Saturday, September 3, 2011

Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje; mchango wangu bungeni

MKUTANO WA NNE-Kikao cha Thelathini na Moja – Tarehe 22 Julai, 2011

JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ina umuhimu wa pekee sana wakati huu dunia iko kwenye mwelekeo wa ubeberu na ubepari, hivyo iongezwe fedha kwenye bajeti yake kwa ajili ya kulinda maslahi ya Taifa Kimataifa.


Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza kazi yake, inahitajika kufanyike mabadiliko ya kisheria na kitaasisi ili kuweka mkazo katika diplomasia ya uchumi na usalama.


Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kitabu cha bajeti, Volume II, Fungu 34; Wizara ieleze sababu za kupanda kwa Kasma 220800 Kifungu 1002, hizi zimepanda kwa kiwango kikubwa ukilinganisha na mwaka 2010/2011 na 2011/2012. Kifungu 2006 ielezwe hatua zilizochukuliwa kurekebisha ongezeko la matumizi ya zaidi ya 832 milioni nje ya bajeti iliyopitishwa na Bunge (Ubalozi wetu London). Kifungu 2009- hatua za kumaliza masuala ya nyuma yaliyotolewa na CAG ya takribani 451 milioni kuhusu Ubalozi wetu Moscow. Hatua zilizochukuliwa kurekebisha kasoro za mawasiliano na sekta mbalimbali kuwezesha utekelezaji wa miradi inayodhaminiwa na Serikali ya China na Taasisi/Makampuni yake, hii ifanyike kwa kutumia vizuri rasilimali zilizotengwa kwenye Kifungu 2014. Kifungu 2027; hatua zilizochukuliwa kushughulikia kasoro ya milioni 865 kutumiwa bila idhini.


Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Volume IV, Fungu 34, Kifungu 1604, Kasma 6391, kwenye utekelezaji 2009/2010, 2010/2011 na malengo 2011/2012, napenda kujua hatua zilizochukuliwa kwa Ubalozi wetu Kigali kulipa nyumba miezi saba bila kutumika, ukarabati wa Ubalozi wetu Nairobi na ujenzi kwenye kiwanja Upper Hill.


Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya kulinda maslahi ya kiuchumi ya nchi yetu,
mkazo uwekwe kwenye Balozi za nchi ambazo tuna maslahi mengi ya kiuchumi kwa 87 kurejea Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano. Aidha, safari za nje za viongozi zipunguzwe ukubwa wa misafara na idadi ili kuweka mkazo kwenye safari zenye tija. Haiwezekani kwa safari zote kati ya 2005-2010 kwa kisingizio cha kutafuta wawekezaji halafu tumeshindwa kuweka mstari wa mbele kuondoa kero ya umeme na upatikanaji wa gesi asilia.


Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ijikite katika kuepusha uongozi wetu kutumiwa
na makuwadi wa kiuchumi bila maslahi ya Taifa na rasilimali zake kulindwa kwa
kiwango cha kutosha hususani kwenye ardhi, madini, gesi n.k Kampuni kama Good Works International zichunguzwe kwa ajili ya maslahi ya umma.


Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ishirikiane na Wizara ya Afya, NSSF na balozi wa India kuharakisha ujenzi wa Hospitali ya Apollo.


Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza ushiriki wa Watanzania wanaoishi ughaibuni (Diaspora) kwenye maendeleo; Wizara ishirikiane na mamlaka nyingine
kuhakikisha inafanyika sensa rasmi.


Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya kiusalama yapewe kipaumbele katika kazi
za Wizara. Serikali itoe kauli kuhusu malalamiko ya Askari wa Tanzania katika vikosi vya kuleta amani vya UN hususani nchini Lebanon na Sudan (Darfur). Malalamiko hayo yanahusisha kuchelewa kwa mishahara na kupelekewa malipo pungufu ya mikataba. Malalamiko hayo yameshaandikwa kwa Rais na Waziri wa Ulinzi badala ya haki zao kulindwa, wameandikiwa Waraka toka Makao Makuu ya Jeshi wa kuwatishia kuwa watarudishwa na kufukuzwa kazi. Ni muhimu Wizara ya Mambo ya Nje ikaingilia kati ili kuhakikisha masharti yote na stahili zote zilizomo kwenye mikataba ya kulinda amani baina ya Tanzania na Umoja wa Mataifa UN yanatekelezwa.


Aidha, kwa ajili ya kusafisha taswira ya Tanzania Kimataifa, ni vizuri Serikali ikatoa kauli ya hatua ambazo imechukua kuhusu tuhuma za baadhi ya Watanzania kuhusika na biashara ya silaha haramu. Mathalani Ripoti ya Timu ya Wataalamu wa Baraza la Usalama la UN ya tarehe 26 Januari 2006. Pia mkataba wa tarehe 17 Agosti 1997 kati ya Kampuni ya Executive Outcomes Inc. na Tanzania kwenye mradi wa madini kupitia mradi wa Meremeta, suala ambalo limehusishwa na usafirishwaji wa silaha haramu Congo (DRC) kati ya 1997 mpaka 2007.


JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. Kupitia kifungu hiki cha Mshahara wa Waziri, ningeomba kupata ufafanuzi kuhusu jambo moja
la Kisera. Ninaelewa kwamba, jukumu mojawapo la Kisera la Wizara hii ni kujenga taswira pana ya nchi yetu Kimataifa. Sasa kuna suala mahususi ambalo nililiuliza kuhusiana na tuhuma juu ya Watanzania kushiriki kwenye masuala ya uuzaji wa silaha haramu ambazo zinachafua taswira ya nchi yetu.


Ninaelewa kwamba, Mheshimiwa Membe, analifahamu jambo hili, kwa sababu
mwaka 2000 lilijadiliwa kwenye Baraza la Usalama wa Umoja wa Mataifa na mwaka wa 2006 lilijadiliwa vilevile Umoja wa Mataifa. Sasa ningependa kupata kauli ili tusichafuke kama Watanzania, kwa sababu ya matendo ya watu binafsi kuhusiana na tuhuma hizi hususan tuhuma zinazoihusu Kampuni ya Meremeta, kwa sababu wengi wamezoea kufikiria kwamba, ilikuwa ni kashfa sijui ya utoroshaji wa madini peke yake na ufisadi wa pesa za Watanzania shilingi bilioni 100, lakini kuna tuhuma nzito vilevile za kuhusiana na utoroshaji wa silaha. Kwa hiyo, ninaomba ufafanuzi kuhusu hilo.


WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi kabisa kusema kwamba, Watanzania na hasa Wizara yetu, wanayo haja ya kujua nini kinachoendelea na kuthibitisha madai mbalimbali yanayotolewa kama hili ambalo limetolewa na Mheshimiwa Mnyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala alilolisema Mheshimiwa John Mnyika ni zito,
linastahili kutoa majibu ya uhakika na nilivyojiandaa leo katika shughuli hizi, suala la silaha na suala la Meremeta, halikuwepo kwenye vocabulary yangu. Tunaomba suala hili tulitafutie muda ili tuweze pengine kulitolea majibu, sitaweza kutoa majibu ya haraka haraka kwa swali zito.

MWENYEKITI: Ahsante

No comments: