Tuesday, March 22, 2011

Serikali itoe kauli katika wiki ya maji

Tarehe 22 Machi 2011 ni kilele cha wiki ya taifa ya maji ambayo pia ni siku ya kimataifa ya maji ambapo ujumbe wa mwaka huu ni “Maji kwa ajili ya Miji: Kukabiliana na changamoto mbalimbali mijini”.

Maadhimisho ya mwaka huu kwa ngazi ya Mkoa wa Dar es salaam yatafanyika katika kata ya Mburahati ndani ya Jimbo la Ubungo katika Manispaa ya Kinondoni.
Pamoja na kushiriki katika uzinduzi wa miradi ya maji, nitatumia siku hiyo kuendelea kufanya ufuatiliaji na kuisimamia serikali ili kuweza kuongeza kasi ya utekelezaji wa mipango ya sekta husika.

Nakubaliana na uamuzi wa serikali uliofanyika mwezi Machi wa kuweka programu maalumu ya kuongeza upatikanaji wa huduma za maji safi na maji taka katika mkoa wa Dar es salaam kama moja ya vipaumbele katika muongozo wa bajeti ya mwaka 2011/12 kuwa kuwa umeendana na mwito ambao tuliutoa katika Kongamano la Maji Jimbo la Ubungo lililofanyika tarehe 31 Januari 2011.

Aidha nakubaliana na uamuzi wa serikali wa kutaka kutenga bilioni 654 kwa ajili ya kuteleza mpango husika huku asilimia 80 za fedha hizo zikipangwa kutoka kwenye vyanzo vya ndani; hata hivyo uamuzi huo utakuwa wa maana ukianza kutekelezwa kwa ukamilifu kuanzia mwaka huu wa fedha. Uchimbaji wa Visima virefu Kimbiji na Mpera na ujenzi wa bwawa la Kidunda pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya Ruvu juu na Ruvu chini ni mipango inayopaswa kuungwa mkono na kufuatiliwa kwa karibu na kila mpenda maendeleo.
Hatahivyo, siridhishwi na viwango na kasi ya utekelezaji wa mipango husika. Kati ya mwaka 2005 mpaka 2010 kiwango cha fedha ambacho kimetumiwa na DAWASA/DAWASCO na mamlaka zingine kutokana na fedha za umma ikiwemo mikopo toka kwa washirika wa kimaendeleo hakilingani na ubora wa miundombinu na huduma inayopatikana; hivyo mifumo thabiti ya usimamizi na ukaguzi inahitajika ili hatua stahili ziweze kuchukuliwa.
Natoa mwito kwa mamlaka mbalimbali za kiserikali kutumia kilele cha siku ya maji kutoa taarifa za kina zaidi kwa umma kuhusu utatuzi wa kero ya maji kwa wananchi wa mkoa wa Dar es salaam hususani wa jimbo la Ubungo.

Mathalani akihutubia Bunge mwezi Juni mwaka 2010 wakati wa kuwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara ya Maji ya mwaka wa fedha 2010/11 Waziri Mark Mwandosya aliahidi kwamba usanifu wa bwawa la Kidunda linatarajiwa kutoa mchango mkubwa wa utatuzi wa kero ya maji kwa wananchi wa Ubungo ungekamilika mwezi Septemba mwaka huo wa 2010; lakini mwezi Machi mwaka huu Waziri ametoa kauli tofauti kuwa upembuzi yakinifu wa ujenzi wa bwawa hilo utakamilika mwezi Juni mwaka 2011 na ujenzi mwaka 2013. Natoa mwito kwa Waziri Mwandosya kueleza wananchi wa Ubungo na watanzania kwa ujumla sababu za kuchelewa kwa mpango huo na mikakati iliyopo ya kuhakikisha bwawa husika linajengwa mapema zaidi ya muda uliotangazwa.

Aidha wakati hatua hizi za muda mrefu zinaendelea kutekelezwa ni muhimu kwa DAWASA, DAWASCO, Manispaa na Wizara husika kuongeza kasi ya kuchukua hatua za muda mfupi za kupunguza kero ya maji kwa kutimiza wajibu ipasavyo.

Mfano mwezi Mei mwaka 2010 Rais Jakaya Kikwete alifanya ziara katika jimbo la Ubungo kata za Mburahati na Kimara eneo la Mavurunza na kuahidi idadi maalum ya visima ambavyo serikali imengevichimba lakini mpaka sasa ahadi hiyo haijatimizwa kwa ukamilifu wake katika muda ambao uliahidiwa. Hivyo, kupitia siku hii ya maji ni muhimu kwa Rais Kikwete au wasaidizi wake kutoa kauli kuhusu utekelezaji wa ahadi husika ama sivyo itabidi tuunganishe nguvu ya umma katika kuchukua hatua za ziada kukabiliana na kero husika ambayo inawasumbua wananchi miaka 50 baada ya uhuru wa nchi yetu.

Kadhalika, upungufu wa maji unachangiwa pia na upotevu wa maji uliopo sasa wa karibu asimilia hamsini (50%) ambao unaambatana na hujuma mbalimbali katika ratiba za mgawo wa maji katika baadhi ya maeneo. Katika kikao cha saba tarehe 18 Februari 2011 niliuliza Swali la Nyongeza kutokana na majibu ya Swali namba 85 kwa Wizara ya Maji. Kwenye swali langu la Nyongeza kuwa pamoja na uwekezaji wa fedha za miradi ya maji za Benki ya Dunia na Wadau wengine wa maendeleo kwenye Ruvu Juu na Ruvu chini ikiwemo kuweka mtandao mpya wa mabomba ya maji maarufu kama mabomba ya wachina; bado maji kwenye kata za Kwembe, Kibamba, Msigani, Mbezi, Saranga, Kimara nk maji hayatoki kwa pamoja na mambo mengine upotevu wa maji na wafanyabiashara wanauza maji bei juu kujiunganishia kinyemela; je Naibu Waziri yuko tayari kufanya ziara ya kukagua miundombinu ya maji ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa? Naibu Waziri alijibu kwa kunipongeza kwa kuweka kipaumbele cha kwanza suala la maji katika kazi zangu na kuahidi kutembelea miundombinu husika. Hata hivyo, ziara ya kutembelea miundombinu husika katika maeneo ambayo wananchi wametoa tuhuma mbalimbali bado haijafanyika. Natoa mwito kwa Wizara husika ambayo ofisi zake zipo ndani ya Jimbo la Ubungo, DAWASCO au Kamati husika ya Bunge kutumia fursa ya maadhimisho ya siku ya maji ambao ujumbe wake mwaka huu ni muhususi kwa mijini kutembelea maeneo husika na kuchukua hatua ili maadhimisho ya mwaka huu yaweze kuchukua sura tofauti kwa kushughulikia kero za msingi za wananchi katika sekta ya maji badala ya hotuba za viongozi pekee.

Imetolewa tarehe 20 Machi 2011 na:

John Mnyika
Mbunge wa Ubungo

1 comment:

sam2net said...

Kwanza nashukuru kufahamu kuwa kumbe siku ya maji inayoadhimishwa tarehe 22.March ni siku yangu ya kuzaliwa. Hivyo najisikia fahari kuzaliwa siku hiyo muhimu. Mimi ni mkazi wa jimbo la Gairo, lakini pamoja na kuwa na vyanzo vingi vya maji bado mji huu hauna huduma hiyo yenye kukidhi mahitaji kwa takribani miaka 50 sasa tangu uhuru, japo serikali ipo... kwa kuwa siku yangu ya kuzaliwa inaoana na maadhimisho, bila shaka nitakuwa suluhusho la maji Gairo In the few years to come as My God wishes