Monday, July 26, 2010

Mnyika apitishwa kwa 100% Ubungo

MGOMBEA wa Ubunge kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. John Mnyika amepitishwa na na chama chake kugombea jimbo hilo kwa asilima 100.

Bw. Mnyika alipitishwa na wajumbe wa Mkutano Mkuu wa jimbo hilo baada ya wajumbe wote 62 kumpa kura ya ndiyo.

Wajumnbe waliohudhuria katika mkutano huo ni Wenyeviti na makatibu wote wa jimbo hilo, wageni waalikwa 60 na wawakilishi wa vyuo vikuu walioko Ubungo na wawakilishi wa matawi ya CHADEMA katika jimbo hilo.



Wakati huo huo, Baraza la Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA) limemtaja, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willibrod Slaa kuwa shujaa baada ya kukubalia maombi ya Kamati Kuu ya kugombea urais wakati baado alikuwa anahitajika katika jimbo lake.

Akizungumza katika mkutano wa wakilishi wa vyuo vikuu Mweyekiti wa Kamati ya baraza hilo, Bw. John Mnyika alisema kitendo alichofanya Dkt. Slaa cha kuachia jimbo ambalo alikuwa na uhakika wa kushinda katika Uchaguzi Mkuu ni la kishujaa.

"Tunakutana leo kwa kuwa tendo alilofanya Mtanzania mwenzetu, Dkt. Slaa kukubali kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni la kishujaa," alisema Bw. Mnyika

Alisema Dkt. Slaa ni sawa mashujaa waliokubali kupoteza maisha yao na kulilinda na kuliteta taifa na hivyo ni shujaa wa demokarsia na maendeleo.

Alisema mashujaa wa namna ya Dkt. Slaa hawafii kwa kuwa fikra zao zitakumbukwa milele uamuzi wa huo utandika historia mpya kwa taifa ni sehemu ya kutekeleza kwa vitendo misingi ya CHADEMA

Alisema Bendera ya chama hicho ni rangi ya nyekundu, nyeupe bluu, bahari na nyeusi uwepo kwa rangi nyekundu unatoka na kuthamini mashujaa wa nchi walipigana vita ili kulikomboa taifa hili.

Alisema maadhimisho yanayofanywa na serikali Julai 25 kila mwaka kuwakumbuka mashujaa ni unafiki kwa kuwa hufanywa kwa maneno na si wa kivitendo

Alisema tunu ya taifa hili ziko kwenye ngao ya taifa ambayo ni Uhuru na Umoja lakini uhuru umetoweka na nchi imekuwa tegemezi kwa kuwa sehemu kubwa ya rasilimli zake zimeuzwa kwa bei ya kutupwa kwa wageni na sehenu kubwa ya Watanzania hawafaidi nayo

Alisema umoja umetelemshwa kutokana na kupuuzwa utawala wa sheria kumea kwa ubaguzi na kupanuka kwa matabaka katika jimii kwenye sekta mbalimbali za afya, elimu na hata mifumo ya haki hali ambayo ni tishio la ustawi na usalama wa nchi.

Alisema Dkt. Slaa ametimiza wajibu huo kwa kusimamia ukweli, uwazi, uadilifu na amani kama rangi nyeupe katika bendera ya CHADEMA inayowakilishwa hususani kupitia ngazi ya ubungeni katika jamii na jimboni kwake karatu

Bw Mnyika alisema umefika wakati wa Dkt. Slaa kuinuliwa na kupewa wajibu mkuu zaidi katika nchi wa ili kuunda serikali na kusimamia utekelezaji ilikurudisha nchi kwa wananchi.

Chanzo: Gazeti la Majira 26/07/2010

Mnyika apita kwa kishindo ubungo

HATIMAYE Mkurugenzi wa Mambo ya Nchi za Nje wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), John Mnyika, amepitishwa kuwania ubunge wa Jimbo la Ubungo kwa kupata ushindi wa asilimia mia moja kwenye kura za maoni.

Kwa mujibu wa matokeo ya kura za maoni za CHADEMA katika Jimbo la Ubungo yaliyotolewa na Nassor Balozi, Mnyika aliyekuwa mgombea pekee katika uchaguzi huo alipata kura za ndiyo 62 zilizopigwa na wajumbe wote 62 waliohudhuria mkutano mkuu wa jimbo hilo.

“Mkutano mkuu umepiga kura za ndiyo na hapana na kati ya wajumbe 62 wote wamepiga ndiyo, hakuna hapana, hakuna iliyoharibika. Hivyo John Mnyika amepitishwa na kura hizo za uteuzi kwa asilimia 100,” alisema Balozi.

Wajumbe wa mkutano huo walikuwa ni wenyeviti na makatibu wote wa CHADEMA Jimbo la Ubungo.

Aidha, mkutano huo pia ulishirikisha wageni waalikwa 60 ambao ni wawakilishi wa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu vilivyomo ndani ya Jimbo la Ubungo pamoja na wawakilishi wa matawi ya chama hicho Jimbo la Ubungo.

Akizungumza baada ya matokeo hayo, Mnyika alisema alitarajiwa kupitishwa kugombea ubunge na mkutano huo lakini hakutegemea kupitishwa kwa asilimia 100 kama ilivyotokea na kuielezea hali hiyo kuwa ni kielelezo cha CHADEMA kuwa moja zaidi ndani ya jimbo hilo.

“Kwa matokeo hayo wamenipa changamoto kubwa, lakini pia ni changamoto kwao katika kuhakikisha wanaitekeleza imani yao kwangu kwa vitendo kwa kushiriki kikamilifu katika harakati zote za kutupatia ushindi,” alisema Mnyika.

Mnyika anayewania ubunge wa jimbo hilo kwa mara ya pili baada ya kudaiwa kushindwa kwa mizengwe katika Uchaguzi Mkuu uliopita, alisema vipaumbele vyake ni kupigania ajira na maslahi ya wafanyakazi, miundombinu bora ya maji, barabara na makazi, kuchochea uwajibikaji wa watendaji wa serikali, idara na mamlaka zake pamoja na kufanikisha upatikanaji wa huduma bora za afya ndani ya jimbo hilo.

Chanzo: Gazeti la Tanzania Daima-26/07/2010

Saturday, July 24, 2010

HOTUBA: Ufunguzi wa Mkutano wa BAVICHA na Wanavyuo

HOTUBA YA MWENYEKITI WA KAMATI YA TAIFA YA BARAZA LA VIJANA WA CHADEMA (BAVICHA) JOHN MNYIKA AKIFUNGUA MKUTANO WA WAWAKILISHI WA WANAVYUO VIKUU VYA MKOA WA DAR ES SALAAM KATIKA VIWANJA VYA MAKAO MAKUU YA CHAMA KINONDONI JUMAPILI TAREHE 25 JULAI 2010

Vijana wenzangu wanavyuo;

Wageni waalikwa na wanahabari;

Ni mara yangu ya kwanza leo kuhutubia vijana wenzangu toka Kamati Kuu ya chama katika kikao chake cha tarehe 25 mpaka 26 Aprili 2010 iliponiteua kuongoza Kamati ya taifa ya BAVICHA katika kipindi hiki mpaka uchaguzi wa vijana utapofanyika baada ya uchaguzi mkuu.

Nimeupokea wajibu huu kwa moyo mkunjufu kwa kuwa umenikumbusha kipindi nilichokuwa Mkurugenzi wa Vijana na hakika ni jukumu muhimu kwa chama hiki cha kizazi kipya wakati huu ambapo ubunifu, uwingi na uthubutu wa vijana unahitajika kuwezesha mabadiliko katika taifa letu.

Awali ya yote naomba tusimame kwa dakika moja ya ukimya kuwakumbuka mashujaa waliomwaga damu yao na kutangulia mbele ya haki wakiwa katika wajibu wa kulinda na kutetea ardhi ya nchi yetu na watu wake.

Nashukuru tumekutana leo tarehe 25 Julai ambayo ni siku ya mashujaa nchini kujadili matendo ya kishujaa yaliyofanywa na yanayokusudiwa kufanywa katika taifa letu.
Tunakutana leo kwa sababu ya tendo la kishujaa la mtanzania mwenzetu Dr Wilbroad Slaa kukubali ombi la kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tendo hili la kishujaa la kuachia jimbo la uchaguzi ambalo alikuwa ana uhakika wa kuletetea na badala yake kugombea nafasi ya urais ambayo baadhi ya watu wametafsiri kama ni ‘kuuawa ama kujiua’ kisiasa.

Kama vile mashujaa walivyokubali kupoteza maisha yao kulilinda na kulitetea taifa, ndivyo ambayo Dr Slaa ni shujaa wa demokrasia na maendeleo kwa kufanya tendo ambalo linaweza kutafsiriwa kuwa ni kutishia maisha yake ya kisiasa hususani katika bunge kwa kuamua kugombea nafasi ya Urais kutokana na kuweka mbele maslahi ya taifa kwanza.
Mashujaa wa aina hii huwa hawafi kwa kuwa fikra zao hukumbukwa milele, uamuzi wa Dr Slaa kujitokeza kugombea wakati huu utaandika historia mpya kwa taifa la Tanzania. Uamuzi huu wa kishujaa ni sehemu ya kutekeleza kwa vitendo misingi ya CHADEMA ambayo inaweza kueleweka vizuri zaidi kupitia bendera anayoipeperusha.

Bendera ya CHADEMA ina rangi nne; nyekundu, nyeupe, bluu bahari na nyeusi. CHADEMA ikiwa ni chama kinachothamini mashujaa wa nchi hii imeweka rangi nyekundu katika bendera yake ambaye imefafanuliwa vizuri katika katiba na kanuni za chama kwamba ni ishara uzalendo na upendo kwa taifa.

Leo tarehe 25 Julai wakati sisi tukiwa hapa kwenye mkutano huu viongozi wa kiserikali wako kwenye viwanja vya mnazi mmoja wakifanya maadhimisho ya kinafiki ya kuwakumbuka mashujaa kwa maneno huku kwa vitendo wakiwa wamewasahau na kusahau misingi waliyoisimamia.

Tunu za taifa hili zilizoko kwenye ngao ya taifa ni “Uhuru na Umoja”, hata hivyo tunavyozungumza hivi sasa uhuru huu umetoweka kwa nchi kuwa tegemezi na rasilimali kwa sehemu kubwa kuuzwa kwa bei ya kutupwa kwa wageni huku sehemu kubwa ya watanzania ikiwa hainufaiki na matunda ya uhuru kutokana na kufungwa na kongwa za umasikini, ujinga, maradhi na ufisadi. Tanzania imegeuzwa chanzo cha malighafi ghafi, soko la bidhaa duni toka nje chini ya soko holela na watawala kukiunga misingi ya uongozi.

Kwa upande mwingine misingi ya umoja inazidi kutetereshwa kutokana na kupuuzwa kwa utawala wa sheria, kumea kwa ubaguzi na kupanuka kwa matabaka katika jamii kwenye sekta mbalimbali iwe ni afya, elimu na hata mifumo ya haki hali ambayo ni tishio kwa ustawi na usalama wa nchi yetu. Hali hii inahitaji mashujaa kujitokeza kutanguliza mbele uzalendo na upendo kwa taifa ili kulikomboa taifa kwa kuleta mabadiliko ya kweli ya uongozi na mfumo mzima wa utawala.

Dr Slaa ametimiza wajibu huo kwa kusimamia ukweli, uwazi, uadilifu na amani kama rangi nyeupe katika bendera ya CHADEMA inavyowakilisha hususani kupitia kazi yake bungeni, katika jamii na jimboni Karatu katika kipindi cha utumishi wake. Hata hivyo baadhi ya mambo hayajaweza kutekelezwa na serikali iliyopo madarakani kutokana na dola chini ya CCM kutekwa na mafisadi na kuwa na mfumo legelege wa uongozi uliofilisika kidira na kimaadili.

Umefika wakati sasa wa Shujaa huyu kuinuliwa kupewa wajibu mkuu zaidi katika nchi yetu wa kuwa Rais wa Tanzania aweze kuunda serikali na kusimamia utekelezaji ili kurudisha nchi kwa wananchi. Ndio maana tunaunga mkono uamuzi wa Kamati kuu ya chama iliyoketi tarehe 20 Julai kumwomba kugombea urais ili ajaze fomu na kupitishwa na Mkutano Mkuu wa chama tarehe 20 Agosti 2010.

Na kabla ya kuanza kuutekeleza wajibu huo akiwa ikulu, uchaguzi ambao kampeni zake zinaanza rasmi tarehe 20 Agosti mpaka 30 Oktoba kabla ya kupiga kura tarehe 31 Oktoba ulipaswa kuwa na mgombea wa uwezo wa Dr Slaa ili uwe sehemu ya mchakato wa kuiwajibisha serikali wakati wote wa kampeni. Dr Slaa akiwa mgombea urais uchaguzi utakuwa ni mchakato wa pekee wa kusambaa kwa elimu ya uraia kwa umma, kuunganisha watanzania bila kujali itikadi katika kuleta mabadiliko, kuibua uozo uliopo na kutoa sera mbadala zenye kuleta tumaini jipya la watanzania kupitia chama na uongozi mbadala. Mchango huu wa kishujaa kwa taifa utapanda mbegu ya mabadiliko ya kisiasa na kuliondoa taifa kutoka kwenye lindi la mazoea ya ufisadi kwa kuhamasisha utamaduni wa uwajibikaji.

Katika kampeni hizo kama sehemu ya dhamira ya pamoja ya kuondoa ukiritimba na hodhi ya chama kimoja kwenye vyombo vya maamuzi Dr Slaa kuwa mgombea urais kwa uzoefu na makini atazunguka nchi nzima kuwanadi wagombea udiwani na ubunge na kuwaongeza nguvu ili tuweze kuwa na wakina Dr Slaa wengi zaidi wazee kwa vijana katika halmashauri na bungeni.

Viongozi hawa mbadala wataweza kujenga taifa lenye kutoa fursa na kutumia vizuri rasilimali za taifa iwe ni mali asili, kodi, utaalamu na vipaji vya watanzania katika kuwezesha maendeleo ya mwanachi kwa ujumla na taifa kwa ujumla kupitia chama mbadala. CHADEMA ikiwa ni chama mbadala kinatambua umuhimu wa kutumia vyema rasilimali katika sera zake na misingi yake, hivyo Dr Slaa atapeperusha bendera ya chama rangi ya bluu bahari ikiwa inawakilisha haki na rasilimali za taifa hususani maji.

Maneno yoyote ya kupingana mwelekeo huu wenye kutanguliza taifa kwanza iwe ni kwa nia njema inayosukumwa na hofu ya ombwe la Dr Slaa bungeni au mashaka ya pengo lake Karatu ama dhamira mbaya ya wapambe wa Kikwete za kuhadaa nafsi za watanzania yanapaswa yapingwe kwa matendo ya wote wenye kuitakia mema nchi yetu kwa kumuunga mkono Dr Slaa kwa hali na mali.

Ndio maana napenda kuchukua fursa hii kuwapongeza vijana wenzangu wasomi wa vyuo vikuu mlioona mbali kabla hata ya kamati kuu kukaa tarehe 20 Julai kwa kutumia ubunifu na uthubutu wa kuweka saini (petition) ya kumwomba kugombea. Naamini kamati kuu ilizingatia kuwa demokrasia ni utawala wa watu kwa ajili ya watu na kukubaliana na wito wenu na wa makundi mengine katika jamii wakiwemo wanachama wa CHADEMA wa kumuomba kugombea.

Tanzania bila CCM inawezakana kila mtu akitimiza wajibu; hivyo nashukuru kwamba baada ya kufanikisha hatua ya kwanza leo mmeomba kukutana nasi kwa hatua ya pili ya kujadiliana namna ya kufanikisha ushindi.

Hivyo ukiondoa hotuba hii ya ufunguzi leo hakutakuwa na mada za viongozi badala yake tutasikiliza kutoka kwenu mawazo yenu na namna ambavyo mmejipanga kumuunga mkono Dr Slaa katika azma ya kuleta mabadiliko tunayoyataka.

Karibuni katika viwanja vya ofisi ya chama chenye fikra za kuamini katika falsafa ya “Nguvu ya Umma” ambayo inakilishwa na rangi nyeusi katika bendera yetu ambayo ni ishara ya utu wetu: kwamba umma ndio wenye mamlaka juu ya viongozi; umma ndio wenye wajibu wa kuamua hatma ya maisha yao na ya taifa; na umma ndio unaopaswa kunufaika na rasilimali za nchi yetu.

Ni falsafa hii hii ndio tutakayotumia kuwezesha ushindi wa Dr Slaa na ushindi wa wabunge na madiwani mbadala kwa vijana kuwa mstari wa mbele kugombea ama kuunga mkono wagombea ikiwemo kutafuta na kulinda kura kwa kupitia pia falsafa ya Baraza la Vijana wa CHADEMA(BAVICHA) kwamba: Vijana; Nguvu ya Mabadiliko.

Serikali yenye woga wa mabadiliko inayotawala kwa hujuma imetoa waraka na kuziingilia ratiba za vyuo husasani vya umma na kufanya vifunguliwe baada ya uchaguzi kwa hoja kanyaboya na hivyo kukwamisha baadhi yenu kupata haki ya msingi ya kikatiba ya raia ya kupiga kura pamoja na kuwa mlishajiandikisha tayari. Aidha ratiba hii ina dalili zote za kukwepa mshikamano wa wasomi wakati wa uchaguzi kwa kila mtu kuwa likizo katika hali inayoweza kutafsiriwa kuwa ni mpango wa ‘wagawe uwatawale’.

Hata hivyo, ni wakati wa vijana kuwaambia watawala kuwa ‘hatudanganyiki wala hatugawanyiki’, uamuzi wenu wa kukukutana wawakilishi wa wanavyuo mbalimbali kabla ya kutawanyika ili kuunganisha nguvu ya pamoja umefanyika katika wakati muafaka.
Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kwamba dhima ya wasomi na kama wajibu wa mtu aliyepewa chakula aweze kupata nguvu ya kwenda kuleta chakula kwa ajili ya wengine katika kijiji chenye njaa; mtu kama huyo asiporudi ni msaliti.

Ni wajibu huu ndio unaopaswa kuwasukuma maeneo yoyote ambayo mtakuwa muifuatilie fursa yenu ya kupiga kura na kufanya hivyo, lakini mnawajibu mkubwa zaidi wa kutafuta kura nyingine nyingi zaidi kwa kuwaelimisha watanzania wengine na kuongoza harakati za mabadiliko ya kweli.

Katika kushinda uchaguzi vipo vipaumbele vinne ambavyo naomba nivitaje kwa kadiri ya umuhimu wake kama sehemu ya kuibua majadiliano yetu siku ya leo; mosi, mgombea; pili, ajenda; tatu, oganizesheni na nne; rasilimali.

Kwa upande wa Urais mgombea tayari tunaye ambaye anasubiri tu kuthibishwa na mkutano mkuu baada ya michakato kukamilika; wa upande wa ubunge na udiwani pia katika maeneo mbalimbali ya nchi wapo wagombea wamejitokeza ingawa milango bado iko wazi kwa kuwa tarehe ya mwisho ya uchukuaji na urudishaji fomu ndani ya chama ni tarehe 9 Agosti kabla ya uteuzi wa kiserikali Agosti 19. Kwa bahati njema pia sehemu kubwa ya wagombea ni vijana wenzetu na wazee wenye kutaka mabadiliko. Hivyo mnawajibu wa kwenda kuwaunga mkono wagombea katika maeneo ambayo mnakwenda.

Kipaumbele cha pili ni ajenda za kisiasa ambazo katika uchaguzi huwekwa katika ilani. Tayari kamati kuu ya chama imepokea rasimu ya ilani na mchakato wa kuiboresha unaendelea kwa kuzingatia mawazo na maoni mbalimbali unaendelea mpaka itakapopitishwa na Mkutano Mkuu wa chama Agosti 12 mwaka huu. Hivyo, nyinyi kama vijana wasomi wa kada za mbalimbali mna wajibu wa kushauri hoja za kuwekwa kwenye ilani katika sekta mbalimbali ambazo mmezisomea na mnaendelea kuzisomea kwa kuzingatia pia hali halisi ya taifa na watanzania kwa sasa. Majadiliano ya leo yatawezesha kuanza kupokea maoni yenu si tu ya kuchambua hali ilivyo chini ya uongozi wa CCM bali pia kupendekeza CHADEMA ifanyeje pindi ikiingia katika uongozi ama ni Tanzania ya namna gani mngependa ijengwe na chama mbadala. Pamoja na kuwa CHADEMA inazo sera zake na mwaka 2005 ilikuwa na ilani ambayo mnaweza kuirejea kupitia www.chadema.or.tz bado tunaamini kwamba chama cha siasa kina wajibu wa kuwasikiliza wananchi badala ya kujifungia na kuandaa ilani zisizosingatia hali halisi ya taifa.

Kipaumbele cha tatu ni oganizesheni ya kampeni ikiwemo mikakati mbalimbali ya kujipenyeza katika jamii kwa kutumia mbinu na timu mbalimbali. Hivyo, natarajia kikosi hiki kitasambaa katika maeneo mbalimbali na kutumia ubunifu, nguvu, uwingi na uthubutu wa vijana kufanya kampeni za kipekee kama ambavyo mtabadilishana mawazo katika mkutano wa leo. Tanzania bila CCM inawezekana kila mmoja akitimiza wajibu.
Kipaumbele cha nne ni rasilimali, izingatiwe kwamba tayari CCM imeshaanza na imejipanga kutumia nyenzo ikiwemo za dola/serikali na fedha nyingi zikiwemo za ufisadi na ubadhirifu katika kulazimisha ushindi kwa ushahidi wa nyaraka ambazo binafsi ninazo mpaka sasa ambazo zitatolewa katika wakati muafaka. Ni wajibu wetu kushirikiana kuwaumbua kila mahali mipango yao ya kiharamia lakini ni wajibu wetu pia kutumia mbinu mbadala na rasilimali mbadala za kukabiliana na hali hiyo. Rasilimali mbadala kwa kutumia nguvu ya umma ni pamoja na vijana wasomi kama nyinyi kujitolea utaalamu wenu, muda wenu, vipaji vyenu na nguvu yenu kuwezesha maandalizi, kampeni na ulinzi wa kura. Haya ni kati ya mambo ambayo ni muhimu mkayatafakari katika mkutano wa leo.

Historia ya duniani inaonyesha kwamba mchango wa vijana na wanafunzi ni wa muhimu sana katika kuanguka kwa tawala za kidikteta, za kibaguzi na za kifisadi. Historia kama hii inapaswa kuandikwa nchini mwetu kwa njia za kidemokrasia kupitia uchaguzi ili kuleta mabadiliko ya kweli na uhuru wa kweli.

Tuyafanye hayo tukitambua kwa pamoja kwamba mabadiliko ya kweli katika taifa letu hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile, chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale kwa Ari, Nguvu na Kasi (ANGUKA) zaidi. Kwa falsafa ya chukua chako mapema(ccm), ya chama cha mafisadi(ccm); Tanzania yenye neema haiwezekani. Tuunganishe nguvu kurudisha nchi kwa wananchi; Tanzania bila CCM inawezekana kupitia chama mbadala na uongozi bora.

Natangaza kwamba mkutano huu umefunguliwa rasmi na tuko tayari kuwasikiliza; Vijana, Nguvu ya Mabadiliko.

Tunu kwa kumbukumbu ya mashujaa

MAKALA IFUATAYO NILIIANDIKA MWAKA 2006, NIMEIREJEA WAKATI HUU KWA AJILI YA KUMBUKUMBU YA MASHUJAA TAREHE 25 JULAI 2010: Kamaradi Kinjeketile na mashujaa wenzako popote mlipo! Hii ni tunu kwenu. Hidaya kwenu mliomwaga damu wakati mapambano kadhaa na Mreno na Mwarabu. Tuzo kwenu nyinyi mliopigana na Ujerumani wakati wa utawala na mliomwaga damu katika vita vya dunia. Heko ninyi ambao damu ilisafisha safari ya kumng’oa Nduli Amin. Heri wewe Sethi Benjamini na wote waliopotesha maisha katika hekaheka za kueneza Azimio la Arusha. Kumbukumbu kwenu mliotoa damu katika mikikimikiki ya mfumo wa vyama vingi kutoka Zanzibar mpaka bara. Damu yenu iliyomwagika haizoleki, ukiwa mlioucha hauzoeleki lakini fikra mlizosimamia hazizeeki. Mapambano bado yanaendelea!

Kwako Bushiri bin Salim wa Tanga, suriama wa kiarabu na kiafrika, pamoja na nia yako tenge ya kulinda maslahi katika biashara ya utumwa ulimwaga damu kwa kunyogwa Pangani baada ya kuongoza maasi makali dhidi ya kuingia kwa ukoloni wa Kijeruamani-damu yako ilimwagika pamoja na damu za wapiganaji wa Pwani, Morogoro mpaka uhehe. Ewe Mtemi Meli, uliowashinda wadachi mpaka mwenzio Sina alipokusaliti hatimaye wewe na mashujaa wenzako mkamwaga damu kaskazini mkilinda uhuru.Wewe Chifu Mkwawa, tunakukumbuka uliovyowaunganisha wahehe-toka Kalenga, Tosamaganga mpaka ulipoamua kuimwaga damu yako mwenyewe kuliko uhuru upotee mikononi mwako. Mtemi Isiki wa Tabora uliendesha mashambulizi ya kishujaa, hatimaye ukaamua kumwaga damu yako na ya familia yako kwa kujilipua na baruti ili tu usipate aibu ya uhuru kuchukuliwa mbele ya macho yako. Ewe Mtemi Makongoro wa Musoma, ulipambana kwa ushujaa mpaka ilibidi kikosi cha wanamaji kiletwe kupitia miji ya Mombasa na Kisumu kukumaliza.

Nakutunuku Kinjeketile kwa kuongoza vita vya kutisha vya Maji Maji kwa miaka kadhaa vilivyoanzia vilima vya Matumbi karibu na Kilwa. Nyinyi mlitaka kumwondoa mkoloni kwa nguvu na mlikuwa tayari kumwaga damu kuliko kuendelea kuishi bila ya uhuru. Mapambano yenu yalisambaa maeneo mengi ya ardhi yetu. Ninyi mlikuwa mashujaa kweli kweli mliojua umuhimu wa imani na falsafa katika mapambano-mkawapa watu ujasiri kwa dawa ya “Kugeuza risasi, Kuwa maji”. Pamoja na kushindwa vita na wazalendo zaidi ya laki moja kupoteza maisha katika wakati ambao ardhi ilikuwa na watu wachache yapo mapigano ambayo mlishinda. Pamoja na machifu 47 wa Kingoni kunyongwa damu yenu ilileta mabadiliko katika utawala. Kwa vyovyote vile damu nyingi kiasi hiki iliyomwagika kwa sababu ya kudai uhuru haiwezi kupuuzwa. Hivyo waraka huu ni tunu kwenu. Mapambano bado yanaendelea!

Nawaandikia waraka huu ninyi wahenga mashujaa muweze kurejea na kurekebisha historia. Najua mnaweza msirudi kimwili, lakini ni vyema kiroho mkandelea kuwa nasi. Fikra zenu za kimapambano hazipaswi kupotea. Kumbukumbu zenu za kishujaa hazistahili kufutika. Taifa lisilo na historia haliishi, linakufa. Kupotosha historia ya mashujaa ni kinyaa. Karibu kila eneo katika nchi yetu yupo shujaa ambaye anaweza kukumbukwa laiti kama historia zenu zingejulikana kizazi hata kizazi na kuwa chimbuko la kujiamini, kujithamini na uzalendo miongoni mwa Watanzania.

Julai 25 ilikuwa siku nyingine ambapo tulifanya maadhimisho ya kinafiki ya siku ya mashujaa. Mtanishangaa kwa kutumia dhana kali- “UNAFIKI”. Namaanisha!. Ni dhana ambayo mnaifahamu na hamkuipenda. Ndio maana hamkutaka kuishi katika unafiki wa kukubaliana ama kutumiwa na watawala. Mkaamua kupambana! Mkamwaga damu mkiukimbia unafiki. Sasa tunawakumbuka! Lakini nasema tena, tunawakumbuka kwa kufanya maadhimisho ya kinafiki ya siku ya mashujaa. Ndani ya dhana ya unafiki kuna tabia nyingi, mojawapo ni kunena tofauti na matendo na kutenda tofauti na kauli. Na ndiyo tabia tunayoifanya wakati wa maadhimisho ya siku ya mashujaa. Ndio maana nasema, tunafanya maadhimisho ya kinafiki.

Labda ni waambie wakina Kinjeketile, nini tulifanya huku kama ishara ya kuuadhimisha ushujaa wenu. Siku chache zilizopita 25 Julai, tulijumuika chini ya Amiri Jeshi Mkuu, kwa sasa ni Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete-Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Yeye mwenyewe hakuwepo, alituma mwakilishi wake. Tulielezwa kwamba Rais yupo kwenye ziara ya kikazi Ujerumani!

Usiku mmoja kabla tuliwasha mwenge wa uhuru pale Mnazi mmoja. Halafu asubuhi yake gwaride lilijipanga kuwapokea wageni wa Kitaifa. Zikatolewa salam za Rais na wimbo wa Taifa ukapigwa kwa heshima yenu. Kikundi cha Buruji kikapiga “last post” na gwaride likaweka silaha begani. Askari sita waliojipanga vyema wakapindua silaha zao chini na baadae mizinga ikapigwa kwa ajili yenu huku watu wote wakiwa kimya. Gwaride likafanya “present arms” na kikundi cha buruji kikapiga “reveilles”. Gwaride likateremsha silaha na kufungua miguu.

Halafu silaha za asili ambazo nyingine nyinyi mashujaa mlizitumia zikawekwa kwenye mnara pamoja na maua. Baadhi ya silaha zilizowekwa ni pamoja na mkuki, ngao, sime, shoka, pinde na mishale. Hizi ni kumbukumbu sanifu za mapambano mliyoyafanya.

Hatimaye zikafuata sala na swala kutoka kwa viongozi wa dini wakiwakilishwa na sheikh, mchungaji, padri na maraji wa wahindu. Ingawaje sikumwona kiongozi wa dini ya jadi-ambao najua baadhi yenu nyinyi mashujaa na wahenga mliwaamini. Pengine dini za jadi zilitoweka na damu zenu. Gwaride likatoa tena heshima na wimbo wa taifa kupigwa ukafuatiwa na itifaki za viongozi wa kitaifa kuondoka. Wakabaki polisi kuzilinda silaha za kumbukumbu ya mashujaa mpaka jioni na hatimaye mwenge wa uhuru ukazimwa kama ishara ya mwisho wa maadhimisho ya kumbukumbu yenu ninyi mashujaa. Niwaulize wakina Kinjeketile, haya siyo maadhimisho ya kinafiki ya mashujaa? Pengine mtanijibu hapana!.

Ngoja niwaeleze masuala kadhaa halafu niwaulize tena. Siku hizi kuna kitu kinaitwa Bunge, hiki ni chombo cha juu chenye uwakilishi wa wananchi ambacho kunafanya maamuzi mbalimbali ambayo mengine huwa sheria. Chombo hiki ni kama yale mabaraza ya jadi yaliyokuwepo wakati wenu. Wiki iliyopita bunge lilijadili kuhusu maadhimisho ya vita vya Maji Maji ambavyo nyinyi wakina Kinjeketile mliviongoza. Miaka mia moja imepita toka damu yenu azizi ilipomwagika katika mapambano hayo ya kumwondoa mkoloni.Ungekuwepo najua ungekuwa Mbunge wa Kilwa, ungeshangaa sana-Eti maadhimisho ya vita mlivyovianza Kilwa na mapambano ya mwisho yakawa Songea, yanafanyika kinyume chake! Maadhimisho yameanzia Songea na waziri ameahidi pengine yataishia Kilwa. Chacha Wangwe, mbunge wa CHADEMA (wakati wenu hakukuwa na vyama vya siasa vyenye majina haya) jimbo la Tarime, yeye akahoji-kwanini bendera ya taifa isiwekwe rangi nyekundu kama ishara ya kuwakumbuka nyinyi mashujaa wetu? Naibu waziri wa habari na michezo, Mheshimiwa Emanuel Nchimbi-yeye akajibu, hakukuwa na sababu ya rangi nyekundu kuwekwa kwenye bendera ya Taifa kama ishara ya kuwakumbuka mashujaa. Eti, historia ya uhuru wa nchi yetu inaamuliwa kuanzia mkoloni wa mwisho aliyetutawala ambaye ni Muingereza. Sasa kwa kuwa tulipata uhuru wetu kwa amani bila kumwaga damu chini ya uongozi wa mwalimu Nyerere basi hakukuwa na sababu ya kuweka rangi nyekundu. Enyi mashujaa Kinjeketile na wenzako tunaowakumbuka leo mnakubaliana na jibu hili?

Ndio maana nikasema ni maadhimisho ya kinafiki. Tunanena tofauti na matendo. Nimesema awali, tunaanza maadhimisho ya leo kwa kuwasha mwenge wa uhuru halafu baadae tunaweka silaha za jadi. Kinjeketile na wenzako, iulizeni serikali- kama uhuru wetu tuliupata kwa amani, iulizeni serikali kwanini tunawasha mwenge wa uhuru na baadaye kuweka silaha za jadi? Tunanena tofauti na tunavyotenda? Iulizeni serikali, je harakati za mwisho za uhuru ni kipimo pekee cha historia ya nchi na hivyo kuwa kigezo pekee cha kuamua alama za nchi ikiwemo bendera?

Enyi mashujaa mlioambana kuulinda uhuru wetu dhidi ya wakoloni kuingia kuanzia wakati wa Mreno, Mwarabu na Mjerumani na kumwaga damu, mnakubaliana na majibu haya? Kushindwa kwenu na hatimaye ukoloni kuingia hakuondoi historia kuwa mlimwaga damu kwa ajili ya kulinda uhuru wa ardhi hii tukiyoirithi!

Enyi mashujaa mliopambana kuondoa ukoloni hususani ule wa Ujerumani mkamwaga damu, mnakubaliana na kumbukumbu hii? Kwamba mliyoyafanya si historia kuu kama historia ya uhuru toka kwa Mwingereza?

Enyi mashujaa, waulizeni wataalamu wa historia-baada ya Ujerumani kushindwa na makoloni yake yote kuwekwa chini ya halmashauri ya mataifa na baadaye baraza la udhamini, Tanganyika ikiwekwa chini ya uangalizi wa Uingereza-si kwamba tulikuwa katika hatua za mwisho kabisa za kupewa uhuru ambao tayari tulishaupata kwa damu? Waulizeni pia, hakuna damu yoyote iliyomwagika wakati wa Mwingereza? Je, historia ya nchi yetu iliyojikita katika kipenzi chetu Nyerere imewajumuisha mashujaa wote wa ardhi hii?

Nasema kwa damu-kuanzia ushindi pamoja na kushindwa dhidi Mjerumani ambao ulileta mabadiliko katika mfumo wa utawala sanjari na mashujaa ambao walikuwa mstari wa mbele katika jeshi la Mwingereza na washirika wake katika vita dhidi ya Mjerumani, vile vita vya dunia ambavyo vilipiganwa pia katika ardhi yetu? Wakina nani walimwaga damu zaidi katika kile kinachoitwa ukombozi ulioletwa na majeshi ya mfalme Afrika (KAR) kama si nyinyi babu zetu?

Hojini serikali, hivi bendera hii ni ya Tanganyika au Tanzania? Jibu la Nchimbi limetolewa katika muktadha wa historia ya Tanganyika, Ingekuwa vipi jibu lingetolewa mintaarafu bendera ya Tanzania ambayo ilipatikana kutokana na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ilihali visiwani kuna historia ya damu kumwagika ama kumwagwa wakati wa mapinduzi? Kama kweli tuna serikali ya mapinduzi Zanzibar na utawala wa Chama cha Mapinduzi(CCM), je ni mapinduzi yasiyo na ‘rangi nyekundu’?

Tunatenda tofauti na kauli! Tunafanya maadhimisho ya kinafiki. Wakina Kinjeketile tunawakumbuka kwa kuwa mlimwaga damu kupinga ukoloni na unyanyasaji. Mtuulize wajukuu zenu, je tunawaadhisha kwa kuendelea kupiga vita yale mliyoyakataa? Kwa hali ilivyo, wapo wanaotenda yale mliyoyakataa pamoja na kuwa wote kwa kauli tunawaenzi ninyi mashujaa. Tunapaswa sasa kuweka fikra zenu katika vitendo kwa ajili ya ukombozi wa taifa letu. Mwalimu Nyerere alikumbuka fikra zenu akatamka na kutenda kwamba uhuru, si uhuru wa maneno. Ni uhuru dhidi ya ujinga, uhuru dhidi ya maradhi, uhuru dhidi ya umaskini na baadaye akaongezea uhuru dhidi ya rushwa ama ufisadi. Enyi wahenga mashujaa, shukeni katika nyoyo za watoto na wajuu zenu, mtufanye kutokana na maadhimisho ya mwaka huu tuweke dhamira ya kupigana vita kwa zana kisasa kuleta mabadiliko ya kweli na uhuru wa kweli, kuleta haki na maisha bora. Hii ndiyo hidaya kwa damu yenu azizi. Sio siri, kwa sera bila silaha, mapambano bado yanaendelea!

Chanzo: http://www.chadema.or.tz/makala/makala.php?id=40

Saturday, July 17, 2010

RIP: Profesa Mwaikusa, Gwamaka na Mtui

Unahitajika mkakati wa pekee kukabiliana na ujambazi maeneo ya pembezoni mwa DSM kama Salasala, Mpiji Magoe, Goba, Temboni, Kwembe, Saranga nk. Wananchi wanalipa kodi wakitarajia kwamba moja ya jukumu kuu la serikali na vyombo vyake ni kulinda usalama wa maisha yao na mali zao. RIP: Profesa Mwaikusa, Gwamaka na Mtui.

Tuesday, July 13, 2010

Hongera Kinondoni kwa kushinda Copa Coca Cola U 17

Nawapongeza timu ya vijana(U 17) wa Mkoa wa kimichezo wa Kinondoni kwa kuwa mabingwa wa Copa Coca Cola tarehe 10 Julai 2010.

Mashindano kama haya ya vijana na watoto na yale ya mashuleni kama umishumta na umiseta ni ya muhimu sana katika kujenga oganizesheni ya soka na kuunda timu bora za baadae(dream team).

Ni muhimu sana tukayapa mkazo na kuwekeza pia katika mafunzo na viwanja kuanzia ngazi ya chini kabisa mitaani na kwenye wilaya.


John Mnyika-Mwenyekiti Mkoa wa Kichama wa Kinondoni (CHADEMA)