Friday, March 11, 2011

MNYIKA AANDAA BONANZA LA SOKA KUADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE

Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika ameandaa bonanza la soka kwa wanawake katika kuadhimisha siku ya Wanawake Duniani.

Bonanza hilo la siku mbili litafanyika katika Uwanja wa Santos Barafu kuanzia tarehe 8 Machi mpaka 9 Machi mwaka 2011.

Bonanza hilo litashirikisha jumla ya timu nne za wanawake; tatu za wanawake katika jimbo la Ubungo za Mlimani, Mburahati na Uzuri pamoja na timu mwalikwa ya Tanzanite toka jimbo la Kinondoni.

Wabunge wanawake wa viti maalum wa CCM na CHADEMA toka manispaa ya Kinondoni na madiwani wa viti maalum jimbo la Ubungo wamealikwa kuwa wageni rasmi kwenye mechi za ufunguzi wa Bonanza hilo wakati mbunge wa Jimbo hilo, John Mnyika atakuwa mgeni rasmi katika kilele cha bonanza hilo.

Izingatiwe kuwa tarehe 8 Machi ni siku ya Wanawake Duniani ambayo kwa mwaka huu ujumbe wake kimataifa ni “Fursa sawa ya elimu na teknolojia ni njia ya ajira bora kwa wanawake”.

Ni muhimu kwa vijana wa kike, wanawake na mashabiki wengine wa soka kujitokeza katika bonanza hilo ambalo halitakuwa na kiingilio chochote ambalo litafanyika kwenye uwanja huo wa wazi uliopo katika kata ya mburahati.

Mechi za Bonanza hilo zitatoa fursa ya kufikisha ujumbe kuhusu masuala mbalimbali yanayowagusa wanawake hasa katika wakati huu ambao dunia inaadhimisha miaka mia moja toka kuanza kwa siku hiyo ya wanawake mnamo mwaka 1911.

No comments: