Showing posts with label Uchaguzi. Show all posts
Showing posts with label Uchaguzi. Show all posts

Wednesday, January 27, 2010

Marekebisho ya Sheria za uchaguzi yaondoe kasoro kwenye upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo

Tunapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ni muhimu kama taifa tuondoe kasoro kwenye upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo. Methodolojia na taratibu zinazosimamia upigaji kura, kuhesabu na kutangaza matokeo vimefafanuliwa katika Sheria ya Uchaguzi na. 1 ya mwaka 1985 kutoka kipengele cha 61(1) mpaka 87 na taratibu zingine za uchaguzi zinazotolewa. Mambo ya kufanya na kutofanya katika uchaguzi yalifafanuliwa katika Taratibu za Uchaguzi za Mwaka 2005 sehemu ya IV kipengele cha 39 mpaka 61. Kwa upande mwingine Sheria ya Uchaguzi na. 1 ya mwaka 1985 kipengele cha 61 mpaka 69 na Taratibu za Uchaguzi za mwaka 2005 kifungu cha 45 mpaka 52 vinaelekeza taratibu zinazopaswa kufuatwa katika vituo vya kupigia kura. Hata hivyo, zipo kasoro kwenye mchakato mzima wa upigaji kura, kuhesabu na kutangaza matokeo ambazo ni muhimu zikajadiliwa.

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010. Hatahivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe. Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi. Katika makala hii tutajadili suala moja la hoja na haya ya kuondoa kasoro kwenye upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo.

Lipo tatizo la wananchi hususani wanachama wa vyama vya upinzani kunyimwa ama kuogopeshwa kwenda kupiga kura. Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 na hata katika chaguzi za marudio kati ya mwaka 2006 na 2009 palikuwa na utaratibu wa majina kubandikwa nje ya vituo ambapo katika maeneo mbalimbali baadhi ya wananchi wengi wao wakiwa ni wanachama wa vyama vya upinzani walizuiwa kupiga kura pamoja na kuwa na vitambulisho vya kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura(DKWK) ama kwa kukosa majina yao nje ya vituo au taarifa zao kuwa na mapungufu au kutokuwepo kabisa katika daftari. Ishara zinaonyesha kuwa pengine huu ulikuwa ni mkakati rasmi kwa kuwa siku kadhaa kabla ya uchaguzi watendaji wa chama tawala hususani wajumbe wa nyumba kumi walipita na kuandikisha namba za wapiga kura katika maeneo yao. Kwa kuwa wananchi wengi walikuwa na elimu finyu ya uraia na kwamba katika baadhi ya maeneo wajumbe hawa wanasikilizwa sana na/au hata kuogopwa, wapiga kura wengi waliorodheshwa na hata wengine kutishwa kuwa kura zao zitajulikana na hivyo wasipoipigia kura CCM watashughulikiwa. Vitisho hivi vilipata nguvu kutokana na utaratibu wa kuchukuliwa namba za shahada za wapiga kura na wasimamizi wa vituo wakati wa kupiga kura. Hii ilifanya uchaguzi usiwe huru.

Pia, vyama vingi havikuweza kuweka mawakala kwenye vituo vyote kutokana na changamoto ya rasilimali na pia mawakala hawakuwa na mafunzo yanayowiana, kila chama kilitoa mafunzo kwa mawakala wake kwa utaratibu wake kwa kuzingatia maelekezo yaliyotolewa na Tume. Hivyo, kulikuwa na utofauti baina ya wasimamizi/wasaidizi wa vituo wa Tume na mawakala wa vyama katika utendaji wao.

Pia, zipo kasoro za moja kwa moja ambazo hujitokeza katika kuhesabu na kutangaza matokeo. Mathalani katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 Jimbo la Ubungo matokeo ya ubunge yalitangazwa kwa shuruti bila kutangaza na kujumlisha kwa pamoja matokeo ya kituo hadi kituo hali iliyoashiria kuwa matokeo ya Ubunge yalikuwa na utata. Kutangaza huku kwa nguvu ilikuwa ni mkakati wa kutaka matokeo hayo yasihojiwe kama ilivyokuwa katika matokeo ya urais ambayo yalichelewa kutangazwa kutokana na kukutwa na mapungufu mengi. Kwa hali iliyodhihirisha wazi kuwa matokeo yalipikwa, waliopiga kura za Ubunge walikuwa 185,684 wakati waliopiga kura za Rais walikuwa 152,525 na hivyo kufanya tofauti ya kura za Ubunge na urais kufikia 33,159. Katika hali ya kawaida na katika uchaguzi uliofanyika kwa wakati mmoja ilikuwa ni vigumu kwa tofauti kubwa ya kura kiasi hiki. Na hata kama wananchi wangekuwa hawapendi kupiga kura za rais kwa kuwa mpiga kura alikuwa akipewa karatasi zote tatu kura hizi zilipaswa kuwepo katika kura zilizoharibika kitu ambacho hakikutokea. Mfano wa Jimbo la Ubungo unaibua hoja ya utofauti mkubwa baina ya jumla ya wapiga kura katika ubunge na urais katika majimbo mbalimbali Tanzania, suala hili linapaswa kujadiliwa. Ufanyike uchambuzi huo kujua utofauti katika kila jimbo ili kuweza kubaini chanzo cha hali hiyo na kukabilina nacho.
Katika kipindi cha mwaka 2006 mpaka 2009, kumeonekana tatizo lingine ambalo nalo linahitaji mjadala wa kina; mwitikio mdogo wa wapiga kura katika chaguzi za marudio. Mathalani chaguzi ndogo za ubunge: Tunduru (48%), Kiteto (47%), Tarime(46%) na Mbeya Vijijini(35%). Kwa upande wa chaguzi ndogo za madiwani hali ilikuwa mbaya zaidi katika baadhi ya kata mathalani: Upanga Mashariki-Dar es salaam (7%) na Sombetini-Arusha(14%) nk. Suala linahitaji kufanyiwa utafiti na chombo zaidi ya kimoja, ili kuwianisha matokeo ya sababu na mazingira yatayoanishwa. Maelezo ya wananchi mbalimbali ni kwamba ‘kadi za kupigia kura zinanunuliwa ama kuchukuliwa kabla ya kwenda kupiga kura’. Uchunguzi wa kina utasaidia kubaini tatizo hili ambalo linaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa misingi ya uhuru na haki katika chaguzi zinazofuata.

Ikumbukwe kuwa Tarehe 11 Disemba 2009 Serikali ilichapisha kwenye gazeti la serikali miswada miwili yenye kulenga kufanya marekebisho katika sheria za uchaguzi na kutangaza kupitia vyombo vya habari tarehe 21 Disemba 2009 maudhui ya miswada hiyo. Miswada hiyo imeshajadiliwa na kamati husika za Bunge na inatarajiwa kujadiliwa ndani ya mkutano wa Bunge unaonza mwezi huu.

Hata hivyo, marekebisho hayo yaliyopendekezwa katika miswada hiyo hayajagusa kikamilifu maeneo yenye kasoro yanayohusu upigaji kura, kuhesabu na utangazwaji wa matokeo. Eneo pekee linaloguswa katika marekebisho ni lile linalohusu zoezi la uandikishaji wapiga kura, ambapo imependekezwa katika ibara ya 7 kuwa na fungu jipya la 15A katika sheria linatoa nafasi kwa vyama vya siasa kuteua mawakala wakaokuwepo katika vituo vya kuandikisha wapiga kura kama ilivyo wakati waupigaji kura.

Hivyo ni muhimu mjadala ukapunuliwa kuwezesha kasoro kushughulikia likiwemo tatizo la kupungua kwa idadi ya wapiga kura. Zipo nchi ambazo sheria ya uchaguzi inalazimisha wananchi kupiga kura ili kuondokana na tatizo la kupungua kwa idadi ya wananchi wanaojitokeza kupiga kura. Mazingira ya kisheria yanaweza kuweka bayana kwamba uhalali wa kiongozi kutangazwa mshindi unategemea asilimia ya wananchi waliopiga kura. Kiongozi aliyechaguliwa na wananchi ambao hawafiki hata asilimia kumi ya wapiga kura waliojiandikisha uhalali wake uko mashakani.
Sheria na taratibu ziwezeshe pia kuwe na mafunzo ya pamoja baina ya mawakala wa vyama na wasimamizi/wasimamizi wasaidizi wa vituo vya kupigia kura. Hii ihusishe pia serikali kugharamia mawakala wa vyama. Ni muhimu kwa Tume na wadau wengine kuwatambua mawakala wa vyama kama sehemu ya msingi ya mchakato mzima wa uchaguzi hivyo mafunzo yao yafanyike sanjari na mafunzo ya wasimamizi/wasimamizi wasaidizi wa vituo. Hii ihusishe pia kuwezesha upatikanaji wa rasilamili kwa ajili ya kugharamia mawakala.
SEHEMU YA MAKALA HII ILITOKA KATIKA GAZETI LA MAJIRA TOLEO LA TAREHE 25 JANUARI 2010

Thursday, January 21, 2010

Marekebisho ya kisheria yafanyike kulinda haki wakati wa uteuzi wa wagombea

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010. Hatahivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe. Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi; na katika kujadili muswada huo makala hii itachambua suala la uteuzi wa wagombea pekee.

Uteuzi wa Wagombea upo katika ngazi mbili: Uteuzi wa Wagombea katika Vyama na Uteuzi wa Wagombea katika Tume ya Uchaguzi. Uteuzi wa ndani ya vyama unasimamia na katiba, kanuni na taratibu za vyama husika. Ni kawaida katika siasa za uteuzi ndani ya vyama kutawaliwa na ushindani mkubwa; lakini ieleweke kuwa kuna tofauti kati siasa chafu na siasa za ushindani. Siasa zenye ushindani chanya zinasababisha uteuzi wa wagombea ambao wenye uwezo kiuongozi mathalani elimu, uzoefu na dira. Siasa za ushindani hasi hupelekea kupatikana kwa wagombea ambao ushindi wao umetokana na rushwa, upendeleo, kupakana matope, udini, ukabila nk. Kwa mfano, uteuzi wa ndani ya CCM uligubikwa na ‘takrima’ na siasa za kupakana matope katika maeneo kadhaa ikiwemo kuanzia ngazi ya udiwani mpaka ya Urais. Mathalani inatajwa jinsi Salim Ahmed Salim (aliyekuwa Katibu Mkuu wa OAU) alivyopakwa matope (kwa mujibu wa Ripoti ya Uchaguzi Mkuu 2005 ya TEMCO). Ilifikia hatua Fredrick Sumaye, mmoja wa wagombea (ambaye pia alikuwa Waziri Mkuu wakati huo), akiwa analaani jinsi ambavyo anapakwa matope alitamka bayana kwamba “anayesafisha njia kwa kalamu, atatawala kwa risasi”.

Uteuzi wa wagombea katika Tume ya Uchaguzi unasimamiwa na Sheria ya Uchaguzi ya Mwaka 1985. Katika uchaguzi Mkuu 2005 wagombea wengi walipitishwa na Tume ya uchaguzi na mapingamizi mengi yalitupiliwa mbali tofauti na chaguzi zingine zilizotangulia.

Katika kipindi cha mwaka 2006 mpaka 2009, pameibuka suala ambalo linahitaji kufanyiwa kazi na marekebisho yakafanyika kuhusu mapingamizi dhidi ya wagombea katika chaguzi. Tutatumia mfano wa suala la mapingamizi katika uchaguzi wa ubunge na udiwani Mbeya Vijijini lakini ipo mifano pia katika chaguzi zingine za marudio ikiwemo za madiwani, mitaa, vijiji na vitongoji. Mgombea wa CHADEMA aliwasilisha fomu zake kwa ajili ya uteuzi tarehe 27 Disemba 2008 na kuteuliwa kuwa mgombea.

Hata hivyo tarehe 28 Disemba, 2008 mgombea aliwekewa pingamizi na mgombea wa CUF na mgombea wa CCM. Misingi ya pingamizi ni pamoja na kuwa mgombea wa CHADEMA alijiapisha mwenyewe na kwamba mgombea aliapa kwa wakili badala ya kuapa kwa hakimu. Msimamizi alimtaka mgombea kuwasilisha maelezo yake, na mgombea aliwasilisha maelezo ya kukanusha kujiapisha, kutoa ufafunuzi kuhusu mpangilio wa majina na kueleza kwamba aliapa mbele ya wakili kwa kuzingatia tarehe ambazo alipaswa kuapa na kwa kuwa ipo sheria nyingine ya viapo inayoruhusu kuapa mbele ya wakili. Na kwamba sheria ya uchaguzi haikatazi moja kwa moja viapo vya waapishaji wengine.

Tarehe 29 Disemba 2008 Msimamizi wa Uchaguzi alikubaliana na eneo moja la pingamizi zilizowasilishwa na CCM na CUF la mgombea kuapa mbele ya wakili badala ya hakimu na kutupilia mbali maeneo mengine ya pingamizi.

Tarehe 30 Disemba 2008 mgombea wa CHADEMA aliwasilisha rufaa dhidi ya maamuzi ya msimamizi wa uchaguzi kutokana na misingi ifuatayo: Kwamba Msimamizi wa uchaguzi wa Jimbo la Mbeya Vijijini hakusoma kwa umakini maelezo ya mrufani na kuyazingatia kikamilifu kabla ya kufanya maamuzi ya kumuengua; Kwamba msimamizi wa uchaguzi hakuzingatia maelezo ya mrufani juu ya muda wa uchukuaji fomu na urejeshaji fomu uliojumuisha siku nyingi takribani tatu mfululizo zisizokuwa za kazi( za sikukuu na siku ya mapumziko ya mwisho wa wiki) ambapo mahakama hazikuwa wazi(operative) na kwamba aliweza kusaini mbele ya wakili tarehe 24 Disemba, 2008 jioni baada ya kumaliza kujaza fomu husika. Na kuomba tume izingatie kifungu 38(1)(4)(proviso) cha sheria ya uchaguzi namba ya mwaka 1985.

Kwamba msimamizi wa uchaguzi wa jimbo alikosea katika kuelezea kuwa sheria ya uchaguzi inasema “mgombea ubunge aape mbele ya hakimu na si vinginevyo” wakati maneno “na si vinginevyo” hayapo kwenye sheria bali ni nyongeza yake tu ili afikie maamuzi ya kumuengua mrufani. Kifungu cha 50 cha sheria ya uchaguzi (National Election Act CAP 343 RE 2002) kinahusika.

Kwamba msimamizi wa uchaguzi amekosea kisheria kwa kutosoma sheria za viapo na kwa kutozingatia maelezo yangu kwamba sheria ya uchaguzi inapaswa kusomwa pamoja na Oaths(Judicial Proceedings and Statutory Declarations Act) pamoja na Notaries Public and Commissiners for Oaths Act(CAP 12 RE 2002), sheria ambazo zinaeleza bayana nani anayepaswa kuapisha kisheria na maana ya kiapo au ‘declaration’. Kifungu cha 11 cha sheria ya viapo “Notary Public and Commissiners for Oath (CAP 12 RE 2002) inaeleza waziwazi kwamba hakuna kizuizi chochote dhidi ya kiapo cha wakili au kamishna yeyote wa viapo.

Kwamba msimamizi wa uchaguzi amekosea kisheria kwa maamuzi yanayoonyesha kuwa sheria ya uchaguzi ni ya kiubaguzi na kwamba inazuia sheria zingine kutumika katika nchi hii. Kwamba msimamizi wa uchaguzi alikosea kisheria kwa kutozingatia maelezo yangu kwamba hakimu anapofanya kazi ya kuapisha hawi hakimu bali anakuwa ‘commissiner for oaths’ kama ilivyoainishwa katika kifungu cha 3 na 10 cha Notaries Public and Commissioner for Oaths Act na kwamba nani anapaswa kufanya jukumu hilo. Kwa maana ya sheria hiyo hakimu hawi tofauti na watu wengine waliotajwa na sheria hiyo wakati anaapisha. Kwamba msimamizi wa uchaguzi amekosea kisheria kwa kushindwa kuelewa hali halisi ya demokrasia ya vyama vingi na mahitaji ya wapiga kura wa jimbo la Mbeya Vijijini kwa kuwanyima haki ya kuwa na uwanja mpana wa uchaguzi kwa ridhaa yao. Kumuengua mrufani ni kulazimisha watu wa Mbeya Vijijini kuchagua vyama ama wagombea waliobakia ambapo ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na kuomba tume izingatie kifungu 38(1)(4)(proviso) cha sheria ya uchaguzi namba ya mwaka 1985. Tarehe 2 Januari 2009 Tume ilitupilia mbali rufaa ya mgombea wa CHADEMA kwa misingi mbalimbali na hivyo mgombea husika akaendelea kuenguliwa.

Taarifa za pingamizi zilifikia viongozi wa chama kabla ya mapingamizi kuwekwa zikieleza mawasiliano ya karibu baina ya viongozi wa waweka pingamizi katika uchaguzi wa Mbeya Vijini na Maofisa wa serikali. Kadhalika ilionyesha wazi kwamba palikuwa na mashinikizo la kutoka nje toka ngazi za juu za CCM na serikali katika kuamua kuhusu pingamizi hilo. Kwa hali ya kisiasa ilivyokuwa, pingamizi hilo lilionekana wazi kuwa ni njia pekee iliyokuwepo ya kuepusha CCM kushindwa na CHADEMA katika uchaguzi huo. Hivyo, tume haikutaka kabisa kuzingatia kwamba siku za kiapo hazikuwa zikitosha na tume haikutaka kabisa kutumia mamlaka yake ya kupokea fomu hata kama haina kiapo ama ina kiapo batili kutokana na mazingira hayo. Hata hivyo, maelezo ya Tume yanaashiria pia kuwa tume ilitambua uwepo wa udhaifu katika sheria ya uchaguzi wa kulazimisha kiapo kufanywa na hakimu pekee.
Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi uliochapwa kwenye gazeti la serikali tarehe 11 Disemba 2009 unaonyesha kwamba marekebisho ya sheria yanayopendekezwa hayatagusa kabisa vifungu vyenye utata kuhusu mamlaka za kuapisha wagombea wala masuala yenye kuwezesha haki na usawa katika uteuzi wa wagombea katika ngazi zote za uteuzi ndani na nje ya vyama.

Suala pekee ambalo Serikali kupitia Ofisi wa Waziri Mkuu imetangaza kuwa imeandaa marekebisho ambayo imeyaita ‘makubwa’ linalogusa uteuzi wa wagombea ni kuhusu utuezi wa mgombea urais au mwenza inapotokea mmoja wao akafariki katikati ya kampeni. Muswada wa marekebisho ya sheria unapendekeza kupunguzwa kwa muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa nafasi ya urais au umakamu inapotokea mmoja wao anafariki kabla ya uchaguzi ambayo imejinadi kuwa yanalenga pia kuipunguzia nguvu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC). Ibara ya 9 inapendekeza marekebisho katika fungu la 35A la sheria kwa lengo la kupunguza muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa urais au umakamu wa rais inapotokea wagombea hao wamefariki.

Masuala yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa na Serikali, Tume ya Uchaguzi, Vyama Vya siasa na Wadau wengeni kama sehemu ya marekebisho ya kisheria yanayopaswa kufanyika kulinda haki wakati wa uteuzi wa wagombea.

Mosi; vyombo vya uangalizi na usimamizi viwezeshwe kisheria kufuatilia kuhakikisha uteuzi wa ndani ya vyama unakuwa huru na haki. Kuna haja ya vyombo mbalimbali viwezeshwe kutupia macho uteuzi ndani ya vyama kuhakikisha haki inatendeka. Mathalani Tume ya uchaguzi na ofisi ya Msajili wa Vyama vya siasa hawapaswi kuwa kimya siasa za kupakana matope zinaoendekezwa wakati wa uteuzi wa baadhi ya vyama hususani CCM. Pia Taasisi ya Kuzuia na Kupambana Rushwa (TAKUKURU) ifuatilie na kuchukua hatua zinazostahili kuhusiana na vitendo vya rushwa vinavyoendelea wakati wa mchakato wa uteuzi katika baadhi ya vyama; utawala wa sheria lazima uheshimiwa hata ndani ya mipaka ya Kikatiba za Vyama vya siasa nchini.

Pili; marekebisho ya sheria ya uchaguzi yahusishe pia kufuta vipengele vibovu vinavyotoa mianya ya mapingamizi yanayokwenda kinyume na haki za kikatiba za wagombea na vyama vyao. Ni vyema mchakato wa kurekebisha sheria ya uchaguzi ukahusisha kuondoa kigezo cha kulazimisha kiapo kwa hakimu pamoja na vigezo vingine ambavyo ni nje ya vigezo kwa kikatiba vya sifa za mgombea. Marekebisho haya yasipofanyika itakuwa ni ishara ya wazi ya kwamba Tume ya Uchaguzi imeacha mwanya kwa mapingamizi kutumika kama zana ya kuhujumu wagombea na vyama vyao katika chaguzi. Tume ya uchaguzi iondoe mianya ya wagombea kukwepa ushindani wa kwenye jukwaa la umma na kukimbilia kutafuta ushindi wa mezani.
SEHEMU YA MAKALA HII ILITOKA KATIKA GAZETI LA MAJIRA TOLEO LA TAREHE 20 JANUARI 2010

Wednesday, January 20, 2010

Mapendekezo ya serikali hayatawezesha kikamilifu uchaguzi huru wa viongozi


KWA kuwa siasa (nikimaanisha siasa safi) ni hitaji muhimu la maendeleo kama alivyowahi kusema hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere; basi uendeshwaji wa uchaguzi (kwa maana ya uchaguzi huru na haki); ndio njia ya kulipata hitaji hili.

Uendeshwaji wa uchaguzi huru na haki hutupatia pia hitaji jingine la msingi kwa maendeleo - yaani “Uongozi Bora”. Suala kuu ni kuwa na mifumo ya kikatiba na kisheria na kiuwanja wa kisiasa ambayo inahakikisha uchaguzi huru na haki.

Katika siku za karibuni pamekuwepo na mjadala kuhusu sheria za uchaguzi uliotokana na uamuzi wa serikali kutoa miswada miwili: Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi na Muswada wa Sheria ya Fedha za Uchaguzi wa mwaka 2010.

Hata hivyo, mjadala huo kwa kiasi kikubwa umejikita katika mapendekezo ya serikali yaliyomo kwenye sheria mpya ya fedha za uchaguzi na kufunika mjadala kuhusu marekebisho ya sheria ya uchaguzi ambayo kwa maoni yangu ndio msingi wa uchaguzi wenyewe.

Hivyo, katika makala hii sitachambua muswada mpya wa fedha za uchaguzi bali nitajikita katika maudhui ya marekebisho ya sheria ya uchaguzi.
Ikumbukwe kwamba tume ya uchaguzi na viongozi wa vyama vya siasa Aprili 21, 2009 mkoani Dar es Salaam mkutano ambao nilishiriki.

Katika mkutano huo nilieleza masikitiko yangu kwamba tangu baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu mwaka 2005, Tume ya Uchaguzi haikuitisha mkutano na vyama vya siasa kuhusu maandalizi ya Uchaguzi Mkuu hadi mwaka 2009, takriban mwaka mmoja tu kabla ya uchaguzi.

Hii inaacha maswali kuhusu dhamira ya tume katika kuhakikisha taifa linakuwa na uchaguzi huru na haki; hasa ukizingatia kwamba toka mwaka 2006; CHADEMA na wadau wengine tumekuwa tukihitaji kukutana na tume na pia tukihimiza mchakato wa mabadiliko ya kweli kuanzishwa.

Niliweka bayana mashaka yangu nikizingatia kuwa masuala ya uchaguzi mkuu yanahusu mabadiliko ya kisheria, kimfumo n.k, ambayo huchukua muda mrefu kuweza kupitishwa na kutekelezwa, hivyo kitendo cha kuanza majadiliano wakati huu, kinaashiria kuwa sehemu kubwa ya yatakayojadiliwa; hayataweza kutekelezwa.

Kwa upande mwingine nilishukuru kuitishwa kwa mkutano huo nikiwa na matarajio kuwa baada ya kukutana huko tume kwa kushirikiana na serikali ingeweza bado kuchukua hatua za haraka kuweza kufanya mabadiliko yanayokusudiwa katika kipindi kifupi kilichobaki.

Mkutano huo, baada ya kupokea maoni ya ujumla kutoka kwa vyama vya siasa uliahirishwa baada ya muda mfupi bila maamuzi yoyote ya msingi kufikiwa kwa maelezo kwamba ungeitishwa mkutano mwingine baada ya kufanya mapitio ya hoja na vielelezo vilivyotolewa na wachangiaji mbalimbali.

Takriban miezi minane, yaani zaidi ya nusu mwaka ukapita mpaka ikafika mwezi Desemba 2009; siku chache kuelekea 2010, si Tume ya Uchaguzi wala serikali ilikuwa imefanya kikao na vyama vya siasa kufikia makubaliano kuhusu marekebisho yanayokusudiwa.

Hata hivyo, katika mwezi wa Desemba 2009 vyombo vyote viwili; tume ya uchaguzi na serikali viliibuka na kutoa kauli zinazoashiria kwamba tayari maamuzi yameshafikiwa kuhusu suala hili nyeti linalohusu mustabali wa wananchi wote bila kujali vyama.

Ilianza Tume ya Uchaguzi ambayo Desemba mosi, 2009 ilifanya mkutano na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari kuelezea kile ilichokiita mkutano wa kubadilishana mawazo na kupeana taarifa kuhusu maandalizi ya uchaguzi mkuu 2010.

Katika mkutano huo mada na hotuba zilionyesha bayana kwamba tayari yapo marekebisho ambayo tume kwa kushirikiana na serikali wameshakusudia kuyafanya; huku mabadiliko mbalimbali ya msingi yakiwa ni sehemu ya hoja zilizowasilishwa.

Siku chache baadaye Desemba 2009 11, serikali ikachapisha kwenye gazeti la serikali miswada miwili yenye kulenga kufanya marekebisho katika sheria za uchaguzi. Siku kumi baadaye serikali ikafanya kile kilichoitwa kuweka hadharani miswada hiyo miwili kupitia taarifa yake fupi kwa vyombo vya habari Desemba 21, 2009.

Serikali ilitangaza marekebisho hayo yakiwa na mapendekezo ya kufanyia marekebisho sheria ya uchaguzi sura ya 343 na sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa sura ya 292, lengo lililoelezwa kuwa ni kuondoa upungufu mbalimbali uliojitokeza katika chaguzi zilizopita kuiwezesha NEC kuendesha uchaguzi kwa ufanisi.

Serikali ikaeleza kuwa upungufu uaokusudiwa kurekebishwa katika muswada huo ni pamoja na NEC kutokuwa na madaraka ya kuteua waratibu waandikishaji wa mikoa.

Pia kushughulikia suala la kipindi cha kuboresha daftari la kudumu la wapiga kura kutotajwa bayana katika sheria na sheria kutoruhusu baadhi ya watendaji wa tume kuingia katika vituo vya kupigia kura ili kufuatilia zoezi la upigaji kura.
Ibara ya 6 imependekeza marekebisho katika fungu la 15 la sheria, ili kuweka bayana kipindi cha kufanya uboreshaji wa daftari la taifa la kudumu la wapiga kura kuwa mara mbili katika Uchaguzi Mkuu mmoja na unaofuata.

Aidha, sehemu hiyo inasisitiza kwamba, kwa lengo la kuongeza uwazi katika zoezi la uandikishaji wapiga kura, imependekezwa katika ibara ya 7 kuwa na fungu jipya la 15A katika sheria linatoa nafasi kwa vyama vya siasa kuteua mawakala wakaokuwepo katika vituo vya kuandikisha wapiga kura kama ilivyo wakati waupigaji kura.

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imetangaza kuwa imeandaa marekebisho ambayo imeyaita ‘makubwa’ ya sheria za uchaguzi ambayo pamoja na mambo mengine, imependekeza kupunguzwa kwa muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa nafasi ya urais au umakamu inapotokea mmoja wao anafariki kabla ya uchaguzi ambayo imejinadi kuwa yanalenga pia kuipunguzia nguvu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Ibara ya 9 inapendekeza marekebisho katika fungu la 35A la sheria kwa lengo la kupunguza muda wa kusubiri kabla ya kufanya uteuzi wa mgombea mwingine wa urais au umakamu wa rais inapotokea wagombea hao wamefariki.

Sehemu ya muswada huo wa sheria ya uchaguzi imependekeza kufutwa kwa vifungu vya sheria vinavyoruhusu utoaji wa takrima.

Muswada unapendekeza pia Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ipewe mamlaka ya kuteua wasimamizi wa uchaguzi kutokana na ofisi au sifa zao tofauti na ilivyo ambapo tume huteua wasimamizi wa uchaguzi kutokana na ofisi pekee.

Marekebisho hayo pia yanapendekeza kuongeza muda wa rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama Kuu, katika Mahakama ya Rufaa kwenye kesi za uchaguzi na kuongezwa kwa muda wa kufungua kesi kutoka siku 14 za sasa hadi siku 30.

Ibara ya 10 imependekeza marekekibisho katika fungu la 37 la sheria ili kuweka ukomo wa muda wa kufanya chaguzi ndogo za Bunge kama inavyobainishwa katika ibara ya 76(3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977.

Katika Ibara ya 3, muswada unapendekeza kuongeza tafsiri ya maneno mbalimbali katika sheria ya uchaguzi; unapendekezwa kurekebisha tafsiri ya maneno “nomination” na “Member of Parliament” ili kujumuishwa katika tafsiri ya uteuzi (nomination) uteuzi wa wabunge wanawake wa viti maalumu na katika tafsiri ya mbunge (member of Parliament) mbunge wa kuteuliwa wa viti maalumu vya wanawake.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Ibara ya 13 inakusudia kufanya marekebisho katika sura ya V ya sheria kwa kuongeza sehemu mpya ya III inayohusu mchakato wa mamlaka ya tume kuwatangaza wabunge wanawake wa viti maalumu walioteuliwa na vyama vyao kuwa wabunge.

Marekebisho hayo ambayo serikali imeyapendekeza yanatarajiwa kujadiliwa katika kikao cha Bunge hivi karibuni ili yatumike kwenye uchaguzi wa mwaka 2010.

Hata hivyo, marekebisho hayo hayajitoshelezi kabisa ukilinganisha mapungufu yaliyopo, muda uliopo, hoja za wadau na rasilimali ambazo zimetolewa na wadau mbalimbali kuwezesha mchakato wa marekebisho ya kisheria na kitaasisi nchini kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Hivyo mjadala utakaowezesha kuunganisha nguvu za kidemokrasia na kimaadili ili kudai na kushawishi mabadiliko ya sheria za uchaguzi na mazingira ya kisiasa ni muhimu uibuliwe na kuendelezwa.

Kuna haja ya serikali kufanya marekebisho mapana zaidi au vyama vya siasa na wadau wengine waelekeze jitihada bungeni na mahakamani kudai mabadiliko ama kufutwa kwa vipengele vya sheria nyingine ambavyo vinafanya mazingira ya kisiasa na kiuchuguzi yanayokwaza uchaguzi huru na wa haki.

Kwa muhtasari lazima kuzipitia sheria na/ama kufanya mabadiliko/marekebisho ya msingi yafuatayo ambayo hayajaguswa katika miswada iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mosi, tume lazima iwe huru na ya kudumu yenye kufanya kazi muda wote na kuwekewa bajeti maalumu na watumishi wa serikali wasitumike katika uchaguzi badala yake kuwe na watendaji huru wa tume katika ngazi zote kama ilivyo kwa mahakama.

Pili, kupanua wigo wa mfumo wa uwakilishi wa uwiano na kuweka mfumo mchanganyiko/mchanyato. Tatu; Kufuta vipengele katika sheria vinavyoruhusu mapingamizi yanayokwenda kinyume na misingi ya masharti ya kikatiba ya wagombea.

Nne, kuchunguza na kukabiliana na tatizo la mwitiko mdogo wa wapiga kura. Tano, kuhakikisha kwamba mafunzo ya pamoja yanafanywa baina ya wasimamizi/wasaidizi wa vituo na mawakala wa vyama; na kuhakikisha wgombea/vyama vinakuwa na rasilimali za kuwezesha kuwa na mawakala katika vituo.

Sita, kutoa uhuru wa vyombo vya habari ikiwemo wakati wa uchaguzi; Kuweka usawa katika matumizi ya vyombo vya habari ikiwamo kuhusu matangazo ya kisiasa ya kulipia wakati wa kampeni.

Ni wazi: Sehemu kubwa ya mabadiliko haya yanahitaji kitu kimoja tu: mabadiliko ya katiba ya nchi.

Hakuna uhuru na haki kwa vyama vya siasa kushiriki kwenye chaguzi zijazo kama mazingira ya kisiasa na kiuchaguzi hayatabadilika katika nchi yetu!