Tuesday, July 8, 2014

Mnyika adai kutishiwa maisha

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (Chadema), amewaomba wapiga kura wake kumuombea kila siku kutokana na madai kuwa amekuwa akiwindwa na watu wanaotishia uhai wake.
Mnyika alitoa kauli hiyo juzi jioni katika eneo la Mbezi mjini Dar es Salaam, wakati akihutubia mkutano wa hadhara.
“Nimekuwa nikizungumza mambo mengi ninapokuwa bungeni Dodoma, hasa ninapowatetea wananchi na wapiga kura wangu, lakini kuna watu hawafurahishwi kabisa…sasa wamefikia hatua ya kunitishia maisha yangu.

“Wengi mnakumbuka kwamba, Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dk. Steven Ulimboka, alitekwa na kupigwa na watu wasiojulikana na kisha kung’olewa meno, baada ya tukio lile aliyekuwa akifuatia nilikuwa mimi, sasa sijui na mimi wanataka kunifanyia hivyo au la,” alisema Mnyika.
Alisema taarifa za yeye kutishiwa maisha zilianza kuvuja baada ya kumalizika kwa vikao vya Bunge la Bajeti.
Alisema kashfa ya Kampuni ya kufua umeme ya IPTL ilianza miaka ya tisini, baada ya maridhiano kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Malaysia ili kuleta mitambo ya kufua umeme nchini na kwamba, Rais Jakaya Kikwete anafahamu kiini cha mzozo.
Alisema IPTL imekuwa ikiitia hasara kubwa Serikali kwa kipindi kirefu, jambo ambalo halina budi sasa kuchukuliwa hatua.

“Wenzetu walikuwa na mtaji mdogo walipokuja kiasi ambacho hata Mtanzania anayefanya biashara ndogo ndogo aliweza kuumiliki, lakini uliongezeka kutokana na sisi kupandishiwa gharama za umeme kwa mujibu wa ushahidi wa Mahakama,” alisema.
Chanzo: Gazeti la Mtanzania (http://mtanzania.co.tz/?p=432)

No comments: