Thursday, February 16, 2012

Kanuni za Uchaguzi wa Wabunge wa EAC zirekebishwe

Mihimili miwili ya nchi yaani bunge na serikali inapaswa kutoa uongozi thabiti wenye kuwezesha Tanzania kupata wabunge wanaokubalika na umma wa Bunge la Afrika Mashariki katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika kwenye mkutano ujao wa bunge.

Ili kutimiza azma hiyo Spika wa Bunge Anna Makinda anapaswa kuwezesha marekebisho ya msingi ya kanuni zinazosimamia uchaguzi husika kabla ya katibu wa bunge kutoa tangazo la uchaguzi tajwa.

Aidha, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki Samuel Sitta anapaswa kutoa kwa umma na kwa vyama vya siasa muswada wa sheria ya uchaguzi wa Afrika Mashariki wa mwaka 2011 uliopitishwa na Bunge la Afrika Mashariki ili uwe msingi wa marekebisho yanayopaswa kufanyika kabla ya uchaguzi husika kufanyika nchini.

Uchaguzi huu una umuhimu wa pekee kwa wananchi wa Tanzania ikiwemo wa Jimbo la Ubungo wakati huu ambapo jumuiya ya Afrika Mashariki ipo katika soko la pamoja na majadiliano ya kuwa na sarafu moja yanaendelea hali ambazo zina athari kwa nchi na wananchi kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Izingatiwe kuwa tarehe 10 Februari 2012 wakati wa kuahirishwa kwa mkutano wa sita wa Bunge Spika Makinda ametangaza kuwa uchaguzi wa wabunge wa kuwakilisha Tanzania kwenye bunge la Afrika Mashariki utafanyika katika mkutano wa saba wa Bunge unaotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 10 Aprili 2012.

Wednesday, February 15, 2012

Kuhusu Kauli za Sekretariati ya Maadili ya Viongozi wa Umma

Kufuatia Sekretariati ya Maadili ya Viongozi wa Umma kutangaza katika vyombo mbalimbali vya habari tarehe 15 Februari 2012 kwamba wameanza kuhakiki fomu za tamko la mali na madeni kwa baadhi ya viongozi tuliojaza fomu husika, mjadala umeibuka jimboni na katika jamii kuhusu suala hilo na baadhi mmeomba maoni yangu juu ya mchakato huo.

Umma ufahamu kuwa nilitimiza masharti ya kuwasilisha fomu kwa wakati na kutoa tamko kwa mujibu wa sheria, uhakiki ni utaratibu wa kawaida. Pamoja uhakiki, natoa mwito kwa Sekretariati kufanya uchunguzi juu ya viongozi wa umma wenye tuhuma mbalimbali ambao tumewataja kwa majina kwa nyakati mbalimbali. Aidha, kuhusu kufanya marekebisho ya sheria ya maadili ya umma kwa ajili ya kuweka mipaka kati ya biashara na siasa, sekretariati badala ya kurudia tena kufanya utafiti irejee kauli ya serikali bungeni kuwa waraka wa marekebisho ulishaandaliwa tayari na itoe mapendekezo kwa serikali yenye kuwezesha muswada kuwasilishwa katika mkutano ujao wa bunge.

Pamoja na uhakiki wa kawaida, sekretariati ifanye uchunguzi kwa watuhumiwa:

Ni vizuri ikazingatiwa kuwa nilitimiza masharti yanayotakiwa kwa mujibu kifungu cha 9 cha Sheria ya maadili ya viongozi wa umma namba 13 ya mwaka 1995 ya kujaza fomu za tamko la mali na madeni na ni jambo la kawaida kwa sekretariati kufanya uhakiki wa fomu tajwa na kabla ya kuwa mbunge nimekuwa nikitoa mwito wa mara kwa mara kwa sekretariati kutimiza wajibu husika.

Ni muhimu sekretariati ya Maadili ya Viongozi wa Umma ikapanua wigo wa uhakiki iongeze orodha ya viongozi wa umma ili walau kwa mwaka iweze kuhakiki sampuli isiyopungua 10% ya viongozi wote wa umma na taarifa ya uhakiki huo iweke wazi kwa umma kuhusu wote wasiotangaza mali kwa mujibu wa sheria au ambao watabainika kutoa taarifa zenye kasoro.

Tuesday, February 14, 2012

DAWASCO kutozingatia ratiba ya mgawo wa maji

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ametoa mwito wa Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) kutoa taarifa kwa umma kuhusu kutozingatiwa kwa ratiba ya mgawo wa maji katika Jiji la Dar es salaam hali ambayo imesababisha kero ya maji katika maeneo mbalimbali ya jimbo la Ubungo.

Mnyika ametoa mwito huo kupitia kwenye barua yake kwa DAWASCO aliyoiwasilisha leo tarehe 14 Februari 2012 na kutoa rai kwa madiwani wa CCM na CHADEMA katika Jimbo la Ubungo kuwasilisha taarifa za hali ya maji katika kata zao kufuatia malalamiko ya wananchi.

Itakumbukwa kwamba tarehe 5 mwezi Septemba 2011 Mbunge Mnyika alifanya mkutano na Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASCO akiwa na baadhi ya wakazi wa kata mbalimbali kuhusu hali ya upatikanaji wa maji katika Jimbo la Ubungo.

Kufuatia mkutano huo DAWASCO ilichukua hatua mbalimbali ambazo ziliboresha mgawo wa maji katika maeneo kadhaa ya Jimbo la Ubungo katika kipindi cha mwishoni mwezi Septamba mpaka katikati ya mwezi Disemba mwaka 2011.

Saturday, February 11, 2012

Nilitaka bunge likae kama kamati ya mipango kuchukua hatua za kunusuru uchumi na kupunguza mfumuko wa bei

Katika kuendelea kutimiza wajibu wa kuisimamia serikali kushughulikia uchaifu wa uchumi wa nchi yetu wa urari tenge kutokana na kuagiza bidhaa nyingi toka nje na upungufu katika uzalishaji na usambazaji wa ndani na kupanda kwa gharama za maisha kwa wananchi nilihoji uongozi wa serikali na bunge sababu za bunge kutokukaa kama kamati ya mipango kama kanuni za bunge zinavyohitaji na badala yake kufanyiwa semina ya hali ya uchumi tarehe 8 Februari 2012.

Nilieleza bayana kwamba matarajio yangu katika mkutano huu wa sita wa bunge ilikuwa ni serikali kuwasilisha bungeni mpango wa haraka wa kunusuru uchumi wa nchi, kupunguza mfumuko wa bei na kudhibiti kuporomoka kwa thamani ya shilingi yetu ukilinganisha na sarafu nyingine badala ya semina ya hali ya uchumi ambapo mada zinaweza zikatolewa na wabunge wakatoa maoni mazuri lakini yasiingizwe katika utekelezaji ya kiserikali na bajeti ya taifa.

Kanuni ya 94 ya Kanuni za Kudumu za Bunge inaelekeza “Ili kutekeleza majukumu yaliyoanishwa katika ibara ya 63(3) (c) ya katiba, Bunge litakaa kama Kamati ya Mipango katika Mkutano wake wa Mwezi Februari ili kujadili na kushauri kuhusu mapendekezo ya Serikali katika mwaka wa fedha unaofuata”.

Pamoja na kuhoji ni lini mpango utaletwa na kujibiwa na Waziri wa Fedha Mustapha Mkullo na Spika wa Bunge Anna Makinda kuwa mpango utajadiliwa katika Mkutano wa Saba wa Bunge mwezi Aprili; nilitoa pia mawazo yangu kuhusu hatua ambazo zinapaswa kuchukuliwa na serikali kwa haraka kupunguza mfumuko wa bei nchini na kudhibiti kupanda kwa gharama za maisha kwa wananchi hali ambayo ni tishio kwa uchumi na usalama wa nchi na maisha ya wananchi kwa ujumla.

Friday, February 10, 2012

Kutoka Bungeni: Sheria ya Katiba; Maji Ubungo na Kiwanda cha Urafiki

Kutoka Bungeni: Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba; Maji Jimboni Ubungo mitaa ya pembezoni na Hatma ya Kiwanda cha Nguo cha Urafiki

09/02/2012 nilichangia kwa maandishi muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba wa mwaka 2011; katika mchango wangu nilirejea pia msingi wa mapendekezo niliyoyatoa awali wakati wa kuwasilisha taarifa ya hoja binafsi kuhusu mchakato wa katiba mpya na uchambuzi niliofanya mara baada ya kuchapwa kwa muswada wa sheria husika kwa mara ya kwanza: http://mnyika.blogspot.com/2011/04/tamko-la-awali-kuhusu-muswada-wa.html. Nashukuru kwamba hatimaye harakati tulizoanza miaka mingi na zikapata msukumo mwezi Disemba 2010 ya kutaka mchakato wa katiba kuanzia bungeni kupitia kwa bunge kutunga sheria juu ya tume shirishi ya katiba, bunge maalum la katiba na hatimaye katiba kuhalalishwa kwa kura ya maoni zimepiga hatua nyingine kwa marekebisho ya sheria kuwasilishwa bungeni. Hata hivyo izingatiwe kuwa marekebisho ya sheria yaliyowasilishwa bungeni tarehe 09 Februari 2011 ni awamu ya kwanza, kuhusu tume na mchakato wa kukusanya maoni pamoja na kuandaa rasimu. Bado mabadiliko yanahitajika katika awamu ya pili na ya tatu; kuhusu bunge maalum la katiba na hatua ya kutunga katiba na kura ya maoni na mchakato wake kusimamiwa na tume ya uchaguzi. Katika mchango wangu nimeeleza pia kwamba bado kifungu cha 21 pamoja na adhabu kupunguzwa bado ziko juu; hivyo nimeendelea kutaka makosa yatenganishwa kati ya makosa ya kijinai ambayo yanaweza kuhukumiwa kwa kutumia sheria ya adhabu (penal code) na makosa ya kawaida katika mchakato wa kutoa elimu juu ya mabadiliko ya katiba na kukusanya maoni. Adhabu ya makosa ya kawaida inapaswa kuwa ndogo ya kawaida ili kutokufanya wananchi wapate hofu ya kushiriki kwa uhuru kwenye mchakato wa katiba na pia ili kulinda haki za msingi za kikatiba za kupata taarifa na kutoa maoni. Nasikitika kwamba sikuwepo jana jioni na leo asubuhi wakati bunge limekaa kama kamati kuhusu muswada husika kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu; hata hivyo kwa kuwa awamu nyingine zitafuata za marekebisho ya sheria husika, bado ipo nafasi ya kuendelea kufanya marekebisho mengine ya ziada.

Wednesday, February 8, 2012

Kutoka Bungeni: Hadhi ya Barabara DSM; mgomo wa madaktari ; Uchaguzi Afrika Mashariki; Sheria ya Fedha Haramu; utalii na ajira pori la Pande

Kutoka Bungeni: Hadhi ya Barabara DSM; mgomo wa madaktari ; Uchaguzi Afrika Mashariki; Sheria ya Fedha Haramu; utalii na ajira pori la Pande

Katika kuendelea kuwawakilisha wananchi nimeendelea kuisimamia serikali katika masuala yafuatayo:

Leo 08/02/2011 nimeulizwa swali la nyongeza kuhusu barabara za Dar es salaam kwa lengo la kuharakisha uboreshaji wa miundombinu ya pembezoni na kuchangia kupunguza foleni. Kwa muda mrefu kikwazo cha ujenzi wa barabara, madaraja na mifereji kimekuwa ni kiwango kidogo cha fedha ambacho TANROADS Mkoa wanatengewa. Nimetoa mfano wa mfereji wa Malapa Ilala Bungoni ulihitaji tu 2.3 Bilioni kukamilika lakini toka mwaka 2009 mpaka leo ujenzi bado unaendelea ukisuasua; nikata Wizara ya Ujenzi ieleze ni lini barabara za Dar es salaam zitapandishwa hadhi kwa orodha ambayo tulishawasilisha serikalini miaka kadhaa iliyopita ili ziongezewe bajeti ujenzi uweze kuharakishwa? Waziri Magufuli amekiri kweli fedha zilikuwa zikitengwa kidogo, amekubali kuwa ameshapokea orodha ya barabara husika na ameahidi kwamba wataalamu wake wanazipitia na karibuni atatoa taarifa ya barabara zilizopandishwa hadhi. (Swali hili nimeuliza kufuatilia masuala niliyowahi kuyazungumza hapa: http://mnyika.blogspot.com/2012/01/kuhusu-msongamano-wa-magari-dsm-na.html

Aidha, nimeandika barua kwa Spika kuhusu mgomo wa madaktari kama ambavyo mlishauri jana nilipoandika ujumbe huu: http://mnyika.blogspot.com/2012/02/mgomo-wa-madaktari-bungeni-tena-leo.html; kikao cha Kamati ya Uongozi ya Bunge cha dharura kinaendelea hivi; nimeshauri hayo mapendekezo saba niliyoyatoa kwenye hiyo barua yazingatiwe na bunge litoe taarifa ya haraka kuhusu hatua ambazo zimechukuliwa mpaka sasa. Aidha, nimetoa mwito kwa Rais kuweza kutaarifiwa naye kuweza kuingilia kati kwa mujibu wa mamlaka yake ya kikatiba ya kwenye ibara ya 34 na 35.

Tuesday, February 7, 2012

Mgomo wa Madaktari bungeni tena leo; nilitaka hatua hizi zichukuliwe

Leo Mbunge wa Mbozi Geofrey Zambi alitoa hoja ya bunge kujadili suala la mgomo wa madaktari kwa dharura kufuatia taarifa kuwa madaktari bingwa nao wameingia kwenye mgomo. Spika Anna Makinda alizuia hoja hiyo kwa maelezo kuwa suala hilo bado linashughulikiwa na bunge kupitia kamati yake ya huduma za jamii. Baada ya maelezo ya Spika niliomba muongozo hata hivyo sikupatiwa nafasi.

Kimsingi nilitaka kuelieza bunge kwamba maelekezo yaliyotolewa na Naibu Spika Job Ndugai yanahitaji kuongezewa maagizo ya ziada na Bunge ili wadau wote wakawa na imani kwamba suala hili linashughulikia kwa dharura na kwa mwelekeo stahiki hali ambayo itashawishi mgomo kuweza kusitishwa.

Hadidu rejea na ratiba ya kamati inapaswa iwe bayana hivyo kuna umuhimu wa uongozi wa bunge kutoa tamko lenye maelezo ya ziada kwa kuwa kimsingi madaktari walishapoteza imani na namna ambavyo serikali kupitia kwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na Ofisi ya Waziri Mkuu imekuwa ikishughulikia masuala yao.

Aidha, imani hiyo ilipoteza zaidi baada ya uamuzi wa Waziri wa Afya na Ustawi wa jamii kutoa maelezo yasiyokuwa ya kweli bungeni kuhusu madai ya madaktari na hali ya mgogoro mzima. Bunge na uongozi wa bunge unapaswa kuwa makini katika mazingira ya sasa ili kuepusha uwezekano wa madaktari na wananchi kwa ujumla kupunguza imani pia na namna ambavyo mgogoro huu unashughulikiwa.

Sunday, February 5, 2012

Kutoka Bungeni: Sheria ya Fedha Haramu; vyama vya siasa na tishio kwa mamlaka ya Bunge

Nashukuru wote waliounga mkono marekebisho niliyowasilisha tarehe 03/02/2012 kwenye sheria (The Anti Money Laundering (Amendments Act) 2012 ya kumwingiza msajili wa vyama vya siasa kuwa sehemu ya wadhibiti wa masuala ya fedha haramu. Kwa upande mwingine, nawashukuru wote waliotikia NDIYO (kwa kujua au kutokujua) kuunga mkono marekebisho mengine ambayo niliyawasilisha katika sheria husika ya kuongeza ukubwa wa adhabu kutoka na makosa ya ujumla ya kukiuka Sheria ya Udhibiti wa Fedha haramu.

Katika kuwasilisha hoja hiyo ya marekebisho nilifanya rejea katika Ripoti ya Utafiti ya Juni mwaka 2011 iitwayo “The Political Economy of the Investment Climate in Tanzania” iliyotolewa na “Africa Power and Politics”, ripoti ambayo imefanya rejea pia ya masuala ambayo vyama vya siasa hususan CHADEMA, vyombo vya habari na asasi za kiraia nchini kwa nyakati mbalimbali viliyaibua kuhusu fedha haramu katika siasa nchini hasa wakati wa uchaguzi uliofanywa na CCM na wagombea wake.

Katika hoja hiyo nilisisitiza kuwa tatizo la dola kutekwa (state capture) lina athari kubwa zaidi kwa nchi na maisha ya wananchi hivyo udhibiti wa fedha haramu kwenye kuingiza viongozi madarakani ni suala la muhimu ili kuepusha baadhi ya vyama kama ilivyokuwa kwa CCM kutumia fedha za kifisadi kama za EPA-Kagoda, Deep Green, Tangold na Meremeta katika uchaguzi.

Nilisema kwamba kumuingiza msajili wa vyama vya siasa ambaye amepewa mamlaka ya kudhibiti matumizi ya fedha katika vyama vya siasa, viongozi wake na wagombea wake nyakati zote ikiwemo katika uchaguzi itaongeza nguvu katika utekelezaji wa sheria ya udhibiti wa fedha haramu. Nilifanya hivyo kwa kurejea Election Expenses Act 2010 (Kifungu 4 na 5) na The Political Parties Acti no. 5 ya 1992 (Kifungu cha 13 na 14).

Kutoka Bungeni: Mgomo wa Madaktari; bado hakijaeleweka

Nashukuru kwamba walau tofauti na tarehe 02/02/2012 ambapo Naibu Spika Ndugai alipotosha muongozo nilioomba akadai kuwa ni hoja isiyoungwa mkono na kuipuuza; tarehe 03/02/2012 amezingatia muongozo nilioomba na kutoa mwelekeo ambao umeongeza msukumo katika bunge kufanya kazi yake ya kuisimamia serikali.

Hata hivyo, bado muongozo uliotolewa haujitoshelezi kwa kuwa jukumu hilo kwa kamati ya huduma za bunge halikuelezwa bayana limeanza lini na litamalizika lini. Vyanzo kadhaa vimeeleza kwamba taarifa ya kamati husika itawasilishwa kwenye mkutano ujao wa bunge (Mkutano wa Saba), suala ambalo halipaswi kukubaliwa. Kutokana na uzito na udharura wa mgogoro huu ni muhimu taarifa ya awali ya kamati iliyopewa jukumu ikawasilishwa katika mkutano huu wa sita unaoendelea ili hatua za haraka zikachukuliwa katika kushughulikia madai ya madaktari na kupata taarifa ya kweli kuhusu athari za mgogoro na mgomo ulioendelea ikiwemo vifo vilivyotokea.

Aidha, Kamati husika ingepewa hadidu rejea za wazi ikiwemo ya kufanya kazi ya usulushi na upatanishi katika mgogoro ambao umetokea baina ya madaktari na serikali na pia kuwezesha bunge kusimamia ipasavyo na kwa haraka serikali katika kushughulikia madai ya wafanyakazi.

Kwa upande mwingine, kwa kuwa imebainika wazi kwamba kuna uzembe na udhaifu miongozi mwa watendaji wakuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii wakiongozwa na Waziri wa Wizara husika ambaye amefikia hatua hata ya kutoa taarifa ya kulidanganya bunge; ni vizuri baada ya Kamati husika kusikiliza pande zote mbili Waziri na watendaji husika walazimishwe kujiuzulu ili hatua za kushughulikia madai ya madaktari na kuboresha huduma za afya katika hospitali za umma zitekelezwe na wateule wengine wenye uwezo na dhamira ya kweli ya kushughulikia matatizo yaliyojitokeza.

Thursday, February 2, 2012

BUNGENI LEO: Mgomo wa madaktari na Sheria ya Bodi ya Mikopo

Asubuhi ya leo Naibu Spika Job Ndugai alitumia kanuni vibaya kuzuia hoja ya dharura bungeni kuhusu mgomo wa madaktari. Kimsingi, sikuwasilisha hoja ila niliomba muongozo wa Spika ili niweze kupatiwa nafasi ya kuwasilisha hoja ya dharura. Kwa kuwa hoja kama hiyo iliwasilishwa juzi na ikaungwa mkono lakini Spika akasema ameshakubaliana na serikali kuwa ingewasilisha kauli. Hata hivyo, jana hakukuwa na kauli ya serikali huku wananchi wakiendelea kupata madhara ya mgomo. Hivyo nikata muongozo kwa kuwa Spika alitumia kanuni ya 49 (2) ambayo kimsingi inatoa mwanya kwa kauli ya serikali kuwasilishwa kwenye wakati atakaoona yeye kuwa na unafaa juu ya jambo linaihusu serikali na lisilozua mjadala. Nilitaka kanuni hiyo isitumike badala yake wabunge tutimize wajibu wa kuisimamia serikali kwa kutumia kanuni ya 47 kuhusu hoja ya dharura. Kwa kuwa ilikuwa muongozo hakukuwa na hitaji la kikanuni la wabunge wengine kuunga mkono lakini akaamua kuilinda serikali kwa kuwa hawakuwa wamejiandaa. Lakini mwishoni ameahidi kuwa kauli ya serikali itatolewa kesho.

Jioni ya leo bunge litajadili Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali na.2 wa mwaka 2011 ambao kwa sehemu kubwa ukiondoa sheria nyingine unahusu marekebisho ya kimsingi katika sheria ya bodi ya mikopo. Ni kwa bahati mbaya kwamba muswada huu umeletwa na hoja ya kusomwa kwa hatua zake zote tatu katika mkutano mmoja hivyo hakutakuwa na muda wa kukusanya maoni ya wadau kwa upana wake. Ni sehemu ndogo sana ya vifungu vya muswada huu ndio inapaswa kukubalika lakini kwa ujumla muswada huu unakwenda kuingiza mambo ambayo tuliyapinga kwa makongamano, migomo na maandamano yakaondolewa wakati sheria husika inatungwa mwaka 2004. Maudhui ya muswada huu yamenifanya nikumbuke makala ambayo niliandika mwezi kama huu lakini mwaka 2007: http://www.chadema.or.tz/makala/makala.php?id=43 Marekebisho haya yanaenda kuweka mazingira mengine ya migogoro katika elimu ya juu nchini kutokana na masuala ya mikopo kwa wanafunzi. Muswada huu ulipaswa kuja bungeni baada ya ripoti ya Tume ya Rais iliyoundwa tarehe 14 Februari 2011 na kukabidhi taarifa yake tarehe 29 Aprili yenye mapendekezo ya jinsi ya kuboresha utaratibu wa sasa wa ugharamiaji, utoaji na urejeshaji wa mikopo ya elimu ya juu kuwekwa wazi kwa bunge na kwa umma ili kufanya marekebisho mapana zaidi ya kimfumo.

Tuesday, January 31, 2012

Hatimaye mkataba wa vijana wa Afrika waletwa bungeni kuridhiwa

Kwa Vijana wenzangu kwa nafasi na wote wenye nafsi za ujana, leo ule mkataba wetu wa Afrika (African Youth Charter) hatimaye unaingia bungeni kuridhiwa. Ni matokeo ya harakati zetu za miaka mingi kabla na hata baada ya Rais Kikwete kuusaini Gambia mwaka 2006 lakini ukaishia makabatini. Baada ya kunituma bungeni kuwatumikia mkataba huu ni kati ya mambo niliyohoji mara kwa mara kutaka uletwe bungeni kuridhiwa ili utekelezaji wake uweze kuanza.

Nawashukuru wote tuliounganisha nguvu kwenye harakati za vijana kwa nyakati mbalimbali kuanzia NYF, TYVA, YUNA, TSNP, UDSM, BAVICHA, asasi zingine na mwisho lakini kwa umuhimu mkubwa vijana wote tuliokesha pamoja kulinda kura Loyola.

Kwa kurejea nyuma katika historia, nawaletea moja ya ujumbe nilioandika kwenu na kwa vijana wa Afrika mwaka 2008: http://mnyika.blogspot.com/2008/10/vijana-tufikiri-na-kuungana-kukomboa.html Kila kizazi lazima kiitambue dira na dhima yake; ama kisaliti au kitimize. Tuendelee kuwajibika; kwa pamoja tunaweza.

John Mnyika
Bungeni, Dodoma-01/02/2012

Saturday, January 28, 2012

Taarifa ya Hoja kuhusu utekelezaji wa maazimio juu ya Richmond

Tarehe 25 Januari 2012 nimewasilisha kwa Katibu wa Bunge taarifa ya hoja kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la 2007 Kanuni 54 (4) na 55 (1) kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge juu ya mkataba baina ya TANESCO na Kampuni ya Richmond Development Company LLC.

Hoja hiyo ikipewa nafasi ya kuwasilishwa na kujadiliwa itaongeza msukumo wa utekelezaji wa maazimio ya bunge na hivyo kuchangia katika mapitio ya mikataba yenye kuongeza bei ya umeme; kuweka mfumo wa kulihusisha bunge katika maandalizi ya mikataba yenye maslahi ya taifa ikiwemo katika mafuta, gesi asilia na ujenzi na kuwezesha uwajibikaji na hatua kamili kuchukuliwa kwa waliohusika na ufisadi na uzembe uliolisababishia hasara taifa.

Taaarifa hii ya hoja niliiwasilisha awali tarehe 13 Aprili 2011 na kupatiwa majibu; hata hivyo niliijibu ofisi ya bunge kupatiwa taarifa ya utekelezaji uliofanywa na serikali baada ya Februari 2010 bila kupatiwa majibu hivyo nimeiwasilisha tena ili hoja husika ijadiliwe.

Lengo la Hoja Binafsi nitakayoiwasilisha kufuatia taarifa hiyo ni kutaka uamuzi wa Bunge uliofanyika katika Bunge la Tisa Mkutano wa 18 mwezi Februari 2010 kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge juu ya mkataba baina ya TANESCO na kampuni ya Richmond Development Company LLC; UBADILISHWE.

Friday, January 27, 2012

Kuhusu Msongamano wa Magari DSM na Ziara Kwembe

Nashukuru kwamba jana Serikali ilituma ujumbe wa kuonana ana kwa ana madaktari; hata hivyo ni muhimu ikayafanyia kazi yaliyowasilishwa jana ili leo kuwa na ujumbe mzito zaidi majadiliano yakamilike kwa haraka ili madaktari warejee kazini. Leo naendelea na kazi za kijimbo:

Mosi, nitashiriki mkutano wa wadau kuhusu tatizo la msongamano wa magari katika mkoa wa Dar es salaam. Serikali imeleta kwa dharura mwaliko wa mkutano huo jana hivyo sijapata wasaa wa kuomba maoni yenu kuhusu utekelezaji, mnaweza kuendelea kuyatoa hapa na tutayaunganisha pamoja na kuyawasilisha kwa mamlaka husika. Nimekosa pia fursa ya kuandika uchambuzi wangu kwa ajili ya kuchochea mjadala hivyo hoja zangu nitakwenda kuzitoa moja kwa moja kwenye mkutano papo kwa papo. Kwa ujumla, huu si wakati wa maneno bali matendo; mikutano kuhusu foleni katika jiji la Dar es salaam imeshafanyika kadhaa kati ya mwaka 2005-2010, maoni yametolewa na mipango imeandaliwa. Kinachotakiwa hivi sasa ni kuunganisha nguvu ya wadau katika kuhamasisha na kuharakisha utekelezaji. Na katika kufanya hivyo, kunahitajika nyongeza ya bajeti kwa kuwa kiwango kilichotengwa kwa ajili ya kupunguza msongamano katika jiji la Dar es salaam kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ni kidogo ukilinganisha na ukubwa wa tatizo, kiasi cha mahitaji na hasara ambayo wananchi na nchi inapata kila siku kutokana na msongamano katika Jiji la Dar es salaam.

Kuitishwa kwa mkutano wa leo kumefanya nikumbuke ujumbe wangu ambao niliuandika kwenye mtandao wa Wanabidii tarehe 14 Disemba mwaka 2011 nikichangia mjadala na kujibu baadhi ya maswali yaliyoulizwa. Takribani mwezi mmoja na nusu umepita toka niandike ujumbe huo, ambapo yapo ambayo tayari nimeshayafuatilia mwezi huu wa Januari kupitia vikao vya bodi ya barabara, RCC, Jiji na Manispaa na hatua zimeanza kuchukuliwa kama sehemu ya kuchangia katika kupunguza foleni katika jiji la Dar es salaam hususani Jimboni Ubungo. Hata hivyo, nanukuu mchango wangu huo kwa kuwa kuna mambo bado ambayo niliyasema wakati huo lakini yanaweza kuendelea kujadiliwa na wadau katika mkutano wa leo:

“ Nitachangia tu kwa ujumla bila kutenganisha hatua kati ya za dharura, muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu.

KUHUSU MGOMO WA MADAKTARI

Mgomo wa madaktari unaoendelea hivi sasa umedhihirisha kwamba tuna serikali dhaifu yenye ombwe la uongozi. Haiwezekani wananchi wakawa wanakufa kwa kukosa matibabu stahiki na wengine wakipata madhara kutokana na kuchelewa kupata matibabu sababu ya mgomo wa madaktari halafu viongozi wenye dhamana hawachukui hatua sahihi.

Rais Jakaya Kikwete ambaye ndiye mwenye dhamana kwa mujibu wa katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 33 ndiye kiongozi wa shughuli za serikali na ibara ya 35 shughuli zote za utendaji wa serikali zinatekelezwa na watumishi wa serikali kwa niaba ya Rais; ameondoka kwenda nje ya nchi mgomo ulipoanza na hakuna kauli yoyote mpaka sasa toka kwa Makamu wa Rais wala kwa Ikulu.

Waziri Mkuu Mizengo Pinda badala ya kwenda kwenye eneo la mgomo na kuzungumza na madaktari naye ameishia kuzungumza na vyombo vya habari. Waziri wa Afya Dk. Haji Mponda na Naibu Waziri Dk. Lucy Nkya nao jana wamezungumza na waandishi wa habari badala ya kwenda kukutana na madaktari na kuzungumza nao kuhusu madai yao ya msingi.

Kwa upande wetu CHADEMA tulitoa kauli tarehe 25 Januari 2012 ya kutaka serikali ichukue hatua na tuliona tuipe serikali nafasi ifanye kazi yake hata hivyo serikali haionyeshi kuupa uzito unaostahili mgogoro huu wenye kuathiri hali za wagonjwa na maisha ya wananchi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Saturday, January 14, 2012

TANZIA

Mh. Regia Mtema; Mbunge wa Viti Maalum na 
Waziri Kivuli wa Kazi na Ajira  
Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimepatwa na majonzi makubwa na kinasikitika sana kwa kifo cha Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Taifa, Mheshimiwa Regia Mtema ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum na Waziri Kivuli wa Kazi na Ajira. Mheshimiwa Regia Mtema amefariki leo tarehe 14 Januari 2011 kwa ajali ya gari katika eneo la Ruvu darajani. 

Katika uhai wake marehemu Regia Mtema amefanya kazi mbalimbali za kisiasa na kijamii katika taifa. Marehemu Regia Mtema amezaliwa tarehe 21 mwezi Aprili mwaka 1980 na kusoma shule za sekondari kidato cha kwanza mpaka cha sita katika shule ya sekondari ya Forodhani na Shule ya Wasichana ya Sekondari ya Machame. Marehemu Regia Mtema alipata shahada yake ya kwanza (Bsc Home Economics and Human Nutrition) katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine. 

Mara baada ya kuhitimu masomo yake marehemu Regia Mtema alifanya kazi katika taasisi mbalimbali kabla ya kujiunga na CHADEMA na kuteuliwa kuwa Afisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Vijana ya CHADEMA na baadaye kuteuliwa kuwa Afisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Mafunzo ya CHADEMA nafasi ambayo aliishikilia hadi mwaka 2010 alipoteuliwa kuwa mbunge wa viti maalum. 

Monday, January 9, 2012

Magufuli hajasema kweli; Anaficha Udhaifu wa Serikali na Wizara yake

TAARIFA KWA UMMA

UTANGULIZI

Tarehe 4 na 5 Januari 2011 Waziri wa Ujenzi Mheshimiwa John Magufuli alinukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari akitoa madai mbalimbali juu yangu wakati akijibu kauli za Wabunge wa Dar es salaam juu ya ongezeko la nauli katika vivuko vya Kigamboni na maeneo mengine nchini.Toka Waziri Magufuli atoe kauli zisizokuwa za kweli dhidi yangu badala ya kujibu hoja za msingi nilizotaka maelezo toka wizara yake na serikali kwa ujumla sikutoa tamko kwa kuwa nilikuwa katikati ya kazi mbalimbali jimboni Ubungo na majukumu mengine ya kitaifa.

Hata hivyo, kuna msemo kwamba ‘uongo ukiachwa ukarudiwa rudiwa unaweza kuaminika kuwa ndio ukweli’; hivyo naomba kutoa taarifa kwa umma kujibu madai hayo kwa lengo la kuweka rekodi sahihi.Namheshimu Waziri Magufuli, hata hivyo kauli alizozitoa dhidi yangu zinadhirisha kuwa ameanza kulewa sifa kwa kiwango cha kuwa mpotoshaji na mzushi. Ni vyema umma ukachukua tahadhari kwamba imani ya wananchi juu yake ameanza kuitumia vibaya kulinda uzembe, ubabe na ufisadi.Aidha, ni muhimu akawa anajielekeza kujibu madai ya msingi ya wananchi badala ya kuibua masuala mengine kwa lengo la kuhamisha mjadala; hivyo nitarudia tena masuala ambayo nilitaka ayatolee maelezo na vielezo kwa maslahi ya umma.

Thursday, January 5, 2012

Kuhusu kauli za Waziri Magufuli

Kwa wote mliotaka maoni yangu juu kuhusu kauli za Waziri Magufuli vyombo vya habari kuhusu mbunge wa Ubungo na Jimbo letu. Katika siku hizi tatu sina muda wa malumbano, niko katikati ya kazi ya kuwatumikia wananchi jimboni na kutekeleza wajibu mwingine wa kitaifa. Wananchi na wadau wengine mnaweza kumwambia ukweli mnaoufahamu kuhusu aliyoyasema mkipenda, kwa kuwa matendo yanazungumza zaidi ya maneno. Mjadala huu na mingine ni muhimu pia kubadilisha mifumo na kurejesha utamaduni wa uwajibikaji katika taifa letu. 

Mambo ambayo amesema kwamba siyashughulikii ukweli ni kwamba nilishachukua hatua kwa nyakati mbalimbali kwenye mwaka 2011 ndani ya bunge, kwenye halmashauri na pia nje ya bunge, na matokeo yameanza kuonekana. Baadhi ya hatua hizo nilimhoji yeye mwenyewe au mamlaka za Wizara yake kama sehemu ya kutimiza wajibu wa kibunge wa kuwakilisha wananchi, kutunga sheria na kuisimamia serikali. 

Kwa bahati mbaya amekuwa msahaulifu hata wa kauli zake mwenyewe kuhusu masuala niliyoyaibua, amelewa sifa kwa kiwango cha kusema maneno yasiyokuwa ya kweli, imani juu yake imempa upofu wa kupindisha mambo mbalimbali na kugeuzia watu wengine mambo ambayo yeye mwenyewe au wenzake katika serikali wamefanya uzembe wa kutochukua hatua kwa wakati. Kwa bahati nzuri, ukweli una sifa moja, huwa unadumu milele; nitamjibu hoja kwa hoja nikipata wasaa kwa sasa naendelea na utumishi, maslahi ya UMMA kwanza.

Wednesday, January 4, 2012

Kazi za leo jimboni Ubungo

Leo nimeendelea na kazi za kibunge jimboni katika kata ya Kwembe nimefanya ziara na kukutana na wananchi, wameniuliza maswali kuhusu maji, barabara ya kwenda Mpiji Magohe, Luguruni Satellite town, mgogoro wa ardhi katika eneo la Msakuzi na uharibifu wa daraja katika mto Mdidimua/Kibwegere (Mji Mpya). Nimewajibu hatua ambazo nimechukua kwa kila jambo.

Pia nimekabidhi Jengo la Kituo cha Afya na Mama na Mtoto Kata ya Kwembe Jimboni Ubungo, tulichojenga kwa fedha za Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo (CDCF). Habari zaidi zitafuata; Maslahi ya Umma KWANZA.