Monday, March 25, 2013

Mnyika na harakati za kuhakikisha Maji ndani ya Jimbo la Ubungo

21 Machi, 2013 Mnyika aitwa Ikulu, JK awakumbuka Mabwepande
na Asha Bani

HOJA ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA) kuhusiana na suala la tatizo la upatikanaji wa maji katika Mkoa wa Dar es Salaam, inaelekea kupata ufumbuzi kutokana na Rais Jakaya Kikwete kumuita Ikulu mbunge huyo Jumatatu wiki ijayo.

Wengine walioitwa kukutana na rais ni Mkuu wa Mkoa, Mecky Sadick, wakuu wote wa wilaya pamoja na wabunge na wataalamu kutoka Wizara ya Maji.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika uzinduzi wa daraja la Mtaa wa Golani, Kata ya Saranga, Rais Kikwete alisema kuwa kutokana na wananchi wa kata hiyo kupiga kelele kuhusiana na suala la maji ameamua kukutana na viongozi hao ili kupatiwa ufumbuzi.

Mwaliko wa kushiriki ufuatiliaji wa mradi wa maji na mkutano wa mbunge na wananchi katika kilele cha wiki ya maji kitaifa na siku ya maji kimataifa leo tarehe 22 Machi Mtaa wa Makoka kata ya Makuburi.

Leo tarehe 22 Machi ni kilele cha wiki ya maji kitaifa na siku ya kimataifa ya maji. Katika kazi zake ikiwa ni sehemu ya siku hiyo Mbunge wa Ubungo John Mnyika saa 9 alasiri atakuwepo eneo la Uluguruni Mtaa wa Makoka Kata ya Makuburi kufanya ufuatiliaji wa mradi wa maji.

Mradi umetekelezwa kwa ushirikiano na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) baada ya kuchochewa kwa kuchangiwa milioni kumi na Mfuko wa Maendeleo (CDCF) Jimbo la Ubungo ambao Mnyika ni mwenyekiti wake pamoja na kuunganisha nguvu za wananchi katika maeneo husika.

Aidha, baada ya kukagua mradi huo kuanzia saa 10 Jioni mbunge atafanya mkutano na wananchi kwa ajili ya kutoa ujumbe kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jiji la Dar Es Salaam zinazopaswa kuchukuliwa hata baada ya wiki ya maji.

Pia kufuatia mwaliko wa Rais Jakaya Kikwete wakukutana tarehe 25 Machi 2013 na Mkuu wa Mkoa, DAWASA, DAWASCO, Mnyika na wabunge wengine wa Mkoa wa Dar es Salaam kujadili hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji, mbunge atatumia mkutano wake na wananchi kusikiliza maoni na mapendekezo kuhusu hatua za ziada zinazopaswa kuchukuliwa.

Imetolewa tarehe 22 Machi 2013 na: 

Gaston Shundo 

Afisa katika Ofisi ya Mbunge Ubungo

Picha za Uzinduzi wa Daraja la Suka-Golani!

















Tujikumbushe harakati na jitihada mbalimbali ambazo zilifanywa mpaka kufikia hatua ya sasa kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora ya miundombinu ya barabara ya Suka-Golani hapa:

1 May, 2012  Daraja Golani-Suca na Barabara Mburahati-Mabibo

Mkandarasi aliyepewa zabuni ya ujenzi wa daraja la Golani-Suka anapaswa kuanza mapema ujenzi wa daraja hilo muhimu linalounganisha kata za Kimara na Saranga ili kupunguza kero kwa wananchi hasa wakati wa mvua.

Mwezi huu wa Aprili nimefuatilia kuhusu hatma ya daraja hilo na hatimaye mkataba wa ujenzi wa daraja husika umesainiwa kati ya Manispaa ya Kinondoni na Mkandarasi Kika Co. Ltd kwa gharama za shilingi milioni 447.

Hata hivyo, ujenzi wa daraja husika haujaanza suala ambalo linahitaji Manispaa ya Kinondoni kumsimamia kwa karibu mkandarasi husika ili ujenzi uanze kwa haraka kwa kuwa mchakato wa zabuni ulianza kuanzia mwanzoni mwa mwaka 2012.

Izingatiwe kwamba kutokuwepo kwa daraja katika eneo hilo mwaka miaka mingi kumefanya mawasiliano katikati maeneo hayo kuwa magumu nyakati za mvua na kusababisha madhara ya kibinadamu na mali wananchi wanapovuka mto katika eneo hilo wakati wa mafuriko.

Baada ya kuwawakilisha wananchi kutaka ujenzi wa daraja hilo lilingizwa kwenye bajeti ya Manispaa ya Kinondoni kwa mwaka wa fedha 2011/2012 hata hivyo miezi ikiwa imebaki takribani miwili kabla ya mwisho wa bajeti husika ujenzi wa daraja hilo ulikuwa haujaanza bado.

Hatua kama hiyo inahitajika pia kwa barabara ya Mburahati mpaka Mabibo NIT ambayo inapaswa kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami ikiwa imetengewa kiasi cha shilingi milioni 504 kwa ajili ya kuchangia katika kupunguza msongamano wa magari katika barabara ya Morogoro . 

Tathmini ya utekelezaji wa bajeti inaonyesha kwamba kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ni ndogo pengo ambalo linapaswa kuzibwa kwa kusimamia kwa karibu miradi inayopaswa kuanza katika muhula uliobaki wa mwaka wa fedha 2011/2012.

Rejea: http://mnyika.blogspot.com/2012/05/daraja-golani-suca-na-barabara.html 


January 27, 2012 Kuhusu Msongamano wa Magari DSM na Ziara Kwembe: http://mnyika.blogspot.com/2012/01/kuhusu-msongamano-wa-magari-dsm-na.html

Thursday, March 21, 2013

MNYIKA ATAKA KAULI YA RAIS KIKWETE KUHUSU UJENZI WA MACHINGA COMPLEX NA JUMBA LA VIWANDA VIDOGO JIMBONI UBUNGO

Mbunge wa Jimbo la Ubungo John Mnyika ametoa mwito kwa Rais Jakaya Kikwete kueleza sababu za kutokutekelezwa mpaka sasa kwa ahadi zake alizotoa mwaka 2010 za ujenzi wa Machinga Complex na jumba la viwanda vidogo katika jimbo hilo kuchangia katika kupanua wigo wa ajira kwa vijana. 

Mnyika aliyasema hayo akijibu swali la mwakilishi wa vijana katika mkutano wake na wananchi alioufanya katika ofisi za Serikali ya Mtaa wa Muungano katika kata ya Manzese uliofanyika mwishoni mwa wiki (16/03/2013). 

Mwakilishi huyo wa vijana alitaka kufahamu hatua ambazo mbunge amechukua kufuatilia kuhusu maeneo ya kufanyia biashara kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo katika jimbo la Ubungo. 

“Kazi ya mbunge ni kuwawakilisha wananchi na kuisimamia serikali ili kuwezesha utatuzi wa kero, matatizo ya maeneo ya wafanyabiashara ndogo ndogo yamedumu kwa muda mrefu kutokana na udhaifu katika mipango miji na hivyo maeneo ya wafanyabiashara na masoko kuuzwa, kuvamiwa au kuwa machache. Nimefuatilia suala hili, kuna ambao wamepata maeneo na wengine wengi bado”, alijibu Mnyika.

Wednesday, March 20, 2013

RUFAA DHIDI AGIZO LA ACP CHARLES KENYELA KAMANDA WA POLISI WA MKOA WA KIPOLISI WA KINONDONI KUZUIA MKUTANO WA HADHARA WA MBUNGE NA WANANCHI TAREHE 16 MACHI 2013



Kumb. Na. OMU/US/003/2013                                                                                               18/03/2013 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,
S.L.P 9223, 
Dar es Salaam. 

Mheshimiwa: 


RUFAA DHIDI AGIZO LA ACP CHARLES KENYELA KAMANDA WA POLISI WA MKOA WA KIPOLISI WA KINONDONI KUZUIA MKUTANO WA HADHARA WA MBUNGE NA WANANCHI TAREHE 16 MACHI 2013 


Kwa barua hii nawasilisha rasmi rufaa kwa kutumia kifungu cha 43 (6) cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma za Polisi wasaidizi sura ya 322 (The Police Force and Auxilliary Service Act Cap 322 RE 2002) dhidi ya agizo la ACP Charles Kenyela Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni kuzuia mkutano wa hadhara wa mbunge na wananchi tarehe 16 Machi 2013. 

Katika kushughulikia rufaa hii zingatia kuwa tarehe 4 Machi 2013 niliwasilisha taarifa kwake kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha Sheria ya Kinga, Madaraka na Haki za Bunge na. 3 ya mwaka 1988 (The Parliamentary Immunities, Powers and Privileges Act) kuwa tarehe 16 Machi 2013 nilipanga kufanya mkutano na wananchi Jimboni. 

Katika taarifa hiyo kupitia barua yangu yenye Kumbu. Na. OMU/US/001/2013 ambayo nilitoa pia nakala kwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Afisa Tawala wa Wilaya ya Kinondoni, Afisa Mtendaji wa Kata ya Manzese na Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Muungano, nilieleza kwamba mkutano huo nilipanga kuufanya katika Kata ya Manzese Eneo la Bakheresa kuanzia saa 3 asubuhi mpaka saa 5 Asubuhi. 

Katika taarifa hiyo nilieleza kwamba lengo la mkutano huo ni kuwapa mrejesho wananchi kuhusu masuala niliyoyawasilisha katika Mkutano wa Kumi wa Bunge uliomalizika tarehe 08 Februari 2013 na kupokea mambo ya kuyazingatia kuelekea Mkutano wa Kumi Na Moja wa Bunge unaotarajiwa kuanza tarehe 9 Aprili 2013. 

Hata hivyo, kupitia mkutano wake na vyombo vya habari tarehe 14 Machi 2013 na barua yake iliyoletwa ofisini kwangu tarehe 15 Machi 2013, ACP Charles Kenyela Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni alitoa agizo la kuzuia mkutano wa hadhara wa mbunge na wananchi niliopanga kuufanya tarehe 16 Machi 2013. 

Katika agizo hilo alilolitoa chini ya kifungu cha 43 (2) na 43 (3) Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma za Polisi sababu iliyohusu mkutano kwa mujibu wa barua yake yenye Kumb. Na. DSM/KINONDONI/SO.7/2/CHADEMA/284 ni: 

“Eneo la Manzese Bakhresa ambalo unakusudia kufanyia mkutano siyo eneo halali kwa ajili ya mikutano. Eneo hilo kwa mujibu wa maelekezo ya Manispaa ya Kinondoni kupitia mipango miji ni eneo linalotumika kwa ajili ya kuegesha magari makubwa (malori) na ndio maana liko katika eneo kuu la barabara ya Morogoro ambayo iko katika matengenezo. Kuruhusu mkutano wako kufanyikia hapo ni kukiuka sheria ya mipango miji ya Manispaa ya Kinondoni pamoja na kuingilia shughuli za ujenzi wa barabara unaoendelea hivi sasa na kuwabugudhi watumiaji wengine wa eneo hilo”.

Tuesday, March 19, 2013

LEO NDIO MWISHO; OMBA UWAKILISHI KWENYE MABARAZA YA KATIBA SASA

Leo tarehe 20 Machi 2013 ni siku ya mwisho ya wananchi kuwasilisha maombi ya kuwa wajumbe wa mabaraza ya katiba ya ngazi ya wilaya ambayo yana wajibu muhimu wa kupitia rasimu ya katiba na kutoa maoni iwapo imezingatia maoni ya wananchi yaliyokunywa katika hatua ya wananchi binafsi na makundi mbalimbali katika jamii. 

Nawakumbusha ambao bado hamjawasilisha maombi na mna dhamira ya kutimiza wajibu huu wa kiraia na kikatiba kwa kuwasilisha barua ya maombi kwa watendaji wa mitaa/vijiji. 

Kuna nafasi nane kwa kila mtaa kwa Dar es salaam, nne kwa maeneo mengine ya Tanzania Bara katika makundi yafuatayo; mwanamke, kijana, mtu mzima na mtu mwingine yoyote: kwa Zanzibar tatu kwa kila shehiya. 

Sifa ni raia, miaka 18 au zaidi mwenye kujua kusoma, kuandika, hekima, busara, uadilifu, uwezo wa kujieleza na kupambanua mambo ambao najua wengi mnazo. Sifa nyingine ni kuwa mkazi wa kudumu kwenye mtaa au kijiji ambayo haimaanishi kwamba ni lazima uwe mwenye nyumba, hata wapangaji mnaruhusiwa kuomba. Sio lazima uwe mwanachama wa chama chochote cha siasa na uteuzi wa awali utafanywa na mkutano mkuu wa mtaa wenu au kijiji chenu ambao wajumbe ni wakazi wote wa mtaa/kijiji husika. 

Tuesday, March 5, 2013

TUTAFANYA MAANDAMANO KWENDA WIZARA YA MAJI TAREHE 16 MACHI 2013; NIMESHAWASILISHA NOTISI, TUENDELEE NA MAANDALIZI

Tarehe 16 Machi 2013 nitaongoza maandamano ya amani ya wananchi kwenda kwa Waziri wa Maji kusimamia uwajibikaji kuwezesha hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es salaam.

Wote mlioshiriki mkutano wa tarehe 10 Februari 2013 (Kwa wale ambao hamkushiriki mnaweza kutazama video hii: http://www.youtube.com/watch?feature=player_embedded&v=O0txSoHqfGY ) , mtakumbuka tulimpa wiki mbili Waziri kujitokeza kwa wananchi kujibu hoja alizokwepa kujibu bungeni.

Tutakusanyika kata ya Manzese eneo la Bakhresa (jirani na daraja) saa 5 asubuhi na tutapita barabara ya Morogoro kuelekea kata ya Ubungo zilipo ofisi za Wizara ya Maji kufuatilia majibu ya ukweli na ukamilifu kuhusu hatua tisa za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka nilizopendekeza kwa niaba ya wananchi bungeni kupitia hoja binafsi na masuala mengine ambayo wananchi watataka yatolewe majibu siku hiyo.

Kila mmoja anaweza kuendelea na maandalizi ya kushiriki kwa kuwa tayari tarehe 4 Machi 2013 nimewasilisha notisi kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni na Maafisa wa Polisi Wasimamizi wa Maeneo kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 43 cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma Saidizi Sura ya 322 (The Police Force and Auxiliary Service Act, Chapter 322).

Sunday, March 3, 2013

WAZIRI MKUU PINDA AINGILIE KATI; WIZARA NA TANESCO HAWAJAJIBU UKWELI KUHUSU MGAWO WA DHARURA WA UMEME

Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kwa nyakati mbalimbali kati ya tarehe 28 Februari na 2 Machi 2013 kupitia baadhi ya vyombo vya habari wametoa majibu yasiyokuwa ya kweli juu ya mgawo wa dharura wa umeme uliotokea mwezi wa Februari. 

Katibu Mkuu wa Wizara Eliackim Maswi na Afisa Habari wa TANESCO Badra Masoud wote wameeleza kwamba hakukuwa na mgawo wa umeme bali kilichotokea ni matatizo madogo madogo ya mitambo na kwamba matengenezo yanaendelea. 

Kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini ninazo taarifa kwamba ukweli ni kuwa umetokea mgawo wa umeme wa dharura kutokana na upungufu zaidi wa kina cha maji katika mabwawa ya kufua umeme, upungufu wa fedha za kununua mafuta mazito ya kuendesha mitambo ya kufua umeme wa dharura na upungufu wa gesi asili ya kuendeshea mitambo ya kufua ya umeme. 

Hivyo, Waziri Mkuu Mizengo Pinda anapaswa kuingilia kati kuwaeleza ukweli wananchi ikiwemo hatua zilizochukuliwa kuhakikisha kwamba hali hiyo haiendelei mwezi Machi kinyume na ahadi iliyotolewa bungeni tarehe 28 Julai 2012 kwamba mgawo wa umeme ungekuwa historia. 

John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini 

02 Machi 2013

Saturday, March 2, 2013

WANANCHI OMBENI UJUMBE WA MABARAZA YA KATIBA LAKINI PINGENI ‘MIANYA YA UCHAKACHUAJI’ WA UTEUZI KWENYE KATA ILIYOWEKWA NA MUONGOZO ULIOTOLEWA NA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA BILA KUZINGATIA MAONI YA WADAU

Mwongozo kuhusu Muundo, Utaratibu wa kuwapata wajumbe wa mabaraza ya Katiba ya Wilaya (Mamlaka za Serikali za Mitaa) na uendeshaji wake uliotangazwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba haujazingatia maoni ya msingi yaliyotolewa na wadau mbalimbali ikiwemo Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). 

CHADEMA inawatahadharisha wananchi kuhusu ‘mianya ya uchakachuaji’ iliyotolewa na muongozo huo kwa kuzingatia kuwa ‘uchakachuaji’ wa uteuzi wa wajumbe wa mabaraza ya katiba, ni ‘uchakachuaji’ wa utoaji maoni kwenye mabaraza ya katiba, ambayo ni hatua ya awali ya ‘uchakachuaji’ wa rasimu ya katiba. 

Kwa mujibu wa Muongozo huo, ‘mianya ya uchakachuaji’ imeachwa kwenye ngazi ya kamati ya maendeleo ya kata ambayo wajumbe wake ni madiwani na wenyeviti wa mitaa/vijiji ambao kwa mujibu wa matokeo ya chaguzi za mwaka 2009 na 2010 kuna hodhi kwenye vikao hivyo ya chama kimoja (CCM).

Friday, March 1, 2013

RUFAA DHIDI YA UENDESHAJI WA BUNGE USIOKUWA WA HAKI NA UKIUKAJI WA KANUNI WA NAIBU SPIKA JOB NDUGAI KATIKA KUONDOA HOJA BINAFSI YA MAJI

Tarehe 28 Februari 2013 nimewasilisha rasmi rufaa kwa mujibu wa Kanuni ya 5 (4) dhidi ya uendeshaji wa Bunge usiokuwa wa haki wa Naibu Spika Job Ndugai kwa kukiuka kanuni ya 58 (5) kwa kulihoji bunge kinyume na kanuni kufanya uamuzi badili wa kuondoa hoja binafsi kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jiji la Dar es salaam.

Nimefanya hivyo baada ya kupata kumbukumbu rasmi ya Bunge (Hansard) za kikao cha tano cha tarehe 4 Februari 2013 cha mkutano wa kumi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katika Mkutano huo Naibu Spika Job Ndugai alisema na kufanya maamuzi kwamba: “Sasa ninahoji wanaoafiki kwamba hoja hii iondolewe waseme ndiyo…..hoja imeondolewa. Walioafiki Wameshinda”; wakati mtoa hoja sikuwa nimeomba idhini yoyote ya hoja yangu kuondolewa.

Maamuzi hayo ni kinyume na Kanuni ya 58 Fasili 5 ambayo inaelekeza kwamba “Endapo hoja imefikishwa Bungeni, mtoa hoja anaweza tu kuiondoa hoja yake kwa kusimama mahali pake na kusema ‘Ninaomba ruhusa kuondoa hoja’ na papo hapo Spika ataliuliza Bunge kama linaafiki hoja hiyo kuondolewa na inapotokea Wabunge walio wengi watakubali, Spika atasema ‘hoja hiyo inaondolewa kwa idhini ya Bunge’ na hoja hiyo itakuwa imeondolewa na Bunge litaendelea na shughuli inayofuata”.

Ushahidi wa Kumbukumbu Rasmi za Bunge (Hansard) za kikao tajwa unathibitisha ukiukwaji huo wa kanuni kama ifuatavyo: