Monday, December 20, 2010

Mnyika kuwasilisha hoja ya katiba mpya

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika amesema kuwa atawasilisha bungeni hoja binafsi ya kutaka mabadiliko ya katiba na kupinga moja ya mapendekezo ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda la kuunda tume ya kuangalia mchakato huo.

Tangu kumalizika uchaguzi mkuu wa Oktoba 31, Chadema imewasha moto wa mabadiliko ya katiba na kufufua mjadala wa kutaka kuandikwa kwa katiba mpya kiasi cha Waziri Pinda kuamua kutoa tamko mwishoni mwa wiki kuwa atamshauri Rais Jakaya Kikwete aunde tume kuchunguza madai hayo.

Miongoni mwa viongozi waliojiunga kwenye mjadala huo wa kutaka katiba mpya ni mawaziri wakuu wa zamani, Joseph Sinde Warioba na Frederick Sumaye, Jaji Mkuu Agustino Ramadhan na Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa ambaye alitahadharisha kuwa bila ya katiba mpya nchi inaweza kuingia kwenye vurugu.

Akizungumza na Mwananchi jana, Mnyika ambaye ni mmoja wa wabunge vijana kwenye Bunge la Kumi, alisema atatimiza ahadi yake katika kipindi cha wiki moja kwa kuwasilisha taarifa kuhusu hoja binafsi ya katiba mpya kwa katibu wa bunge.
"Ibara ya 8 kifungu kwanza cha katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na mapungufu yake inaeleza wazi umuhimu wa wananchi kushirikishwa katika uundwaji wa katiba. Pia Ibara ya 63-(2) nayo inaeleza wazi," alisema Mnyika.
Aliongeza kuwa kama mbunge ana haki ya kuwasilisha hoja binafsi kuhusu katiba mpya na kwamba ni vyema suala la uundwaji wa katiba likarejeshwa mikononi mwa Bunge kwa kuwa ni mhimili wa dola unaofanya kazi kwa niaba ya wananchi.

"Ibara ya 98 ya katiba ndio sehemu pekee inayozungumzia marekebisho ya katiba hivyo ni wakati muafaka suala hili la katiba likapelekwa bungeni ili wananchi wawakilishwe," alifafanua Mnyika.
Mwanasiasa huyo kinda, ambaye pia ni mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Chadema, alieleza sababu za kutaka kupeleka hoja hiyo bungeni ni kutaka chombo hicho lipitishe mchakato wa kuundwa kwa katiba mpya.

"Unajua katiba ni sheria na kwa kuwa bungeni ndiko kunakotungwa sheria basi wanaopaswa kutoa mwelekeo wa katiba mpya ni Bunge," aliongeza.
"Pia katiba ni mkataba kati ya wananchi na watawala... ikumbukwe kuwa anayeandika mkataba ni mwenye mali, na hapa mwenye mali ni mwananchi na Bunge lipo kwa ajili ya wananchi. Kutokana na hilo, ipo kila sababu ya suala hili kurudi bungeni."

Lakini Mnyika alipingana na moja ya mapendekezo ya Waziri Pinda ya kuunda tume ya kuangalia mchakato wa kuandikwa kwa katiba mpya.
"Sikubaliani na kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuhusu katiba,” Mnyika aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es salaam jana.
“(Waziri Mkuu) Amesema atamshauri rais kuunda timu itakayoangalia mapendekezo ya tume zilizoundwa na pia kuanzisha utaratibu wa marekebisho ya katiba. Naona kauli yake haijalenga kuwepo kwa katiba mpya, bali inalenga zaidi marekebisho ya katiba."

Mnyika alifafanua kwamba, hoja hiyo ya Pinda ina mwelekeo wa kuchukua suala la katiba mpya mikononi mwa wananchi na kulipeleka kwa kundi fulani.
Waziri Pinda aliwaeleza wahariri wa vyombo vya habari mwishoni mwa wiki kuwa kuna njia mbili za kushughulikia kilio cha wananchi cha katiba mpya, akiitaja ya kwanza kuwa ni kumshauri rais aunde kamati ya watu ambao wataangalie maeneo gani ya kuingiza katika katiba.

Alisema njia ya pili ni rais kuunda timu yake ya kiserikali itakayoangalia mapendekezo ya tume zilizoundwa awali kuangalia marekebisho ya katiba na kuchukua mapendekezo yaliyojirudia yatakayoonekana kufaa kuingia katika katiba.

Lakini Mnyika alipingana na mapendekezo hayo akisema haoni sababu ya kuundwa kwa tume nyingine kwa kuwa tangu nchi ipate uhuru, zimeshaundwa tume nyingi kushughulikia suala la katiba.
Alitoa mfano wa Tume ya Jaji Nyalali ambayo ilipendekezwa kufutwa kwa sheria kadhaa ambazo zinaonekana kukandamiza haki za binadamu na Tume ya Jaji Kisanga, akisema matokeo ya uchunguzi wa vyombo hivyo viwili hayajafanyiwa kazi.

"Kutokana na hoja hii napendekeza kwamba, Bunge liweke mfumo wa tume ya kikatiba pamoja na kupitisha azimio ili nchi ifanye mkutano mkuu wa kikatiba kujadili suala hili na kisha zipigwe kura za maoni," alisema.
Alisisitiza kuwa katika suala la katiba mpya, ni lazima wananchi washirikishwe kwa kuwa sasa Watanzaania wanataka katiba mpya.

"Kwanza, katiba inayotumika hii leo ni ya mwaka 1977, tangu kipindi hicho kuna mabadiliko mengi yameshatokea kama ya kiuchumi, kiteknolojia; pili uundwaji wa katiba hiyo haukuwashirikisha wananchi; tatu katiba hii inakabiliwa na changamoto nyingi, mfano suala la Muungano na Tume ya Uchaguzi," alisema.

Chadema ilionyesha kwa vitendo dhamira yake ya kudai katiba mpya wakati wabunge wake walipoondoka kwenye ukumbi wa Bunge wakati Rais Jakaya Kikwete akianza kutoa hotuba ya ufunguzi. Viongozi wa chama hicho pia walisusia hafla ya kutangazwa kwa matokeo na sherehe za kuapishwa kwa rais na wiki mbili zilizopita hawakuonekana kwenye sherehe za uhuru.

Chanzo: Mwananchi-20/12/2010

No comments: