrefu wa CCM unaanzisha mipango tofauti tofauti inayoshindwa baada ya muda mfupi. Kwa hali hii badala ya CCM kusherehekea itumie fursa hii kuwaeleza watanzania ni nini kimefilisi kampuni ya Usafirishaji Dar es salaam (UDA) na pia waeleze wazi ilipokwenda michango iliyotolewa na wananchi mkoani Dar es salaam kwa ajili ya mradi wa mabasi ya wanafunzi ambao fedha zake inatuhumiwa kuwa zimeishia mikononi mwa vigogo wa UVCCM wakati walengwa wanaendelea kupata adha ya usafiri.


Katika mazingira haya ni muhimu kuhamasisha mabadiliko ya kweli katika taifa kwa wananchi kuchagua viongozi mbadala. Mwaka 2005 Mkoa wa Dar es salaam uliwaangusha watanzania kwa kuwa pamoja na kuwa na wasomi wengi, wananchi wenye kufikiwa zaidi na vyombo vya habari na pia wananchi ambao wanaelezwa kuwa na elimu ya kuridisha ya uraia ukilinganisha na wa vijijini; lakini mkoa huu wabunge wake wote 7 ni CCM na madiwani wake wote wa kuchaguliwa na wa viti maalumu katika manispaa zote tatu ni CCM. Wananchi wa Dar es salaam wakiwemo wajanja wa Kinondoni wanafurahia hoja za wabunge wa upinzani kama Dr Wilbroad Slaa bungeni ama kazi ya madiwani wa upinzani wanaongoza halmashauri kama kule Karatu lakini hawajui kwamba viongozi hawa mbadala wametokana na wenzao wa vijijini ambao waliamua kuunganisha nguvu katika uchaguzi uliopita kwa kupiga kura kwa wingi lakini pia kushiriki kulinda ushindi wao mpaka hatua ya mwisho. Natarajia mafunzo haya yatawawezesha kuwaunganisha wananchi wa Jimbo la Ubungo kurekebisha kasoro hizo na kusimamia mabadiliko kwani katika miji mingi mikubwa ya Afrika wananchi wanaunga mkono vyama mbadala.


Mafunzo haya yawawezesha kwenda kwa umma kuwaeleza udhaifu wa uongozi ulioko madarakani na ufisadi uliokithiri lakini msiishie kukosoa tu bali muweze kueleza kwa kina sera mbadala za CHADEMA na kuondoa upotoshaji unaofanywa kuhusu sera hizo.


Mathalani waelezeni watu kuhusu sera ya mfumo mpya wa utawala ya CHADEMA maarufu kama sera ya majimbo. Napenda kuchukua fursa hii kuwaeleza kwa maneno machache sana namna sera hii inavyoweza kuwa mkombozi kwa watanzania kwa kutoa mamlaka zaidi kwa umma katika kuleta maendeleo.
Kwa kutumia falsafa ya CHADEMA ya nguvu ya umma sera hii inalenga kupeleka mamlaka kwa umma ili kuepusha masuala yanayowahusu wananchi kuchelewa kushughulikiwa kwa urasimu wa serikali kuu badala yake serikali za majimbo na za mitaa zitapewa mamlaka zaidi kutatua kero za wananchi.


Sera ya mfumo mpya wa utawala inalengo la kupeleka madaraka zaidi kwa wananchi katika kuchagua viongozi wetu. Kama Tanzania ingekuwa inaongozwa kwa sera hii leo hapa Halmashauri ya Kinondoni msingekuwa na mkuu wa wilaya, maana CHADEMA imeshatangaza kufuta vyeo hivi. Haiwezekani kuwa na mkuu wa wilaya, mkurugenzi wa halmashauri na meya wa manispaa wote wakifanyakazi zinazokaribiana hali inayosababisha mwingiliano wa madaraka. Vyeo hivi vya mkuu wilaya na vya mkuu wa mikoa vilikuwa vikitumiwa na serikali ya mkoloni wakati wa ‘wagawe uwatawale’, wakati huo uteuzi ukifanywa na gavana. Ni mfumo huo huo umebakizwa leo ambao Rais anateuwa watendaji wake mpaka serikali za mitaa ambao hawawajibiki kwa wananchi wala serikali za mitaa bali serikali kuu. Madaraka haya ya serikali kuu yanaenda mbele zaidi mpaka katika uteuzi wakurugenzi wa halmashauri badala ya uteuzi wa watumishi hawa kufanywa na halmashuri zenyewe.


Pia, CHADEMA inataka mameya na wenyeviti wa halmashauri wachaguliwe na wananchi moja kwa moja badala ya kuchaguliwa na madiwani pekee. Kama Halmashauri ya Kinondoni ingeongozwa kwa sera hii ya CHADEMA basi msingekuwa hapa na Meya Londa ambaye hawajibiki moja kwa moja kwa wananchi kwa kuwa wananchi wote wa manispaa hawakushiriki katika kumchagua. CCM haiwezi kuteleza mabadiliko makubwa kama haya kwa hofu ya kupoteza vyeo vyao lakini pia izingatiwe kuwa mabadiliko haya yanahitaji katiba mpya suala ambao serikali wanayoiongoza imeshatangaza kuwa haikusudii kulifanya.


Hali hii inatufanya tukumbuke; mabadiliko ya kweli katika taifa letu hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile, chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale. Kwa falsafa ya chukua chako mapema; Tanzania yenye neema haiwezekani. Tuunganishe nguvu kubadili mfumo wa utawala; mabadiliko yanawezekana. Tunahitaji uongozi wenye dira na uadilifu wa kulikomboa taifa na tunaweza kufanya hivyo kwa kubadili mfumo wa utawala na kuiwezesha CHADEMA kuongoza dola ama kupunguza hodhi ya chama kimoja bungeni na kwenye halmashauri za wilaya/manispaa ikiwemo ya kwetu ya Kinondoni.


Nimefungua rasmi mafunzo haya na Asante sana kwa kunisikiliza.



Friday, January 29, 2010

Muundo wa tume uboreshwe rasilimali zitengwe kuwezesha usimamizi huru wa uchaguzi

Kwa mara ya tatu chini ya mfumo wa vyama vingi; Tume ya Uchaguzi ilisimamia na kuratibu uchaguzi mkuu mwaka 2005 kwa kutumia uzoefu ilioupata katika chaguzi za mwaka 1995 na mwaka 2000. Pia Tume imesimamia chaguzi ndogo 4 za bunge na chaguzi ndogo 75 za udiwani tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu 2005. Kwa ujumla Tume ya Uchaguzi iliendesha vizuri zaidi uchaguzi uliopita ukilinganisha na chaguzi zilizotangulia lakini bado mchakato wa uchaguzi haukukidhi vigezo vyote vya uchaguzi huru na haki.

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010. Hatahivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe. Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi; na katika kujadili muswada huo makala hii itachambua suala la muundo na utaratibu wa tume ya uchaguzi pekee.

Ni muhimu tuijadili mifumo ya kisheria na kiuchaguzi kwa ajili ya uchaguzi na Muundo wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Pamoja na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sheria mbalimbali zimekuwa zikisimamia uchaguzi hususani: Sheria ya Uchaguzi na. 1 ya mwaka 1985; Sheria ya Vyama vya siasa na. 5 ya mwaka 1992 na Sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambazo zimetoa mamlaka kwa tume kusimamia na kuratibu uchaguzi ikiwemo kutoa maelekezo na taratibu mbalimbali.

Muundo wa Tume ulichukua mfumo ule ule ambao ulitumika katika uchaguzi mkuu 2005 unatokana na Katiba Kifungu 74(1) kama ilivyofanyiwa marekebisho na Sheria na. 4 ya 1992 na Sheria na. 7 ya mwaka 1993; Tume inateuliwa na Rais(Katiba na Sheria husika zimeeleza sifa za wanaoweza kuteuliwa). Mkurugenzi wa Uchaguzi naye anateuliwa na Rais kwa mapendekezo ya Tume. Katiba kifungu 74 imebainisha majukumu ya Tume ya Uchaguzi. Vyama vya siasa viliendelea kudai tume huru ya uchaguzi wakati wa marekebisho ya 14 ya katiba yaliyofanyika karibu na uchaguzi mkuu. Hata hivyo suala la muundo wa tume huru ya uchaguzi halikujadiliwa wala kuingizwa kama sehemu ya marekebisho hayo. Matokeo yake maandalizi ya uchaguzi yalifanywa na tume ile ile ambayo ilisemwa kipindi chote kwamba haiko huru. Kamati mbalimbali ziliundwa na kufanya kazi kipindi cha uchaguzi pekee. Hali hii haijabadilika kati ya kipindi cha 2006 mpaka 2009, pamoja na vyama vya siasa na wadau wengine kutaka mapema marekebisho yaweze kufanyika.

Ni muhimu kujadili kuhusu rasilimali kwa ajili ya usimamizi wa uchaguzi na Usimamizi wa Uchaguzi kama sehemu ya kuwezesha usimamizi huru wa uchaguzi. Tofauti na chaguzi za 1995 na 2000, katika uchaguzi mkuu 2005 fedha za uchaguzi kwa ajili ya shughuli za uendeshaji wa Tume ya Uchaguzi zilitolewa katika wakati mwafaka na sehumu kubwa zilitolewa na serikali. Kupungua kwa utegemezi kwa wahisani katika kutoa fedha za kusimamia uchaguzi pamoja na kutoa fedha mapema vilisaidia kuboresha uendweshwaji wa uchaguzi kwa kiwango Fulani. Hata hivyo, hali hii iliwezekana kutokana na ukweli kuwa serikali katika chaguzi zilizofuata baada ya uchaguzi wa mwaka 1995 ilijivua jukumu la kugharamia kampeni za wagombea na mawakala wa vyama vya siasa.

Uhusiano katika ya vyama vya siasa na Tume ya Uchaguzi katika ngazi ya Taifa kwa kiwango fulani; vyama vilialikwa katika vikao mbalimbali na vilikuwa na wajumbe katika kamati mbalimbali za tume ya Uchaguzi. Hata hivyo malalamiko yalitolewa baadhi ya maeneo mengi hususani yale yaliyokuwa na upinzani mkali kwamba vyama havikushirikishwa ipasavyo na watendaji wa tume ya taifa ya uchaguzi ngazi ya wilaya, majimbo na kata. Wakati wa kampeni watendaji hawa wameonekana kuegemea chama tawala. Hali hii iliendelea katika maeneo mengi hata katika hatua za kuhesabu kura, kujumlisha kura na kutangaza matokeo hususani katika ngazi za majimbo. Katika mfumo wa tume hakuna utenganisho kati ya usimamizi na utekelezaji katika muundo wa tume ngazi za chini ya makao makuu ya tume. Uteuzi wa watendaji wa chini ulifanywa na wasimamizi wa uchaguzi ambao ni watekelezaji(ambao walikuwa ni watumishi wa serikali) badala ya chombo huru cha kusimamia uchaguzi hivyo walitumiwa na dola kupika ama kuchezea matokeo.

Muswada kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi uliochapwa kwenye gazeti la serikali tarehe 11 Disemba 2009 unapendekeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ipewe mamlaka ya kuteua wasimamizi wa uchaguzi kutokana na ofisi au sifa zao tofauti na ilivyo ambapo tume huteua wasimamizi wa uchaguzi kutokana na ofisi pekee. Upenyo wa tume kuachiwa kuamua kati ya vyeo na sifa unatoa mianya ya kuruhusu hujuma. Mathalani, katika uchaguzi wa serikali ya mitaa wa mwaka 2009 pamoja na kuwa haukusimamiwa na tume; kanuni za uchaguzi huo zilitaja kwamba wasimamizi wa uchaguzi wangeteuliwa kwa cheo au kwa sifa; matokeo yake idadi kubwa iliteuliwa kutokana na vyeo ndio maana uchaguzi husika kwa sehemu kubwa ulisimamiwa na watendaji wa serikali kwa nafasi zao. Kama mapendekezo hayo ya muswada wa sheria yakaachwa kama yalivyo maana yake ni kwamba; kwenye chaguzi tume inaweza kuamua kuangalia vyeo na kuteua wakurugenzi na maafisa watendaji wa kata kusimamia uchaguzi badala ya uteuzi kuegemea zaidi katika sifa na kuepuka kuwateua watendaji wa serikali.

Masuala yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa na Serikali, Tume ya Uchaguzi, Vyama Vya siasa na wadau na kuingizwa kama sehemu ya marekebisho ya sheria za uchaguzi katika miswada ambayo imetolewa:

Pawepo na Sheria ya Tume ya Uchaguzi ili kuipa uhuru na mamlaka zaidi tume ya uchaguzi kama ilivyo katika nchi kadhaa za Kusini mwa Afrika.(Pendekezo hili limetolewa pia na Tume ya Uchaguzi na Vyombo mbalimbali vya Ufuatiliaji/Uangalizi wa uchaguzi).

Katiba na Sheria vifanyiwe mabadiliko/marekebisho ili kutoa uhuru na mamlaka ya Tume ya Uchaguzi wa Kuzingatia vigezo vya Kanuni/Matamko na Misingi mbalimbali ya Uchaguzi ya Kimataifa ambayo taifa letu limeridhia. Baadhi ya masuala mahususi ni pamoja na: Tume iwe nje ya mfumo wa kiutendaji wa kiserikali(Watendaji wa Serikali kama Wakurugenzi na Watendaji wa Kata wasiwe watumishi wa Tume ya uchaguzi hata wakati wa uchaguzi); Wajumbe wa Tume wachaguliwe kwa mashauriano na Wadau wengine vikiwemo vyama vya siasa na baadaye wathibitishwe na Bunge; Utumishi wa Wajumbe waandamizi wa Tume wa ulindwe(durability and security of tenure) kisheria na kikatiba kama walivyo majaji; Uwakilishi wa Tume uzingatie jinsia, uwakilishi wa kijamii na makundi rika; Tume ya Uchaguzi iwajibike kwa Bunge badala ya Kuwajibika kwa Serikali; Tume ya Uchaguzi iwe na Bajeti inayojitegemea itakayopitishwa moja kwa moja na Bunge. Kamati za Tume ziwe ni za kudumu; ziendelee na kazi hata baada ya uchaguzi. Vitengo vya TEKNOHAMA (ICT) na Elimu ya Uraia viwe sehemu ya vitengo vya kudumu vya Tume. Tume ya Uchaguzi iwe na watendaji wa Kudumu katika ngazi mbalimbali; utaratibu wa kuwatumia maofisa wa serikali kama wasimamizi na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi usitishwe. Hii ihusishe kuwezesha bajeti ya Tume ya uchaguzi iwekewe fungu pekee kutoka katika mfuko mkuu wa fedha za umma(consolidated fund) badala ya kuwa sehemu ya bajeti za kawaida za wizara.Hivyo mjadala utakaowezesha kuunganisha nguvu za kidemokrasia na kimaadili ili kudai na kushawishi mabadiliko ya sheria za uchaguzi na mazingira ya kisiasa ikiwemo wenye kuboresha usimamizi wa uchaguzi ni muhimu uibuliwe na kuendelezwa. Kuna haja ya serikali kufanya marekebisho mapana zaidi kuhusu muundo wa tume au vyama vya siasa na wadau wengine waelekeze jitihada bungeni na mahakamani kudai mabadiliko ama kufutwa kwa vipengele vya sheria nyingine ambavyo vinafanya mazingira ya kisiasa na kiuchuguzi yanayokwaza uchaguzi huru na wa haki. Sehemu ya marekebisho hayo yanahitaji kwanza marekebisho ya katiba ili muundo wa tume uboreshwe rasilimali zitengwe kuwezesha usimamizi huru wa uchaguzi.

Mchakato wa Uboreshaji Daftari na Uhakiki wa Wapiga kura urekebishwe

Katika uchaguzi orodha ya wapiga kura ni kitu muhimu. Katika uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 hapakuwa na orodha ya kudumu ya wapiga kura badala yake wananchi waliandikishwa karibu na uchaguzi na kupewa shahada za mpiga kura badala ya kadi za kudumu. Ili kuruhusu mchakato wa kuanzisha Daftari na Kudumu la Wapiga Kura (DKWK), katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kifungu 5(3) na kipengele cha 12 cha sheria ya uchaguzi ya mwaka 1985 vilifanyiwa marekebisho January 2000. Lakini hili halikufanyika na matokeo yake DKWK halikuweza kutumika katika uchaguzi wa 2000; hata hivyo June 9, 2004 Bunge la Muungano lilifanya marekebisho mbalimbali ambayo yaliwezesha mchakato wa kuandaa DKWK kuanza. Mchakato wa kuandikisha wapiga kura kwa upande wa Tanzania bara ulianza 7 Oktoba 2004 na kukamilika 18 April 2005.
]
Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010. Hatahivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe. Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi. Katika makala hii tutauchambua mchakato wa uboreshaji na uhakiki wa daftari la kudumu la wapiga kura pekee.

Ni muhimu nikiri kuwa daftari la kudumu la wapiga kura limeongeza ufanisi kiasi katika mchakato wa uchaguzi. Wananchi wengi hususani vijana walijitokeza kujiandikisha na wengi wao kwa matarajio kuwa kadi ya mpiga kura inaweza kutumika kama kitambulisho. Uwezekano wa watu kupiga kura zaidi ya mara moja ulipunguzwa isipokuwa kwa Zanzibar ambapo ulivurugwa na unaendelea kuvurugwa.

Lakini ni muhimu zaidi tuchambue mapungufu ya chaguzi zilizopita hatua kwa hatua na kuhusisha na marekebisho yanayopendekezwa ili kubaini kama mabadiliko yanayokusudiwa yanakidhi haja ya kuondoa kasoro husika.

Mwaka 2004 yapo mapungufu katika mchakato wa uandikishaji; mapungufu ambayo yamejirudia tena katika mchakato wa uboreshaji wa daftari katika awamu ya kwanza ya pili miaka ya 2007 na 2009.

Vituo vya kujiandikisha vilikuwa mbali na hivyo baadhi ya watu kushindwa kuandikishwa.(Vituo vilikuwa vichache hata kuliko vituo vya kujiandikisha vya mwaka 2000). Pia wananchi wa maeneo mapana waliandikishwa katika eneo moja na hivyo kufanya utaratibu wa kugawa vituo na wananchi kufahamu vituo vyao kuwa mgumu.(Mifano halisi imetolewa hata katika ripoti ya uchaguzi ya TEMCO, 2006).

Ushiriki wa vyama vya siasa katika kuhakikisha kuwa mawakala wa vyama wanakuwepo siku zote za uandikishaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura(DKWK) ulikuwa mdogo. Pia vifaa vilikosekana katika baadhi ya maeneo kabla ya siku ya mwisho ya uandikishaji na hivyo wengine kukosa fursa ya kuandikishwa. Zoezi la kuhakiki daftari nalo lilikuwa duni. Vyama vilipewa DKWK kamili siku chache kabla ya kwenda kupiga kura na taratibu hazikutoa fursa ya wapinzani kuhakiki. Wananchi hawakujitokeza kwa wingi kwenda kuhakiki majina yao baada ya daftari la awali la wapiga kura(provisional voter registry) kutolewa. Hivyo watu mbalimbali wengi wao wakiwa wanachama wa upinzani walinyimwa kuandikishwa na wengine waliofamika kuwa ni wana CCM hata wasio na sifa waliandikishwa hasa Zanzibar. Mapungufu haya yaliyojitokeza wakati wa uandikishaji mwaka 2004 mpaka 2005, hayakufanyiwa kazi kikamilifu wakati wa zoezi la Uboreshaji wa Awamu ya Kwanza lililofanyika kati ya Oktoba 2007 na Disemba 2008.

Tarehe 11 Disemba 2009 serikali imechapa muswada wa marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambao umegusa pia marekebisho yanayohusiana na mchakato wa daftari la kudumu la wapiga kura. Baadhi ya mapungufu yanayokusudiwa kurekebishwa katika muswada huo ni pamoja na NEC kutokuwa na madaraka ya kuteua waratibu waandikishaji wa mikoa. Pia kushughulikia suala la kipindi cha kuboresha daftari la kudumu la wapigakura kutotajwa bayana katika sheria na sheria kutoruhusu baadhi ya watendaji wa tume kuingia katika vituo vya kupigiakura ili kufuatilia zoezi la upigaji kura. Ibara ya 6 imependekeza marekebisho katika fungu la 15 la sheria, ili kuweka bayana kipindi cha kufanya uboreshaji wa daftari la taifa la kudumu la wapiga kura kuwa mara mbili katika Uchaguzi Mkuu mmoja na unaofuata. Aidha, sehemu hiyo inasisitiza kwamba, kwa lengo la kuongeza uwazi katika zoezi la uandikishaji wapiga kura, imependekezwa katika ibara ya 7 kuwa na fungu jipya la 15A katika sheria linatoa nafasi kwa vyama vya siasa kuteua mawakala wakaokuwepo katika vituo vya kuandikisha wapiga kura kama ilivyo wakati waupigaji kura.

Hata hivyo; kasoro za msingi kuhusu uboreshaji na uhakiki wa wapiga kura bado hazijashughulikiwa kikamilifu kisheria katika muswada uliopendekezwa na hata kiuendaji katika zoezi la uboreshaji linaloendelea hivi sasa. Ili kurekebisha hali hiyo asuala yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa na Serikali, Tume ya Uchaguzi, Vyama Vya siasa na Wadau wengeni kama sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010(hususani katika Uboreshaji wa Daftari katika Awamu ya Pili DKWK unaondelea na unaotarajiwa kukamilishwa mapema mwaka 2010).

Kwa ujumla daftari la kudumu la wapiga kura(DKWK) liboreshwe zaidi. Uanzishwaji wa daftari la kudumu la wapiga kura unasaidia kupunguza gharama za uandikishaji wa wapiga kura mara kwa mara. Pia uwepo wa kumbukumbu za kudumu unasaidia kuondoa utata wa upotevu au kuharibika kwa nyaraka. Hata hivyo daftari hili linapaswa kuhakikiwa upya kwa kuwashirikisha kikamilifu wananchi na wadau muhimu hususani vyama vya siasa mapema sana kabla ya uchaguzi mkuu ujao kukaribia. Pia uwepo mfumo na mtandao wa kudumu mpaka ngazi za wilaya wa kuendelea kuingizia takwimu za wapiga kura wapya na kuondoa za ambao wamepoteza sifa za kupiga kura katika mahali husika. Orodha za wapiga kura zipangwe upya ili ziweke makundi ya wapiga kura kwa kuzingatia maeneo yao ya makazi mathalani mitaa midogo na vitongoji ili mpangilio uwezeshe daftari litumike katika chaguzi za ngazi ya chini. Kila raia atambue kuwa ana haki na wajibu wa kujiandikisha na kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura. Nichukue fursa hii kuhimiza wapiga kura wapya kwenda kujiandikisha na wale waliopoteza kadi zao ama kuhama maeneo yao nao kushiriki zoezi la uboreshaji wa daftari linaloendelea katika maeneo mbalimbali. Kwa upande wa Dar es salaam zoezi hilo kwa mujibu wa ratiba tuliyopatiwa na Tume litafanyika kuanza 22 Machi mpaka 27 Machi.

Pia uwepo utaratibu wa kuwezesha vyama kupata rasilimali ikiwemo mafunzo ili kuhakikisha kwamba mawakala wa vyama wanasimamia kikamilifu na kuhakiki zoezi la uandikishaji. Aidha mkazo uwekwe kwa vyama vya siasa ili kuhakikisha vinashiriki kutoa elimu ya uraia na ya mpiga kura ili kuhamasisha wanachama wao na wananchi kushiriki kikamilifu katika zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Kadhalika pawepo na utaratibu utakaowezesha vyama vya siasa kupata DKWK wakati muafaka linapohitajika badala ya kutokupewa daftari hilo mpaka uteuzi wa wagombea unapofanyika (Rejea Tarime, Mbeya Vijijini, Busanda nk). Izingatiwe kuwa Daftari la Wapiga Kura, si nyaraka ya vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi tu bali ni nyaraka ya mpiga kura na wadau wengine ikiwemo waangalizi wa uchaguzi. Hivyo, Tume inapaswa kuwa na mfumo wa kuwezesha daftari hilo kuwa wazi kwa pamoja na mambo mengine kuliweka katika tovuti (website) kila uboreshaji unapofanyika. Mchakato wa uboreshaji wa daftari la kudumu na uhakiki wa wapiga kura ujadiliwe kama moja ya misingi muhimu ya marekebisho mapana ya kisheria kuwezesha uchaguzi huru na haki nchini ili kupata uongozi bora.
SEHEMU YA MAKALA HII ILITOKA KATIKA GAZETI LA NIPASHE TOLEO LA TAREHE 27 JANUARI 2010

Uhuru wa vyombo vya habari na utoaji wa elimu ya uraia vipewe kipaumbele katika marekebisho ya sheria za uchaguzi

Katika uchaguzi mkuu 2005 vyombo vya habari pamoja na mapungufu katika maeneo kadhaa vilifanikiwa kutoa taarifa kwa wapiga kura hususani kuandika habari za matukio mbalimbali ya kiuchaguzi. Hata hivyo havikufanikiwa kwa kiasi cha kutosha kutoa elimu ya uraia na kufanya uchambuzi wa kina kuhusu mwelekeo wa uchaguzi ikiwemo kufichua ufisadi/rushwa wakati wa uchaguzi. (habari pekee kubwa kuhusu rushwa katika uchaguzi ni ile iliyoandikwa na Gazeti la RADI toleo la April 27 mpaka Mei 6, 2005 ambayo lilichambua kwa kina kwamba Mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete ameleta kwa siri toka Oman mamilioni ya dola za mafuta kwa ajili ya kampeni zake. Habari ambayo haikukanushwa na timu ya Kikwete badala yake toleo la gazeti husika lilinunuliwa kwa bei ya jumla na kuisha mitaani mapema).

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010. Hatahivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe. Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi. Katika makala hii tutajadili suala moja la haja uhuru wa vyombo vya habari na utoaji wa elimu ya uraia kupewa kipaumbele katika marekebisho ya sheria za uchaguzi.

Kwa ujumla Vyombo kadhaa vya habari vilikiuka Maadili ya Vyombo vya Habari katika Uchaguzi ambavyo vyombo husika vilikubaliana kuyafuata ikiwemo ushabiki, upotoshaji na kutotoa nafasi sawa baina ya wagombea mbalimbali ( Ripoti ya Ufuatiliaji wa Vyombo vya Habari wakati wa Uchaguzi iliyotolewa na MISA-TAN na Ripoti ya Uchaguzi Mkuu iliyotolewa na TEMCO zimefafanua ukiukwaji huo). Hata hivyo, katika kipindi cha kuelekea uchaguzi wa mwaka 2010 nafasi ya vyombo vya habari katika siasa inaacha mengi kutokana na kuzuka kwa uandishi wa kushafuana na kushambuliana.

Midahalo ya wagombea urais kupitia vyombo vya habari ilipangwa mara tatu lakini haikuweza kufanyika kutokana na mgombea wa CCM kukataa kushiriki bila sababu kutolewa; hii imefanya historia kubaki kwamba mdahalo wa wagombea urais uliwahi kufanyika katika uchaguzi wa mwaka 1995 tu.

Ikumbukwe kuwa Tarehe 11 Disemba 2009 Serikali ilichapisha kwenye gazeti la serikali miswada miwili yenye kulenga kufanya marekebisho katika sheria za uchaguzi na kutangaza kupitia vyombo vya habari tarehe 21 Disemba 2009 maudhui ya miswada hiyo. Hata hivyo, marekebisho hayo yanayopendekezwa hayajagusa kikamilifu maeneo yanayoweza kuongeza mchango wa vyombo vya habari katika uchaguzi.

Masuala yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa na Serikali, Tume ya Uchaguzi, Vyama Vya siasa na Wadau wengine kama sehemu ya marekebisho ya kisheria yanayokusudiwa kufanyika kama sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010:

Utaratibu wa kikanuni na kisheria uwekwe kusimamia matangazo katika vyombo vya habari; katika mazingira ya matangazo ya kulipia ya kisiasa ni vyema ukatolewa utaratibu wenye usawa. Gharama za malipo lazima ziwiane baina ya vyama mbalimbali pamoja na muda wa matangazo kutangazwa. Kama haiwezekani kuweka mfumo wenye usawa katika eneo hili basi ni vyema sheria ikakataza matangazo ya kisiasa ya kulipia kama ilivyo katika baadhi ya nchi.

Nafasi ya vyama katika vyombo vya habari itolewe kwa usawa wakati wote, si wakati wa uchaguzi pekee; muda wa bure unaotolewa kwa vyama vya siasa na vyombo vya habari hususani vya umma uendelee kutolewa kwa vyama hata baada ya uchaguzi. Uwepo uratibu wa kisheria wa kutoa idadi ya wastani wa dakika kwa kila chama kwa mwezi katika vyombo vya habari vya umma.

Vyombo vya habari viwe na mkakati na mwelekeo wa kuibua masuala muhimu kwa wananchi na rushwa za kisiasa wakati wa uchaguzi; pamoja na kwamba vyombo vya habari vimefanikiwa kufanya rushwa/ufisadi kuwa ajenda ya msingi inayojitokeza mara kwa mara wakati wa kawaida, vyombo vya habari havijafanikiwa kuibua masuala ya rushwa zinaozoendelea wakati wa uchaguzi. Hili ni eneo ambalo linapaswa kufanyiwa kazi zaidi.

Sheria zinazozuia uhuru wa vyombo vya habari ikiwemo wakati wa uchaguzi zinapaswa kufanyiwa marekebisho; baadhi ya sheria hizo ni pamoja na Sheria inayolipa Bunge madaraka ya kumtaka mwandishi atoe kwa bunge chanzo chake cha habari; Sheria ya Kanuni ya adhabu ya mwaka 1945 kifungu 114(1) inayotoa mamlaka kwa mahakama kulazimisha chombo cha habari kutaja kufichua chanzo chake cha habari; Sheria ya Usalama wa Taifa ya Mwaka 1976 kipengele cha 15(2) inayotoa hukumu kwa yoyote anayekataa kutoa taarifa kwa usalama wa taifa; Sheria ya Magezeti ya Mwaka 1976 kinachotoa mamlaka ya kufungia chombo cha habari (kwa kutumia sheria hii gazeti la Tanzania Daima lilifungiwa kwa siku tatu wakati wa uchaguzi mkuu 2005). Tumeshuhudia hivi karibuni magazeti ya Kulikoni na Leo Tena yakifungiwa kwa kutumia sheria hiyo hali inayotoa ishara mbaya tunapoelekea uchaguzi mkuu. Hivyo, za miaka mingi ambazo zilianzishwa na wadau mbalimbali kutaka sheria ya uhuru wa taarifa na sheria ya vyombo vya habari ni muhimu zikapewa msukumo wa ziada ili miswada ya sheria hizo mbili itolewe na kupitishwa kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Kwa upande mwingine, katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 Taratibu zilizotolewa na Tume ya Uchaguzi ziliipa mamlaka Tume ya Uchaguzi kama chombo pekee chenye mamlaka ya kutoa elimu ya mpiga kura na kwamba asasi/taasisi yoyote ilipaswa kuomba kibali/ridhaa ya Tume kutoa elimu ya mpiga kura.

Elimu duni ya uraia na ya kisomo miongoni mwa wananchi ni moja ya kasoro ambayo imekuwa ikijitokeza katika uchaguzi. Kiashiria cha haraka ikiwa ni jinsi ambavyo walikubali kurubuniwa na kunyanyaswa kwa sababu za kisiasa. Elimu ya mpiga kura badala ya elimu ya uraia iliyopana ilitolewa na tume na wadau wengine hususani asasi zisizo za kiserikali(AZISE) kwa kiasi ambacho hakikufikia wapiga kura walio wengi na ilichelewa kuanza kutolewa. Ukosefu wa elimu ya kisomo hususani kutokujua kusoma na kuandika ulitumika kuwakosesha wananchi wasiokujua hakusoma na kuandika uhuru wao kwa ‘kupigiwa kura’ kwenda chama tawala kupitia mikakati mbalimbali.

Katika muktadha huo masuala yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa na Serikali, Tume ya Uchaguzi, Vyama Vya siasa na Wadau wengine kama sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 na kuzingatiwa pia katika marekebisho ya sheria husika yanayokusudiwa.

Tatizo la wananchi wengi kutokujua kusoma na kuandika linapaswa kujadiliwa na kushughulikiwa kwani linaathiri uchaguzi huru na haki wa viongozi. Uwepo wa watu wengi wasiojua kusoma na kuandika unaathiri uhuru wa kupiga kura na umetumika kuhujumu upinzani wakati wa uchaguzi. Serikali kwa miaka mingi imeshindwa kuwawezesha watanzania walio wengi hususani vijijini kujua kusoma na kuandika na kuitumia fursa hii kushinda uchaguzi. Hivyo kuna haja ya kujadili kama kuna sababu ya wananchi wasiojua kusoma na kuandika kupiga kura kama uhuru wao utaendelea kutumika visivyo na hivyo kupoteza haki yao ya kuchagua viongozi wanaowataka. Hivyo kama serikali ina nia njema ya kisiasa kuhakikisha kuwa kila mwananchi anapata uhuru na haki ya kupiga kura ni lazima kuweka mkazo kuhakikisha kuwa wananchi wote wanajua kusoma na kuandika.

Ni lazima kwa serikali, vyombo vya habari, asasi za kiraia na vyama vya siasa kutoa elimu ya kutosha ya uraia ili kuwezesha uchaguzi wenye amani ulio huru na haki. Mkazo uwekwe katika kuhakikisha elimu ya uraia inatolewa kwa wananchi walio wengi kama mchakato wa mapema na endelevu bila kusubiri wakati wa uchaguzi pekee. Elimu hii ya uraia ijumuishe pia elimu ya siasa, elimu ya mpiga kura, uzalendo, haki na wajibu wa mwananchi na haki za binadamu kwa ujumla. Ni muhimu kutambua kuwa ufahamu wa wananchi kuhusu michakato ya kisiasa katika mfumo wa vyama vingi ni muhimu kwa uchaguzi wa haki na kushamiri kwa demokrasia. Hii ni pamoja na kuboresha mitaala ya elimu ya uraia katika shule na vyuo iweze kukidhi mahitaji kwa pamoja na mambo mengine kuzingatia maoni ya wadau mbalimbali vikiwemo vyama vya siasa. Pia wananchi wawezeshwe kutambua mchango wa upinzani na mfumo wa vyama vingi katika kuchochea maendeleo ikiwemo kwa kuboresha uwajibikaji wa viongozi walioko madarakani.

Masuala haya yenye kuweka uwanja sawa wa ushindani katika uchaguzi wa demokrasia ya vyama vingi yanahitaji jambo moja kuweza kuzingatiwa: dhamira ya kisiasa ya utawala ulioko madarakani. Pasipo na dhamira; panahitajika mjadala wa umma utakaowezesha kuunganisha nguvu za kidemokrasia na kimaadili ili kudai na kushawishi mabadiliko ya sheria za uchaguzi na mazingira ya kisiasa. Kuna haja ya serikali kufanya marekebisho mapana zaidi au vyama vya siasa na wadau wengine waelekeze jitihada bungeni na mahakamani kudai mabadiliko ama kufutwa kwa vipengele vya sheria nyingine ambavyo vinafanya mazingira ya kisiasa na kiuchuguzi yanayokwaza uchaguzi huru na wa haki.
SEHEMU YA MAKALA HII ILITOKA KATIKA GAZETI LA TANZANIA DAIMA TOLEO LA TAREHE 27 JANUARI 2010

Wednesday, January 27, 2010

Marekebisho ya Sheria za uchaguzi yaondoe kasoro kwenye upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo

Tunapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ni muhimu kama taifa tuondoe kasoro kwenye upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo. Methodolojia na taratibu zinazosimamia upigaji kura, kuhesabu na kutangaza matokeo vimefafanuliwa katika Sheria ya Uchaguzi na. 1 ya mwaka 1985 kutoka kipengele cha 61(1) mpaka 87 na taratibu zingine za uchaguzi zinazotolewa. Mambo ya kufanya na kutofanya katika uchaguzi yalifafanuliwa katika Taratibu za Uchaguzi za Mwaka 2005 sehemu ya IV kipengele cha 39 mpaka 61. Kwa upande mwingine Sheria ya Uchaguzi na. 1 ya mwaka 1985 kipengele cha 61 mpaka 69 na Taratibu za Uchaguzi za mwaka 2005 kifungu cha 45 mpaka 52 vinaelekeza taratibu zinazopaswa kufuatwa katika vituo vya kupigia kura. Hata hivyo, zipo kasoro kwenye mchakato mzima wa upigaji kura, kuhesabu na kutangaza matokeo ambazo ni muhimu zikajadiliwa.

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010. Hatahivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe. Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi. Katika makala hii tutajadili suala moja la hoja na haya ya kuondoa kasoro kwenye upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo.

Lipo tatizo la wananchi hususani wanachama wa vyama vya upinzani kunyimwa ama kuogopeshwa kwenda kupiga kura. Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 na hata katika chaguzi za marudio kati ya mwaka 2006 na 2009 palikuwa na utaratibu wa majina kubandikwa nje ya vituo ambapo katika maeneo mbalimbali baadhi ya wananchi wengi wao wakiwa ni wanachama wa vyama vya upinzani walizuiwa kupiga kura pamoja na kuwa na vitambulisho vya kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura(DKWK) ama kwa kukosa majina yao nje ya vituo au taarifa zao kuwa na mapungufu au kutokuwepo kabisa katika daftari. Ishara zinaonyesha kuwa pengine huu ulikuwa ni mkakati rasmi kwa kuwa siku kadhaa kabla ya uchaguzi watendaji wa chama tawala hususani wajumbe wa nyumba kumi walipita na kuandikisha namba za wapiga kura katika maeneo yao. Kwa kuwa wananchi wengi walikuwa na elimu finyu ya uraia na kwamba katika baadhi ya maeneo wajumbe hawa wanasikilizwa sana na/au hata kuogopwa, wapiga kura wengi waliorodheshwa na hata wengine kutishwa kuwa kura zao zitajulikana na hivyo wasipoipigia kura CCM watashughulikiwa. Vitisho hivi vilipata nguvu kutokana na utaratibu wa kuchukuliwa namba za shahada za wapiga kura na wasimamizi wa vituo wakati wa kupiga kura. Hii ilifanya uchaguzi usiwe huru.

Pia, vyama vingi havikuweza kuweka mawakala kwenye vituo vyote kutokana na changamoto ya rasilimali na pia mawakala hawakuwa na mafunzo yanayowiana, kila chama kilitoa mafunzo kwa mawakala wake kwa utaratibu wake kwa kuzingatia maelekezo yaliyotolewa na Tume. Hivyo, kulikuwa na utofauti baina ya wasimamizi/wasaidizi wa vituo wa Tume na mawakala wa vyama katika utendaji wao.

Pia, zipo kasoro za moja kwa moja ambazo hujitokeza katika kuhesabu na kutangaza matokeo. Mathalani katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 Jimbo la Ubungo matokeo ya ubunge yalitangazwa kwa shuruti bila kutangaza na kujumlisha kwa pamoja matokeo ya kituo hadi kituo hali iliyoashiria kuwa matokeo ya Ubunge yalikuwa na utata. Kutangaza huku kwa nguvu ilikuwa ni mkakati wa kutaka matokeo hayo yasihojiwe kama ilivyokuwa katika matokeo ya urais ambayo yalichelewa kutangazwa kutokana na kukutwa na mapungufu mengi. Kwa hali iliyodhihirisha wazi kuwa matokeo yalipikwa, waliopiga kura za Ubunge walikuwa 185,684 wakati waliopiga kura za Rais walikuwa 152,525 na hivyo kufanya tofauti ya kura za Ubunge na urais kufikia 33,159. Katika hali ya kawaida na katika uchaguzi uliofanyika kwa wakati mmoja ilikuwa ni vigumu kwa tofauti kubwa ya kura kiasi hiki. Na hata kama wananchi wangekuwa hawapendi kupiga kura za rais kwa kuwa mpiga kura alikuwa akipewa karatasi zote tatu kura hizi zilipaswa kuwepo katika kura zilizoharibika kitu ambacho hakikutokea. Mfano wa Jimbo la Ubungo unaibua hoja ya utofauti mkubwa baina ya jumla ya wapiga kura katika ubunge na urais katika majimbo mbalimbali Tanzania, suala hili linapaswa kujadiliwa. Ufanyike uchambuzi huo kujua utofauti katika kila jimbo ili kuweza kubaini chanzo cha hali hiyo na kukabilina nacho.
Katika kipindi cha mwaka 2006 mpaka 2009, kumeonekana tatizo lingine ambalo nalo linahitaji mjadala wa kina; mwitikio mdogo wa wapiga kura katika chaguzi za marudio. Mathalani chaguzi ndogo za ubunge: Tunduru (48%), Kiteto (47%), Tarime(46%) na Mbeya Vijijini(35%). Kwa upande wa chaguzi ndogo za madiwani hali ilikuwa mbaya zaidi katika baadhi ya kata mathalani: Upanga Mashariki-Dar es salaam (7%) na Sombetini-Arusha(14%) nk. Suala linahitaji kufanyiwa utafiti na chombo zaidi ya kimoja, ili kuwianisha matokeo ya sababu na mazingira yatayoanishwa. Maelezo ya wananchi mbalimbali ni kwamba ‘kadi za kupigia kura zinanunuliwa ama kuchukuliwa kabla ya kwenda kupiga kura’. Uchunguzi wa kina utasaidia kubaini tatizo hili ambalo linaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa misingi ya uhuru na haki katika chaguzi zinazofuata.

Ikumbukwe kuwa Tarehe 11 Disemba 2009 Serikali ilichapisha kwenye gazeti la serikali miswada miwili yenye kulenga kufanya marekebisho katika sheria za uchaguzi na kutangaza kupitia vyombo vya habari tarehe 21 Disemba 2009 maudhui ya miswada hiyo. Miswada hiyo imeshajadiliwa na kamati husika za Bunge na inatarajiwa kujadiliwa ndani ya mkutano wa Bunge unaonza mwezi huu.

Hata hivyo, marekebisho hayo yaliyopendekezwa katika miswada hiyo hayajagusa kikamilifu maeneo yenye kasoro yanayohusu upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo. Eneo pekee linaloguswa katika marekebisho ni lile linalohusu zoezi la uandikishaji wapiga kura, ambapo imependekezwa katika ibara ya 7 kuwa na fungu jipya la 15A katika sheria linatoa nafasi kwa vyama vya siasa kuteua mawakala wakaokuwepo katika vituo vya kuandikisha wapiga kura kama ilivyo wakati waupigaji kura.

Hivyo ni muhimu mjadala ukapunuliwa kuwezesha kasoro kushughulikia likiwemo tatizo la kupungua kwa idadi ya wapiga kura. Zipo nchi ambazo sheria ya uchaguzi inalazimisha wananchi kupiga kura ili kuondokana na tatizo la kupungua kwa idadi ya wananchi wanaojitokeza kupiga kura. Mazingira ya kisheria yanaweza kuweka bayana kwamba uhalali wa kiongozi kutangazwa mshindi unategemea asilimia ya wananchi waliopiga kura. Kiongozi aliyechaguliwa na wananchi ambao hawafiki hata asilimia kumi ya wapiga kura waliojiandikisha uhalali wake uko mashakani.
Sheria na taratibu ziwezeshe pia kuwe na mafunzo ya pamoja baina ya mawakala wa vyama na wasimamizi/wasimamizi wasaidizi wa vituo vya kupigia kura. Hii ihusishe pia serikali kugharamia mawakala wa vyama. Ni muhimu kwa Tume na wadau wengine kuwatambua mawakala wa vyama kama sehemu ya msingi ya mchakato mzima wa uchaguzi hivyo mafunzo yao yafanyike sanjari na mafunzo ya wasimamizi/wasimamizi wasaidizi wa vituo. Hii ihusishe pia kuwezesha upatikanaji wa rasilamili kwa ajili ya kugharamia mawakala.
SEHEMU YA MAKALA HII ILITOKA KATIKA GAZETI LA MAJIRA TOLEO LA TAREHE 25 JANUARI 2010

Thursday, January 21, 2010

Marekebisho ya kisheria yafanyike kulinda haki wakati wa uteuzi wa wagombea

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010. Hatahivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe. Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi; na katika kujadili muswada huo makala hii itachambua suala la uteuzi wa wagombea pekee.

Uteuzi wa Wagombea upo katika ngazi mbili: Uteuzi wa Wagombea katika Vyama na Uteuzi wa Wagombea katika Tume ya Uchaguzi. Uteuzi wa ndani ya vyama unasimamia na katiba, kanuni na taratibu za vyama husika. Ni kawaida katika siasa za uteuzi ndani ya vyama kutawaliwa na ushindani mkubwa; lakini ieleweke kuwa kuna tofauti kati siasa chafu na siasa za ushindani. Siasa zenye ushindani chanya zinasababisha uteuzi wa wagombea ambao wenye uwezo kiuongozi mathalani elimu, uzoefu na dira. Siasa za ushindani hasi hupelekea kupatikana kwa wagombea ambao ushindi wao umetokana na rushwa, upendeleo, kupakana matope, udini, ukabila nk. Kwa mfano, uteuzi wa ndani ya CCM uligubikwa na ‘takrima’ na siasa za kupakana matope katika maeneo kadhaa ikiwemo kuanzia ngazi ya udiwani mpaka ya Urais. Mathalani inatajwa jinsi Salim Ahmed Salim (aliyekuwa Katibu Mkuu wa OAU) alivyopakwa matope (kwa mujibu wa Ripoti ya Uchaguzi Mkuu 2005 ya TEMCO). Ilifikia hatua Fredrick Sumaye, mmoja wa wagombea (ambaye pia alikuwa Waziri Mkuu wakati huo), akiwa analaani jinsi ambavyo anapakwa matope alitamka bayana kwamba “anayesafisha njia kwa kalamu, atatawala kwa risasi”.

Uteuzi wa wagombea katika Tume ya Uchaguzi unasimamiwa na Sheria ya Uchaguzi ya Mwaka 1985. Katika uchaguzi Mkuu 2005 wagombea wengi walipitishwa na Tume ya uchaguzi na mapingamizi mengi yalitupiliwa mbali tofauti na chaguzi zingine zilizotangulia.

Katika kipindi cha mwaka 2006 mpaka 2009, pameibuka suala ambalo linahitaji kufanyiwa kazi na marekebisho yakafanyika kuhusu mapingamizi dhidi ya wagombea katika chaguzi. Tutatumia mfano wa suala la mapingamizi katika uchaguzi wa ubunge na udiwani Mbeya Vijijini lakini ipo mifano pia katika chaguzi zingine za marudio ikiwemo za madiwani, mitaa, vijiji na vitongoji. Mgombea wa CHADEMA aliwasilisha fomu zake kwa ajili ya uteuzi tarehe 27 Disemba 2008 na kuteuliwa kuwa mgombea.

Hata hivyo tarehe 28 Disemba, 2008 mgombea aliwekewa pingamizi na mgombea wa CUF na mgombea wa CCM. Misingi ya pingamizi ni pamoja na kuwa mgombea wa CHADEMA alijiapisha mwenyewe na kwamba mgombea aliapa kwa wakili badala ya kuapa kwa hakimu. Msimamizi alimtaka mgombea kuwasilisha maelezo yake, na mgombea aliwasilisha maelezo ya kukanusha kujiapisha, kutoa ufafunuzi kuhusu mpangilio wa majina na kueleza kwamba aliapa mbele ya wakili kwa kuzingatia tarehe ambazo alipaswa kuapa na kwa kuwa ipo sheria nyingine ya viapo inayoruhusu kuapa mbele ya wakili. Na kwamba sheria ya uchaguzi haikatazi moja kwa moja viapo vya waapishaji wengine.

Tarehe 29 Disemba 2008 Msimamizi wa Uchaguzi alikubaliana na eneo moja la pingamizi zilizowasilishwa na CCM na CUF la mgombea kuapa mbele ya wakili badala ya hakimu na kutupilia mbali maeneo mengine ya pingamizi.

Tarehe 30 Disemba 2008 mgombea wa CHADEMA aliwasilisha rufaa dhidi ya maamuzi ya msimamizi wa uchaguzi kutokana na misingi ifuatayo: Kwamba Msimamizi wa uchaguzi wa Jimbo la Mbeya Vijijini hakusoma kwa umakini maelezo ya mrufani na kuyazingatia kikamilifu kabla ya kufanya maamuzi ya kumuengua; Kwamba msimamizi wa uchaguzi hakuzingatia maelezo ya mrufani juu ya muda wa uchukuaji fomu na urejeshaji fomu uliojumuisha siku nyingi takribani tatu mfululizo zisizokuwa za kazi( za sikukuu na siku ya mapumziko ya mwisho wa wiki) ambapo mahakama hazikuwa wazi(operative) na kwamba aliweza kusaini mbele ya wakili tarehe 24 Disemba, 2008 jioni baada ya kumaliza kujaza fomu husika. Na kuomba tume izingatie kifungu 38(1)(4)(proviso) cha sheria ya uchaguzi namba ya mwaka 1985.

Kwamba msimamizi wa uchaguzi wa jimbo alikosea katika kuelezea kuwa sheria ya uchaguzi inasema “mgombea ubunge aape mbele ya hakimu na si vinginevyo” wakati maneno “na si vinginevyo” hayapo kwenye sheria bali ni nyongeza yake tu ili afikie maamuzi ya kumuengua mrufani. Kifungu cha 50 cha sheria ya uchaguzi (National Election Act CAP 343 RE 2002) kinahusika.

Kwamba msimamizi wa uchaguzi amekosea kisheria kwa kutosoma sheria za viapo na kwa kutozingatia maelezo yangu kwamba sheria ya uchaguzi inapaswa kusomwa pamoja na Oaths(Judicial Proceedings and Statutory Declarations Act) pamoja na Notaries Public and Commissiners for Oaths Act(CAP 12 RE 2002), sheria ambazo zinaeleza bayana nani anayepaswa kuapisha kisheria na maana ya kiapo au ‘declaration’. Kifungu cha 11 cha sheria ya viapo “Notary Public and Commissiners for Oath (CAP 12 RE 2002) inaeleza waziwazi kwamba hakuna kizuizi chochote dhidi ya kiapo cha wakili au kamishna yeyote wa viapo.

Kwamba msimamizi wa uchaguzi amekosea kisheria kwa maamuzi yanayoonyesha kuwa sheria ya uchaguzi ni ya kiubaguzi na kwamba inazuia sheria zingine kutumika katika nchi hii. Kwamba msimamizi wa uchaguzi alikosea kisheria kwa kutozingatia maelezo yangu kwamba hakimu anapofanya kazi ya kuapisha hawi hakimu bali anakuwa ‘commissiner for oaths’ kama ilivyoainishwa katika kifungu cha 3 na 10 cha Notaries Public and Commissioner for Oaths Act na kwamba nani anapaswa kufanya jukumu hilo. Kwa maana ya sheria hiyo hakimu hawi tofauti na watu wengine waliotajwa na sheria hiyo wakati anaapisha. Kwamba msimamizi wa uchaguzi amekosea kisheria kwa kushindwa kuelewa hali halisi ya demokrasia ya vyama vingi na mahitaji ya wapiga kura wa jimbo la Mbeya Vijijini kwa kuwanyima haki ya kuwa na uwanja mpana wa uchaguzi kwa ridhaa yao. Kumuengua mrufani ni kulazimisha watu wa Mbeya Vijijini kuchagua vyama ama wagombea waliobakia ambapo ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na kuomba tume izingatie kifungu 38(1)(4)(proviso) cha sheria ya uchaguzi namba ya mwaka 1985. Tarehe 2 Januari 2009 Tume ilitupilia mbali rufaa ya mgombea wa CHADEMA kwa misingi mbalimbali na hivyo mgombea husika akaendelea kuenguliwa.

Taarifa za pingamizi zilifikia viongozi wa chama kabla ya mapingamizi kuwekwa zikieleza mawasiliano ya karibu baina ya viongozi wa waweka pingamizi katika uchaguzi wa Mbeya Vijini na Maofisa wa serikali. Kadhalika ilionyesha wazi kwamba palikuwa na mashinikizo la kutoka nje toka ngazi za juu za CCM na serikali katika kuamua kuhusu pingamizi hilo. Kwa hali ya kisiasa ilivyokuwa, pingamizi hilo lilionekana wazi kuwa ni njia pekee iliyokuwepo ya kuepusha CCM kushindwa na CHADEMA katika uchaguzi huo. Hivyo, tume haikutaka kabisa kuzingatia kwamba siku za kiapo hazikuwa zikitosha na tume haikutaka kabisa kutumia mamlaka yake ya kupokea fomu hata kama haina kiapo ama ina kiapo batili kutokana na mazingira hayo. Hata hivyo, maelezo ya Tume yanaashiria pia kuwa tume ilitambua uwepo wa udhaifu katika sheria ya uchaguzi wa kulazimisha kiapo kufanywa na hakimu pekee.
Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi uliochapwa kwenye gazeti la serikali tarehe 11 Disemba 2009 unaonyesha kwamba marekebisho ya sheria yanayopendekezwa hayatagusa kabisa vifungu vyenye utata kuhusu mamlaka za kuapisha wagombea wala masuala yenye kuwezesha haki na usawa katika uteuzi wa wagombea katika ngazi zote za uteuzi ndani na nje ya vyama.

Suala pekee ambalo Serikali kupitia Ofisi wa Waziri Mkuu imetangaza kuwa imeandaa marekebisho ambayo imeyaita ‘makubwa’ linalogusa uteuzi wa wagombea ni kuhusu utuezi wa mgombea urais au mwenza inapotokea mmoja wao akafariki katikati ya kampeni. Muswada wa marekebisho ya sheria unapendekeza kupunguzwa kwa muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa nafasi ya urais au umakamu inapotokea mmoja wao anafariki kabla ya uchaguzi ambayo imejinadi kuwa yanalenga pia kuipunguzia nguvu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC). Ibara ya 9 inapendekeza marekebisho katika fungu la 35A la sheria kwa lengo la kupunguza muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa urais au umakamu wa rais inapotokea wagombea hao wamefariki.

Masuala yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa na Serikali, Tume ya Uchaguzi, Vyama Vya siasa na Wadau wengeni kama sehemu ya marekebisho ya kisheria yanayopaswa kufanyika kulinda haki wakati wa uteuzi wa wagombea.

Mosi; vyombo vya uangalizi na usimamizi viwezeshwe kisheria kufuatilia kuhakikisha uteuzi wa ndani ya vyama unakuwa huru na haki. Kuna haja ya vyombo mbalimbali viwezeshwe kutupia macho uteuzi ndani ya vyama kuhakikisha haki inatendeka. Mathalani Tume ya uchaguzi na ofisi ya Msajili wa Vyama vya siasa hawapaswi kuwa kimya siasa za kupakana matope zinaoendekezwa wakati wa uteuzi wa baadhi ya vyama hususani CCM. Pia Taasisi ya Kuzuia na Kupambana Rushwa (TAKUKURU) ifuatilie na kuchukua hatua zinazostahili kuhusiana na vitendo vya rushwa vinavyoendelea wakati wa mchakato wa uteuzi katika baadhi ya vyama; utawala wa sheria lazima uheshimiwa hata ndani ya mipaka ya Kikatiba za Vyama vya siasa nchini.

Pili; marekebisho ya sheria ya uchaguzi yahusishe pia kufuta vipengele vibovu vinavyotoa mianya ya mapingamizi yanayokwenda kinyume na haki za kikatiba za wagombea na vyama vyao. Ni vyema mchakato wa kurekebisha sheria ya uchaguzi ukahusisha kuondoa kigezo cha kulazimisha kiapo kwa hakimu pamoja na vigezo vingine ambavyo ni nje ya vigezo kwa kikatiba vya sifa za mgombea. Marekebisho haya yasipofanyika itakuwa ni ishara ya wazi ya kwamba Tume ya Uchaguzi imeacha mwanya kwa mapingamizi kutumika kama zana ya kuhujumu wagombea na vyama vyao katika chaguzi. Tume ya uchaguzi iondoe mianya ya wagombea kukwepa ushindani wa kwenye jukwaa la umma na kukimbilia kutafuta ushindi wa mezani.
SEHEMU YA MAKALA HII ILITOKA KATIKA GAZETI LA MAJIRA TOLEO LA TAREHE 20 JANUARI 2010

Wednesday, January 20, 2010

Mapendekezo ya serikali hayatawezesha kikamilifu uchaguzi huru wa viongozi


KWA kuwa siasa (nikimaanisha siasa safi) ni hitaji muhimu la maendeleo kama alivyowahi kusema hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere; basi uendeshwaji wa uchaguzi (kwa maana ya uchaguzi huru na haki); ndio njia ya kulipata hitaji hili.

Uendeshwaji wa uchaguzi huru na haki hutupatia pia hitaji jingine la msingi kwa maendeleo - yaani “Uongozi Bora”. Suala kuu ni kuwa na mifumo ya kikatiba na kisheria na kiuwanja wa kisiasa ambayo inahakikisha uchaguzi huru na haki.

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010.

Hata hivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe.

Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi.
Ikumbukwe kwamba tume ya uchaguzi na viongozi wa vyama vya siasa Aprili 21, 2009 mkoani Dar es Salaam mkutano ambao nilishiriki.

Katika mkutano huo nilieleza masikitiko yangu kwamba tangu baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu mwaka 2005, Tume ya Uchaguzi haikuitisha mkutano na vyama vya siasa kuhusu maandalizi ya Uchaguzi Mkuu hadi mwaka 2009, takriban mwaka mmoja tu kabla ya uchaguzi.

Hii inaacha maswali kuhusu dhamira ya tume katika kuhakikisha taifa linakuwa na uchaguzi huru na haki; hasa ukizingatia kwamba toka mwaka 2006; CHADEMA na wadau wengine tumekuwa tukihitaji kukutana na tume na pia tukihimiza mchakato wa mabadiliko ya kweli kuanzishwa.

Niliweka bayana mashaka yangu nikizingatia kuwa masuala ya uchaguzi mkuu yanahusu mabadiliko ya kisheria, kimfumo n.k, ambayo huchukua muda mrefu kuweza kupitishwa na kutekelezwa, hivyo kitendo cha kuanza majadiliano wakati huu, kinaashiria kuwa sehemu kubwa ya yatakayojadiliwa; hayataweza kutekelezwa.

Kwa upande mwingine nilishukuru kuitishwa kwa mkutano huo nikiwa na matarajio kuwa baada ya kukutana huko tume kwa kushirikiana na serikali ingeweza bado kuchukua hatua za haraka kuweza kufanya mabadiliko yanayokusudiwa katika kipindi kifupi kilichobaki.

Mkutano huo, baada ya kupokea maoni ya ujumla kutoka kwa vyama vya siasa uliahirishwa baada ya muda mfupi bila maamuzi yoyote ya msingi kufikiwa kwa maelezo kwamba ungeitishwa mkutano mwingine baada ya kufanya mapitio ya hoja na vielelezo vilivyotolewa na wachangiaji mbalimbali.

Takriban miezi minane, yaani zaidi ya nusu mwaka ukapita mpaka ikafika mwezi Desemba 2009; siku chache kuelekea 2010, si Tume ya Uchaguzi wala serikali ilikuwa imefanya kikao na vyama vya siasa kufikia makubaliano kuhusu marekebisho yanayokusudiwa.

Hata hivyo, katika mwezi wa Desemba 2009 vyombo vyote viwili; tume ya uchaguzi na serikali viliibuka na kutoa kauli zinazoashiria kwamba tayari maamuzi yameshafikiwa kuhusu suala hili nyeti linalohusu mustabali wa wananchi wote bila kujali vyama.

Ilianza Tume ya Uchaguzi ambayo Desemba mosi, 2009 ilifanya mkutano na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari kuelezea kile ilichokiita mkutano wa kubadilishana mawazo na kupeana taarifa kuhusu maandalizi ya uchaguzi mkuu 2010.

Katika mkutano huo mada na hotuba zilionyesha bayana kwamba tayari yapo marekebisho ambayo tume kwa kushirikiana na serikali wameshakusudia kuyafanya; huku mabadiliko mbalimbali ya msingi yakiwa ni sehemu ya hoja zilizowasilishwa.

Siku chache baadaye Desemba 2009 11, serikali ikachapisha kwenye gazeti la serikali miswada miwili yenye kulenga kufanya marekebisho katika sheria za uchaguzi. Siku kumi baadaye serikali ikafanya kile kilichoitwa kuweka hadharani miswada hiyo miwili kupitia taarifa yake fupi kwa vyombo vya habari Desemba 21, 2009.

Serikali ilitangaza marekebisho hayo yakiwa na mapendekezo ya kufanyia marekebisho sheria ya uchaguzi sura ya 343 na sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa sura ya 292, lengo lililoelezwa kuwa ni kuondoa upungufu mbalimbali uliojitokeza katika chaguzi zilizopita kuiwezesha NEC kuendesha uchaguzi kwa ufanisi.

Serikali ikaeleza kuwa upungufu uaokusudiwa kurekebishwa katika muswada huo ni pamoja na NEC kutokuwa na madaraka ya kuteua waratibu waandikishaji wa mikoa.

Pia kushughulikia suala la kipindi cha kuboresha daftari la kudumu la wapiga kura kutotajwa bayana katika sheria na sheria kutoruhusu baadhi ya watendaji wa tume kuingia katika vituo vya kupigia kura ili kufuatilia zoezi la upigaji kura.
Ibara ya 6 imependekeza marekebisho katika fungu la 15 la sheria, ili kuweka bayana kipindi cha kufanya uboreshaji wa daftari la taifa la kudumu la wapiga kura kuwa mara mbili katika Uchaguzi Mkuu mmoja na unaofuata.

Aidha, sehemu hiyo inasisitiza kwamba, kwa lengo la kuongeza uwazi katika zoezi la uandikishaji wapiga kura, imependekezwa katika ibara ya 7 kuwa na fungu jipya la 15A katika sheria linatoa nafasi kwa vyama vya siasa kuteua mawakala wakaokuwepo katika vituo vya kuandikisha wapiga kura kama ilivyo wakati waupigaji kura.

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imetangaza kuwa imeandaa marekebisho ambayo imeyaita ‘makubwa’ ya sheria za uchaguzi ambayo pamoja na mambo mengine, imependekeza kupunguzwa kwa muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa nafasi ya urais au umakamu inapotokea mmoja wao anafariki kabla ya uchaguzi ambayo imejinadi kuwa yanalenga pia kuipunguzia nguvu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Ibara ya 9 inapendekeza marekebisho katika fungu la 35A la sheria kwa lengo la kupunguza muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa urais au umakamu wa rais inapotokea wagombea hao wamefariki.

Sehemu ya muswada huo wa sheria ya uchaguzi imependekeza kufutwa kwa vifungu vya sheria vinavyoruhusu utoaji wa takrima.

Muswada unapendekeza pia Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ipewe mamlaka ya kuteua wasimamizi wa uchaguzi kutokana na ofisi au sifa zao tofauti na ilivyo ambapo tume huteua wasimamizi wa uchaguzi kutokana na ofisi pekee.

Marekebisho hayo pia yanapendekeza kuongeza muda wa rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama Kuu, katika Mahakama ya Rufaa kwenye kesi za uchaguzi na kuongezwa kwa muda wa kufungua kesi kutoka siku 14 za sasa hadi siku 30.

Ibara ya 10 imependekeza marekekibisho katika fungu la 37 la sheria ili kuweka ukomo wa muda wa kufanya chaguzi ndogo za Bunge kama inavyobainishwa katika ibara ya 76(3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977.

Katika Ibara ya 3, muswada unapendekeza kuongeza tafsiri ya maneno mbalimbali katika sheria ya uchaguzi; unapendekezwa kurekebisha tafsiri ya maneno “nomination” na “Member of Parliament” ili kujumuishwa katika tafsiri ya uteuzi (nomination) uteuzi wa wabunge wanawake wa viti maalumu na katika tafsiri ya mbunge (member of Parliament) mbunge wa kuteuliwa wa viti maalumu vya wanawake.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Ibara ya 13 inakusudia kufanya marekebisho katika sura ya V ya sheria kwa kuongeza sehemu mpya ya III inayohusu mchakato wa mamlaka ya tume kuwatangaza wabunge wanawake wa viti maalumu walioteuliwa na vyama vyao kuwa wabunge.

Marekebisho hayo ambayo serikali imeyapendekeza yanatarajiwa kujadiliwa katika kikao cha Bunge hivi karibuni ili yatumike kwenye uchaguzi wa mwaka 2010.

Hata hivyo, marekebisho hayo hayajitoshelezi kabisa ukilinganisha mapungufu yaliyopo, muda uliopo, hoja za wadau na rasilimali ambazo zimetolewa na wadau mbalimbali kuwezesha mchakato wa marekebisho ya kisheria na kitaasisi nchini kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Hivyo mjadala utakaowezesha kuunganisha nguvu za kidemokrasia na kimaadili ili kudai na kushawishi mabadiliko ya sheria za uchaguzi na mazingira ya kisiasa ni muhimu uibuliwe na kuendelezwa.

Kuna haja ya serikali kufanya marekebisho mapana zaidi au vyama vya siasa na wadau wengine waelekeze jitihada bungeni na mahakamani kudai mabadiliko ama kufutwa kwa vipengele vya sheria nyingine ambavyo vinafanya mazingira ya kisiasa na kiuchuguzi yanayokwaza uchaguzi huru na wa haki.

Kwa muhtasari lazima kuzipitia sheria na/ama kufanya mabadiliko/marekebisho ya msingi yafuatayo ambayo hayajaguswa katika miswada iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mosi, tume lazima iwe huru na ya kudumu yenye kufanya kazi muda wote na kuwekewa bajeti maalumu na watumishi wa serikali wasitumike katika uchaguzi badala yake kuwe na watendaji huru wa tume katika ngazi zote kama ilivyo kwa mahakama.

Pili, kupanua wigo wa mfumo wa uwakilishi wa uwiano na kuweka mfumo mchanganyiko/mchanyato. Tatu; Kufuta vipengele katika sheria vinavyoruhusu mapingamizi yanayokwenda kinyume na misingi ya masharti ya kikatiba ya wagombea.

Nne, kuchunguza na kukabiliana na tatizo la mwitiko mdogo wa wapiga kura. Tano, kuhakikisha kwamba mafunzo ya pamoja yanafanywa baina ya wasimamizi/wasaidizi wa vituo na mawakala wa vyama; na kuhakikisha wgombea/vyama vinakuwa na rasilimali za kuwezesha kuwa na mawakala katika vituo.

Sita, kutoa uhuru wa vyombo vya habari ikiwemo wakati wa uchaguzi; Kuweka usawa katika matumizi ya vyombo vya habari ikiwamo kuhusu matangazo ya kisiasa ya kulipia wakati wa kampeni.

Ni wazi: Sehemu kubwa ya mabadiliko haya yanahitaji kitu kimoja tu: mabadiliko ya katiba ya nchi.

Hakuna uhuru na haki kwa vyama vya siasa kushiriki kwenye chaguzi zijazo kama mazingira ya kisiasa na kiuchaguzi hayatabadilika katika nchi yetu!

Monday, January 18, 2010

Uchaguzi Mkuu 2010: Kwa Pamoja Tutashinda


Kwa kuwa hii ni makala yangu ya kwanza kwa mwaka huu inayotoka katika toleo la kwanza kabisa la Mwanahalisi kwa mwaka 2010 nianze kwa kuitakia timu nzima ya gazeti hili na wewe msomaji wake heri ya mwaka mpya wenye upendo, furaha na mafanikio.

Mwishoni mwa mwaka 2009 paliibuka majadiliano ambayo yanaendelea mpaka hivi sasa kwenye mtandao kupitia www.facebook.com/john.mnyika kuhusu ‘Ubunge Ubungo 2010: Nigombee Nisigombee?’

Wachangiaji wote waliotoa maoni yao mpaka sasa wamenitaka nigombee huku wakitoa sababu mbalimbali. Wapo waliotoa hoja ya kutambua uwezo, haja ya kubeba harakati za kizazi kipya kushiriki kwenye uongozi wa taifa letu na kufanya vizuri mwaka 2005 wakati huo nilipogombea ubunge wa jimbo hilo nikiwa na umri wa miaka 24.

Mchangiaji mmoja alirejea mfano wa Barack Obama ambaye alikuwa na mashaka kuhusu kugombea kwake lakini mmoja wa washauri wake wa karibu akamweleza kwamba ‘usipogombea umechagua kushindwa; lakini ukigombea una chaguo la kushinda ama kushindwa’. Walatini wana msemo ‘Sauti ya watu ni sauti ya Mungu’; hivyo zitazijadili kwa sasa hoja husika.

Majadiliano hayo yalifanya nihitimishe mwaka 2009 kwa makala “Kuelekea 2010: Kwa Pamoja Tunaweza” kuwezesha tafakari ya wengine ambao ni sehemu ya wapiga kura ama wananchi kwa ujumla hawana fursa ya kushiriki majadiliano kwenye tovuti. Tafakari pana zaidi tunapoelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010; nini kinawasukuma wagombea kujitokeza kugombea: dhamira binafsi ama msukumo wa umma au vyote?

Katika makala hiyo nilijenga hoja kwamba kwa mgombea ambaye utumishi wake bado haufahamika kwa umma anaweza kusukumwa kugombea kwa dhamira binafsi lakini kwa mgombea mtarajiwa ambaye anafahamika tayari: nguvu alizonazo, udhaifu alionao, fursa alizonazo na vikwazo vinavyomkabili; si vizuri naye asukumwe na dhamira binafsi pekee.

Kwa mgombea mtarajiwa ambaye anafahamika kwa wananchi ni muhimu pamoja na dhamira yake binafsi pawe pia na msukumo wa umma; hii ni kwa sababu nafasi za kuchaguliwa kama ubunge ni za kuwakilisha wananchi. Ni muhimu sehemu ya wananchi: iwe ni wanachama wa chama, wapiga kura ama baadhi ya watu katika jumuia waone haja hiyo na watoe hoja hiyo kwake au kwa wapiga kura wenzake.

Nashukuru kwamba wananchi karibu wote (isipokuwa mmoja) waliopiga simu ama kutuma ujumbe mfupi wa maneno waliunga mkono maudhui ya makala hiyo; maoni mbalimbali waliyoyatoa ndio yamenihamasisha kuandika makala hii kuendeleza mjadala.

Mtu mmoja (namba yake naihifadhi) alituma ujumbe mfupi ufuatao, namnukuu “unajisumbua tu huo ubunge wa Ubungo hatukupi, hili sio jimbo la dini yenu tu kila wakati, tunajitaji mwenzetu sisi”.

Ujumbe ukanipa hisia kwamba wapo watu wachache katika jamii yetu wanaotazama watu wengine- si kwa haiba yao, dira yao, maadili yao au uwezo wao; bali dini zao. Hali hii ikiendelezwa katika taifa letu inaweza kututumbukiza katika ubaguzi; iwe wa kidini, kikabila au wa aina nyingine yoyote.

Nilimjibu kwa ufupi tu kwamba “Mwenyezi Mungu akuwezeshe kutambua kwamba Bunge sio kanisa, msikiti wala sinagogi na kwamba mbunge sio padri, shehe au kasisi”; hakujibu tena chochote mpaka sasa.

Taifa letu dini (secular state) lakini inaheshimu uhuru wa kuabudu na watu wake wanadini zao; hii ni moja ya tunu katika katiba ya nchi yetu. Natambua nafasi ya dini zetu katika kujenga maadili ya wananchi, tunapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 tukiwa na haja na hoja za kufanya mabadiliko umoja wetu ni jambo la muhimu; kwa pamoja tutashinda.

Kugombea nafasi za kuchaguliwa zinazohusisha kuwakilisha umma hakupaswi kuwa suala la mtu binafsi pekee au maslahi ya wachache kwa kisingizio cha dini au kabila. Matokeo ya kuwaachia wagombea binafsi, au vikundi vyao ama vyama vyao pekee ni kuwa na viongozi ambao baada ya kuchaguliwa kwao; kwa sababu waliingia kwa dhamira zao na wakafanya kampeni ‘kivyaovyao’; hawawajibiki kwa umma.

Hivyo tunapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ni muhimu kwa wapiga kura na wananchi kwa ujumla kutambua kwamba suala la uongozi wa kuchaguliwa kuwakilisha umma ni wajibu wa pamoja (shared responsibility).

Ni wajibu wa yoyote (bila kujali chama, hali, dini au kabila) anayetambua kwamba Mwenyezi Mungu ameijalia nchi yetu na watu wake rasilimali; iwe ni vipaji vyetu, kodi zetu ama maliasili: hivyo tunawajibika kujenga taifa lenye kutoa fursa ya ustawi wa wananchi. Kwa pamoja tutashinda!.

Tuzingatie bila kujali chama, dini wala kabila kwamba mabadiliko ya kweli katika taifa letu hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile, chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale. Kwa falsafa ya chukua chako mapema; Tanzania yenye neema haiwezekani. Tunahitaji fikra mbadala za kuleta ukombozi kwa kuwa mabadiliko yanawezekana. Tuunganishe nguvu kubadili mfumo wa utawala; kwa pamoja tutashinda.

Wazazi, wanafunzi, wazee, wanawake na masikini kwa ujumla wenye kuathirika na kuongezeka kwa gharama za maisha na kuporomoka kwa huduma za kijamii nchini iwe ni elimu, afya, maji, mafao ya wastaafu kwa pamoja tutashinda na kuweka mifumo thabiti ya usalama na haki katika jamii (social security and social justice) ili kuepusha migogoro.

Hata mwenye uwezo na fursa anayeona hatari inayolinyemelea taifa kutokana na kuongezeka kwa pengo kati ya wenye nacho na wasiokuwa nacho, ukosefu wa ajira hususani kwa vijana nk ambayo ni mabomu ya wakati yenye athari vizazi hata vizazi yanayoweza kuepukwa ujumbe wangu kwake ni kuwa pamoja tutashinda ikiwa tutaweka pembeni ubinafsi na kujali maendeleo ya sekta zinazogusa mustakabali wa waliopembezoni.

Natoa rai kwa watumishi wa umma iwe ni walimu, polisi, wahudumu wa sekta ya afya nk ama wafanyakazi binafsi ambao wanataka mabadiliko kutoka katika mishahara midogo na mazingira magumu ya kazi, maslahi duni kwa kwa pamoja tutashinda na kujenga taifa lenye kuthamini utaalamu.

Watanzania wote waadilifu wanapaswa kukerwa na ufisadi mkubwa unaolitafuna taifa huku hatua zinazostahili kushindwa kuchukuliwa kutokana na ufisadi kutapakaa katika mfumo mzima wa utawala na kuteteresha hata utawala wa sheria. Hivyo pamoja tutashinda na kufanya mabadiliko ili turejeshe uwajibikaji na maadili ya taifa.

Hivyo, ni muhimu kwa yoyote anayetaka mabadiliko; mosi, ajiandikishe kupiga, ajitokeze kugombea au ashawishi wenye msimamo wa kuunga mkono mabadiliko ya kweli kujitokeza kugombea katika kata, majimbo, taifa na kupiga kura katika uchaguzi mkuu. Pili, ajiunge na harakati za kufanikisha ushindi katika uchaguzi mkuu kwa hali na mali; pamoja tutashinda.

Tushirikiane katika kufikia azma ya kugombea kama njia ya kuunganisha nguvu ya umma hata katika kampeni za uchaguzi. Katika siasa za ushindani, ni muhimu harakati za uchaguzi zikaendeshwa katika mfumo wa vuguvugu (movement) hususani kwa wagombea wanaopitia vyama mbadala ambavyo havitegemei nguvu ya dola.

Ikumbukwe kuwa kushiriki kuleta mabadiliko ni zaidi ya matukio ya kugombea ama kupiga kura; ni pamoja na kushiriki katika mchakato mzima wa kuleta mabadiliko kwa njia mbalimbali. Kwa pamoja tutashinda hivyo tunahitaji nguvu yako katika kufanya mabadiliko; kama alivyosema Mahatma Gandhi ‘kuwa wakala wa mabadiliko unayotoka kuyaona’.

Tutashinda ikiwa wapenda demokrasia wote watatambua kwamba hujuma za kwenye uchaguzi zinaweza kudhibitiwa kwa kuunganisha nguvu ya umma kuweka uwanja sawa wa kisiasa ikiwemo kwa kujenga vuguvugu thabiti la ulinzi wa kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Tuwasiliane, tushauriane na tushirikiane kwa pamoja tutashinda.


Mwandishi wa makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa CHADEMA anayepatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.or.tz na http://mnyika.blogspot.com

Friday, January 15, 2010

The Two Bills: Electoral Reform or Assault on Democracy in Tanzania?

You will know that 11th December 2009 the Prime Minister’s Office of the Government of the United Republic of Tanzania published a Bill Supplement to the Gazette of the United Republic of Tanzania. The bills are scheduled to be discussed by responsible Parliamentary committees from 18th January 2010 on wards.

The Bill Supplement introduces Government proposals to amend certain electoral laws as well as to enact a completely new law to regulate election financing in Tanzania.

The electoral laws sought to be to amended by the proposed Electoral Laws (Miscellaneous Amendments) Act, 2009 are the Elections Act, 1985 Chapter 343 of the Revised Edition of the Laws of Tanzania, and the Local Government (Elections) Act, 1979 Chapter 292 of the Revised Edition of the Laws of Tanzania.

On the other hand, the proposed Election Expenses Act, 2009 seeks to regulate all aspects of election financing of general elections in Tanzania. The latter Bill makes wide-ranging proposals which, if enacted into law, will have far reaching and serious implications on the right to participate in electoral processes of not only the opposition political parties but also of all sections of the organized civil society. The amendments it proposes are a mere shuffling of provisions of the current electoral laws and/or a nibbling at the edges of existing law.

I kindly bring to your attention the Position Paper of CHADEMA’s Directorate of Legal and Constitutional Affairs and Human Rights on the respective bills. (Attached)

The paper analyses the Bills in the current and immediate past historical context in order to understand their import or true meanings.

On proposed Electoral Laws (Miscellaneous Amendments) Act, 2009

The statement of objects and reasons accompanying the Amendment Bill gives its object as being “to improve the efficiency and performance of the Commission in discharging its mandate in conducting elections.” The reason for the Amendment Bill is given as “the experience and short-comings or deficiencies that were noted in the last election.” The shortcomings or deficiencies the Bill identifies are lack of mandate to appoint regional election coordinators, lack of clarity regarding the updating of the voters register and lack of access to election centres by officers of the Commission.

The paper maintains that these cannot be the real reasons for the Amendment Bill. The paper indicates that the most of the proposals made are part of the current electoral laws and have not in any case been identified in the statement of objects and reasons as being problematic. They have also never been the subject of any serious demand for change by opposition parties or the organized civil society. The proposed amendments to the electoral laws are largely cosmetic as they do not alter the basic, or even formal, structure of the current electoral system. The proposed amendments also do not create any significant new rights or obligations. There is, in other words, nothing reformist in these proposals.

The paper maintains that the Amendment Bill is intended to deceive the people and perhaps the donors by creating the illusions of electoral reform while leaving intact the pillars of the current electoral system. Its proposals are intended to consolidate and buttress status quo while giving the fig leaf of reform. The real intent is to divert attention away from calls for real reforms that have been at the centre of demands by opposition parties and the organized civil society. The paper reveals that crucial questions such as the demand for an independent electoral commission and concomitant institutional machinery; independent candidates; and the streamlining of electoral procedures to expand rather than constrict electoral rights and freedoms have been swept under the legislative carpet.

The paper recommends that the Amendment Bill be significantly revamped by deleting all proposals that are already part of the existing electoral laws and/or do not add any value to the current electoral system. On the other hand, the paper recommends proposals that have to be incorporated to form part of the Amendment Bill.


On the proposed Election Expenses Act, 2009

According to its statement of objects and reasons, the thrust of the Election Expenses Bill is, inter alia, “to control the use of funds and illegal practices in the nomination process....” Other objects are “restricting foreigners, be it a government, an international organization, or institution to provide funds for election expenses”; and checking illegal practices in the election process. These objects are to be attained through pre-and post-election disclosure and reporting mechanisms.

The paper analytically reveals that the above may not be the real objects and reasons for this Bill. That the real objectives may be much more sinister than the pious declarations of the statement of objects and reasons. If enacted into law and rigorously enforced, these proposals will radically affect the rights of political parties and the organized civil society to participate in electoral politics and processes. The proposals will deny rights of citizens to contribute financially to the election of candidates of their choice. They will deny candidates the right to raise and use their own funds for legitimate election expenses even where their political parties are unable to do so. They will prohibit or restrict the right of weaker political parties and/or candidates to raise funds for election expenses throughout the election cycle while favouring and protecting the wealthy CCM state party. They will not check the influx of dirty money and/or proceeds of crime from being laundered in electoral processes. They will not prevent the influence of foreign interests in our electoral politics. They are also eminently anti-democratic in granting unchecked and/or arbitrary powers to party leaders to remove candidates on mere suspicion and without due process of the law.

Given the above the paper recommends, the Election Expenses Bill should be opposed and its enactment into law resisted by all those concerned about the health of our electoral politics and our fundamental rights to participate in the election of our government. On the other hand, the paper recommends provisions that have to be incorporated into the bill.

The position paper is available at http://www.chadema.or.tz/nyaraka/Assault_on_Democracy.pdf


With Best wishes regards,

JJ

Monday, January 11, 2010

Watanzania mlio nje ya nchi amkeni (Tanzanians in Diaspora Arise)


Watanzania mlio nje ya nchi amkeni (Tanzanians in Diaspora Arise): Wakati Tanzania Bara (wakati huo ikiitwa Tanganyika) ikiwa katika harakati za kudai uhuru; tunasimuliwa na wazee wetu, vijana wa wakati huo kwamba palikuwa na mchango mkubwa sana wa watanzania waliokwenda kupigana vita nje ya mipaka ya nchi yetu. Hawa waliwaelewa vizuri wakoloni wa wakati huo kuanzia udhaifu wao na hata mbinu za kuwakabili; na kwa ujumla walijifunza kwamba nchi kupata uhuru inawezekana.

Ni hakika kwamba wakati taifa letu linapoendelea kukabiliwa na changamoto za maadui ujinga, umasikini na maradhi huku ukoloni mamboleo ukiweka mirija katika rasilimali na maliasili; tunahitaji mabadiliko ya kweli yenye kuleta uhuru wa kweli.

Katika mazingira haya, kama ilivyokuwa wakati wa kuundoa ukoloni mkongwe, mchango wa watanzania mlio nje ya nchi (Diaspora) ni wa muhimu sana.

Watanzania nyie mnaelewa matunda ya mabadiliko katika kukabiliana na changamoto za ujinga, umasikini na maradhi na mbinu za kidemokrasia za kufikia mabadiliko hayo. Katika kukabiliana na ukoloni mamboleo, watanzania mlio nje ya nchi mnafahamu udhaifu wa mabeberu hivyo mnauwezo wa kusimama kidete kuunganisha nguvu kujenga taifa lenye uwajibikaji na kutoa fursa kwa watanzania wengine walio wengi.

Kwa sasa mchango mkubwa wa watanzania mlio nje ya nchi umekuwa katika kuleta rasilimali kwa wenzenu walio nyumbani (remittances); kwa wachache uwekezaji na wengine kutoa uzoefu wao wa kitaalamu.

Tunapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010; ni wakati wa Diaspora kuchukua hatua kama ilivyokuwa wakati wa kudai uhuru ili kuweke madarakani uongozi wenye dira, uadilifu na uwezo kuifikisha Tanzania katika kipeo cha demokrasia, maendeleo na ustawi wa watu wake. Mnaweza kufanya hivyo kwa wengine kujitokeza kugombea lakini wengi kuunga mkono harakati za mabadiliko kwa njia mbalimbali; kwa kutoa mawazo, kuchangia rasilimali na kupiga kura.

Naotoa ujumbe huu wakati huu Taifa likiwa katika mjadala wa sheria mbili muhimu zenye taathira katika uchaguzi ambazo watanzania mlio nje ya nchi mnapaswa kuzitazama kama kikwazo kwenu na kutoa maoni ya kuzibadili ili ziwe fursa kwenu kuwezesha mabadiliko kupitia uchaguzi.

Mosi; muswada wa marekebisho ya sheria za uchaguzi; huu umekwepa kuweka mabadiliko ya msingi ya kuwezesha uchaguzi kuwa huru na haki ikiwemo kutokuwepo mfumo huru wa usimamizi wa uchaguzi kama wadau walivyohitaji. Lakini kwenu mlio nje ya nchi, muswada huu haujaingiza ombi lenu la muda mrefu la kutaka mruhusiwe kupiga kura. Inashangaza kwamba nchi masikini kama Msumbiji, na nchi iliyotoka vitani karibuni kama Rwanda; raia wake wanawekewa utaratibu wa kupewa haki ya kupiga kura kupitia balozi zao katika nchi mbalimbali, Tanzania inashindwa kuweka kifungu hiki katika marekebisho ya sheria na hivyo kuendelea kunyima haki hii muhimu ya kikatiba kwa watanzania walio nje ya nchi.

Pili; Muswada wa Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010; huu pamoja na kuweka vifungu kuminya wagombea kuchangisha fedha za uchaguzi ndani ya nchi, na kutoa mianya ya wagombea kufutwa bila kupewa haki ya kusikilizwa kabla ya kuhukumiwa. Umelenga pia kudhibiti hata fedha za watanzania walio nje ya nchi kuchangia uchaguzi. Kama sheria hii itapita, watanzania mlio nje ya nchi, hamtaweza kuchangia vyama ama wagombea kwenye kampeni ya uchaguzi hata kama ni michango midogo midogo ya kuwezesha mabadiliko. Katika mazingira haya, uchaguzi wa mwaka 2010; mchango wenu utakuwa ni upi? Maana nyie ni raia halali, lakini hamtakuwa na haki ya kupiga kura wala hamtakuwa na haki hata ya kuchangia wagombea iwe ni fedha au rasilimali nyingine yoyote ile kwa chama ama kwa wagombea.

Amkeni sasa, wekeni msimamo wa kuwezesha taifa kuwa na sheria itayolinda uhuru wa nchi na kuweka uwanja sawa wa ushindani wa kisiasa wakati huo huo ikawawezesha kupata haki zenu za kikatiba muweze kutimiza wajibu wenu wa kidemokrasia katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Ukimaliza kusoma ujumbe huu; tafadhali mtumie na mwenzako au usambaze katika majukwaa mbalimbali ya mijadala. Wako katika demokrasia na maendeleo: John Mnyika, Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa (CHADEMA); tuwasiliane- 0754694553, mnyika@yahoo.com au mnyika@chadema.or.tz.





Sunday, January 10, 2010

Kikwete na serikali acheni vitisho kwa mabalozi kuekelea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010

Katika kipindi cha karibuni kumeibuka kauli za mara kwa mara kutoka serikalini zikilenga kuwaonya na kuwatisha mabalozi na jumuia ya kimataifa katika muktadha wa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Kauli nzito zaidi zikiwa zimetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe Bungeni Dodoma mwezi Julai mwaka 2009 na kauli kama hiyo imerudiwa tena kwa maneno makali na Rais Kikwete mwanzoni wa mwezi huu wa Januari 2010.
Kauli hizi zinapaswa kujadiliwa na kutafakariwa na duru za kidiplomasia na kutolewa kauli mbadala kwa lengo la kudumisha mahusiano mema wakati huo huo kulinda haki kwa kurejea Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mikataba Mbalimbali ya Kimataifa ambayo Tanzania imeridhia.
Kwa nafasi yangu ya Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa wa CHADEMA nimeshangazwa na Hotuba ya Rais Kikwete ya Sherehe kati yake na Mabalozi ya mwaka mpya(New Year Sherry Party) ya tarehe 7 Januari 2010 ambayo badala ya Rais kuwaeleza utekelezaji wa ahadi alizozitoa kwao kwenye hotuba yake ya mwaka katika tukio kama hilo mwaka 2006 mara baada ya kuingia madarakani ametumia nafasi hiyo kutoa kauli zenye kuonyesha vitisho kwa mabalozi.
Ikimbukwe kwamba mara baada tu ya kuingia madarakani, Rais Kikwete alitoa ahadi mahususi kwa mabalozi kwamba serikali yake ingefanya mabadiliko kwa lengo la kuweka uwanja sawa wa kisiasa, kudumisha demokrasia na majadiliano na vyama mbalimbali. Pia alitoa kwao ahadi mahususi za kubadili mazingira ya kiuchumi na kiuwekezaji na kuweka utaratibu wa kunufaisha watanzania walio wengi hususani masikini. Kwa upande wa diplomasia za kikanda na kimataifa, Rais Kikwete alitoa ahadi ya Tanzania kuwa kinara katika utatuzi wa migogoro eneo la maziwa makuu (great lakes) na Umoja wa Mataifa(UN).
Miaka minne imepita lakini Rais Kikwete na Serikali yake hawajatekeleza kikamilifu ahadi hizo kwa watanzania ambazo walizitoa mbele ya mabalozi; badala yake Rais Kikwete anatoa kauli mbadala zenye mwelekeo wa vitisho kwa mabalozi.
Nakubaliana na ukweli kwamba ni muhimu kwa mabalozi kuzingatia Mkataba wa Vienna na kwamba hawapaswi kuwachagulia watanzania mtu au chama tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2010; lakini ni kinyume kabisa kwa mikataba ya kimataifa ambayo Tanzania imeridhia kuwaziba midomo mabalozi wasitoe kauli kwenye masuala yanayogusa demokrasia na maendeleo katika muktadha wa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Rais Kikwete na serikali yake wakumbuke kwamba ni mabalozi hawa hawa na washirika wa kimaendeleo ndio ambao serikali imewaomba fedha na kupewa rasilimali za kutekeleza mipango mbalimbali mathalani mradi wa Deeping Democracy Programme pamoja na Mfumo wa Maandalizi ya Uchaguzi Mkuu 2010(Busket Fund); miradi ambayo yote inaratibiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa(UN) kwa kushirikiana washirika mbalimbali wa kimaendeleo zikiwemo balozi mbalimbali.
Hata hivyo, mpaka sasa miezi michache kuelekea uchaguzi mkuu marekebisho ya msingi hayajafanyika ya kikatiba, kisheria, kitaasisi na kitaratibu kuweka mazingira ya uchaguzi huru na wa kidemokrasia kama ilivyoahidiwa.
Hivyo, natoa mwito kwa jamii ya wanadiplomasia kupuuza vitisho hivyo vya serikali na badala yake kuongeza nguvu zaidi ya kuhoji kuhusu utekelezaji wa ahadi ambazo Rais Kikwete na serikali yake wametoa kwao na kwa watanzania kwa kuwa serikali za nchi zao na taasisi zake zimetoa fedha na msaada wa kiufundi kutekeleza mipango husika. Mabalozi wazingatie kuwa wao ndio watakaohojiwa na walipa kodi wa nchi zao(sio Rais Kikwete wala Membe) kuhusu matumizi ya kodi zao kwa miradi hiyo ambayo kuna mashaka kama malengo yaliyokusudiwa yatatimia kwa wakati uliopangwa.
Pamoja na vitisho vya Waziri Membe na sasa Rais Kikwete ni muhimu kwa mabalozi na jumuia ya wanadiplomasia kuendelea kuurejea Mkataba wa Vienna sanjari na mikataba, itifaki na maazimio mengine ya kimataifa ambayo nchi zetu imeridhia.
Katika dunia ya sasa yenye changamoto mbalimbali ambapo udhaifu kwenye taifa moja una taathira kwa majirani zake na ubinadamu kwa ujumla wake; ni muhimu kwa msingi muhimu wa utetezi wa haki za binadamu unaovuka mipaka na mamlaka ya kinchi kuzingatiwa.
Haiwezekani jumuia ya kidiplomasia ikaendelea kukaa kimya wakati haki za msingi za binadamu zinavunjwa katika chaguzi kwa hofu ya vitisho vya Rais Kikwete ama Waziri Membe ya kwamba wanaingilia mambo ya ndani ya kisiasa ya nchi.
Msingi huu wa kuepusha watu wengine kutoa kauli zenye kuashiria kuingiliwa kwa mamlaka ya ndani ya nchi(sovereignity of the state) ingekuwa na maana kama serikali inayoongozwa na CCM ingekuwa inazingatia kikamilifu katiba ya nchi, sheria za nchi na mikataba ya kimataifa.
Hali ni tofuati, kwani pamoja na ahadi za Rais Kikwete kwa mabalozi mwaka 2006, Taifa limeshuhudia ukiukwaji wa haki za binadamu katika chaguzi za marudio za ubunge Tanzania bara mathalani Kiteto, Tarime, Busanda na Biharamulo ikiwemo vitendo vya viongozi wa CHADEMA kukatwa mapanga wakati wa kampeni za chaguzi husika. Hali hiyo hiyo imejitokeza Tanzania visiwani(Zanzibar) wakati wa uandikishaji wa wapiga kura hususani katika kisiwa cha Pemba.
Ni wazi kwamba vyama vya siasa hususani vya upinzani, mashirika ya kiraia na viongozi mbalimbali wa dini wamekuwa wakitoa kauli kama hizi; hivyo vitisho kwa mabalozi vinaweza kufanya jumuia ya kimataifa ikwepe kutoa kauli za kuunga mkono madai hayo ya haki kwa kuhofia kutafsiriwa kuwa wanaunga mkono 'chama' au 'watu' kwa lengo la kukiondoa chama tawala madarakani.
Ni muhimu kwa watanzania na jamii ya kidiplomasia kwa ujumla kuitafsiri kauli ya sasa ya Rais Kikwete katika muktadha wa matukio yanayotokea ndani Serikali na kwa umma tunaopoelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Rais Kikwete ametoa kauli hiyo siku chache baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuchapisha kwenye gazeti la Serikali la Disemba 11 na kutoa tamko kwa umma Disemba 22 kuhusu mapendekezo ya Miswada miwili ya sheria zinazogusa uchaguzi.
Muswada wa kwanza ni wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Uchaguzi ambao kimsingi haujagusa mabadiliko ya msingi yaliyohitajiwa na vyama vya siasa hususani vya upinzani, wadau wengine na mengine kuuungwa mkono hata na baadhi ya wanadiplomasia na Taasisi zao.
Muswada wa pili ni wa sheria mpya ya Matumizi ya Uchaguzi wa Mwaka 2010, ambao pamoja na malengo mazuri yanayotajwa ya kudhibiti fedha chafu na fedha kutoka nje kuingia katika uchaguzi Tanzania; maudhui ya muswada mpya ni mabaya ambayo kama yakipishwa kama yalivyo yanalenga kunyonga vyama vya upinzani, wagombea wa upinzani, makundi ya kiraia yakiwemo ya kidini na hata baadhi ya wagombea ndani ya chama tawala; jambo ambalo likiachwa lihujumu uchaguzi mkuu 2010 na demokrasia kwa ujumla wake.
Kitendo cha Rais Kikwete kutoa kauli hiyo wakati ambapo tayari baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani ikiwemo wa CHADEMA wametoa kupinga maudhui ya miswada inaweza kutafsiriwa kuwa inalenga kuwatisha mabalozi wakwepe kutoa kauli za kuunga mkono misimamo hiyo kwa kuhofia kutafsiriwa kuwa "mabalozi wanaunga mkono 'chama' ama 'watu".
Hivyo, ni muhimu kwa washirika wa kimaendeleo kupuuza kauli hizo na kuunga mkono vyama, vikundi vya kiraia na viongozi mbalimbali kila wanapotoa kauli zinazoendana na misingi ya Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu(UDHR) na Mikataba ya Kimataifa ambayo nchi yetu imeridhia.
Wakati huo huo; natumia fursa hii kutoa mwito kwa jumuia ya kimataifa kuzirejea ahadi za Rais Kikwete za Mwaka 2006 kuhusu ushiriki wa Tanzania katika diplomasia ya kimataifa katika muktadha wa matukio yaliyojitokeza baadaye. Mathalani, inashangaza kwa Tanzania kuahidi kuwa mstari wa mbele kulinda Amani eneo la Maziwa Makuu (Great Lakes) na kutekeleza maazimio ya Umoja wa Mataifa(UN). Lakini miaka minne baadaye, serikali ya Rais Kikwete huyo huyo inatuhumiwa kwenye ripoti ambayo kwa taarifa tulizonazo tayari imeshawasilishwa kwenye Kamati ya Vikwazo ya Baraza la Usalama wa Umoja wa Mataifa(UN) kwamba baadhi ya Raia wake wakiwemo Vigogo wa Serikali na taasisi zake wameshiriki kwa namna moja au nyingine katika usafirishaji wa Silaha kwenda maeneo ya Vita ndani ya ukanda wa maziwa makuu na utoroshaji wa madini haramu toka maeneo hayo. Aidha Tanzania kama nchi imetuhumiwa pia kwa serikali kushindwa kusimamia kikamilifu maazimio ya UN ambayo Serikali yetu ilikubaliana nayo ya kuzuia madini na silaha haramu visipite katika ardhi ya nchi yetu bila kuchukua hatua.
Kutokana na hali hiyo, nachukua fursa kutoa rai kwa Mabalozi wa nchi za Maziwa Makuu na hata kundi la marafiki (Group of Friends) kutoa kauli kuhusu tuhuma hizi; kauli ambayo inapaswa kutolewa pia na Mkuu wa Mabalozi Tanzania (Dean Of Diplomatic Corps)-Balozi Juma Mpango (ambaye pia ni Balozi wa DRC nchini Tanzania).
Imetolewa na:
John Mnyika
Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa(CHADEMA)