Wednesday, May 22, 2013

Maoni na Mapendekezo ya CHADEMA juu ya Rasimu Muongozo uliotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuhusu Mabaraza ya Katiba ya Asasi, Taasisi na Makundi yenye mlengo yanayofanana


1.0. UTANGULIZI 

Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Sura ya 83 (kifungu cha 18 (3)) imetoa wajibu kwa tume wa kuunda Mabaraza ya Katiba kwa ajili ya kupitia na kutoa maoni juu ya Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume.

Kifungu cha 17 (8) kinaeleza kuwa, isipokuwa kama mazingira yatahitaji vinginevyo, Tume itabuni utaratibu unaofanana ambao utatumika kila upande wa Muungano. 

Kifungu cha 18 (6) kinaeleza aina nyingine ya Mabaraza ya Katiba kwa kueleza kuwa Tume inaweza kuruhusu Asasi, Taasisi au Makundi ya Watu kuwasilisha maoni yao kuhusu Rasimu ya Katiba. 

Ikumbukwe kwamba Kamati Maalum ya CHADEMA ilikutana na Tume ya Mabadiliko ya Katiba tarehe 7 Januari 2013 kuwasilisha maoni ya CHADEMA kuhusu katiba mpya kama ilivyoalikwa lakini pia kutumia fursa hiyo kuwasilisha mapendekezo ya CHADEMA kuhusu marekebisho na maboresho yanayohitajika kuhusu mchakato wa mabadiliko ya katiba ili kupata katiba bora. 

Tarehe 31 Januari 2013 Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilitoa taarifa kwamba imeamua kuwa Mabaraza ya Katiba yatakuwa katika makundi mawili yafuatayo: Mabaraza ambayo Tume itayasimamia na kukusanya Maoni (Mabaraza ya Katiba ya Wilaya – Ngazi ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa) na Mabaraza ambayo Tume haitayasimamia. Mabaraza hayo yatajisimamia yenyewe na kukusanya maoni yatakayowasilishwa kwenye Tume kwa mujibu wa maelekezo. (Mabaraza ya Katiba ya Asasi, Taasisi na Makundi ya Watu). 

CHADEMA baada ya kupitia muongozo huo na kwa kuzingatia kuwa tayari tume ilishafanya uamuzi kuwa mabaraza ya katiba yatakuwa ya wilaya, tarehe 14 Februari 2013 kiliwasilisha maoni na mapendekezo yake kuhusu uteuzi wa wajumbe ambayo kwa sehemu kubwa hayakuzingatiwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na hivyo kusababisha matatizo makubwa katika mchakato mzima wa uteuzi wa mabaraza ya katiba ya wilaya. 

Kufuatia hali hiyo katika Maoni ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusu hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tulitangaza kwamba CHADEMA itajitoa ushiriki wake katika mchakato wa Katiba Mpya endapo mambo yafuatayo hayatapatiwa ufumbuzi hadi kufikia tarehe 30 Aprili, 2013: 

HOTUBA YA MSEMAJI WA KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI WIZARA YA NISHATI NA MADINI JOHN JOHN MNYIKA (MB) KUHUSU MAONI YA KAMBI RASMI YA UPINZANI JUU YA MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA MWAKA 2012/2013 NA MAKADIRIO YA MATUMIZI YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014

(Inatolewa chini ya kanuni ya 99(9) toleo la mwaka 2013)


A: UTANGULIZI

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Waziri wa Nishati na Madini ilianzishwa kwa mujibu wa kipengele cha 21 cha Nyongeza ya Waraka wa Rais uliochapishwa kama Tangazo la Serikali Na. 494 la tarehe 17 Desemba 2010. Majukumu ya Ofisi hii yameainishwa katika Tangazo la Ukasimishaji wa Majukumu ya Kiuwaziri la mwaka 2010 (The Ministers [Assignment of Ministerial Functions] Notice, 2010) lililochapishwa katika Gazeti la Serikali kama Tangazo la Serikali Na. 494A la tarehe 17 Desemba 2010.

Mheshimiwa Spika, Katika kujadili Mapitio ya Utekelezaji kwa mwaka wa fedha 2012/2013 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2013/2014 naomba tuyatafakari maandiko ya katika muktadha wa uongozi wetu wa leo na hatma ya sekta hizi mbili muhimu za nishati na madini.

Mheshimiwa Spika, Mwalimu Nyerere katika kitabu chake cha TUJISAHIHISHE katika ukurasa wa pili tutafakari kwamba, naomba kumnukuu ‘ukweli una tabia moja nzuri sana. Haujali mkubwa wala mdogo; haujali adui wala rafiki. Kwake wote ni sawa. Pia ukweli unayo tabia ya kujilipiza kisasi kama ukipuuzwa.Ukiniona nataka kulipiga teke jiwe kwa kuwa nafikiri kuwa ni dongo au mpira, natumaini utanionya. Lakini nikilipuuza onyo lako kwa sababu eti wewe ni mdogo au kwa sababu sikupendi, nitalipiga teke, basi litanivunja dole japo ningekuwa nani. Ukweli haupendi kupuuzwapuuzwa.


Mheshimiwa Spika, Tuendelee kutafakari maandiko ya Nyerere kwamba ‘Wakati mwingine, mtu tunayempinga huwa anamakosa kweli, lakini hoja tunazozitoa ni za kinafsi na hazihusiani kabisa na hoja zake.Nikisema mbili na tatu ni sita, nakosa. Lakini ni bora kunionyesha kwamba pengine nilifikiri tunazidisha kumbe tunajumlisha.Ni kweli mbili mara tatu ni sita;lakini mbili na tatu ni tano, siyo sita. Lakini ukijaribu kuwashawishi wenzetu wakatae mawazo yangu na kukubali yako kwa kusema kuwa meno yangu ni machafu ,au natoa kamasi daima, utakuwa unatumia hoja ambazo hazina maana, Huu ni mfano wa upuuzi; lakini mara nyingi hoja tunazozitumia kuwashawishi watu wakatae mawazo ya wale tusiowapenda,au kukubali mawazo yetu, huwa hazihusiani kabisa na mambo tunayojadili’.

Sunday, May 19, 2013

Waraka kuhusu muswada wa Baraza la Vijana la Taifa wa Mwaka 2013

Vijana wenzangu na wote wenye dhamira ya kuwezesha maendeleo ya vijana nchini, salaam! 

Mtakumbuka kwamba mwezi Januari 2013 nilitoa taarifa kwa umma ya kueleza kuwa niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge Muswada Binafsi wa Sheria ya Baraza la Vijana la Taifa na kuomba hatua za ziada toka ofisi ya Bunge kwa kuzingatia Kanuni ya 21 na Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za Bunge. 

Toka wakati huo muswada huo mpaka sasa Mei 2013 haujachapwa katika gazeti la Serikali na nimepokea barua toka kwa ofisi ya Bunge kwamba wamepokea ushauri toka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwa muswada huo hauwezi kuchapishwa katika gazeti la Serikali kwa kuwa umekiuka masharti ya ibara ya 99 ya Katiba ya Nchi. 

Sababu ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutoa ushauri huo ni kuwa muswada unalenga pamoja na mambo mengine kupitia kifungu cha 31 kipengele cha kwanza kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwa madhumuni ya kugharamia shughuli za baraza la vijana la taifa, mipango ya baraza na kutekeleza miradi ya vijana kwa ajili ya maendeleo ya vijana. 

Kwa maoni yangu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ametoa ushauri huo bila kuzingatia kwamba kifungu cha 31 kipengele cha pili kinataja vyanzo mbalimbali vya fedha za mfuko ikiwemo kutaja kuwa fedha za mfuko zitatokana na fedha zilizotengwa na Serikali na Bunge kwa ajili ya Baraza kwa mujibu wa Ibara ya 135 kifungu cha pili cha katiba ya Nchi.

Monday, March 25, 2013

Mnyika na harakati za kuhakikisha Maji ndani ya Jimbo la Ubungo

21 Machi, 2013 Mnyika aitwa Ikulu, JK awakumbuka Mabwepande
na Asha Bani

HOJA ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA) kuhusiana na suala la tatizo la upatikanaji wa maji katika Mkoa wa Dar es Salaam, inaelekea kupata ufumbuzi kutokana na Rais Jakaya Kikwete kumuita Ikulu mbunge huyo Jumatatu wiki ijayo.

Wengine walioitwa kukutana na rais ni Mkuu wa Mkoa, Mecky Sadick, wakuu wote wa wilaya pamoja na wabunge na wataalamu kutoka Wizara ya Maji.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika uzinduzi wa daraja la Mtaa wa Golani, Kata ya Saranga, Rais Kikwete alisema kuwa kutokana na wananchi wa kata hiyo kupiga kelele kuhusiana na suala la maji ameamua kukutana na viongozi hao ili kupatiwa ufumbuzi.

Mwaliko wa kushiriki ufuatiliaji wa mradi wa maji na mkutano wa mbunge na wananchi katika kilele cha wiki ya maji kitaifa na siku ya maji kimataifa leo tarehe 22 Machi Mtaa wa Makoka kata ya Makuburi.

Leo tarehe 22 Machi ni kilele cha wiki ya maji kitaifa na siku ya kimataifa ya maji. Katika kazi zake ikiwa ni sehemu ya siku hiyo Mbunge wa Ubungo John Mnyika saa 9 alasiri atakuwepo eneo la Uluguruni Mtaa wa Makoka Kata ya Makuburi kufanya ufuatiliaji wa mradi wa maji.

Mradi umetekelezwa kwa ushirikiano na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) baada ya kuchochewa kwa kuchangiwa milioni kumi na Mfuko wa Maendeleo (CDCF) Jimbo la Ubungo ambao Mnyika ni mwenyekiti wake pamoja na kuunganisha nguvu za wananchi katika maeneo husika.

Aidha, baada ya kukagua mradi huo kuanzia saa 10 Jioni mbunge atafanya mkutano na wananchi kwa ajili ya kutoa ujumbe kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jiji la Dar Es Salaam zinazopaswa kuchukuliwa hata baada ya wiki ya maji.

Pia kufuatia mwaliko wa Rais Jakaya Kikwete wakukutana tarehe 25 Machi 2013 na Mkuu wa Mkoa, DAWASA, DAWASCO, Mnyika na wabunge wengine wa Mkoa wa Dar es Salaam kujadili hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji, mbunge atatumia mkutano wake na wananchi kusikiliza maoni na mapendekezo kuhusu hatua za ziada zinazopaswa kuchukuliwa.

Imetolewa tarehe 22 Machi 2013 na: 

Gaston Shundo 

Afisa katika Ofisi ya Mbunge Ubungo

Picha za Uzinduzi wa Daraja la Suka-Golani!

















Tujikumbushe harakati na jitihada mbalimbali ambazo zilifanywa mpaka kufikia hatua ya sasa kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora ya miundombinu ya barabara ya Suka-Golani hapa:

1 May, 2012  Daraja Golani-Suca na Barabara Mburahati-Mabibo

Mkandarasi aliyepewa zabuni ya ujenzi wa daraja la Golani-Suka anapaswa kuanza mapema ujenzi wa daraja hilo muhimu linalounganisha kata za Kimara na Saranga ili kupunguza kero kwa wananchi hasa wakati wa mvua.

Mwezi huu wa Aprili nimefuatilia kuhusu hatma ya daraja hilo na hatimaye mkataba wa ujenzi wa daraja husika umesainiwa kati ya Manispaa ya Kinondoni na Mkandarasi Kika Co. Ltd kwa gharama za shilingi milioni 447.

Hata hivyo, ujenzi wa daraja husika haujaanza suala ambalo linahitaji Manispaa ya Kinondoni kumsimamia kwa karibu mkandarasi husika ili ujenzi uanze kwa haraka kwa kuwa mchakato wa zabuni ulianza kuanzia mwanzoni mwa mwaka 2012.

Izingatiwe kwamba kutokuwepo kwa daraja katika eneo hilo mwaka miaka mingi kumefanya mawasiliano katikati maeneo hayo kuwa magumu nyakati za mvua na kusababisha madhara ya kibinadamu na mali wananchi wanapovuka mto katika eneo hilo wakati wa mafuriko.

Baada ya kuwawakilisha wananchi kutaka ujenzi wa daraja hilo lilingizwa kwenye bajeti ya Manispaa ya Kinondoni kwa mwaka wa fedha 2011/2012 hata hivyo miezi ikiwa imebaki takribani miwili kabla ya mwisho wa bajeti husika ujenzi wa daraja hilo ulikuwa haujaanza bado.

Hatua kama hiyo inahitajika pia kwa barabara ya Mburahati mpaka Mabibo NIT ambayo inapaswa kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami ikiwa imetengewa kiasi cha shilingi milioni 504 kwa ajili ya kuchangia katika kupunguza msongamano wa magari katika barabara ya Morogoro . 

Tathmini ya utekelezaji wa bajeti inaonyesha kwamba kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ni ndogo pengo ambalo linapaswa kuzibwa kwa kusimamia kwa karibu miradi inayopaswa kuanza katika muhula uliobaki wa mwaka wa fedha 2011/2012.

Rejea: http://mnyika.blogspot.com/2012/05/daraja-golani-suca-na-barabara.html 


January 27, 2012 Kuhusu Msongamano wa Magari DSM na Ziara Kwembe: http://mnyika.blogspot.com/2012/01/kuhusu-msongamano-wa-magari-dsm-na.html

Thursday, March 21, 2013

MNYIKA ATAKA KAULI YA RAIS KIKWETE KUHUSU UJENZI WA MACHINGA COMPLEX NA JUMBA LA VIWANDA VIDOGO JIMBONI UBUNGO

Mbunge wa Jimbo la Ubungo John Mnyika ametoa mwito kwa Rais Jakaya Kikwete kueleza sababu za kutokutekelezwa mpaka sasa kwa ahadi zake alizotoa mwaka 2010 za ujenzi wa Machinga Complex na jumba la viwanda vidogo katika jimbo hilo kuchangia katika kupanua wigo wa ajira kwa vijana. 

Mnyika aliyasema hayo akijibu swali la mwakilishi wa vijana katika mkutano wake na wananchi alioufanya katika ofisi za Serikali ya Mtaa wa Muungano katika kata ya Manzese uliofanyika mwishoni mwa wiki (16/03/2013). 

Mwakilishi huyo wa vijana alitaka kufahamu hatua ambazo mbunge amechukua kufuatilia kuhusu maeneo ya kufanyia biashara kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo katika jimbo la Ubungo. 

“Kazi ya mbunge ni kuwawakilisha wananchi na kuisimamia serikali ili kuwezesha utatuzi wa kero, matatizo ya maeneo ya wafanyabiashara ndogo ndogo yamedumu kwa muda mrefu kutokana na udhaifu katika mipango miji na hivyo maeneo ya wafanyabiashara na masoko kuuzwa, kuvamiwa au kuwa machache. Nimefuatilia suala hili, kuna ambao wamepata maeneo na wengine wengi bado”, alijibu Mnyika.

Wednesday, March 20, 2013

RUFAA DHIDI AGIZO LA ACP CHARLES KENYELA KAMANDA WA POLISI WA MKOA WA KIPOLISI WA KINONDONI KUZUIA MKUTANO WA HADHARA WA MBUNGE NA WANANCHI TAREHE 16 MACHI 2013



Kumb. Na. OMU/US/003/2013                                                                                               18/03/2013 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,
S.L.P 9223, 
Dar es Salaam. 

Mheshimiwa: 


RUFAA DHIDI AGIZO LA ACP CHARLES KENYELA KAMANDA WA POLISI WA MKOA WA KIPOLISI WA KINONDONI KUZUIA MKUTANO WA HADHARA WA MBUNGE NA WANANCHI TAREHE 16 MACHI 2013 


Kwa barua hii nawasilisha rasmi rufaa kwa kutumia kifungu cha 43 (6) cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma za Polisi wasaidizi sura ya 322 (The Police Force and Auxilliary Service Act Cap 322 RE 2002) dhidi ya agizo la ACP Charles Kenyela Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni kuzuia mkutano wa hadhara wa mbunge na wananchi tarehe 16 Machi 2013. 

Katika kushughulikia rufaa hii zingatia kuwa tarehe 4 Machi 2013 niliwasilisha taarifa kwake kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha Sheria ya Kinga, Madaraka na Haki za Bunge na. 3 ya mwaka 1988 (The Parliamentary Immunities, Powers and Privileges Act) kuwa tarehe 16 Machi 2013 nilipanga kufanya mkutano na wananchi Jimboni. 

Katika taarifa hiyo kupitia barua yangu yenye Kumbu. Na. OMU/US/001/2013 ambayo nilitoa pia nakala kwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Afisa Tawala wa Wilaya ya Kinondoni, Afisa Mtendaji wa Kata ya Manzese na Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Muungano, nilieleza kwamba mkutano huo nilipanga kuufanya katika Kata ya Manzese Eneo la Bakheresa kuanzia saa 3 asubuhi mpaka saa 5 Asubuhi. 

Katika taarifa hiyo nilieleza kwamba lengo la mkutano huo ni kuwapa mrejesho wananchi kuhusu masuala niliyoyawasilisha katika Mkutano wa Kumi wa Bunge uliomalizika tarehe 08 Februari 2013 na kupokea mambo ya kuyazingatia kuelekea Mkutano wa Kumi Na Moja wa Bunge unaotarajiwa kuanza tarehe 9 Aprili 2013. 

Hata hivyo, kupitia mkutano wake na vyombo vya habari tarehe 14 Machi 2013 na barua yake iliyoletwa ofisini kwangu tarehe 15 Machi 2013, ACP Charles Kenyela Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni alitoa agizo la kuzuia mkutano wa hadhara wa mbunge na wananchi niliopanga kuufanya tarehe 16 Machi 2013. 

Katika agizo hilo alilolitoa chini ya kifungu cha 43 (2) na 43 (3) Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma za Polisi sababu iliyohusu mkutano kwa mujibu wa barua yake yenye Kumb. Na. DSM/KINONDONI/SO.7/2/CHADEMA/284 ni: 

“Eneo la Manzese Bakhresa ambalo unakusudia kufanyia mkutano siyo eneo halali kwa ajili ya mikutano. Eneo hilo kwa mujibu wa maelekezo ya Manispaa ya Kinondoni kupitia mipango miji ni eneo linalotumika kwa ajili ya kuegesha magari makubwa (malori) na ndio maana liko katika eneo kuu la barabara ya Morogoro ambayo iko katika matengenezo. Kuruhusu mkutano wako kufanyikia hapo ni kukiuka sheria ya mipango miji ya Manispaa ya Kinondoni pamoja na kuingilia shughuli za ujenzi wa barabara unaoendelea hivi sasa na kuwabugudhi watumiaji wengine wa eneo hilo”.

Tuesday, March 19, 2013

LEO NDIO MWISHO; OMBA UWAKILISHI KWENYE MABARAZA YA KATIBA SASA

Leo tarehe 20 Machi 2013 ni siku ya mwisho ya wananchi kuwasilisha maombi ya kuwa wajumbe wa mabaraza ya katiba ya ngazi ya wilaya ambayo yana wajibu muhimu wa kupitia rasimu ya katiba na kutoa maoni iwapo imezingatia maoni ya wananchi yaliyokunywa katika hatua ya wananchi binafsi na makundi mbalimbali katika jamii. 

Nawakumbusha ambao bado hamjawasilisha maombi na mna dhamira ya kutimiza wajibu huu wa kiraia na kikatiba kwa kuwasilisha barua ya maombi kwa watendaji wa mitaa/vijiji. 

Kuna nafasi nane kwa kila mtaa kwa Dar es salaam, nne kwa maeneo mengine ya Tanzania Bara katika makundi yafuatayo; mwanamke, kijana, mtu mzima na mtu mwingine yoyote: kwa Zanzibar tatu kwa kila shehiya. 

Sifa ni raia, miaka 18 au zaidi mwenye kujua kusoma, kuandika, hekima, busara, uadilifu, uwezo wa kujieleza na kupambanua mambo ambao najua wengi mnazo. Sifa nyingine ni kuwa mkazi wa kudumu kwenye mtaa au kijiji ambayo haimaanishi kwamba ni lazima uwe mwenye nyumba, hata wapangaji mnaruhusiwa kuomba. Sio lazima uwe mwanachama wa chama chochote cha siasa na uteuzi wa awali utafanywa na mkutano mkuu wa mtaa wenu au kijiji chenu ambao wajumbe ni wakazi wote wa mtaa/kijiji husika. 

Tuesday, March 5, 2013

TUTAFANYA MAANDAMANO KWENDA WIZARA YA MAJI TAREHE 16 MACHI 2013; NIMESHAWASILISHA NOTISI, TUENDELEE NA MAANDALIZI

Tarehe 16 Machi 2013 nitaongoza maandamano ya amani ya wananchi kwenda kwa Waziri wa Maji kusimamia uwajibikaji kuwezesha hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es salaam.

Wote mlioshiriki mkutano wa tarehe 10 Februari 2013 (Kwa wale ambao hamkushiriki mnaweza kutazama video hii: http://www.youtube.com/watch?feature=player_embedded&v=O0txSoHqfGY ) , mtakumbuka tulimpa wiki mbili Waziri kujitokeza kwa wananchi kujibu hoja alizokwepa kujibu bungeni.

Tutakusanyika kata ya Manzese eneo la Bakhresa (jirani na daraja) saa 5 asubuhi na tutapita barabara ya Morogoro kuelekea kata ya Ubungo zilipo ofisi za Wizara ya Maji kufuatilia majibu ya ukweli na ukamilifu kuhusu hatua tisa za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka nilizopendekeza kwa niaba ya wananchi bungeni kupitia hoja binafsi na masuala mengine ambayo wananchi watataka yatolewe majibu siku hiyo.

Kila mmoja anaweza kuendelea na maandalizi ya kushiriki kwa kuwa tayari tarehe 4 Machi 2013 nimewasilisha notisi kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni na Maafisa wa Polisi Wasimamizi wa Maeneo kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 43 cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma Saidizi Sura ya 322 (The Police Force and Auxiliary Service Act, Chapter 322).

Sunday, March 3, 2013

WAZIRI MKUU PINDA AINGILIE KATI; WIZARA NA TANESCO HAWAJAJIBU UKWELI KUHUSU MGAWO WA DHARURA WA UMEME

Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kwa nyakati mbalimbali kati ya tarehe 28 Februari na 2 Machi 2013 kupitia baadhi ya vyombo vya habari wametoa majibu yasiyokuwa ya kweli juu ya mgawo wa dharura wa umeme uliotokea mwezi wa Februari. 

Katibu Mkuu wa Wizara Eliackim Maswi na Afisa Habari wa TANESCO Badra Masoud wote wameeleza kwamba hakukuwa na mgawo wa umeme bali kilichotokea ni matatizo madogo madogo ya mitambo na kwamba matengenezo yanaendelea. 

Kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini ninazo taarifa kwamba ukweli ni kuwa umetokea mgawo wa umeme wa dharura kutokana na upungufu zaidi wa kina cha maji katika mabwawa ya kufua umeme, upungufu wa fedha za kununua mafuta mazito ya kuendesha mitambo ya kufua umeme wa dharura na upungufu wa gesi asili ya kuendeshea mitambo ya kufua ya umeme. 

Hivyo, Waziri Mkuu Mizengo Pinda anapaswa kuingilia kati kuwaeleza ukweli wananchi ikiwemo hatua zilizochukuliwa kuhakikisha kwamba hali hiyo haiendelei mwezi Machi kinyume na ahadi iliyotolewa bungeni tarehe 28 Julai 2012 kwamba mgawo wa umeme ungekuwa historia. 

John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini 

02 Machi 2013

Saturday, March 2, 2013

WANANCHI OMBENI UJUMBE WA MABARAZA YA KATIBA LAKINI PINGENI ‘MIANYA YA UCHAKACHUAJI’ WA UTEUZI KWENYE KATA ILIYOWEKWA NA MUONGOZO ULIOTOLEWA NA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA BILA KUZINGATIA MAONI YA WADAU

Mwongozo kuhusu Muundo, Utaratibu wa kuwapata wajumbe wa mabaraza ya Katiba ya Wilaya (Mamlaka za Serikali za Mitaa) na uendeshaji wake uliotangazwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba haujazingatia maoni ya msingi yaliyotolewa na wadau mbalimbali ikiwemo Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). 

CHADEMA inawatahadharisha wananchi kuhusu ‘mianya ya uchakachuaji’ iliyotolewa na muongozo huo kwa kuzingatia kuwa ‘uchakachuaji’ wa uteuzi wa wajumbe wa mabaraza ya katiba, ni ‘uchakachuaji’ wa utoaji maoni kwenye mabaraza ya katiba, ambayo ni hatua ya awali ya ‘uchakachuaji’ wa rasimu ya katiba. 

Kwa mujibu wa Muongozo huo, ‘mianya ya uchakachuaji’ imeachwa kwenye ngazi ya kamati ya maendeleo ya kata ambayo wajumbe wake ni madiwani na wenyeviti wa mitaa/vijiji ambao kwa mujibu wa matokeo ya chaguzi za mwaka 2009 na 2010 kuna hodhi kwenye vikao hivyo ya chama kimoja (CCM).

Friday, March 1, 2013

RUFAA DHIDI YA UENDESHAJI WA BUNGE USIOKUWA WA HAKI NA UKIUKAJI WA KANUNI WA NAIBU SPIKA JOB NDUGAI KATIKA KUONDOA HOJA BINAFSI YA MAJI

Tarehe 28 Februari 2013 nimewasilisha rasmi rufaa kwa mujibu wa Kanuni ya 5 (4) dhidi ya uendeshaji wa Bunge usiokuwa wa haki wa Naibu Spika Job Ndugai kwa kukiuka kanuni ya 58 (5) kwa kulihoji bunge kinyume na kanuni kufanya uamuzi badili wa kuondoa hoja binafsi kuhusu hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jiji la Dar es salaam.

Nimefanya hivyo baada ya kupata kumbukumbu rasmi ya Bunge (Hansard) za kikao cha tano cha tarehe 4 Februari 2013 cha mkutano wa kumi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katika Mkutano huo Naibu Spika Job Ndugai alisema na kufanya maamuzi kwamba: “Sasa ninahoji wanaoafiki kwamba hoja hii iondolewe waseme ndiyo…..hoja imeondolewa. Walioafiki Wameshinda”; wakati mtoa hoja sikuwa nimeomba idhini yoyote ya hoja yangu kuondolewa.

Maamuzi hayo ni kinyume na Kanuni ya 58 Fasili 5 ambayo inaelekeza kwamba “Endapo hoja imefikishwa Bungeni, mtoa hoja anaweza tu kuiondoa hoja yake kwa kusimama mahali pake na kusema ‘Ninaomba ruhusa kuondoa hoja’ na papo hapo Spika ataliuliza Bunge kama linaafiki hoja hiyo kuondolewa na inapotokea Wabunge walio wengi watakubali, Spika atasema ‘hoja hiyo inaondolewa kwa idhini ya Bunge’ na hoja hiyo itakuwa imeondolewa na Bunge litaendelea na shughuli inayofuata”.

Ushahidi wa Kumbukumbu Rasmi za Bunge (Hansard) za kikao tajwa unathibitisha ukiukwaji huo wa kanuni kama ifuatavyo:

Wednesday, February 27, 2013

NCHI IMEINGIA TENA KWENYE MGAWO WA UMEME, SERIKALI IELEZE WANANCHI UKWELI NA HATUA KUHUSU UDHAIFU KWENYE UTEKELEZAJI WA MPANGO WA DHARURA

Nchi imeingia tena katika mgawo wa umeme kinyume na ahadi iliyotolewa na Waziri wa Nishati na Madini Prof Sospeter Muhongo bungeni tarehe 28 Julai 2012. 

Hali hiyo ni matokeo ya Serikali kutozingatia tahadhari niliyoitoa bungeni tarehe 27 Julai 2012 kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani na kwa nyakati mbalimbali kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini juu ya hali tete iliyotarajiwa kuwepo na hatua zinazopaswa kuchukuliwa katika utekelezaji wa mpango wa dharura wa umeme. 

Ikiwa ni sehemu ya wajibu wa kibunge wa kuisimamia Serikali nawataka viongozi na watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kuacha kuficha hali ya mambo na kuwaeleza ukweli wananchi kuhusu mgawo wa umeme uliojitokeza na hatua za haraka zinazochukuliwa kurekebisha hali hiyo. 

Iwapo Wizara na TANESCO hawatatoa matangazo ya ukweli kwa wananchi, kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini nitaeleza vyanzo vya mgawo wa umeme uliojitokeza ili hatua ziweze kuchukuliwa wakati huu ambapo wajumbe wa kamati ya nishati na madini wenye wajibu wa kuisimamia Serikali kwa niaba ya Bunge katika sekta hizo nyeti hawajateuliwa.

Monday, February 25, 2013

Mnyika amuweka Maghembe kitanzini

NA RICHARD MAKORE

Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, amemuweka katika wakati mgumu Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, baada ya kutoa hadharani namba ya simu ya waziri huyo ili wananchi wamuulize ni lini atatekeleza ahadi ya kuwapatia huduma ya maji wananchi wa jimbo hilo.

Mnyika alitoa namba ya simu ya Profesa Maghembe na Naibu wake, Dk. Binillith Mahenge, wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika viwanja vya Goba mwisho na kuwataka wananchi kuwauliza viongozi hao wakuu wa Wizara ya Maji ni lini watapatiwa huduma ya maji ambayo imekosekana kwa zaidi ya miaka miwili sasa.

Mnyika alisema Profesa Maghembe akihututubia wananchi hao aliwapa namba ya simu ‘feki’ na kwamba alifanya hivyo kutokana na kuwadharau.

Februari 17 mwaka huu, Profesa Maghembe akihutubia mkutano wa hadhara eneo la Goba mwisho alikaririwa akisema kwamba huduma ya maji ingeanza kupatikana Februari 20, mwaka huu, lakini hadi kufikia juzi ahadi hiyo haijatekelezwa.

Profesa Maghembe alikaririwa akisema serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndiyo ina funguo za kufungua maji ama kuyafunga na kuwataka wananchi wa Kata ya Goba kumuamini kwamba Februari 20, mwaka huu wangepata maji.

Mnyika alisema ni aibu kwa Waziri akiwa na viongozi wa kitaifa wa CCM kutoa ahadi hewa na kwamba ataongoza maandamano makubwa ya wananchi wa jimbo lake kuvamia ofisi za Profesa Maghembe kwenda kudai maji.

Sunday, February 24, 2013

UFUMBUZI WA MADAI YA FIDIA MILIONI 278 KWENYE UJENZI WA BARABARA NA DARAJA GOLANI SUCA

Tarehe 19 Februari 2013 Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alifanya ziara ya kikazi katika kata za Kimara na Saranga kufuatilia kuhusu matengenezo ya barabara na daraja la Golani. 

Mnyika alifanya hivyo siku mbili tangu afanye mkutano wa kikazi na viongozi wa Serikali ya Mtaa wa Kanuni na wananchi katika kata ya Mabibo tarehe 16 Februari 2013 kulitolewa malalamiko kuhusu Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) kutoshughulikia maombi ya wananchi yaliyowasilishwa kwa kampuni hiyo kwa nyakati mbalimbali kati ya mwaka 2010 mpaka 2012. 

Ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji huo kuhusu barabara, Mnyika alikutana na wananchi ambapo walipaswa kulipwa fidia inayokadiriwa kufikia shilingi milioni 278 ili kuruhusu njia mbadala kupatikana kufuatia ujenzi wa daraja katika eneo hilo. 

Aidha, Mbunge amekagua matumizi ya daraja hilo yaliyoanza kupitia njia ya zamani na athari zake katika mfumo mzima wa usafiri katika eneo husika; na kubaini kwamba daraja husika haliwezi kuzinduliwa pamoja na kuwa limeanza kukamilika mpaka ujenzi wa kingo za mito ukamilike pamoja na kupatikana kwa barabara mbadala baada ya wananchi kulipwa fidia. 

Mara baada ya ziara hiyo Mbunge alikutana na uongozi wa Manispaa ya Kinondoni na kuwasilisha madai hayo ya wananchi ambao miezi zaidi ya sita imepita toka nyumba zao ziwekewe X bila hata ya kufanyiwa tathmini. Baada ya Mnyika kuwawakilisha wananchi hao uongozi wa Manispaa umeamua kutuma timu ya uthamini na mara baada ya uthamini huo, kutuma uongozi kukamilisha majadiliano na wananchi husika kabla ya tarehe 25 Februari 2013

Saturday, February 23, 2013

Ziara Kimara: Ukaguzi ulipaji fidia, upanuzi wa barabara na kuhakiki ujenzi wa daraja!


Mbunge wa Ubungo, John Mnyika akizungumza na mkazi wa Kimara Korogwe, Richard Paul wakati mbunge huyo alipokutana na wakazi hao kutaka kujua fidia wanazotaka kulipwa kutokana na upanuzi wa barabara, pia alitembelea ujenzi wa daraja katika eneo hilo. 



Tuesday, February 19, 2013

BAADA YA HOJA BINAFSI NA KUSUDIO LA MAANDAMANO; WAZIRI WA MAJI NA MKUU WA WILAYA WAENDA GOBA NA MAENEO MENGINE KUFUATILIA MIRADI YA MAJI

Nitafuatilia ahadi alizotoa Waziri wa Maji Prof. Jumanne Maghembe tarehe 17 Februari 2013 kuwa maji yataanza kutoka kata ya Goba tarehe 20 Februari 2013 na ziara ya Mkuu wa Wilaya Jordan Rugimbana kwenye kata hiyo. 

Hata hivyo, ni vizuri umma ukatambua kuwa pamoja na mabadiliko ya hoja kwa kuongeza maneno ya kupendekeza hoja kuondolewa yaliyofanywa na Waziri wa Maji Prof. Jumanne Maghembe kinyume na kanuni za Bunge tarehe 4 Februari 2013, maelezo na hoja binafsi niliyowasilisha bungeni yameongeza uwajibikaji wa Waziri wa Maji, Mkuu wa wilaya ya Kinondoni na Halmashauri kuhusu masuala ya maji. 

Siku chache baada ya kutangaza tarehe 10 Februari 2013 kwenye mkutano wa hadhara kuipa Serikali wiki mbili, Mkuu wa Wilaya na Meya wa Halmashauri ya Kinondoni waliitisha mkutano na viongozi wa mitaa pamoja na kamati za miradi ya maji ya jumuiya na leo tarehe 18 Februari 2013 Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Jordan Rugimbana ameanza ziara ya ufuatiliaji wa miradi ya maji katika Jimbo la Ubungo. 

Sunday, February 17, 2013

HALI TETE YA UPATIKANAJI WA MAJI JIJINI DSM; DAWASA NA DAWASCO WAWAJIBISHWE

Kwa nyakati mbalimbali kuanzia mwezi Januari mpaka Februari 2013 pametokea matatizo ya kuharibika kwa baadhi ya mitambo na kupungua kwa uzalishaji wa maji katika vyanzo vya mto Ruvu na hivyo kusababisha matatizo ya maji kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam na maeneo yanayohudumiwa na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) katika Mkoa wa Pwani. 

DAWASA imeingia mkataba wa uendeshaji na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO) wa kutekeleza majukumu mbalimbali ikiwemo kuendesha mitambo, kusimamia usambazaji wa maji na kufanya matengenezo na kutoa taarifa kwa wananchi kuhusu huduma zinazotolewa. Aidha, DAWASCO wanapaswa kuzingatia mikataba ya huduma kwa wateja ambayo inaitaka kutoa taarifa kwa umma pale kunapotokea matatizo ya maji. 

Kwa kuzingatia mikataba hiyo, DAWASA na DAWASCO wanapaswa kutoa matangazo kwa umma kuhusu matatizo mapya yaliyojitokeza mwezi Januari na Februari 2013 ili kuepusha matatizo hayo kuhusishwa na hatua ya kuwasilishwa na kuondolewa bungeni kwa hoja binafsi niliyoiwasilisha tarehe 4 Februari 2013 juu ya hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam. 

Kwa wakazi wa Kibamba, Kwembe, Msigani, Mbezi, Saranga na Kimara ni muhimu wakatambua kwamba nimefuatilia na kujulishwa kwamba palikuwa na tatizo la kupungua kwa uzalishaji wa maji katika chanzo cha Ruvu Juu ambalo limerekebishwa tarehe 12 Februari 2013 hivyo maji yataendelea kupatikana kwa mujibu wa ratiba ya mgawo kama ilivyokuwa awali katika maeneo ambayo yalikuwa yakipata maji tangu mwaka 2012. 

Kwa wateja ambao bado watakuwa na matatizo katika maeneo yao wawasiliane na DAWASCO kupitia namba ya huduma kwa wateja 022 55 00 240 au 0779090904 au info@dawasco.com ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa.