Friday, May 28, 2010

Tuwekeze kwenye oganizesheni ya michezo


KUTOKA MAKTABA: Nikitoa zawadi kwa Mburahati Queens kwa kuchukua ubingwa wa soka la wanawake. Katika hotuba yangu fupi siku hiyo pamoja na mambo mingine nilitoa mwito kwa mkazo kuwekwa katika kuwekeza katika oganizesheni ya michezo kuanzia ngazi za chini. Hii ni pamoja na kulinda maeneo ya wazi na kujenga viwanja vya michezo, kuwekeza katika mafunzo na kuwezesha michezo kujiendesha kibiashara

Monday, May 17, 2010

Kikwete Abanwa

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemtaka Rais Jakaya Kikwete akanushe kauli ya kubariki rushwa katika uchaguzi, vinginevyo chama hicho kitamuumbua.
Mkurugenzi wa Vijana wa CHADEMA, John Mnyika, alitoa kauli hiyo jana alipokuwa anachukua fomu ya kugombea ubunge wa Ubungo; akasema kitendo cha Rais Kikwete kutetea rushwa kwa kisingizio cha takrima, ni ishara kuwa hakuwa na dhamira ya kweli ya kudhibiti matumizi makubwa ya fedha katika uchaguzi.

Mnyika alisema kuwa Rais Kikwete asipokanusha kauli yake hiyo, aliyoitoa Ijumaa wiki iliyopita mbele ya viongozi wa dini, atakuwa amelithibitishia taifa kuwa haheshimu utawala wa sheria.

Rais Kikwete aliwaambia viongozi wa dini kuwa takrima haikwepeki katika uchaguzi, licha ya uamuzi wa mahakama kuu iliyofuta vifungu vya sheria vilivyokuwa vinatetea takrima katika hukumu yake ya Aprili 24, 2006.

Akihutubia wananchi waliojitokeza kushuhudia akichukua fomu ya kugombea ubunge jana, Mnyika, alisema: “Wananchi wa Ubungo na Watanzania kwa ujumla puuzeni kauli za wanasiasa walioshindwa kuongoza nchi vizuri na kutumbukiza nchi katika katika mfumuko wa bei na kuzorotesha huduma za jamii huku wakiwaacha mafisadi wakivuna mamilioni ya fedha za umma.”

Alisema kauli ya Rais Kikwete ni kinyume cha sheria maana inachochea rushwa kwenye uchaguzi.

Mnyika alichukua fomu za kuwania ubunge katika ofisi za chama hicho jimbo la Ubungo na kukabidhiwa fomu hizo na Katibu wa CHADEMA Jimbo la Ubungo, Nasor Balozi.

Aidha, alisema amechukua fomu ya CHADEMA kwa kuwa anaamini ni chama mbadala na tumaini jimpya la Watanzania.

“Nachukua fomu kugombea ubunge kwa lengo la kushiriki katika kuleta mabadiliko ya kweli kwenye jimbo letu na taifa kwa ujumla kupitia siasa safi na uongozi.

“Nachukua fomu ya kugombea kwa lengo la kuchangia katika maendeleo ya nchi kwa kuondoa hodhi na nguvu ya chama kimoja bungeni na kwenye baraza la madiwani ambayo imesababisha kukosekana kwa uwajibikaji na hivyo wananchi kubaki na kero mbalimbali.

“Mimi naamini mbunge ni mwakilishi na mtumishi wa wananchi wenzake, hivyo pamoja na kuwa ninayo maadili na maono ya nini nakusudia kufanya natambua umuhimu wa kusikiliza. Sikubaliani na wanasiasa wanaopenda kusikilizwa badala ya kusikiliza, hivyo kabla sijatoa ilani yangu ya uchaguzi na ahadi zangu kwa wapigakura na wananchi kwa ujumla ningependa kusikiliza kwanza kutoka kwao,” alisema Mnyika.

Pamoja na hayo, Mnyika aliwahimiza watu wengine kujitokeza kugombea udiwani jimbo la Ubungo, ili halmashauri ya Kinondoni iwe na madiwani wa vyama mchanganyiko, kwani sasa hivi Dar es Salaam nzima inaongozwa na chama kimoja, jambo linaloifanya idorore.

Chanzo: Betty Kagonga- Tanzania Daima: http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=15748

Saturday, May 15, 2010

`Pinda, toa tamko kuhusu mgawo wa kata, tarafa`

Waziri Mkuu,Mizengo Pinda, ametakiwa kutoa tamko ikiwa ofisi yake kupitia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) imeamua kuzigawa kata na tarafa za wilaya ya Kinondoni jijini Dares Salaam.

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Mkoa wa Kinondoni katika kanda maalum ya Dar es Salaam, John Mnyika, alisema hayo jana katika taarifa yake kwa Nipashe.

“Ni muhimu kufanya hivyo sasa ili kama kuna kata mpya zinaundwa vyama vya siasa viweze kujiandaa kwa uchaguzi na wagombea waweze kutangaza nia,” alisema.

Mnyika alisema inapaswa kuzingatiwa kwamba kwa mujibu wa sheria, wakati mamlaka ya kugawa majimbo yako chini ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), mgawanyo wa kata uko Tamisemi.

“Tume imeshatangaza mgawo wa majimbo lakini Tamisemi haijatangaza hadharani kama kuna kata imezigawa au la kwenye halmashauri ya Kinondoni,” alisema.

Kwa mujibu wa Mnyika, Oktoba 2008 baadhi ya wilaya ikiwemo Kinondoni, ziliwasilisha mapendekezo ya mgawo wa kata na tarafa kwa Tamisemi.

Alisema Mei na Desemba mwaka jana, halmashauri ya Kinondoni ilipitisha tena mapendekezo hayo yaliyopitishwa na vikao vya mkoa Januari mwaka huu.

Mnyika alisema kwa mujibu wa muundo wa sasa wa serikali, pamoja na kuwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Celina Kombani, mwenye dhamana ya kutoa tamko hilo ni Waziri Mkuu akiwa mwenye dhamana.

Alidai kuwa kwa upande wa Kinondoni, mapendekezo yaliyopitishwa na Baraza la Madiwani na kuwasilishwa Tamisemi miezi kadhaa iliyopita, yanataka kuundwa kata mpya saba na tarafa kuongezwa kutoka nne mpaka saba.

“Haya ndiyo madhara ya sheria kutoa mamlaka kwa kiongozi wa serikali ambaye chama chake na yeye mwenyewe ni wagombea kupanga taratibu nyeti zenye athari za uchaguzi kama mipaka ya kata,” alisema.

Mnyika alisema ukimya wa Tamisemi kuhusu suala hilo unaweza kuibua hisia za kuwepo hujuma zinazopangwa kama ilivyokuwa katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka jana, na kwamba suluhu pekee ni kutolewa kwa tamko la Waziri Mkuu.

Jitihada za kumpata Kombani kupitia simu yake ya mkononi jana, ili atoe ufafanuzi kuhusu suala hilo, zilishindikana kutokana na kuita pasipo kupokewa.

CHANZO: NIPASHE(Tarehe 10 Mei 2010)

Thursday, May 13, 2010

Maadili ya Uchaguzi wa Urais, Ubunge na Udiwani

Tutafakari kuhusu maadili ya Uchaguzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani wa mwaka 2010. Izingatiwe kuwa Kanuni na taratibu zinazosimamia kampeni za uchaguzi Tanzania zinafafanuliwa katika sehemu ya VI ya Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985 kifungu cha 51 (1-6). Hata hivyo pamoja na uwepo wa sheria hiyo kuna mapungufu kadhaa ambayo yanapaswa kujadiliwa.

Ipo changamoto ya ukiukwaji wa maadili ya uchaguzi wakati wa kampeni. Kabla ya kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 kuanza maadili ya uchaguzi yalisainiwa na vyama mbalimbali vya siasa (isipokuwa DP na NCCR-Mageuzi), tume ya uchaguzi na serikali. Kampeni za uchaguzi ziligubikwa na matatizo kadhaa ikiwemo wagombea kutumia lugha za asili katika baadhi ya maeneo, ratiba za mikutano kutofuatwa katika baadhi ya maeneo, ufanyaji wa kampeni hasi (negative campaigns) nk. Mifano ya matukio ya namna hii ni mingi, mathalani katika tukio moja wafuasi wa CCM walipita na gari wakitangaza kwamba mgombea Urais na Ubunge wa CHADEMA wote wamejitoa na kujiunga na chama chao.(Kisa hiki kimesimuliwa kwa kina katika ripoti ya uchaguzi ya TEMCO).

Pia mikutano ya kampeni hususani katika ngazi za ubunge na udiwani ilitawaliwa na siasa za kushambulia haiba ikiwemo kwa njia ya matusi badala ya sera. Matukio mengine ya ukiukwaji wa maadili ambayo yameripotiwa katika baadhi ya maeneo ni pamoja na utoaji wa taarifa za upotoshaji, uharibifu wa alama za wagombea/vyama, udini/ukabila (katika baadhi ya maeneo) na vurugu (hususani maeneo yaliyokuwa na upinzani mkali).

Katika kipindi cha 2006 mpaka 2009, hali haikubadilika katika chaguzi za marudio hususani wa kampeni za ubunge. Mathalani, uchaguzi wa Kiteto (2007 ulihusisha Mbunge wa CCM, John Komba; kuvamia Mkutano wa CHADEMA, polisi walimshusha jukwaani baada ya shinikizo. Hata hivyo, hakuna hatua za msingi zilizochukuliwa hata baada ya CHADEMA kufungua jalada polisi la kosa la jinai. Pia katika uchaguzi huo, viongozi wa CHADEMA walipigwa na kujeruhiwa na polisi kwa kushirikiana na makada wa CCM. Katika uchaguzi wa Tarime (2008), kampeni zilihusisha baadhi ya Vyama kuhutubia jukwaani na kusambaza nyaraka zikiitaja CHADEMA na viongozi wake kama ‘genge la wauaji’ waliomuua Chacha Wangwe (Mungu Amlaze Mahali Pema). Hata hivyo, hakuna hatua zozote madhubuti zilizochukuliwa na Tume ya Uchaguzi ama Vyombo vya Dola hata baada ya kiongozi mmojawapo wa CHADEMA kushtaki suala hilo polisi na jalada la uchunguzi kufunguliwa. Pia kampeni zilihusisha baadhi ya viongozi wa vya upinzani kushambuliwa kwa mawe na baadhi ya wanachama wa CHADEMA kukatwa na mapanga. Kadhalika, jeshi la polisi liliwavamia, kuwapiga na kuwakamata viongozi wa CHADEMA pamoja na mgombea ubunge na mgombea udiwani. Matuko ya namna hiyo viongozi na makada wa CHADEMA kukatwa mapanga katika kampeni za uchaguzi wa marudio za ubunge katika majimbo ya Busanda na Biharamulo mwaka 2009; hakuna hatua za kisheria zilizochukuliwa mpaka sasa pamoja na majalada ya uchunguzi wa jinai kufunguliwa polisi.

Fungamano lililokuwepo wakati wa chama kimoja kati ya chama na dola limeendelea na linaendelea. Hali hii ya kuwa na ‘chama dola’ imekuwa ikitumika kuhujumu wapinzani nyakati za uchaguzi. Katika mchakato mzima wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 palikuwa na fungamano la mara kwa mara kati ya chama kwa upande mmoja na serikali na dola kwa upande mwingine. Yalitolewa maelekezo na mengine ya wazi kabisa kutoka kwa viongozi wa CCM akiwemo Mwenyekiti (wakati huo akiwa pia Rais wa nchi) kwa viongozi wa serikali kwamba watumie nguvu zote ikiwemo za dola kuhakikisha upinzani haushindi katika maeneo yao. Hivyo viongozi wa serikali hususani wakuu wa mikoa, wilaya na watendaji wa kata walikuwa mstari wa mbele kwenye kampeni za chama tawala na mahali pengine kuvitumia hata vyombo vya dola. Hii ni changamoto ambayo marekebisho ya kisheria yanayokusudiwa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 yalipaswa kuishughulikia lakini hayajafanya hivyo, na tayari kuna wimbi la matumizi haya mabaya ya madaraka kuelekea uchaguzi mkuu.

Viongozi wa serikali waliokuwa na nafasi zao mathalani mawaziri waliendelea kuzitumikia nafasi hizo sanjari na kupigia kampeni chama tawala. Miradi mbalimbali ya maendeleo ilielekezwa kuzinduliwa ama kufunguliwa kipindi cha kampeni. Taasisi za umma zilitumika kupiga kampeni mathalani matangazo ya pongezi ya kulipia yalitolewa na taasisi hizi kwa wagombea wa CCM mara baada ya kuteuliwa ndani ya chama. Vyombo vya dola yakiwemo majeshi vilitumika kukandamiza upinzani hasa Zanzibar na maeneo yaliyokuwa na upinzani mkubwa bara. Hali haikuwa tofauti katika kipindi cha kati ya mwaka 2006 mpaka 2009. Hii ni changamoto ambazo marekebisho ya Sheria ya Uchaguzi yaliyofanyika mwaka 2010 hayakuzingatia kwa CCM kutumia uwingi na hodhi(monopoly) bungeni kuyakataa. Tume ya Uchaguzi inakapokaa tena mwaka huu na vyama vya siasa kuandaa Maadili ya Uchaguzi kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani wa mwaka 2010.

Tuesday, May 11, 2010

Ndoa sio fasheni

Ndoa si msukumo rika, wala kufuata mila,
Ndoa ni kukubalika, bila kufanyiwa hila,
Ndoa si kuhangaika, ili kulipa fadhila,
Ndoa ikikamilika, hutayapata madhila.

Ndoa si kuwa na gari, wala kupanda daraja,
Ndoa isiwe kamari, bali jambo la faraja,
Ndoa isiwe kwa amri, ila ni kuwa wamoja,
Ndoa haitokani na umri, bali nia ya pamoja.

Ndoa sio maigizo, haimei ka uyoga,
Ndoa isiwe likizo, ya kuanza kujikoga,
Ndoa sio bambikizo, hivyo isije kwa woga,
Ndoa ikiwa agizo, kwamwe haiwezi noga.

Ndoa suala la hiyari, si kupigiwa zumari,
Ndoa si kulipa mahari, bali ni kuwa tayari,
Ndoa inakuwa shwari, ifungwapo bila shari,
Ndoa maisha ya heri, yasiyotaka kwaheri

(JJ-8 Mei, 2010; Dar es Salaam, Tunu kwa makapera)

Tuesday, May 4, 2010

Rais Kikwete na Wafanyakazi

Madai ya wafanyakazi kutaka nyongeza ya mshahara yalianza muda mrefu, kiwango hicho ambazo Rais Kikwete amekitaja leo kwa dhihaka kilianza kuzungumziwa toka mwaka 2007; ni hatua gani serikali yake ilichukua toka wakati huo mpaka wakati huu?
Hotuba ya Rais imenifanya nikumbuke makala hii ambayo niliindika mwaka 2007: http://www.chadema.or.tz/makala/makala.php?id=51

Katika makala hiyo nilinukuu kipande cha hotuba ya Nyerere ambacho ni muhimu nikakirejea hivi sasa katika muktadha wa Hotuba ya Kikwete.
Mwalimu Nyerere yeye alikabiliana moja kwa moja na wahuhusika na kuwaeleza: “Mna haki mnapozungumzia mishahara…..mishahara yetu ipo juu sana. Mnataka niipunguze? (makofi)…..mnataka nianzie na mshahara wangu? Ndio, naanza kuukata wa kwangu (vilio vya ‘hapana’). Nitapunguuza hii mishahara katika nchi hii. Wangu naukata kwa asilimia ishirini kuanzia sasa…..hii mishahara hii. Hii mishahara ndio inajenga huu mtazamo kwa wasomi, wote kabisa. Mimi na wewe. Tuko katika tabaka la wanyonyaji. Niko katika tabaka lenu. Ambapo nafikiri paundi mia tatu na themanini kwa mwaka (kiwango cha chini cha mshahara uliokuwa ukilipwa katika Jeshi la Kujenga Taifa) ni kambi ya gereza, ni kufanyishwa kazi kwa shuruti. Tuko katika tabaka la juu la wanyonyaji. Je hiki ndicho ambacho taifa letu kilipigania? Je hiki ndicho tulichokihangaikia? Ili tuendeleze tabaka la juu la wanyonyaji?....mko sawa, mishahara ipo juu sana. Kila mtu katika nchi hii anahitaji paundi ya ziada. Kila mtu isipokuwa mkulima masikini. Anawezaje kutaka? Haijui lugha…je ni nchi ya namna gani tunajenga?” (tafsiri yangu toka nukuu ya hotuba ya kingereza ya Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliitoa papo kwa papo akizungumza na wanafunzi wa Chuo cha Dar es Salaam baada ya maandamano ya wanafunzi Oktoba mwaka 1966)
Nyerere wakati huo alikwenda kuihutubia hadhira muafaka kwa suala alilolizungumzia, lakini kwa Kikwete yeye alikwenda kuwahutubia wazee na kuhusu ‘wafanyakazi’; je, alikuwa anapeleka mashtaka au alikuwa anatafuta kupigiwa makofi na hadhira isiyohusika ama ni ishara ya hofu ya kuogopa kukabiliana na wafanyakazi ana kwa ana?
Kuhusu Hotuba la Rais kusema kwamba mgomo ni batili anapewa taarifa nusu nusu au anapotoshwa ama ameamua kuupotosha umma. Ni vizuri serikali ikarejea na kukumbuka kuwa kusudio la mgomo lilitolewa siku nyingi nyuma kama sheria inavyohitaji; na wafanyakazi walieleza wazi kwamba walirejea kwenye majadiliano kwa maombi ya umma huku kusudio lao likiwepo pale pale. Hivyo, ni muhimu serikali ikaepusha mgomo kwa kushughulikia madai ya msingi ya wafanyakazi ambayo ni nyongeza ya mshahara hususani kima cha chini, punguzo la makato ya kodi na uboreshaji wa pensheni wakati wa kustaafu. Nilisoma tangazo la baraza husika ambalo limeshapwa na serikali katika magazeti mbalimbali hivi karibuni lilieleza bayana kwamba katika suala la kiwango cha kima cha chini 'wamekubaliana kutokukubaliana'; hivyo nimeshangazwa na kauli ya Rais Kikwete ya kwamba majadiliano yalifikia makubaliano kuhusu kiwango.

Tafsiri ya matukio haya ni ama kuna ufa mkali ndani ya serikali ama serikali imekerwa na kutoalikwa Mei Mosi huku ikijaribu kutumia kila mbinu kuficha aibu ya mgomo wa wafanyakazi wakati nchi ikiwa mwenyeji wa World Economic Forum-Africa(mbinu waliyoitumia kupanda miti mikubwa ya haraka haraka along Sam Nujoma Road).

Lakini naamini Rais anatambua kwamba watu wachache wanaweza kudanganywa kwa muda mchache, lakini sio watu watu wakati wote. Jaribio la hotuba ya Rais kuwatweza viongozi wafanyakazi linaweza likaishia kuwakweza zaidi, jaribio la kuwachangonanisha wafanyakazi kuwa wanataka mishahara mikubwa wakati serikali inahitaji fedha za kutoa huduma kwa jamii ili wananchi wawajie juu wafanyakazi kuwa wanajipendelea nalo limeelekea kushindwa. Jaribu la kuwachonganisha wafanyakazi kwa wafanyakazi, wafanyabiashara kwa wafanyakazi( kwa kutumia mifano ya mwenye baa na mifano ya house girl) nalo limeelekea kupuuzwa. Taasisi ya Urais sio idara ya propaganda za kutumia kejeli ama uchonganishi; Rais alipaswa kujenga hoja, kutoa matumaini na kutoa uongozi mbadala.

Hasira alizozionyesha kwa TUCTA ndio amekuwa amezionyesha kwa kiwango hicho hicho kwa mafisadi, na nguvu hizo hizo za kuzima hoja angekuwa amezitumia kwenye kutoa uongozi bora na kusimamia vizuri rasilimali za taifa mapato ya serikali yangewezesha kuwa na nyongeza ya mishahara kwa wafanyakazi na ukuaji wa uchumi ungewezesha hata kukuka kwa kipato katika sekta binafsi huku mfumuko wa bei ungedhibitiwa kwa kiwango cha kuridhisha. Wakati wafanyakazi wanaendelea kutozwa kodi kubwa(dai ambalo Rais hakulizungumzia), ni serikali yake hii ambayo iko mstari wa mbele kutoa katika mazingira ya utata misamaha mikubwa ya kodi.

Kama divide and rule hii ikiindelea kwa kiwango cha wafanyakazi kushindwa kushikamana, bado kila mmoja anayo fursa ya kugoma kumpa kura (kwanza ameshatangaza mwenyewe kuwa kura hazitaki). Upo msemo kwamba madaraka hulevya, na madaraka zaidi hulevya zaidi; unapokuwa na taifa lenye hodhi (monopoly) ya chama kimoja katika vyombo vya maamuzi; si ajabu kupata kauli za namna hii. Hii ndio athari ya kura zilizoitwa za mafiga matatu; lakini ipo fursa bado ya kubadili mfumo wa utawala ili tuwe na uwajibikaji wa kutosha si kwenye sererikali tu, hata kwenye taasisi zingine ikiwemo vyama vya wafanyakazi vyenyewe.

Kwa walio nje ya ajira zenye malipo duni suala hili wanaweza wakaona haliwahusu, lakini ukweli ni kuwa kuna uhusiano mkubwa katika ya ubovu wa huduma tunazozipata kwenye sekta mbalimbali na hali duni katika sekta hizo; hili ni bomu la wakati. Wafanyakazi wa Tanzania wamekuwa wawafanyi migomo rasmi kama nchi nyingine duniani, lakini aina ya mgomo unaoendelea chini kwa chini nchini ni mbaya zaidi kwa mustakabali wa nchi yetu. Tanzania kuna mgomo wa kutokuwajibika, katika hususani katika utumishi wa umma; wapo wanaokwenda kazini mwaka mzima lakini wanafanya kazi masaa machache au siku chache; muda mwingine kwenye warsha/semina kufidia kipato duni wanachopata ama muda mwingi zaidi kwenye shughuli zao binafsi. Mfano; walimu wenye wanaofundisha masomo ya ziada (tuition) ama kufanya biashara za visheti kwa wanafunzi shuleni; ama daktari anayetumia muda mwingi zaidi kwenye shughuli binafsi kuliko ndani ya hospitali ya umma, sasa 'consultancy' ndani ya serikali kwa serikali ndio zimekuwa utamaduni wa kawaida.

Rais atangaze mshahara wake hadharani na atueleze baraza lake la mawaziri limeshughulikiaje madai makuu matatu ya wafanyakazi toka aingine madarakani mwaka 2005 badala ya kukimbilia kuwapa jina baya viongozi wa wafanyakazi kuwa 'wanatumiwa'. Kama kweli wanatumiwa atueleze wanatumiwa na nani kwa kwanini? Na yeye na serikali yake waulizwe 'wanatumiwa na nani' au wanamtumikia nani?