Nimepokea
mwaliko wa kikao maalumu cha kikao cha fedha na uongozi wa tarehe 3/01/2014
kikao kufanyika tarehe 06/01/2013 saa nane mchana kujadili mapendekezo ya
kuongeza maeneo mapya ya utawala katika Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na ajenda
zingine.
Nimeonelea
tija kuwasilisha mapendekezo yangu kwa maandishi kwa umma na baadae katika
kikao tajwa. Kwa hatua hii, ni fursa kwa kila mwananchi kutoa maoni yake juu ya
haya;
Kwa ukuaji wa kasi wa Dar es Salaam ambao
ndiyo mji mkubwa nchini Tanzania, jiji kitovu cha biashara na viwanda ambalo
kadiri ya takwimu linakadiriwa kuwa na idadi ya watu milioni nne na nusu. Jiji
hili limeshika nafasi ya tatu katika miji inayokuwa kwa kasi barani Afrika na miongoni
mwa miji kumi inayokuwa kwa kasi duniani.
Ifahamike pia, Jiji la Dar es Salaam ndilo
linashikilia asilimia themanini na tatu (83%) ya mapato ya serikali kitaifa na
takribani asilimia sabini (70%) ya kodi zote zinazokusanywa nchini Tanzania.
Yafuatayo ndiyo mapendekezo yangu ya
wasilisho la nyaraka ya mapendekezo yaliyoletwa katika ofisi yangu toka
Manispaa ya Kinondoni;
Mosi, Pendekezo
la kutumia “Manispaa” badala ya “Wilaya”:
Kadiri ya wasilisho, imetumika pendekezo la
“wilaya”. Ningeshauri na kupendekeza kutokana na uhalisia na ukuaji wa kasi
kutumika kwa “Manispaa” badala ya wilaya.
Pili, Pendekezo
bora la mgawanyo wa Manispaa:
Katika wasilisho lenye uwepo wa mapendekezo
saba. Ninaungana na kuafiki utumiaji wa pendekezo la pili lililowasilishwa la
kuwa na Manispaa tano (5) ambazo ni;
i.
Manispaa
ya Ilala
ii.
Manispaa
ya Temeke
iii.
Manispaa
ya Kinondoni
iv.
Manispaa
ya Kigamboni
v.
Manispaa
ya Ubungo
Sababu
muhimu:
1.
Ukubwa
kijiografia: Kwa kuongeza wilaya mbili mpya yaani Manispaa ya Kigamboni na
Manispaa ya Ubungo hii itasaidia wilaya hizi kuweza kuhimili ukubwa wa eneo wa
kijiografia ambalo kwa sasa inaelemea wilaya hizi za sasa yaani Manispaa ya
Kinondoni na Manispaa ya Temeke.
2. Ukuaji wa kasi wa
jiji: Katika ukuaji wa kasi unaoendelea jiji la Dar es Salaam maeneo yaliyopo
katika wilaya hasa ya Kinondoni na Temeke ndiyo ambayo yanaongoza pia katika
ukuaji huo wa kasi wa kimakazi na shughuli za kiuchumi kama viwanda na
uwekezaji. Hivyo kwa kuwa na Manispaa mpya mbili(Manispaa ya Ubungo na Manispaa
ya Kigamboni) zitasaidia kwa kiasi kikubwa kuweza kusimamia vyema mipango miji,
kuujenga vyema mji na kusimamia kihuduma.
3. Uwepo wa mipango ya
kuimarisha ukuaji wa jiji kupitia miji ya pembezoni “satellite cities”: tayari serikali imeweka dhamira ya kuimarisha
ukuaji wa jiji kupitia satellite cities. Hivyo uwepo wa wilaya mbili yaani
Kigamboni (Satellite city Kigamboni)
na Ubungo (“Luguruni Satellite City” ndani
ya Kata ya Kwembe na Kata ya Kibamba) zitamudu kusimamia vyema ujenzi imara wa satellite cities na pia kuwezesha wilaya
zitakazoachwa kama wilaya ya Kinondoni kuwa na ahueni ya kuelemewa na kazi
hivyo nazo kusimamia vyema mipango ya ujenzi wa satellite cities zilizomo ktk maeneo hayo