Thursday, June 30, 2011

Marekebisho niliyowasilisha kupunguza bei ya mafuta

MHE. JOHN MNYIKA (22/06/2011) : Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba kuwasilisha mabadiliko ambayo yanahusu kifungu cha (8) cha Muswada wa Sheria ya Fedha ukurasa wa (5) na yanahusiana vile vile na ukurasa wa (2) wa schedule iliyowasilishwa na Serikali kipengele cha (e).


Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu yanakusudia na nitasoma: “In clause eight which relates to the fourth schedule by inserting under heading 27.10 and just before its code 27.10, the following particulars, particulars nyingine ziko kama ambavyo zimeelezwa na Serikali isipokuwa kwenye sehemu ya new excise rate ambapo napendekeza kwamba iwe ni shilingi 300.30 kwa upande wa mafuta ya taa na shilingi 115/= kwa upande wa gas oil.


Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa mapendekezo haya, hoja ambayo Serikali imeikubali ambayo ni ya wananchi na imetolewa na Kambi ya Upinzani ni kushusha gharama za maisha. Hoja hii imekuwa na sura mbili kwa upande wa suala hili tunalozungumza la mafuta, kuna suala la tozo za mafuta na kuna suala la kodi za mafuta, lakini ukiyatazama sasa mapendekezo ya Serikali yaliyoko kwenye ukurasa wa pili wa schedule ya kupandisha kodi ya mafuta ya taa kutoka shilingi 52/= mpaka shilingi 400.30 ikiwa ni ongezeko la zaidi ya takriban 600%, wakati huo huo kupunguza kodi ya mafuta haya mengine ikiwemo dizeli kwa kiwango kidogo sana cha kutoka shilingi 314/= mpaka shilingi 215/= peke yake ambayo ni sawasawa na punguzo la sh 99/=, peke yake kwenye kodi iliyoko kwenye mafuta


Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni kwamba halikujikita kwenye lile lengo la msingi la kupunguza gharama za maisha, bali imelenga lengo la msingi lingine ambalo na lenyewe naliunga mkono la kupunguza uchakachuaji ambao umekuwa ukiligharimu Taifa hasara ya sh. bilioni takriban 50, gharama ya uharibifu wa magari na kuharibu biashara ya usafirishaji wa mafuta. Ni hoja ambayo naiunga mkono lakini namna ambavyo imechukuliwa na Serikali imelenga kuondoa uchakachuaji bila kuelekea kwenye suala la kupunguza bei za mafuta.


Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi naunga mkono kabisa msimamo na maoni ya wote kwamba tusiguse kodi ya ushuru wa magari kwa maana ya fuel levy shilingi 200/= kwa sababu inatusaidia kwenye kujenga barabara zetu. Lakini pamoja na kuacha kugusa fuel levy Serikali imeshindwa kufanya uamuzi mgumu wa kukubali kugusa kwa kiwango kikubwa zaidi kidogo excise duty ili kuweza kwenda kweli kupunguza bei ya mafuta.


Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa marekebisho haya ya kuwianisha bei ya mafuta na bei ya petroli yazingatiwe ili usimwongezee mzigo sana mtu anayetumia mafuta ya taa na wakati huo huo usimwongezee mzigo mtumiaji wa daladala, pikipiki na vyombo vingine vya usafiri.

Nakala ya Jedwali la Marekebisho unaweza kuipata kupitia: http://mnyika.blogspot.com/2011/06/schedule-of-ammendments-on-finance-bill.html

No comments: