Tuesday, March 22, 2011

Wananchi kuandamana kuhusu bomoa bomoa Ubungo

LICHA ya Rais Jakaya Kikwete kuwaonya viongozi wa Chadema kwa kuandaa maandamano na kupandikiza kile alichoita mbegu mbaya za chuki dhidi ya serikali, Chama hicho kipo katika harakati za kuongoza maandamano mengine, jijini Dar es Salaam.Hayo yatakuwa maandamano ya tatu kufanywa na Chadema tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu Oktoba Mwaka jana.

Maandamano ya kwanza yalifanyika mkoani Arusha kupinga uchaguzi wa Meya wa jiji hilo na maandamano mengine yakafanyika katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.Maandamano ya Dar es Salaam ambayo Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika (Chadema) amethibitisha kuyaongoza, yatafanywa na wananchi wanaoishi kando ya barabara ya Morogoro, kuanzia eneo la Ubungo mpaka Kimara ambao nyumba zao zipo katika mpango wa kubomolewa kupisha upanuzi wa barabara hiyo.

“Mmesema mmemwandikia barua Mkuu wa Mkoa, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Waziri wa Ujenzi, Mkurugenzi wa jiji na Mkuu wa wilaya ya Kinondoni kuomba msaada na kukutana nao lakini hamjajibiwa lolote,” alisema MnyikaAliongeza, “Kama ni hivyo pitisheni azimio ili serikali itoe ufafanuzi wa sakata hili. Wapeni siku saba ili wawajibu, wakishindwa kufanya hivyo, itabidi mwende kwa Waziri Mkuu mkamweleze matatizo haya, mtaniambia tu ni lini, mimi pia nitashiriki.

”Mnyika alisema kama mwakilishi wa wananchi bungeni na kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 63 (2), kama sakata hilo litakuwa halijapatiwa ufumbuzi, atalipeleka bungeni ili lijadiliwe.“Kwanza naweza kuliuliza kama swali la papo kwa papo, ikishindikana nitalichangia katika hoja mbalimbali, pia hiyo ikishindikana nitalipeleka suala hili kama hoja binafsi,”alisema Mnyika.Aliongeza, “Ila njia nzuri kwangu ni kulipeleka suala hili kama ombi, tena sio langu bali ni ombi la wananchi. Hili litakwenda bungeni kama hoja ya wananchi.

”Baada ya kauli hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya waathirika wa bomoa bomoa hiyo ambao wamepewa siku 60 wawe wameondoka maeneo hayo, Naomi Alimanoti alipitisha azimio hilo na kuongeza kuwa wanaipa serikali siku saba zinazoanzia kesho.“Tutakutana Jumamosi ijayo, pale pale katika eneo letu la siku zote ili kuona kama tumejibiwa ama laa. Kama tutakuwa hatutajibiwa tutaandamana hilo halina mjadala. Hapa mpaka kieleweke, hatuwezi kuvunjiwa nyumba zetu wakati tuna hati halali na sheria inatulinda,” alisema Alimanoti.

Awali Mnyika alisema kuwa propaganda zinazoenezwa kwamba Chadema wanapinga mikakati mbalimbali ya maendeleo si za kweli bali maendeleo hayo yanatakiwa kufanywa bila kukiuka sheria na haki.“Iweje mwaka 1973 katika ubomoaji wa nyumba katika barabara hii watu walipwe, lakini hivi sasa watu hawa waambiwe kuwa wamevamia eneo la hifadhi ya barabara,” alihoji Mnyika.Kwa mujibu wa Mnyika, katika eneo hilo kuna nyumba ambazo zitaathirika kutokana na mradi wa mabasi yaendayo kasi (DAT) hivyo akatoa wito kwa serikali kumjibu kimaandishi juu ya miradi yote ya barabara katika eneo hilo kwa kuwa inawezekana wanaobomolewa nyumba zao wakati eneo lenyewe halihusiki na mradi wowote.

“Kwa tafsiri ya serikali, wananchi walioko katika eneo la barabara hii hawatalipwa fidia, mwaka 1997 mpaka 2001 watu walivunjiwa na hawakulipwa kwa maelezo kwamba wote walilipwa mwaka 1973,” alisema Mnyika.Alifafanua kuwa serikali inatakiwa kutorudia makosa ya mwaka 1997, ambapo wakimbizi wa Tanzania walihifadhiwa ndani ya nchi yao wenyewe.

“Waliovunjiwa kipindi hicho walihifadhiwa katika ofisi za Umoja wa Mataifa jijini Dar es Salaam, serikali isipokuwa makini itatengeneza mazingira ya mwaka 1997. Katika hili hauwezi kukaa kimya, tena bomoa bomoa hii si Kimara ni karibu mikoa yote nchini,”alisema Mnyika.

Mnyika aliwataka wananchi hao kujiorodhesha ikiwa ni pamoja na kuwa na vielelezo vyao vyote kwa kuwa kati yao wapo waliovamia na wapo walio na umiliki halali wa maeneo hayo.Alisema wanatakiwa kuwa na jopo la mawakili watakaowasimamia katika kesi ambayo wataifungua kama hatua zote watakazozichukua zitagonga mwamba pamoja na kuandaa utaratibu wa kufanya uthamini wa nyumba zao kabla hazijavunjwa.

Mnyika aliendelea kueleza kuwa jambo lolote linapotokea kabla ya kuanza kulizungumza, inatakiwa ufanyike uchunguzi na kusisitiza kuwa ilitakiwa uchunguzwe uhalali wa wananchi wa Kimara kudai haki zao kwanza kuliko kuanza kuwashutumu kuwa wanapinga maendeleo.“Huu si wakati wa serikali kuendeshwa kwa shinikizo.

Ni wakati wa kuchunguza na kujua ukweli. Hatua yoyote itakayochukuliwa na wananchi hawa itakuwa ya kidemokrasia,”alisema Mnyika.Mmoja wa wananchi hao, Charles Mwandembwa alisema kuwa Rais Jakaya Kikwete anatakiwa kuwa makini, kwa kuwa wanaomwangusha ni watendaji wake ambao wamekuwa waking’ang’ania kuwaondoa wananchi wa Kimara ili wao wamiliki ardhi.

Naye Joshua Mlekani alisema wanatakiwa kuweka kutafuta zuio la Mahakama ili ubomoaji wa nyumba katika eneo hilo, usitishwe kwa muda ili wapate nafasi ya kufuatilia haki zao.Mwisho


Chanzo: Mwananchi-6/3/2011

1 comment:

sam2net said...

Wewe ni jembe la ukweli. Tupo nyuma yako. Ulinifurahisha sana siku ya ufunguzi wa tawi la Mipango Dodoma. Viva Mnyika