Wednesday, July 22, 2009

Pinda kupindisha kanuni za Uchaguzi wa Vitongoji, Vijiji na Mitaa?

Pinda kupindisha kanuni za Uchaguzi wa Vitongoji, Vijiji na Mitaa?

Na John Mnyika

Katika mchezo wowote haiyumkiniki refa kuwa mchezaji wa moja ya timu zinazoshindana. Wala haifikiriki wakati huo huo refa huyo huyo akawa kocha, mchezaji na mtungaji wa kanuni za mchezo. Lakini maajabu hayo ni jambo la kawaida katika sheria zetu kuhusu chaguzi za vitongoji, vijiji na mitaa.

Chini ya sheria zetu, kanuni za chaguzi hizo hutungwa na Waziri mwenye dhamana ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI). Na kwa mujibu wa muundo wa sasa wa utawala wa Tanzania pamoja na kuwa na waziri wa nchi anayehusika na TAMISEMI, mwisho wa siku mwenye dhamana kamili ya “Wizara” hii ni Waziri Mkuu, ambaye kwa sasa ni Mheshimiwa Mizengo Pinda.

Izingatiwe kuwa mfumo wa utawala wa nchi yetu unaanzia katika vitongoji, vijiji na mitaa ambayo ina mamlaka kadhaa ya kiutendaji na kimaamuzi.

Uchaguzi wa ngazi hii umekuwa ukifanyika mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu hivyo hutumika kama msingi wa vyama vya siasa katika uchaguzi mkuu na kuandaa mfumo wa chama kutawala kuanzia ngazi ya chini.

Ama kwa hakika Waziri Mkuu yuko katika majaribu makubwa mwezi huu wakati ambapo watanzania wanasubiri mwezi ujao wa Agosti atangaze rasmi katika gazeti la serikali kanuni za uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa. Hii ni kwa sababu kwa mujibu wa sheria, kanuni hizi kwa sasa zinatungwa na Waziri mwenye dhamana ya tawala za mikaoa na serikali za mitaa.

Mtihani huu unakuwa mgumu kwa kuwa miezi michache iliyopita mnamo tarehe 20 Februari 2009, wadau mbalimbali ikiwemo ofisi yake, vyama vya siasa, asasi za kiraia na msajili wa vyama vya siasa walifikia makubaliano kuhusu masuala ambayo yanapaswa kuingizwa kwenye kanuni husika.

Wahenga walisema kinyozi hajinyoi; lakini hapa Waziri Mkuu Pinda amepewa mtihani wa kujinyoa kwa kupewa jukumu la kutunga kanuni za uchaguzi ambazo yeye na chama chake ni sehemu ya washiriki.

Wadau wanasubiri kuona kama atatekeleza makubaliano ya wadau na kutunga kanuni zenye kusimamia misingi ya uchaguzi huru na haki. Ama Waziri Mizengo atafanya mizengwe na kutunga kanuni za uchaguzi zisizoweka uwanja sawa wa kisiasa na hatimaye kuleta uchafuzi badala ya uchaguzi?

Kujiuliza huku kwa wadau kunasababishwa na kumbukumbu za mwaka 2004, ambapo kama ilivyo sasa kanuni za uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa zilitungwa na Waziri mwenye dhamana badala ya chombo huru cha kusimamia uchaguzi mathalani tume ya uchaguzi.

Mwanya huu wa kisheria wa mchezaji kujitungia mwenyewe kanuni za mchezo ulifanya kanuni hizo kutungwa kupendelea chama kinachotawala kwa kuweka mianya ya hujuma za kiuchaguzi. Matokeo yake ni uchaguzi uliopita wa vitongoji, vijiji na mitaa kutokuwa huru na haki kutokana na mapungufu mengi ambayo hata serikali yenyewe iliyakiri.

Mathalani upigaji kura kutokuwa wa siri, fujo katika mikutano ya uchaguzi, matayarisho kuwa hafifu, kuinguliwa na maafisa na watendaji wa kata na vijiji ambao walifikia hatua ya kuwatisha wananchi na kutotoa taarifa za muhimu za uchaguzi, kukosekana kwa daftari la wapiga kura na uchaguzi kusimamiwa na chombo kisicho huru cha kiserikali moja kwa moja(Wizara ya TAMISEMI).

Wakati mchakato wa uchaguzi huo ukiendelea vyama vya upinzani vikaenda mahakamani, baadhi ya taratibu za uchaguzi huo zikazuiwa lakini uchaguzi wenyewe haukuzuiwa. Mahakama ikaamua uchaguzi uendelee wakati kesi ya msingi inaendelea kusikilizwa kwa maelezo kuwa serikali tayari ilishaingia gharama za maandalizi ya uchaguzi!

Kutokana na mapungufu hayo CCM ilishinda kwa asilimia 96 na kupata mtaji haramu wa kisiasa ambao ilianza nao kama hujuma katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 na kufanya uwanja wa ushindani wa kisiasa usiwe sawa. Na hivyo, CCM ikashinda kwa takribani asilimia 80 katika uchaguzi mkuu mwaka mmoja baadaye.

Ilitarajiwa kwamba marekebisho ya haraka yangefanyika, hata hivyo hakuna hatua za maana zilizochukuliwa kati ya mwaka 2005 mpaka 2008. Kesi iliyofunguliwa na vyama vya upinzani mwaka 2004 mpaka sasa bado ni kizungumkuti. Kwa upande mwingine, Serikali ilikuwa ikiitisha mikutano na vyama na kuiahirisha bila maamuzi ya msingi kufikiwa kuhusu marekebisho yanayostahili kufanywa katika sheria na kanuni zinazosimamia chaguzi husika. Mithili ya mbinu ya timu iliyoshinda kupoteza muda ili mpira umalizike; lakini kwa kuwa refa ni kocha mchezaji, hakukuwa na wa kupuliza filimbi wala kutoa kadi!

Mwaka 2009, mwezi Februari ndipo serikali imesaini makubaliano na wadau kuhusu uchaguzi huu. Kwa kisingizio cha ufinyu wa muda, masuala ya msingi yaliyopaswa kufanyiwa marekebisho mengi hayapo kama sehemu ya makubaliano hayo. Kwa mara nyingine tena, serikali imechelewesha muda na baadaye kutumia kisingizio cha muda kukwepa kufanya mabadiliko ya msingi ya kisheria ya kuhakikisha uchaguzi huu unakuwa huru na wa haki.

Shabaha ya makala hii ni kuibua mjadala wa kukumbusha makubaliano haya ili wadau waweze kufuatilia kwa karibu kuhakikisha kwamba walau makubaliano hayo yanazingatiwa na Waziri Mkuu Pinda katika kutunga kanuni.

Kama mchakato wa utungaji wa kanuni utaendelea kufanyika kimya kimya bila rasimu ya kanuni kupelekwa kwa wadau ikiwemo vyama vya siasa kupitiwa kabla ya kuchapwa kwenye gazeti la serikali makubaliano hayo yanaweza kupindishwa.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo; yafuatayo hayatafanyiwa marekebisho: umri wa kugombea; utabaki miaka 21 badala ya kushuka mpaka 18. Wagombea binafsi;hawataruhusiwa.

Kuhusu kilio cha miaka mingi cha wadau cha kutaka Uchaguzi usimamiwe na Tume ya uchaguzi kama ilivyo katika baadhi ya nchi nyingine duniani; makubaliano yameweka bayana kuwa uchaguzi utaendelea kusimamiwa na serikali kupitia waziri mwenye dhamana ya serikali za mitaa. Kwa mantiki hiyo basi hata hoja ya kutaka kanuni za uchaguzi zitungwe na chombo huru haitazingatiwa.

Mwito wa Vyama vya siasa kutaka viwezeshwe kutoa elimu ya uraia nao hautazingatiwa. Serikali ilishaweka msimamo kuwa jukumu la kutoa elimu ya uraia litaendelea kuwa la serikali, vyama vya siasa vinaweza kutoa kwa kutumia rasilimali zao.

Hoja ya kutaka uchaguzi wa madiwani uende sambamba na chaguzi zingine za mitaa nayo haitarajiwi kuwepo katika kanuni zitakazotolewa na Waziri Mkuu Pinda. Uchaguzi wa madiwani utaendelea kuwa na uchaguzi mkuu mwaka 2010; hii ni kwa sababu suala hili linahitaji marekebisho ya kisheria na serikali imeshatamka wazi kwamba muda umeshakwisha wa kufanya marekebisho husika.

Haya ni masuala nyeti ambayo wadau wengi wangependa yafanyiwe marekebisho lakini hakuna mabadiliko yoyote ambayo Serikali itayafanya kuhusu masuala hayo katika kanuni zinazotungwa ambazo Waziri Mkuu Pinda atazitangaza siku za usoni.

Mtiririko wa masuala haya kwa ujumla unadhihirisha kwamba serikali haikupanga kufanya mabadiliko ya msingi na kutoa uzito unaostahili kwa uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa. Kirasilimali makubaliano yalilenga tu kwamba katika bajeti ya mwaka wa fedha 2009/10 serikali itatenga bilioni nane(8) tu zitakazotumika kusimamia na kuratibu uchaguzi wenyewe ngazi ya halmashauri ifikapo Oktoba 2009.

Wakati serikali ikipanga kutenga fedha kiasi kidogo kama hicho kwa ajili ya kuendesha uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa nchi nzima, tume ya uchaguzi kwa upande wake inatarajia kutumia bilioni 42.9 kama gharama za kuboresha daftari la wapiga kura pekee kuanzia mwaka 2009. Tume hiyo hiyo inakadiria kutumia bilioni 64.5 kuendesha uchaguzi wa mwaka 2010. Itakumbukwa kuwa mwaka 2005, Tume ya uchaguzi ilitumia bilioni 62.5 katika uchaguzi mkuu.

Hata wadau wengine wa maendeleo hawajaweka mkazo wa kutosha kuhusiana na uchaguzi huu, mathalani miradi ya Shirika la Umoja wa Mataifa na michango ya washirika wa kimaendeleo kuhusu uchaguzi, imeelekezwa katika uchaguzi wa mwaka 2010 pekee.

Hata hivyo, kwa mujibu wa makubaliano; marekebisho yafuatayo yatafanyika na kuzingatiwa katika kanuni zinazotarajiwa kutolewa mwezi Agosti mwaka 2009. Hivyo wadau wanapaswa kujadili na kufuatilia kuhakikisha kwamba Waziri Mkuu Pinda hapindishi maamuzi hayo.

Kanuni zinapaswa kuelekeza kwamba kutakuwa na karatasi maalum za kura zenye nembo ya halmashauri husika; karatasi hazitakuwa na majina ya wagombea, majina yatabandikwa sehemu ya wazi baada ya uteuzi. Ndoo maalum za plastiki zenye kuonyesha(transparent) zitatumika kupigia kura badala ya masanduku ya kura.

Uchaguzi utafanyika kwenye majengo ya umma, kama hakuna msimamizi atashirikiana na vyama kupata sehemu muafaka. Kanuni zinapaswa zieleze kuwa uchaguzi wa Wenyeviti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri za Kijiji na Wenyeviti wa Vitongoji utafanyika katika kitongoji ili kuwafanya wapiga kura wengi kuweza kufika na kupiga kura zao; Kampeni zitafanyika kwa muda wa siku saba kama ilivyo kwa kanuni za 2004. Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Mitaa na wajumbe wa Kamati za Mitaa utafanyika katika mitaa husika, vituo vitakuwa zaidi ya kimoja kulingana na wakazi wa mtaa.

Kwa mujibu wa makubaliano Orodha ya wapiga kura(Local Voter register) itaandaliwa siku 21 kabla ya uchaguzi ili kutoa nafasi kwa wapiga kura kukagua orodha na kuweka pingamizi. Orodha itaandaliwa na watumishi wa umma lakini wasiwe watendaji wa vijiji, mitaa au kata. Uthibitisho wa mpiga kura utatokana na jina lake kuwepo katika orodha ya wapiga kura, vitambulisho vitavyotumika kumtambulisha chochote kati ya vifuatavyo- kadi ya mpiga kura, kitambulisho cha kazi, hati ya kusafiria, kadi ya benki, kadi ya bima ya afya, kitambulisho cha chuo/shule, leseni ya uderava au wakazi kama mpiga kura hana kitambulisho chochote.

Kanuni zinapaswa kuwa na kifungu cha kamati ya rufaa ambayo wajumbe wake watateuliwa kutokana na hali ya eneo husika ila hawatakuwa kati ya wafuatao; afisa anayehusika na uteuzi wa wagombea, msimamizi au msimamizi msaidizi wa uchaguzi, kiongozi wa ngazi yoyote wa chama cha siasa, mtumishi wa halmashauri, kiongozi yoyote wa dini. Masuala haya na mengine yako mikononi mwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, wadau wanajiuliza; atatunga kanuni za uchaguzi zenye kuzingatia haki na demokrasia au ataleta mizengwe ya kupindisha makubaliano? Tunasubiri!

Mwandishi wa makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa CHADEMA anayepatikana kupitia 0754694553, mnyika@yahoo.com na http://mnyika.blogspot.com

Tuesday, July 21, 2009

“Ruksa” kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-4


“Ruksa” kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-4

Na John Mnyika


Makala zilizotangulia zimedokeza wakina nani ni watumishi wa umma na ushiriki wao katika siasa katika vipindi vilivyotangulia; wakati wa mfumo wa chama kimoja 1965 mpaka 1992 na kipindi cha awali cha mfumo wa vyama vingi 1992 mpaka 2000. Pia nilianza kufanya mapitio ya kuhusu maadili ya watumishi wa umma katika mfumo wa vyama vingi vya siasa kuanzia mwaka 2000 na tunapoelekea katika chaguzi za mwaka 2009 na uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Katika makala hii tutafanya mapitio ya mambo ambayo watumishi wa umma wanaruhusiwa kuyafanya kama sehemu ya ushiriki wao katika siasa. Makala ijayo tutafanya mapitio ya mambo yasiyoruhusiwa kufanywa na watumishi wa umma katika ushiriki wao kwenye siasa.

Kwa ujumla washiriki wa umma wanaruhusiwa kushiriki katika siasa. Ikumbukwe kuwa utumishi wa umma katika nchi yetu unaongozwa na Sheria ya Utumishi Serikalini namba 16 ya mwaka 1989 na Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma Toleo la 1994 pamoja na marekebisho yake. Kifungu cha 4(1) cha Sheria hiyo kinampa mamlaka Mkuu wa Utumishi wa Umma, ambaye ni Katibu Mkuu kiongozi kutoa waraka kuhusu taratibu mbalimbali za utumishi wa umma.

Chini ya Mamlaka hayo, Katibu Mkuu Kiongozi wakati huo akiwa Martem Y.C. Lumbanga tarehe 26 Juni, 2000 alitoa Waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma na. 1 wa mwaka 2000 wenye kumb. Na. SHC/C.180/2/113. Waraka huu ulihusu maadili ya Watumishi wa Umma katika mfumo wa vyama vingi vya siasa. Waraka huo ulianza kutumika kuanzia Julai Mosi, mwaka 2000.Waraka huo umetoa ruhusa kwa watumishi umma kushiriki katika mambo ya siasa na umeelekeza wazi kwamba wanaweza kushiriki katika shughuli ambazo tutazipitia katika makala hii.

Mtumishi wa umma anaruhusiwa kuwa mwanachama wa chama cha siasa anachokipenda isipokuwa watumishi wachache ambao wametajwa kwenye waraka huo. Tafsiri ya waraka huo ni kwamba wafanyakazi mbalimbali wa serikali na taasisi zake wanaweza kujiunga na vyama vya siasa mathalani Rais, Mawaziri, wabunge, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa halmashauri na Mashirika ya umma, watendaji wa kata nk. Orodha hii inahusisha pia waajiriwa wa kawaida wa serikali mathalani walimu wa shule za umma, watumishi wa sekta ya afya wa serikali, maofisa wote waajiriwa wa halmashauri/serikali za mitaa nk. Kumekuwa na baadhi ya watumishi waandamizi wa serikali wanawakataza watumishi wa kawaida mathalani walimu kujiunga na vyama vya siasa wanavyovipenda; ni vyema ikaeleweka kwamba vitendo hivyo ni vya uvunjaji wa haki za kikatiba, kisheria na kitaratibu hivyo watumishi hao wanapaswa kuwasilisha malalamiko yao kwa vyombo na wadau wanaohusika kwa ajili ya hatua kuweza kuchukuliwa.

Watumishi pekee wa umma wasioruhusiwa kushiriki katika mambo ya siasa ni wale walio katika makundi ya utumishi maalum.

Hawa ni watumishi ambao katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza wazi kwamba hawaruhusiwi kuwa wanachama wa chama chochote cha siasa. Ni kundi la watumishi wa umma ambao hawaruhusiwi kushiriki katika shughuli zozote zingine za kisiasa isipokuwa kupiga kura tu. Ibara ya 147(3) na (4) ya Katiba imewataja Askari wa Jeshi la Wananchi(JWTZ), Jeshi la Kujenga Taifa(JKT), Polisi na Magereza. Pia Ibara ya 113A imewakataza majaji na mahakimu wa ngazi zote. Kadhalika Ibara 74(14) na (15) imewazuia wajumbe na watumishi wa Tume ya Uchaguzi na Wasimamizi wa Uchaguzi.

Pia waraka huo na. 1 wa mwaka 2000 umeyataja makundi mengine ambayo pamoja ni kuwa hayajakatazwa na katiba kushiriki kwenye shughuli za kawaida za kisiasa ikiwemo kujiunga na vyama vya siasa. Mathalani, watumishi wa idara ya usalama wa taifa, taasisi ya kuzuia rushwa(sasa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa-TAKUKURU), watumishi wa ofisi ya msajili wa vyama vya siasa, watumishi wa ofisi ya bunge na mawakili wa serikali. Hata hivyo, nao wanaweza kushiriki kwenye siasa kwa kupiga kura. Hivyo, kwa ujumla, raia wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliofikia umri wa kupiga kura wanaruhusa ya kushiriki kwenye siasa ikiwemo watumishi wote wa umma kwa kupiga kura.

Haki na wajibu huu wa watumishi wa kupiga kura unazaa ruhusa ya watumishi wa umma kuhudhuria mikutano halali ya kisiasa nje ya saa za kazi kama msikilizaji. Inafahamika kwamba wapo watumishi wa umma ambao huwatishia watumishi wao wa kawaida wasihudhurie mikutano ya kisiasa hata baada ya kazi. Utata wa ziada unaibuka hapa ni kuhusu watumishi wa umma ambo kwa asili ya kazi yao hawaruhusiwi ‘kujihusisha na shughuli za kisiasa isipokuwa kupiga kura’. Swali la kujiuliza: Je, zuio hili linahusu vile vile kuwazuia kushiriki mikutano ya hadhara ya vyama wakati wa kampeni na wakati wa kawaida kwa ajili ya kusikiliza sera ama ilani za vyama na viongozi ama wagombea? Kwa tafsiri ya kawaida; jibu ni ndio. Kama hivyo ndivyo, sasa kundi hili ina maana limepewa haki ya kupiga kura lakini halina haki ya kusikiliza ili kuweza kufanya maamuzi sahihi ya nani mtumishi husika wa umma ampigie kura? Hivyo, ni vyema waraka husika ukafanyiwa marekebisho katika eneo hili ili kuondoa utata wa tafsiri. Katiba, Sheria na Taratibu zinapaswa tu kuwakataza watumishi hawa maalumu wa umma kuwa wanachama wa chama chochote cha siasa, na si kuwakataza hata kuhudhuria mikutano halali ya kisiasa.

Pia, waraka huo umeelekeza kwamba watumishi wa umma wanapaswa kuhudhuria mikutano ya kisiasa kama wasikilizaji tu. Huku ni kuminya uhuru wa kikatiba wa kutoa maoni na wa kuzungumza. Haiwezekani ukawa na raia ambaye amepewa haki ya kujiunga na chama cha siasa lakini hana haki ya kuzungumza katika mikutano, tafsiri yake ni kwamba hana hata haki ya kuzungumza katika vikao vya wanachama. Lakini tumeona wakati wote watumishi wa umma, ikiwemo waandamizi wa serikali wakivunja kipengele hiki kwa kuzungumza katika mikitano ya kisiasa; ya ndani na hata ya hadhara. Hivyo, kifungu hiki nacho kinapaswa kufanyiwa marekebisho kwa kuwa hakitekelezwi wala hakitekelezeki.
Waraka Na. 1 wa Mkuu wa Utumishi wa Umma pia umeruhusu mtumishi wa umma kutoa michango yake binafsi kwa ajili ya chama chake akiwa nje ya mahali pa kazi na nje ya saa za kazi. Haki hii inamaanisha kwamba mtumishi wa umma anaweza kutumiza wajibu wa kuchangia chama chake kwa maana ya kulipa kiingilio na ada ya uanachama. Hii inamaanisha pia kwamba watumishi wa serikali wa uhuru wa kuchangia rasilimali zao kwa ajili ya kufanikisha harakati za kisiasa, hii ni pamona na kuwa na ruhusa ya kuchangia wagombea katika kampeni za uchaguzi. Hata hivyo, ruhusu hii nayo ina utata wa kitafsiri kwa kuwa hakuna mali kumefafanuliwa maana ya neno ‘michango’. Kwa tafsiri ya juu juu na kwa kuzingatia mipaka ilidokezwa hapo juu ya kumtaka mtumishi husika kuwa msikilizaji pekee; tafsiri ya michango inayokusudiwa hapa inaweza kuonekana kuwa ni michango ya fedha na mali.

Hata hivyo, ieleweke kwamba katika medani ya siasa, uzoefu wa kimataifa unaonyesha kwamba katika michakato ya kidemokrasia michango ni zaidi ya fedha na mali. Rasilimali kwa sasa zinatafsiriwa kwa upana wake kujumuisha nguvu kazi ikiwemo vipaji, utaalamu na hata mawazo. Kwa maneno mengine, michango ambayo mtumishi wa umma anaweza kutoa kwa chama chake inaweza pia kuhusisha kuchangia mawazo, kutumia muda wake, vipaji vyake na utaalamu wake. Jambo hili ni muhimu sana likatafakariwa kwa umakini wake kwa kuwa kati ya changamoto zinazokabili ujenzi wa oganizesheni ya vyama vya siasa hususani vya upinzani ni upungufu wa rasilimali watu ya kutosha yenye utaalamu mbalimbali. Kitendo cha kuwazuia watumishi wa umma, ambao kwa kiasi kikubwa wanahusisha kada ya wasomi hususani katika maeneo ya vijijini kunaacha vyama vya siasa kuungwa mkono na umma wa wananchi wa kawaida bila mchango wa kutosha wa kada hii muhimu kwa mwelekeo wa taifa.

Katika muktadha huo, kama sehemu ya ushiriki wao katika siasa watumishi wa umma wanapaswa wakiwa nje ya maeneo ya kazi na nje ya saa za kazi kuchangia katika mwelekeo wa vyama vya siasa. Mathalani, mwalimu anaweza kabisa kuchangia mwelekeo wa kisera wa chama cha siasa kuhusu masuala ya elimu na haki za walimu. Kadhalika mtumishi wa sekta ya afya anaweza kufanya hivyo hivyo kwenye eneo lake la uzoefu. Maofisa Kilimo ama Madini nao wanaweza kutoa mchango mkubwa kutokana na utaalamu wao. Kwa ujumla kama ambavyo watumishi wa umma wanapaswa kusaidia watumishi wengine wa kiserikali wakiwa kazini ndivyo ambavyo wanapaswa kusaidia kimawazo na kirasilimali viongozi wa vyama vyao vya siasa. Yapo mambo ambayo kutokana na tofauti za kiitikadi na kisera, mtumishi wa umma anaweza akayependekeza lakini yasiweze kutekelezwa na chama kilichoko madarakani. Masuala kama hayo anaweza kuyatoa katika chama chake chenye mwelekeo anaoubaliana nayo na pindi yakiweza kutekelezwa matokeo yake yanaweza kuleta tija kwa taifa kwa ujumla. Hizi ndizo siasa ambazo zinafanywa na nchi ambazo zina demokrasia ya vyama vingi kwa muda mrefu zinazotambua kwamba siasa sio uadui bali ni mfumo wa uwagawanyaji rasilimali unaopaswa kuongozwa kwa ushindani wa hoja mbadala.


Pamoja na kutumia fursa zilizomo kwenye waraka Na. 1 wa Mkuu wa Utumishi wa Umma kama nilivyozidokeza na haja ya kufanya marekebisho katika waraka huo ili kutoa tafsiri zinazoeleweka ni muhimu pia kuendeleza harakati za kufanya mabadiliko ya kweli katika sekta ya utumishi wa umma. Harakati hizi zinapaswa kuendeshwa na vyama vya wafanyakazi hususani wa sekta ya umma. Mabadiliko hayo ya kikatiba, kisheria na kimitazamo yatawezesha kuwa na tunu za kitaifa, misingi kamili ya haki za raia, mifumo ya uwajibakaji wa viongozi na uwanja sawa wa kisiasa. Mabadiliko hayo yatawezesha pia kujenga taasisi za kitaifa, uongozi bora na dira ya pamoja yenye kuunganisha nguvu za umma katika kupambana na ufisadi, kutetea rasilimali na kusimamia fikra mbadala zenye kujenga taifa lenye kutoa fursa kwa wote. Taifa wananchi wanaweza kuneemeka na uwezo ambao wamejaliwa wao na nchi kwa ujumla. Watumishi wa umma wanapopigania ongezeko la mishahara na uboreshwaji wa maslahi waelewe kwamba uongozi wa kisiasa umeshikilia hatma yao. Hivyo, ushiriki wa watumishi wa umma kwenye siasa ni suala lenye maslahi kwao binafsi na kwa taifa kwa ujumla. Watumishi wa umma Tanzania wakumbuke wosia wa Hayati Kwame Nkurumah ya kwamba ‘utafuteni ufalme wa siasa’ na yote mtaongezewa.

Mwandishi wa Makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje(CHADEMA) anapatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.net na http://mnyika.blogspot.com


“Ruksa” kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-3



“Ruksa” kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-3

Na John Mnyika


Makala zilizotangulia zimedokeza wakina nani ni watumishi wa umma na ushiriki wao katika siasa katika vipindi vilivyotangulia; wakati wa mfumo wa chama kimoja 1965 mpaka 1992 na kipindi cha awali cha mfumo wa vyama vingi 1992 mpaka 2000. Makala hii inalenga kuanza kufanya mapitio ya kuhusu maadili ya watumishi wa umma katika mfumo wa vyama vingi vya siasa kuanzia mwaka 2000 na tunapoelekea katika chaguzi za mwaka 2009 na uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Ikumbukwe kuwa utumishi wa umma katika nchi yetu unaongozwa na Sheria ya Utumishi Serikalini namba 16 ya mwaka 1989 na Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma Toleo la 1994 pamoja na marekebisho yake. Kifungu cha 4(1) cha Sheria hiyo kinampa mamlaka Mkuu wa Utumishi wa Umma, ambaye ni Katibu Mkuu kiongozi kutoa waraka kuhusu taratibu mbalimbali za utumishi wa umma.

Chini ya Mamlaka hayo, Katibu Mkuu Kiongozi wakati huo akiwa Martem Y.C. Lumbanga tarehe 26 Juni, 2000 alitoa Waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma na. 1 wa mwaka 2000 wenye kumb. Na. SHC/C.180/2/113. Waraka huu ulihusu maadili ya Watumishi wa Umma katika mfumo wa vyama vingi vya siasa. Waraka huo ulianza kutumika kuanzia Julai 2000 na ulifuta waraka wa mwaka 1992.

Katika waraka huo serikali imeamua kwamba hakutakuwa na makundi mawili ya watumishi kama ilivyokuwa hapo awali, bali watumishi wote wa umma sasa watatawaliwa na masharti yanayofanana. Katika waraka huo serikali pia imeamua kuanisha utaratibu utakaozingatiwa na watumishi wa umma watakaoamua kugombea ubunge kupitia viti maalumu, pamoja na wale walioteuliwa na Rais kwa mujibu wa katiba kuwa wabunge.

Pia mnamo tarehe 22 Aprili mwaka 2002 Mkuu wa Utumishi alitoa Rekebisho Na. 1 lenye kumb. Na. SHC/C.180/2/152 kwa lengo la kuboresha baadhi ya masharti yaliyotolewa na waraka wa mwaka 2000. Marekebisho hayo yalihusu wagombea udiwani, wagombea ubunge wa viti maalum, ubunge wa kuteuliwa na Rais katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wagombea Ubunge katika Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hizi ni nyaraka ambazo si za siri za serikali, ni nyaraka za wazi anazopaswa kupatiwa kila mtumishi wa umma mara anapoajiriwa. Hata hivyo, watumishi wengi wa umma, hawafahamu kuhusu nyaraka hizi na hivyo kuwafanya kutotambua haki, wajibu na mipaka waliyonayo kuhusu ushiriki wao katika siasa ikiwemo za vyama.

Katika mazingira hayo ndipo zipozushwa hisia finyu kuwa watumishi wa umma hawaruhusiwi kushiriki kwenye siasa ama mawazo potofu kwamba watumishi wa umma wanajibika kushiriki kwenye siasa kupitia chama kinachotawala pekee. Hii ni changamoto kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais(Utumishi wa Umma), Hawa Ghasia, kuweza kutumia njia zote kuhakikisha waraka huu unafahamika kwa watumishi wa umma na wadau wengine wa siasa wakiwemo wananchi.

Kila mtumishi wa umma ni muhimu akahakikisha anafahamu waraka huu ambao madhumuni yake ni kuweka utaratibu ambao pamoja na masharti yake, unazingatia umuhimu wa kuendelea kuwa watumishi wa umma nafasi ya kutumia haki ya kikatiba ya kushiriki kwenye siasa. Kwa mtizamo wa serikali, waraka huo unalenga pia kuweka mipaka ili kuepuka madhara yanayoweza kuathiri utendaji wa shughuli za umma.

Kabla ya kufanya mapitio kuhusu yanayoruhusiwa na yasiyoruhusiwa kufanywa na watumishi wa umma katika ushiriki kwenye siasa ni vyema tukapitia kwanza misingi ya utumishi wa umma kwa kadiri ya katiba, sheria, kanuni na taratibu mbalimbali. Hii ni misingi ambayo mataifa mbalimbali wanaitumia katika kuongoza maadili ya watumishi wa umma.

Ikumbukwe kwamba watumishi wa umma ni waajiriwa wote kamili wa serikali na taasisi zake. Hii inajumuisha Rais, Mawaziri, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa halmashauri na Mashirika ya umma, watendaji wa kata nk. Orodha hii inahusisha pia waajiriwa wa kawaida wa serikali mathalani walimu wa shule za umma, watumishi wa sekta ya afya wa serikali, maofisa wote waajiriwa wa halmashauri/serikali za mitaa nk. Watumishi wa umma ni pamoja pia watumishi wa mihimili mingine ya serikali kama mahakama kwa maana ya majaji na mahakimu na Bunge kwa maana ya wabunge na watumishi wa bunge. Watumishi wa umma ni pamoja na wafanyakazi wa vyombo vya ulinzi na usalama wakiwemo askari wa majeshi mbalimbali.

Hawa wote wanapaswa kutekeleza wajibu wao kama watumishi wa umma bila kufanya upendeleo wala ubaguzi wa chama chochote cha siasa. Wanapaswa kuwa na utii kwa serikali ya chama kinachotawala kwa kutekeleza kwa dhati na kwa ufanisi sera za serikali. Wanapaswa kutoshiriki katika mambo ya siasa yanayozuia utendaji mzuri katika vyombo vya umma(hii haimaanishi kwamba hawaruhusiwi kujiunga na vyama au kushiriki kwenye siasa). Maadili yanawahitaji kutoa huduma kwa misingi ya haki na kufanya kazi kwa hekima na uadilifu. Pia wanawajibika kutunza siri za serikali, serikali za mitaa na taasisi za mashirika ya umma. Na kwa ujumla wanapaswa kuheshimu maadili ya taaluma. Maadili hayo yamefafanuliwa vizuri katika kijitabu cha Maadili ya Utendaji katika utumishi wa umma, Tanzania kilichotolewa na Idara Kuu ya Utumishi Serikalini, mwaka 1998.

Tunaweza kufanya tathmini na kujaza kurasa nyingi za mifano ya ambavyo maadili hayo yamekuwa yakikiukwa na watumishi wa umma wa ngazi mbalimbali kuanzia ya juu kabisa katika taifa mpaka ngazi ya chini. Kuanzia mwaka 2000 waraka huo ulipotolewa taifa limeshuhudia baadhi ya watumishi wa umma wakishiriki katika kufanya ubaguzi na upendeleo wa chama cha siasa, hususani kinachotawala. Imekuwa ni kawaida kusikia wananchi wakiambiwa na watumishi wa umma kwamba mkichagua upinzani mtanyimwa maendeleo ama watumishi wa umma wakilazimishwa kuunga mkono chama kinachotawala kwa vitisho vya kuondolewa katika utumishi wa umma. Aidha ziara za kiserikali za watumishi wa umma zimekuwa zikiingiza masuala ya kisiasa yenye kubagua na kubomoa vyama vingine. Ukiukwaji huu wa maadili umekuwa ukifumbiwa macho na Mkuu wa Utumishi wa Umma, ambaye ni Katibu Mkuu kiongozi.

Aidha suala la utii na kutekeleza sera za chama kinachotawala limezua mzozo baina ya serikali kuu na serikali za mitaa katika maeneo ambayo vyama vinavoongoza ni tofauti. Mathalani, wakati CCM ni chama tawala katika serikali kuu; katika halmashauri ya Karatu, CHADEMA ni chama kiongozi. Sasa kwa kuwa CCM ni chama cha upinzani katika halmashauri hiyo, watumishi wa umma katika halmashauri wanapaswa kuwa na utii kwa serikali ya chama kinachotawala kwa kutekeleza kwa dhati na kwa ufanisi sera za serikali hiyo ya CHADEMA. Hii ni katika masuala ambayo yako chini ya utekelezaji wa halmashauri chini ya mfumo wa mgawanyo wa madaraka baina ya serikali kuu na serikali za mitaa. Watumishi hao watafuata maelekezo ya serikali kuu katika masuala yanayosimamia kiutekelezaji na serikali kuu pekee.

Pamoja na kuwa maadili yanawahitaji watumishi wa umma kutoa huduma kwa misingi ya haki na kufanya kazi kwa hekima na uadilifu katika kipindi hiki umeshuhudiwa ufisadi mkubwa na/ama matumizi mabaya ya madaraka kuanzia uongozi wa juu kabisa wa taifa mpaka ngazi za chini za utumishi wa umma. Badala ya kuwa na utamaduni wa uwajibikaji pamekuwa na mazoea ya ufisadi kwa kisingizio cha ‘kila mbuzi kula kwa kadiri ya urefu wa kamba yake’. Wakati katika kada za juu za utumishi wa umma, hali hii ikichangiwa na ubinafsi katika kada za chini hali hii imechagiwa na mishahara/maslahi duni ya watumishi wa umma. Asili ya yote haya ikiwa ni mmomonyoko wa maadili kwa ujumla wake katika taifa. Mambo haya yanataathira kubwa katika ushiriki wa watumishi wa umma katika siasa na hivyo kuzalisha mfumo mpya wa ushiriki wa watumishi wa umma kwenye siasa wa ‘nipe nikupe’ au ‘ambao ni hatari kwa mwelekeo wa taifa.

Katika mazingira haya ya uozo wa kimaadili ndipo walipozuka baadhi ya watumishi wa umma wenye uzalendo ambao wameamua ‘kukiuka’ maadili ya kutunza ‘siri’ za serikali na kuanza kuvujisha nyaraka za kiserikali za ‘kifisadi’. Ni wazi, hakuna maadili ya utumishi wa umma yanayomtaka mtumishi wa umma kutunza siri ya serikali hata kama ikiwa ni siri ya wizi; kwani ni kosa la jinai kuficha wizi. Suala hili limezua zogo hivi karibuni bungeni mlengwa mkuu wa kuonyooshewa vidole akiwa ni Mbunge wa Karatu, Dr Wilbroad Slaa kutokana na kuwa mstari wa mbele kuzitumia nyaraka kama hizo katika mapambano ya kupinga ufisadi na kutetea rasilimali za Taifa. Ni vyema watanzania wakakumbuka kuwa ni ushiriki wa namna hiyo wa watumishi wa umma wazalendo ndio uliowezesha Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Kaskazini kuibua kashfa ya Buzwagi, na baadaye ikafuatiwa na Dr Slaa kusoma Orodha ya Mafisadi pale Mwembe Yanga Septemba 15 mwaka 2007. Matukio yaliyofuata baada ya hapo yakiwemo ya kuzomewa kwa watumishi wengine wa umma waliokuwa wakizunguka mikoani kukanusha tuhuma hizo za ufisadi kwa kizingizio cha kutetea uzuri wa bajeti ndio yaliyosukuma kuundwa kwa Kamati ya Bomani kuhusu Madini, Kamati Teule ya Bunge Kuhusu Richmond, Kamati Kazi(Task Force) kuhusu fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje(EPA). Kutokana na hayo taifa limeshuhudia baadhi ya watumishi wa umma wakijiuzulu, na wengine wakipelekwa mahakamani. Hata hivyo, iliweke wazi kwamba safari bado ni ndefu hivyo ushiriki wa watumishi wa umma katika siasa ni jambo linalohitaji mjadala endelevu. Hivyo katika makala ijayo tutafanya mapitio ya mambo ambayo yanaruhusiwa kufanywa kwa uwazi kabisa na watumishi wa umma wanaopenda kushiriki kwenye siasa.

Mwandishi wa Makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje(CHADEMA) anapatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.net na http://mnyika.blogspot.com




“Ruksa” kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-2

“Ruksa” kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-2


Na John Mnyika

Katika makala iliyopita tulijibu swali nani ni ‘mtumishi wa umma’, tukadokeza uzoefu kutoka mataifa mbalimbali kuhusu namna ambavyo watumishi wa umma wanaweza kushiriki katika siasa. Kadhalika, makala iligusia ushiriki wa watumishi wa umma katika siasa kuanzia mwaka 1965 mpaka 1992 wakati huo nchi ikiwa katika mfumo wa siasa wa chama kimoja. Katika makala hii tutaangalia ushiriki wa watumishi wa umma katika siasa katika kipindi cha awali cha mfumo wa vyama vingi kuanzia mwaka 1992 mpaka mwaka 2000.

Ni muhimu kusisitiza kuwa wakati tunatafakari namna ambayo watumishi wa umma wanavyoweza kujihusisha na vyama vya siasa kwa sasa na kuwa wakala wa mabadiliko wanayotaka kuyaona, ni muhimu kama taifa tukakumbuka ushiriki wao katika wakati uliopita na taathira yake katika demokrasia katika wakati huu. Hii itawezesha kuchukua maamuzi thabiti ya kuweka mwelekeo mwafaka wenye kujenga katika mafanikio ya zamani na wakati huo huo kutibu majeraha ya kisiasa, kijamii na kiuchumi yaliyotokana na hodhi ya chama kimoja ambao sasa taifa linadhamiria kuondokana nao.

Kufuatia mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yaliyofanyika Julai, 1992 na kuruhusu mfumo wa vyama vingi vya siasa kurejea Tanzania, Serikali ilitoa maelekezo ya jinsi watumishi wa umma watavyoshiriki katika mambo ya Siasa kupitia waraka wa Utumishi wa Umma Na. 1 wa mwaka 1992. Waraka huu uliotolewa wakati wa Urais wa Mzee Ali Hassan Mwinyi, maarufu kama “Ruksa”. Na wa kweli waraka huo ulitoa ruksa pana ya ushiriki wa watumishi wa umma katika siasa ukilinganisha na waraka uliofuatia ambao tutaurejea katika makala inayofuata.

Utaratibu uliotolewa na waraka huo uliwagawa watumishi wa umma katika makundi mawili na kuweka masharti ya namna watavyoshiriki katika siasa. Watumishi wa kundi “A” walijumuisha Watumishi wa ngazi za juu wa Serikalini, Serikali za Mitaa na Katika Mashirika ya Umma wanaoshughulikia uandaaji na usimamizi wa sera. Hawa walikuwa ni watumishi waandamizi kwenye madaraka kuanzia ngazi za mkurugenzi na kuendelea juu, Meneja Msaidizi na kuendelea juu na ngazi ya Mkurugenzi Mtendaji. Watumishi wa Kundi “B” walijumuisha watumishi wa ngazi za chini na kati ambao hawahusiki na maandalizi ya sera mbalimbali.

Chini ya waraka Na. 1 wa mwaka 1992 watumishi katika kundi “A” na “B” walipewa masharti kuhusu mambo wanayoruhusiwa kufanya na wasiyoruhusiwa kufanya kuhusu ushiriki wao katika siasa ikiwemo za vyama.

Waraka huu uliotoa mwanya wa watumishi wa umma kushiriki katika siasa hususani kupitia uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 na pia chaguzi za Serikali za Mitaa zilizofanyika katika ngazi za Mitaa, Vitongoji na Vijiji mwaka 1994 na 1999.

“Ruksa” iliyotolewa na waraka huo iliotoa uhuru wa watumishi wa umma kushiriki katika masuala ya siasa na kwa kiasi kikubwa watumishi wengi wa umma wakati huo walijitokeza kuunga mkono vyama vya siasa; hususani vya upinzani. Harakati hizo za watumishi wa umma kushiriki siasa wakati huo pamoja ni moja ya sababu zilizochangia upinzani kupata viti vingi bungeni katika uchaguzi wa mwaka 1995 ukilinganisha na chaguzi zote zilizofuata.

Hata hivyo, baada ya chaguzi hizo serikali ilionyesha dhahiri kutoridhishwa na hali hiyo na kueleza kwamba ‘ruksa’ hiyo ya watumishi wa umma kushiriki kwenye siasa ‘imeathiri maadili ya msingi ya utendaji kazi serikalini na vyombo vyake”.

Ilipofika mwanzoni mwa mwaka 2000, wakati taifa likiwa linajiandaa na uchaguzi mkuu wa pili chini ya mfumo wa vyama vingi serikali ya wakati huo chini ya Urais wa Benjamin Mkapa ilieleza kutoridhishwa na kiwango cha ‘ruksa’ ambayo watumishi wa umma wamepewa kushiriki katika siasa.

Serikali ikaeleza kwamba uhuru ambao watumishi wa umma wapewa kushiriki kwenye siasa unafanya baadhi yao kutotekeleza kwa dhati sera za chama tawala. Kadhalika serikali ikalalamika kwamba wapo watumishi wa umma wanaoikashifu serikali kufuatana na msimamo wa kisiasa. Pia yalikuwepo malalamiko ya pande zote kuhusu athari za kujihusisha na masuala ya siasa mahali pa kazi na wakati wa saa za kazi. Baadhi ya watumishi wa umma pia walilalamikiwa kwa kutoa huduma za kiutumishi kwa upendeleo unaotokana na msimamo wa kisiasa. Kwa upande mwingine, waliokuwepo pia watumishi wa serikali kuu waliojitokeza kugombea nafasi za uongozi/siasa katika serikali za mitaa jambo ambalo lilikwenda kinyume na dhana ya utenganishaji wa madaraka kati ya watungaji wa sera ambao ni viongozi wenye mwelekeo wa kisiasa na wale watekelezaji wa sera ambao kwa kawaida wanatakiwa kuwa watendaji.

Aidha palikuwepo na utata kuhusu mgawanyo wa watumishi katika makundi “A” na “B” kutokana na vigezo kutokuwa wazi na kutoeleweka vizuri hivyo wakati mwingine ulizua mkanganyiko juu ya mtumishi yupi yupo katika kundi lipi.

Kwa kiasi kikubwa baadhi ya kasoro zilichangiwa na ombwe na udhaifu iliokuwepo kwenye waraka wenyewe. Kwa mfano mbali na makundi ambayo nimeyadokeza hapo juu kuna makundi ya watumishi wa umma ambao hawakuorodheshwa kabisa katika waraka lakini kwa mujibu wa katiba wametajwa. Hawa ni watumishi ambao katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza wazi kwamba hawaruhusiwi kuwa wanachama wa chama chochote cha siasa. Hawa ni watumishi wa umma ambao ruksa yao pekee ya kushiriki kwenye vyama vya siasa ni ya kupiga kura. Ni kundi la watumishi wa umma ambao hawaruhusiwi kushiriki katika shughuli zozote zingine za kisiasa isipokuwa kupiga kura tu. Ibara ya 147(3) na (4) ya Katiba imewataja Askari wa Jeshi la Wananchi(JWTZ), Jeshi la Kujenga Taifa(JKT), Polisi na Magereza. Pia Ibara ya 113A imewakataza majaji na mahakimu wa ngazi zote. Kadhalika Ibara 74(14) na (15) imewazuia wajumbe na watumishi wa Tume ya Uchaguzi na Wasimamizi wa Uchaguzi.

Kasoro nyingine ya waraka huo ilikuwa ni kutoyaraja makundi mengine ambayo pamoja ni kuwa hayajakatazwa na katiba kushiriki kwenye shughuli za kawaida za kisiasa lakini kwa mujibu wa kazi zao wanapaswa kushiriki kwa kupiga kura tu. Mathalani, watumishi wa idara ya usalama wa taifa, taasisi ya kuzuia rushwa(wakati huo), msajili wa vyama vya siasa, watumishi wa ofisi ya bunge na mawakili wa serikali.

Kutokana na hali hiyo, ilipofika Mwezi Juni mwaka 2000 serikali ilitangaza kufuta waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma Na. 1 wa Mwaka 1992 na kutoa waraka mwingine kuhusu maadili ya watumishi wa umma katika mfumo wa vyama vingi vya siasa ambao tutaufanyia mapitio kuanzia makala inayofuata. Sababu kuu iliyopelekea serikali kufikia maamuzi hayo ni kile kilichoelezwa kuwa ni ‘vitendo vya watumishi wa umma vinavyokiuka maadili ya utumishi wa umma kwa kisingizio cha uhuru uliotolewa wa kushiriki katika mambo ya siasa’.

Hata hivyo kwa watetezi wa demokrasia na maendeleo waraka huo wa mwaka 1992 ulionekana kuwa na udhaifu wa msingi wa kimaudhui na kimaadili. Waraka huo haukuweza kuviruka viunzi vya kikatiba na kisheria ambavyo vilikuwepo ambavyo vimeendeleza fungamano kati watumishi wa umma, chama kinachotawala na serikali ikiwemo vyombo vya dola na hivyo kuathiri ushindani wa kisiasa. Ikumbukwe kwamba mapendekezo ya Tume ya Nyalali ya mwaka 1991 na marekebisho ya Katiba ya mwaka 1992 kuingia katika mfumo wa vyama vingi na marekebisho ya sheria yaliyofuata yameweza kupunguza kwa kiasi hali hiyo.

Lakini bado fungamano kati ya chama tawala na serikali ikiwemo vyombo vya dola linahitaji kuendelea kujadiliwa ili mabadiliko ya kweli yaweze kufanyika. Mabadiliko hayo ya kikatiba, kisheria na kimitazamo yatawezesha kuwa na tunu za kitaifa, misingi kamili ya haki za raia, mifumo ya uwajibakaji wa viongozi na uwanja sawa wa kisiasa. Mabadiliko hayo yatawezesha pia kujenga taasisi za kitaifa, uongozi bora na dira ya pamoja yenye kuunganisha nguvu za umma katika kupambana na ufisadi, kutetea rasilimali na kusimamia fikra mbadala zenye kujenga taifa lenye kutoa fursa kwa wote. Taifa wananchi wanaweza kuneemeka na uwezo ambao wamejaliwa wao na nchi kwa ujumla. Sehemu ya wananchi hao ambao ushiriki wao kwenye siasa unapaswa kuwa wa maana na wenye manufaa ni watumishi wa umma.


Mwandishi wa Makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje(CHADEMA) anapatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.net na http://mnyika.blogspot.com

‘Ruksa’ kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-1



‘Ruksa’ kwa watumishi wa umma kushiriki siasa-1


Na John Mnyika

Kati ya maswali na masuala ambayo watumishi wengi wa umma wamekuwa wakijiuliza ama kuyatakakari baada ya kuanza kwa mfumo wa vyama vingi ni haki, wajibu na mipaka yao katika kujihusisha na siasa zikiwemo za vyama. Aidha majibu mepesi ya maswali hayo yamekuwa ni hisia finyu kuwa watumishi wote wa umma hawapaswi kujihusisha na vyama vya siasa. Ama kwa kwa upande mwingine yamekuwepo pia mawazo potofu kwamba watumishi wa umma wanapaswa kujihusisha na chama kinachotawala pekee na hawapaswi kabisa kujihusisha na vyama vya upinzani. Makala hii itachambua suala hili mintaarafu Waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma kuhusu maadili ya watumishi wa umma katika mfumo wa vyama vingi kwa kurejea pia sheria na kanuni zinazohusika.

Utumishi wa umma katika nchi yetu unaongozwa na Sheria ya Utumishi Serikalini namba 16 ya mwaka 1989 na Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma Toleo la 1994 pamoja na marekebisho yake. Kwa madhumuni ya makala hii Neno Mtumishi wa Umma lina maana kama iliyoanishwa katika Kanuni za kudumu za utumishi kifungu Na. A.1(66) ambacho kinatafsiri mtumishi wa umma kama mtu yoyote anayeshikilia ofisi ya umma ambayo imepewa mamlaka ama inatekeleza wajibu wenye asili ya umma, iwe chini ya utawala wa moja kwa moja wa Rais au la. Na inajumuisha maofisa walio chini ya Serikali za Mitaa ama Mashirika ya umma; lakini haijumuishi wanaoshikilia nafasi hizo kwa sehemu ya muda wa ziada(Part Time basis).

Kwa mantiki hiyo, tafsiri hii inafanya wafanyakazi wote wa serikali na taasisi zake kuwa ni watumishi wa umma. Hii inajumuisha Rais, Mawaziri, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa halmashauri na Mashirika ya umma, watendaji wa kata nk. Orodha hii inahusisha pia waajiriwa wa kawaida wa serikali mathalani walimu wa shule za umma, watumishi wa sekta ya afya wa serikali, maofisa wote waajiriwa wa halmashauri/serikali za mitaa nk. Watumishi wa umma ni pamoja pia watumishi wa mihimili mingine ya serikali kama mahakama kwa maana ya majaji na mahakimu na Bunge kwa maana ya wabunge na watumishi wa bunge. Watumishi wa umma ni pamoja na wafanyakazi wa vyombo vya ulinzi na usalama wakiwemo askari wa majeshi mbalimbali. Ukiitafakari orodha hii ndefu utaona kwamba jambo hili linahusu watu wengi; hivyo suala la ushiriki wao katika siasa katika mfumo wa vyama vingi linapaswa kutafakariwa na kujadiliwa na umma.

Uzoefu katika nchi mbalimbali duniani unaonyesha kuwa ziko njia mbalimbali za watumishi wa umma kuweza kujihusisha na vyama vya siasa. Njia iliyozoeleka zaidi ni ile ya kushiriki katika kupiga kura ama kuweza kushiriki katika kupigiwa kura kwa maana ya kugombea. Kushiriki katika kupiga kura kunaweza kuwa ni katika kupiga kura za kuchagua viongozi wa umma wa kiserikali ama kupiga kura katika kuchagua viongozi wa ndani ya chama. Kwa upande wa kugombea nayo inaweza ikawa katika chaguzi za kiserikali ama kugombea katika nafasi za uongozi za ndani ya chama cha siasa. Katika hali hiyo, njia nyingine ya watumishi wa umma kujihusisha na vyama vya siasa ni kwa kuwa wanachama wa vyama hivyo. Aidha katika nchi ambazo demokrasia imeendelea, ushiriki wa watumishi wa umma katika vyama vya siasa na siasa kwa ujumla unahusisha ushiriki wao katika kupiga kura kuhusu masuala mbalimbali(issue voting) mathalani kura za maoni(referendum). Pia, watumishi wa umma wanaweza kujihusisha kwa kutoa maoni na mitazamo yao kuhusu masuala mbalimbali ya kisiasa na yanayohusu vyama vya siasa kwa kutumia njia mbalimbali.

Kuanzia mwaka 1965 hadi 1992 Tanzania ilipokuwa na mfumo wa siasa wa chama kimoja kundi lote hili la watumishi wa serikali na vyombo vyake siyo tu waliruhusiwa bali ilionekana ni wajibu wao kushiriki katika mambo ya kisiasa. Shughuli nyingi za kiserikali na za kisiasa zilikwenda kwa pamoja na palikuwepo na maingiliano makubwa kati ya sehemu hizi mbili katika shughuli zote za kiutendaji, kiuongozi na kiitikadi.

Na kwa kweli suala hili lilianza mara baada ya uhuru kabla hata ya nchi kutangaza kuingia katika mfumo wa chama kimoja. Mathalani, baada ya Maasi ya Jeshi ya mwaka 1964 uamuzi wa Rais wa Kwanza Hayati Mwalimu Nyerere wa kulisuka upya jeshi ambalo lilirithiwa toka kwa mkoloni, kuunda jeshi la wananchi wa Tanzania ulihusisha fungamano la kipekee baina ya Jeshi na Chama tawala. Wakati ule, sehemu kubwa ya wanajeshi ilichaguliwa kutoka vijana wa chama TANU. Hodhi hii iliendelezwa zaidi chini ya mfumo wa chama kushika hatamu ambao ulioweka mahusiano ya karibu baina ya chama kinachotawala na serikali ikiwemo vyombo vyake vya dola. Ni fungamano hili kati ya watumishi wa umma wa kada zote, na chama ndio uliofanya chama kinachotawala kuwa chama dola; suala lenye athari mpaka hivi sasa hususani katika nyakati za uchaguzi.

Mapendekezo ya Tume ya Nyalali ya mwaka 1991 na marekebisho ya Katiba ya mwaka 1992 kuingia katika mfumo wa vyama vingi na marekebisho ya sheria yaliyofuata yameweza kupunguza kwa kiasi hali hiyo. Lakini bado fungamano kati ya chama tawala na serikali ikiwemo vyombo vya dola linahitaji kujadiliwa ili mabadiliko ya kweli yaweze kufanyika. Mabadiliko hayo ya kikatiba, kisheria na kimitazamo yatawezesha kuwa na tunu za kitaifa, misingi kamili ya haki za raia, mifumo ya uwajibakaji wa viongozi na uwanja sawa wa kisiasa. Mabadiliko hayo yatawezesha pia kujenga taasisi za kitaifa, uongozi bora na dira ya pamoja yenye kuunganisha nguvu za umma katika kupambana na ufisadi, kutetea rasilimali na kusimamia fikra mbadala zenye kujenga taifa lenye kutoa fursa kwa wote. Taifa wananchi wanaweza kuneemeka na uwezo ambao wamejaliwa wao na nchi kwa ujumla.

Wakati tunapoanza kutafakari namna ambayo watumishi wa umma wanavyoweza kujihusisha na vyama vya siasa kwa sasa na kuwa wakala wa mabadiliko wanayotaka kuyaona, ni muhimu kama taifa tukakumbuka ushiriki wao katika wakati uliopita na taathira yake katika demokrasia katika wakati huu. Hii itawezesha kuchukua maamuzi thabiti ya kuweka mwelekeo mwafaka wenye kujenga katika mafanikio ya zamani na wakati huo huo kutibu majeraha ya kisiasa, kijamii na kiuchumi yaliyotokana na hodhi ya chama kimoja ambayo sasa taifa linadhamiria kuondokana nao.

Mwandishi wa Makala hii ni Mkurugenzi wa Mambo ya Nje(CHADEMA) anapatikana kupitia 0754694553, mnyika@chadema.net na http://mnyika.blogspot.com